Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi (100)

Tunu aliviringika na kutambaa kama nyoka akihama kutoka sofa lile dogo na kwenda kwenye sofa kubwa. Akajilaza kimya akijaribu kusikilizia lakini akahisi chuma kikielekezwa kichwani kwake, moja kwa moja akatambua kuwa ulikuwa ni mtutu wa bastola na aliyeshika bastola hiyo alikuwa hatua moja tu toka alipolala. Mwili wake ukaingiwa na baridi.

Tunu hakutikisika wala kuinua mikono yake iliyoshika bastola. Alijua wazi kuwa alikuwa amepatikana. Hakuwa na ujanja na wala hakutakiwa kufanya lolote lile kwa pupa isipokuwa kuutii kila atakachoambiwa na mtu yule.

“Weka bastola zako chini na uinuke taratibu,” sauti ya ukakamavu ya yule mtu ilimwamrisha Tunu. Taratibu akaziweka chini bastola na kusimama akiwa amenyoosha mikono yake juu.

Alihisi kama ameona mzimu, alijikuta akitazamana na mtutu wa bastola aina ya FNX 45 Tactical yenye kiwambo cha kuzuia sauti. Bastola ile ilikuwa imeshikwa na mwanamume mfupi mwenye umbo lililojengeka kwa misuli kutokana na ratiba nzuri ya mazoezi. Mwanamume yule alikuwa amevaa fulana nyekundu iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli, suruali ya bluu ya jeans na miguuni alivaa raba nyeusi.

Tunu alimtazama kwa wasiwasi. Macho ya yule mwanamume yalikuwa na dalili zote za ukatili, uwendawazimu na unyama uliokubuhu.

“Uledi!” Tunu alimaka kwa mshangao. Alikuwa akimfahamu vyema Uledi Mkama tangu alipokutana naye katika ofisi ya Mr. Oduya wakati huo yeye Tunu akifanya kazi hapo. Alifahamu kuwa Uledi alikuwa mmoja wa vijana wawili waliokuwa wakitumwa kufanya kazi maalumu na za siri za Mr. Oduya, yeye na Dulla Mcomoro. Alikumbuka kuwa ni hawa wawili wakishirikiana na Spoiler waliohusika kwenye mauaji ya Jaji Lutego.

“Uledi!” Tunu aliita katika namna ya kutaka kumzubaisha lakini Uledi hakutaka maongezi yoyote na Tunu, yeye alidhamiria kuua na kupeleka kichwa kama alivyoagizwa na Mr. Oduya.

Alianza kuvuta ndimi ya bastola, Tunu akafumba macho kwani alijua kile ambacho kingetokea na hakutaka kuona. Mara ukasikika mlio mkubwa wa risasi kutoka kwenye bastola isiyo na kiwambo cha kuzuia sauti, damu zikamrukia Tunu ambaye alianguka sakafuni huku akihisi moyo wake ulikuwa umepoteza mapigo yake, kisha akatulia kama mfu akiwa hajui iwapo alikuwa amekufa au alikuwa ndotoni.

Sister! Sister!” Tunu akasikia sauti ya mwanamume ambayo haikuwa ngeni masikioni mwake, alihisi kuitambua vyema. Akajiuliza ameisikia wapi?

Sister... ni mimi dereva wako. Inuka tuondoke haraka kuna wenzao wataingia hapa dakika yoyote kuanzia sasa,” ile sauti ilisema tena kwa wasiwasi. Sasa aliikumba vyema. Ni kweli ilikuwa ni sauti ya yule dereva wa teksi aliyoikodi. Hata hivyo hakujitokeza kwa kuogopa kuwa huenda ulikuwa ni mtego.

Tunu aliinua uso wake kwa wasiwasi na kumwona yule dereva akiwa ameshika bastola akiangalia kule kwenye mlango mkubwa wa kuingilia sebuleni kwa wasiwasi na kuanza kutoka haraka. Tunu hakutaka kuwa mbishi, akainuka na kuokota haraka bastola yake na mkoba wake, akautupia jicho mwili wa Uledi na kuona jinsi kichwa chake kilivyokuwa kimefumuliwa kwa risasi, hakutaka kuzubaa akatoka kuanza kumfuata nyuma yule dereva.

Walielekea nyuma ya ile nyumba na wakati huo huo ukasikika muungurumo wa gari lililokuwa linaikaribia ile nyumba na kukomea mbele ya geti kubwa la nyumba ile. Hawakusubiri, wakarukia matawi ya mti yaliyokuwa yameinamia mle ndani na kupanda haraka kisha wakajirusha na kuangukia nje ya ukuta wa ile nyumba. Yule dereva akaanza kutimua mbio kuelekea bondeni. Tunu akamfuata. Baada ya mwendo mfupi wakaanza kuambaa na ule Mto Msimbazi kabla hawajaanza tena kupandisha kama wanarudi juu lakini wakiwa mbali na eneo la ile nyumba waliyotoka.

Tunu, are you okay?” yule dereva alimuuliza Tunu wakati wakikimbia. Tunu akashtuka sana kusikia yule dereva akimwita kwa jina lake, muda huo walikuwa wanapita katika vichochoro vya nyumba za eneo lile.

I’m okay!” Tunu akamjibu yule dereva kwa ufupi huku akiwa katika tahadhari kubwa. Bastola amezishika mkononi tayari kwa lolote.

“Endelea kunifuata, gari nilikwenda kulificha sehemu huko mbele ili wasinishtukie.” yule dereva alisema huku akiendelea kukimbia.

Pamoja na kuendelea kumfuata yule dereva lakini Tunu bado alikuwa katika mawazo kumuhusu yule dereva. Alikuwa anajiuliza yule nin nani hasa? Kwa nini amemwokoa toka kwa wale watu wakati inasemekana yeye pia ni mmoja wao? Je, katumwa na nani aje amwokoe? Au yeye pia ni undercover? Tunu alijiambia kuwa alikwisha hisi tangu mwanzo kuwa yule dereva hakuwa wa kawaida kama walivyo madereva wengine, alionekana mwelewa sana wa mambo na mwepesi wa kushika maelekezo.

Waliendelea kukimbia kwa kasi, yule dereva akiwa mbele na Tunu akiwa nyuma ingawa kwa upande fulani alianza kumwogopa sana. Jasho jingi lilikuwa linamtoka kwa kukimbia. Baada ya dakika kadhaa za kukimbia wakatokea kwenye kichochoro kimoja na kuikuta ile taxi ikiwa imeegeshwa hapo. Yule dereva akageuka kumtazama Tunu kwa macho makali.

“Pole sana, huo ndiyo uzalendo kwa nchi yako,” yule dereva alisema lakini Tunu hakumjibu. Alimtazama usoni kwa makini.

Mchezo unazidi kunoga, wamejitokeza wengi na sasa kuna huyu dereva wa taxi! Kuna nini ndani ya Taxi? Endelea kufuatilia hadi mwisho...

Thisi is for you Shunie
Mmh!😵😵😵 Huyu Shunie huyu si wa mchezo!🙂🙂🙂 kamfanya nini askofu hadi kasalimu amri hivihivi! Ama kweli kila mbabe ana mbabe wake!
 
View attachment 1216986

Na Bishop Hiluka
(Mwandishi wa stori za kusisimua zilizowahi kuchapishwa hapa JF za Kizungumkuti!; Laiti Ningejua!; Hekaheka!; Hadi Lini! na nyinginezo)

0685 666964 au bjhiluka@yahoo.com


SAA 1:35 asubuhi, Samuel Kambona alishuka kutoka ndani ya gari aina ya Toyota Alphard la rangi ya bluu katika viunga vya maegesho ya magari vya majengo ya hoteli ya Udzungwa Beach Resort, iliyopo katika ufukwe wa Oystebay, jijini Dar es Salaam.

Gari lile lilikuwa na nembo ubavuni iliyokuwa na maandishi ya Udzungwa Beach Resort.

Samuel maarufu kama Sammy, alikuwa kijana mtanashati mwenye umri wa miaka 35 na msomi wa Shahada ya Umahili ya Biashara za Kimataifa na Lugha (M.A in International Business with Languages), aliyoipata kutoka Chuo Kikuu cha Warwick nchini Uingereza,

Alikuwa mrefu na mweupe mithili ya chotara wa kizungu, mwenye sura ya tabasamu muda wote. Urefu, mwili wake wa kimazoezi, utanashati na asili ya ngozi yake nyeupe ni vitu vilivyowavutia wasichana wengi aliokutana nao.

Ukiongezea na ndevu nyingi alizopenda kuzinyoa katika mtindo wa circle beard au kama wengi walivyozoea kuita “O”, vilimfanya azidi kuwa mvuto mkubwa kwa walimbende pindi walipomtia machoni.

Siku ile ilikuwa Ijumaa, kama kawaida yake, Sammy alikuwa katika mwonekano maridadi kabisa, akiwa amevalia shati zuri la rangi ya samawati la kitambaa brandi ya Barba ndani ya suti nyeusi ya aina ya Dunhill, tai ya rangi ya bluu shingoni na viatu ghali vya ngozi halisi kutoka nchini Switzerland.

Pia alikuwa amevaa saa ya mkononi aina ya Cartier iliyokuwa na nakshi ya madini ya dhahabu na kujipulizia manukato ghali aina ya Dolce & Gabbana. Mkononi alikuwa amebeba mkoba wake mdogo wa kiofisi aina ya Pad & Quill wa rangi ya hudhurungi.

Wakati akishuka kutoka kwenye gari manyunyu mepesi ya mvua yalikuwa yakianguka ardhini, lakini bado hayakumzuia Sammy kutembea taratibu akikatisha kwenye viunga vya maegesho ya magari na kuelekea mbele ya jengo la mbele la ile hoteli ya kitalii yenye hadhi ya nyota tano.

Wakati akitembea macho yake yaliangaza huku na kule kana kwamba alikuwa akitafuta kitu. Alipishana na askari mmoja wa ulinzi kutoka kampuni ya ulinzi ya Spark K7 aliyekuwa akilinda eneo lile la viunga vya maegesho ya magari.

Eneo lile lilikuwa pana likiwa na uwezo wa kuruhusu magari madogo hadi 100 kuegeshwa kwa wakati mmoja, na lilikuwa limepandwa miti mirefu ya kivuli aina ya ‘Quercus virginiana’ na ‘Arecaceae’ iliyojulikana pia kama ‘coconut palms’.

Pia eneo lile lilipandwa nyasi nzuri laini aina ya ‘Citronella’ na kulikuwa na bustani ya maua ya kupendeza yaliyotoa hewa safi ya upepo wa asili baina ya sehemu moja ya maegesho ya magari na sehemu nyingine, ndani ya uzio wa yale majengo ya hoteli.

Kwa yeyote aliyefika Udzungwa Beach Resort angeweza kubaini mara moja kuwa majengo ya hoteli hiyo yalijengwa kwa ufanisi wa hali ya juu.

Kulikuwa na majengo makuu mawili, moja lilikuwa mbele na la pili lilikuwa nyuma na kila moja lilikuwa na ghorofa saba za juu na mbili za chini, zilizotumika kwa ajili ya kumbi za burudani, kumbi za mikutano na migahawa ya kisasa ya chakula cha kitanzania na cha kimataifa. Pia kulikuwa na maduka na ofisi za utawala kwenye orofa ya chini nay a kwanza ya jengo la mbele.

Katika eneo lile kulikuwa na duka kubwa la bidhaa mbalimbali maarufu kama “supermarket”, duka kubwa la vipodozi na nguo za kisasa (boutique), na duka la kubadilishia fedha za kigeni maarufu kama “Bureau de Change” na vyumba viwili vidogo vyenye Mashine za ATM

Pia kulikuwa na jengo maalumu la klabu iliyojulikana kama Paradise Club, ambayo ilikuwa kwenye jengo la nyuma iliyowakutanisha mabilionea na baadhi ya vigogo serikalini na ilikuwa na ulinzi mkubwa sana, nje na ndani ya klabu.

Walioruhusiwa kuingia ndani ya klabu hiyo ni wanachama tu waliokidhi vigezo na kusajiliwa, ambao walilipa kiasi kikubwa cha ada ya uanachama kila mwaka.

Ndani ya majengo yote ya hoteli hiyo kulikuwa na kamera za usalama (CCTV) kila kona, viyoyozi vilivyosambaa kila mahali, na kutoka ghorofa moja kwenda nyingine kulikuwa na ngazi za kawaida na vyumba maalumu vya lifti za kisasa. Pia kulikuwa na ngazi iliyoendeshwa kwa umeme.

Yale majengo yalijengwa katika eneo tulivu mno lisilo na bughudha la ufukwe wa Oysterbay, jirani kabisa na ofisi za kibalozi na makazi ya watu wenye ukwasi, takriban kilomita tatu tu kutoka katikati ya jiji la Dar es Salaam.

Kwa watu wengi wenye ukwasi, Udzungwa Beach Resort ilikuwa ndiyo sehemu nzuri na tulivu zaidi ya kwenda kujipumzisha na kufurahia maisha, kwani ilikuwa imezungushiwa uzio madhubuti wenye ulinzi na kamera za usalama ulioifanya kuwa mahali patulivu zaidi na pa usalama wa uhakika.

Asubuhi ile kulikuwa na magari machache madogo na mabasi mawili ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya Cape Town cha nchini Afrika Kusini na Chinhoyi cha nchini Zimbabwe yaliyokuwa yameegeshwa katika viunga vya maegesho ya magari.

Pia kulikuwa na malori mawili makubwa ya kubebea watalii wa masafa marefu aina ya Mercedes Benz, yaliyokuwa yameegeshwa mwisho kabisa wa yale majengo.

Mbele ya ile hoteli katika jengo la mbele Sammy aliipita milingoti saba iliyokuwa na bendera za Afrika Mashariki, Marekani, Uingereza, India, China, Afrika Kusini na bendera yenye nembo ya Udzungwa Beach Resort, zilizokuwa zinapepea taratibu.

Kulikuwa na mlango mkubwa wa vioo mbele ya jengo na varanda pana yenye ngazi iliyofunikwa kwa kofia nzuri ya zege ikiwa na sakafu nzuri yenye marumaru iliyonakshiwa kwa maandishi ya “Udzungwa Beach Resort”.

Kijana mmoja askari wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7 alikuwa amesimama kikakamavu kwenye ile varanda pana akiwa kando ya ule mlango mkubwa wa vioo wa kuingilia ndani. Yule askari wa ulinzi aliyeitwa Fred Luvanda alimuona Sammy na kumpokea kwa tabasamu la kirafiki lililokuwa na bashasha zote kwenye uso wake.

Endelea kufuatilia...
huyo kijana askari ni mnoko mnoko anaonekana...
 
Taxi - (103)

ILIPOISHIA

Tunu alikiri kuwa hajawahi kumwona Tom miongoni mwa mashushushu wa Tanzania ingawa tangu mwanzo alihisi kuwa alikuwa amemkodi mtu mwenye ujuzi wa ziada katika shughuli za aina ile. Alimshukuru sana Mungu kwa kumleta Tom katika maisha yake.

Tom alikuwa mzaliwa wa Dodoma na alikuwa na umri wa miaka thelathini. Alisoma Shule ya Sekondari Ilboru hadi kidato cha nne na baadaye kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora kisha akajiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa masomo ya Sayansi ya Jamii. Alipohitimu akapata udhamini wa kwenda nchni Ubelgiji kwa masomo ya saikolojia kabla hajajiunga na mafunzo ya awali ya ujasusi nchini Ufaransa na baadaye akaelekea nchini China ambako alihitimu vyema.

Tangu ajiunge na Idara ya Usalama wa Taifa, Tom alionekana kuwa na uwezo mkubwa sana na mbinu nyingi za kiupelelezi, akipenda kufanya kazi zake kama undercover (akijifanya dereva wa taxi na kazi nyingine za kujishusha ili kukamilisha majukumu yake). Kwa sababu ya tabia yake ya ucheshi, kujichanganya na watu, kutokubagua kazi na heshima kwa kila mtu ilikuwa rahisi sana kwa Tom kupata taarifa nyingi na haikuwa rahisi kushtukiwa.

SASA ENDELEA...

Likiwa gari lenye miaka minne katika mitaa ya jiji la Dar es Salaam, Tom alipata kuchukua abiria wa aina mbalimbali ndani ya gari hilo, akiwatoa hapa na kuwapeleka pale. Wapo wenye tabia za ajabu, wenye maneno ya ajabu, wenye mipango ya ajabu, wapiga dili na matapeli, wazinzi wa wake au waume wa watu n.k. ili mradi kila abiria alitofautiana na mwingine kwa hili na lile. Hata hivyo, wote walikuwa abiria wake.

Ni katika kazi hiyo amekuwa akipata taarifa nyeti za kiintelijensia kutoka kwa abiria wake, kwani alizifahamu lugha nyingi. Ukiacha lugha za kimataifa za Kiingereza, Kifaransa, Kihispaniola na Kichina, aliweza pia kuongea lugha za makabila mbalimbali ya Tanzania. Ni katika kazi yake ya kuendesha taxi ndipo alipoweza kukutana na akina Lisa, Uledi na Dulla Mcomoro.

Mwanzoni hakuwa akiwaelewa kabisa, walikuwa ni watu wenye maneno na vitendo visivyoeleweka wala kuelezeka. Japo walikuwa na magari yao, tena ya kifahari, lakini walipenda kukodi taxi kwa mambo yao ili kupoteza lengo la waliokuwa wakiwafuatilia.

“Tunu!” Tom alimwita Tunu baada ya kumaliza kuongea na simu, maongezi yaliyomchukua zaidi ya dakika ishirini. “Umepata taarifa yoyote kuhusu Sammy?” Tom alimuuliza Tunu huku akimkazia macho.

“Hapana, Tom, sijapata taarifa zozote. Kwani kuna taarifa gani?” Tunu aliuliza huku uso wake ukionesha mashaka makubwa.

“Chanzo changu cha taarifa ndani ya jeshi la polisi kinanieleza kuwa watu wawili walimteka wakati akirudi nyumbani kwake baada ya kupigiwa simu na mkewe, wakalipekua gari lake, inaonesha kuna kitu walikuwa wanatafuta lakini hawakukipata...”

“Hilo nalifahamu,” Tunu alisema kwa sauti tulivu huku akiyatuliza macho yake kwenye uso wa Tom.

“Unalifahamu!” Tom akauliza kwa mshangao.

Yeah! Walikuwa watu wangu. Niliwatuma kuitafuta memory card yenye ushahidi muhimu sana kuhusu kifo cha Jaji Lutego,” Tunu alisema.

“Ushahidi wa mauaji ya Jaji Lutego upo kwenye memory card! Imefikaje kwenye gari la Sammy?” Tom alionesha kuchanganyikiwa. “Tunu, naona unazidi kunishangaza! Naomba nikiri katika kazi zangu sijawahi kukutana na shushushu wa aina yako, haukuwepo nchini kwa kipindi kirefu lakini unaelewa mambo mengi!”

“Suala la memory card nitakueleza baadaye lakini kwanza naomba unisaidie kupata taarifa zote kuhusu mikakati ya Mr. Oduya,” Tunu alisema huku akiachia tabasamu. “Narudia tena kukushukuru kwa kuniokoa, najua umehatarisha maisha yako ili kuhakikisha ninakuwa salama. Wakati nakukodi sikuwa najua kabisa kuwa nimemchukua mtu hatari lakini ni muhimu sana kwenye mission yangu...”

“Usijali, nilipokuona unakimbilia taxi nilihisi wewe ni mtu wa kitengo na una mission muhimu sana ya ku-accomplish, ndiyo maana ilibidi nikuwahi kabla mtu mwingine hajakuwahi. Mimi pia siko tayari kuona Mr. Oduya anakuwa rais wa nchi hii,” Tom alisema na kuendelea, “Kwa kuwa sasa nimekupata wewe, sina hofu tena ya kitu chochote. Natumai tutafanikiwa kulizima jaribio hilo…”

“Siyo tu kulizima, bali pia maisha ya mzee huyo yanaishia gerezani,” Tunu alidakia. Kikapita kitambo kifupi cha ukimya.
“Kwa hiyo na hili la Sammy kuvamiwa nyumbani kwake na mkewe kupigwa risasi pia unalijua?” Tom alimuuliza Tunu huku akimkazia macho baada ya kitambo kifupi cha ukimya.

“Unasema nani kavamiwa nyumbani kwake?” Tunu aliuliza huku akionesha mshtuko mkubwa.

“Sammy,” Tom alisema, macho yake alikuwa ameyatuliza usoni kwa Tunu.

Oh my God!” Tunu alimaka kwa mshtuko huku akihisi kuchanganyikiwa. Alikuwa anapumua kwa nguvu. “Kwa vyovyote waliofanya hivyo watakuwa ni watu wa Mr. Oduya,” Tunu alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

* * * * *

Saa kumi na moja alfajiri usiku Mr. Oduya alikuwa amesimama jirani na dirisha ndani ya ofisi yake binafsi kwenye jengo lake la kifahari la ghorofa mbili lililopo Mikocheni jirani na Rose Garden. Hadi muda huo hakuwa ameambua japo lepe la usingizi kutokana na taarifa alizokuwa akizipata kutoka kwa watu wake aliowatuma kukamilisha kazi maalumu.

Alikuwa amefika katika nyumba hiyo baada tu ya kupata taarifa ya kile kilichotokea kule Karakata nyumbani kwa Lisa. Kama kuna siku aliumia sana basi ni siku hiyo, vifo vya watu wake muhimu watatu: Dulla Mcomoro, Uledi na Lisa vilikuwa vimemchanganya kupita maelezo. Hawa watatu pamoja na Spoiler walikuwa watu wake muhimu sana katika oparesheni zake za siri.

Tangu afike katika nyumba hiyo saa mbili zilizopita alikuwa anavuta sigara mfululizo na hadi muda huo alikuwa tayari amekwisha maliza pakti mbili na nusu za sigara akiwaza na kuwazua pasipo kupata majibu. Alikuwa amekanganyikiwa, mambo hayo hayakuwa yamemwingia kichwani kabisa! Ni vipi Tunu akafanikiwa kutoroka kwenye mikono ya Lisa na Uledi? Watu wenye mafunzo ya mapigano, wenye silaha na wafanisi?

Aliwatazama Spoiler na Job walioketi mbele yake huku wamejiinamia. Walikuwa na nyuso zilizoonesha wasiwasi mkubwa.

“Kwa hiyo?” Mr. Oduya akauliza. Alikuwa bado amesimama jirani na dirisha kandokando ya meza yake akiwa ameshika kiuno. Mche wa sigara ukiwa umebanwa kwenye pembe ya mdomo wake na uso wake ukiwa umemezwa na fikra lakini pia sononeko.

“Kwa hiyo si Sammy wala gari lake vilivyopatikana hadi muda huu! Na Tunu naye amefanikiwa kutoroka,” Mr. Oduya alisema kwa sauti ya chini kama aliyekuwa akiwaza. Akatingisha kichwa. “Sielewi, ninaomba maelezo mafupi sasa hivi kwa nini umeshindwa kukamilisha kazi hii.”

“Nadhani, bosi, nadhani hatutakuwa na maelezo ya kukuridhisha kwa nini hadi sasa hatukufanikiwa katika msheni, kwa sababu...”

“Ni wazembe!” Mr. Oduya alimkatiza kwa kufoka, uso wake kaukunja. “Au kuna sababu nyingine?”

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko
 
Taxi - (104)

Spoiler alimtupia jicho Job mara moja kisha akajiweka vizuri kitini. Alishaanza kuingiwa na hofu iliyochanganyika na woga. Alikuwa na kila sababu ya kujisikia vile. Mr. Oduya hakuwa tu mfanyabiashara na mwanasiasa wa kawaida, alikuwa mafia na katili kupindukia asiyeruhusu makosa ya kipumbavu yaliyoashiria uzembe yatokee kwenye mipango yake.

Kwa macho ya kawaida ungeweza kudhani Mr. Oduya ni mfanyabiashara wa kawaida kama walivyo wafanyabiashara na mabilionea wengine lakini huyu ni mtu ambaye kwa sifa zake za umafia angeweza kumfuatilia hata shetani katika harakati zake za kuharibu misheni zake, akamtia adabu... alikuwa na watu wa kuifanya kazi hii wa nyanja zote, kuanzia kwenye taasisi nyeti serikalini hadi watoto wa kihuni, ambao wala wao wenyewe wala hawakujuana. Spoiler alitambua alikuwa anaongea na mtu wa aina gani.

“Siyo wazembe, boss,” Spoiler alisema kwa sauti ya chini.

“Kumbe nini?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler huku akimtolea macho.

“Kama ulivyosikia kuhusu Sammy, wakati sisi tukiwa nyumbani kwake yeye alikuwa na Tunu kule ELLI’S, kama ni kufeli ni Lisa na Uledi ndio waliotufelisha...” Spoiler alisema na kutowesha koo lake lililokauka. “Nitajitahidi ku...”

“Kufanya nini?” Mr. Oduya akafoka. “Hivi kinachowashinda kumaliza kazi hii tukakaa kwa amani ni kitu gani? Mbona mnaanza kuwa wajinga kiasi hiki?” Mr. Oduya alifoka na kufoka huku mate yakiruka. Alikuwa ameghafirika kweli kweli. Mikakati ya muda mrefu kuutaka urais wa nchi lakini mwisho wa siku anapewa taarifa za upuuzi. Inamaana kazi yake nzima ilikuwa imeharibika!

“Wangefanya wengine ningeweza kuelewa lakini siyo wewe Silas, hivi ni wewe wa kushindwa kumpata Sammy eti kwa sababu alikuwa na Tunu? Ni wewe wa kushindwa kuliteketeza gari lake?” Mr. Oduya alifoka kwa hasira. “Unajua upo hapa kwa sababu una uwezo mkubwa, kwa sababu ninakulipa fedha nzuri sana ambayo hata mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano hawalipwi! Sasa unapoanza kushindwa kwenye kazi ndogo kama hii unanifanya nianze kukutilia mashaka. Ina maana unazidiwa akili na Tunu? Hii ni mara ya pili sasa Tunu amekutoa knock out!

“Hapana, si...”

“Ni nini basi? Kweli upo hapa kuniambia eti binti shushushu amekushinda?”

Spoiler alimlaani Mr. Oduya kimoyomoyo, kisha akasema, “Mkuu… mkuu, hai...”

“Hai kitu gani?”

“Ni kweli kosa limefanyika lakini sisi si wazembe, kama unavyotutuhumu. Tumefanya kazi ngapi kubwa na za hatari zaidi ya hii?” Spoiler alisema huku akijitahidi kuzuia hasira zake zilizoanza kumpanda. Hakuwa mtu wa kudharauliwa kiasi hicho. Kitu fulani cha moto kilikuwa kinauchemsha mwili na joto kali likaibuka ndani yake. Lakini alijizuia kufanya chochote mbele ya Mr. Oduya.

Mr. Oduya alishusha pumzi, akaketi juu ya kiti na kuegemea. Ni kweli kabisa Spoiler ni mtu shupavu, anayefanya kazi kwa kujituma bila ya kuhitaji kusimamiwa au kuhimizwa. Mr. Oduya mwenyewe humtegemea yeye katika kazi zake zote hatari.
“Okay!” Mr. Oduya alisema, safari hii sauti yake ilikuwa yenye utulivu, na mikunjo ya hasira usoni mwake ilipungua.

Alianza kuwaza, sasa mambo yalizidi kuwa magumu. Hakuwa amelichukulia suala la Sammy kwa uzito mkubwa kwa kujua alikuwa anadili na Sammy peke yake, mtu wa kawaida ambaye angeweza kummudu pasipo kuhitaji kutumia nguvu na rasilimali zake nyingi. Lakini sasa kulikuwa na huyu Tunu, hata hakujua alitokea wapi na kuja kutibua mipango yake! Huyu Tunu hakuwa mwanamke wa kawaida.

Mr. Oduya aliona anatakiwa kutafuta njia mbadala za kuwapata wote, Tunu na Sammy. Kwa Sammy isingeweza kazi ngumu kumpata na kumyamazisha pamoja na makosa yaliyofanyika, lakini huyo Tunu angempataje? Alihisi kama kichwa chake kinapasuka. Njia mbadala ya kumpata binti huyo ingekuwa ni kwa kupitia Nelson Mtokambali, aliyekuwa boyfriend wake, lakini walishatibuana. Ni Nelson ndiye aliyewashtua kuwa Tunu ni shushushu aliyebobea ambaye alikuwa pale kuchunguza nyendo za Mr. Oduya.

Aliamini kuwa Tunu alikuwa anajua kila mbinu za kiintelijensia. Alikuwa anajua michezo yote ya silaha na amefundishwa namna gani ya kutumia akili yake mara tatu zaidi ya shushushu wa kawaida. Ni mtaalamu wa mapigano ya silaha na pia pasipo silaha. Kwake yeye, Tunu ni adui mkubwa kuliko gaidi yeyote toka kwenye makundi hatari ya kigaidi, kwani alimfahamu vizuri yeye (Mr. Oduya) na kampani yake karibu yote.

Tunu aliifahamu mifumo, mipango na harakati zake kama kiganja cha mkono wake wa kuume. Hivyo Mr. Oduya alijionya kuwa makini sana anapotaka kudili na binti huyo.

“Nataka kusikia habari za kifo cha Tunu, sijui mmenielewa!” Mr. Oduya alipaza sauti kana kwamba alikuwa anaongea na watu waliokuwa mita hamsini mbali na yeye. Aliposema hayo alitulia tena akafikiria kidogo, mdomo wake ulikuwa mkavu kwa sababu ya moshi wa sigara.

“Atakayefanikiwa kumuua Tunu, ama kuniletea hapa mwili wake nitamlipa shilingi bilioni hamsini papo hapo! Cash!” Mr. Oduya alisema kwa msisitizo, na kuendelea, “Kama mnadhani ni kazi ngumu semeni niwatume watu wengine kuifanya, maana nina watu wengi wa kuifanya kazi hii.”

Spoiler na Job wakatazamana kama vile wakiulizana nani hawezi kufanya kazi ile. Kisha wote wawili wakashusha pumzi kwa pamoja.

* * * * *

Saa tatu na nusu asubuhi Sammy alikuwa ameketi nje ya chumba cha uangalizi maalumu katika hospitali ya Amana, alikuwa amefika hapo mara tu alipoweka mambo sawa nyumbani kwake. Kwa kushirikiana na Elli, Sammy aliwahamisha Winifrida na Pendo na kuwapeleka Kurasini, nyumbani kwa Elli.

Alichokikuta pale hospitali baada ya kufika kilimmaliza nguvu. Joyce alikuwa amewekewa mashine maalumu ya kumsaidia kupumua baada ya hali yake kubadilika ghafla. Muda ule madaktari na wauguzi walikuwa wanahangaika kuokoa maisha yake, Sammy hakuruhusiwa kuingia wodini.

Itaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom