Wana JF na Wanyamwezi wenzangu popote pale mlipo.
Kumekuwa na lawama nyingi sana kwetu sisi Wanyamwezi na haswa Wadakama wa Mkoa wa Tabora kuwa tumekuwa kichaka cha CCM kuja kujificha. Sisi tumekuwa ndiyo kimbilio la CCM kuja kupata kura za bure na kuchakachua matokeo. Sisi ndiyo tumeonakana kuwa tumekuwa Muhuli wa kuiingiza CCM madarakani na Rais wake kumuweka Ikulu.
Nakumbuka kusoma makala za wana JF kadhaa zikihimiza vyama vya upinzani kuhamia Tabora mara kwa mara na kutoa shule/somo la Utaifa au Uraia. Ombi hili lilikuwa likikubaliwa ila kutekelezwa imekuwa ni shida. Labda kwa sababu gharama ni kubwa, sijui maana mie sipo ndani ya chama.
Kwa mfano tuangalie uchaguzi wa mwaka 2010, nilisubiri sana kuona Dr. Slaa akienda Sikonge kuwaona Wanyamwezi wa huko. Nikashangaa kumuona Kikwete tu na huku ikiwa mara yake ya ngapi sijui kufika huko. Tabora umeme wenyewe wa shida na hivyo mawasiliano inakuwa ngumu. Pia media nyingi za Tanzania tunajua jinsi wanavyotangaza kile kinachotakiwa kusikilizwa na Watu wa Chama na Serikali ya CCM.
Tuangalia matokeo ya Uchaguzi mdogo wa Nzega wa mwaka jana na mwaka 2010 mtagundua kuwa kuna tofauti kubwa sana. Rostam Azziz alikuwa kama Mungu huko Igunga ila Chadema walipoenda huko na kujikita kisawasawa, basi mambo yamebadilika kabisa. Nafikiri mmeona jinsi Igunga ilivyopata Mwamko ghafla na kuwa sasa moja ya ngome imara ya Chadema ingawa uchaguzi Chadema ilishindwa kwa kuchakachuliwa.
Si kweli kuwa ni Wanyamwezi tu ndiyo wajinga kiasi hicho. Ukiangalia hata uchaguzi wa Arumeru ambako watu wamepata somo la Uraia kwa siku nyingi, wameona kwenye TV na kusikia kwenye Radio na uzuri wa wenzetu wa huko hata kipato chao kipo juu zaidi na Mwamko wa Kisiasa na maisha yapo juu zaidi, bado watu zaidi ya 26,000 wameichagua CCM. Watu pamoja na ugumu wa maisha na kuonyeshwa kabisa mbaya wao ni nani na kushuhudia matusi ya akina Mkapa, Lusinde nk lakini bado 26,000 wamekichagua CCM.
Sasa mnategemea nini kwa watu wa kijiji changu nilipozaliwa cha Mkolye (katikati ya Tutuo na Sikonge) wamchague Slaa ambaye hawajawahi hata kumuona zaidi ya kumsikia? Wanamsikia tu Zitto Kabwe, Sugu, Mnyika, Lema nk. Kwao wao, ni heri wamchague Kikwete na CCM yake maana mara moja moja wanakuja na Magari yao makubwa mazuri, wamependeza na kunawiri. Wanatuahidi na sisi tunaweza kupendeza tukiwachagua na kwa sababu kila mtu anapenda KUOTA ndoto za alinacha, basi walau tunakuwa tumeshaona kuwa ukiota basi ota na wewe umekuwa Dereva wa gari zuri la Kikwete au hata Tarishi ofisini na kwenye msafara maana upo ndani ya suti nzito.
Lawama nyingine kwa upande fulani ntaomba tuzielekeze kwa Chama cha Chadema na upinzani kwa ujumla kwa kuiacha Tabora na Wanyamwezi kama Mwana mpotevu. Kama kweli Chadema inajiandaa kuchukua nchi, basi labda niseme tu jambo moja fupi na muhimu sana:
Wanyamwezi ni kama Maharage ya Mbeya. Si wagumu kiasi hicho kubadilishwa. Ukiwaweka sana na kuwaonyesha jinsi wanavyoibiwa na KULIWA SANA wakati wao wakila kidogo au kutokula kabisa, basi watabadilika. Ningelisisitiza Chadema wahahamishe kambi walau kwa wiki mbili mkoani Tabora na kushusha shule ya kufa mtu wakati wa kiangazi ukifika. Uzuri ni kuwa kidogokidogo, watu wameanza kuamka na kudai haki zai ila woga bado ni mkubwa sana. Serikali za mitaa na vijiji zina nguvu sana na vitisho kwa mtu yeyote aliye nje ya CCM. Na mbaya zaidi ni pale unapohamia UPINZANI, hapo unakuwa umejipalia moto.
Kama mnavyozunguka mara kwa mara, Arusha, Mbeya, Mwanza, Moshi nk basi mjitahidi na Tabora muwe mnafika mara moja moja. Nina imani kabisa kwa wimbi la mabadiliko linaloendelea sasa, mgomo wa Madaktari, huduma mbaya za afya na maendeleo zinazochangiwa na ukosefu wa fedha serikalini, Chadema ni mtaji mkubwa kabisa wa kuwaambia Wanyamwezi mambo haswa yalivyo na kuwakumbusha kuwa wanaibiwa na wabadilike.
Hebu fikiri ni mikutano mingapi ya hadhara imeshafanyika huko Tabora tangu uchaguzi ufanyike. Ukiacha Igunga ambapo kambi ya Chadema ilihamia, sijawasikia wakija na lile gari lao la kuhutubia mkoani Tabora na kuzungukia walau TARAFA zote za Tabora.
Nafikiri sababu nyingine kwa nini vyama vya upinzani havijali sana Tabora ni idadi ndogo ya watu. Wilaya mbili kubwa za Arusha, zinaweza kuwa na watu wengi zaidi ya Tabora kwa ujumla. Sasa hapo linakuja swali, je kuna haja ya kupoteza muda huko? Kwa kura za Rais, ndiyo hakuna haja ila kwa Wabunge, ni kuwa Chadema inapoteza sana.
Kutokana na idadi kubwa ya Waislaam, CUF ndiyo ilikuwa na uwezo mkubwa sana kushinda Tabora ila CUF ni chama ambacho wenye nacho wameamua kuhakikisha kinakufa taratibu na kuzikwa na ndiyo maana sijakitaja hapo juu na kuachia tegemeo kubwa kwa CHADEMA.
Tafadhali tafadhali uongozi wa Chadema, nendeni Tabora na mkashushe somo la Uraia sasa. Watanzania wanazidi kuamka na si kweli kuwa Wanyamwezi wote wamelala. Mkijipanga vizuri, Mwaka 2015, Chadema inaweza kusinda uchaguzi wa Rais na Bunge. Zimebaki miaka 3 ikiwa na maana muda hautoshi. Fanyeji juhudi kwa kutafuta watu mapema kujenga vyama huko Tabora na mwaka 2015 kuwasimamisha kama Wagombea Udiwani na Ubunge wa Majimbo yote ya Tabora.
CCM ni chama kizuri sana ila kimepotea njia. Inabidi mtu akisimamishe, kirudi sehemu kilipoanza kupotea na akirudishe kwenye njia sahihi. Kitapendeza sana kikiwa chama cha upinzani na nina imani ndipo wengi wataona haswa uwezo wa chama cha CCM. Ila kwa leo, hiki chama kimekuwa mbali kabisa na dira ya Nyerere.
Mwisho niseme kuwa MSITUTUKANE WANYAMWEZI kwa kutufunga wote kwenye pakacha moja. Tabora ni zaidi ya Wanyamwezi. Kuna wanyamwezi tumebadilika zaidi ya wale Wameru 26,000 na kuna Wameru wamebadilika zaidi ya Wanyamwezi wanaoichagua CCM. Hata kama ntakuwa Mnyamwezi pekee wa Mkolye ninayechagua mabadiliko, ukitutukana Wanyamwezi, basi utakuwa unafanya makosa. Nafikiri neno zuri la kutumia ni WANA TABORA BADILIKENI maana Tanzania haina mipaka ya ndani na kuna makabila kibao yanaishi Tabora.