UCHAFU katika maeneo mengi ya jiji la Dar es Salaam ni moja ya matatizo makubwa ambayo dhahiri uongozi wa jiji hilo umeonekana kushindwa kuyapatia ufumbuzi. Ni aibu kubwa kwa jiji hili ambalo linapaswa kuwa kioo cha taifa letu kwa usafi, kukithiri kwa uchafu katika maeneo yake mbalimbali, pamoja na wanayofikia wageni kutoka nje.
Nionavyo ni kama viongozi wetu wanazidi kufumbia macho tatizo hilo, licha ya kupata nafasi ya kutembelea nchi nyingi duniani ambazo mimi naamini wamepata fursa ya kujifunza.
Naamini wamejifunza mambo mengi, lakini pia hili la usafi wakafahamu wenzetu wanafanyaje hata miji yao ikawa katika viwango vya usafi vya hali ya juu.
Iwapo wameshindwa kufanya wao waende kwingine kujifunza hasa katika Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro au katika Manispaa ya Iringa. Ni hakika kuwa miji hii imepiga hatua kubwa inayofaa kupigiwa mfano kwa usafi na ziara za watendaji wa Dar es Salaam zinaweza kusaidia kutimiza azma hiyo.
Lakini, sioni kwa nini Moshi au Iringa waweze na Dar es Salaam ambako ni makao makuu ya shughuli karibu zote za nchi, washindwe. Naamini hapa kuna tatizo tena tatizo linalofaa kutazamwa kwa jicho kali kama la fundi saa anapomhudumia mteja wake.
Ni wazi kuwa katika Jiji la Dar es Salaam kuna upungufu mkubwa wa vifaa vya kuwekea takataka hasa katika vituo vya mabasi ya abiria (daladala), viwanja vya mpira na maeneo ya kazi.
Ni kutokana na hali hiyo ni vigumu kumshawishi mtu kwa kumbebesha taka kuanzia eneo la kazi au kituoni na kwenda nao hadi nyumbani kwake kwenye kifaa cha kuhifadhia taka kabla ya kuzitupa.
Hali hiyo inawashawishi watu kutupa takataka ovyo, hasa chupa za maji na mifuko ya plastiki.Ni wazi kuwa uchafu husababisha magonjwa ya milipuko hususan kuhara na kipindupindu.
Ni bora kuepuka hali ya uchafu badala ya kuiachia na likitokea tatizo ndio kuanza kukimbizana nalo bila mpango na kuingia gharama kubwa za matibabu kwa magonjwa ya kuambukiza. Tukumbuke kuwa kuzuia ni bora kuliko kutibu na hili ndilo linaloweza kuisaidia Dar es Salaam.
Sioni sababu za magonjwa ya mlipuko kuendelea kuisumbua Dar es Salaam na wakazi wake hasa wakatio huu wa mvua za masika. Nakubali kuwa mvua hizo zinaongeza changamoto na hatari ya magonjwa ya mlipuko kwani wapo wanaozitumia vibaya kwa kufungulia mifereji ya maji machachu na kinyesi.
Inashangaza upitapo maeneo mbalimbali ya jiji hili kama Kariakoo, Manzese, Tandale na kukutana na baadhi ya watu katika maeneo tofauti wakiwa wameyafungulia mabomba yao yanayotoka vyooni na kumwaga uchafu huo nje, tena katikati ya jiji.
Tatizo lililopo ni kwa viongozi wa ngazi mbalimbali za jijini Dar es Salaam kuzoea kufanya kazi kwa mazoea, wamekariri utendaji baada ya mambo kadhaa kufanyika.
Nikumbushe siku moja nikiwa katika moja ya ofisi za jiji hilo nilimsikia mmoja wa mabosi akitamba, "Bwana, sisi tunashukuru kwa kipindi hiki tumepiga hatua sana katika maeneo yetu hakuna mtu aliyeugua wala kubainika kuwa na magonjwa ya milipuko (kipindupindu)."
Sikuamini kuwa kauli ile ilikuwa ya bosi huyo aliyekuwa akitamka hayo, kisa eti hajatokea mtu mwenye maradhi hayo mwaka huu, lakini wakati anaongea hayo maeneo yanayozingira ofisi zake ni machafu mno kiasi cha kutoelezeka.
Ni jambo la msingi na ni wakati muafaka kwa watendaji wa jiji la Dar es Salaam sasa waende wakajifunze kwa wenzao wa Moshi na Iringa waliweza kufanya nini katika kuimarisha usafi.Wanachotakiwa kufanya ni kujifunza na kuchota mafanikio ya miji hiyo na kuondoa changamoto hizo za usafi kwa jiji la Dar es Salaam.
Binafsi nafikiri kuna kila sababu kwa Dar es Salaam kuwa safi tena kwa wakati wote.
Natambua kuwa manispaa za jiji hilo zimejiwekea sheria ndogo ya kuwakamata na kuwatoza faini wanaotupa ovyo taka, hilo sipingani nalo na ninaliunga mkono.
Lakini, hili la kujikusanyia mamilioni ya faini hakutasaidia chochote, ikiwa hakuna mabadiliko ya kusambaza vifaa vya kutosha kukusanyia taka.Nashauri kwamba pamoja na kujifunza kutoka Iringa na Moshi, elimu kwa umma kuhusu usafi wa manispaa na Jiji kwa ujumla yake inahitajika.
Ni muhimu pia kwa jiji na manispaa zake zote tatu kuweka mfumo wa mafunzo kwa wakazi wake badala ya kuishia kufukuzana na wamachinga na kujikusanyia faini kutoka kwa watu wanaotupa ovyo taka.Elimu hii inayohusu usafi wa mazingira yafaa iwashirikishe watendaji wote kuanzia ngazi za chini katika serikali za mitaa, kata hata tarafa.
Kwa kutenda hayo yote kuwe na mashindano ya usafi yatakayoanza kwa kushindanisha ngazi ya mtaa kwa mtaa hadi kufikia hatua ya mwisho ya kushindanisha manispaa kwa manispaa na washindi kupewa zawadi kwa lengo la kuhamasisha wananchi kufanya usafi mara kwa mara.
Nionavyo, bila darasa la kutosha kwa wananchi kuhusu usafi wa mazingira itakuwa ni ndoto Dar es Salaam kuwa safi na ni kazi bure isiyokuwa na tija kuendelea kuwakamata na kuwatoza faini watu wanaotupa ovyo taka.
UNAONAJE KAMA UKIWAALIKA WATENDAJI WA JIJI WAKAJA KUJIFUNZA NYUMBANI KWAKO KBLA YA MS/IR