Taxi - (118)
Waliongea kwa dakika kadhaa kisha wakakubaliana, alipokata simu akabadili uelekeo, badala ya kuelekea hospitali ya Amana akaelekeza gari lake eneo la Shaurimoyo, Ilala.
* * * * *
Sammy na Jengo walipoondoka pale hospitali ya Amana na kuwaacha Madame Norah na Bi. Pamela, walielekea moja kwa moja katika mgahawa wa kisasa wa Elli’s ili kupata chakula. Wakati wakienda huko hawakujua kuwa walikuwa wanafuatwa. Kulikuwa na gari jingine aina ya
Toyota Vanguard jeusi lenye vioo vya
tinted visivyomruhusu mtu kuona ndani lilikuwa linawafuatilia.
Walipofika hapo Elli’s Sammy aliegesha gari lake kwenye maegesho, wakaingia ndani ya mgahawa na iliwachukua dakika arobaini na tano kupata chakula na kutoka nje tayari kwa safari ya kuelekea kwenye makazi ya Sammy. Waliagana na Elli kwa ahadi ya kumpitia pale kwenye mgahawa muda wa jioni wakati wanaelekea hospitali ya Amana.
Wakajipaki kwenye gari lao walilokuja nalo na kutimka eneo hilo. Dakika takriban mbili tu tangu waondoke, lile
Toyota Vanguard likawashwa na kuanza kuwafuatilia, lakini wakiwa na tahadhari zote, hadi walipofika nyumbani kwa Sammy eneo la Tabata Chang’ombe.
“Karibu sana, baba,” Sammy alimkaribisha baba mkwe wake, Jengo mara tu walipoingia ndani.
“Ahsante sana, mwanangu,” Jengo alijibu huku akijipweteka juu ya sofa. Alionekana kuchoka sana na macho yake yalikuwa yamelewa kutokana na kukosa usingizi.
Sammy aliyabeba mabegi waliyokuja nayo na kuelekea vyumbani akiyapeleka kwenye chumba maalumu cha wageni akimwacha Jengo mpweke. Baada ya kama dakika tano hivi alirejea na kumkuta Jengo akinyemelewa na usingizi pale pale sebuleni kwenye sofa. Miguu yake alikuwa kainyoosha. Alikuwa mchovu aliyechoshwa na mambo mengi, usingizi, safari na mawazo juu ya hali ya binti’ake Joyce.
Sammy alimwangalia kwa makini akamhurumia kisha alimwamsha na kumwelekeza chumba ili akajipumzishe kisha yeye alielekea chumbani kwake na kuingia moja kwa moja bafuni ili kupooza mwili wake. Alijimwagia maji harakaharaka kisha akajirejesha pale sebuleni ambapo alishangaa kumkuta mkwe wake akiwa bado ameketi palepale, sasa usingizi ulikuwa umemchukua kabisa.
Sammy hakutaka kumwamsha, akaketi na kuwasha runinga huku akiweka sauti ndogo akichelea kumwamsha mkwewe. Si kwamba alikuwa anatazana runinga hiyo bali ilikuwa inampa tu ‘kampani’ na kujaribu kumsahaulisha huzuni ya mkasa uliomkuta mkewe. Alijaribu kuwaza mambo kadhaa kuhusu mkasa ule, mara akahisi sauti hafifu ya kishindo ndani ya uwa wa nyumba yake.
Alinyanyuka haraka akatazama dirishani na kisha mlangoni, hakuona mtu. Akaelekea upande wa mlango wa jikoni, patupu! Akatoka nje na kuzunguka kuelekea upande wa mbele alipoegesha gari lake, akabaini kulikuwa na sauti ndogo ya kubipu. Alipata shaka, akatazama huku na kule akisaka na baada ya sekunde kama tano hivi akabaini kulikuwa na kitu fulani kimepachikwa kwenye gari! Akahisi kuwa eneo lile halikuwa salama.
“Bomu!” Sammy akawaza, na hapo akili yake ikafanya kazi haraka sana. Alirudi ndani haraka, akamshtua Jengo kuhusu uwepo wa bomu, wakatoka na kukimbilia upande wa nyuma wa ile nyumba kulikokuwa na geti dogo la dharura. Muda huo bomu lilikuwa limebakia kama sekunde tano tu kulipuka. Hata hivyo alibaini kuwa wasingeweza kufanikiwa kufungua lile geti na kutoka ndani ya muda.
“Baba, lala chini!” Sammy alimwamuru baba mkwe wake huku yeye mwenyewe akijitupa chini na kulala kifudifudi. Sekunde mbili baadaye ukasikika mlipuko mkubwa na kuisambaratisha kabisa nyumba ya Sammy. Sammy na Jengo wakaangukiwa na mabaki ya ile nyumba. Fahamu zikawapotea.
* * * * *
Gari la kifahari aina ya
Range Rover Velar la rangi nyeupe liliingia kwenye geti la kuingilia la hospitali ya Amana na kuelekezwa moja kwa moja kwenye viunga vya maegesho, likaegeshwa. Mr. Oduya na Mr. Mafuru wakashuka toka ndani ya gari na kuanza kukatiza eneo lile la maegesho. Mr. Mafuru alitoa simu yake na kumpigia Madame Norah.
“Madame, tayari tumeshafika hapa hospitali ya Amana, uko sehemu gani?” Mr. Mafuru aliongea baada ya simu kupokelewa.
“Njooni hapa kwenye mgahawa, mtatukuta tumeketi hapa,” Madame Norah alisema na mara simu ikakatwa.
Wakati wakielekea pale kwenye mgahawa kama walivyoelekezwa na Madame Norah, simu ya Mr. Oduya ikaanza kuita. Aliitoa na kuiangalia, akashusha pumzi na kuminya midomi yake, kisha akaipokea na kuiweka moja kwa moja sikioni. “Hallo!”
“Mzee, tayari kazi imeisha. Nimeshatekeleza ule mpango mzima na hakuna kilichotoka ndani,” sauti toka upande wa pili wa simu ikasikika.
“Umehakikisha haujaacha kielelezo chochote?” Mr. Oduya akauliza kwa sauti iliyoonesha wasiwasi ili kupata uhakika.
“Usiwe na wasiwasi, mkuu, kila kitu kimekwenda kama kilivyopangwa. Bado yule malaya tu,” mtu upande wa pili wa simu alijibu kwa kujiamini.
“Vizuri, lakini kumbuka yule ni mtu hatari mno na wewe kazi hii ni mpango wa kando, kosa lolote hata dogo linaweza kukugharimu na kitakachofuata kinaweza kuwa kibaya siyo kwako tu, bali kwetu sote, sijui umenielewa?” Mr. Oduya alisema huku akipiga hatua taratibu.
“Kwa hilo wala usijali, mkuu. Niko makini sana,” alisema yule mtu na simu ikakatwa. Mr. Oduya akaachia tabasamu na kutembea haraka kwa kujiamini akimfuata Mr. Mafuru aliyekuwa ametangulia mbele.
Walipotokea jirani na mgahawa wakamwona Madame Norah aliyekuwa anapunga mkono wake kuwaonesha mahali alipoketi akiwa ameketi na mwanamke mwingine ambaye hawakuweza kumtambua. Mr. Oduya na Mafuru wakamfuata, wakawasalimia wote huku wakiwapa pole kwa mkasa ule uliotokea.
Mambo bado ni 🔥🔥🔥 kwelikweli. Naona Mr. Oduya ameamua kufuta kabisa ushahidi. Je, nini kitaendelea? Ndoto ya Tunu kuipata memory card itafanikiwa? Usikose kufuatilia mkasa huu wa kusisimua uliosababishwa na 🚖...
NB:
Litro 👩🦱