Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

haloooooooothis iz 4u shunie
Taxi (100)

Tunu aliviringika na kutambaa kama nyoka akihama kutoka sofa lile dogo na kwenda kwenye sofa kubwa. Akajilaza kimya akijaribu kusikilizia lakini akahisi chuma kikielekezwa kichwani kwake, moja kwa moja akatambua kuwa ulikuwa ni mtutu wa bastola na aliyeshika bastola hiyo alikuwa hatua moja tu toka alipolala. Mwili wake ukaingiwa na baridi.

Tunu hakutikisika wala kuinua mikono yake iliyoshika bastola. Alijua wazi kuwa alikuwa amepatikana. Hakuwa na ujanja na wala hakutakiwa kufanya lolote lile kwa pupa isipokuwa kuutii kila atakachoambiwa na mtu yule.

“Weka bastola zako chini na uinuke taratibu,” sauti ya ukakamavu ya yule mtu ilimwamrisha Tunu. Taratibu akaziweka chini bastola na kusimama akiwa amenyoosha mikono yake juu.

Alihisi kama ameona mzimu, alijikuta akitazamana na mtutu wa bastola aina ya FNX 45 Tactical yenye kiwambo cha kuzuia sauti. Bastola ile ilikuwa imeshikwa na mwanamume mfupi mwenye umbo lililojengeka kwa misuli kutokana na ratiba nzuri ya mazoezi. Mwanamume yule alikuwa amevaa fulana nyekundu iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli, suruali ya bluu ya jeans na miguuni alivaa raba nyeusi.

Tunu alimtazama kwa wasiwasi. Macho ya yule mwanamume yalikuwa na dalili zote za ukatili, uwendawazimu na unyama uliokubuhu.

“Uledi!” Tunu alimaka kwa mshangao. Alikuwa akimfahamu vyema Uledi Mkama tangu alipokutana naye katika ofisi ya Mr. Oduya wakati huo yeye Tunu akifanya kazi hapo. Alifahamu kuwa Uledi alikuwa mmoja wa vijana wawili waliokuwa wakitumwa kufanya kazi maalumu na za siri za Mr. Oduya, yeye na Dulla Mcomoro. Alikumbuka kuwa ni hawa wawili wakishirikiana na Spoiler waliohusika kwenye mauaji ya Jaji Lutego.

“Uledi!” Tunu aliita katika namna ya kutaka kumzubaisha lakini Uledi hakutaka maongezi yoyote na Tunu, yeye alidhamiria kuua na kupeleka kichwa kama alivyoagizwa na Mr. Oduya.

Alianza kuvuta ndimi ya bastola, Tunu akafumba macho kwani alijua kile ambacho kingetokea na hakutaka kuona. Mara ukasikika mlio mkubwa wa risasi kutoka kwenye bastola isiyo na kiwambo cha kuzuia sauti, damu zikamrukia Tunu ambaye alianguka sakafuni huku akihisi moyo wake ulikuwa umepoteza mapigo yake, kisha akatulia kama mfu akiwa hajui iwapo alikuwa amekufa au alikuwa ndotoni.

Sister! Sister!” Tunu akasikia sauti ya mwanamume ambayo haikuwa ngeni masikioni mwake, alihisi kuitambua vyema. Akajiuliza ameisikia wapi?

Sister... ni mimi dereva wako. Inuka tuondoke haraka kuna wenzao wataingia hapa dakika yoyote kuanzia sasa,” ile sauti ilisema tena kwa wasiwasi. Sasa aliikumba vyema. Ni kweli ilikuwa ni sauti ya yule dereva wa teksi aliyoikodi. Hata hivyo hakujitokeza kwa kuogopa kuwa huenda ulikuwa ni mtego.

Tunu aliinua uso wake kwa wasiwasi na kumwona yule dereva akiwa ameshika bastola akiangalia kule kwenye mlango mkubwa wa kuingilia sebuleni kwa wasiwasi na kuanza kutoka haraka. Tunu hakutaka kuwa mbishi, akainuka na kuokota haraka bastola yake na mkoba wake, akautupia jicho mwili wa Uledi na kuona jinsi kichwa chake kilivyokuwa kimefumuliwa kwa risasi, hakutaka kuzubaa akatoka kuanza kumfuata nyuma yule dereva.

Walielekea nyuma ya ile nyumba na wakati huo huo ukasikika muungurumo wa gari lililokuwa linaikaribia ile nyumba na kukomea mbele ya geti kubwa la nyumba ile. Hawakusubiri, wakarukia matawi ya mti yaliyokuwa yameinamia mle ndani na kupanda haraka kisha wakajirusha na kuangukia nje ya ukuta wa ile nyumba. Yule dereva akaanza kutimua mbio kuelekea bondeni. Tunu akamfuata. Baada ya mwendo mfupi wakaanza kuambaa na ule Mto Msimbazi kabla hawajaanza tena kupandisha kama wanarudi juu lakini wakiwa mbali na eneo la ile nyumba waliyotoka.

Tunu, are you okay?” yule dereva alimuuliza Tunu wakati wakikimbia. Tunu akashtuka sana kusikia yule dereva akimwita kwa jina lake, muda huo walikuwa wanapita katika vichochoro vya nyumba za eneo lile.

I’m okay!” Tunu akamjibu yule dereva kwa ufupi huku akiwa katika tahadhari kubwa. Bastola amezishika mkononi tayari kwa lolote.

“Endelea kunifuata, gari nilikwenda kulificha sehemu huko mbele ili wasinishtukie.” yule dereva alisema huku akiendelea kukimbia.

Pamoja na kuendelea kumfuata yule dereva lakini Tunu bado alikuwa katika mawazo kumuhusu yule dereva. Alikuwa anajiuliza yule nin nani hasa? Kwa nini amemwokoa toka kwa wale watu wakati inasemekana yeye pia ni mmoja wao? Je, katumwa na nani aje amwokoe? Au yeye pia ni undercover? Tunu alijiambia kuwa alikwisha hisi tangu mwanzo kuwa yule dereva hakuwa wa kawaida kama walivyo madereva wengine, alionekana mwelewa sana wa mambo na mwepesi wa kushika maelekezo.

Waliendelea kukimbia kwa kasi, yule dereva akiwa mbele na Tunu akiwa nyuma ingawa kwa upande fulani alianza kumwogopa sana. Jasho jingi lilikuwa linamtoka kwa kukimbia. Baada ya dakika kadhaa za kukimbia wakatokea kwenye kichochoro kimoja na kuikuta ile taxi ikiwa imeegeshwa hapo. Yule dereva akageuka kumtazama Tunu kwa macho makali.

“Pole sana, huo ndiyo uzalendo kwa nchi yako,” yule dereva alisema lakini Tunu hakumjibu. Alimtazama usoni kwa makini.

Mchezo unazidi kunoga, wamejitokeza wengi na sasa kuna huyu dereva wa taxi! Kuna nini ndani ya Taxi? Endelea kufuatilia hadi mwisho...

Thisi is for you Shunie
 
Taxi - (101)

ILIPOISHIA

Pamoja na kuendelea kumfuata yule dereva lakini Tunu bado alikuwa katika mawazo kumuhusu yule dereva. Alikuwa anajiuliza yule nin nani hasa? Kwa nini amemwokoa toka kwa wale watu wakati inasemekana yeye pia ni mmoja wao? Je, katumwa na nani aje amwokoe? Au yeye pia ni undercover? Tunu alijiambia kuwa alikwisha hisi tangu mwanzo kuwa yule dereva hakuwa wa kawaida kama walivyo madereva wengine, alionekana mwelewa sana wa mambo na mwepesi wa kushika maelekezo.

Waliendelea kukimbia kwa kasi, yule dereva akiwa mbele na Tunu akiwa nyuma ingawa kwa upande fulani alianza kumwogopa sana. Jasho jingi lilikuwa linamtoka kwa kukimbia. Baada ya dakika kadhaa za kukimbia wakatokea kwenye kichochoro kimoja na kuikuta ile taxi ikiwa imeegeshwa hapo. Yule dereva akageuka kumtazama Tunu kwa macho makali.

“Pole sana, huo ndiyo uzalendo kwa nchi yako,” yule dereva alisema lakini Tunu hakumjibu. Alimtazama usoni kwa makini.

SASA ENDELEA...

“Panda tuondoke, hapa pia si mahala salama. Bado tunakabiliwa na hatari kubwa,” yule dereva alisema huku akifungua mlango na kuingia ndani ya gari. Tunu naye akaingia na gari likaondoka kwa mwendo wa kasi.

* * * * *
Saa saba usiku katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ilala, ya Amana, Sammy alikuwa amesimama jirani na mlango wa chumba cha upasuaji uliokuwa umefungwa na hakuruhusiwa mtu asiyehusika kuingia ndani ya chumba kile, aliamua asubirie pale nje huku akijaribu kuchungulia mle ndani kupitia kioo kikubwa cha mlangoni.

“Ee Mungu, naomba umponye mke wangu, Joyce,” Sammy alikuwa akiomba Mungu kimoyomoyo na aliendelea kuyatamka maneno hayo mara kwa mara.

Elli alikuwa ameketi kando kwenye benchi akiwa amejiinamia kwa huzuni, mambo mengi yalipita kichwani kwake akijaribu kuwaza na kuwazua hili na lile pasipo kupata majibu.

“Maskini mke wangu, tafadhali usiniache... Tafadhali usiondoke na kuniacha na mtoto!” Sammy aliwaza huku akichungulia ndani ya kile chumba cha upasuaji kupitia kile kioo.

Hadi muda ule hali ya Joyce iliendelea kuwa tete na Sammy hakuwa ameketi wala kubanduka pale karibu na mlango, alikuwa akifuatilia kwa karibu sana kila hatua akihofia hali ya mkewe.

Alianza kujiuliza, ni nani waliomshambulia Joyce? Je, shida yao ilikuwa kuiba au kuna kitu walikuwa wakikihitaji? Nini walikuwa wanakihitaji kutoka kwake? Je, kulikuwa na uhusiano wowote kati ya simu aliyopigiwa na Joyce kuwa Pendo amezidiwa na tukio lile la kuvamiwa na kupigwa risasi? Kilichomshangaza ni pale alipofika nyumbani akamkuta Pendo mzima wa afya akiwa hana dalili yoyote ya kuumwa.

“Hii inaweza kuwa nini maana yake?” Sammy akajiuliza. Akiwa ametulia akitafakari mara akaona mlango wa kile chumba cha upasuaji ukifunguliwa na mhudumu mmoja wa chumba cha upasuaji akatoka. Alikuwa mwanamke mrefu aliyekuwa amevaa mavazi rasmi ya hospitali. Alipotaka kupiga hatua Sammy na Elli wakamkabili ili kujua hali ya Joyce.

“Bado yuko kwenye upasuaji. Endeleeni kusubiri hadi upasuaji ukimalizika mtajulishwa kila kitu,” yule mhudumu alisema na kuendelea na safari yake.

Sammy alishusha pumzi na kushika kiuno chake kwa mikono yote miwili, ni wazi alionekana kukata tamaa. Elli alimtazama Sammy kwa huzuni na kumshika kwenye bega.

“Sammy, hebu kaa utulie, ukiendelea kusimama hapa utachoka sana kwani hatujui upasuaji utachukua muda gani, yawezekana ukachukua muda mrefu,” Elli alimsihi Sammy.

“Nashindwa kukaa, Elli. Ninapata wakati mgumu sana ni kwa vile hujui tu,” Sammy alijibu huku machozi yakimlengalenga machoni na mara akakumbuka jambo na kuchukua simu yake, akatafuta namba fulani na kupiga, kisha akaweka simu kwenye sikio lake. Simu iliita kwa muda mrefu bila kupokewa hadi ikakata. Akapiga tena, simu ikaita mara moja tu na kupokewa.

“Hallo!” sauti ya mwanamume upande wa pili wa simu ikasikika mara baada ya simu kupokewa. Sammy aliitambua sauti ile, ilikuwa sauti ya Rafael Jengo, baba’ake Joyce.

“Shikamoo, mzee wangu!” Sammy alisalimia kwa unyenyekevu, hata hivyo uso wake haukuficha wasiwasi wake.
“Marhaba, mwanangu, vipi mbona usiku sana, kwema huko?” sauti ya upande wa pili wa simu ikasikika ikiuliza kwa wasiwasi.

“Kuna tatizo, mzee wangu... niko hapa hospitali, Joyce amepigwa risasi na watu wasiojulikana...” Sammy alianza kuelezea lakini sauti upande wa pili wa simu ikamkata kauli.

“Tafadhali usinitanie,” Mzee Jengo alisema kwa sauti ya kutetemeka akionekana kushtushwa sana na taarifa zile.
“Si utani, baba’angu, ni kitu cha kweli kabisa. Tupo hapa hospitali ya Amana na Joyce yupo katika chumba cha upasuaji,” Sammy alisema huku hofu ikimtambaa mwilini mwake.

“Mungu wangu!” Mzee Jengo alimaka kwa mshtuko, alihisi moyo wake ukipoteza mapigo yake. Kikatokea kitambo fulani cha ukimya. “Amepigwa risasi saa ngapi na imetokeaje?” hatimaye Mzee Jengo aliuliza baada ya kile kitambo cha ukimya.

“Mimi sikuwepo nyumbani, ilikuwa around saa nne usiku kuelekea saa tano, watu wawili walivamia nyumbani wakiwa na pikipiki, inasemekana walikuwa wamevaa mavazi yaliyoficha sura zao zisiweze kutambulika...” Sammy alisema na kushusha pumzi, akafuta machozi yaliyokuwa yakimlengalenga machoni.

Kikapita tena kitambo kingine cha ukimya, kisha Mzee Jengo akashusha pumzi ndefu, “Ahsante sana kwa taarifa hii. Ngoja nimwambie na mama’ake, kesho mchana tutakuwa hapo,” alisema na kukata simu.

Sammy alibaki akiitazama simu yake kana kwamba alikuwa akiiona kwa mara ya kwanza. Hata hivyo, mawazo hayakuwa kwenye ile simu. Baada ya kitambo aliirudisha simu yake mfukoni kisha wakaendelea kukaa pale nje kwa muda mrefu. Ilipotimia saa kumi na moja alfajiri ndipo daktari mmoja alitoka na kuwapa taarifa.

Aliitwa Daktari Mshana, alikuwa mtu mzima, mrefu wa futi sita na ushee, mweupe na mwembamba aliyekuwa na macho ya upole. Aliwatazama Sammy na Elli kwa makini na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Vipi, daktari, vipi hali ya mgonjwa wetu?” Elli aliuliza kwa wasiwasi.

“Poleni sana kwa kusubiri. Upasuaji umefanikiwa kwa asilimia mia moja, tumeweza kuondoa risasi mbili mwilini mwake zilizopigwa mgongoni lakini hazikuleta madhara makubwa kwake wala kwa mapacha aliowabeba tumboni. Kwa sasa atapelekwa katika chumba cha uangalizi maalumu huku tukiangalia hali yake kwa ukaribu zaidi,” yule daktari alisema.

Sammy na Elli wakatazama, ulikuwa mtazamo wa matumaini. Hata hivyo, suala la Joyce kuwa na mimba ya mapacha lilikuwa geni kwa Sammy. Alifumba macho yake na kushusha pumzi.

“Daktari tunakushukuru sana kwa kazi kubwa mliyoifanya, sijui tunaruhusiwa kumwona?” Sammy alisema huku akiwa bado ameyafumba macho yake. Machozi ya furaha yalionekana machoni pake.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO
 
Taxi - (102)

“Kwa sasa hamtaruhusiwa maana bado yupo kwenye coma na anaandaliwa kupelekwa chumba cha uangalizi maalumu. Ila kutakapokucha huenda mkaruhusiwa kutegemeana na hali ya mgonjwa itakavyokuwa,” Daktari Mshana alisema.

Sammy alitaka kusema neon lakini akasita baada ya kuona mlango mkubwa wa chumba cha upasuaji ukifunguliwa. Macho yao yakaelekezwa kule mlangoni ambako kitanda alicholazwa Joyce kilitolewa, kikasukumwa taratibu na wauguzi wa chumba cha upasuaji.

Juu ya kitanda kile alikuwa amelala Joyce akiwa hana fahamu. Dalili pekee ya uhai katika mwili wake yalikuwa macho yake yaliyokuwa wazi kidogo, yakiwa yamejaa kila dalili ya maumivu na mateso makubwa. Sammy na Elli wakasimama wakimtazama Joyce kwa huzuni.

Sammy alihisi kisu cha moto kikipenya tumboni mwake na kuanza kumkatakata maini, akili yake ilikuwa imepoteza uhai wake na mwili wake ulikuwa umekufa ganzi. Kisha kwa uwezo ambao hakujua ulikotokea alianza kupiga hatua kuwafuata wauguzi wale hadi katika chumba cha uangalizi maalumu ambako hakuruhusiwa kuingia kwa usiku ule.

Wakati akitembea kukifuata kile kitanda alikuwa akiita kwa sauti ya upole huku machozi yakimtoka. “Joyce! Mama Pendo!” lakini Joyce hakuonesha dalili zozote za kuitika wala kumsikia.

“Sammy, hakuna tunachoweza kukifanya kwa sasa, kwa kuwa tumefahamu kuwa hayupo tena kwenye hatari kama mwanzo, twende nyumbani ukapumzike, tutakuja tena kutakapokucha ili kujua maendeleo yake. Kama kutakuwa na mabadiliko yoyote simu zetu zipo wauguzi watatujulisha,” Elli alishauri.

“Nyumbani kufanya nini! Nitabaki hapa hapa hadi kunakucha nijue...” Sammy alisema lakini Elli akamkatisha.

“Huwezi kuendelea kukaa hapa, rudi nyumbani ukajue hali ya watoto. Wanahitaji pia faraja yako. Hujui wana hali gani kwa sasa, huenda wameathirika kisaikolojia kutokana na tukio hili na huenda wakatakiwa kupelekwa kwa mwanasaikolojia kwa ajili ya ushauri nasaha,” Elli alisema. Sammy akaonesha kumwelewa na kubetua kichwa chake kukubali.

“Ni kweli. Hata hivyo, bado najiuliza... nimejiuliza sana sababu ya Joyce kupigwa risasi lakini nimekosa majibu. Ni kwa sababu gani hasa haya yakatokea?” Sammy aliuliza.

“Nadhani tutapata majibu yote baada ya kuongea na Winifrida au pale Joyce atakapozinduka. Pia jeshi la polisi wakikamilisha uchunguzi wao wanaweza kuwa na jibu zuri zaidi hasa wakiwapata watu waliofanya shambulio hili,” Elli alisema kisha akamshika Sammy mkono na kuanza kuondoka eneo lile.

* * * * *

Saa sita usiku katika nyumba moja iliyopo eneo la Kinyerezi, Tunu alikuwa ameketi sebuleni akimwangalia kwa makini Tom ambaye alikuwa anaongea na mtu fulani kwenye simu. Tom kama alivyojulikana kwa wengi ingawa jina lake halisi aliitwa Faustine Thomas Ndejembi, ndiye yule dereva wa taxi aliyoikodi Tunu. Tom alikuwa amejitambulisha kwa Tunu wakati walipokuwa wakielekea katika nyumba ile aliyodai ni mahali salama zaidi kwao.

Ile ilikuwa nyumba yake aliyoijenga kwa siri na ilikuwa bado haijaanza kukaliwa na mtu, walikuwa amefika kwenye nyumba ile baada ya mizunguko ya hapa na pale ili kuwachanganya watu ambao wangeweza kuwa wanalifuatilia gari lao.

Nyumba ile ilikuwa kubwa na nzuri ya kifahari iliyozungukwa na miti mizuri ya vivuli na sehemu za wazi zenye bustani nzuri ya maua na nyasi za kijani kibichi zilizokatwa vizuri. Ilikuwa imezungukwa na ukuta mrefu uliofungwa mfumo maalumu ya umeme wa kuzuia wezi juu yake na kulikuwa na vibao vidogo vyenye maandishi mekundu ya tahadhari yaliyoandikwa: ‘Nyumba hii inalindwa na mitambo maalumu ya kuzuia wezi’ huku ikionesha kuwa inalindwa na kampuni ya ulinzi ya Darforce 1.

Urefu wa ukuta ulioizunguka nyumba ile haukumwezesha mtu yeyote aliyepita nje kuona mle ndani na ulikuwa umekorezwa kwa nakshi za hapa na pale zilizoifanya nyumba kuvutia zaidi. Kwa ujumla ilikuwa ni nyumba kubwa ya kisasa iliyokuwa na madirisha makubwa ya kisasa na baraza kubwa iliyokuwa mbele yake ikipangwa seti moja ya makochi ya sofa.

Muda ule Tunu alikuwa bado katika fikara nzito kumuhusu Tom aliyekuwa ameyaokoa maisha yake toka katika mtutu wa bastola ya Uledi, mwanamume aliyeonekana kuwa na kazi moja tu ya kutaka kuutoa uhai wake. Tunu alijikuta akimshukuru Mungu kwa kumleta Tom katika maisha yake.

Muda huo hakuwa na wasiwasi kwani alishapata majibu ya yale maswali aliyokuwa akijiuliza kabla kumuhusu Tom, kama: yule dereva ni nani? Kwa nini aliamua kumwokoa toka kwa wale watu ingawa ilisemekana kuwa na yeye alikuwa mtu wao? Alikuwa ametumwa na nani amwokoe?

Tunu alikiri kuwa hajawahi kumwona Tom miongoni mwa mashushushu wa Tanzania ingawa alihisi kuwa alikuwa amemkodi mtu mwenye ujuzi wa ziada katika shughuli za aina ile.

Tom alikuwa mzaliwa wa Dodoma na alikuwa na umri wa miaka thelathini. Alisoma Shule ya Sekondari Ilboru hadi kidato cha nne na baadaye kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora kisha akajiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa masomo ya Sayansi ya Jamii. Alipohitimu akapata udhamini wa kwenda nchni Ubelgiji kwa masomo ya saikolojia kabla hajajiunga na mafunzo ya awali ya ujasusi nchini Ufaransa na baadaye akaelekea nchini China ambako alihitimu vyema.

Tangu ajiunge na Idara ya Usalama wa Taifa, Tom alionekana kuwa na uwezo mkubwa sana na mbinu nyingi za kiupelelezi, akipenda kufanya kazi zake kama undercover (akijifanya dereva wa taxi na kazi nyingine za kujishusha ili kukamilisha majukumu yake). Kwa sababu ya tabia yake ya ucheshi, kujichanganya na watu, kutokubagua kazi na heshima kwa kila mtu ilikuwa rahisi sana kwa Tom kupata taarifa nyingi na haikuwa rahisi kushtukiwa.

Kazi ndiyo kwanza inaanza, nini kitaendelea? Tufuatane katika safari hii ndefu ndani ya Taxi...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom