elivina shambuni
JF-Expert Member
- May 31, 2018
- 461
- 295
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) katika kipindi cha miaka minne imeongeza mapato yake na kufikia Sh. trilioni 58.3 Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Msafiri Mbibo, aliyasema hayo jana wakati akizungumzia mafanikio ya miaka minne tangu Rais John Magufuli aingie madarakani, na kueleza kuwa katika kipindi cha miaka minne kabla ya hapo, TRA ilikusanya Sh. trilioni 34.97.
"Mwaka 2015/16 mapato yalikuwa Sh. trilioni 12.5, 2016/17 yaliongezeka na kufikia Sh. trilioni 14.4, mwaka 2017/18 yalikuwa Sh. trilioni 15.5 na mwaka 2018/19 yaliongezeka zaidi na kufikia Sh. trilioni 15.9 hivyo kufanya mapato kwa miaka minne kufikia Sh. trilioni 58.3," alisema. Akilinganisha na miaka minne kabla ya utawala la Rais Magufuli, Mbibo alisema mwaka 2011/12 TRA ilikusanya Sh. trilioni 6.76, mwaka 2012/13 zilikusanywa Sh. trilioni 7.88, mwaka 2013/14 Sh. trilioni 9.52 na mwaka 2014/15 ilikusanywa Sh. trilioni 10.81. "Kwa miaka minne, TRA imekusanya wastani wa Sh. trilioni 1.3 ikilinganishwa na wastani wa Sh. bilioni 850 kabla ya awamu ya tano. Kuanzia Julai hadi Oktoba 2019/20 wastani wa makusanyo umepanda hadi kufikia Sh. trilioni 1.45 kwa mwezi," alisema.
Alisema ongezeko hilo linatokana na sababu mbalimbali ikiwamo kuimarishwa matumizi ya mashine za kieletroniki za kutokea risiti (EFD), kuongezeka kwa mizigo kutoka nje ya nchi inayopitia bandari ya Dar es Salaam na udhibiti wa makusanyo ya bidhaa zinazopaswa kulipa kodi. Mbibo alisema wamefanikiwa kuanzisha mfumo wa stempu za kodi za kielektroniki (ETS) ambazo ni mbadala wa za karatasi.
Alisema utekelezaji wa mfumo huo kwenye eneo la pombe kali na mvinyo katika kipindi cha mwezi Februari hadi Oktoba mwaka huu, TRA imekusanya ushuru wa bidhaa Sh. bilioni 77.8 na kodi ya ongezeko la thamani (VAT) Sh. bilioni 23.5. Alisema katika eneo la vinywaji laini matumizi ya ETS yalianza Agosti mwaka huu ambapo Septemba na Oktoba walikusanya Sh. bilioni 10 huku VAT ikiwa na Sh. bilioni 14.1.
Pia alisema serikali iliyafanyia kazi malalamiko ya wafanyabiashara ikiwamo makadirio makubwa ya viwango vya kodi ambapo yamefanyika mabadiliko ya sheria mbalimbali na kupunguza viwango vya kodi na kufuta tozo takriban 54. "Tumepunguza viwango vya kodi vya wafanyabiashara wadogo kutoka Sh. 150,000 hadi kufikia Sh. 100,000 hawa ni kwa wale wenye mzunguko wa mauzo yanayozidi Sh. milioni nne," alisema. Pia alisema wafanyabiashara wenye mauzo kati ya Sh. milioni 7 hadi Sh. milioni 11 viwango vya kodi vimepungua na kufikia Sh. 250,000 kutoka Sh. 318,000. Mbibo alisema wenye mauzo kati ya Sh. milioni 11 hadi Sh. Milioni 14 viwango vimepungua hadi Sh. 450,000 kutoka Sh. 456,000.
Alisema wanaopaswa kutengeneza hesabu za mizania, viwango vimebadilika kutoka mauzo ghafi ya Sh. milioni 20 hadi kufikia Sh. milioni 100 kwa mwaka. Alisema kutokana na mabadiliko hayo, wafanyabiashara wapya watakaosajiliwa TRA na kupewa Namba ya Utambukisho wa Mlipakodi (TIN) watapaswa kulipa kodi baada ya miezi sita. "Tumeongeza idadi ya walipa kodi kutoka milioni 2.2 mwaka 2015/16 hadi milioni 3.0 hadi kufikia mwezi Oktoba, " alisema.
Mbibo alisema mamlaka ilitangaza msamaha maalum wa riba na adhabu kwenye malimbikizo ya madeni ya kodi kwa asilimia 100 tofauti na asilimia 50 iliyokuwapo awali.
Mbibo alisema serikali iliongeza muda hadi Desemba 31 na kuwataka wale wote walioomba msamaha na kukubaliwa walipe. Kuhusu changamoto, alizitaja kuwa ni ukwepaji kodi wa makusudi, biashara za magendo kutokana na kuwapo kwa ukanda mrefu wa Pwani, mipaka mingi na rushwa. Pia alisema changamoto nyingine ni utunzaji dhaifu wa kumbukumbu na baadhi ya wafanyabiashara