Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (120)

ILIPOISHIA

“Ninahisi gari hili limewekwa GPS device ili kuni-track waweze kujua kila ninapokwenda,” Tunu alisema.

Wale wanaume wakaanza kulikagua gari wakianzia kwenye sehemu za ndani ambazo magurudumu hufungwa kuona kama vifaa vya GPS vilikuwa vimepachikwa lakini hawakuona kitu, inaaminika kuwa kwa vyovyote mtu mtaalamu wa mambo hayo asingeweza kufunga kifaa kama hicho sehemu hiyo.

Wakafungua boneti la gari na kuchunguza kila sehemu kwa uangalifu sana, walikagua injini nzima kwa kutumia kioo maalumu na tochi lakini hawakuona chochote. Wakachunguza chini ya gari wakiiangalia injini kutokea chini hadi juu lakini hakukuwa na kifaa chochote cha GPS. Wakafungua siti za gari na kuangalia chini, pia hakukuwa na chochote.

Walipokosa maeneo yote hayo wakaondoa redio kwenye dashbodi na kuchunguza kwa ndani na kila sehemu, hakukuwa na kitu. Kisha wakaondoa paneli za milango na kava za spika na kuchunguza. Walipokosa wakaangalia kwenye mikono ya milango (handles) na kwenye vifungo vyake, wakakiona kifaa kimoja cha GPS kilichokuwa kimewekwa kitaalamu sana kwenye kifungo cha mkono wa mlango wa kushoto, kiasi cha kumfanya mtu asiye mjuzi wa mambo hayo asiweze kugundua.

SASA ENDELEA...

Tunu na Tom wakaangaliana, macho yao yaliweza kuongea mengi kuliko ambavyo wangeweza kuongea kwa midomo yao kisha Tunu akashusha pumzi za ndani kwa ndani.

You were right! Ulikuwa umechezewa mchezo ili waweze kujua kila unapokwenda,” Tom akasema huku akiweka mikono yote miwili kwenye kiuno chake. Alikuwa anatweta.

I dont believe this, Victor ndiyo kaamua kunichezea mchezo, siyo? I knew it!” Tunu alisema kwa sauti tulivu lakini iliyobeba hasira ndani yake huku akimtazama Tom. Aliuma midomo yake na kushusha pumzi kisha akabetua kichwa chake huku akijitahidi kudhibiti hasira zake.

“Hivi huyu ni Victor yupi?” Tom akauliza huku akimtazama Tunu kwa makini.

“Nitakuelezea baadaye, I truted the guy lakini kumbe ni nyoka! Hata sijui kwa nini roho yangu ilikuwa nzito sana kumweleza chochote kuhusiana na mambo haya japo alikuwa ananiuliza maswali mengi sana yaliyonifanya kuanza kuwa na shaka kidogo!” Tunu akasema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

Wale wanaume wa kazi walimaliza kazi yao kulikagua lile gari kwa makini katika kila sehemu waliyodhani kungeweza kufichwa kifaa cha GPS na hakuona kifaa kingine. Wakampatia Tunu kile kifaa walichoking’amua, Tunu akakitazama kwa makini na kuachia tabasamu la uchungu, kisha akabana taya zake na kuanza kukereza meno yake huku akizuia hasira zilizoanza kumpanda.

“Sasa nitawafanyia uhuni ambao hawajawahi kufanyiwa, ninakwenda kukitelekeza hiki kifaa Central Police, hapo ndipo watakapofurahi na roho yao!” Tunu alisema kisha wote wakaangua kicheko. Alitoka nje na kuwaacha wanaendelea kurudishia vitu vyote kwenye gari kwa usimamizi wa Tom, yeye akakodi pikipiki na kuelekea moja kwa moja Kituo Kikuu cha Polisi cha Dar es Salaam.

* * * * *

Magari mawili ya zimamoto na ving’ora vya magari ya polisi yalionekana yakielekea katika mtaa ilipokuwa nyumba ya Sammy, eneo la Tabata Chang’ombe yakiwa katika mwendo wa kasi. Yalipofika kazi ya kuuzima moto ilianza harakaharaka ili kuzuia moto ule usiweze kusambaa katika nyumba za jirani na kusababisha maafa zaidi na baada ya muda mfupi juhudi zao kuuzima moto huo zikaonekana kufanikiwa.

Nyumba ya Sammy ilikuwa imebomoka na kubaki kama gofu huku gari lake aina ya Cadillac DeVille likiwa limeteketea kabisa na kubakichuma chakavu.

Ndani ya muda mfupi barabara zote za kuingia na kutoka katika mtaa ule zilikuwa zimewekwa kizuizi cha askari na eneo la nyumba ya Sammy likazungushiwa utepe maalumu wa njano maarufu kama Barricade tape wenye maandishi ya “Police Line Do Not Cross”. Kila mtu aliyetaka kupita eneo lile alisimamishwa, akahojiwa na kama alionekana hahusiki basi alizuiwa kupita.

Dakika zilizofuata eneo lote lilijaa magari, yakiwemo ya polisi, mawili ya jeshi la wananchi na magari mawili ya wagonjwa yaliyokuwa yameegeshwa kandokando ya barabara kulizunguka eneo lile huku askari wenye silaha wakishika doria kulinda iwapo kungetokea vibaka waliotaka kupora. Askari wale walikuwa makini sana wakizungusha macgo yao pembe zote. Pia walikuwepo wataalamu wa mabomu toka jeshini waliokuwa wakikagua eneo lote kuona kama kulikuwa na mabomu mengine ambayo hayajalipuka.

Makundi mbalimbali ya watu yalikuwa yamekusanyika katika eneo lile, watu hao, wakubwa kwa wadogo, walikuwa wanashangaa na wengine wakisimuliana jinsi walivyoshuhudia mlipuko mkubwa ulioliteketeza kabisa gari la Sammy na kubomoa ile nyumba. Hakuna kati yao aliyekuwa anaruhusiwa kusogea karibu na eneo ambalo mlipuko huo au kuvuka uzio uliokuwa umewekwa kwa hofu kuwa huenda kulikuwa bado na masalia ya mabomu mengine.

Kati ya watu waliokuwepo eneo lile wakionekana kushangaa ni mwanamume mmoja mrefu mwenye ndevu nyingi aliyekuwa amevaa suti nzuri ya rangi ya hudhurungi na viatu vyenye rangi hiyo hiyo. Alitembea kwa hatua za wastani, macho yake yakilenga zaidi kuangalia kwenye kifusi cha nyumba kuona kama kulikuwa na majeruhi yeyote wa lile tukio. Alipobakiza kama hatua mbili kuufikia ule uzio wa njano wenye maandishi ya “Police Line Do Not Cross” alijitoa katika kundi la watu wengine, akajiegemeza ukutani mwa duka moja la Mangi.

Alisimama pale akawa anashangaa huku akijaribu kuuliza kama kuna mtu yeyote aliyeokolewa kwenye lile tukio akiwa hai. Hakuna aliyejishughulisha naye kwani wote aliokuwa akiwauliza na wao walikuwa wamefika hapo muda mfupi tu kabla yake, akatoa sigara yake na kuwasha kisha akawa anavuta taratibu huku akiangaza macho yake pembe zote, kisha akayatuliza kwa wanajeshi wa kutegua mabomu na askari wa uokoaji ambao walikuwa wanafukua kifusi kuona kama kulikuwa na mtu yeyote aliye hai.

Muda huohuo gari la Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam likaingia. Naibu Kamishna Ramon Mamboleo akashuka haraka toka kwenye gari lake na kuanza kutembea kwa ukakamavu huku akiangaza macho yake pembe zote kama aliyekuwa anachunguza kitu. Alikuwa askari makini sana na mkakamavu asiyeruhusu makosa ya kipumbavu yaliyoashiria uzembe yatokee awapo kazini.

Kabla ya kupandishwa kuwa Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna Mamboleo alikuwa Mkuu wa Upepelezi. Hakuwa na mzaha kabisa awapo kazi, angeweza kumfuatilia hata shetani katika harakati zake za kuharibu Amani au maadili mema ya wana wa Mungu na akamtia mbaroni kisha akamburuza mahakamani, tena peke yake.

Itaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus

NB: Litro 👩‍🦱
 
Taxi - (121)

Waandishi wa habari waliokuwepo eneo lile walianza kumzonga wakitaka kupatiwa maelezo ya tukio zima: ni nani washukiwa wa uhalifu huo kwani mlolongo wa matukio hayo ulionekana kuikumba familia ile katika kipindi kisichozidi saa kumi nan ne. Usiku watu wasiojulikana walivamia nyumba na kumpiga risasi mke wa Sammy, na sasa wamerudi tena na kutega bomu, nadhani wakikusudia kumuua Sammy mwenyewe ambaye hadi wakati huo haikujulikana kama yupo hai au amekufa.

Kamishna Mamboleo, kutokana na kuchanganyikiwa hakupenda kuongea hata na mmoja wao. Aliwaomba wawe wavumilivu, wasubiri kwanza ripoti ya wataalamu wa upelelezi, aidha, hakuwaruhusu hata askari wake mmoja aongee na mwandishi wa habari yeyote juu ya matukio hayo.

Wakati huo askari wengine wa upelelezi walikuwa wakiwahoji majirani na baadhi ya wapita njia waliodai kushuhudia tukio hilo. Watu saba, wakiwamo Godlove Nyari maarufu kama Mangi aliyekuwa na duka katika mtaa huo na mwanafunzi mmoja wa shule ya sekondari aliyekuwepo dukani kwa Mangi wakati mlipuko huo unatokea walihojiwa na polisi.

Katika watu hao saba, wanaume watano, mwanamke mmoja na yule mwanafunzi walipohojiwa na askari wa upelelezi, watatu akiwemo yule mwanafunzi walikiri kuliona gari moja aina ya Toyota Vanguard jeusi lenye vioo vya tinted visivyomruhusu mtu kuona ndani likifika eneo lile dakika tano tu baada ya gari la Sammy kuingia, na mtu mmoja mwanamume aliyekuwa amevaa kofia pana ya pama iliyoficha sura yake na miwani mikubwa ya jua alishuka toka ndani ya gari lile, kisha lile gari likaondoka.

Baada ya hapo, yule mwanamume alionekana akiangalia huku na kule kama aliyekuwa akitafuta kitu kabla hajaondoka na kuambaa ambaa na ukuta wa nyumba ya Sammy, akaelekea upande wa nyuma wa nyumba. Hata hivyo, watu wote waliomwona yule mtu hakuna aliyemfuatilia kujua alikuwa anakwenda wapi kwa kuwa hawakujua kama alikuwa na lengo baya.

Baada ya maelezo, wale askari wa upelelezi waligundua jambo ambalo lingeweza kuwaongoza katika upelelezi wao kwenye maelezo watu wawili tu, Mangi na yule mwanafunzi wa sekondari na waliwataka kwenda nao kituoni kwa mahojiano zaidi. Mkuu wa kitengo cha upelelezi wa Ilala, Inspekta Abel aliondoka nao, wakaelekea kituoni.

Wakati huo huo wale askari wa uokoaji waliweza kugundua uwepo wa mtu katika kifusi baada ya kuona akihangaika kuinuka, lakini kwa kuwa alikuwa amekandamizwa hakuweza kuinuka. Kwa kushirikiana na wanajeshi wa kutegua mabomu walifanikiwa kumtoa yule mtu ambaye alikuwa na michubuko midogo midogo na hakuonekana kuwa na majeraha makubwa sana. Hata hivyo alikuwa analalamika maumivu mwilini.

Kisha wakamwona mtu mwingine mwanamume akiwa pia amenasa kwenye kifusi. Huyu alikuwa amejeruhiwa eneo la kichwani na alionekana ama amekufa au amepoteza fahamu, lakini walipomchunguza kwa makini waligundua kuwa yeye pia alikuwa bado yupo hai. Haraka sana walileta machela wakambeba na kumkimbiza kwenye gari la wagonjwa, huku yule mwanamume mwingine akisaidiwa kutembea na kuingizwa kwenye gari lile lile la wagonjwa, kisha wakakimbizwa hospitali.

Yule mwanamume mrefu mwenye ndevu nyingi aliyevaa suti ya hudhurungi aliwashuhudia wale watu wawili waliojeruhiwa, na aliamini kuwa mmoja wa watu hao ni Sammy, wakiondolewa pale na kuingizwa ndani ya gari la wagonjwa, kisha lile gari likaondoka toka eneo lile likisindikizwa na magari mawili ya polisi wenye silaha.

Moyo wake ukapiga mshindo mkubwa! Sigara aliyokuwa anavuta ikadondoka. Alilitazama lile gari kama vile chui aliyejeruhiwa amtazamavyo mwindaji aliyemjeruhi. Akavuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu kisha alitoa simu yake ya mkononi na kuanza kuondoka eneo lile.

Haukupita muda mrefu tangu tukio la kulipuliwa kwa nyumba ya Sammy litokee, habari zilizagaa karibu kila mahali jijini Dar es Salaam na hata nje ya jiji na nchi. Taarifa zilienea haraka kama moto wa kifuu kupitia mitandao ya intaneti, hasa mitandao ya WhatsApp na YouTube. Watu walitumiana picha na vipande vifupi vya video za tukio. Elli akiwa ofisini kwake aliziona taarifa zile za kushtusha baada ya kutumiwa picha na mmoja wa rafiki zake.

Oh my God!” Elli aling’aka kwa mshtuko mkubwa. Alijikuta akichanganyikiwa, akajaribu kumpigia simu Sammy lakini simu yake ilikuwa haipatikani. Akaingiwa na hofu kubwa huku hisia mbaya zikianza kumtawala juu ya usalama wa Sammy na familia yake. Hakutaka kusubiri, aliingia kwenye gari lake aina ya BMW X6 na kuondoka haraka, akaelekea eneo la Tabata Chang’ombe, nyumbani kwa Sammy.

Akiwa katika eneo la Malapa Hostel aliona msafara wa magari matatu ukielekea upande wake kwa mwendo wa kasi huku magari mengine yakiwekwa pembeni, yeye pia alikaa pembeni na kuliona gari la wagonjwa lililokuwa katika mwendo wa kasi huku likisindikizwa na magari mawili ya polisi yakipita kuelekea hospitali ya Amana. Hata hivyo, Elli hakujishughulisha nao, yeye mawazo yake yalikuwa ni kufika nyumbani kwa Sammy tu, hivyo alikanyaga pedeli ya mafuta kuelekea Tabata Chang’ombe.

Alipokaribia eneo hilo alishtuka baada ya kuona kulikuwa na ulinzi mkubwa askari wenye silaha waliokuwa wametanda eneo lile. Elli alihisi mwili wake ukiishiwa nguvu. Hata hivyo, hakutaka kuegesha gari lake pembeni, akazidi kusonga mbele huku moyo wake nao ukizidi kupiga mshindo mkubwa. Katika eneo lile kulikuwa na magari ya polisi na mengine yaliyokuwa yameegeshwa pembeni mwa barabara. Askari mmoja mwenye silaha akamsimamisha.

“Unaelekea wapi, si unaona barabara imefungwa na hakuna mtu anayeruhusiwa kupita mtaa huu!” yule askari akamuuliza Elli kwa ukali huku akimkazia macho yake kwa makini.

Inaendelea...

NB: Litro 👩‍🦱
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom