Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Sehemu ya 33.



Wakachukua namba za gari na baada ya siku husika kufika, wakaanza kuelekea huko uwanjani. Kulikuwa na watu wengi waliokwenda kutazama mechi ya Hertha Berlin dhidi ya Fc Koln, kila mtu alitamani sana kuitazama mechi hiyo kwa sababu ya Amon tu.

Wao Jumanji Boys waliingia hapo kama wafanyakazi wa ukaguzi wa uwanja, walivalia mavazi yao lakini kwa ndani walikuwa na bastola. Ilikuwa ni vigumu kuwagundua kwamba walikuwa ni watu wabaya, walionekana kuwa kama wafanyakazi wa ukaguzi wa uwanja kwa jinsi walivyokuwa wamevalia sare zao.

Walikuwa wakitembeatembea huku wakiwaangalia mashabiki waliokuwa wakiendelea kuingia ndani ya uwanja huo, walikuwa makini kuangalia kila gari la mchezaji lililokuwa likiingia mahali hapo.

Baada ya dakika kadhaa, magari ya wachezaji yakaanza kuingia, haraka sana mmojawapo akaelekea kule mahali pa kupaki magari huku akisubiri kuona ni mahali gani gari la Amon lilikuwa likienda kuegeshwa. Baada ya kufahamu hilo, wakarudi na kujifanya kuendelea kufuatilia mechi kwenye moja ya runinga iliyokuwa nje ya uwanja huo.

Wakati huohuo wakiwa wameondoka, vijana wengine wawili waliokuwa na mavazi kama ya watu waliokuwa wakihakikisha ulinzi wa magari unakuwepo nao wakaingia kazini.

Waliambiwa mahali gari hilo lilipokuwa hivyo wakaanza kwenda huko. Kama ilivyokuwa kwa wale wengine, hata nao hawakugundulika kirahisi, wakafanikiwa kuelekea mpaka kule kulipokuwa na magari ya wachezaji na wafanyakazi na kulifuata gari la Amon, walipolifikia, wakaanza kufungua mlango kwa kupitisha waya juu ya kioo cha mlango na kuhakikisha wanatoa loki.

“Tap,” loki ilisikika ikijifungua.

Mlango ukafungua, walichokifanya ni kuingia ndani ya gari hilo kwenye siti na nyuma na kutulia kwa kujilaza. Wakaanza kumsubiri Amon atoke uwanjani na kuingia ndani ya gari lake.

Walisubiri mpaka mpira ulipomalizika huku Hertha Berlin wakiwa wameshinda kwa mabao matatu ambayo yote yalifungwa na Amon na kuendelea kuwapa pesa watu waliokuwa wakibeti akiwemo Konn.

Mashabiki wakaanza kutoka, wao walitulia tu, baada kama ya saa moja, nao wachezaji wakaanza kutoka na kufuata magari yao. Walijichimbia zaidi huku wakiwa kimya, baada ya dakika kadhaa, wakasikia mlango wa mbele ukifunguliwa, alikuwa Amon, akaingia ndani, kabla ya kuliondoa gari hilo akasali kisha kuliwasha.

“Don’t do anything stupid,” (Usifanye ujinga wowote ule) alisema kijana mmoja, Amon alishtuka, hakuamini kama ndani ya gari lake kulikuwa na watu viti vya nyuma.

“Whaaaaat?” (Nini?) aliuliza huku akitetemeka.

“Stay calm, you have to do what we want you to,” (Kaa kwa kutulia, utatakiwa kufanya kile tunachotaka ufanye) alisema mwanaume mwingine.

“Anything...” (Chochote kile..) alisema kwa hofu.

“Just drive...” (Endesha...) alisema jamaa mmoja, akawa hana jinsi, akalitoa gari mahali hapo huku akitetemeka kupita kawaida, akajua kabisa kwamba huo ulikuwa mwisho wa maisha yake hapa duniani.

Amon alikuwa akitetemeka tu huku akiendesha gari kuelekea mahali asipopafahamu, alikuwa akienda kwa maelezo ya wale watu waliomteka na kumwambia afanye kile alichotakiwa kukifanya.

Safari ilikuwa ikiendelea, alitamani kuuliza maswali mengi kuhusu utekaji huo lakini hakuona kama hilo lilikuwa jambo jema. Mara nyingi watekaji huwa hawatakiwi kuulizwa maswali mengi, walipokuwa wakikwambia fanya hivi basi ulitakiwa kufanya bila kuuliza swali lolote lile.

Aliendesha gari mpaka walipofika mahali ambapo hapakuwa na watu wengi, akaambiwa aelekee kule nyuma, akafanya hivyo lakini humohumo ndani ya gari na kijana mmoja kuelekea mbele na kushikilia usukani.

Gari liliendeshwa mpaka nje ya jumba moja kubwa na kuchukuliwa kisha kuingizwa humo. Hakujua palikuwa wapi, lilikuwa moja ya jumba zuri sana, lilipendeza na kuvutia lakini kwa upande wake muda huo, jumba hilo lilionekana kama kuzimu kwani alijua humo ndipo ambapo angekwenda kuuawa na wanaume waliokuwa wamemteka.

Akaingizwa ndani ya jumba hilo, kulikuwa na wanaume wengi, kwa jinsi walivyoonekana tu hawakuwa wa kawaida hata kidogo. Mikononi mwao walikuwa na misokoto ya bangi, bastola na vitu vingine vya hatari.

Hao walikuwa vijana wa Jumanji Boys, waliokuwa wakifanya utekaji sehemu mbalimbali nchini Ujerumani. Walimwangalia Amon, hawakuamini kama kijana huyo alikuwa mbele yao, alikuwa maarufu na mchezaji aliyekuwa akipendwa mno nchini humo.

Akaingizwa ndani na kupelekwa ndani ya chumba kimoja kilichokuwa humo, kwa kukiangalia tu, hakikuwa chumba cha kawaida hata kidogo, kilikuwa na muonekano wa kutisha, kulionekana michirizi ya damu ikiwa sakafuni, michirizi iliyoonyesha kulikuwa na watu waliowahi kufanyiwa unyama humo ndani.

“Nimefanya nini?” aliuliza Amon lakini hapakuwa na mtu aliyemjibu lolote lile.

Akaachwa ndani ya chumba kile na wanaume wale kutoka. Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu Konn na kumwambia kilichotokea, walifanikiwa kumteka Amon na muda huo alikuwa mikononi mwao.

Kwa kuwa alikuwa huko Munich, alichowaambia ni kwamba angekwenda huko Berlin kwa lengo la kumuona kwa macho yake, ajihakikishie kama kweli alitekwa ama la.

“Nakuja leo hiihii!’ alisema.

Kutoka Munich mpaka Berlin hapakuwa mbali, hasa kwa usafiri wa treni ya umeme, muda huohuo Konn akaanza safari ya kuelekea Berlin, na alipofika huko, akapelekwa mpaka kwenye chumba alichokuwemo Amon na kumwangalia, alikuwa yeye.

Uso wake ulikuwa na tabasamu pana, ni saa moja lililopita alipiga pesa kwenye mchezo wa kubeti kama kawaida yake. Aliwabetia Hertha Berlin ushindi, na huyo Amon alifanya maajabu, akampa pesa nyingi, hakuamini kuonana na shujaa huyo.

Amon alimwangalia Konn, kwa jinsi mwanaume huyo alivyoonekana, hapakuwa na hofu wala swali lolote lile kwamba alikuwa muuaji mkubwa. Alitisha na alionekana kuua kwake lilikuwa jambo la kawaida kabisa kama kwenda bafuni kuoga.

“Wewe ndiye Amon ninayekusikia sana?” aliuliza, japokuwa alikuwa shujaa kwake ila kwenye kazi alitakiwa kubadilika kidogo, lile tabasamu lililokuwa usoni mwake likapotea, sasa ukaja uso wa kazi.

“Ndiyo!” alijibu Amon huku akitetemeka.

“Umeaga kwenu?” alimuuliza.

“Kuaga?”

“Ndiyo! Kwamba unakufa leo! Uliiaga familia yako?” aliuliza Konn huku akimwangalia Amon.

Kusikia hivyo Amon akanyog’onyea, hakuamini kama kweli siku hiyo ilikuwa ni yake kufa. Alijutia uamuzi wake wa kwenda nchini Ujerumani kucheza mpira, hakujua kama alikuwa akikifuta kifo chake huko.

Mtu ambaye alimkumbuka zaidi alikuwa mpenzi wake, Jeniffer, kama kweli alikuwa akienda kuuawa ndani ya chumba hicho basi lingekuwa jambo jema kama angempigia simu na kumwambia kwamba wataonana mbinguni, yeye alikuwa akienda kufa kikatili.

“Sikuiaga, naomba nimpigie simu mpenzi wangu,” alimwambia Konn.

“Ili umuage?”

“Ndiyo!”

“Hamna! Yaani wewe tunakuua halafu tunakwenda kukutupa barabarani. Wala usijali, tutamwambia hata baada ya kifo chako,” alimwambia.

Hakutaka kuzungumza mambo mengi, huyo akaondoka zake kuzungumza na marafiki zake, usiu wa siku hiyo huyo Amon alitakiwa kuuawa, taarifa zisambazwe kila kona na wao kujipa ushujaa wa roho mbaya na kuwatisha Wajerumani wote.



Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 34.

Jeniffer alikuwa nyumbani, baada ya kutazama mechi ya Hertha Berlin na Fc Koln, akaamua kuandaa chakula ili Amon atakapofika nyumbani basi moja kwa moja ale. Hiyo ilikuwa ratiba yake ya kila siku kulipokuwa na mechi.
Aliandaa kila kitu na kurudi tena sebuleni na kuanza kusoma vitabu kama kawaida yake. Alisoma huku wakati mwingine akiangalia saa yake, dakika zilizidi kukatika lakini hakusikia hata dalili za gari kuingia nyumbani hapo wala simu yake kupigwa.
Haikuwa kawaida kabisa, alizoea kupokea simu kutoka kwa mpenzi wake na kumwambia alikuwa njiani akirudi nyumbani ama hata kama asingefanya hivyo basi ilikuwa ni lazima kusikia muungurumo wa gari na kujua kwamba mpenzi wake huyo hatimaye alirudi nyumbani.
Siku hiyo alikaa na kukaa lakini hakusikia kitu kama hicho. Hilo likaanza kumpa hofu na kuhisi inawezekana kulikuwa na kitu. Haraka sana akachukua simu yake na kumpigia Amon, simu haikuwa ikipatikana.
Hapakuwa na kitu kilichomchanganya kama hicho, hakujua kilichokuwa kikiendelea, alihisi kabisa kulikuwa na kitu, kitu gani hicho? Kwa nini mpenzi wake hakuwa akipatikana.
Sasa akatoka ndani na kuelekea nje, akasimama huku akiliangalia geti la nyumba hiyo. Moyo wake ulikuwa na hofu tele, alimsubiri mpenzi wake lakini hakutokea. Alipoona imechukua zaidi ya saa mbili, akaamua kuchukua simu yake na kumpigia Gideon, alihisi labda aliungana na mwanaume huyo kwenda sehemu, alitaka kujua.
“Amon hajarudi nyumbani! Upo naye?” alimuuliza.
“Hapana! Aliondoka uwanjani akiwa na gari lake!” alimjibu.
“Una uhakika?”
“Kabisa!”
“Nyumbani hajafika!”
“Unamaana gani?”
“Hajafika nyumbani!” alisema na kuanza kulia.
Alikuwa kwenye wakati mgumu mno, baada ya kupigiwa simu na Jeniffer, haraka sana Gideon akawapigia wachezaji wengine na kuwauliza kuhusu Amon, wote hao walimwambia hawakuwa wamewasiliana naye na hawakujua alikuwa wapi.
Ikambidi aondoke nyumbani kwake na kuelekea kwa Amon, ilikuwa ni lazima kwenda kuzungumza na Jeniffer, kwa kile kilichotokea ilionyesha kabisa msichana huyo amechanganyikiwa hivyo alitakiwa kwenda kama kumfariji na kumpoza.
Hakuchukua dakika nyingi akafika huko na kuanza kuzungumza naye. Kitu cha kwanza alichotaka kujua kama alifanya mawasiliano na polisi, akamwambia hakufanya, hivyo haraka sana wakawapigia na kuwaambia.
Polisi wakafika nyumbani hapo, kila mmoja alionekana kushangaa, haikuwa kawaida kwa mchezaji mkubwa kutokuonekana, wakafanya mawasiliano na wachezaji, viongozi wa timu kujua kilichotokea, nao hawakujua lolote lile.
Taarifa hiyo ikamfikia Anita, kwanza hakuamini alichokisikia, kwake lilionekana kuwa jambo lisilowezekana hata kidogo, iweje ghafla tu Amon hakuonekana, alikuwa wapi, naye akajaribu kumtafuta kwa njia alizozifahamu lakini hakuweza kumpata.
Kwa kuwa taarifa zilfika kwa polisi mpaka wachezaji, tayari zikawafikia waandishi wa habari na kujua kilichotokea, wao ndiyo wakaripoti na hatimaye Wajerumani kufahamu, zikasambaa zaidi na hatimaye dunia kujua kilichotokea.
Hapakuwa na mtu aliyeamini kama kweli Amon alipotea kwenye mazingira ya kutatanisha. Kwenye video zilizokuwa uwanjani zilionyesha gari lake likitoka, je, aliyekuwa akiendesha alikuwa yeye?
“Yeye ndiye alikuwa akiendesha,” alijibu jamaa aliyekuwa mbele ya kompyuta yake, aliyekuwa akihusika na kamera zilizokuwa nje na ndani ya uwanja.
“Kwa hiyo alikuwepo ndani ya gari?” aliuliza polisi.
“Ndiyo!”
“Sasa imekuwaje haonekani?”
“Labda gari limepata ajali sehemu!”
“”Hapana! Kama polisi tungepata taarifa hiyo!”
“Sasa atakuwa wapi?”
Hilo ndilo swali ambalo lilimchanganya kila mtu, hawakujua mahali alipokuwa huyo Amon, alitoweka ghafla, wengi walisema alitekwa, alitekwaje? Nani alikuwa na uwezo wa kufanya utekaji kwa mchezaji kama Amon?
Watu wakaanza kufanya harakati mitandaoni kwa hashtag ya #freeamon ambayo ilitakiwa kutumika kwa kila mtu aliyetaka kumuona Amon kwa mara nyingine tena. Polisi hawakuwa kimya, walihakikisha wanamtafuta kila kona lakini kwa bahati mbaya sana kwao hawakuweza kufanikiwa.
Siku ya kwanza ikapita, ikaingia ya pili lakini bado hali ilikuwa ya ukimya kabisa. Mashabiki wa soka duniani ni kama walifiwa, kila mmoja hakuonekana kuwa na furaha, huzuni ziliwatawala kwa kuona huo ndiyo ungekuwa mwisho wa Amon.
Hawakumfaidi, alikuwa kijana aliyechipukia kwenye soka, alikuwa akiupenda mchezo wa miguu, alianza kuishi kwenye ndoto zake lakini ghafla kabisa, akapotea na hapakuwa na mtu aliyejua mahali alipokuwa.
Wazazi wake wakachanganyikiwa, hawakutaka kukaa Tanzania tena, haraka sana wakaondoka na kwenda Ujerumani, huko wakaungana na Jeniffer, Gideon na kuomboleza pamoja.
Tayari kwa kilichotokea ikawa kama kashfa kwa nchi kama Ujerumani. Serikali ikaonekana kushindwa kuwalinda watu waliokuwa wakiishi humo, kubwa zaidi walishindwa kumlinda mtu kama Amon ambaye alionekana kuwa na thamani kubwa.
Kwa watu weusi wakaliingiza suala hilo na mambo ya kibaguzi, wakahisi labda kulikuwa na kundi fulani la watu waliokuwa wakiwabagua watu weusi na kuamua kumteka Amon kwa lengo la kutaka kumuua.
Yalikuwa mawazo mabaya sana, yakaleta chuki na hofu, watu wakajitokeza mitaani na kuanza kuandamana, kila mmoja alitaka kujua mahali Amon alipokuwa, polisi walisaidiana na vitengo vya kipelelezi, walifuatilia jambo hilo kwa karibu zaidi lakini wakashindwa kugundua hilo.
Wakati hayo yakiendelea, tayari Dawson alikwishafanya mawasiliano na Konn na kumuuliza kama alikamilisha kumteka Amon ama la.
“Tayari tangu nusu saa iliyopita! Tumuue ama utakuja mwenyewe kumuua?” aliuliza Konn kwenye simu.
“Wewe unaonaje?”
“Tunakusikiliza wewe tu!”
“Basi muueni halafu unitumie picha yake akiwa amakwishakufa!”
“Sawa. Na pesa zetu?”
Tutaonana mgahawani na kufanya malipo!”
“Hatuwezi kumuua kabla ya kumaliziwa chetu. Tumekamilisha kitu cha kwanza, lipa ili tukamilishe kitu cha pili, tusije kumuua halafu ukazingua kufanya malipo,” alisema Konn.
“Basi tuonane kwanza.”
“Haina shida. Hakikisha tunaonana huku ukiwa na pesa tayari,” alisema Konn.
“Haina shida.”
Baada ya saa moja wakaonana kwenye mgahawa mmoja uliokuwa hapo Berlin na kuonyesha picha ya amon akiwa ameuawa huku damu zikiwa zimetawala kila kona. Dawson aliziangalia zile picha, ni kweli alichokuwa akikiona ni maiti lakini hakutaka kujiridhisha kwa asilimia mia moja, ilikuwa ni lazima akaione hiyo maiti, ikiwezekana aichome hata kisu kwani kiasi cha pesa alichokuwa akikitoa kilikuwa kikubwa mno.
“Haina shida. Twende,” alisema Konn, yeye na vijana wake wakamchukua Dawson na kuanza kuondoka mahali hapo kwenda kwenye lile jumba walilokuwa wamelitumia kumuua Amon na kuuhifadhi mwili wake.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 35.

Ni siku ya tatu ilikuwa imeingia, dunia ilikuwa kimya, masikio yao yalikuwa nchini Ujerumani kusikilizia kile kilichokuwa kimetokea. Shirika la FIFA likatoa pole zao kwa familia ya Amon huku wakiwasisitiza polisi kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha huyo Amon anapatikana, kama si yeye basi hata mwili wake.
Polisi hawakulala, muda wote walikuwa bize kumtafuta Amon, walijitahidi kwenda kila kona, kutumia kamera mbalimbali jijini Berlin lakini hawakufanikiwa kupata lolote lile.
Mpelelezi wa polisi, Bwana Thomason Tuchel alipewa jukumu hilo la kumtafuta Amon na kujua mahali alipokuwa, ilikuwa ni lazima aifanye kazi hiyo kwa ufanisi zaidi na kujua mahali alipokuwa mtu huyo.
Kitu cha kwanza kama mpelelezi ilikuwa ni lazima kwenda kuonana na Jeniffer, ilikuwa ni lazima kuonana na msichana huyo kwa lengo la kuzungumza naye na kujua kilichokuwa kimetokea.
Jeniffer alikuwa mpole, majonzi tele, yaani mpaka kipindi hicho hakujua kilichokuwa kikiendelea kwa mpenzi wake. Akaanza kuzungumza na Tuchel, alichomwambia ni kuhusu kile kilichotokea. Mpenzi wake alikuwa na kawaida ya kuwasiliana naye kila alipotoka uwanjani lakini haikuwa hivyo kwa siku ile ya tukio.
“Unahisi atakuwa na adui mahali unayemfahamu?” alimuuliza.
“Hapana! Sikuwahi kusikia ama kuona kama alikuwa na adui,” alimjibu.
“Kabla ya tukio hilo, kulikuwa na mtu ambaye alionana naye unayeweza kumtilia mashaka?” alimuuliza.
“Hapana! Sikumuona mtu huyo!”
“Labda kulikuwa na mtu aliyekuwa na ugomvi naye wa kimapenzi?”
“Napo hakuna!”
“Labda wewe uliwahi kumdanganya kwa kutoka kimapenzi na mwanaume mwingine?”
“Hapana sijawahi kufanya hi...” alisema lakini hata kabla ya kumaliza sentensi yake, akanyamaza, ni kama kulikuwa na kitu alichokuwa amekifikiria.
“Dawson!” alijikuta akilisema jina hilo.
“Dawson! Ndiye nani?” aliuliza Tuchel huku akimwangalia Jeniffer.
Msichana huyo akaamua kumwambia kilichotokea, kwa kipindi hicho alitakiwa kuzungumza kila kitu ambacho aliamini kingeweza kusaidia upelelezi wa Tuchel ili kujua mahali mpenzi wake alipokuwa.
Msichana huyo alisimulia historia ndefu kidogo ya mahusiano yake na Dawson mpaka aliporudi na kutaka sana kuwa naye lakini alikataa kwa sababu tayari alikuwa na mtu mwingine, tena alikuwa na mimba yake.
“Kwa hiyo ulimwambia kuhusu Amon?” aliuliza Tuchel.
“Hapana! Sikumwambia. Kama ni yeye, atakuwa amejuaje kama ni Amon ndiye ninatoka naye kimapenzi? Au...” alisema lakini hata kabla ya kumaliza sentensi hiyo, kitu jingine likaja kichwani mwake.
“Glory!”
“Ndiye nani?”
Napo akaanza kumwambia kuhusu msichana huyo, namna alivyokuwa karibu naye, huyo ndiye aliyeonana na Dawson na kumwambia kuhusu yeye, mahali alipokuwa akiishi, kama aliweza kufanya hivyo, je, isingewezekana kumwambia kuhusu mpenzi wake?
Hilo likaingia kichwani mwa Tuchel, kwa kawaida ya mpelelezi yeyote yule hakutakiwa kupuuzia kitu chochote kile, hata kama lilikuwa suala la kijinga ilikuwa ni lazima kulifuatilia na kuona mwisho wake ungekuwa nini.
Haraka sana akawasiliana na Glory na kutaka kuonana naye nyumbani kwa Jeniffer, hilo halikuwa tatizo, ni ndani ya dakika kadhaa msichana huyo alikuwa mahali hapo kwa lengo la kuzungumza naye.
“Unamfahamu Dawson?” hilo lilikuwa swali la kwanza aliloulizwa na Tuchel.
“Ndiyo!”
“Unamfahamu kama nani?”
“Mtu aliyekuwa mpenzi wa Jeniffer.”
“Uliwahi kuonana na mwanaume huyo na kumwambia mambo mengi kuhusu Jeniffer, unaweza kuniambia ulimwambia kuhusu nini?” alimuuliza.
“Mahali anapoishi tu kwa kuwa alitaka kuonana naye!”
“Na baada ya hapo una uhakika wawili hawa walionana na kuzungumza?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Ulijuaje?”
“Jeniffer aliniambia!”
“Hakuna kingine ulichomwambia kuhusu Jeniffer?” alimuuliza.
“Zaidi ya hayo? Hakuna!”
“Dawson alijuaje kama Jeniffer alikuwa akitoka kimapenzi na Amon?” alimuuliza swali hilo makusudi kabisa, alitaka kujua kama msichana huyo alimwambia kuhusu hilo ama la.
“Nilimwambia!”
“Ila hukusema kama ulimwambia baada ya kuonana naye!”
“Haikuwa siku hiyo. Ilikuwa siku nyingine. Hapo kabla sikujua kama Jeniffer alikuwa kwenye uhusiano na Amon, baada ya kugundua tu, nikaamua kumwambia hayo yote Dawson,” alijibu.
“Kwa sababu gani?”
“Nilitaka aachane na Jeniffer, si vizuri kumfuatilia msichana ambaye ana uhusiano wa kimapenzi na mwanaume mwingine,” alijibu.
“Ulimwambia lini?”
“Jumapili!”
Tuchel akakaa kimya kwa sekunde chache akifikiria mambo fulani, baada ya Glory kumwambia hivyo Dawson, baada ya wiki moja, mwanaume huyo akatekwa na watu wasiojulikana, je, lisingekuwa jambo jepesi kuhisi kama huyo Dawson anaweza kuhusika kwenye hilo?
“Na baada ya kumwambia kuhusu Jeniffer kuwa na uhusiano na Amon, alikwambiaje?”
“Kwamba atafanya lolote lile ili kumpata!”
“Inawezekana alihisi baada ya kumuua Amon, ataweza kumpata tena Jeniffer,” alisema Tuchel, wanawake hao wakaangaliana, kile alichokizungumza inawezekana kabisa ikawa kweli.
Alichokisema Tuchel ilikuwa ni lazima kuwasiliana na Dawson kwa lengo la kumuuliza baadhi ya maswali kadhaa. Akachukua namba yake kutoka kwa Glory kwani Jeniffer hakuwa ameihifadhi kwenye simu yake, alipoondoka na kufika ofisini kwake, akaanza kumpigia simu mwanaume huyo lakini haikuwa ikipatikana.
Alichukia mno, aliona kabisa hiyo ndiyo ingekuwa nafasi yake ya kujua kilichotokea. Alikuwa na uhakika huyo Dawson kulikuwa na kitu alichokuwa akikijua kuhusu Amon, hivyo ilikuwa ni lazima kuwasiliana naye kwanza.
Alipoona hapatikani, akamwambia mkuu wake wa kazi kilichokuwa kimetokea, mkuu wake aliposikia hivyo, akamwambia Tuchel alitakiwa kufuatilia zaidi inawezekana kabisa huyo Dawson alikuwa amehusika.
Huku wakiwa na uhakika na hilo la Dawson, wakapokea simu kwamba kulikuwa na miti ilionekana imetupwa mtaani, ilikuwa ni maiti ya Mzungu ambaye mpaka muda huo hakuwa akifahamika alikuwa nani.
Tuchel akawa na hamu ya kutaka kwenda kuiona maiti hiyo, alipofika hospitalini, akaiona, ilikuwa ni sura ya mwanaume ambaye hakumjua, ila akaanza kuhisi inawezekana alikuwa Dawson, haraka sana akampigia simu Glory kwa lengo la kuongea naye.
“Hivi unamjua Dawson hata ukimuona sehemu?” alimuuliza.
“Ndiyo!”
“Kuna picha nakutumia, niambie kama ni yeye ama la!” alimwambia.
“Sawa.”
Baada ya kuipiga maiti ile ya Dawson na kumtumia picha msichana huyo, akamwambia ni kweli alikuwa Dawson, alimpata wapi na nini kilitokea mpaka mwanaume huyo kuuawa?
“Bado sijajua! Ila nahisi kile nilichohisi ndicho kilichotokea,” alisema Tuchel na kukata simu.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 36.

Kwa kumwangalia mara moja tu usingeweza kuwa na shaka kwamba Angelina alikuwa anaumwa, alipungua sana na kila alipokuwa akipita mbele ya watu waliokuwa wakimfahamu walimshangaa, alipungua na kuhuzunisha mno.
Chuoni hakuwa na furaha, alisema baada ya kufanikiwa na kwenda kujiunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam basi angeweza kutumia muda wake mwingi na mpenzi wake lakini mambo yakabadilika, sasa huko chuo kukawa kama jehanamu.
Hapakuwa na mtu aliyejua kama yeye na Edmund walikuwa na mahusiano ya kimapenzi, wengi walihisi inawezekana walikuwa marafiki tu kwa kuwa walikuwa wakifahamiana tangu shuleni, moyo wake ulichoma, kila alipokuwa akimuona Edmund, alisikia kabisa maumivu moyoni mwake.
Hakuamini kama ingetokea siku moja maumivu hayo yangetoka, kwake alijua kabisa yangeishi milele yote. Ilikuwa ni lazima afanye tiba ya moyo huo na kitu kikubwa ambacho alikifikiria ni kuondoka Tanzania na kuelekea Ujerumani kwa ajili ya kusoma moja ya chuo cha huko kutimiza ndoto zake.
Haraka sana akawasiliana na Gideon na kumwambia kuhusu mpango huo, kwa sababu tayari alikwishaambiwa na Amon, hakuwa na tatizo, akamkubalia msichana huyo na hivyo kuelekea Ujerumani.
Akiwa njiani, shauku yake kubwa ilikuwa ni kuonana na Amon tena na kumuomba msamaha, alijuta kwa kilichotokea hivyo alitamani sana kurudiana naye na kamwe kwenye maisha yake asingeweza kumuacha tena.
Hakujua kama Amon angekuwa tayari ama la lakini kwa jinsi alivyozungumza naye na kuonekana kuwa kawaida, aliamini angemsamehe na hatimaye kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa mara nyingine tena.
Baada ya siku kadhaa akawa nchini Ujerumani, alifika leo tu na kesho akasikia taarifa kuhusu kupotea kwa Amon. Moyo wake uliumia sana na hakujua hasa kilichotokea, alifika nchini humo kwa ajili ya kusoma, ila jingine lilikuwa ni kuonana na Amon na kumwambia kuhusu kurudiana naye, mbaya zaidi mwanaume huyo alipotea.
Wakati Gideon akiondoka kuelekea nyumbani kwa Amon alitaka kwenda naye ila Gideon akakataa, alifanya hivyo kwa sababu hakutaka kwanza ajue kuhusu Jenniffer, angeweza kuharibu kitu huko na kuonekana vibaya.
Akabaki nyumbani lakini akaanza kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Alimuomba Mungu Amon apatikane, alihisi kabisa mwanaume huyo alizaliwa na kuletwa duniani kwa ajili yake na alikuwa na uhakika angemsamehe zaidi kwa kukubali kuwa naye tena kwa mara nyingine.
Alitamani kumshirikisha kaka yake kuhusu kile kilichokuwa moyoni mwake lakini aliogopa kufanya hivyo, aliyakumbuka maneno aliyomwambia wakati akiwa amemuacha Amon, aliyakumbuka vilivyo kitu kilichomfanya kujisikia vibaya zaidi.
“Nimwambie? Hapana! Nitaanzaje? Nilimuacha Amon kwa maneno machafu sana,” alisema Angelina.
Maneno aliyotumia kumwacha Amon yalijirudia kichwani mwake na kumfanya kujisikia vibaya mno. Kuna wakati alijiona kuwa mjinga sana, hakujua ni kwa sababu gani alidanganyika na kuwa na Edmund na wakati kulikuwa na mwanaume aliyekuwa akimpenda sana.
Akajilaumu lakini kuna kipindi alitakiwa kukubaliana na kile kilichotokea, ndiyo alifaya makosa, alikuwa mjinga lakini wakati mwingine alijiona kusimamia alichokuwa akikiamini, ndicho kitu alichokisema Amon alipokuwa akizungumza naye, hivyo hakutakiwa kujutia.
Alikaa kwa siku kama mbili hivi, kila alipomwangalia kaka yake alionekana kabisa kuwa na majonzi tele, alimkumbuka rafiki yake, Amon, hakuwepo tena, alitekwa na watu wasiojulikana na hakujua mahali alipokuwa.
Baada ya siku hizo mbili, jioni moja ndipo Gideon akapigiwa simu na Jeniffer na kuambiwa Amon alipatikana akiwa mzima wa afya kabisa. Gideon akashtuka, hakuamini alichokisikia, haraka sana akamuuliza Jeniffer alipokuwa, akamjibu nyumbani.
Akamwambia Angelina, msichana huyo hakutaka kubaki, yaani kwa kipindi hicho ilikuwa ni lazima kwenda huko, kumuona Amon, alimkumbuka mno, na kile kilichotokea, hakika kilimfanya kutamani kumuona tena.
Ndani ya gari hamukuwa na mtu aliyeongea lolote lile, walikaa kimya mpaka baada ya dakika kadhaa, wakafika alipokuwa akiishi Amon na kuelekea ndani, walipofika humo, wakamkuta Amon akiwa na Jeniffer, Anita na mwanaume mwingine ambaye hawakuwa wakimfahamu, alikuwa Tuchel.
Haraka sana Gideon akamfuata na kumkumbatia rafiki yake huyo na kumuuliza kilichokuwa kimetokea. Hakutakiwa kuzungumza kitu kwanza, hapakuwa na watu wengi waliokuwa wakijua kama alipatikana, ni polisi wachache na huyo Tuchel, nini kilitokea? Alitekwa na nani?
Hapakuwa na mtu aliyejua hilo, na kwa jicho la Angelina alipokuwa akimwangalia Amon na Jeniffer, kwa jinsi walivyokuwa wakishikana tu, akagundua hakuwa na chake, ilikuwa ni lazima wawili hao wawe wapenzi.
Moyo wake ukauma sana.
***
Konn alibaki akimwangalia Amon aliyekuwa ndani ya chumba kile huku akiwa hajui ni kwa sababu alikuwa humo. Alimwangalia kijana huyo, kwake hakuonekana kuwa mtu wa kawaida hata kidogo. Alikuwa na uwezo mkubwa mno uwanjani.
Kulikuwa na watu waliotajirishwa na kijana huyo, kila walipokuwa wakiweka pesa zao kuitaka Hertha Berlin ishinde, basi yeye alifanya kila liwezekanalo kuhakikisha wanashinda.
Amon alipendwa na wacheza kamari wote, hakuwa akiwaangusha, wakati mwingine timu nzima ya Hertha Berlin uliiona ikikamatwa kabisa lakini bila kutarajia kijana huyo alikuwa akiibuka na kufanya maajabu makubwa.
Yeye mwenyewe Konn alikuwa mmoja wa watu waliokuwa wakinufaika na kijana huyo, leo eti alikuja mtu na kumpa ofa ya kumuua mwanaume huyo, hakutaka kufanya, badala yake akataka kumuua huyo kwani aliamini endapo angeondoka, angeweza kumpa dili hilo mtu mwingine na kumuua kitu ambacho hakutaka kabisa kuona kikitokea.
“Unajua kwa sababu gani upo hapa?” aliuliza Konn huku akimwangalia Amon.
“Hapana! Nilichukuliwa tu kutoka uwanjani!” alijibu.
“Ni kwa sababu kuna mtu anataka ufe.”
“Kwa sababu gani?”
“Sijui! Ila usiogope, huwezi kufa aisee. Leo umenifanya niingize kiasi cha euro laki moja na nusu,” alimwambia.
“Kivipi?”
“Kwa uliyoyafanya uwanjani! Wewe ni mtu muhimu sana. Pamoja ya kwamba sitoifanya kazi ya mwanaume huyo, ni lazima pia nikushikilie kwa siku kadhaa,” alimwambia.
Pamoja na kuambiwa hayo yote lakini hakutaka kumwamini mwanaume huyo hata kidogo, alikuwa muuaji tu, alikuwa na uwezo mkubwa wa kufanya jambo lolote lile mbele yake, aliyapenda maisha yake hivyo hakuacha kusali moyoni mwake.
Alishikiliwa humo na baada ya siku mbili simu ikapigwa kwa Dawson na kuambiwa tayari Amon aliuawa. Walichokifanya ni kumchukua na kumlaza chini, wakachukua damu ya ng’ombe, wakammwagia usoni na pembeni kidogo kuonyesha alipigwa risasi. Kwa jinsi alivyoonekana usingejua kama mtu huyo hakuuawa.
Baada ya hapo simu ikapigwa mpaka kwa Dawson na kuambiwa kila kitu kilifanikiwa na ni yeye tu ndiye aliyekuwa akihitajika huko, kwenda kuuona mwili wa Amon lakini pia kumalizia kiasi cha pesa alichoahidi.
Haraka sana Dawson akatoka na kwenda huko, alipofika, akachukuliwa na kupelekwa ndani ya chumba kile na kuonyeshwa Amon aliyekuwa amekaa tu kwenye kiti akimwangalia.
Hakujua mwanaume huyo alikuwa nani, hakujua ni kwa sababu gani alitaka kummaliza, alimwangalia na kuishiwa maneno ya kusema. Dawson alishtuka, alibaki akimshangaa Amon.
Kwenye simu aliambiwa kijana huyo aliuawa, na picha akatumiwa lakini cha kushangza kabisa, alimkuta akiwa mzima wa afya, hakujua sababu ya kudanganywa na wakati tayari alifanya malipo.
“Mbona ham...” aliuliza lakini hata kabla ya kumalizia sentensi yake, mwanaume aliyekuwa nyuma yake akamtuliza kwa kumuwekea bastola mgongoni.
“Tulia!” alisema mwanaume huyo, baada ya sekunde chache, mlango ukafunguliwa na Konn kuingia.
Sura yake ilikuwa na tabasamu pana, alimwangalia Dawson, alimuona kama mtu fulani mjinga ambaye alimtaka kufanya kitu ambacho hakuwa radhi kabisa kukifanya.
Kumuua Amon ni kitu kisichowezekana, kummaliza kijana huyo kwa yeye mcheza kamari ya mpira ambaye alikuwa akipunwa mara kwa mara ilimaanisha angeendelea kupunwa endapo tu huyo Amon asingekuwa kwenye dunia hii.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 37.

Tangu Amon aanze kucheza soka, alikuwa akifanikiwa, alipanda madau makubwa mno na alimshukuru kwa kuwa ‘alikula’ kila mkeka aliokuwa akikata. Aliambiwa na Dawson kulipwa kiasi cha euro laki saba lakini mpaka muda huo huyo Amon alimpatia zaidi ya euro milioni mbili kwa kubeti tu, sasa itakuwaje mtu huyo akauawa?
“Nisingeweza kumuua mtu kama Amon,” alimwambia huku akimwangalia.
“Lakini yalikuwa makubaliano yetu!” alisema Dawson.
“Kwani tuliandikiana sehemu?”
“Lakini si mnafanya kazi ambayo mteja wenu anataka muifanye?”
“Ndiyo ya kumuua Amon?”
“Ila nilitaka iwe hivyo kama mteja!”
“Sasa wewe ungekuwa mimi ungemuua?”
“Kwa nini nisimuue kama tayari nishakubaliana na mteja na pesa amenilipa?”
“Ila siyo kwangu. Huyu mtu amenipa pesa nyingi zaidi ya ulizonipa, na ataendelea kunipa pesa nyingi zaidi ya hizo ulizonipa,” alimwambia, maneno hayo yakamfanya Dawson kushangaa, akaona kabisa aligeukiwa.
“Kwa hiyo?” aliuliza, manake aliona mambo kuwa mengi.
“Hakuna mtu anayekufa humu chumbani!”
“Sawa,” alisema na kutaka kuondoka. Kijana aliyeshika bastola akamzuia.
“Kuna nini?”
“Huwezi kuondoka kiholela hivyo, najua utaweza kummaliza Amon ukiondoka hapa,” alisema Konn.
“Hilo ndilo nitakalolifanya nyie hamkunifanyia kazi, mmenigeuka!”
“Kwa sababu sitotaka Amon auawe, ni lazima nikuue wewe!”
“Mimi?”
“Sam! Mchukue mkamfanyie kama mlivyomfanyia yule mvuvi,” alisema na kijana huyo, wenzake wakamchukua na kuondoka naye.
Dawson alibaki akilia, alihitaji msamaha lakini hapakuwa na mtu aliyemsamehe kwa lolote lile. Ili Amon awe salama ilikuwa ni lazima mwanaume huyo auawe mara moja. Alishangaa sana ndani ya chumba hicho, akagundua kwa yale aliyokuwa akiyafanya uwanjani yaliwanufaisha watu wengi mno.
Kipaji chake cha mpira kilimpa maisha mazuri, kubwa zaidi kikamuokoa mbele ya mdomo wa kifo. Alimshukuru Mungu sana, alichoambiwa na Konn ni kuchukuliwa na kwenda kutupwa sehemu akiwa amefungwa kamba na baada ya hapo, simu ingepigwa polisi na kufuatwa.
Hilo ndilo lililotokea, akachukuliwa na kwenda kutupwa sehemu, huko akaambiwa hakutakiwa kusema kile kilichotokea kwani endapo angediriki basi ingekuwa shida kwake, akakubaliana nao.
Baada ya kutupwa hapo pembezoni mwa barabara, watu waliokuwa wakipita ndiyo walimuona, hawakujua kama alikuwa Amon kwa kuwa kulikuwa na giza, wakapiga simu polisi na kufika hapo na kumchukua.
Walipoondoka naye ndipo wakagundua alikuwa Amon, haraka sana wakampigia simu Tuchel na kuzungumza naye, walimwambia kuhusu jambo hilo, mwanaume huyo akataka kupelekewa mtu huyo kituoni, hilo likafanyika ila akiwa amewekewa kitambaa kuficha sura yake nzima ili asigundulike.
Baada ya kufikishwa kituoni, akahojiwa, alichokisema ni kwamba alitekwa na watu ambao hakuwafahamu, alizungumza mengi lakini bado Tuchel aliamini kulikuwa na mambo mengi kijana huyo alificha, inawezekana kwa usalama wake.
Alichokifanya ni kumpigia simu Anita na kumwambia kilichotokea, baada ya mahojiano, akamchukua na kuelekea nyumbani kwake. Macho ya Jeniffer yalipotua kwa mpenzi wake hakuamini, alishtuka, alihisi kama alikuwa akiota.
Akasimama na kumsogelea, akampapasa usoni na kumkumbatia, wote wakaanza kulia. Ilikuwa ni furaha tena kuonana baada ya siku tatu kupita. Baada ya dakika kadhaa, Anita akafika nyumbani hapo na kumuona Amon, kitu cha kwanza akamshukuru Mungu.
“Ahsante Mungu,” alisema huku akinyanyua mikono yake juu.
Wakakumbatiana na kuanza kuzungumza mambo mengi yaliyotokea baada ya kutekwa. Amon hakutaka kuzungumza yote na kitu alichowaambia ni kwamba hakuwajua watu hao walikuwa akina nani kwani walivalia vinyago.
“Kwa nini walikuteka?”
“Wanasema mambo ya kamari! Walizungumza hayo tu, mengine hawakutaka kuniambia,” aliwaambia.
“Na kwa nini hawakukuua?” aliuliza Anita.
“Ulitaka waniue?” naye akauliza.
“Sina maana hiyo!”
Hakutoa ushirikiano wa kutosha, hata Gideon alipofika nyumbani hapo akiwa na Angelina, msimamo wake ulikuwa uleule, hakutaka kuwaambia lolote lile.
Taarifa za kupatikana kwake zikaanza kusambazwa kila kona, wote waliosikia kupatikana kwake wakamshukuru Mungu kwa kuwa lilikuwa jambo gumu kwa mtu kutekwa na kupatikana akiwa hajajeruhiwa popote pale.
Maandamano yaliyokuwa yakiendelea, yakasitishwa na kwa sababu polisi nao walitaka kuonekana walifanya kazi kwenye hilo, Tuchel ndiye aliyezungumza na waandishi wa habari na kuwaelezea kila kitu kwamba walimtafuta na hatimaye kumpata.
“Ni nani alihusika kwenye utekaji huo?” aliuliza mwandishi mmoja.
“Mpaka sasa hatujafahamu na hata Amon mwenyewe anasema muda wote walivalia vitambaa kuziba nyuso zao,” alijibu.
“Na kwa nini hawakumuua wala kujeruhi?”
“Wewe ulitaka wamuue na kumjeruhi?” naye aliuliza.
“Sijamaanisha hivyo!”
“Basi cha msingi amerudi akiwa salama, basi tumshukuru Mungu,” alisema na kumaliza kuonoka zake, akafunga mahojiano hayo.
Kwa kuwa Angelina alimkuta Amon akiwa na maisha yake na mwanamke mwingine, hakuwa na chake, akatakiwa kukubaliana na alichokiona, alibaki akiumia tu kila alipokuwa akimuona Amon akiwa na mpenzi wake.
Kwa kuwa alikwenda huko kwa lengo la kusoma, baada ya mwezi mmoja akaanza kusomea masuala ya Utabibu wa Misuli katika Chuo Kikuu cha Berlin hapohapo Ujerumani.
Kwa Amon aliendelea na maisha yake ya soka kwa mafanikio makubwa. Baada ya kucheza Hertha Berlin kwa mafanikio, hatimaye miaka mitano baadaye akanunuliwa na FC Barcelona ya Hispania kwa dau kubwa la Euro milioni mia 350 na kuwa mwanasoka aliyenunuliwa kwa pesa nyingi duniani.
Baada ya kuipa Hertha Berlin kombe la Klabu Bingwa mara tatu, akaipa FC Barcelona kombe hilo mara tano huku akichukua tuzo ya uchezaji bora mara saba na kumfanya kushikilia rekodi ya kuchukua tuzo hiyo mara nyingi kuliko mchezaji yeyote yule.
Alipofikisha umri wa miaka arobaini akaamua kustaafu na kumuachia mikoba mtoto wake aliyezaa na Jeniffer aitwaye Roben ambaye naye alianza kuichezea timu ya watoto wa Hertha Berlin.
Aliamua kumpa jina hilo mtoto wake kama kumkumbuka kocha wa Lyon, Roben ambaye aliwaita yeye na Gideon na kuwaambia walitakiwa kujiamini sana, maneno hayo yaliwabadilisha na kuanza kufanya makubwa.
Mpaka anastaafu kucheza mpira Amon alifanikiwa kupata watoto watatu, wa kwanza akiwa Roben, wa pili msichana aliyempa jina la mama yake, Zuri na wa tatu alikuwa wa kiume aliyempa jina la Gideon, mmoja wa marafiki zake wakubwa wa tangu huko ujanani mwao.
Kwa msichana Angelina, alifanikiwa kuwa daktari wa misuli katika Hospitali kubwa ya hapo Berlin, aliamua kuishi huko, akaolewa na mwanasheria mkubwa nchini Ujerumani. Kila kitu kilichotokea baina yake na Amon kilibaki kuwa historia na kubwa zaidi mpaka kipindi hicho hapakuwa na mtu yeyote aliyewahi kujua nchini humo kama wawili hao waliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi.
Kwa kila kitu alichokifanya kilibaki kuwa katika historia ya mashabiki wengi wa mpira duniani. Sasa swali kubwa ambalo liliwasumbua ni kumtambua mchezaji aliyewahi kuwa hatari kuliko wote duniani.
Wengine walisema Messi, wengine Pele, wengine Ronaldo lakini idadi kubwa ya watu walisema Amon, mwanaume wa ajabu aliyekuwa akicheza mpira kama hakuwa binadamu aliyezaliwa kwenye sayari hii.
Kila alipokuwa akifanya mahojiano na waandishi wa habari juu ya mafanikio yake aliwaambia kitu kimoja tu, kwamba tangu akiwa mtoto aliamini alikuwa na ndoto kubwa sana kuwa kwenye ulimwengu wa kitajiri, pamoja na kuzaliwa kwenye umasikini lakini kila siku aliamini itatokea kipindi atakachokuja kuishi kwenye ulimwengu mkubwa wa kitajiri, ndoto ambayo alikuwa nayo tangu zamani.



MWISHO



Ahsante sana kwa kuifuatilia mwanzo mpaka mwisho.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom