Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Sehemu ya 09


Amon alibaki akiwa amesimama tu, hakuamini kile kilichotokea, aliiangalia pikipiki iliyombeba mpenzi wake ikiondoka machoni mwake. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, ilimshangaza kwa kuwa ilikuwa ghafla sana, yaani Angelina alibadilika na kutotaka kuwa naye.
Akaanza kukumbuka kama kuna kitu kibaya kilichotokea, mara nyingi hali kama hiyo inapotokea ghafla tu ni lazima kuwe na kitu fulani kilichotokea na kusababisha matatizo yote, alijaribu kufikiria ili kama kungekuwa na tatizo lolote amuombe msamaha lakini hakuona kama aliwahi kumkosea binti huyo mrembo.
Alikuwa mwanaume, aliyekuwa akijiambia kila siku alikuwa na nguvu, ujasiri mkubwa lakini kwa kile kilichotokea alishindwa kabisa kuyazuia machozi yake kuanza kutiririka mashavuni mwake, aliumia, alijiona kama mtu aliyekuwa amechomwa na sindano moyoni mwake, sindano iliyochochewa na moto mwingi.
Palepale alipokuwa amesimama, akahisi miguu ikikosa nguvu, akatafuta sehemu na kukaa, kila mtu aliyekuwa akipita karibu naye alimshangaa, alikalia jiwe, sehemu ambayo haikuwa safi lakini kwa kile kilichotokea muda huo, mahali pale palionekana kusafi kama kwenye hekalu la mfalme.
“Nini kimetokea?” alijiuliza.
Kila swali ambalo alijiuliza alikosa jibu kabisa, alibaki akiwa ameduwaa tu na asijue ni kitu gani alitakiwa kufanya mahali hapo. Huku akiwa kwenye hali hiyo akakumbuka kumtafuta mtu mmoja ambaye alikuwa muhimu sana, inawezekana huyo ndiye angemwambia kilichotokea, kama kulikuwa na kosa amwambie, mtu huyo alikuwa Gideon.
Haraka sana akampigia simu na kuomba kuonana naye, kwa jinsi alivyokuwa akiongea, upande wa pili Gideon alihisi kulikuwa na tatizo sehemu, sauti ile aliyokuwa akiisikia kutoka kwa Amon haikuwa ya kawaida kabisa hivyo kupanga kuonana na baada ya nusu saa, wote walikuwa kwenye mgahawa mmoja na kuanza kuongea.
Amon hakutaka kumficha, alimwambia kila kitu kilichotokea, jinsi alivyoumia kwa kile alichofanyiwa na Angelina. Gideon alimsikiliza kwa makini, kwake, hasa masikioni mwake hakuamini kile alichosimuliwa na rafiki yake huyo.
Yeye ndiye alikuwa mstari wa kwanza kumwambia hakutakiwa kumuumiza mdogo wake kwa kuwa alikuwa akimpenda mno, kijana huyo alikubaliana naye lakini cha kushangaza, kilichotokea huyo mdogo wake ndiye aliyekuwa wa kwanza kumuumiza Amon.
Kwa jinsi alivyoongea tu alionekana kuumizwa na kitu hicho, Gideon akaanza kumpoza na kumwambia angekwenda kuzungumza naye, ikiwezekana awakutanishe na kuwaunganisha tena kitu ambacho kwa Amon alikubaliana nacho moja kwa moja.
Baada ya kuzungumza kwa dakika kadhaa, Gideon akaondoka na kurudi nyumbani. Moyo wake ulikuwa kwenye hasira kali, hakuamini kama ndugu yake huyo angefanya uamuzi wa kijinga kama ule alioufanya.
Kwa Amon, kwa jinsi alivyokuwa akielekea kwenye mafanikio hakutakiwa kuachwa, kwa mwanamke yeyote yule alitamani kuwa na mwanaume aliyekuwa na ndoto kubwa kama rafiki yake huyo, kitu cha ajabu kabisa, macho ya Angelina yalipigwa na upovu na kutokuyaona hayo.
Alipofika nyumbani, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumuona Angelina chumbani kwake kwa lengo la kuzungumza naye. Muda huo msichana huyo alikuwa chumbani kwake, alijifunika shuka na kuanza kulia kama mtoto mdogo, hakuamini kama yeye ndiye aliyeamua kufanya jambo kama hilo.
Alijua ni kwa namna gani Amon alikuwa akimpenda, alivyomuheshimu na kumfanya kuwa msichana wa kipekee sana, lakini kitu cha ajabu kabisa, akaamua kumuacha kwa kuwa tu alimpata mwanaume mwingine aliyekuwa ameonyesha mapenzi makubwa kwa muda mfupi.
Gideon akamuita Angelina na kuanza kuzungumza naye, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumlaumu kwa kile alichokifanya, kulikuwa na mambo mengi ya kijinga aliyokuwa ameyafanya katika maisha yake lakini lile lililotokea, hakika lilikuwa la kijinga kuliko kitu chochote kile.
“Kwa nini umefanya hivi?” alimuuliza huku akimwangalia.
“Naomba anisamehe tu!” alisema Angelina huku machozi yakimtiririka.
“Hilo si jibu nilitakalo! Kwa nini?”
“Nimeshindwa kuwa naye!”
“Kwa nini?”
“Moyo wangu haupo tena kwake!”
“Upo kwa nani?”
“Kwa mwingine!”
Gideon akabaki kimya kwa sekunde kadhaa, kichwa chake kilijaribu kumfikiria ndugu yake huyo ni kundi gani alitakiwa kuwekwa. Kulikuwa na makundi kadhaa, ya watu wasiojielewa na wale wapumbavu, kwake, alimchukua na kumuweka kwenye kundi la wapumbavu.
Kila mwanamke kwenye dunia hii alikuwa akitamani kuwa na mwanaume mwenye mafanikio, na kama hakuwa na mafanikio basi yule aliyekuwa akionyesha dalili za kufanikiwa siku za usoni.
Kila mwanamke huwa na ndoto zake, mwanaume anayekuwa naye kimapenzi huwa anajua kabisa huyu acha nimvumilie kuna siku atafanikiwa ama huyu napoteza muda tu.
Kwa mtu kama Angelina alitakiwa kufahamu mapema kuwa mwanaume aliyekuwa naye kwenye uhusiano wa kimapenzi alikuwa na ndoto kubwa kiasi gani. Kwa kitendo cha kutokugundua hilo ilionyesha ni kwa namna gani alikuwa msichana mpumbavu kuliko wote.
“Yaani umemuacha Amon, nitauficha wapi uso wangu mimi!” alisema Gideon.
Moyo wake uliumia kuliko hata alivyoumia Amon mwenyewe. Alimfanyia wema, kwa kitendo cha kuwa na ndugu yake kilikuwa kama malipo kwa kile alichomfanyia lakini jambo la ajabu kabisa ndugu yake huyo akaamua kumuachia maumivu makali ya moyo.
Wakati yeye akihuzunikia hilo, kwa Amon ilikuwa ni shida mno. Moyo wake ulikuwa kwenye mateso makali mno, alijaribu kumsahau Angelina, alishindwa, alitamani kufanya jambo lolote lile kuirudisha furaha yake lakini alishindwa kabisa.
Wakati mwingine alikuwa akijuta kujiingiza kwenye masuala ya kimapenzi kwani hapo ndipo alipopata picha ni kwa sababu kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakijimaliza ama kuchukua uamuzi wa ajabu kabisa. Mzigo wa huzuni ulikuwa mkubwa mno moyoni mwake kiasi cha kushindwa kuvumilia, akazidi kutokwa na machozi.
Baba yake alihisi kulikuwa na jambo lililotokea, tangu Amon atoke na kumsindikiza Angelina alibadilika, hakuwa kama alivyokuwa dakika chache zilizopita, alihisi kulikuwa na kitu kilichotokea na alitaka kujua kulikuwa na nini. Akaingia chumbani kwa kijana wake na kumfuata.
Alimwangalia, macho yake yalikuwa mekundu kuonyesha alikuwa amelia sana, akakaa kitandani na kumwangalia huku akiwa na dukuduku la kuzungumza naye juu ya kile kilichokuwa kimetokea. Akamshika mkono.
“Kuna nini?” alimuuliza huku akimwangalia.
“Hakuna kitu!” alimjibu.
“Basi acha nibadilishe swali. Yule msichana amekufanya nini?” alimuuliza.
Amon akanyamaza, hakutegemea kama baba yake angejua kama mtu aliyesababisha hali ile alikuwa Angelina, akatamani kumwambia lakini akashindwa kufanya hivyo, alijisikia aibu mno kuzungumza na baba yake kuhusu masuala ya mahusiano.
“Hakuna kitu baba!”
“Nisikilize Amon. Ni jambo zuri sana kuzungumza kuhusu mahusiano na mimi baba yako, mimi ndiye mshauri wako kwa kuwa nimepitia huko. Sasa kama hutaki kuongea na mimi kuhusu mahusiano, unataka kuongea na mama yako? Ama dada yako? Ama shangazi yako?” alimuuliza maswali yaliyomfanya Amon kwanza kutulia.
“Hebu niambie kuna nini!” alimwambia.
“Angelina ameniacha!”
“Kisa?”
“Sijui! Ameamua kuniacha!”
“Nisikilize, hakuna uamuzi unaopangwa bila sababu. Kama amekuacha, jua kuna sababu ya yeye kufanya hivyo,” alimwambia.
“Ila hakuniambia!”
“Hahaha! Amon acha nikwambie kitu kimoja rafiki yangu,” alisema baba yake, Amon akakaa vizuri.
“Kitu cha kwanza kwenye maisha yako hutakiwi kumwamini mtu kupitiliza. Unajua unapomwamini sana mtu, siku akitokea kuvunja uaminifu ni lazima uumie sana,” alimwambia na kuendelea:
“Kwenye maisha yangu sikuwahi kumwamini mama yako kwa asilimia mia moja, analijua hilo. Unapokuwa humuamini mtu kwa asilimia zote inamaanisha hata siku akija kukuumiza, hutoumia kwa kuwa moyo wako ulikosa imani naye. Kwenye hili kumbuka kitu kimoja, kila mtu unayemuona kwenye dunia hii ni binadamu, asili ya binadamu ni dhambi,” alimwambia na kuendelea:
“Binadamu hawezi kuwa sahihi muda wote, kuna kipindi atakosea kama binadamu, kuna kipindi atakuumiza, kuna kipindi utamchukia, ndivyo tulivyo. Unapoingia kwenye mahusiano ya kimapenzi, jua kuna siku huyo mtu atakuacha, atauvunja uaminifu wako, nini kitatokea hayo yakitokea?” alimwambia.
“Nitaachana naye!”
“Huo ndiyo uamuzi wa kiume. Wakati mwingine unapofanyiwa jambo lenye kuumiza moyo, achana nalo, fanya mambo mengine. Wakati mwingine hutakiwi kulia ama kuhuzunika sana. Mungu anaujua mwisho wetu, anapoona fulani hakuwa mtu sahihi kwako, anakuachanisha naye kwa kuwa anataka kukuandalia mwisho mwema,” alimwambia na kuendelea:
“Watu wengi wamelazimisha mapenzi sehemu ambayo Mungu alijaribu kuwatenganisha, mwisho wa siku wakawa na maisha mabaya sana. Hakuna linalotokea bila sababu, Mungu ana sababu zake, hivyo kama hilo limetokea, mshukuru Mungu kwani hujui amekuepusha na kitu gani hapo baadaye, inawezekana ungeendelea kuwa na Angelina utakuwa na mwisho mbaya, Mungu ameliona hilo na ameamua kukuepusha nalo mapema,” alimwambia.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumanne na Ijumaa.

Simulizi hii hata nusu haijafika, atakayeitaka yote kuinunua aisome kwa muda wake, anicheki WhatsApp kwa namba 0718069269.

Tukumbuke tu hii itaandikwa mwanzo mpaka mwisho, ila itakuwa inakwenda taratibu sana.
 
Sehemu ya 10.

Maneno yote aliyokuwa akizungumza mbele yake yaliuchoma moyo wake Amon na kuingia ndani kabisa. Yalikuwa maneno ya kweli kabisa, wakati mwingine Mungu alijaribu kufanya jambo fulani kwa sababu aliangalia mwisho wako ungekuwaje baada ya hapo.
Mungu hakuwahi kukosea, kila kitu anachokifanya anakifanya kwa maana yake hivyo amon akaambiwa alitakiwa kukubaliana na kila kitu kilichotokea, asingeweza kuwa na Angelina tena maishani mwake.
“Ila ninampenda sana,” alimwambia baba yake.
“Hata kama! Wakati mwingine inaweza kukugharimu kwa kutaka kupingana na mpango wa Mungu. Unachotakiwa kufanya ni kuendelea na maisha yako kana kwamba hakuna kitu kilichotokea,” alimwambia.
“Nitaweza kweli kumsahau?” alimuuliza.
“Kitu kimojawapo Mungu alichokiweka katika roho ya binadamu ni kusahau, kusingekuwa na usahaulifu inawezekana mpaka leo hii ningekuwa namlilia mama yangu. Utasahau tu,” alimwambia.
Kwa kipindi kama hicho Amon hakuamini kama angeweza kumsahau Angelina, msichana huyo alimzoea, alimfikiria kila wakati na alitamani sana kuwa naye muda wote. Moyoni mwake ni kama alipigwa chapa, alihisi kabisa lingekuwa jambo gumu kumsahau maisha yake yote.
Siku iliyofuata Amon hakutaka kukubali, moyo wake haukukubaliana na kile kilichotokea, asubuhi alikwenda mazoezini, mazoezi ya jioni akaachana nayo na kwenda shuleni kwa akina Angelina, alitaka kumuona kwa mara nyingine kwani bado hakukubaliana na matokeo kwamba aliachwa.
Alipofika, kulikuwa na mti uliokuwa nje ya eneo la shule, akatulia hapo huku akiwa kimya kabisa. Baada ya dakika kadhaa kengele ikagongwa kumaanisha ulilikuwa ni muda wa kurudi nyumbani kwa wanafunzi waliokuwa wameingia vipindi vya mchana.
Hakutaka kusimama, alichoamini Angelina angetokea na kumfuata, alitamani sana kuongea naye kwani alijua asingeweza kuendelea kuishi bila msichana huyo mrembo.
Alikaa kwa dakika kadhaa hatimaye wanafunzi wakaanza kutoka, sasa hapo akayainua macho yake na kumwangalia kila aliyekuwa akitoka ndani ya eneo la shule. Alisubiri na kusubiri, huku akiwa amekata tamaa na kuhisi Angelina hakwenda shule, akaiona gari ndogo ikitoka shuleni.
Kwanza akaipuuzia, akataka kuingia ndani ya eneo la shule, wakati akipiga hatua huku akipishana na wanafunzi, ghafla macho yake yakaangalia ndani ya gari lile, alichokiona hakuamini macho yake.
Alimuona Angelina akiwa na mwanafunzi mwingine ndani ya gari la milango mitatu. Hapakuwa na viti zaidi ya hivyo vya mbele tu. Yule aliyekuwa akimuona alikuwa msichana aliyewahi kuwa mpenzi wake lakini akataka kuudanganya moyo wake hakuwa Angelina.
Aliwaangalia vizuri, walivyoonekana tu hapakuwa na shaka walikuwa wapenzi waliokuwa wakipendana kupita kawaida. Amon hakutaka kukubali kuona akichukuliwa msichana wake, hapohapo akaanza kulisogelea gari na kulisimamisha.
Angelina alipomuona Amon, moyo wake ukapiga paa! Hakuamini kama kijana huyo angefika mpaka shuleni kwao, alizungumza naye, alimwambia aachane na maisha yake, asahau kuhusu yeye lakini kitu cha ajabu kabisa alikuja mpaka shuleni. Edmund akasimamisha gari na kumwangalia Amon aliyekwenda upande wa Angelina.
“Angelina! Tatizo nini mama?” alimuuliza msichana huyo huku akiwa nje ya gari hilo karibu na kioo cha dirisha.
“Edmund! Ondoa gari,” alimwambia mpenzi wake.
“Huyo ni nani?” aliuliza Edmund.
“Ondoa gari pleaseee...”
“Subiri kwanza mpenzi! Oya wee jamaa unataka nini?” alimuuliza Amon huku akimwangalia.
“Namtaka Angelina wangu! Angelina mama tatizo nini? Kwa nini unanifanyia hivi? Niambie mpenzi nimekukosea nini? Mbona unataka kunitesa kiasi hiki?” alimuuliza, Angelina akajifanya kama kuona akisumbuliwa na kelele zile, akachukua earphone, akaziweka sikioni na kufungulia muziki wa simu yake kwa sauti kubwa.
“Angelina...Angelinaaaa...” alimuita lakini mwenzake hakumsikia kabisa.
“Angelina, nini kinaendelea?” aliuliza Edmund huku akimgusa pajani.
“Unaliondoa gari ama niteremke nikachukue daladala?’ aliuliza Angelina huku akionekana kubadilika.
Edmund hakuwa na jinsi, alitaka kumridhisha mpenzi wake hivyo akaliondoa gari mahali hapo na kuondoka zake. Huku nyuma Amon alikuwa akiliangalia gari lile lilivyokuwa likiondoka, hakutaka kusimama tu kama mlingoti, alichokifanya ni kulikimbilia huku akimtaka dereva kusimama.
Kila mtu aliyekuwa akiliangalia tukio lile alibaki akishangaa, walimshangaa Amon aliyeonekana kama kuchanganyikiwa. Wengine wakahisi kama yalikuwa maigizo fulani yaliyokuwa yakiendelea mahali hapo, hivyo wakaanza kuangalia huku na kule kuona kama kulikuwa na kamera.
“Imekuwaje tena mwanaume unalia hovyo kama mtoto?” alihoji jamaa mmoja huku akimwangalia Amon aliyesimama na kulia kama mtoto mdogo, mpaka makamasi yakawa yanamtoka.
Kilichotokea kiliendelea kumuumiza, ilikuwa ni siku ambayo alijua asingekuja kuisahau maishani mwake mpaka anaingia kaburini. Kwa kile kilichotokea alihisi kama alikuwa ndotoni ambapo baada ya dakika kadhaa angeamka na kujikuta akiwa kitandani.
Haikuwa ndoto, lilikuwa tukio halisi lililokuwa likitokea kwenye maisha yake. Aliondokewa na msichana aliyekuwa akimpenda kupita kawaida, akaamua kurudi nyumbani kwao.
Njiani mawazo yalikuwa kwa Angelina tu, hata mazoezini hakwenda, alichanganyikiwa, mapenzi yalimuendesha na kugundua kweli yalikuwa yakiumiza kuliko msiba, mapenzi ya kuachwa yalikuwa yakitesa kuliko fimbo za wakoloni.
Alipofika nyumbani, akajifungia chumbani na kuanza kulia kama mtoto. Kwa siku hizo mbili hayo yakawa maisha yake, hakuacha kulia, hakuacha kuumia moyo wake, kila alipokaa, picha ya Angelina ilionekana ubongoni mwake, ilikataa kabisa kutoka.
Alikaa chumbani mpaka majira ya saa moja, akasikia simu yake ikiita, alipoangalia kioo, mpigaji alikuwa Angelina. Moyo wake ukapiga paa! Harakahara akaipeleka sikioni.
“Halo mpenzi!” aliita.
“Njoo Shojozi, Sinza Kumekucha,” alisema msichana huyo na kukata simu.
Haraka sana Amon akakurupuka, akavaa nguo zake harakaharaka, akatoka na kuchukua bodaboda na kuanza kwenda huko.
Simu hiyo ilimfariji, kulikuwa na sauti moyoni mwake iliyomwambia sasa Angelina aliamua kujirudi, alimuita huko kwa lengo la kumuomba msamaha na mapenzi yarudi kama yalivyokuwa siku zilizopita.
Akiwa kwenye bodaboda, uso wake ulionekana kuwa na furaha, kwenye vitu ambavyo hakutaka kabisa kuona vikitokea, basi cha kwanza kilikuwa ni kumpoteza msichana huyo. Angelina alikuwa roho yake, moyo wake na alimpenda kupita kawaida.
Baada ya kufika kwenye mgahawa huo mdogo, akaingia ndani na macho yake kutua kwa msichana huyo, akamwangalia, aiseee Angelina alikuwa mrembo, alikuwa ni zaidi ya kipindi cha nyuma. Ile kumuona tu, moyo wake ukaingiwa na hali fulani ya furaha. Akamsogelea, akamsalimia kwa furaha na kukaa kitini.
“Amon! Nimekuita kwa jambo moja tu,” alisema msichana huyo.
“Niambie mama!”
“Naomba usinisumbue. Ile picha ya shuleni haikuwa nzuri, unataka kunigombanisha na mpenzi wangu, unataka nifukuzwe shule?” alimuuliza huku akimwangalia.
Maneno hayo tu ni kama yalikuwa msumali wa moto moyoni mwa Amon, hakuamini alichokisikia, alihisi kama alisikia vibaya, hivyo akamtaka Angelina arudie tena na tena.
“Naomba unisaidie kitu kimoja, endelea na maisha yako! Mbona simpo tu jamani, mambo ya kufuatiliana kwani mwanamke nipo peke yangu? Nimeachana na wewe kwa sababu kuna mtu amekuja maishani mwangu, ananipenda zaidi ya unavyonipenda, ananijali na kunilinda sasa. Naomba tu, nakuomba sana uendelee na maisha yako. Mbona unakuwa mbishi we’ kaka?” alisema Angelina na kusimama, Amon akamshika mkono.
“Angelina! Niambie tatizo nini!” alimuuliza, tayari machozi yakaanza kujikusanya machoni mwake.
“Wala hakuna tatizo, ninachoomba ni uachane na mimi tu.”
“Kuna baya nimekufanyia?”
“Hapana!”
“Kuna kitu kilikukera?”
“Hapana!”
“Sasa kwa nini umeamua kuniacha na kuniadhibu kiasi hiki?”
“Nimekwambia hapo kabla, nimempata mtu anayenipenda na kunijali zaidi yako!”
“Kwa maa....” alisema lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake msichana huyo akaanza kuondoka.
“Angelina!”
“Amon! Mbona unakuwa king’ang’anizi hiviiiii?”
“Ninakupenda sana!”
“Najua hilo!”
“Unanipenda?”
“Nakupenda ila sitoweza kuwa na wewe. Endelea na maisha yako kaka yangu. Uwe na maisha mema na huyo utakayempata!” alisema Angelina na kuanza kuondoka.
Sasa hapo Amon akapata ukweli kwamba alikuwa ameachwa mazima, kwa namna Angelina alivyokuwa ameongea, aliamini huo ndiyo ulikuwa mwisho wa mapenzi yao yaliyodumu kwa kipindi kama cha miaka miwili na nusu.
Alimwangalia Angelina alivyokuwa akiondoka, moyo wake ulimuuma sana alipogundua huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kuwa na msichana huyo mrembo.
“Mshukuru Mungu kwani hujui amekuepusha na kitu gani hapo baadaye, inawezekana ungeendelea kuwa na Angelina utakuwa na mwisho mbaya, Mungu ameliona hilo na ameamua kukuepusha nalo mapema,” ni maneno pekee ya baba yake ndiyo yaliyojirudia kichwani mwake, akaamua kuishi nayo.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Ijumaa hapahapa.
Tukumbuke kwamba hadithi itamalizikia hapahapa ila kwa wenye haraka unaweza kuipata WhatsApp kwa namba 0718069269.
 
Pole sana Amon ndio mapenzi hayo
Acha nitulie hapa sijui lini tena
 
Sehemu ya 11.

Anita alikuwa mfanyabiashara, alizaliwa kwenye familia iliyokuwa ikijua masuala ya biashara na kubwa zaidi alisoma masomo ya biashara. Kila alipokuwa akikaa, kichwa chake kilikuwa kinafikiria ni kwa namna gani angeweza kuingiza pesa nyingi kwenye akaunti ya baba yake.
Alitumia kiasi kikubwa cha pesa kununua wachezaji kwenye timu ya FC Hertha Berlin lakini hakuwa amepata mafanikio yale waliyokuwa wakiyapata wenzake. Alihangaikia wachezaji wengi lakini bado hawakupata walichokuwa wakikitaka.
Hawakuwa na uwezo mkubwa wa kupambana na timu kubwa kama Bayern Munich ama Borussia Dortmund, walichokuwa wakikifanya ni kununua wachezaji kwa gharama nafuu sana na baadaye wakishakuwa hatari waliwauza kwa bei kubwa na kujiingizia kiasi kikubwa cha pesa.
Hiyo ndiyo ilikuwa biashara yao, walichokuwa wakikifanya ni kuwasiliana na maskauti wao waliokuwa wakienda mitaani na vyuoni na kuwachukua wachezaji ambao waliwakuza na baadaye kuwa wakubwa na kuwapiga bei.
Kwa jinsi alivyosikia sifa za Amon na alivyomuona, moyo wake ulimwambia angekuja kuwa mchezaji hatari hapo baadaye, alikuwa na uwezo mkubwa uliomfanya kila mmoja kutokuamini kama kwenye maisha yake angemuona mchezaji mwingine aliyekuwa akicheza kama Lionel Messi.
Alitamani sana kumuita kwenye timu yao, alizungumza naye lakini mpaka muda huo hakuwa na uhakika kama kweli angeweza kujiunga na timu yao.
Huko Tanzania alipokwenda Amon ilikuwa ni lazima afuatwe, kwa jinsi alivyokuwa akicheza, aliamini hata maskauti wengine walikuwa wakimnyemelea, kama kweli alimtaka basi amfuate vinginevyo angepelekwa Ujerumani na watu wengine na kusajiliwa.
Hakutaka kupoteza muda, haraka sana akazungumza na baba yake na kumwambia kuhusu hilo. Lilikuwa wazo zuri sana, akakubaliwa na haraka sana kuondoka kuelekea nchini Tanzania.
Njiani akili yake ilikuwa ikimuwaza Amon tu, aliamini angemchukua na baadaye kumuuza hata kwa paundi milioni mia moja kama tu angetua kwao na kumtangaza.
Ndege ilichukua saa nyingi sana na hatimaye kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Hali ya hewa ilikuwa ni ya joto sana lakini hakutaka kujali, alilijua hilo kwamba alikuwa akienda katika nchi zilizokuwa zimepitiwa na mstari wa Ikweta, hivyo alijiandaa kwa kila kitu.
Haraka sana akachukua teksi ambayo ilimpeleka mpaka katika Hoteli ya Kilimanjaro na kutulia hapo. Alichukua chumba alichoweka oda mapema na kujifungia chumbani kwake. Alimshukuru Mungu kwa kufika nchini humo salama na hivyo alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anamuona Amon na kuonana naye.
Kwa kuwa ilikuwa ni usiku sana, hakutaka kujisumbua, akapumzika na siku iliyofuata kazi ya kwanza kabisa ni kuulizia mahali kituo kile cha mpira kilipokuwa kikipatikana na kuanza kuelekezwa, akachukua teksi na kuelekea huko.
Akafika mahali hapo. Kulikuwa na vijana wengi waliokuwa wakicheza mpira, alifurahi kuwa mahali hapo hivyo alisimama na kuanza kuwaangalia. Aliungana na watu wengine waliokuwa wakitazama jinsi mazoezi yalivyokuwa yakiendelea.
Kwenye kutazama huko, macho yake yakatua kwa mtu aliyekuwa akimtaka sana, alikuwa Amon. Kwa jinsi alivyokuwa akicheza, alionekana kuwa tofauti na watu wengine, alicheza kwa uwezo mkubwa na mipira yake mingi ilikuwa ikifika kwa mtu mmoja aliyeonekana kuwa mmaliziaji mzuri, alikuwa Gideon.
Anita alifurahi, alijua kabisa yule mtu aliyekuwa ameambiwa na Amon alikuwa huyo aliyekuwa akimpa mipira kila wakati. Kwa kuwa na watu hao wawili kwenye timu yako ilimaanisha ingekwenda kutisha sana siku za usoni, na kubwa zaidi ni kuwa ungetengeneza pesa sana kutoka kwenye timu nyingine.
Hakutaka kumfuata Amon na kuzungumza naye, alikaa na watazamani wengine mpaka mazoezi yalipomalizika na walipokuwa wakiondoka tu, haraka sana akaanza kumfuatilia Amon aliyekuwa na Gideon.
Kwa siku hiyo alimuona kuwa tofauti sana, hakuwa kama kipindi cha nyuma, hakuonekana kuwa na furaha hata kidogo, alionekana kuwa na jambo fulani lililokuwa likimtatiza nyuma ya pazia, hakujua ni jambo gani lakini aliamini baada ya kumuona basi furaha ingerudi tena kwa kuamini sasa angekuwa anakwenda kuishi Ulaya.
Alimfuatilia Amon mpaka alipoingia ndani ya daladala na kurudi nyumbani, naye akaingia humo na kuanza kuondoka mahali hapo. Hakuwa amemshtua wala kumwambia lolote lile, safari iliendelea na gari lilipofika kwenye kituo alichokuwa akiteremka, akateremka, naye Anita akateremka.
“Amon!” aliamua kumuita.
Amon akageuka na kumwangalia mtu aliyemuita, kwa jinsi sauti ilivyotoka alijua kabisa hakuwa Mswahili, kama alikuwa Mzungu, ni nani huyo? Alipomuona Anita, akashtuka, alimkumbuka msichana huyo, alikuwa yule wa nchini Ujerumani.
“I found you, at last,” (Hatimaye nimekuona) alisema Anita na kuanza kumsogelea, wakakumbatiana na kuanza kusalimiana.
Kwa Amon hakuamini kama angeweza kumuona msichana huyo nchini Tanzania, hakufikiria hilo hata kidogo kwani aliamini baada ya kila kitu angempigia simu na kuanza kuzungumza naye.
Watu waliokuwa pembezoni mwa barabara walikuwa wakiwaangalia wawili hao, walionekana kufahamiana na hata walipokuwa wakiongea kila mmoja alionekana kuwa na furaha tele.
Amon akamwambia ni lazima ampeleke nyumbani kwao, akawaone hata wazazi wake na kuzungumza nao. Hilo ndilo alilokuwa akilitaka sana Anita, alitaka kuonana na wazazi wake, wazungumze, hilo lingekuwa rahisi sana kumchukua kijana huyo.
“You seem so upset,” (Unaonekana huna furaha) alimwambia Amon huku akimwangalia.
“How do you know that?” (Umejuaje?)
“I know you!” (Nakufahamu) alimjibu na kutoa tabasamu.
“A little bit,” (Kidogo tu)
“Yeah! Is there anything wrong?” (Ndiyo! Kuna tatizo lolote?) alimuuliza.
Amon hakuona sahihi kumwambia Anita kile kilichotokea. Ni kweli hakuwa na furaha hata kidogo, mapenzi yalimsumbua na kumfanya kutokuwa na raha kabisa lakini hiyo haikuwa sababu ya kumwambia msichana huyo.
Aliangalia kama angeweza kumsaidia kwenye hilo, akagundua asingeweza hivyo hakuona umuhimu wa kumshirikisha kwenye hilo. Alichomwambia ni kwamba hakujisikia vizuri kiafya, alikuwa akiumwa na ndiyo maana alikuwa hivyo.
Kwa Anita halikuwa tatizo, walizungumza mpaka walipofika nyumbani. Wazazi wake walishangaa Amon kuingia na Mzungu, hawakujua alikuwa nani na kulikuwa na kitu gani kilichokuwa kikiendelea.
Hapo ndipo alipoanza kutoa utambulisho kwa wote, wakagundua huyo ndiye yule Mzungu aliyeonana naye nchini Ujerumani na kumwambia alitaka awe mchezaji kwenye timu ya FC Hertha Berlin.
Siku hiyo walizungumza mambo mengi sana, mzee Stephano alikuwa na furaha mno, alikubali kwa moyo mmoja mtoto wake aende nchini Ujerumani lakini la muhimu lilikuwa ni kuzungumza na kituo kilichokuwa kikimlea kwenye mambo ya mpira.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, akakubali na kuondoka zake huku akiwaahidi kukamilisha kila kitu, ndani ya siku kadhaa wangekuwa ndani ya ndege na kuelekea nchini Ujerumani na mtu mwingine aliyeitwa Gideon.
Usiku wa siku hiyohiyo Amon akampigia simu Gideon na kumwambia kilichotokea, kwa kijana huyo hakuamini kama ingekuwa haraka namna hiyo, kwa Anita kusafiri kutoka Ujerumani na kwenda nchini Tanzania kwa ajili yao hakika ilikuwa ni bahati sana.
“Nashukuru sana rafiki yangu kwa msaada wako,” alisema Gideon.
“Usijali! Ila naomba kitu kimoja,” alimwambia.
“Kitu gani?”
“Sihitaji Angelina afahamu lolote lile. Kama unamwambia utaondoka, basi mwambie mimi nimebaki! Sitotaka afahamu lolote kuhusu maisha yangu,” alimwambia.
“Unadhani itaendelea kuwa siri?”
“Acha mpaka atakapogundua kwa kuona na si kuambiwa,” alimwambia.
“Haina shida!”
“Sawa. Usiku mwema.”

Je, nini kitaendelea?
Tukumbuke simulizi hii inaendelea kupatikana WhatsApp kwa namba 0718069269 kwa gharama nafuu. Kwa wasiokuwa na hela, tuendelee kuisoma hapahapa mpaka mwisho japo itakuwa ikienda taratibu sana.
 
Sehemu ya 12.

Kitu cha kwanza alichofanya Anita siku iliyofuata ni kwenda kuonana na uongozi wa kituo cha kulelea vijana wa mpira na kuzungumza nao, aliwaambia jinsi alivyokuwa akiwakubali Amon na Gideon na alifika mahali hapo kwa ajili ya kuzungumza nao na kuondoka nao.
Hilo halikuwa tatizo, bosi wa kituo aliangalia maslahi kwanza, hakutaka kuleta tamaa, alichomwambia Anita kama wangeingia mkataba basi wakubaliane kwenye kila bei atakayouzwa Amon kwenda timu yoyote ile kuwe na fungu lao la asilimia tano ya mauzo hayo.
“Hilo halina tatizo!”
“Kwa sasa hivi hana wakala, wakala wakubwa ni wazazi wake, hivyo utatakiwa kuzungumza nao na kuingia makubaliano ya maandishi,” alisema bosi.
“Pia hakuna tatizo!”
Siku hiyohiyo wazazi wa Amon na Gideon wakapigiwa simu na kwenda kituoni ambapo walizungumza na Anita na baada ya makubaliano yote kufanyika, hatimaye vijana hao wawili wakatakiwa kujiandaa na kuanza safari baada ya siku mbili.
Ilikuwa ni furaha kwa wote, hawakuamini kama sasa maisha yao yangekwenda kuanza nchini Ujerumani. Kwa kila kilichotokea walihisi kama walikuwa wakiota. Kwa Amon sasa akawa na hamu ya kutimiza ndoto yake ya kuwa mchezaji mkubwa duniani, alitaka kupambana kwa nguvu zote kuhakikisha anakuwa mchezaji hatari na wa kuogopwa sana.
Kama alivyoambiwa Gideon naye alifanya hivyohivyo, hakutaka kumwambia Angelina kilichotokea, alimwambia tu kwamba ni yeye pekee ndiye aliyekuwa akienda nchini Ujerumani kuanza maisha ya mpira huko.
Msichana huyo alifurahi mno kwa kuona sasa hata naye safari za kwenda Ujerumani na hata kuzunguka Ulaya nzima zingemuhusu kwa kuwa angekuwa na ndugu huko. Akayaona maisha yake yakibadilika na kuwa mtu mwingine kabisa.
Hakuacha kumuombea kaka yake kwani aliamini endapo angefanikiwa basi hata naye pia angeonja utamu wa mafanikio hayo, angepata pesa nyingi na yeye kuwa tajiri.
“Nitamuomba Mungu kila siku ufanikiwe na kuwa na mafanikio makubwa,” alisema Angelina huku akimwangalia kaka yake.
“Omba Mungu sana! Nitakuwa mchezaji mkubwa mno,” alimwambia ndugu yake huyo.
Wakati akimwambia hayo moyoni mwake alikuwa akimuona kuwa msichana mpumbavu sana, alisumbuka na mambo madogo na wakati kulikuwa na makubwa ambayo Mungu alimuandalia.
Alitamani kumwambia kuhusu Amon lakini aliyakumbuka maneno ya kijana huyo kwamba hakutakiwa kumwambia lolote lile kuhusu yeye, alitaka kwa macho yake baadaye ajionee jinsi alivyokuwa akifanikiwa bila kuwa pembeni yake.
Baada ya siku nne, hatimaye walikuwa ndani ya ndege wakiondoka na kuelekea nchini Ujerumani. Kila mmoja alikuwa haamini alichokuwa akikiona, wakati mwingine bado waliamini walikuwa kwenye ndoto ya kusisimua tu lakini hawakuwa wakielekea nchini humo.
Wakati wakiwa humo, Anita alikaa kwenye kiti kingine kabisa, alikuwa akiwaangalia vijana hao jinsi walivyokuwa na furaha, kwenye suala hilo walikuwa wakisaidiana, yeye alikuwa akiwasaidia kwenye kutimiza ndoto zao za kucheza Ulaya lakini naye alikuwa akisaidiwa kupata pesa nyingi zaidi ya zile walizokuwanazo.
“Tunaondoka tukiwa masikini! Ila tutarudi tukiwa matajiri!” alisema Gideon.
“Hakika! Ninaondoka nikiwa sina kitu, ila nitarudi nikiwa na medali ya kombe la Champions League na Tuzo ya Mchezaji Bora wa Dunia,” alisema Amon huku akijaribu kuangalia mawingu kupitia kidirisha kidogo.
“Na tuseme Amen!”
“Amen.”
Baada ya masaa mengi, ndege ikaanza kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Berlin, Amon na Gideon walikuwa wakichungulia nje kupitia dirishani, hawakuamini hatimaye walirudi nchini Ujerumani, kwa kipindi hiki haikuwa mara moja na kurudi Tanzania bali wangeendelea kuishi hapo kwa kipindi kirefu kijacho.
Katika kipindi hicho msimu wa baridi kali ndiyo ulikuwa umeanza, kila mmoja alivalia koti kubwa lakini hawakuacha kutetemeka, baridi lile liliwaingia mpaka ndani ya mifupa yao na kupata shida kwa kiasi kikubwa lakini hawakujali, hilo baridi halikuwafanya kutamani kurudi nchini Tanzania pasipo kufanikiwa, ilikuwa ni lazima wafanikiwe tu.
Baada ya ndege kusimama, abiria wakaanza kuteremka wakiwemo wao, walikuwa wakitembea huku wakionekana kujishtukia, walimwangalia Anita aliyekuwa akifurahi, kwake kwenda Tanzania na kuwachukua vijana hao hakika yalikuwa ni mafanikio makubwa ambayo hakuwa akiyafikiria kabisa.
Kama wafanyabiashara wengine, hata naye alikuwa akiangalia pesa tu, kila alipowaangalia vijana hao aliziona pesa nyingi kwenye akaunti yake na kilichokuwa kimebaki kilikuwa ni kuzitumia kadiri alivyoweza.
Wakateremka na kuanza kutembea kuelekea kwenye jengo kubwa la uwanja huo. Macho yao hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, waliendelea kutokuamini kama walirudi tena nchini humo na kuanza maisha yao mapya.
Kwa kila mchezaji mpira barani Afrika ndoto yake kubwa ilikuwa ni kwenda kucheza mpira barani Ulaya. Hiyo ilikuwa ni moja ya sehemu ambayo kila mmoja aliamini kufanikiwa kimaisha na kuweka historia kwenye maisha yako endapo tu ungebahatika kucheza klabu yoyote huko.
Hiyo ndoto waliyokuwanayo wachezaji wengi wa Afrika, waliipata wao, walikuwa tayari kuitimiza na kufikia malengo yao makubwa katika maisha yao ya hapo baadaye.
Walipofika ndani ya jengo hilo mizigo yao na hati za kusafiria zikakaguliwa na walipoonekana kutokuwa na tatizo lolote lile, wakaruhusiwa na kuvuka kwenda mbele.
Huku wakiwa wanatembea, ghafla msichana mmoja ambaye alionekana kuwa na mchanganyiko wa rangi akaanza kumkimbilia Anita na alipomfikia tu, akamkumbatia huku kila mmoja akionekana kuwa na furaha tele.
“Where have you been?” (Ulikuwa wapi?) alimuuliza huku akimwangalia.
“I had a long journey,” (Nilikuwa na safari ndefu) alimwambia.
Msichana huyo akayageuza macho yake na kuwaangalia vijana wawili waliosimama pembeni mwa Anita, kwa jinsi walivyoonekana walikuwa watu wa mazoezi, miili yao ilikomaa na walimwangalia huku wakiwa na tabasamu pana.
Hakuwajua walikuwa akina nani na alisubiri kupata utambulisho kutoka kwa rafiki yake huyo ambaye bila tatizo lolote lile wala kupoteza muda, akaanza kuwatambulisha, na baada ya hapo, naye akajitambulisha kwa jina la Jeniffer Fork.
Jeniffer alifika hapo kwa lengo la kuwapokea watu hao, baada ya utambulisho huo wakaondoka na kuelekea nje kabisa ambapo wakapanda gari alillokuwa amekuja nalo na kuondoka mahali hapo.
Bado macho yao hayakutulia, ilikuwa ni kwa mara ya pili kufika nchini humo lakini hawakuacha kushangaa, kwao ilikuwa ni ndoto moja kubwa na ya kusisimua sana kwamba hatimaye walifika Ujerumani kwa mara ya pili na katika kipindi hiki walifika kwa lengo la kucheza mpira tu.
“Hast du seine augen gesehem” (Umeyaona macho yake?) aliuliza Jeniffer kwa Kijerumani, hakutaka kueleweka.
“Wessen augen?” (Macho ya nani?)
“Der grobe,” (Huyo mrefu)
“Was zur holle ist los mit ihnen?” (Yamefanyaje?)
“Sie sind so schon,” (Ni mazuri mno) alijibu.
“Lieben sie ihn?” (Umempenda?) aliuliza Anita.
Jeniffer hakutaka kujibu swali hilo, akalipotezea na kuongelea mambo mengine tu huku akionekana kuwa na furaha kupita kawaida. Mtu ambaye alikuwa akimzungumzia alikuwa Amon aliyekuwa mrefu kidogo zaidi ya Gideon.

Je, nini kitaendelea?
Tukumbuke simulizi hii inaendelea kupatikana WhatsApp kwa namba 0718069269 kwa gharama nafuu. Kwa wasiokuwa na hela, tuendelee kuisoma hapahapa mpaka mwisho japo itakuwa ikienda taratibu sana.
 
Sehemu ya 13.

Safari hiyo ilitumia dakika kumi hatimaye wakafika kwenye hoteli moja nzuri iliyoandikwa Paradise na kuteremka, wakapokewa mizigo na kupelekwa mapokezini ambapo hapo wakachukua vyumba na kuelekea ndani.
Anita aliongozana nao, wakaingia kwenye chumba kimoja kilichokuwa na vitanda viwili na kutulia. Msichana huyo huku akiwa na Jeniffer wakaanza kuongea, alichowaambia ni kuwa hoteli hiyo ilikuwa ikimilikiwa na baba yake Jeniffer hivyo hawakutakiwa kuwa na hofu hata kidogo.
Hapo ndipo wakagundua ili kupata marafiki wenye pesa ilikuwa ni lazima na wewe uwe na pesa. Walimfikiria mtu kama Anita, alizaliwa kwenye familia yenye pesa, alikuwa na pesa lakini pia akampata rafiki ambaye naye alikuwa na pesa kama alivyokuwa.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha, mfumo wake ulikuwa wa namna hiyo. Masikini walikuwa marafiki na matajiri nao walikuwa marafiki, ilikuwa ni vigumu kuona watu wenye madaraja tofauti wakiwa marafiki walioshibana kwa asilimia mia moja.
Walizungumza kwa dakika chache huku dakika zote hizo Jeniffer akiwa anamwangalia Amon kwa macho yaliyoonyesha alikuwa akimuhitaji sana kuwa naye lakini mpaka kipindi hicho, kutokana na roho ya hofu aliyokuwanayo, Amon hakuweza kuyasoma macho ya msichana huyo.
Walipomaliza kuongea, wakaondoka na Anita kumwambia angekuja kuongea nao kesho yake, walitakiwa kujiandaa kupumzika kwani tayari ilikuwa ni saa mbili usiku na kulikuwa na baridi kali mno.
Jeniffer hakujiweza, alimwambia rafiki yake kwamba moyo wake ulichanganyikiwa, kila alipokuwa akimwangalia Amon, alihisi kabisa nyota yake ikiburuzwa na ya kijana huyo hivyo alitamani sana kuwa naye.
Kwa Anita alifurahi sana kusikia hivyo, alitamani kuwaunganisha wawili hao kwa sababu moja kubwa. Kama Amon angekubali kuwa na msichana huyo na wakapendana sana basi hapo baadaye ingekuwa rahisi sana kwake kumtumia Jeniffer kufanikisha mambo yake.
Alijua kabisa huko mbeleni Amon angetakiwa na timu nyingi baada ya kuona uwezo wake, aliamini timu hizo zingekwenda na pesa ndefu ambazo angeshindwa kumzuia hivyo msaada wake mkubwa ungekuwa kwa msichana huyo, angemtumia kuzungumza na Amon na hivyo kukubaliana na kile alichokuwa akikihitaji.
“Nitafurahi sana kumpata!” alisema Jeniffer.
Usiku wa siku hiyo hakulala, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria sana Amon, alitokea kumpenda kupita kawaida na kwa kipindi hicho hakutaka kuwa na mwanaume yeyote yule zaidi ya huyo Amon.
Alikuwa msichana aliyezaliwa kwenye familia ya watu wenye pesa, kama ilivyokuwa kwa Anita hata naye baba yake alikuwa na utajiri mkubwa huku akiwa amemuoa mwanamke mweusi kitu kilichomfanya kuzaliwa yeye na kuwa na mchanganyiko wa rangi.
Jeniffer alikuwa mzuri mno, uzuri wake ulikuwa ni zaidi ya Anita, alijipenda, alitamani sana kuwa kwenye uhusiano na mtu ambaye angemuonyesha mapenzi ya dhati, mtu ambaye angesimama mbele yake, akamwangalia machoni na kumwambia ni kwa namna gani alikuwa akimpenda kwa moyo wote.
Hakuwahi kupata mwanaume wa hivyo, wengi wao walikuwa wadanganyifu, walimdanganya kumpenda lakini baada ya kumvua nguo, wakamkimbia.
Mapenzi yalimkoroga, akakorogeka na kuamua kuachana nayo huku akisema asingeingia tena kwenye mapenzi lakini baada ya kumuona Amon, moyo wake ukaanza kiherehere cha kuanza kumpenda.
Huku akiwa chumbani kwake akimfikiria Amon, kuna kitu alikifikiria na aliona lingekuwa jambo zuri kama kingefanyika, haraka sana akaichukua simu yake na kumpigia Anita, alitaka kumwambia jambo fulani kwanza.
“Nimempenda sana yule Amon,” alimwambia.
“Sawa. Ulishaniambia hilo!”
“Ninahitaji uniunganishe naye! Niwe karibu naye kabla ya wanawake wengine kumuona na kumuiba,” alimwambia.
“Unataka nikufanyie nini?”
“Kesho umwambie niende naye sehemu, nimtembeze auone mji. Ninataka anizoee kwa staili hiyo!” alimwambia.
“Halafu na mwenzake?”
“Sasa huyo si uende naye wewe!”
“Kwamba na mimi nimpende?”
“Wala sijasema hivyo! Wewe nenda naye, mzururishe sehemu huku ukisubiri mimi nimalizane na huyu mtu,” alimwambia.
“Jeniffer....”
“Naomba unisaidie rafiki yangu!”
“Sawa.”
“Nakupenda sana!”
“Nakupenda pia.”
Sasa moyo wake ukawa na furaha tele, hakuamini kama rafiki yake huyo angemkubalia kirahisi namna hiyo. Kesho yake ilipoingia, haraka sana akawasiliana na Anita na kumwambia tayari alifika hotelini hivyo alitakiwa kwenda kuonana naye.
Wakaonana, wakazungumza na hatimaye kuwaita vijana hao ambao walikunywa chai na kuwaambia muda wa kwenda kutembea ulifika hivyo kwanza walitakiwa kufanya hivyo kabla ya kuelekea kituoni.
Hilo halikuwa tatizo, wakajigawa na Jeniffer kwenda na Amon. Msichana huyo alifurahi sana kuwa karibu na Amon, alimpenda kutoka moyoni mwake na kila alipokuwa akitembea naye na kugusana kidogo tu, alihisi kama alikuwa akipigwa na shoti ya umeme.
Amon alizaliwa uswahilini, alijua mitikasi yote ya wanawake, tangu alipokutana naye uwanja wa ndege, walivyoingia ndani ya gari na hata kufika hotelini tayari alijua kabisa msichana huyo alitokea kumpenda.
Macho yake hayakudanganya, kila alipokuwa akimwangalia, alionekana kuvutiwa naye, hivyo akasubiri mpaka pale atakapoambiwa, na bila hiyana naye angemwambia anampenda na hivyo kuanza uhusiano wa kimapenzi.
Moyo wake ulimkumbuka sana Angelina, na kila alipokuwa akimkumbuka aliumia moyoni mwake, hakumsahau na aliamini njia mojawapo ya kumkumbuka msichana huyo ni kuingia kwenye uhusiano na msichana mwingine, na hilo ndilo alilotaka kulifanya.
“Huu ni ukuta wa Berlin,” alimwambia huku akimuonyesha ukuta huo ambao ulivunjwa na kubaki sehemu chache kama kumbukumbu.
“Ndipo Wajerumani wa Mashariki na Magharibi walipokuwa wamegawanyika?” aliuliza Amon.
“Ndiyo! Kama ulishawahi kuusoma, basi ndiyo huu hapa,” alimwambia. Amon akabaki akiyaangalia mabaki ya ukuta huo tu.
Kwa kuwa kulikuwa na watu wengi, wakamwambia mtu mmoja awapige picha ya ukumbusho mahali hapo, picha hiyo ikapigwa huku wakiwa wamesimama kwa karibu, baada ya hapo wakaondoka na kuelekea mgahawani kula.
“Huwa unapenda kufanya nini?” alimuuliza Amon huku wakiendelea kula.
“Kucheza mpira!”
“Hilo tu?”
“Labda na kusikiliza muziki!”
“Oh! Na unajua kucheza huo muziki?”
“Si sana! Labda kidogo tu, huwa nachezaga kwa kuwaangalia Jabbawockeez,” alijibu.
“Wale Wamarekani?”
“Yeah! Haohao! Na wewe unapendelea kitu gani?” alimuuliza.
“Labda kula!”
“Mbona hunenepi?” aliuliza huku akitabasamu.
“Huwa sili sana mafuta!”
“Sawa! Nimefurahi kusikia hivyo!”
“Labda una swali jingine?”
“Labda kuhusu familia yako! Ningependa sana kujua kuhusu wazazi wako, ndugu na mambo ambayo ungependa niyafahamu,” alimwambia.
Hilo halikuwa tatizo, Jeniffer akaanza kumwambia mambo mengi kuhusu yeye, elimu yake, maisha yake ya shule na nyumbani, jinsi wazazi wake walivyomlea na kumpa usimamizi wa moja ya hoteli zao, yaani kwa jinsi alivyojielezea, Amon akagundua alikuwa akizungumza na msichana aliyetoka kwenye familia ya kitajiri.
“Nimefurahi kusikia mengi kuhusu wewe!” alimwambia.
“Nashukuru sana!” alisema msichana huyo.
Wakabaki kimya kwa sekunde kadhaa, sasa walizoeana. Jeniffer alikuwa akitafuta nafasi ya kumwambia mwanaume huyo ni kwa jinsi gani alikuwa akimpenda naye Amon alikuwa akisubiri aambiwe hilo tu ili akubaliane naye na hatimaye kuingia kwenye uhusiano wa kimapenzi.
Msichana huyo akawa hamwambii, kazi yake ilikuwa ni kuzunguka kwa kupiga stori ambazo hazikuwa na kichwa wala miguu ilimradi tu kupoteza muda.
“Sogea karibu yangu,” alisema Amon, tayari aligundua msichana huyo alikuwa muoga, hivyo alitaka kumsaidia kwenye hilo, msichana huyo akasogea. Wakaanza kuangalia kwa karibu.
“Una lipsi nzuri sana,” alimwambia.
“Ahsante!” alijibu Anita huku akionekana kusikia aibu, Amon akamsogelea zaidi na kuanza kubadilishana mate humohumo hotelini, japokuwa kulikuwa na watu wengi lakini hapakuwa na mtu yeyote aliyeshangaa kwani kilikuwa kitu cha kawaida sana kwa nchi za Ulaya na Marekani.
“Macho yako yalinieleza kila kitu!” alimwambia baada ya sekunde thelathini za kubadilishana mate.
“Ila niliogopa kukwambia!”
“Najua sana! Nini kinachofuata?” alimuuliza.
“Labda ni kupendana kwa moyo wa dhati, kuwa wakweli na kujaliana. Uongo usichukue nafasi kati yetu,” alisema Jeniffer.
“Haina shida. Nitakupenda siku zote!”
“Nashukuru sana!”


Je, nini kitaendelea?
Tukumbuke simulizi hii inaendelea kupatikana WhatsApp kwa namba 0718069269 kwa gharama nafuu. Kwa wasiokuwa na hela, tuendelee kuisoma hapahapa mpaka mwisho japo itakuwa ikienda taratibu sana.
 
Mambo yameanza kunoga
Sisi tusiokuwa na hela acha tubaki hukuhuku jf
 
Sehemu ya 15.

Kadiri ziku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele ndivyo uzuri wa Angelina ulivyokuwa ukiongezeka, kila siku alionekana msichana mpya kama aliyeshushwa kutoka Mbinguni.
Hakuisha hamu, mwili wake ulikuwa ukizidi kujiboresha kila siku, hipsi zilikuwa zikionekana vyema, kifua chake kilizidi kujaa kuonyesha sasa alikuwa akienda kwenye urembo uliopitiliza.
Kila kona aliyokuwa akipita wanaume walibaki wakimwangalia, na alipopotea walikuwa wakimjadili ni kwa namna gani Mungu alimpendelea, hakuwa msichana wa kawaida hata kidogo, kama angesimama na wanawake ambao unawaamini ni warembo halafu ukaambiwa uchague mmoja, bila shaka ungemchagua Angelina.
Edmund hakutaka kumuacha Angelina, japokuwa alikuwa na mambo yake mengi lakini kwa msichana huyo alitulia kabisa.
Hakuacha kufuata wanawake mbalimbali, alijiambia baada ya kuwa na Angelina angebadilika, asingekuwa malaya tena lakini akashindwa kuvumilia kwa sababu moja tu, alimzoea.
Akawa anamuona msichana wa kawaida ila kwa sababu alisifiwa kila kona, akaona endapo angeachana naye basi kuna siku angekuja kujuta na kutamani sana kuwa naye. Alivumilia na kuvumilia, kutembea na wanawake wengine ilikuwa ni kwa siri kubwa, hapakuwa na mtu aliyekuwa akifahamu kama alikuwa wa aina hiyo.
Kitu kingine ambacho Edmund alimuweza Angelina ni kwa namna alivyokuwa mnyenyekevu mbele yake, alikuwa mtu aliyemuheshimu na alipokuwa akifanya kosa, haraka sana alimuomba msamaha na kuendelea na mambo mengine.
Kwa Angelina huyo alikuwa mwanaume wake wa ndoto, kulikuwa na wanaume wengi waliokuwa na kiburi ambao walimuona mwanamke kuwa takataka fulani lakini ilikuwa tofauti kwa huyo Edmund.
Kwa jinsi alivyokuwa akiishi na Angelina, kila mwanamke alitamani sana kuwa na mwanaume wa aina hiyo, alikuwa ni wa kipekee sana kiasi cha kuwafanya mpaka wanawake wengine kutamani hata siku moja wasimamishwe na mwanaume aliyekuwa na kariba kama ya Edmund.
“Ninakupenda kwa sababu unanielewa mpenzi,” alisema Edmund huku akimwangalia Angelina.
“Ninakupenda kwa sababu u mnyenyekevu na unajua kupenda,” alisema Angelina.
“Sidhani kama nisingekuwa na msichana kama wewe, nisingeweza kupata msichana sahihi kama wewe. Ninakupenda sana Angelina, nitakupenda maisha yangu yote,” alisema Edmund huku akimwangalia msichana huyo aliyekuwa akivaa nguo zake chumbani baada ya kazi nzito ya kukilazimisha kitanda kipige kelele.
Edmund akabaki kitandani akimwangalia Angelina pale alipokuwa amesimama, naye akasimama na kumsogelea, akiwa nyuma yake, akamshika kiuno na kusogeza mdomo wake shingoni mwa nyuma na kumbusu.
“Kila siku unazidi kuwa mzuri mpenzi,” alimwambia huku akiwa nyuma yake.
“Na wewe pia mpenzi! Kila siku moyo wangu unazidi kukupenda, nadhani wewe ni mwanaume sahihi kwangu,” alisema Angelina.
“Unadhani! Huna uhakika?”
“Simaanishi hivyo!”
“Unachokimaanisha wewe ni kipi?”
“Wanaume si wa kuwaamini sana!”
“Na wanawake?”
“Hahah! Kwa hiyo unataka kusemaje?” aliuliza Angelina na kugeuka, wakaanza kuangaliana, kila mmoja alikuwa akitabasamu.
“Kwamba sisi tuaminiane, tupendane na tuheshimiane,” alimwambia.
“Hilo lipo sawa. Unaahidi kufanya hayo yote?”
“Nakuahidi!”
“Nashukuru!”
Wakati huo Angelina alikuwa kidato cha tano, aliendelea kusoma kwa bidii huku akitamani sana kutimiza ndoto yake ya kuwa daktari wa misuli, aliamini kwenye kusoma, japokuwa aliendekeza mapenzi lakini bado ndoto yake ilikuwa ni kuwa daktari mkubwa.
Huo mwaka ukaisha na kuingia mwaka mwingine. Wakati huo Edmund alimaliza shule na hatimaye kufaulu vizuri na kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa ajili ya kusomea masomo yake ya biashara.
Aliendelea kuwasiliana na mpenzi wake, Angelina, kila siku ilikuwa ni lazima kuzungumza kwenye simu na wakati mwingine kuonana na kuongea mengi.
Chuoni hapo Edmund alikuwa msumali kwa wanawake wengi, kila mtu aliyekuwa akimwangalia, alimpenda, alikuwa na sura nzuri lakini kubwa zaidi alitoka kwenye familia iliyokuwa na pesa.
Alipenda sana wanawake lakini baada ya kuficha chuoni, akapunguza mambo ya wanawake kwa sababu alisikia tu kulikuwa na taasisi nyingi za UKIMWI zilizokuwa zikiwasomesha wanafunzi wao huko, wanafunzi walionona, waliovutia lakini waliathirika.
Hakutaka kuathirika, mawazo yake yalikuwa finyu kama ya watu wengine kwamba ukiathirika basi ndoto zako zote zimepotea, hivyo hakutaka kabisa kujihusisha na mwanamke yeyote yule.
Alikuwa mkimya lakini wanawake hawakuchoka kummendea, kila siku walijigongagonga, na mwanamke aliyekuwa tayari kwa lolote lile alikuwa Esta, msichana kutoka nchini Iringa aliyefika jijini Dar kwa mara ya kwanza, na alipomuona Edmund tu, moyo wake ukapiga paa.
Wakati Esta akitoka huko Iringa aliwaambia wazazi wake katika maisha yake ya chuo asingethubutu kabisa kuwa kwenye uhusiano na mwanaume yeyote yule, asingetaka kufanya mapenzi tena na mtu yeyote mpaka siku ambayo angeolewa na kuwekwa ndani.
Hakuwa bikira, tayari alitolewa na baada ya hapo alikutana kimwili na wanaume wengine wawili aliokuwa nao kwenye uhusiano kwa nyakati tofauti na alipoachana nao, akaamua kutulia, hakutaka tena mwanaume.
Esta alikuwa mwanamke fulani mweupe, mzuri aliyekuwa na lipsi pana, alikuwa na uzuri wa ajabu, kila alipokuwa akipita nao wanaume walikuwa wakimwangalia kwa matamanio, alivutia, alikuwa na ule mwili wa kuita ambao kwa rijali yeyote yule ilikuwa ni lazima kutokwa na udenda kwanza.
Esta hakugusika, alikuwa mkali, aliumizwa mapenzini na hakutaka kabisa kuwa na mpenzi mwingine, alijitahidi sana kujitunza kwa kila kitu kitu kilichomfanya kila siku kwenye maisha yake hapo chuoni kutamani kusoma sana.
Siku aliyomuona Edmund moyo wake ukapiga paa! Hakuamini kama angekutana na mwanaume mzuri kama alivyokuwa huyo, alitamani kuzungumza naye na kitu kizuri kwake ni kwamba wote walikuwa wakisomea Biashara.

Je, nini kitaendelea?

Kwa wanaotaka kusoma simulizi zangu BURE Whatsapp wabonyeze hiyo link, waingie moja kwa moja kundini

 
Sehemu ya 16.

Ni majira ya saa mbili usiku, watu wengi hasa kwa nchi za Ulaya walikuwa wamejifungia ndani kutokana na baridi kali lililokuwa likipiga. Wale waliokuwa na kazi zao, walifanya kwa haraka zaidi ili wawahi majumbani kwao.
Theluji ilikuwa ikidondoka kama kawaida, kila mtu alikuwa akiichukia hali hiyo, iliwatesa wengi na ndiyo maana wengi wao walitamani mno kipindi cha joto kwani kilikuwa kipindi kizuri kuliko vyote, ndicho kipindi ambacho shule na vyuo vilifungwa na wafanyakazi wengi kuomba likizo.
Muda huo Amon na Gideon walikuwa chumbani kwao, walikuwa wakilala wawili tu, muda mwingi walikuwa wakipiga stori na kukumbushiana yale yaliyokuwa yametokea kipindi cha nyuma, walipokuwa na maisha yao nchini Tanzania.
Mbali na hayo yote walikuwa wakizungumzia ndoto zao, mambo ambayo wangekwenda kuyafanya mbele ya safari. Walikuwa na safari kubwa mno, walitakiwa kupambana kuhakikisha wanafanikiwa na kufika pale walipotakiwa kufika.
Kila mmoja mawazo yake yalikuwa mpirani, walitamani mno kufanya zaidi ya kile walichokuwa wamekifanya kwa kuwa kila mmoja aliwaamini, na kamwe hawakutaka kuwaangusha.
Wakati wakiendelea kupiga stori, mara simu ya Amon ikaanza kuita, haraka sana akaichukua kutoka kwenye kimeza kidogo chumbani humo na kuangalia kioo, jina la Anita lilikuwa likionekana. Haraka sana akaipokea.
“Nimezungumza na kocha, nataka mjiandae, dereva atawaleta nilipo. Nataka kuzungumza nanyi,” alisema Anita baada ya salamu na kukata simu.
“Nani?” aliuliza Gideon.
“Anita!”
“Anasemaje?”
“Anataka twende tukamuone sehemu!”
“Wapi?”
“Sijajua! Ila amesema dereva atakuja kutuchukua,” alijibu.
Walichokifanya kilikuwa ni kujiandaa tu, ilikuwa ni lazima waende huko walipoitwa, hawakujua waliitiwa nini lakini walijua hapakuwa na habari mbaya hata kidogo.
Kilikuwa ni kipindi cha likizo lakini hawakutaka kurudi nchini Tanzania, walitaka kuendelea kukaa huko huku miili yao ikiendelea kuizoea hali ya hapo Ujerumani. Huo ulikuwa uamuzi mzuri sana kwa kiasi kikubwa uliwasaidia mno.
Baada ya dakika kadhaa, wakafuatwa na kuambiwa kulikuwa na gari lililokuja kuwachukua hivyo walitakiwa kujiandaa na kuondoka. Wakafanya hivyo, wakaingia ndani ya gari na safari kuanza.
Ni ndani ya dakika chache walikuwa ndani ya mgahawa mmoja mkubwa kabisa uliokuwa katikati ya Jiji la Berlin, mbele yao alikuwepo Anita aliyekuwa akiwaangalia huku akionekana kuwa na mawazo fulani kichwani mwake.
Kila mmoja alihisi kabisa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, walitaka kujua hasa kilikuwa ni kitu gani. Waliongea naye kwa dakika chache na kuwapa simu ambayo ilionekana habari moja, ilikuwa na picha ya wachezaji wawili, waliwafahamu kabisa, alikuwa Gerd na mwenzake Nerd. Habari ile iliandikwa Kijerumani.
“Sijajua hiyo picha inamaanisha nini!” alisema Amon.
“Hao walikuwa wachezaji wetu!” alijibu.
“Walikuwa wachezaji wetu! Kivipi? Mbona bado wanacheza kwetu?” aliuliza Gideon.
“Walikuwa! Sasa hivi si wetu! Wameomba kuondoka, nimewaruhusu kufanya hivyo!” alijibu Anita kwa sauti ya upole.
“Kwa nini umewaruhusu wachezaji wazuri kuondoka? Itakuwaje sasa?” aliuliza Amon.
“Mnajiamini?”
“Kujiamini kivipi?”
“Nimewaruhusu watu hawa kuondoka kwa ajili yetu!”
“Kwa ajili yetu?”
“Ndiyo! Waliomba kuondoka baada ya ujio wenu, nikawa sina jinsi, nikawaruhusu!” aliwaambia.
“Kwa sababu gani?”
“Kwa sababu ninawaamini nyie ni bora zaidi ya hawa watu,” alijibu. Vijana hao wakaangaliana.
“Nisikilizeni! Kwenye biashara yoyote ile kuna kucheza kamari kutokana na maamuzi yako utakayoyafanya. Kwenye biashara hii ya mpira wa miguu nimecheza kamari kwa kuwaamini nyie. Hapa kuna moja kati ya mawili, mniangushe na kujutia maamuzi yangu ama mniinue na kuona nilifanya maamuzi sahihi,” aliwaambia huku akiwaangalia, watu hao wakaangaliana.
Kwao iliwashangaza sana, hawakuamini kama wanaume wale waliomba kuondoka kwa ajili yao, walijiona kuwa wachezaji wa kawaida lakini kwa kitendo kile kiliwaonyesha kwamba hawakuwa wa kawaida hata kidogo.
Walimwangalia Anita, mpaka kuchukua uamuzi wa kuwaruhusu wachezaji wale kuondoka na wakati walikuwa tegemeo kubwa kwenye timu hiyo ilimaanisha aliwaamini kwa asilimia mia moja kwamba wangefanya mambo makubwa.
Walikuwa na mtihani mkubwa na mzito mbele yao, ilikuwa ni lazima wafanye kila liwezekanalo kuhakikisha wanafanya kilichokuwa bora kabisa, Anita asijutie maamuzi yao na viongozi wa timu hiyo kumwamini kwa asilimia mia moja.
“Ninakuahidi nitafanya vizuri mpaka utashangaa,” alisema Amon huku akimwangalia Anita.
“Na Gideon?”
“Ninakuahidi kufanya vizuri zaidi, hakika hutojuta,” alisema Gideon.
Moyo wa Anita ukafurahi, hatimaye tabasamu pana likaonekana usoni mwake, alichokifanya ni kumpigia simu kocha wa timu ya wakubwa ambaye siku hiyo aliondoka kurejea nchini kwake Ubelgiji na kumwambia kila kitu kilikamilika na hivyo alitakiwa kuwaanzisha vijana hao mbele.
Hilo halikuwa tatizo. Amon na Gideon wakatambulishwa kwa waandishi wa habari kwamba walikuwa ni wachezaji wapya wa timu ya wakubwa ya Hertha Berlin.
Kila shabiki aliyesikia hivyo alikasirika, aliwaangalia wachezaji hao kwa jinsi walivyokuwa, hawakuwa na maumbo makubwa, kwa jinsi walivyoonekana tu hawakuwa na uwezo wowote ule.
Haraka sana watu wakakimbilia kwenye mtandao wa Youtube, walitaka kuwaangalia huko, waliyaona mambo yao, jinsi walivyokuwa wakali lakini bado hawakuamini kama wangeweza kuleta mabadiliko na kuifanya timu hiyo kuwa bora.
“Yaani unawatoa akina Nerd kwa ajili ya hawa wapuuzi!” alisema jamaa mmoja, alikuwa shabiki kweli wa Hertha Berlin.
“Hata mimi nashangaa! Hii timu ya kipuuzi sana,” alisema jamaa mwingine.
Japokuwa kulikuwa na maneno mengi mitaani wachezaji hao hawakutaka kuzungumza lolote lile. Kila siku kazi yao ilikuwa ni kuamka asubuhi na mapema na kwenda mazoezini.
Yalikuwa ni mateso makubwa. Asubuhi kulikuwa na usingizi mzuri na mtamu lakini walitakiwa kuachana nao na kwenda mazoezini huku kila mmoja akiamini hiyo ilikuwa nafasi yao ya kufanya vizuri.
Siku ziliendelea kukatika, Amon aliendelea kuonana na Jeniffer na kulifanya penzi lao kuanza kukomaa, walizoeana na muda mwingi walikuwa pamoja, wakifanya mambo mengi pamoja.
Baada ya miezi miwili, hatimaye wachezaji wakarudi kwa ajili ya kujiandaa na ligi ambayo ilitakiwa kuanza katikati ya mwezi wa nane.

Je, nini kitaendelea?
Tukumbuke simulizi hii inaendelea kupatikana WhatsApp kwa namba 0718069269 kwa gharama nafuu. Kwa wasiokuwa na hela, tuendelee kuisoma hapahapa mpaka mwisho japo itakuwa ikienda taratibu sana
 
Sehemu ya 17.

Wachezaji wa timu ya wakubwa walipokuwa wakiwaangalia Amon na Gideon hawakuona kama wangekuwa msaada mkubwa kama walivyokuwa akina Nerd, walitakiwa kupambana zaidi mpaka kufika pale walipofika wenzao.
Baada ya kufanya mazoezi kwa wiki moja, hatimaye wakasafiri na kuelekea nchini Ufaransa kwa ajili ya kucheza baadhi ya mechi kama njia mojawapo ya kujiweka fiti.
Huko walitakiwa kucheza mechi nne na timu za Ufaransa. Hilo halikuwa tatizo, walicheza mechi ya kwanza, wakaonekana kuwa wachezaji wa kawaida, wakacheza mechi ya pili mpaka mechi ya tatu lakini kwa bahati mbaya hapakuwa na makali yoyote yale waliyokuwa wameonyesha. Ikabaki mechi moja dhidi ya Lyon.
Hilo likawahuzunisha, kwa mechi tatu zote hawakuwa wamefanya lolote lile la maana, walionekana kuwa wazito, walikosa maamuzi ya haraka, yaani kwa jinsi walivyokuwa wakicheza walionekana kabisa kuwa na kitete.
Timu nzima ikaingia kwenye majonzi, kila mmoja alikuwa na huzuni kubwa, wakaanza kuwakumbuka akina Nerd ambao kama kawaida yao huko walipokuwa walikuwa wakionyesha mambo makubwa na kuwa msaada kwa timu zao.
Mashabiki wa Hertha Berlin wakazidi kuchukia, waliwachukia Amon na Gideon na mbaya zaidi wakaanza kuwafanyia ubaguzi wa rangi kwenye mitandao mbalimbali lakini hawakutaka kujali.
Walikaa kwa siku kadhaa Ufaransa na baada ya hapo walitakiwa kujiandaa na mechi ya mwisho dhidi ya Lyon. Mashabiki nchini Ujerumani walikataa kuiangalia timu hiyo, ilianza kupoteza mvuto taratibu na wengine kuona ni afadhali kuendelea na majukumu yao ya kila siku.
Japokuwa walikuwa wakipitia hayo yote lakini Anita hakutaka kuwakimbia, aliendelea kuamini vijana hao wangekuwa tegemeo la timu hiyo, aliamini kulikuwa na vitu vichache walivikosa na bahati mbaya zaidi kocha wao hakuwa navyo.
Wengi walimpigia simu na kumuuliza sababu iliyomfanya kuwaachia akina Nerd na kuwaingiza vijana hao lakini alichowaambia ni kwamba aliamini wangefanya vizuri kabisa, na kila mtu angetamani hata kuwa wachezaji wao.
“Tatizo wewe Anita mbishi sana,” alisema mwandishi mmoja aliyekuwa akiwasiliana sana na Anita.
“Labda tunatakiwa kuwapa muda,” alisema Anita.
“Unaamini kabisa kama watafanya vizuri? Wamecheza mechi tatu, wamepiga pasi kumi na mbili kila mmoja, unahisi hawa ni suluhisho sahihi?” aliuliza mwandishi huyo.
“Nadhani! Naomba tuwape muda.”
Japokuwa walikuwa wakifanya vibaya lakini Anita alimwambia kocha ilikuwa ni lazima kuwapanga kwani aliamini wangefanya mambo mengi makubwa na kila mtu angevutiwa nayo.
Walifanya vibaya lakini wao wenyewe walishindwa kuelewa ni kitu gani hasa kilichokuwa kikiendelea, walikuwa na uwezo mkubwa, sasa kwa nini uwezo huo haukuwa ukionekana?
Wakazidi kudharauliwa mpaka siku ya mechi dhidi ya Lyon kufika, timu iliyokuwa ikiongozwa na kocha wa Uholanzi, Thadeo Robben. Mechi ilianza kwa kasi kubwa, Amon na Gideon walijitahidi kufanya kila liwezekanalo kuonyesha ubora wao lakini ilishindikana kabisa.
Watu walichukia, timu nzima ilitamani hata kuwatoa lakini kila walipomfikiria Anita, jinsi alivyokuwa akiwaamini, waliona kungekuwa na tatizo kubwa, hivyo wakaamua kuwavumilia.
Mechi ilipomalizika, Hertha Berlin ilifungwa kwa mabao manne kwa sifuri, kocha wa Lyon, Robben akawafuata wachezaji hao kwa lengo la kuzungumza nao.
Alikwenda nao mbali kabisa, karibu na kibendera cha kona na kuanza kuzungumza nao, hapakuwa na mtu aliyekuwa akisikia alichokuwa akiwaambia, kilikuwa kitendo kigeni sana lakini hakuwa na jinsi.
“Mmetoka wapi?” aliwauliza.
“Tanzania!”
“Mlikwenda Ujerumani kufanya nini?”
“Kucheza mpira!”
“Mbona hamuonyeshi? Nasikia kuna wachezaji wazuri wameuzwa kwa ajili yenu, mbona hamtaki kuwaonyesha watu kwamba nyie ni wazuri zaidi ya hao waliouzwa? Mnapewa pasi, mnapoteza kizembe, hamtoi pasi za uhakika, na hata kufunga hamuwezi. Hivi kweli mnatamani kurudi Afrika kwenda kucheza kwenye viwanja vya hovyo?” aliwauliza huku akiwaangalia.
“Hapana!”
“Mnataka kurudi Afrika kuendelea kula chakula cha kugombania?”
“Hapana!”
“Mnataka kurudi Afrika muendelee kula chakula kimoja kwa siku?”
“Hapana!”
“Kama hamtaki hayo yote, mbona hamuonyeshi chochote kile? Onyesheni uwezo wenu. Mimi nataka muonyeshe, muwe wachezaji wazuri. Kuna vitu nimeviona kwenye miguuni yenu ila hamjiamini kabisa. Hebu jiaminini, mpira unachezwa na binadamu wenye miguu miwili kama nyie, sasa mbona hamtaki kuonyesha. Hebu onyesheni!” alisema Robben.
“Tutajitahidi!”
“Sio mtajitahidi! Semeni mtaonyesha!”
“Tutaonyesha!”
“Sawa. Nawatakia siku njema, kila mmoja aondoke huku akijua yeye ni mchezaji bora kabisa,” alisema Robben, alipomaliza akaanza kuondoka na vijana hao.
Kila mmoja alikuwa akiwaangalia, hawakujua waliambiwa nini lakini kwa jinsi Robben alivyokuwa akionekana ni kama mtu aliyekuwa akiwashauri jambo fulani.
Wakaungana na wenzao na kuondoka, siku hiyo walionekana kuwa wapole mno, kitu pekee walichokigundua ni kwamba hawakuwa wakijiamini kabisa. Huo ulikuwa ukweli, walitakiwa kujua kila mtu waliyekuwa wakicheza naye alikuwa binadamu, walitakiwa kujiamini kwa asilimia mia moja.
“Tujiamini!” alisema Gideon huku akimwangalia Amon.
“Kabisa yaani! Sijui tunatetemekea nini! Yaani mpaka nashangaa!” alisema Amon, muda huo walikuwa ndani ya ndege, walipofika, wakapewa siku mbili tu za mapumziko, baada ya hapo, wakarudi mazoezini tayari kwa kuanza mazoezi ya mwisho kwa ajili ya mechi ya kwanza ya ligi kuu ya Ujerumani ambayo walitakiwa kupambana na timu iitwayo Schalke 04 uwanja wa nyumbani.

Je, nini kitaendelea?
Tukumbuke simulizi hii inaendelea kupatikana WhatsApp kwa namba 0718069269 kwa gharama nafuu. Kwa wasiokuwa na hela, tuendelee kuisoma hapahapa mpaka mwisho japo itakuwa ikienda taratibu sana.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom