THE SPIRIT THINKER
JF-Expert Member
- Sep 9, 2019
- 419
- 654
Ukipachika naomba nijulishwe.
Mic u alot yaaaniAsante Nyemo
Jamani leo moja tu🧐Nyemo Chilongani
Ulimwengu Ndotoni Mwangu
0718069269
Sehemu ya 30.
Glory akaanza kumwambia Jeniffer kila kitu alichokuwa amezungumza na mwanaume huyo, kuhusu namna alivyoondoka zake kuelekea Marekani kwa kuwa wazazi walitaka kumuoa msichana mwingine.
Alivyofika huko, akaanza kuishi naye kwenye uhusiano, alimpenda lakini baada ya muda fulani akahisi kabisa hakuwa msichana wake sahihi kwa kuwa hakuwa akiyapata yale yote aliyoyapata kutoka kwake.
Akatafuta njia ya kumuacha, ilikuwa vigumu kwa sababu wazazi wake walikuwa sehemu ya uhusiano huo, aliteseka mno lakini mwisho wa siku akaamua kusimama kama mwanaume na hivyo kuamua kumuacha kinguvu.
Baada ya hapo ndipo akaanza kuwakumbuka watu aliowahi kuwa nao kwenye uhusiano, kwa wote hao, mtu sahihi aliyekuja kwake alikuwa huyo Jeniffer na ndiyo maana leo alikuwa nchini Ujerumani kwa lengo la kuonana naye, azungumze naye na kuwa kama zamani.
“Kwa sasa haiwezekani kabisa,” alisema Jeniffer huku akimwangalia Glory.
“Jeniffer! Nimezungumza na Dawson, yaani anaonyesha kabisa kujutia alichokifanya, yaani ungeonana naye ungeligundua hilo. Naomba umsamehe!” alisema Glory.
“Nimekwishamsamehe!”
“Kwa hiyo upo tayari kurudiana naye?”
“Hapana!”
“Hata kuonana naye?”
“Ndiyo! Sipo tayari!” alimwambia.
Glory aliumia sana, hakujua kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia, kubwa zaidi alianza kumuona rafiki yake akiwa anazingua, mtu kama Dawson, mwanaume ambaye mwisho wa siku aliamua kurudi na kuomba msamaha, alitakiwa kusamehewa kwa kuwa angebadilika na kuwa mtu mwema.
Msimamo wa Jeniffer haukubadilika, ulikuwa uleule kwamba hakutaka kurudiana naye. Moyoni mwake alikuwa na amani, furaha kwa kuwa alikuwa na mtu aliyempenda kwa mapenzi ya dhati na kubwa zaidi alikuwa na mimba yake.
Glory hakuwa na jinsi, akamtafuta Dawson, wakaonana na kumwambia kile kilichotokea kwamba Jeniffer alikataa katakata kurudiana naye kwani alikuwa na maisha yake mengine kabisa.
“Kwani ana mtu?” alimuuliza.
“Sidhani! Endapo angekuwa na mtu angeniambia tu!”
“Sasa tatizo nini? Au hukumwambia kwamba nimetubu na sitorudia tena kufanya ule upumbavu?”
“Vyote nilimwambia!”
“Sasa kwa nini amekataa?”
“Nadhani ni msimamo wake. Ila si unajua watoto wa kike, jaribu kuonana naye, nadhani atakubali. Ngoja nikuelekeze anapoishi kwa sasa,” alisema Glory, na bila shaka akaanza kumuelekeza mwanaume huyo alipokuwa akiishi Jeniffer.
Dawson hakutaka kushindwa, aliamini huyo Jeniffer ndiye alikuwa msichana wa ndoto zake, hata kama hakuwa akitaka kwa wakati huo aliamini ingetokea siku moja angekubali kuonana naye na kurudiana.
Alitakiwa kupambana kama mwanaume, hakuwa radhi kuona Jeniffer akiolewa na mwanaume mwingine zaidi yake, ilikuwa ni lazima kupambana kiume na mwisho wa siku ampate na kumuweka kwenye himaya yake kama kawaida.
Akaanza kumtafuta kivyakevyake kwa kwenda katika nyumba aliyokuwa akiishi, ilikuwa moja ya nyumba kubwa na ilikuwa kwenye mtaa wa kitajiri. Kwa Dawson hakutaka kuwa na hofu juu ya hilo kwani msichana huyo alitoka kwenye familia ya kitajiri mno.
Baada ya dakika kadhaa kulisimamisha gari mbali kidogo na nyumba hiyo, akaliona gari la Jeniffer likiingia ndani ya himaya la jengo hilo, haraka sana akateremka akiwa na maua mkononi, hata kabla ya geti kujifunga, akaingia na kuanza kulifuata gari la msichana huyo ambalo tayari nalo liliingia nani ya nyumba hiyo huku mkononi mwake akiwa na maua kwa lengo la kumuomba msamaha.
Jeniffer hakutegemea kumuona mwanaume huyo mahali hao, alishtuka, akawa anamwangalia mara mbili mbili kama ni yule aliyekuwa akimfahamu ama alikuwa mtu mwingine. Dawson alimwangalia Jeniffer huku akiwa kwenye hali fulani ya kutaka kuonewa huruma, hapohapo akaanza kumsogelea huku akiwa na maua yake kwa lengo la kumuomba msamaha.
Kitu cha kwanza kabisa kukifanya kilikuwa ni kupiga magoti mbele yake huku akimnyooshea mkono uliokuwa na maua kwa lengo la kuyachukua na kumsamehe kwa kila kitu alichokifanya miaka ya nyuma. Alimsamehe mwanaume huyo kitambo sana lakini kitu ambacho hakutaka kabisa kukiona ni kurudi kwenye uhusiano ambao alijiahidi asingeweza tena.
Kama kuhuzunika, alihuzunika sana, kama kulia alilia sana, hivyo vyote vilitosha na kitu alichokihitaji kwa nguvu zote kilikuwa ni mapenzi, furaha na amani, vyote hivyo alivipata kwa Amon, hakuona kama kulikuwa na uhitaji mwingine wa kutaka vitu hivyo kutoka kwa mtu mwingine.
“Naomba unisamehe Jeniffer, nilikuumiza, nilikuwa mpumbavu sana kuwasikiliza wazazi wangu ambao waliniacha nikiteseka katika mtego mkubwa niliouingia,” alisema Dawson huku akimwangalia msichana huyo, Jeniffer alibaki akiwa amesimama, hakujua kitu cha kusema kwanza, alitaka kumsikiliza.
“Nilipata kila kitu kutoka kwako! Nilipoondolewa niliamini haya huko ambapo nilikwenda basi ningepata kila kitu kama ilivyokuwa kwako, niliteseka sana, niliiona dunia kuwa chungu, naomba unisamehe Jeniffer, dunia imenifundisha,” alisema Dawson huku akimwangalia Jeniffer.
“Dawson! Naomba usimame!” alisema Jeniffer huku akimuinua mwanaume huyo ambaye alisimama, wakaanza kuangalian usoni, wakati huo Dawson alikuwa akilengwa na machozi ambayo baada ya sekunde chache tu yakaanza kutiririka.
“Nilikusamehe zamani sana!” alimwambia huku akimshika mkono.
“Najua ni wazazi wako ndiyo waliamua hivyo, ulikuwa ukinipenda sana, tulikuwa na ndoto pamoja lakini wazazi wako wakaingilia, wakanipokonya wewe kutoka mikononi mwangu, hakika niliumia sana, nililia usiku na mchana,” alisema Jeniffer na kunyamaza kwanza, yale yaliyotokea kipindi cha nyuma yakaanza kujirudia kichwani mwake.
“Naomba unisamehe sana kwa kukuumiza,” alimwambia.
“Nilikusamehe tangu zamani, nisingekuwa nimekusamehe sidhani kama ningeendelea kusimama hapa nilipokuwa,” alimwambia huku akimwangalia.
“Nashukuru sana! Nakuhitaji Jeniffer, ninakuhitaji sana maishani mwangu!”
“Najua unanihitaji! Ila sina tena nafasi ya kukuingiza moyoni mwangu!” alimwambia.
“Kwa sababu gani?”
“Kuna mtu ambaye tayari ameingia kwenye ule moyo uliouacha! Naomba unisamehe kwa hilo. Tubaki tu kuwa marafiki, tushauriane kwenye mambo mengine kama hutojali,” alisema Jeniffer huku akimwangalia.
Kulikuwa na maneno mengi sana aliyowahi kuambiwa maishani mwake ambayo yalimuumiza mno lakini kwa yale aliyokuwa akiambiwa kipindi hicho, hakika yalimuumiza kuliko maneno yote aliyowahi kuambiwa.
Alimwangalia Jeniffer, msichana huyo alikuwa mrembo hasa, alimpenda na alitamani sana kuwa naye lakini alimwambia ilishindikana kwa sababu tayari alikuwa na mwanaume mwingine. Hakutaka kuona hilo likitokea, alitamani kuwa na Jeniffer tu, hakutaka kusikia kitu chochote kuhusu huyo mwanaume mwingine.
Alinyamaza! Aliangalia chini, machozi yakaanza kumtoka, ya sasa hivi hayakuwa ya kutaka kuonewa huruma bali yalikuwa machozi yaliyokuwa na maumivu makali moyoni mwake. Alitamani hata muda urudi nyuma, kipindi kile alichokuwa na msichana huyo na kuwakatalia wazazi wake lakini hakuweza kufanya hivyo.
“Jeniffer!”
“Dawson! Nashukuru sana kwa kipindi chote nilichokuwanacho, hakika ulikuwa mwanaume mwema sana kwangu, ulinifundisha maisha, namna ya kujiamini na pia ukanifundisha kuhusu mapenzi!” alimwambia.
“Jeniffer!”
“Sitoweza kuwa nawe! Naomba unielewe kwa hilo,” alisema Jeniffer, naye sura yake aliiweka kwenye hali ya huzuni kwa kutaka kueleweka kwa kile alichokuwa amekisema.
Dawson akanyamaza kwanza, yaani alihisi kama alikuwa akiota, kile alichoambiwa hakikumuingia kabisa kichwani mwake. Akahisi kabisa Jeniffer alikuwa na mtu mwingine, hakuwa yeye, sasa alikuwa nani?
Alimuuliza maswali ya kutaka kumfahamu mtu huyo lakini Jeniffer hakuwa radhi kumwambia kwa kipindi hicho, hakutaka kwanza dunia ijue kama alikuwa kwenye uhusiano na Amon mpaka pale ambapo aliamini muda ungefika na kumwacha kila mtu afahamu.
Dawson aliomba sana lakini hakukubaliwa hivyo kuondoka zake. Njiani alikuwa na majonzi yake lakini upande mmoja wa moyo ulimkumbusha kwamba Jeniffer alikuwa mwanamke, siku zote wanawake walikuwa watu wa huruma, ulipomuomba kitu, mara ya kwanza alikukazia lakini baada ya kumsumbua zaidi na zaidi, alikubali na hivyo kukipata kwa urahisi kabisa.
Alipokuwa ndani ya gari akaona ni jambo jema kumpigia simu Glory kwa lengo la kuzungumza naye na kumwambia kilichotokea. Haraka sana akafanya hivyo na simu kuanza kuita, iliita kwa sekunde kama kumi, hatimaye ikapokewa na sauti ya msichana huyo kuanza kusikika kutoka upande wa pili.
“Ndiyo nimetoka kwa Jeniffer!” alimwambia.
“Imekuwaje tena?”
“Amenikataa!”
“Amekukataa? Kwa sababu gani?”
“Basi tu, labda kwa yale yaliyotokea, anahisi nitafanya vile tena,” alimwambia.
“Mh!”
“Hivi una uhakika Jeniffer hana mtu?”
“Hana! Kama angekuwa na mtu ningejua tu!”
“Sasa kwa nini anikatae?”
“Ndiyo wanawake tulivyo! Wewe endelea tu kumbembeleza, nina uhakika atakubali tu,” alisema Glory.
“Nashukuru sana kwa msaada wako. Nitafanya hivyo!” alimwambia.
“Sawa.”
Akakata simu na kukubaliana na Glory kwamba angeendelea kumfuatilia msichana huyo, awe anawasiliana naye kwenye simu mara kwa mara kwani alihisi hilo lingemsaidia kwa kiasi kikubwa. Alichukua dakika kadhaa, hatimaye akafika katika nyumba aliyokuwa amechukua kwa muda na kujipumzisha ndani. Sasa mawazo juu ya Jeniffer yakaanza kumsumbua, akaanza kupanga mikakati yake mipya.
Je, nini kitaendelea?
Kumbuka simulizi yangu ya kipelelezi na uchawi ndani yake inaendelea kupatikana kwa sh. 5000 Whatsapp, inaitwa Medusa: Malkia wa Damu.
Inamuhusu msichana Zulfa, aliolewa na tajiri kutoka Kisiwani Mafia. Wakiwa fungate huko Zenji, anamtoroka usiku, anahamisha 100M kwa akaunti yake. Kosa alilolifanya, alichukua kila kitu chake, akasahau chupi.
Yaap! Chupi. Mumewe, mzee Hussein akaichukua na kwenda Mafia, akaloga kupitia chupi hiyo. Kilichotokea, Zulfa akaanza kupata matatizo, anaota ndoto mbaya na za kutisha, akishtuka, ana muhemko wa kufanya mapenzi, akinchukua mwanaume na kwenda naye hotel, jini linatoka ndani yake na kumuua mwanaume huyo.
Ameua watu wengi...sasa kesi inafika mezani kwa mpelelezi Ashrafu Maganza, anaanza kufuatilia hayo mauaji. Ni hadithi nzuri na inasomeka. Njoo Whatsapp kwa namba 0718069269.