Taxi - (154)
Taarifa na salamu hizo zilikuwa zimebebwa kwenye nakala kadhaa za CD maalumu zilizorudufiwa na kuhifadhi sauti na video kuhusiana na mauaji ya Jaji Mkuu, Sylvester Lutego. Tom na Dumba walipoondoka, Tunu alimtaka Bob ampeleke Kurasini ili akaonane na Victoria. Hivyo aliingia chumbani akajiandaa kwa ajili ya safari ya kuelekea Kurasini.
Baada ya dakika chache Tunu alitoka chumbani akiwa amebadilisha nguo na sasa alikuwa amevaa suruali ya
Jamsuit ya rangi ya bluu iliyolionesha vyema umbo lake refu maridadi lenye minofu ya mapaja iliyokaza kutokana na mazoezi ya kila siku. Miguuni alikuwa amevaa viatu vya mchumumio vye visigino virefu vya rangi nyeusi na kujipulizia manukato ghali mwilini yaliyofanya harufu yake itamalaki sebule yote na kuzifanya pua za Bob zipate uhai mpya.
Muda huo huo wakaisikia sauti ya kengele iliyokuwa imewekwa getini ikiita kwa fujo. Tunu na Bob wakatazamana kwa makini katika namna ya kuulizana “huyo atakuwa nani?” huku wakijitahidi kusikiliza kwa makini. Kengele ile iliendelea kuita kwa fujo.
Mlango wa hisia ya sita katika ubongo wa Tunu ulifunguka, ilikuwa ni hisia iliyomfahamisha kuwa yeyote aliyekuwa pale nje anabonyeza ile kengele hakuwa amefika pale kwa jambo la heri. Tunu alikumbuka katika mafunzo ya ushushushu nchini Israel, maendeleo ya hisia ya sita yalikuwa yanapewa uzito mkubwa kwa wanafunzi wa ushushushu, na kadri yalivyosisitizwa ndivyo ambavyo yalimjenga Tunu kutambua umuhimu wa nyenzo hiyo muhimu.
Kwa mara ya kwanza tangu apate sehemu ya maficho katika eneo lile la Kinyerezi alijikuta akigundua kuwa alikuwa amekosea sana kuwadharau watu wa Mr. Oduya kiasi hicho. Mwanzoni aliamini kuwa wasingeweza kugundua uwepo wake katika nyumba ile. Hata hivyo, hakutaka kumfanya mtu yeyote aliyepo nje ya ile nyumba ahisi kuwa alikuwa amegundulika na watu waliokuwemo mle ndani, hivyo akamtumia Bob jicho ambalo lilibeba ujumbe wote, ujumbe ambao masikioni mwa Bob ulijieleza waziwazi “Kazi kwako, mzee!”
Papo hapo Bob akanyanyuka na kutoka nje kisha akaelekea getini huku akiwa makini sana kama mbwa awindaye. Alipolifikia geti akaufungua mlango mdogo uliokuwa pembeni ya lile geti kubwa. Kama walivyotegemea, aliwaona wanaume wawili warefu wenye miili iliyojengeka wakiwa wamesimama nje ya lile geti, wote walikuwa makini sana. Macho yao tu yalitosha kumfahamisha Bob kuwa wale watu walikuwa wazee wa kazi.
“Samahani sana, bro,” mwanamume mmoja alianza kujieleza mbele ya Bob. “Tumelazimika kukusumbua kidogo. Nadhani utatuwia radhi. Mimi ni mwenyekiti wa mtaa huu na huyu ni mjumbe wa eneo hili, nadhani wewe ndiye mwenye nyumba hii?”
Bob aliwatazama kwa makini na kutaka kucheka, lakini hakuweza kufanya hivyo, kwani alishaelewa wale walikuwa kina nani na kwa nini walikuwa pale. Hata hivyo, aliitikia kwa kubetua kichwa chake huku akiendelea kujifanya mjinga aone nini walitaka kufanya. Wakati huo mkono wake wa kulia aliupeleka kiunoni na kuigusa bastola yake, mwili wake ukasisimka.
“Nyumba hii imeonekana kutokaliwa na mtu tangu ikamilike, hivyo tupo katika ziara ya kutembelea wakazi ambao bado ni wageni katika mtaa wetu huu ili kujua mambo mawili matatu ambayo nadhani utatujibu. Uisijali, ni mzunguko wa kawaida tu kwa wakazi wote wageni ili kufahamiana. Samahani kama tutakuwa tumekusumbua kidogo, kwa kawaida hapa mtaani kwetu hatupendi kusumbua wakazi wetu,” yule mwanamume mwingine alidakia.
“Bila samahani, mnakaribishwa sana,” Bob aliitikia, “Karibuni basi ndani,” akasema na kuwapisha ili waingie kisha aliwaongozana kuelekea sebuleni.
“Sijui mwenzetu unaitwa nani?” mwanaume mmoja alimuuliza Bob wakati wakielekea kwenye mlango wa kuingilia ndani.
“Godwin Tyson,” Bob alijibu mara moja pasipo hata kufikiria.
“Wewe ni mwenyeji wa wapi?”
“Hapa hapa Dar es Salaam.”
“Umeoa?”
“Nina mke na mtoto mmoja,” Bob alijibu huku akiufungua mlango na kuwaruhusu waingine ndani.
“Nao wanaishi hapa hapa?”
“Kumbe ulitaka wakaishi wapi?” Bob aliuliza kwa mshangao huku akimtazama yule mwanamume aliyekuwa akimuuliza maswali, kisha akawapisha wale wanaume waingie ndani.
“Sahamani, bwana mkubwa, kama nimekukwaza kwa maswali yangu, nilimaanisha wapo ndani?”
“Wala usijali, ukihitaji kuwaona utawaona tu,” Bob alijibu huku akianza kushindwa kuzizuia hasira zake.
Walipoingia tu sebuleni Bob aliufungua ule mlango wa ufunguo kisha akauchomoa ule ufunguo na kuuweka mfukoni, wale watu wakashtuka na kugeuka haraka kumtazama kwa mshangao, na hapo wakakutana na mtutu ukiwaelekea, lakini ni kama walikuwa wamejiandaa kwa jambo hilo. Walijigawa na kuruka juu huku wakiachia mapigo ya haraka kumwelekea Bob lakini mapigo yao hayakutimiza wajibu wake ingawa walifanikiwa kuidondosha bastola ya Bob iliyokuwa mkononi huku Bob akifanikiwa kuyakwepa mapigo hayo na kujiweka sawa.
Kabla hawajafanya jambo jingine lolote walishtukia wakimwona Tunu akiibuka toka kusikojulikana na kuruka juu huku akijipindua hewani akiwa ametanua miguu yake na kuutanguliza mguu wake wa kushoto usiokuwa na jeraha, ukifuatiwa na mguu wa kulia. Mwanamume mmoja aliyekuwa karibu na Tunu akafanya jitihada za kujikinga na shambulizi hilo huku akiwa tayari amechomoa bastola yake.
Tunu alikiwa bado hewani aliachia pigo moja matata lililomfanya mwanamume yule na kumfanya apepesuke na kugonga kichwa chake kwenye ukuta. Bastola iliyokuwa mkononi mwake ilimtoka na kuanguka kando. Kabla Tunu hajatua sakafuni akampa pigo jingine la judo ambalo lilitua ubavuni mwake na kumlegeza kabisa. Pigo lililofuata lilimlazimisha yule mwanamume kuanguka sakafuni akiwa hana fahamu.
Wakati hayo yakiendelea yule mwanamume wa pili alijikuta akikabiliwa na Bob aliyeachia pigo maridadi lakini yule mwanamume aliliona na kuinua mkono wake juu kulikinga huku mkono wake wa pili ukijiandaa kubonyeza kitufe cha bastola yake. Bob hakuruhusu mkono huo ufanikiwe kuifyatua ile bastola. Aliruka akampiga kichwa kikavu kilichompa kisurisuri na kufanya ateremke sakafuni bila ubishi na kupoteza kabisa fahamu.
Mpambano unazidi kupamba 🔥🔥🔥. Je, baada ya kufahamika kwa maficho hayo Tunu na Bob watafanikiwa kutoka salama ndani ya nyumba hiyo? Endelea kusafiri nami katika safari hii ya kusisimua ndani ya 🚖🚖 hadi mwisho...
NB:
Litro 👩