Moja ya makala iliyoyumbisha fikra zangu wakati kijana zitto akitundikwa msalabani kufuatia sekeseke la mgao wa umeme ni hii iliyochapwa gazeti la Tanzania Daima
..ni hapo nilianza kuona ugumu wa siasa za bongo vs taaluma. Nikaona umuhimu wa wanasiasa kunoa zaidi bongo zao zaidi
..Katika kipindi hiki ambacho hali inazidi kuwa ngumu, wengi sasa tunaanza kurejea huko tulikotoka tayari
.Mwalimu Nyerere alisema ukweli una tabia ya kulipiza
je, ukweli huu unalipiza?
.kwa mgao wa umeme?
..kweli sifa adimu ya kiongozi ni kuona mbali
SAKATA LA DOWANS; ZITTO KAMA OBAMA
Siku chache zilizopita, Machi11, 2009 niliposoma makala ya Daktari wa Falsafa katika masomo ya falsafa Chuokikuu cha Dar es Salaam, makala iliyochapishwa kwenye gazeti la The Citizen toleo la Na 1410 ambayo ilibeba ujumbe wa kumfananisha Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma na ambaye tangu mwaka 2007 aliteuliwa kuingia timu ya washauri wa Rais wa ujerumani kuhusu uchumi kutoka Afrika, Kijana mpambambanaji Zitto Kabwe na Rais wa sasa wa Marekani aliyetingisha historia ya dunia, Barack Obama nilipata msisimko na kubaki na fikiri kuhusu fikra zake.
Dk Lwaitama anasema Zitto ni mwanasiasa wa kizazi kipya, mwenye mawazo ya kizazi kipya kama yanayozungumzwa na Barack Obama katika kitabu chake cha The Audacity of hope. Kwamba Waliojaliwa uwezo wa kufikiri kwa kina wanaweza kusema Zitto Kabwe ameonesha tena kuwa ni mwanasiasa wa kizazi kipya, kiasi kwamba akishawishiwa kwa hoja za kitaalamu kuhusu pendekezo fulani yupo tayari kuliunga mkono hata kama kwa kufanya hivyo itamgharimu umaarufu wake na wa chama chake kwa muda mfupi.
Wakati Daktari huyo wa falsafa akizungumza hayo, pembeni naona malalamiko ya muda mrefu sasa kutoka kwa mmoja wa wachambuzi wa masuala ya siasa, Kaka yangu Absalom Kibanda, ambaye pia ni Mhariri mkuu wa gazeti la TanzaniaDaima. Kibanda yeye analia na mwenendo wa mijadala ya siasa nchini kwamba inakwenda kombo,hovyo na hivyo amekuwa na mashaka sana kuhusu huko tuendako! Pengine ndio sababu ya kubatiza waraka wake jina la Tuendako.
Ilinibidi niumize kichwa sana kufikiri mawazo ya walimu wangu hawa pamoja na ule waraka wa Mh Zitto Kabwe mwenyewe alioutuma kwetu watanzania kutueleza misingi ya yeye kuamini anachokiamini, kwa upande mmoja, huku kambi nyingine ya wajuzi wa mambo, akina Dk Harrison Mwakyembe, Spika Sitta na Mzee Shellukindo ambao kwa matukio kadhaa ikiwa ni pamoja na kusaidia mchakato wa kumwondoa Waziri Mkuu wa kwanza wa seriikali ya Jakaya Kikwete kwa tuhuma za ufisadi wamefanikiwa kujijengea uhalali wa kuitwa wazalendo kirahisi.
Lakini wakati hayo yakiendelea. Na mjadala ulitaka kuhama kwenye hoja na kuchukua sura ile ile ya awali. Kwamba akina Mwakyembe wanapinga ufisadi na hivyo kila anayetofautiana nao katika lolote, kwa nguvu ya vyombo vya habari vilivyopo kambi yao mtu huyo anaweza kufanywa aonekane anapingana na vita dhidi ya ufisadi.
Nimesema kwa kutumia vyombo vya kambi yao kwasababu kwa jinsi siasa za Tanzania zinavyokwenda, vyombo vya habari vinaelekea kupoteza mantiki ya uhuru wake kama wamiliki wataendelea kuwa waamuzi wakuu wa vyombo vyao viandike nini, visiandike nini! Wakati haya yakiendelea, unajitokeza mkanganyiko mwingine wa aina yake, ambao mpaka sasa sijapata majibu yake. Mana kwa upande mmoja, Waziri wa Nishati na Madini, Bwana William Ngereje kwa kutumia kitambu cha kumbukumbu za mijadala ya bunge- hansard, ametuthibitishia mkanganyiko mkubwa wa mawazo ya watu walewale lakini wanaothibitisha kufikiria tofauti katika kadhia yenye muktadha uleule.
Mpaka sasa Waziri Ngereja amefanikiwa kutuonesha kwamba, kwanza mazingira ya mkataba wa IPTL hayana tofauti na ule wa Dowans, isipokuwa anashangaa kuona wabunge walewale(akina Shellukindo na Mwakyembe) walioisukuma na wanaoendelea kusukuma serikali inunue mitambo iliyoingia nchini kifisadi ya IPTL wanakataa serikali isinunue mitambo ya DOWANS iliyoingia nchini katika mazingira hayo hayo ya kifisadi.Tuhuma hizi ni kipimo cha uadilifu, na zaidi ni kipimo cha kama mawazo wanayoyatoa akina Mwakyembe, Spika Sitta na Shellukindo hayaendi sambamba ama maslahi binfasi ya kibiashara au kambi za kisiasa ndani ya chama cha Mapinduzi.
Binafsi naamini ni muhimu akina Dk Mwakyembe na Mzee Shellukindo wafafanue suala hili kwa heshima yao kama wanasiasa. Maana ni ukweli usiopingika kwamba hata maelezo ya awali yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Mzee Shellukindo kukosoa msimamo wa Waziri Ngereja bado maelezo hayo yanapwaya kuweza kuitwa majibu. Swali linalohitaji majibu ni hili, kwanini Dk Mwakyembe na Mzee Shellukindo walipokuwa Kamati ya Viwanda na Biashara walisisitiza na bado wameendelea kusisitiza serikali inunue mitambo/kampuni ya IPTL ilhali kampuni hiyo imekwishathibitika mahakamani kuwa mchakato wake unahusika na ufisadi mkubwa unaoligharimu taifa hili hasara ya zaidi ya bilioni3 kila mwezi?.
Sisemi kwamba ni muhimu wala ni lazimaTANESCO wanunue DOWANS, ila napata mashaka makubwa kama wananchi tunaweza kufanya maamuzi kwa kuzingatia aina hii ya wabunge, na kama tunaweza kuwa na wabunge wa aina hii. Napata mashaka kwamba inawezekana kumbe tatizo sio TANESCO au serikali, na kwamba huenda tatizo ni aina ya wabunge tulionao. Mana inapofika mahala Mzee Shellukindo na wenzake wanataka kutuaminisha kuwa mazingira ya mikataba hii(DOWANS na IPTL) ni tofauti lakini wameshindwa kutueleza tofauti hiyo ni ipi?Inatisha. Ninachojua na kuamini ni kwamba; Yote ni mitakaba ya kifisadi, Yote ni mitumba. IPTL ni mitumba ya tangu mwaka 1990, wakati DOWANS ni mitumba ya tangu mwaka 2006.
Tumeambiwa kuwa sheria ya manunuzi ya mwaka 2004 anakataza kununua mitambo ambayo ni mitumba. Lakini katika maelezo ya Mh Zitto Kabwe, TanzaniaDaima ya Jumatano,Machi11,2009, Mh Zitto Kabwe anasema hakuna sheria inayokataza kununua mitambo ambayo ni mitumba, na kwamba kinachokataza ni kanuni(regulations), sio sheria(laws).
Hapa napo ninapata shida. Kwani machi4, 2009 Bwana Mwakyembe ambaye ni daktari wa sheria alisisitiza katika kipindi maalumu kuhusu suala hili, kilichorushwa ITV akijenga hoja kuwa Zitto kabwe anataka sheria ya manunuzi iliyotungwa na bunge ivunjwe ili mitambo ya Dowans inunuliwe haya ni maneno yanayotia hasira, mana bunge ni chombo na mamlaka kubwa sana. Na sheria ya nchi ni kitu kikubwa sana . Sasa swali ambalo Daktari wa sheria, Bwana Mwakyembe hajajibu ni kama kweli aliupotosha Umma kwa makusudi au bahati mbaya kwamba sheria ya manunuzi(ambayo kimsingi inatungwa na bunge) haizungumzii kutonnunua mitumba bali kanuni (ambazo kimsingi zinatungwa na waziri) ndio zinazungumzia kutonunua mitumba.Sisemi kwamba watanzania wapo tayari kuingia gizani ili kulinda sheria ya manunuzi kama ingekuwepo kama kikwazo, bali ninachosema ni usahihi wa kipi kinakataza kununua mitumba; sheria ya nchi au kanuni ya wizara?
Ni muhimu sana mjadala huu ukaachwa uchukue sura ya kitaalamu zaidi kuliko hivi tunavyokwenda kisiasa mno ihali siasa zetu bado changa na hajiwa za kitaaluma vya kutosha. Maana kama tutaenda hivi hasara yake ni kuacha umma upoteze mwelekeo katika mambo ya msingi. Ndio maana nakubaliana kabisa na hoja iliyotolewa na gazeti maarufu Afrika Mashariki-The east Africa la machi 09-15, 2009 ambapo mtaalamu aliyebobea katika masuala ya nishati pale benki ya dunia, Bwana Ralph Karhammar alisema mjadala unaendelea kati ya makao makuu ya benki Washington na mwakilishi wa benki hiyo wa Dar es Salaam kupima athari za mgawanyiko kati ya kambi hizo mbili na kuongeza kwamba Suala la ununuzi wa mitambo ya DOWANS limebebwa na siasa kiasi cha kuvuka mijadala ya kitaalamu na Kwa mujibu wa gazeti hilo, linasema kuwa Vyanzo vya karibu na Benki ya dunia vinaonesha kwamba benki ya dunia inakubaliana na hoja za kambi inayounga mkono ununuzi wa mitambo ya DOWANS ili kupunguza uhaba wa umeme ambao kwa sasa unafikia mapungufu ya kiasi cha 192 MW
Kauli ya Mtaalamu huyu wa Benki ya dunia inanikumbusha umuhimu wa azimio la Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma chini ya Mh Zitto Kabwe waliopendekeza Kamati mbili, ile ya Hesabu za Mashirika ya Umma na ile ya Nishati na Madini zikutane ili kupata mwafaka kwa kupambambanua tatizo hili kwa kina. Na huu ndio msimamo ulioungwa mkono hata na Dk Willibrod Slaa alipohojiwa na ITV kwamba kwakuwa Kamati hizi mbili ndizo zenye taarifa za TANESCO ni vema zingekutanishwa ili kubadilishana mawazo na uzoefu kabla ya kuishauri serikali juu ya uamuzi wa kufanya kwa sasa.
Najua wengine wanaweza kusema kwamba Spika Sitta ameshasema kanuni haziruhusu Kamati mbili kukutana. Sawa. Lakini ni muhimu tukumbuke tu kwamba Spika Sitta alichosema ni kwamba hakuna mahala kwenye kanuni panaporuhusu Kamati mbili kukutana. Kwahiyo kanuni ipo kimya. Ndio maana mi nahoji, Hivi kanuni zikiwa kimya inakuwa zimekataza au zimeruhusu?
Maana akili ya kawaida inaniaminisha kwamba kanuni za bunge sio msahafu wala biblia, vitabu ambavyo tunaamini vimekamilika. Ndio sababu katika mazingira mengine kinachotumika ni ama busara ya Spika wa bunge au uzoefu wa maamuzi yaliyokwishafanywa au yanayofanywa katika mabunge ya Jumuiya ya madola
Kimsingi kama hakuna kinachofichwa wala kutafutwa hapakuwa na sababu za kwanini Spika asiruhusu Kamati hizi mbili kukutana tena kwa suala nyeti na linalottikisa siasa za nchi yetu kiasi hiki. Nasema hivyo kwasababu kuna wengi waliposikia Spika amesema kanuni haziruhusu walifikiri kabisa kwamba kuna sehemu ya kitabu cha kanuni za bunge inakaza kamati mbili kukutana au kutokutana . Kumbe hoja ni kwamba hakuna kipengele kinachozungumzia uhalali au uhalamu wa Kamati mbili za bunge kukutana.
Ni katika misingi hiyo, busara ya kawaida zinazonesha kwamba uamuzi sahihi ilikuwa ni kwa Kamati mbili hizo kukutana badala ya kamati hizo mbili pamoja na Spika wao wa bunge kulumbana kwenye magazeti kiasi cha kutilia mashaka kama kweli bunge letu lina viwango na speed tuliyoahidiwa na Spika Sitta!..Tatizo limejitokeza, Kamati inayohusika na sera imeshafanya maamuzi, lakini inaelezwa bila kuhusisha TANESCO. Kamati ya hesabu za Mashirika ya Umma ikiwa ni pamoja na TANESCO, limepitia hali ya TANESCO kifedha inaona kuna tatizo(kwasababu TANESCO inatumia asilimia 84 ya mapato yake kulipia asilimia42 ya umeme inaopata toka makampuni), TANESCO wanaeleza msingi wa tatizo lakini Kamati ya Mahesabu inaona msingi wake upo kisera, inaogopa kufanya maamuzi ili isigongane na Kamati nyingine ya Nishati na Madini.Uamuzi ambao ni wa busara! Lakini cha kushangaza alianza Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini Bwana Shellukindo kukataa mwitto huo akifuatiwa na Makamu wake, Dk Harrison Mwakyembe na kuhitimishwa na Spika Samweli Sitta, wote wakikataa!
Katika mazingira hayo, ndipo watu walio huru kifikra wanaona kwamba pengine kuna tatizo la ziada. Mana kama kweli umeme ni tatizo, na Kama Kamati moja inaomba kukutana kujadili, Tatizo liko wapi?.... hata kama kila moja itakuwa na msimamo wake, si ndio utapatikana ufumbuzi kwa kuchanga mawazo ya pande mbili? Spika aliogopa nini kukubali Kamati mbili zikutane?.
Kama kanuni hazisemi kuruhusu , je ni kweli maamuzi yote ya bunge yanafanywa kwa mujibu wa kanuni kusema? Kama Kamati ya akina Dk Harrison Mwakyembe na Shellukindo inazo hoja za msingi, si ndio ingezitumia kuishawishi Kamati ya akina Zitto Kabwe?..Mana kitendo cha Spika Sitta kuzuia Kamati hizi mbili kukutana ndio kumesababisha dunia nzima kujua kwamba Kamati mbili za bunge zinavutana kufuatia sakata la DOWANS.kitu ambacho hakikuwa na ulazima wowote..na sasa kimezidi kuzusha maswali mengine ya ziada kuhusu misingi ya mvutano huo.
Nimesema maswali mengi yameanza kuibuka kwasababu, ni hivi karibuni tu, gazeti la Mtanzania Jumapili, liliandika habari kwamba Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Bwana Harrison Mwakyembe ni mmoja wa wamiliki wa mradi wa umeme wa POWER POOL EAST AFRICA LTD, yenye usajili wa BRELA Na 49624 na kwamba kwa thamini ya hisa alizo nazo kufikia mwaka 2007 ni karibu bilioni1.5. Sasa swali linalojitokeza hapa ni ile hoja ya mgongano wa maslahi.
Kwamba mtu anayelilia TANESCO impe biashara ya kuiuzia umeme ndo anapewa kazi ya kusimamia sera ikiwa ni pamoja na kuangalia mwenendo wa miradi ya Umeme..Sipindi kwamba Dk Mwakyembe asifanye biashara ya miradi ya Umeme kwasababu yeye ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Kamati ambayo inatazama mwenendo wa miradi ya Umeme nchini na mwelekeo wa Shirika la Umeme kwa ujumla wake. Ninachosema, na ambacho kanuni za bunge; ile ya 61(1) na ile ya 114(19) ni umuhimu wa mbunge mwenye maslahi katika jambo husika kutangaza kuwa ana maslahi na kiasi cha maslahi hayo. Kitu ambacho Mwalimu wetu Dk Mwakyembe hajafanya tangu awe mbunge.Kwanini hajasema? Anajua yeye!
Ndio maana ni rahisi kuhusisha msimamo wa Dk Harrison Mwakyembe pengine na kushindwa kwa kampuni yake kupewa mradi wa kuzalisha umeme na TANESCO hata kama inawezekana tuhuma anazotoa dhidi ya shirika hilo ni za kweli. Na endapo atapewa mradi na kubadili msimamo ni rahisi kuhusianisha masimamo huo kwa mabadiliko hayo, kitu ambacho sio afya kwa mwanasiasa. Siandiki hivi kwa kupuuza kazi ya Dk Mwakyembe kwa Taifa hili, la hasha! Natambua mchango wake, nathamini mchango wake. Ninachokifanya hapa ni kujaribu kuwekana sawa tunapojadili mijadala mikubwa kama hii ili siku moja tufikie viwango vya kujadiliana maswala na maswali makubwa ya kitaifa bila harufu ya maslahi binafsi ambayo sasa harufu yake imeanza kudhihiri.
Ni muhimu tujue kwamba watu sio mawe. Leo anaweza kuwa hivi, kesho akawa vile. Ni Dk Mwakyembe huyuhuyu aliyetukana waandishi wa habari mwaka 2006 kwasababu za kulinda alichotaka kulinda, na Ni Dk Mwakyembe huyuhuyu aliyeponda harakati za wanazuoni kudai haki zao mwaka 2007, kiasi cha Dk Willibrod Slaa kwa uchungu, alipokuwa akihutubia wanazuoni wa mkoa wa Morogoro kwenye Kongamano kuhusu Elimu ya juu nchini, akioneshwa kusikitishwa kwake na mchango wa Dk Mwakyembe bungeni kuhusu elimu ya juu alisema Elimu zingine bora wangepewa mbwa. Ndio maana nakubaliana na Falsafa ya Profesa Shivji! Kwamba Tilia mashaka kila kitu.