Tamko la Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunnah Tanzania (BASUTA) kuhusu mkataba baina ya Tanzania na DP World

The Sunk Cost Fallacy 2

JF-Expert Member
Nov 8, 2022
7,382
8,437
Helo Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunna Tanzania (BASUTA) Wameshutumu Vikali kile wamepita Undumilakuwili na Ukosefu wa Uadilifu Kwa Wanaopinga mkataba wa Bandari kwa kile wameita kugumbia macho Mikataba ya hovyo iliyowahi ingiwa hapo kabla.
---

Tamko la Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunna Tanzania (BASUTA) likielezea kuhusu makubaliano ya uendeshaji na uendelezaji wa bandari."

BASUTA haturidhishwi na 'undumilakuwili' na ukosefu wa uadilifu wa wapingaji wa mkataba ambao walifumbia macho mikataba mingi ya hovyo huko nyuma katika sekta mbalimbali ikiwemo madini na hawakutaka ifutwe lakini wako tayari kwa gharama yoyote kuhakikisha mkataba huu unafutwa na unakufa".
---
TAMKO LA BARAZA KUU LA JUMUIYA ZA ANSAAR SUNNAH TANZANIA (BASUTA) KUHUSU MKATABA BAINA YA SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA SERIKALI YA DUBAI KUHUSU USHIRIKIANO WA KIUCHUMI NA KIJAMII KWA AJILI YA UENDELEZAJI NA UBORESHAJI WA

UTENDAJI KAZI WA BANDARI TANZANIA

MJADALA WA MKATABA WA BANDARI USITAWALIWE NA UZUSHI NA CHUKI ZA KIDINI

Utangulizi
a) Kwa kuwa katiba ya nchi yetu ya mwaka 1977 toleo la 2000 ibara ya 18 (1) na 19 (1) zinatoa haki ya kila mtu kuwa na uhuru wa kuwa na maoni yake na kutoa nje mawazo yake;

b) Kwa kuwa katiba yetu inatoa haki sawa kwa raia wote pasina ubaguzi wowote kwa misingi ya dini, rangi, kabila, jinsia au vyovyote vile;

c) Kwa kuwa watu wengine wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini, wanataaluma, wanahabari na wadau wengine wamekuwa wanatoa maoni yao kuhusu suala la Mkataba baina ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na serikali ya Dubai kuhusu Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii kwa ajili ya Uendelezaji na Uboreshaji wa Utendaji kazi wa Bandari Tanzania kupitia kampuni ya DP World inayomilikiwa na serikali ya nchi hiyo;

d) Kwa kuwa katika mijadala hiyo kumekuwa na upotoshaji mwingi wa makusudi wa matukio na taarifa kuhusu Mkataba huo wa bandari kwa chuki au kwa ajili ya kutetea maslahi binafsi ya kiuchumi, kisiasa au ya kidini ya makundi fulani

e) Na kwa kuwa na sisi, BASUTA, ni Watanzania, viongozi wa taasisi ya dini, kama ilivyo kwa viongozi madhehebu mengine yaliyotoa maoni.

Hivyo basi, sisi viongozi wa Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunnah Tanzania (BASUTA) kutoka sehemu mbalimbali nchini Tanzania, kwa kujali maslahi mapana ya taifa, tumeamua leo Agosti 23, 2023 kutoa tamko letu kuhusu mwenendo wa mjadala wa Mkataba huo wa bandari, kama ifuatavyo:

Maoni Yetu

1.0 Kuhusu maudhui ya Mkataba wenyewe

a) Kwa kuwa, tunaamini Serikali kupitia wataalamu wake imetoa ufafanuzi wa kutosha kwa wadau wanaokosoa baadhi ya vifungu vya Mkataba huo na hivyo kutaka yafanyike maboresho na kundi jingine (ambalo hatukubaliani nalo) linalopinga Mkataba wote;

b) Na kwa kuwa wanaopinga Mkataba wote na kutaka ufutwe, walifungua kesi Mahakama Kuu ya kuomba tafsiri ya kisheria ambayo, kama utawala sheria unavyotaka, ilisikilizwa kwa haki na uwazi; kisha hukumu kutolewa kwamba, licha ya kasoro ndogo ndogo Mkataba huu ni halali kwa mujibu wa sheria za nchi na unaweza ukaendelea.

c) Na kwa kuwa serikali sikivu ya awamu ya sita, inayoongozwa na Rais Dr Samia Suluhu Hassan imeahidi kusikiliza na kurekebsha kasoro zote zilizoainishwa kwa maslahi ya taifa.

Hivyo basi, sisi BASUTA tusingependa kujikita kwenye mjadala wa vipengele mahususi wa Mkataba wenyewe wa bandari tukiamini mchakato unaenda vizuri na maslahi mapana ya taifa yatafikiwa.

2.0 Katika mjadala wa Mkataba huu, BASUTA haturidhishwi na undumilakuwili na ukosefu wa uadilifu wa wapingaji wa Mkataba ambao walifumbia macho mikataba mingi na ya hovyo zaidi huko nyuma katika sekta mbalimbali, ikiwemo madini, na hawakutaka ifutwe; lakini wako tayari kwa gharama yoyote kuhakikisha Mkataba huu unafutwa na unakufa. Wanasahau kuwa huu si Mkataba wa kwanza wa ukodishaji wa uendeshaji bandarini, bali awali ilipewa jukumu hilo kampuni ya TICTS na kufanya kazi hiyo kwa miaka takriban 22. Hadi TICTS inaondoshwa, hakujawahi kuwa na mijadala ya hisia kama hii kupinga sera za uwekezaji na eti kutaka Watanzania wenyewe ndio waendeshe rasilimali zao, kama lilivyodai kanisa Katoliki na wadau wengine.

3.0 BASUTA tunatambua na kuheshimu haki ya makundi ya watu wakiwemo wanasiasa, madhehebu ya dini, wasomi na wanahabari, kuwa na maoni, lakini haturidhishwi na baadhi ya hoja za kibaguzi dhidi ya Uarabu, na hata Uislamu zinazotolewa na makundi yanayotaka Mkataba huu wa bandari ufutwe. Badala ya kauli kama vile “Hatuwezi kuwapa Waarabu bandari zetu”, tunadhani jambo bora na la busara ni kujikita kwenye vipengele vya Mkataba kuainisha maeneo yenye udhaifu ili serikali iangalie namna ya kuboresha.

4.0 Vilevile, BASUTA inashangazwa na kusikitishwa na upotoshaji wa makusudi wa baadhi ya mambo katika mjadala wa Mkataba huu wa bandari, licha ya ufafanuzi uliotolewa na serikali, ikiwemo madai kuwa bandari inauzwa, DP World wanapewa waendeshe bandari zote na mengineyo.

Kipekee, tunasikitishwa sana na kauli isiyo na ushahidi wa kidodoso wa Kanisa Katoliki iliyodai eti wananchi wengi wanapinga Mkataba na wanataka ufutwe, ilihali hakuna utati kuhusu hilo uliofanyika.

BASUTA inashangazwa zaidi na makundi ya wapingaji kutotaka kusikiliza hoja zozote za ufafanuzi na kung’ang’ania misimamo.

Tunajiuliza, tatizo ni Mkataba tu au kuna waliyoyaficha vifuani mwao?

5.0 BASUTA tunasikitishwa na lugha za shinikizo na vitisho vya kuiangusha serikali kwa maandamano, fujo na vitendo vya jinai na uhaini. Iwapo kila kundi litataka matakwa yake yatimizwe kwa njia hizo, nchi inaweza kutumbukia katika machafuko makubwa.

Katiba inazungumzia haki ya kutoa maoni na kusikilizwa lakini haisemi lazima yafuatwe.

Utayari wa baadhi ya watu kuvuruga amani ili yao yatimie unazidi kutupa wasiwasi kuwa tatizo hasa sio Mkataba tu bali kuna chuki zilizojicha. Kwa kuliona hili, BASUTA tunatoa wito wa kuheshimiwa utawala wa sheria, hususan mfumo wa kukiwa maamuzi ya kiserikali katika uendeshaji wa nchi, kama yalivyoanishwa katika Katiba na Sheria za nchi kupitia vyombo rasmi kama Serikali, Bunge na Mahakama.

6.0 BASUTA imefurahishwa na kauli ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Dr Samia Suluhu Hassan aliyoitoa Agosti 21, 2023 wakati akihutubia katika

sherehe za miaka 60 ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) ya kuonesha

msimamo imara wa serikali na utayari wa kupambana na wanaotishia kuvuruga amani, pale aliposema: “Hakuna mwenye misuli na ubavu wa kuligawa taifa hili…. wa kuivunja amani ya nchi yetu.”

7.0 Pamoja na kufurahishwa na msimamo wa Serikali, BASUTA tunaipa rai isikubali kuendeshwa kwa shinikizo la kundi lolote la kisiasa, kidini au kijamii na kufanya maamuzi kwa kutii matakwa ya kundi hilo kwani kwa kufanya hivyo itaendeleza mbegu mbaya iliyopandwa huko nyuma, ikamea na kuzaa tabaka la watu (wa aidha chama au dhehebu moja la dini) ambao ni raia zaidi kuliko wengine, na hivyo kuwa na kura ya

‘Veto’ katika maamuzi. Watu hao wasipolitaka jambo haliwi na wakilitaka huwa – tena kwa sababu ya maslahi yao binafsi.

8.0 Kwa msingi wa tuliyoyataja katika 4.0, kuhusu kauli za ubaguzi, tunawahimiza Watanzania wenzetu hususan viongozi wa dini, ambao kauli zao ndiyo hatari zaidi kwa sababu ya ushawishi mkubwa walionao, kujiepusha na matamko ambayo yanaweza kuipelekea nchi yetu katika laana ya uvunjifu wa amani kama ilivyotokea Rwanda 1994 na nchi nyingine.

Tunakumbusha kuwa katika baadhi ya nchi hizo, mambo yalianza hivi hivi kwa nyaraka namatamko ya kichungaji. BASUTA tusingependa kuyaona hayo yakitokea katika nchi yetu na tunatoa rai kwa serikali na vyombo vyake vya usalama viwe makini sasa kuliko wakati wowote ule.

9.0 BASUTA, kama tulivyotaja awali, tunaamini katika ukosoaji wenye afya wa kutaka maboresho ya baadhi ya vipengele vya Mkataba na sio upingaji wa jumlajumla wa kuukataa Mkataba wote.

Tunaamini aina ya pili ya upingaji unachangiwa zaidi na hisia kuliko hoja za msingi kwa ushahidi wa wazi wa kauli za chuki na ubaguzi dhidi ya Uarabu zinazotolewa na baadhi ya watu hususan mitandaoni na pia kwa ushahidi wa kampeni kubwa ya ‘kiimani’ ya Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC) kupinga Mkataba huu kupitia kanisani.

Kwa msingi huo, BASUTA tunatoa rai kwa TEC na makundi mengine kutafakari upya misimamo yao kwa maslahi ya taifa na waweke pembeni hisia. Wakifanya hivyo, watagundua kuwa huu siyo Mkataba wa kwanza wa aina hii duniani na hata hivyo ipo nafasi ya maboresho. Pia, nchi nyingi duniani za Wakristo tena Wakatoliki zinafanya kazi na DP World zikiwemo Angola kupitia bandari ya Lobito yenye urefu wa kilometa 7.2 wakati gati la Dar es Salaam linalokusudiwa lina urefu wa kilometa 2 tu.

Pia, zipo nchi kama Msumbiji kupitia bandari ya Beira, Brazil na Ufiilipino.

Hivyo, mikataba ya DP World na nchi hizi itoshe kuwahikikishia kuwa uwekezaji huu unahusu biashara yenye tija kwa taifa, na sio kitu kingine.

10.0 BASUTA, tunaungana na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, kutahadharisha dhidi ya tabia ya kutumia majukwaa ya dini kwa maslahi ya siasa au kinyume chake, kwani kufanya hivyo kunaweza kuleta uvunjifu wa amani na kuharibu utulivu wa taifa.

Katika suala hili, tumesikitishwa kuona TEC inaendesha kampeni kubwa za kanisani kupinga Mkataba.

Iwapo mamlaka za dini nyingine zikianza kampeni kutetea Mkataba katika nyumba zao za ibada, tuna wasiwasi suala hili la kiuchumi halitaamuliwa kwa uzito wa hoja bali ufuasi wa dini.

Mheshimiwa Kikwete alionya: “Siku ikika uanachama wa chama cha kisiasa au uumini thabiti wa dini ukawianishwa na chama cha kisiasa anachokifuata ndiyo mwisho wa nchi yetu…kutakuwa na chama cha siasa cha Wakristo, cha Waislamu vyama vya siasa vya Walokole.

Kuwafanya Watanzania kuyatazama masuala ya kisiasa, Serikali na utawala kwa mtazamo wa dini zetu ni jambo hatari.”

11.0 Kwa kuwa imeibuliwa hoja ya ukomo wa Mkataba wa bandari, BASUTA inatoa wito wa kufanywa mapitio ya mikataba mingine isiyo na ukomo, ikiwemo ule ulioingiwa mwaka 1992 kati ya Serikali na makanisa (Memorandum of Understanding) ambapo sehemu ya mabilioni ya walipakodi, hata wasio Wakristo, hutolewa na serikali kwa ajili ya hospitali na vyuo vikuu vya makanisa hayo. Pia, tunataka makubaliano yanayozungumzwa mara kwa mara kati ya serikali na kanisa ya kutojengwa hospitali za umma mahali zilipo hospitali za makanisa yafutwe kwa sababu wananchi wana Mkataba na Serikali kuwakishia huduma za jamii kwa gharama wanayoweza kuzimudu na sio kanisa.

12.0 Hata hivyo, kwa ujumla, BASUTA inaungana na msimamo wa Serikali, Bunge na Mahakama Kuu kwamba Mkataba huu siyo tu ni sahihi bali pia ni muhimu kwa maslahi ya nchi.

Uwekezaji wa kampuni kubwa yenye uwezo wa mkubwa wa kimitaji na kiteknolojia, na yenye uzoefu na weledi kama DP World ya Dubai utaleta ufanisi katika biashara ya bandari hasa katika mazingira ya sasa ya ushindani mkubwa uliopo, na hivyo kuliwezesha taifa kuvutia nchi nyingi kutumia bandari zetu kupitisha mizigo yao na kuliingizia taifa mapato makubwa.

Angalizo:
Kuhusu vipengele vya mkataba wa bandari, majadiliano mengi yamefanyika huko nyuma na serikali Imeshatoa ufafanuzi dhidi y aupotoshaji unaofanywa hivyo BASUTA haikujikita katika mawanda hayo.

Hitimisho
Kwa maslahi ya umoja, mshikamano, utulivu na ustawi wa nchi yetu, tumetoa tamko letu hili kwa nia njema kabisa kwa maslahi ya nchi yetu na Watanzania wote pasina kujali dini, rangi, kabila, jinsia wala tofauti zao za kisiasa.

Tanzania ni kubwa kuliko sisi sote na wala baadhi yetu wasijitwishe ukiranja wa kuwasemea wengine ilhali wako hai na wanazo haki za kiraia kama walizo nazo wao.

Mungu Ibariki Tanzania.

1692890462816.jpeg

1692890476075.jpeg

My Take
TEC wamechokonoa vingi.
 
Tamko la Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunna Tanzania (BASUTA) likielezea kuhusu makubaliano ya uendeshaji na uendelezaji wa bandari."BASUTA haturidhishwi na 'undumilakuwili' na ukosefu wa uadilifu wa wapingaji wa mkataba ambao walifumbia macho mikataba mingi ya hovyo huko nyuma katika sekta mbalimbali ikiwemo madini na hawakutaka ifutwe lakini wako tayari kwa gharama yoyote kuhakikisha mkataba huu unafutwa na unakufa.
 
Helo Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunna Tanzania (BASUTA) Wameshutumu Vikali kile wamepita Undumilakuwili na Ukosefu wa Uadilifu Kwa Wanaopinga mkataba wa Bandari Kwa kile wameita kugumbia macho Mikataba ya hovyo iliyowahi ingiwa hapo kabla...
Kama mktaba gani wauweke hapa wazi ili great thinkers wawape darasa walilonyimwa tena kwa bure tu
 
Helo Baraza Kuu la Jumuiya za Ansaar Sunna Tanzania (BASUTA) Wameshutumu Vikali kile wamepita Undumilakuwili na Ukosefu wa Uadilifu Kwa Wanaopinga mkataba wa Bandari Kwa kile wameita kugumbia macho Mikataba ya hovyo iliyowahi ingiwa hapo kabla...
Binafsi, anayewapinga TEC, kama hachambui vipengele vya mkataba against tamko la TEC, NAMWONA HANA AKILI..!!
 
Back
Top Bottom