karibu mkuu tuwe wote
Taxi - (113)
ILIPOISHIA
Tunu alimwangalia kwa makini huku akiendelea kutabasamu na kusema, “Ndiyo, tafadhali unaweza kuniruhusu kuingia ndani?” Tunu alisema kwa sauti tulivu.
Kidogo Lucy akaonekana kusita, hakumwamini mgeni wake. “Unaweza kuniambia hitaji lako?”
“Naomba uniruhusu niinge ndani, ninahitaji kuonana na Winifrida, nimeelekezwa hapa na kaka’ake anayeitwa Sammy,” Tunu alisema na kugeuza shingo yake, akatazama kushoto na kulia kwake kuhakikisha kuna hali ya usalama kisha halafu akamtazama tena Lucy.
Lucy akashusha pumzi. Kimya kifupi kikapita huku Lucy akionekana kutafakari kisha akauma magego na kufanya mataya yake kuchezacheza kama aliyekuwa anatafuna kitu kigumu. Mara ikasikika sauti ya Victoria, “Dada, kwani unaongea na nani?”
Lucy aligeuza shingo yake na kumwona Victoria akiwa amesimama kwenye baraza kubwa ya ile nyumba. “Anasema amekuja kumwona Winifrida, ameelekezwa hapa na Sammy,” Lucy alisema.
SASA ENDELEA...
Victoria alielekea kule getini na alipofika alichungulia nje, akamwona Tunu akiwa bado amesimama pale pale huku tabasamu usoni kwake likiwa halijaenda likizo. Victoria alimtazama kwa makini. “Habari yako, dada?” Victoria alimsalimia.
“Nzuri, anti... naitwa Tunu na...” Tunu aliitikia na kuanza kujitambulisha.
“Ooh, Tunu! Karibu ndani,” Victoria alisema na kuachia tabasamu pana kisha akamgeukia Lucy. “Mfungulie geti aingize gari lake.”
Lucy alishusha pumzi na kulifungua lile geti kubwa akimruhusu Tunu kuingia. Tunu aliingiza gari lake ndani ya uzio wa ile nyumba, akaliegesha kwenye eneo la wazi jirani na banda maalumu la wazi la maegesho ya magari. Ndani ya banda lile kulikuwa na magari mawili, moja lilikuwa
Toyota Hilux double cabin la rangi nyeupe na jingine ni aina ya
Landcruiser GX V8 rangi nyeusi.
Alitulia kidogo ndani ya gari akiliacha liungurume kwa dakika chache kisha akazima injini na kushuka. Victoria alimwongoza kuelekea ndani ambako walimkuta Pendo akiwa ameketi juu ya sofa, peke yake, akionekana mwenye huzuni. Winifrida hakuwepo.
Wakati Tunu anaingia Pendo alimwangalia pasipo kuonesha tashwishwi yoyote usoni kwake, akili yake ya kitoto ilikuwa inawaza mbali sana. Alikuwa akimwaza mama yake.
“Shemeji Sammy alinipigia simu kunijulisha kuhusu ujio wako, nilipoona muda unazidi kwenda nikajua labda umeahirisha. Karibu sana, Tunu,” Victoria alisema wakati wanaketi juu ya masofa pale sebuleni.
“Ahsante. Kuna mambo fulani yaliingiliana, ikanibidi kwanza niyaweke sawa ndipo nije huku,” Tunu alisema huku akishusha pumzi kisha akaendelea. “Na kwa kuwa nimechelewa kidogo ningeomba twende moja kwa moja kwenye suala lililonileta hapa... shida yangu ni kuongea na Winifrida, sijui yupo?”
“Alikuwapo hapa sasa hivi, nadhani kaingia chumbani maana tangu tukio la jana hawajihisi tena kama wapo salama,” Victoria alisema na kugeuza shingo yake kumwangalia Pendo. “Huyu ni mtoto wa Sammy.”
“
Okay!” Tunu alisema huku akimtupia jicho Pendo, “Hujambo, mtoto mzuri?”
“Sijambo, shikamoo anti!” Pendo alisalimia, hakuonesha ule uchangamfu ambao amekuwa nao siku zote.
“Marhaba!” Tunu alisema huku akiachia tabasamu pana.
“Pendo nenda kamwite anti Winnie,” Victoria alimwambia Pendo. Pendo akatoka na kuelekea chumbani huku akiita kwa sauti. “Anti Winnie!”
“Nawahurumia sana hawa watoto, hawako sawa kisaikolojia,” Victoria alisema kwa huzuni.
“Mnapaswa kuhakikisha wanaonana na mwanasaikolojia wa watoto ili ajaribu kuwaweka sawa,” Tunu alishauri.
“Ndiyo maana wapo hapa kwani hiyo ndiyo taaluma yangu. Nimeomba ruhusa ya siku saba kazini ili kushughulikia suala hili,” Victoria alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.
“Umefanya vyema. Hili ni suala tata zito sana na watoto hawa hawawezi kulibeba,” Tunu alisema huku akishusha pumzi. “Pia, awali ya kila jambo tunatakiwa kumshukuru Mungu.”
“Kabisa!” Victoria aliafiki na wakati huo huo Winifrida na Pendo wakaingia sebuleni. Winifrida alimtazama Tunu kwa wasiwasi mkubwa, akashusha pumzi na kumsalimia kisha akaketi juu ya sofa.
Victoria na Tunu wakaangaliana kwa muda kisha Victoria akakohoa kidogo ili kusafisha sauti yake. “Winnie, huyu dada anaitwa Tunu, ameelekezwa hapa na kaka’ako, anataka kuongea na wewe,” Victoria alisema na kuinuka, akamshika mkono Pendo.
“Sasa, da’ Tunu, ngoja tuwaache wenyewe muongee kwa uhuru zaidi,” Victoria alisema huku akianza kuondoka.
“Haina shida, dada. Tukimalizana nitakwambia,” Tunu alisema huku akijiweka sawa pale kwenye sofa. Kikatokea kitambo kifupi cha ukimya, kila mmoja alionekana kutafakari. Winifrida alikuwa anamwangalia Tunu kwa jicho la kuibia, uso wake ulionesha wasiwasi fulani.
“Winnie, kwanza nikupe pole kwa yote yaliyotokea jana usiku... Najua hivi sasa unapitia mengi tu na huoni mtu wa kumweleza. Labda si kosa lako. Na sijui ni kwa nini umeshindwa kumweleza hata kaka’ako, au unaogopa?” Tunu alimuuliza Winifrida huku akiwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wake.
Winifrida hakujibu, alibaki kimya akiangalia viganja vyake alivyoviweka juu ya mapaja yake. Tunu aliiona hali ya Winifrida kwa jinsi alivyokuwa na hofu, akatabasamu na kutafuta namna ya kuyaelekeza mazungumzo.
“Niko hapa mimi na wewe, wawili tu...” Tunu alisema na kusita, akashusha pumzi za ndani kwa ndani huku akionekana kama aliyekuwa akitafakari nini cha kusema. “Labda nikutoe wasiwasi, mimi nafanya kazi usalama wa taifa na chochote utakachoniambia, kama hupendi kaka’ako ajue kitabaki kuwa siri kati yetu. Nikutoe hofu kuwa wote waliofanya tukio hilo la kinyama watapatikana tu kama utakuwa muwazi...” Tunu alinyamaza kidogo ili maneno yale yamwingie Winifrida.
“Kwa sasa polisi wapo kazini wanawatafuta, mimi pia nimejitolea kusaidia ili kuhakikisha wote wanakamatwa... labda tu nikudokeze kuwa wapo watu ninaowahisi kufanya tukio hilo na ninazo picha zao, kwa hiyo huna sababu ya kunificha chochote unachokijua.” Tunu aliweka kituo, akaminya midomo yake yenye maki na kuficha vishimo vidogo vijitokeze kwenye mashavu yake.
“Sijui umenielewa?” Tunu alimuuliza Winifrida huku akimwangalia kwa makini.
“Nimekuelewa, dada,” Winifrida alisema, akavuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu huku akifanya kifua chake kipande na kushuka. Matiti yake madogo yaliyochongoka yalimiliki vyema eneo la kifua.
Tunu alitoa simu yake ya mkononi, ilikuwa simu nzuri na mpya kabisa aina ya
iPhone 11 Pro Max, akaanza kupekuapekua kwenye ile simu kisha akamwonesha Winifrida picha ya Spoiler. “Ulimwona mtu mwenye sura kama hii?” alimuuliza huku akimtazama katika hali ya kumkagua.
Inaendelea
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal
NB: Litro 👩