Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Wakuu, mafua yamenibana sana tangu Jumamosi, kichwa kinaniuma, kifua kimenibana na mwili wote unauma. Hata hivyo, nitajitahidi baadaye kidogo nije nitupie, naomba tuvumiliane tu...

NB: Litro 👩
Bishop pole pole sana pole tena............ukipata nguvu bas tupia tu za kutosha za kukomesha za kukomoa ee baba
 
Taxi - (151)

ILIPOISHIA

Katika Hospitali ya Amana, Joyce na Bi. Pamela walikuwa wameketi kwa utulivu mkubwa wakimsubiri Madame Norah aliyekuwa amefuata dawa ambazo Joyce alitakiwa kuondoka nazo na kwenda kutumia nyumbani baada ya kuruhusiwa, hii ilikuwa ni baada ya daktari wa zamu kumwandikia Joyce ruhusa ya kwenda kuugulia nyumbani baada ya hali yake kiafya kuimarika.

Hadi muda ule bado Joyce alikuwa ana maswali mengi kichwani kwake ambayo hakuwa ameyapatia majibu. Alikuwa akimwangalia mama yake Bi. Pamela kwa macho yaliyojaribu kuuliza mambo mengi lakini Bi. Pamela alikuwa akiyakwepa macho ya Joyce, kwa kuwa hakuwa tayari kuyajibu maswali yake kwa muda ule. Muda wote alijaribu kumtaka Joyce avute subira na muda si mrefu angefahamu kila kitu, baada ya kufika nyumbani.

Akiwa katika wakati mgumu wa kuendelea kuyakwepa macho ya Joyce mara alimwona Madame Norah akirejea na kuwataka waondoke na kuelekea kule alikokuwa ameegesha gari lake la kifahari aina ya Mercedes Benz E-class limousine jeusi la milango sita.

Walipoingia dereva aliliondoa gari, likatoka kwenye geti la kuingilia la Hospitali ya Amana na kukata kushoto kisha likaifuata barabara iliyokwenda kuungana na barabara ya Uhuru katika eneo la Amana Vijana, kisha dereva akakunja tena kuingia upande wa kushoto akiifuata barabara ya Uhuru. Joyce akashangaa sana maana hakujua walikuwa wanaelekea wapi.

Hata hivyo aliamua kubaki kimya tu akiwatazama Bi. Pamela na Madame Norah kwa kuibia bila kusema lolote. Wote walikuwa kimya kabisa. Lile gari lilipofika eneo la vianda vya wasusi wa Kimasai likaingia kushoto likiufuata mtaa wa Mafao na kuyapita maghorofa ya Ilala kisha likatokea katika barabara ya Kawawa, hapo dereva akaingia upande wa kushoto akiifuata barabara ya Kawawa kama anaelekea Magomeni.

ENDELEA...

Joyce aliendelea kuwa kimya akijaribu kutafakari, muda wote macho yake yalikuwa yakiangalia nje wakati gari waliloabiri likipita katika eneo la Msimbazi Centre, kisha likavuka eneo la Kigogo Sambusa na baadaye Kigogo Mbuyuni, kwenye mzunguko wa barabara za Kawawa na ile ya Kigogo. Kutoka hapo wakaanza kuteremsha katika bonde la Msimbazi na kuibukia Magomeni Mikumi na baadaye waliivuka Barabara ya Morogoro.

Bado Joyce hakujua walikuwa wakielekea wapi, kuanzia hapo alianza kuzama kwenye lindo la mawazo, alijiuliza ni nini kilikuwa kimemtokea Sammy? Kitendo cha kutomwona akimtembelea hospitali kilizidi kumshangaza sana Joyce, alihisi labda Sammy alikuwa bado ana kinyongo kutokana na kile alichokuwa amemweleza, juu ya mwanamuziki Dynamo Plus. Hata hivyo, Joyce aliamini kuwa Sammy hakuwa mtu wa kinyongo bali lilikuwepo jambo ambalo hakuwa akilijua.

Mawazo kibao yaliendelea kupita kichwani kwake kiasi kwamba hakuweza kukumbuka kitu kingine chochote na alipokuja kuzinduka tayari lile gari lilikuwa limesimama mbele ya geti kubwa katika jumba la kifahari la Madame Norah lililopo ufukweni mwa Bahari ya Hindi eneo la Mikocheni.

Joyce aliyatazama vizuri mandhari ya kuvutia ya jumba lile yaliyozungukwa na miti mirefu na mikubwa ya kivuli aina ya ‘Quercus virginiana’ na barabara ya lami yenye usafi wa hali ya juu iliyokuwa ikieleka katika jumba hilo na kupandwa miti ya kivuli iliyovutia na maua aina ya ‘lotus’. Baada ya kuyaona mandhari yale ndipo alipoweza kugundua kuwa alikuwa amepelekwa Mikocheni nyumbani kwa Madame Norah. Joyce akazidi kushangaa.

Joyce hakutaka kuendelea kuumiza kichwa chake kwa maswali yasiyo na majibu, sasa aliazimia kuufahamu ukweli, kwa njia yoyote ile. Aligoma kushuka kwenye gari akitaka aelezwe kwanza ukweli wote kuhusu yote yaliyotokea wakati alipokuwa hana fahamu, na aelezwe Sammy yupo wapi na kwa nini waliamua kumleta pale nyumbani kwa Madame Norah badala ya kumpeleka nyumbani kwake, Tabata Chang’ombe.

Madame Norah na Bi. Pamela waliangaliana katika namna ya kuulizana kama walipaswa kumwambia chochote muda huo, kisha Bi. Pamela akashusha pumzi za ndani huku akionekana kusita sana. Hata hivyo, hawakuwa na namna nyingine ya kumshawishi ili ashuke kwenye gari.

Madame Norah alinyanyua mabega yake juu na kuyashusha huku akiminya midomo yake. Akajaribu kumwomba Joyce aingie kwanza ndani na mambo mengine wangeyazungumza wakiwa ndani lakini Joyce alikataa katakata akitaka aelezwe ukweli wote ndipo aamue kama angeingia ndani au lah.

“Tumeamua kukuleta hapa kwa sababu ndipo nyumbani kwenu, kwa mama yako,” Madame Norah alisema baada ya kufikiria sana. Hakuwa na namna nyingine isipokuwa kumweleza ukweli.

“Nyumbani kwa mama yangu kivipi?” Joyce aliuliza kwa mshangao huku akiwatazama Madame Norah na Bi. Pamela kwa zamu.

“Labda kitu ambacho hujajua ni kwamba Madame Norah ndiye mama’ako mzazi,” Bi. Pamela alisema kwa sauti tulivu.
“Mama’angu mzazi!” Joyce aliuliza kwa mshangao. “Ni mama’angu tangu lini? Mbona sijawahi kuambiwa kuhusu jambo hili! Na vipi kuhusu wewe, mama?”

“Ni hadithi ndefu kidogo, mwanangu. Ila kwa kifupi ni kwamba Madame Norah ndiye mama’ako mzazi. Mimi si mama’ako mzazi ingawa ndiye niliyekulea tangu utoto wako,” alisema Bi. Pamela kwa huzuni.

Joyce alihisi ubaridi mwepesi ukimtambaa mwilini mwake na kuzifanya nywele zake kusisimka. Alitaka kusema neno lakini akasita. Japo hakuweza kuelewa mara moja kama taarifa zile alizozisikia zilikuwa na ukweli wowote au lah, lakini alijikuta akichanganyikiwa zaidi ya kushangaa. Alidhani maelezo yale yangemsaidia kupata majibu sahihi ya maswali yake machache yaliyokuwa yakimsumbua kichwani kwake lakini sasa akajikuta maswali mengi zaidi yakiibuka kichwani kwake.

Aliwaza kuwa huenda ile ilikuwa ndoto tu kama ndoto zingine na mara tu angeamka kutoka usingizini na kukuta kila kitu kikiwa tofauti kabisa. Hata hivyo, hisia zake zilimtanabaisha kuwa ile haikuwa ndoto bali ni kitu halisi kilikuwa kinamtokea. Alitambua kuwa ni kweli alikuwa yupo nyumbani kwa Madame Norah na alipewa taarifa kuwa Madame Norah ndiye mama’ake mzazi! Mama mzazi kivipi? Hilo hakulijua kwani hajawahi kuambiwa. Alijiuliza, ni kwa nini siku zote hizo hakuwahi kuambiwa kuwa Bi. Pamela hakuwa mama’ake mzazi isipokuwa Madame Norah?

Alihisi kutaka kuchanganyikiwa. Hisia za tukio lile zikasababisha koo lake likauke ghafla na milango yake ya fahamu ilikuwa makini zaidi huku akijaribu kuishirikisha akili yake kikamilifu katika kumletea taarifa za kuaminika ili kubaini endapo tukio lile lilikuwa katika mlolongo wa matukio yoyote ya ndotoni au lah!

Baada yah apo hakuweza kukumbuka ni vipi alishuka toka kwenye gari na kuingia ndani, alipokuja kurudiwa na fahamu alijikuta akiwa ameketi juu ya sofa kubwa la kifahari kwenye sebule kubwa ya nyumba ile, huku macho yake yakiwa yamejawa na machozi. Hakuelewa mara moja kuwa machozi yale yalikuwa ya huzuni au ya furaha?

Madame Norah na Bi. Pamela walikuwa wakimtazama kwa makini pasipo kusema neno. Sebule nzima ilikuwa katika hali ya utulivu na ukimya mkubwa. Joyce aliyatupa machjo yake kuangaza pembe zote lakini hakuona dalili za uwepo wa watu wa familia yake, si mwanawe Pendo, Winifrida wala Sammy. Hali ile ikazidi kumtia hofu na kusababisha jasho jepesi lianze kumtoka sehemu mbalimbali za mwili wake huku mapigo ya moyo wake yakibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida!

Joyce alimwangalia Madame Norah usoni kwa makini akitaka kuelezwa ukweli, akagundua kuwa kulikuwa na jambo kwenye uso wa Madame Norah, ni kama huzuni fulani japokuwa alijitahidi kulazimisha tabasamu. Hata hivyo, tabasamu lake halikuweza kuiondoa hisia fulani ya majonzi usoni kwake. Madame Norah alikuwa ameketi kimya kabisa huku akionekana kutafuta maneno ya kumwambia Joyce.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus mtugani wa wapi huyo chiqutitta ndukulusudicho ADK aggyd BAHARI J

NB: Litro 👩
 
Taxi - (152)

“Joyce, najua unayo maswali mengi sana kichwani kwako na hili tulilokwambia limekuzidishia mkanganyiko badala ya kujibu maswali yako. Naomba ufahamu kuwa mimi ndiye mama’ako, nilipata ujauzito wako nikiwa kidato cha nne, nikakatisha masomo na mambo fulani yakatokea, nilipokuzaa nikakuacha na baba’ako Jengo,” Madame Norah alisema kwa sauti ya kutetemeka huku machozi yakianza kumtoka.

“Huwezi kuamini, kwa miaka yote hii nimekuwa nikikutafuta sana, ilifikia kipindi nikaamini kuwa wewe na baba’ako mlikufa kwenye ajali ya moto ulioteketeza nyumba mliyokuwa mkiishi eneo la Ngamiani Tanga. Baada yah apo sikujua ningewapata wapi hadi jana nilipokutana na baba’ako pale hospitali. Nisamehe sana binti’angu, najua sikukutendea haki lakini itoshe tu kusema kuwa najutia sana kitendo changu, kwani tangu wakati huo nimekuwa nikiishi maisha ya huzuni kubwa na majuto mengi ingawa watu wakiniangalia hudhani labda nina furaha...”

Maneno yale yalizidi kumuumiza Joyce, hakujua aseme nini. Hata hivyo, aliendelea kuwa kimya kabisa. Alihisi labda akili yake ilikuwa haifanyi kazi sawasawa. Aliendelea kumtazama Madame Norah kwa makini. Kikatokea tena kitambo kirefu cha ukimya.

Haikuwa rahisi kwa Joyce kuipokea taarifa ile. Ilikuwa ni taarifa ngeni kabisa masikioni mwake na akili yake ilikataa kuikubali. Siku zote alikuwa akimchukulia Madame Norah kama mfano wa mwanamke mwenye mafanikio, akitamani siku moja kufikia japo nusu ya mafanikio yake, hakuwahi kudhani kama angeweza kuwa mama’ake mzazi.

Japo alitaka kuamini lakini akili yake likataa, ila alipowatazama wale wanawake wawili alikiona kitu kwenye macho yao na nyuso zao, kitu kilichomhakikishia kuwa yote aliyoyasikia yakisemwa juu yake yalikuwa kweli kabisa!

Baada ya kitambo kirefu hatimaye Joyce aliwataka wamwache kwanza, kwani alihitaji muda wa kuwa peke yake ili aweze kutafakari kabla hajaamua lipi la kufanya. Hata hivyo, kabla hajajitenga aliomba afahamishwe ni wapi ilipokuwa familia yake. Madame Norah alimtaka kuwa jasiri huku akijitahidi kuifanya sauti yake iwe za kawaida.

Kisha walimweleza Joyce yote kuhusu nyumba yao kushambuliwa na bomu lililotegwa kwenye gari na watu wasiojulikana, wakati huo Sammy na Jengo wakiwa ndani ya nyumba hiyo. Wakamweleza kuhusu majeraha waliyoyapata na Sammy kulazwa Muhimbili, na kwamba hali yake ilikuwa inaendelea vizuri.

* * * * *

Mr. Oduya aliwasili katika jengo la makao makuu ya ofisi za The Splendid Group lililopo barabara ya Bagamoyo, eneo la Kijitonyama. Alikuwa akitokea Paradise Club alikokwenda kuonana wa mshirika wake mkubwa, Kamishna Omalla, Mkuu wa Kamisheni ya Intelijensia wa Jeshi la Polisi.

Kama mtu mkubwa, Mr. Oduya alitumia lifti maalumu ambayo ilimfikisha katika ghorofa ya saba ilikokuwa ofisi yake na kuutumia mlango maalumu ili kuingia ofisini kwake bila kubughudhiwa na mtu mwingine. Alipoingia alijibwaga juu ya kiti chake na kuitazama saa yake ya mkononi, ilionesha kuwa ilishatimia saa nne na nusu asubuhi. Mr. Oduya alishusha pumzi na kupandisha miguu yake juu ya meza na kuinyoosha, akatulia akitafakari.

Japokuwa alipaswa kufurahia kazi nzuri iliyofanywa na Robert Kamau ya kumsababisha ajali ya gari Inspekta Abel, mtu aliyeanza kuwa tishio kwake, huku akihakikishiwa kuwa asingeweza kuamka tena na kama angefanikiwa kuamka basi angekuwa mlemavu maisha yake yote, lakini Mr. Oduya alishangaa kuona kuwa bado hakuwa na furaha wala amani kabisa moyoni.

Alijihisi kama yupo uchi kabisa kwa Tunu na hilo halikuwa na mjadala. Kwanza binti huyo alikuwa amefanikiwa kuepuka mitego yote aliyomtegea kwa miaka mitatu na kusababisha vifo vya watu wake muhimu sana kwenye harakati zake, huku Victor akiwa mahututi akipigania roho yake hospitali, na pili alishagundua mambo yao mengi.

Mr. Oduya alidhani kuwa ili kuwa salama alipaswa kuhakikisha anammaliza Tunu kabla jua halijatua. Hata hivyo jambo la ajabu, hadi wakati huo hakuna yeyote miongoni mwa watu wake aliyejua Tunu alikuwa wapi. watu wote aliowapa jukumu la kumfuatilia Tunu hawakujua alikuwa wapi, tangu alipookolewa na watu wake usiku wa kuamkia siku ile. Alianza kuingiwa na mawazo kuwa huenda alikufa kwenye ile ajali.

Alijikuta akianza kupata furaha moyoni ingawa hakupendaa kuamini, alitoa maagizo kwa watu wake wote kuwa makini sana na kuhakikisha wanafuatilia kila taarifa na maeneo yote waliyodhani huenda Tunu angeweza kuwepo. Maeneo kama Hospitali ya Amana, Muhimbili au katika mgahawa wa kisasa wa Elli’s ambako Tunu aliliacha gari lake.

Muda huo Mr. Oduya alikuwa mchovu aliyechoshwa na fikra nzito. Aliwasha kiyoyozi ndani ya ofisi yake kilichojaribu kuupooza mwili wake. Kisha alianza kumezwa na fikra nzito mpaka pale alipokuja kushtushwa na simu yake ya mkononi iliyoanza kuita kwa fujo. Mr. Oduya aliichukua ile simu na kuitazama kwa makini, akaachia tabasamu baada ya kuliona jina la Kamishna Omalla. Aliipokea ile simu na kuipeleka sikioni.

“Hallo, poti!” Mr. Oduya alisema kwa sauti tulivu huku akibana pumzi zake.

“Ni nini hiki umefanya?” sauti nzito ya Kamishna Omalla ilisikika ikimuuliza Mr. Oduya pasipo kujuliana hali.

“Kwani ulitarajia nini, poti?” Mr. Oduya aliuliza huku akiminya midomo yake kuzuia kicheko kilichotaka kumtoka. “Vipi, amekufa?”

Kamishna Omalla hakujibu mara moja, alibaki kimya kwa kitambo kirefu hadi Mr. Oduya akadhani labda alikuwa amekata simu. Alipotaka kuita akamsikia Kamishna Omalla akikohoa kidogo kusafisha koo lake.

“Oduya, hii tabia ya kutaka kuua watu wote unaodhani ni tishio kwako inabidi uipunguze, imezidi sasa!” Kamishna Omalla alisema kwa sauti ya majonzi. Ilionekana wazi kuwa alikuwa haipendi tabia ile ya mauaji, aliamini kama yangeendelea basi mwisho wake si Mr. Oduya tu ambaye angetiwa hatiani bali hata yeye, endapo angegundulika kuwa ni mshirika wake mkubwa.

“Kamishna, najua huwezi kunielewa,” Mr. Oduya aliongea kwa sauti ya chini, “Ulimwengu huu haupo sawa kama unavyodhani. Muda mwingine yatupasa kufanya hivyo kabla hatujafanyiwa hivyo sisi wenyewe!” Mr. Oduya alisema na kumfanya Kamishna Omalla agune.

“Nakuelewa, lakini nilidhani tulikubaliana nilipokwambia suala hilo nitalishughulikia. Hukupaswa kufanya ulichokifanya,” Kamishna Omalla alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. “Hata hivyo, ngoja nione itakavyokuwa.” Kamishna Omalla alisema na kukata simu.

Usichoke kufuatilia simulizi hii ili kuujua mwisho wake...

NB: Litro 👩
 
. ...
Pole sana bishop na kuumwa
Wakuu, mafua yamenibana sana tangu Jumamosi, kichwa kinaniuma, kifua kimenibana na mwili wote unauma. Hata hivyo, nitajitahidi baadaye kidogo nije nitupie, naomba tuvumiliane tu...

NB: Litro 👩
 
Pole sana mkuu

Wakuu, mafua yamenibana sana tangu Jumamosi, kichwa kinaniuma, kifua kimenibana na mwili wote unauma. Hata hivyo, nitajitahidi baadaye kidogo nije nitupie, naomba tuvumiliane tu...

NB: Litro 👩
[/QUOTE]
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom