Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

ingekua sio utovu wa nidham kwa mtunzi mahiri ningesema hivi 'Bishop ee basi upande huu imetosha tujalie pande za tunu na za sammy na joy' ila siwez kusema naheshimu sana na kushukuru sana mtunzi mwema.
 
Taxi - (148)

ILIPOISHIA

“Mr. Oduya, you are not serious, brother! Unadhani utaua wangapi?” yule kigogo wa polisi alisema huku akimtazama Mr. Oduya kwa mshangao. Kisha kikaibuka kitambo kifupi cha ukimya, kila mmoja alionekana kufikiria kwa muda na kushusha pumzi.

“Sioni namna nyingine ya kufanya ili kuepuka janga hili, kumbuka kuwa akizidi kuchimba kiundani basi hata wewe huwezi kukwepa kwenye hili, ndiyo maana nadhani kuwa yeyote atakayekaa mbele yetu anapaswa kunyamazishwa haraka!” Mr. Oduya alisema baada ya kitambo kile cha ukimya.

“Hapana, sidhani kama kuua litakuwa jambo jema, kwani hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwako kuliko hata kwangu!” yule kigogo wa polisi alishauri.

“Sasa tutafanyaje wakati naona maji yanaanza kuzidi unga?” Mr. Oduya aliuliza kwa sauti yenye mchanganyiko wa hasira na wasiwasi.

Yule kigogo wa polisi aliwaza kidogo kisha akasema, “Wacha niende, hadi nikifika ofisini kwangu nitakuwa nimeshapata jibu!” yule kigogo wa polisi alisema kisha akaangalia huku na kule ili kuhakikisha hakuna mtu aliyemwona, akashuka haraka toka ndani ya gari la Mr. Oduya na kuondoka.

Muda huohuo simu ya Mr. Oduya ikaanza kuita. Mr. Oduya aliitazama kwa makini na kuliona jina la Spoiler. Akaipokea ile simu mara moja na kuipeleka kwenye sikio lake. ”Niambie!” alisema kwa sauti tulivu huku akiilamba midomo yake iliyoanza kukauka.

“Nimekamilisha kila kitu, mzee. Casmir amekufa,” Spoiler alisema kwenye simu kwa sauti ya ushindi.

“Una uhakika?” Mr. Oduya aliuliza kwa sauti iliyoonesha kutoamini kile alichokuwa akiambiwa.

“Ninao uhakika, mzee... daktari aliyekuwa anamhudumia ndiye ameifanya kazi hiyo kwa umakini na amenihakikishia. Nimetoka kuongea naye sasa hivi kwenye simu, ameniambia kuwa Inspekta Abel amechanganyikiwa kwelikweli baada ya kuambiwa kuhusu kifo cha Casmir!” Spoiler alisema huku akiachia kicheko hafifu.

ENDELEA...

“Okay, hiyo ni habari nzuri. Sasa nataka na yule binti anayejiita mpelelezi wa kimataifa naye afuate njia hiyo hiyo. Hakikisha anapatikana kabla jua halijatua,” Mr. Oduya alisema kisha simu ikakatwa. Aliwaza kidogo na kutafuta namba ya Robert Kamau kwenye simu yake, alipoipata akapiga simu na kuiweka sikioni. Ile simu ikaita mara tatu na kupokelewa.

“Rob, upo wapi?” Mr. Oduya aliuliza pasipo hata salamu.

“Bado nipo hapa hotelini Udzungwa Beach Resort, nipo na Tom, mkuu,” Job alijibu.

“Naona sasa kazi imekushinda! Umeamua kulala tu, hujui hiyo fedha unayolipwa inatokana na kazi gani?” Mr. Oduya aliuliza kwa hasira na kumfanya Job aduwae kidogo.

“Najua, mkuu,” Robert alijibu kwa sauti tulivu.

Okay, mwambie Tom ninawahitaji haraka sana hapa Paradise Club, mkifika getini jitambulisheni kuwa ni wageni wa PC.008.19, hakikisheni mnafika hapa ndani ya dakika tano tu, hatuna muda wa kupoteza,” Mr. Oduya aliongea na kukata simu.

* * * * *

Saa tatu asubuhi, kwenye sebule kubwa ya kifahari iliyo katika mazingira ya upweke, eneo la Kinyerezi, sebule yote ilikuwa imetulia sana na wanaume watatu walikuwa wakimwangalia Tunu kwa mshangao mkubwa. Macho yao yalikuwa yametulia yakimtazama usoni. Tunu alikuwa ameketi kwenye sofa akiwa amekunja nne na mikono yake ikiwa imepakata laptop yake.

Japo Tunu alikuwa akiwaangalia kwa tabasamu na mwili wake ukiwa umetulia kwenye sofa, lakini moyo wake ulikuwa unakita kwa nguvu kifuani kwake na akili yake ilikuwa mbali sana. Akili yake ilikuwa nje ya zile kuta nne za ile sebule.

Hali hii ilikuwa imejitokeza baada ya wote kushuhudia mambo ya kutisha kwenye ile memory card baada ya kupachikwa kwenye laptop ya Tunu.

Walikuwa wamesikiliza mazungumzo ya simu kati ya Mr. Oduya na kigogo mmoja wa jeshi la polisi, waliokuwa wanapanga mikakati ya jinsi ya kumteka nyara Jaji Lutego kwa kumtumia mwanadada Lisa, na kisha kutekeleza mauaji yake. Yule kigogo wa polisi alibainisha kuwa alikwishaandaa mipango yote na alikuwa na uhakika Jaji Lutego angenasa kwenye mtego.

Jesus Christ!” Bob alijikuta akiropoka kwa mshangao mkubwa baada ya kuyasikia yale mazungumzo. “Una hakika kabisa zile sauti ni za Mr. Oduya na Kamishna Omalla, Mkuu wa Kamisheni ya Intelijensia wa Jeshi la Polisi? Siyo kwamba kuna watu wametumia teknolojia wakatengeneza sauti zinazofanana na zao?”

“Hiki si kitu cha kutengeneza, Bob. Hizi ni sauti zao za kweli. Niliyanasa mazungumzo yao mimi mwenyewe kwa kutumia simu yangu,” Tunu alisema huku akiachia tabasamu.

“Dah! Nimeishiwa kabisa nguvu!” Bob alisema huku akipiga mluzi mdogo, mshangao ulikuwa bado haujamtoka usoni.

Baada ya yale mazungumzo ya simu kati ya Mr. Oduya na kigogo wa jeshi la polisi, Tunu aliwawekea video iliyomwonesha Jaji Lutego akipata mateso makali na baadaye kuuawa kinyama. Katika video hiyo, Mr. Oduya alionekana katika picha ndogo akiwasiliana kwa mfumo wa Videotelephony na watu aliowapa kazi ya kuua, waliokuwa katika eneo ambalo halikujulikana.

Mr. Oduya ambaye hakuwa katika eneo la tukio alionekana akitaka kujionea kwa macho yake jinsi jaji huyo alivyokuwa akiteswa kabla ya kifo chake. Alimsomea Jaji Lutego mashtaka yake kama aliyekuwa mahakamani akihukumu kesi, kisha akawaamuru watu wake kummaliza. Dulla na Uledi wakamwelekezea Jaji Lutego bastola zao, wakammiminia risasi nyingi mwilini na walipohakikisha amekufa wakamwekwa kwenye mfuko na kumpakia kwenye buti la gari aina ya Cadillac DeVille lenye muundo wa kizamani. Haikueleweka mwili wake waliupeleka wapi ule.

Video ile iliishia pale Mr. Oduya mwenye furaha alipotamka, “Good bye, my dear judge. This is a die-or-survive world!

“Na hii video, una uhakika si ya kutengeneza?” Tom aliuliza huku akizidi kushangaa.

“Ndiyo,” Tunu alisema kwa utulivu huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Mimi sina mengi sana ya kutaka kujua isipokuwa hili moja tu... uliwezaje kuyarekodi matukio hayo yote pasipo kushtukiwa?” Tom aliuliza huku akimimina mvinyo aina ya Madeira kwenye bilauri ya Tunu iliyokuwa tupu.

Tunu alimwangalia Tom kwa makini na kuachia tabasamu pana, kisha akawaelezea kisa kizima aliporudi toka Israel na kupata taarifa za mauaji ya rafiki yake Layla, waliyesoma darasa moja katika Shule ya Jangwani, alivyoumia sana kujiingiza kufanya uchunguzi baada ya kuhisi polisi hawakutaka kujishughulisha na kesi hiyo kwa kuwa aliyefanya hivyo alikuwa mtoto wa bilionea.

Alieleza alivyojipenyeza na baadaye kuajiriwa kwenye kampuni ya Mr. Oduya na baadaye kuhamishiwa makao makuu ya kampuni ya The Splendid Group kama mkuu wa kitengo cha ‘tehama’ kutokana na taaluma yake ya Computer System Analysis.

Kwa kutumia laptop yake iliyokuwa na mfumo maalumu wa udukuzi wa taarifa, Tunu aliweza kutengeneza kirusi maalumu aina ya Trojans alichokituma kuiba taarifa za siri za kampuni hiyo baada ya kukituma kwenye kompyuta alizozichagua za kampuni hiyo kikiwa kama keyloggers na RAT (Remote Administration Tools), na aliweza kupata taarifa baada ya mtu kubonyeza kwenye keyboard yake, na bila kujua akawa amekiingiza kwenye mfumo bila kujua na kutuma taarifa zote nyeti kwenye laptop ya Tunu.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus mtugani wa wapi huyo chiqutitta ndukulusudicho ADK aggyd BAHARI J

NB: Litro 👩
 
Taxi - (149)

Hakuishia hapo, alifanikiwa pia kudukua mawasiliano katika simu ya Mr. Oduya na kuweza kusikiliza maongezi yote kutoka simu zote ambazo Mr. Oduya alikuwa anapiga au kupigiwa. Hapo ndipo alipogundua mambo ya kutisha yaliyokaribia kuyagharimu Maisha yake baada ya kugunduliwa kuwa ni shushushu.

“Hebu subiri kidogo, Tunu... How did you get Oduya’s phone?” Tom aliuliza akiwa katika mshangao mkubwa.

“Kwa mtu mwenye taaluma kama yangu ni rahisi sana, wala sikuhitaji hata kuigusa simu yake bali nilihitaji kujua namba yake tu ya simu, kisha nikamaliza kazi,” Tunu alisema huku akitabasamu.

“Sasa walijuaje kama wewe ni shushushu?” Tom aliuliza tena akiwa bado ana mshangao mkubwa.

Ex-boyfriend wangu, Nelson Mtokambali ndiye aliyewafanya watambue kuwa mimi ni shushushu baada ya kunikuta ofisini kwa Mr. Oduya. Sikujua kuwa Nelson alikuwa mshirika na mmoja wa watu wa Mr. Oduya. Tena siku aliyonikuta ndiyo siku ile ile niliyofanikiwa kudukua hizi taarifa,” Tunu alieleza.

“Na hiyo memory card ilifikaje kwenye lile gari la kizamani aina ya Cadillac DeVille?” Tom aliuliza tena akionekana kuwa na shauku kubwa.

“Ni hadithi ndefu kidogo, nitaieleza siku nyingine lakini naomba tu ufahamu kwamba, kama nisingeshtuka mapema huenda sasa ningekuwa marehemu, maana Mr. Oduya ni mtu hatari sana tofauti na wengi wanavyomchukulia,” Tunu alisema na kushusha pumzi ndefu, akanyanyua bilauri ya mvinyo na kugida mvinyo wote uliokuwemo ndani ya ile bilauri, kisha akaikita ile bilauri juu ya meza huku akiusikilizia ule mvinyo ulivyokuwa ukisafiri kwenye koo lake na kutua tumboni.

“Hongera, ulifanya jambo zuri na kubwa sana,” Tom alisema huku akivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu.

This is what I’ve been looking for three years... ni moja ya kazi ambazo zimekuwa ngumu sana kwangu na kukaribia kuyagharimu maisha yangu, lakini siku zote Mungu amekuwa upande wangu,” Tunu alisema kwa furaha.

Mara simu yake ya mkononi ikaanza kuita. Tunu aliitazama ile simu kwa makini na kuliona jina la Victoria, mke wa Elli. Hisia za hofu, kitu ambacho kwa kawaida kilitokea kwa nadra sana katika damu yake, zilianza kumnyemelea. Tunu aliikodolea macho ile simu kana kwamba alikuwa ameona guruneti la kutupa kwa mkono, akili yake taratibu ikaanza kuzama kwenye kuwaza kuwa huenda jambo baya lilikuwa limetokea.

Kilichomtia hofu Tunu ni kwamba hakuwa tayari kupokea taarifa yoyote mbaya kumhusu Sammy wala familia yake. Aliendelea kuitazama ile simu kwa wasiwasi, hata hivyo, hakutaka kuendelea kuiacha ile simu iendelee kuita zaidi kwani ilikuwa mbioni kukatika baada ya kuita kwa muda mrefu. Haraka akaipokea na kukiweka sikioni huku akiipa akili yake utulivu wa hali ya juu.

“Hallo!” Tunu alisema mara tu alipoiweka ile simu sikioni na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Hallow, habari za asubuhi, dada?” Victoria aliongea kwa sauti iliyoonesha kujawa na furaha. Tunu aliihisi ile furaha kwenye sauti ya Victoria upande wa pili wa simu.

Kitendo cha kuisikia sauti adimu ya Victoria ikiwa na furaha kikamfanya Tunu ameze funda kubwa la mate kuutuliza mtima wake huku akianza kuhisi ahueni fulani.

“Nzuri, dada, nipe taarifa za huko,” Tunu aliongea huku ile hofu ikianza kupotea.

“Huku kwema kabisa. Vipi unaendeleaje na mambo yako?”

“Namshukuru Mungu nimefanikiwa kwa kiasi kikubwa...”

Okay! Nilitaka kukujulia hali na pia kukujulisha kuhusu maendeleo ya wagonjwa wetu. Nimepigiwa simu asubuhi hii na Elli kuwa Sammy ameweza kuamka ingawa hajaanza kuongea, madaktari wamefanikiwa kuyaokoa maisha yake na sasa hana tena tishio kubwa la kiafya...” Victoria alisema na kumfanya Tunu aruke juu kwa furaha.

Oh, thanks God!” Tunu alisema kwa sauti yenye kitetemeshi huku machozi ya furaha yakimtoka machoni. Watu wote pale sebuleni walimtazama kwa mshangao uliochanganyikana na shauku ya kutaka kujua kilichomfanya atokwe na machozi. “Thanks God!” alisema tena na kushusha pumzi. Kisha kikatokea kitambo kifupi cha ukimya.

“Vipi kuhusu Joyce?” Tunu aliuliza huku akifuta machozi yaliyokuwa yakimtoka machoni kwake.

“Hali yake imezidi kuimarika, nimepata taarifa kuwa leo madaktari wanamruhusu...” Victoria alisema kwa sauti tulivu lakini yenye furaha.

“Oh, Mungu amsaidie...” Tunu alisema kwa furaha. “Nitapenda kuja kumwona baadaye, nadhani atakuwa hapo kwako?”

“Hapana, atakuwa kwa mama yake, Madame Norah,” Victoria alisema na kumfanya Tunu ashangae kidogo.

“Joyce ni mtoto wa Madame Norah?” Tunu aliuliza ili kupata uhakika, alidhani labda hakuwa amesikia vizuri.

“Ndiyo, ingawa hili tumelijua jana tu na wala Joyce mwenyewe bado hajui kama Madame Norah ndiye mama yake mzazi,” Victoria alisema, maneno yaliyozidi kumshangaza Tunu.

“Kivipi? Mbona sielewi?”

“Ni hadithi ndefu kidogo, ukipata nafasi nitakuelezea...” Victoria alisema na kushusha pumzi.

“Sawa, nitakuja mchana hapo nyumbani tuongee, kwa sasa kuna mambo fulanifulani natakiwa kuyakamilisha,” Tunu alisema kwa furaha kisha wakaagana. Akakata simu.

* * * * *

Gari la Inspekta Abel liliondoka taratibu na kuyaacha maegesho ya magari katika Hospitali ya Mwananyamala. Koplo Rashid ndiye aliyekuwa anaendesha gari na Inspekta Abel alikuwa ameketi kushoto kwake akiwa mtulivu sana. Muda wote akili ya Inspekta Abel ilikuwa kazini ikijaribu kupambanua hili na lile ili kupata jibu endapo kifo cha Casmir kilikuwa kimetokana na hali yake kiafya kudhorota au ulikuwa ni mpango wa mauaji ili asiweze kutoa siri.

Inaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (150)

Japokuwa katika katika kesi ile Inspekta Abel alikuwa akifanya kazi na Sajenti Mapunda lakini kwenye safari hiyo aliamua kuambatana na Koplo Rashid, ambaye vilevile alikuwa komando wa daraja la pili, kwa kuwa alimwamini zaidi ya askari wengine wa kada yake.

Gari lao lilipotoka kwenye geti la kutokea la hospitali ile ya Mwananyamala Koplo Rashid alikata kona na kuingia upande wa kushoto akiifuata barabara iliyokwenda kuungana na barabara ya Mwinjuma. Walipofika kwenye makutano ya barabara zile wakaingia kushoto wakiifuata barabara ya Mwinjuma iliyokuwa inakwenda Kinondoni. Muda ule wa asubuhi barabara ya Mwinjuma ilikuwa na magari mengi.

Inspekta Abel alikusudia kuelekea katika Hospitali ya Amana ili kuonana na Joyce, katika harakati ya kutaka kupata maelezo zaidi ya kumsaidia katika ile kesi.

Kwa kupitia barabara ile ya Mwinjuma, iliwachukua takriban dakika arobaini na tano, badala ya dakika ishirini, kutoka katika Hospitali ya Mwananyamala hadi kuifikia barabara ya Kawawa, katika eneo la Kinondoni Studio. Hali ile ilikuwa imesababishwa na msongamano wa magari katika barabara ile, hasa daladala.

Taa za kuongea magari barabarani ziliwaruhusu, wakati wakiingia katika barabara ya Kawawa ili kuelekea Ilala, gari kubwa la mizigo aina ya Tata Daewoo likatokea mbele yao kwa mwendo wa kasi na kuwabamiza kwa mbele. Lile gari lilikuwa likitokea katika mtaa wa Togo.

Kitendo kile cha kugongwa kilisababisha sauti ya mshindo mkubwa na moshi mzito ukaanza kufuka toka kwenye boneti la gari lile la polisi ambalo lilikuwa halitamaniki kabisa. Eneo lile likageuka kuwa sehemu ya vurumai na mshikemshike.

Koplo Rashid aliyekuwa kwenye usukani aliumia kichwani na alikuwa anavuja damu katika eneo la kichwa, japo si kwa wingi sana ingawa alikuwa hoi kwa maumivu. Inspekta Abel alikuwa amejeruhiwa zaidi kwa kuwa upande aliokuwa ameketi ndiko ambako lile gari lao lilikuwa limebamizwa zaidi kiasi cha kupinda. Alikuwa amepoteza fahamu na alivuja damu nyingi kichwani na nyingine zilimtoka mdomoni.

Ndani ya lile gari kubwa aina ya Tata Daewoo kulikuwa na mtu mmoja tu aliyekuwa akiliendesha lile gari, alikuwa amevaa kofia pana nyeusi aina ya pama, miwani myeusi mikubwa ya jua iliyoyaficha macho yake na glavu maalumu mikononi mwake. Hakutaka kusimama baada ya kusababisha ajali, aliliendesha gari lake kama aliyepandwa na kichaa na kuvuka barabara ya Kawawa kisha akaingia katika barabara ya Mwinjuma akielekea upande wa Mwananyamala na kuongeza mwendo.

Askari wawili wa usalama barabarani waliokuwepo eneo lile na kuishuhudia ile ajali ya kiutisha waliwasiliana na wenzao waliokuwa katika eneo la Mwananyamala ‘A’ ili wahakikishe yule dereva wa lile gari aina ya Tata Daewoo anatiwa mbaroni. Kisha wao wakatafuta gari nyingine harakaharaka na kuwaingia wale majeruhi ili kuwawahisha hospitali.

Yule dereva wa lile gari kubwa aina ya Tata Daewoo alipofanikiwa kukimbia eneo la tuklio aliendesha kwa mweno wa kasi huku akipishana na magari mengine yaliyokuwa yakitokea eneo la Mwananyamala ‘A’ na alipofika katika eneo la baa ta MK Grand, akakata kona na kuingia kulia akiufuata mtaa wa Kasaba, alikuwa bado katika mwendo wa kasi. Baada ya mwendo wa kama dakika mbili alifika katika baa ya Pachoto, akashuka na kulitelekeza lile gari huku yeye akipotelea uchochoroni, asijulikane alikoelekea.

Dakika iliyofuata pikipiki mbili na gari moja dogo zilifika hapo, askari watatu waliteremka haraka na kulizunguka lile gari lakini dereva alikuwa amekwishatoweka. Walipolikagua vizuri lile hgari wakagundua kuwa nyuma ya lile gari kulikuwa na mtu mmoja aliyekuwa hana fahamu akidhaniwa kuchomwa kiasi kikubwa cha dawa maalumu za kupumbaza akili yake ili asiweze kutambua kitu.

* * * * *

Katika Hospitali ya Amana, Joyce na Bi. Pamela walikuwa wameketi kwa utulivu mkubwa wakimsubiri Madame Norah aliyekuwa amefuata dawa ambazo Joyce alitakiwa kuondoka nazo na kwenda kutumia nyumbani baada ya kuruhusiwa, hii ilikuwa ni baada ya daktari wa zamu kumwandikia Joyce ruhusa ya kwenda kuugulia nyumbani baada ya hali yake kiafya kuimarika.

Hadi muda ule bado Joyce alikuwa ana maswali mengi kichwani kwake ambayo hakuwa ameyapatia majibu. Alikuwa akimwangalia mama yake Bi. Pamela kwa macho yaliyojaribu kuuliza mambo mengi lakini Bi. Pamela alikuwa akiyakwepa macho ya Joyce, kwa kuwa hakuwa tayari kuyajibu maswali yake kwa muda ule. Muda wote alijaribu kumtaka Joyce avute subira na muda si mrefu angefahamu kila kitu, baada ya kufika nyumbani.

Akiwa katika wakati mgumu wa kuendelea kuyakwepa macho ya Joyce mara alimwona Madame Norah akirejea na kuwataka waondoke na kuelekea kule alikokuwa ameegesha gari lake la kifahari aina ya Mercedes Benz E-class limousine jeusi la milango sita.

Walipoingia dereva aliliondoa gari, likatoka kwenye geti la kuingilia la Hospitali ya Amana na kukata kushoto kisha likaifuata barabara iliyokwenda kuungana na barabara ya Uhuru katika eneo la Amana Vijana, kisha dereva akakunja tena kuingia upande wa kushoto akiifuata barabara ya Uhuru. Joyce akashangaa sana maana hakujua walikuwa wanaelekea wapi.

Hata hivyo aliamua kubaki kimya tu akiwatazama Bi. Pamela na Madame Norah kwa kuibia bila kusema lolote. Wote walikuwa kimya kabisa. Lile gari lilipofika eneo la vianda vya wasusi wa Kimasai likaingia kushoto likiufuata mtaa wa Mafao na kuyapita maghorofa ya Ilala kisha likatokea katika barabara ya Kawawa, hapo dereva akaingia upande wa kushoto akiifuata barabara ya Kawawa kama anaelekea Magomeni.

Endelea kuwemo kwenye safari hii ya kusisimua ya 🚖🚖 ili kuufahamu mwisho wake...

NB: Litro 👩
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom