si uiweke tu hapa na story zenu za kujirudia
Muro aongeza utata
• Awasilisha risiti za pingu alizokamatwa nazo
na Martin Malera
SAKATA la mwandishi wa habari za uchunguzi, Jerry Muro, limeingia katika hatua mpya baada ya kubainika kuwa ana risiti za pingu ambazo polisi walimkamata nazo.
Umiliki huo wa pingu unaongeza utata katika sakata zima linalomhusisha na utapeli, ingawa linajibu swali la Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova aliyetilia shaka zilikotoka pingu hizo.
Juzi alikaririwa akimtaka Muro awapelekee polisi risiti, akisema si rahisi kupata pingu kwa kuwa "haziuzwi hovyo kama njugu."
Kamanda Kova alisema ni marufuku kwa raia kumiliki pingu, na kwamba kupatikana nazo ni kosa la jinai.
Alisisitiza kuwa pingu ni mali ya polisi, magereza na jeshi; hivyo mtu wa kawaida kukutwa nazo ni kosa la jinai. Na alidai kwamba Muro asingeweza kupata risiti.
"Pamoja na kumwambia atuletee risiti, tunajua hatafanikiwa kuzipata kwa kuwa pingu haziuzwi ovyo kwani mwenye mamlaka ya kumuweka nguvuni mtu ni polisi pekee," alisema Kamanda Kova.
Hata hivyo, jana Muro alilithibitishia Tanzania Daima kwamba anamiliki kihalali pingu na bastola aina ya CZ 97B namba A6466 iliyotengenezwa nchini Czechoslovakia.
Risiti hiyo inaonyesha Muro alinunua pingu hizo Mei 20 (mwaka umefutikafutika) katika duka la silaha la Mzinga Corporation lililoko Upanga, jijini Dar es Salaam, akapewa risiti namba 34357310.
Kwa mujibu wa risiti hiyo iliyoandikwa jina kamili la Muro, pingu hizo zilinunuliwa kwa sh 25,000.
Tanzania Daima ilipowasiliana na duka hilo la silaha, mmoja wa wafanyakazi wake ambaye hakutaka kutaja jina, alikataa kuzungumzia risiti hiyo kwa madai kuwa si msemaji.
Mfanyakazi huyo alilitaka Tanzania Daima kuwasiliana na Meneja Mkuu wa Mzinga Corporation, lakini hakupatikana. Ilidaiwa kuwa alikuwa nje ya ofisi.
Muro anayekabiliwa na tuhuma za kudai rushwa kwa vitisho pamoja na kukutwa na pingu isivyo halali, amekuwa gumzo tangu kuanza kwa sakata hili kutokana na utata wa taarifa zinazomhusu, hasa zinolewazo na polisi.