Simulizi: Roho yake inadai

*ROHO YAKE INADAI --- 34*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Muda kidogo, yule polisi aliyekuwa amekaa dirishani akimtazama mwenzake, akamwona mtu fulani akiwa anakuja kumjongea mwenziwe na wale watoto. Alimtazama mtu huyo lakini hakuweza kumtambua. Mtu huyo alikuwa akiambatana na mtoto mwingine kwa pembeni yake.
.
.
Akajaribu kumshtua mwenzake, “Tazama nyuma yako! Hey! Tazama!”
.
.
ENDELEA
.
.
Mwenzake huyo alipotazama, kabla hajajitetea na bunduki yake, akanyakwa koo na kunyanyulia juu haswa kisha akaminywa kwanguvu mpaka koo lake kuanza kuchuruza damu. Bunduki ambayo huenda ingemsaidia kutetea uhai wake, ikadondokea chini.
.
.
“Hapana! Hapana!” mwenzake akatahamaki pale dirishani. Upesi akatoka kwenda kumsaidia mwenzake abaki na pumzi. Alipofungua mlango, akamnyooshea mtu yule bunduki na kumfyatulia tatu. Ajabu hazikusaidia. Zaidi yule mtu wa ajabu akamtupia mwenzake chini na kumfuata yeye kwa kasi!
.
.
Naye akamyaka shingo na kumnyanyua juu, akamminya koo na kumpasua, kisha akalichanja na kumfanya avuje damu kama sharubati toka kwenye kopo. Polisi huyo akapoteza uhai. Dubwana hilo likamtupa na kisha likapotea zake!
.
.
Baadhi ya watu wakafungua milango na madirisha kutazama. Milio ya risasi iliwaamsha na kuwapa mashaka. Wakaona maiti mbili za polisi na wale watoto wakiwa wanatembea. Kwakuwa hali ilikuwa shwari, wakatoka kwenda kutazama.
.
.
Waliwaokoa wale watoto na pia wakatoa taarifa polisi wakidhani polisi wameuawa na majambazi baada ya kurushiana risasi.
.
.
Muda mfupi, polisi wengine wakaja na kuanza kuipemua miili na kukusanya taarifa toka kwa washuhudiaji. Hawakuelewa jambo. Hakuna aliyesema amewaona hao watu waliokuwa wanapambana na polisi, lakini pia vilevile hakuna aliyetoa maelezo ya kueleweka juu ya watoto wale mapacha waliokuwa wanatembea wenyewe usiku huo.
.
.
Wakiwa kwenye mahangaiko ya kutafuta taarifa sahihi, Mama Brian akatoka akiwa amejikunyata, amejifunika blanketi, akawaambia polisi, “Mimi najua nani waliyekuwa wanapambana naye.” kwa maelezo zaidi, polisi mmoja akaongozana na Mama Brian kwenda ndani kumhoji.
.
.
“ … Mtu huyo ndiye ambaye hupoteza watoto kila siku. Polisi hao walipotaka kuwaokoa watoto hao, ndipo akajiri na kuwamaliza,” Mama Brian akaeleza. Polisi akamuuliza, “Unamjua yupoje na wapi anaishi?”
.
.
Mama Brian akanyamaza kwanza kisha akauliza, “Hata nikisema mtasadiki?”
.
.
“Usijali,” Polisi akamtoa hofu. “Unaweza tu kueleza.” basi Mama Brian akamweleza kinagaubaga ya kuwa mtu huyo ni Helo, Hernandez Lorenzo, wa miaka mingi iliyopita. Nyumba yake ipo msituni na anafanya kila anachofanya kwa ajili ya kulipiza kisasi kwa mji wa Boston.
.
.
Polisi akanakili maelezo yake yote, ila yakamletea shaka kwenye kuamini. Simulizi ile ilikuwa ni ya kufikirika zaidi kuliko uhalisia. Ni kwa namna gani mtu mfu akarejea na kufanya mauaji?
.
.
“Nashukuru sana.” Polisi akampatia mkono na kunyanyuka, “Naweza kwenda sasa. Au kuna cha ziada wataka kuniambia?”
.
.
Mama Brian akamjibu, “Ndio, kipo!”
.
.
“Niambie.” Polisi akasema akimpatia masikio yake kwa utulivu. Mama Brian akasema, “nendeni mkatazame kwenye korongo la kanisa …”
.
.
.
**
.
.
.
Gari la polisi lilisimama, wakashuka wanaume wawili waliovalia sare. Mmoja wao alikuwa ni yule Polisi aliyemhoji Mama Brian. Mkononi alikuwa amebebelea ngowe ya mawasiliano na bunduki ndogo. Mwenzake anayemfuatia alikuwa mikono mitupu ila viganja vyake vikiwa karibu na mkanda wake uliobebelea silaha.
.
.
Ndani ya muda mfupi, wakaonana na Padri Alfonso na Dada Magdalena, wakawafanyia mahojiano mafupi kabla ya kuwataka waongozane kwenda korongoni. Padri Alfonso akapata shaka, akauliza, “Afisa, kuna lolote lile?”
.
.
“Tunataka kupatazama!” Polisi akasema kwa amri basi Padri Alfonso na Dada Magdalena wakaongozana nao kwenda huko kwenye korongo. Walipofika, polisi hao wakangaza na kuangaza, hawakuona kitu.
.
.
“Mnaweza kutuambia mnatafuta nini ili tuwasaidie?” akauliza Padri Alfonso. Polisi akamwambia, “Usijali.” kisha wakajikokota zao kwenda kwenye usafiri wao na kutimka.
.
.
“Hamna kitu!” akasema Polisi dereva na kuongezea, “Nilijua tu mama yule atakuwa na matatizo.” wakayoyoma wakati Padri Alfonso na Dada Magdalena wakiwatazama. Walipoishilia, Padri Alfonso akauliza, “Watakuwa wameambiwa na nani kuhusu korongo lile?”
.
.
Dada Magdalena akajibu, “Si wengine bali wale waliokuja kulitembelea.” Basi Padri Alfonso akashusha pumzi ndefu na kusema, “Nadhani umefikia mwisho wao!” na mara katikati yao akasonga mtumishi mwingine. Naye alikuwa ni Dada kama yule Magdalena, akasimama kandokando yao na kuuliza, “Nami nafanyaje?”
.
.
Padri Alfonso akamtazama na kuweka mkono wake begani. Kumbe alikuwa Dada yule aliyekumbwa na kadhia na yule polisi wa mwanzoni wakiwa korongoni kuwafuata wakina Brian.
.
.
“Dada Marietta, wewe bado u mpya kabisa,” akasema Padri Alfonso. “Utafanya kazi pamoja na Dada Magdalena akuonyeshe namna ya kuenenda. Ila bila shaka usiku wa leo umekuwa mrefu sana, tuuache uende.”
.
.
Dada hao wakainamisha vichwa vyao, Padri akaenda zake.
.
.
**
.
.
Saa nane ya mchana …
.
.
Akiwa juu ya baiskeli yake, Brian alirusha macho yake huku na kule kuangazia kama kuna tangazo jipya la watoto waliopotea. Hakukuwapo, yote yalikuwa ya zamani. Mpaka anafika nyumbani hakuona tangazo lolote tofauti na yale aliyoyaona hapo kabla.
.
.
Akazama ndani na kuteta machache na Wisconsin juu ya mpango wao. Bwana huyo akamwambia kuwa siku hiyo wataenda kumtembelea Brewster majira ya usiku. Brian akauliza, “Haitakuwa hatari kutokana na yale yaliyotokea jana yake?”
.
.
Wisconsin akakuna kidevu chake na kumwambia Brian, “Hatuna muda, ni lazima tufanye hivyo. Kama tusipoyatembelea maeneo haya tukiwa na mwili wa nyama, basi itakuwia vigumu utakapoenda huko kiroho. Lazima ujue ni maeneo yapi utakayokatiza na kuyafanyia kazi.”
.
.
Basi japo kishingo upande, Brian akaridhia. Akala na kupumzika kidogo. Baadae kwenye majira ya jioni akajikwea kwenye baiskeli yake na kwenda kule kwenye makazi ya marehemu Dkt Hamill. Alipoingia, akaegesha baiskeli yake pembeni kidogo ya geti kisha akaanza kusonga kuendea jengo hilo.
.
.
Akiwa bado hajalifikia, akastaajabu kusikia sauti ya geti likifungwa. Akapata shaka. Haraka akakimbilia getini na kujaribu kulifungua. Halikufunguka. Akajaribu kwanguvu zote lakini bure, hakuweza kufungua. Akajiuliza nani kamfungia humo?
.
.
Akapigapiga geti kwanguvu akiita watu wamsaidie lakini hakuna mtu aliyemsikia wala kujali. Mpaka mikono ikawa inamuuma asifanikiwe kitu. Mara akasikia sauti nyuma yake ikimwambia, “Acha kujichosha, Brian.”
.
.
Haraka akatazama nani huyo amwongeleshaye, hamaki akamwona Brewster! Alikuwa amesimama mbele ya mlango wa jengo akiwa ameshikilia bakora ya kutembelea. Yu ndani ya suti nyeusi na kofia yake.
.
.
“ … tupo wawili tu humu, acha kusumbuka.” akamalizia na kisha akatabasamu. Brian akamuuliza, “Ni nini unataka kwangu?”
.
.
“Unajua nitakacho,” Brewster akamjibu kisha taratibu akaanza kusonga kumjongea. “Nilijitahidi sana kukuepusha na kifo, lakini …” akabinua mdomo wake. “ … hukutaka kusikia, Brian. Umekuwa mkaidi sana. Sasa mimi nifanye nini?”
.
.
Brian akamnyooshea mkono na kumwamuru, “Usinisogelee!” Brewster akaangua kicheko kisha akauliza, “Nikikusogelea, utanifanya nini, Brian?” Kabla Brian hajajibu, Brewster akiwa anatembea taratibu, akasema, “Leo ni mwisho wako. Hamna mtu wa kukusaidia, ni mimi na wewe tu … mimi na wewe, Brian.”
.
.
Brian akapiga kelele kuomba msaada. Brewster akacheka sana mpaka kushika mbavu zake. Akakohoa mara kadhaa na kusema, “Brian, acha kupoteza nguvu zako bure. Ni-me-ku-a-mbi-a …” wakati Brewster anaongea akawa anabadilika toka kwenye ubinadamu kwenda kwenye ushetani. “… u-po-na-mi-mi-tu! Ni we-we-na-mi-mi-tu!”
.
.
Uso wake ukageuka na kuwa wa mnyama. Mikono yake ikavimba na kuchomoza makucha vidoleni. Ulimi ukamtoka nje na meno yakapandana kwana kwamba tengo la miba! Miguuni akavalia kwato za ng’ombe.
.
.
Brian akaogopa sana. Akakimbia kuufuata ukuta na alipoenda mbali akajitahidi kuurukia ukuta atorokee kwa nje, lakini ukuta ulikuwa mrefu sana. Hata aliponyoosha mikono yake, hakufua dafu. Akajaribu na tena na tena. Mara mkono wake wa kuume ukafanikiwa kushika kingo ya ukuta. Akijitahidi kuunyoosha mkono wa pili, ule wa kushoto, udake ajivute, akashikwa na kuvutwa chini! Akadondoka na kulalama kwa maumivu.
.
.
Brewster akamdaka shingo na kumminya kwanguvu. Brian akaanza kutapatapa.
.
.
.
***
 
*ROHO YAKE INADAI --- 35*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Brian akaogopa sana. Akakimbia kuufuata ukuta na alipoenda mbali akajitahidi kuurukia ukuta atorokee kwa nje, lakini ukuta ulikuwa mrefu sana. Hata aliponyoosha mikono yake, hakufua dafu. Akajaribu na tena na tena. Mara mkono wake wa kuume ukafanikiwa kushika kingo ya ukuta. Akijitahidi kuunyoosha mkono wa pili, ule wa kushoto, udake ajivute, akashikwa na kuvutwa chini! Akadondoka na kulalama kwa maumivu.
.
.
Brewster akamdaka shingo na kumminya kwanguvu. Brian akaanza kutapatapa.
.
.
ENDELEA
.
.
“Nakumaliza, Brian!” akasema Brewster ambaye hakuwa binadamu tena bali mnyama. Brian akaendelea kutafuta pumzi yake na kupigania uhai wake pasipo mafanikio. Ni bahati wakati anatafuta la kufanya, akamkita Brewster kwenye sehemu zake za siri na kumsababishia maumivu makali!
.
.
Akamwacha Brian na kukimbizia mikono yake yote sehemu zake za siri, ndipo Brian akachoropoka na kukimbia haswa. Alikuwa anahema kana kwamba mbwa. Na baada ya muda mfupi akawa haonekani wapi amekimbilia.
.
.
Basi Brewster akiwa anagugumia sana kwa maumivu, akasimama, bado uso wake ukionyesha anahisi maumivu, akatazama huku na kule kumtafuta Brian. Macho yake yalikuwa mekundu yaliyojawa na hasira.

“Nitakuua, Brian!” akasema akiwa anakunja ngumi yake kwanguvu. Meno anayasaga.
.
.
Akanguruma kana kwamba simba kisha akaanza kumsaka Brian ndani ya eneo hilo akitumia pua yake kama nyenzo kuu. Akanusanusa na kusonga. Akanusa na kusonga. Akatazama kushoto na kulia. Akasonga.
.
.
Mwishowe akafika nyuma ya nyumba ambapo aliamini Brian atakuwa huko. Akaangaza macho, kheri akaona mlango ukiwa wazi. Akaamini alikuwa sahihi. Akasonga na kuzama ndani, bado akitumia pua yake kama dira.
.
.
Alipoendelea kunusa zaidi, akajikuta mbele ya kabati kubwa. Hapo akaguna kwa kebehi na kusema, “Unaweza kukimbia, Brian, ila si kujificha.”
.
.
Mara akaanza kufungua milango ya makabati kwa pupa na kutupia humo macho yake kutazama. Mlango wa kwanza, hakubahatika kuona kitu, wa pili nao wa tatu, hakukuwa na kitu zaidi ya nguo tu! Sasa mlango uliobakia, ule wa nne, akajua Brian yupo humo.
.
.
Basi akavuta pumzi kwanza, alafu puh! Akaufungua. Loh! Namo hakukuwa na kitu. Hajakaa vema, kabati likaanza kuinama. Akadhani pengine ni macho yake, kumbe lah! Kabati lilikuwa linadondoka.
.
.
Likamparamia na kumwangusha chini kama mbuyu. Brian akatoka kwa nyuma yake na kukimbia upesi kwenda ndani. Muda mfupi, hauonekana tena wapi alipoelekea.
.
.
Brewster aliyeachwa akiwa amevamiwa na kabati, akalalama sana kwa maumivu. Kana kwamba kabati lile ni bua, akalinyanyua na kulitupia kando kwa nguvu! Kabati likaparanganyika na kuwa vipisi vya mbao.
.
.
Uso wake ulikuwa unatoa damu na alikuwa pia amekasirika maradufu. Akapiga kelele kali na kunyanyuka kisha kwa pupa akaanza kumsaka Brian! Akanusa na kufuata harufu mpaka kufika chumba kimoja ambacho kilikuwa kimefungwa. Akabamiza mlango kwanguvu, ukavunjika kutengeneza tobo!
.
.
Akaubamiza tena na tena, mlango ukawa inyang’anyang’a, akazama ndani na kuangaza. Hakukuwa na mtu, chumba kilikuwa kitupu kabisa. Hakuamini macho yake, mbona amesikia harufu humo? Alipotazama vema, akagundua ya kuwa Brian alikuwa ametupia nguo yake humo.
.
.
Akaifuata na kuinyanyua kuipeleka puani. Akainusa. Ama kweli, alikuwa amedanganywa! Akasaga meno yake kwa hasira kisha akatoka humo chumbani.
.
.
.
**
.
.
“Tafadhali, kubali! Tafadhali! Tafadhali!” Brian alilalama akiwa anaibonda simu ya mezani kiganjani mwake. Alikuwa anataka kuwasiliana na polisi ama familia yake lakini simu hiyo ilimsumbua. Kila alipotia namba, ikakata. Kila alipotia namba …
.
.
“Shabash!” akalaani. Akiwa yu kifua wazi, mjawa na hofu, akawaza nini cha kufanya. Hakuwa anajua sasa. Endapo Brewster angelitokea hapo basi angemmaliza mara moja.
.
.
Akatazama kushoto na kulia. Makabati hayakuwa sehemu salama ya yeye kujificha. Na hata kitanda kilichokuwamo humo ndani hakikuwa na uvungu.
.
.
Akiwa anawaza vivyo, mara akaona simu ile ya mezani ikiwa inawaka taa. Taa ndogo nyekundu ambayo ilikuwa imepachikwa kwenye kitako chake. Basi haraka Brian akapata moyo. Upesi akaikwapua simu hiyo na kuibandika sikioni, akapiga polisi.
.
.
Simu ikaita mara mbili, mara ikapokelewa na sauti ya kike.
.
.
“Unaongea na idara ya Polisi, Boston. Una dharura yoyote?”
.
.
Kabla Brian hajafungua mdomo, mlango ukabamizwa kwanguvu na kupasuka! Kutazama akamwona Brewster, macho kwa macho. Akiwa amejawa woga, akapayuka simuni kuwa anahitaji msaada kuna mtu anataka kumuua.
.
.
“Upo wapi? Tupe anwani yako tafadhali!” sauti ile ya kike ikanguruma. Brian kufungua mdomo wake, Brewster akawa tayari ameshamfikia. Akamnyonga shingo yake kwanguvu!
.
.
Bado Brian alikuwa ameshikilia simu mkononi. Brewster alikuwa anamtazama kwa hasira na hamu ya kumfundisha adabu. Kutetea uhai wake, Brian akambamiza Brewster usoni kwa kutumia simu ile ya mkononi.
.
.
Simu ikavunjika na kumwacha Brewster bado yupo ‘gado’. Kwa upesi, Brian akanyanyua tena kitako cha simu na kumkandika nacho Brewster usoni, karibu kabisa na jicho lake la kushoto, hapo Brewster akahisi maumivu. Jicho lake lilijeruhiwa pia.
.
.
Brian akamng’ata mkono kwanguvu, kwa hasira Brewster akamtupia ukutani yeye akiugumia maumivu. Brian akakajibamiza na kulala akihisi maumivu makali kichwani. Alipomtazama Brewster akamwona akiwa anajirepea kukaa sawa. Akafikiria upesi na kuona ni hekima kuruka kupitia dirishani kuliko kukaa humo angoje kuuawa.
.
.
Akajivuta upesi, akipumbaza maumivu aliyokuwa nayo, akasongea dirisha na kujitupia huko nje pasipo kujali kuna urefu wa aina gani. Akafikia bustanini na kujeruhi mguu wake wa kushoto kwa kujichanja na ua kubwa komavu. Mguu ukawa unavuja damu. Tumbo nalo na kifua vyamuuma mno. Alikuwa ameruka toka ghorofa ya pili!
.
.
Akatema damu na kutazama kule juu alipotoka, dirishani akamwona yule dubwana akiwa anamtazama. Basi akajikokota kusimama, kisha akanza kujongea kwenda getini. Mwendo wake wa chechema sababu ya majeraha.
.
.
Brewster akabinua mdomowe. Na hamaki, kufumba na kufumbua, naye akajitupa kurukia kule chini! Akafikia kwato zake na kusimama imara kabisa. Taratibu akaanza kumfuata Brian akiwa anajua ashakuwa njiwa wake. Hana haja ya kumfukuza.
.
.
“Huu ni mwisho wako, Brian. Haijalishi ni namna gani unauchelewesha.”
.
.
Brian akakunja shingo kumtazama. Uso wake nao ulikuwa unavuja damu toka upande wa kulia wa paji lake la uso. Macho yake yalikuwa mekundu … mekundu yakionyesha maumivu mazito anayopitia.
.
.
“Simama, Brian. Naapa hutosikia maumivu hata kidogo. Nitakumaliza pasipo maumivu yoyote yale,” akasema Brewster huku akisugua kwato zake ardhini. Brian hakujali, akaendelea kusonga kwa mwendo wake wa kinyonga. Punde, Brewster akakimbia na kusimama mbele yake. Alikimbia kwa kasi sana, si ya binadamu. Kiganja chake kipana kikadaka shingo ya Brian na kumnyanyua juu! Akamuuliza, “Utajitetea na nini hivi sasa?”
.
.
Brian akiwa ametulia kana kwamba mtu anayengoja kifo kimtwae, akachuruza damu mdomoni. Tone lake likamdondokea Brewster jichoni na kumfanya kiumbe huyo afumbe macho. Akapepesapepesa na kuyafungua tena.
.
.
Ajabu alipotazama, akaona mkono wa Brian ukiwa unaishilia kooni mwake. Hakutambua nini kilichotokea, ila ghafla akahisi maumivu makali mno na damu zamtiririka! Kumbe Brian aliuwa ana kipande ha chupa mkononi mwake. Kipande alichokiokota wakati ananyanyuka toka pale chini alipoangukia.
.
.
Alimkita nacho Brewster mara tatu shingoni pasipo kukoma, Brewster akayakodoa macho haswa! Brian asiwe hata na lepe la huruma, akaendelea kumtoboatoa shingoni kana kwamba anataka kutengeneza nyavu. Damu zikamruka kwa hasira!
.
.
Upesi Brewster akamwachia na kisha akadaka shingo yake iliyokuwa inavuja damu pomoni. Akalia kwa uchungu wa maumivu. Akamtazama Brian kwa hasira, akajaribu kumdaka ila mkono wake ukalegea kwa kukosa nguvu. Akadondoka chini akiendea pumzi yake ya mwisho.
.
.
Brian akabaki akimtazama kandokando yake. Pale Brewster alipokata pumzi, akamtupia kipande kile cha kioo alichomuulia nacho, yeye akaenda zake taratibu akifuata geti. Taratibu kwa mwendo wa kinyonga. Kabla hajafikia geti, akatazama nyuma. Haki alikuwa amemuua dubwana.
.
.
Simulizi ya daudi na Goliathi.
.
.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 36*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Brian akabaki akimtazama kandokando yake. Pale Brewster alipokata pumzi, akamtupia kipande kile cha kioo alichomuulia nacho, yeye akaenda zake taratibu akifuata geti. Taratibu kwa mwendo wa kinyonga. Kabla hajafikia geti, akatazama nyuma. Haki alikuwa amemuua dubwana.
.
.
Simulizi ya daudi na Goliathi.
.
.
ENDELEA
.
.
“Mungu wangu, Brian!” Mama akatahamaki baada ya kumwona mwanae. Ndiyo kwanza Brian alikuwa amewasili eneo la nyumbani. Alikuwa anakokota baiskeli yake ambayo punde aliiangushia kando na msingi wa nyumba.
.
.
Mama yake akamsogelea upesi kumtazama.
.
.
“Nini kimekutokea?” Mama akauliza akiwa anamkagua kwa macho. Punde mlango ukafunguliwa, Wisconsin akatoka ndani. Naye akarusha macho yake kumtazama Brian kisha haraka akasonga eneo la tukio.
.
.
“Alikuwa ni Brewster,” Brian akasema na kusita. “… Nimemuua!”
.
.
Mama akaziba mdomo wake kwa kiganja chake cha kulia. Akauliza, “Umemuulia wapi? Watu wamekuona?” Brian akatikisa kichwa na kujibu, “Hamna aliyeniona. Tulikuwa peke yetu.”

Mama akamtazama mguuni, akamwona akiwa amelowanisha suruali na kiatu chake kwa damu.
.
.
“Twende ndani, hapa si salama,” akashauri Wisconsin. Mama akaona ni stara, hata hivyo Brian alikuwa anahitaji huduma ya kwanza. Upesi wakazama ndani na Mama akamshughulikia Brian kwa dakika kadhaa kabla ya kukaa na kuendelea na maongezi yao.
.
.
“ … alibadilika na kuwa mnyama,” Brian akasema kwa sauti yake ya pole. “Alitaka kuniua. Aliahidi kufanya hivyo. Kila alipodaka shingo yangu nilimwona akiwa na dhamira hiyo. Kunimaliza.”
.
.
Akaweka kituo kirefu akitazama mkono wake wa kuume ambao ulifungwa ‘bandage’. Kwa muda kidogo akamezwa na kumbukumbu juu ya namna mkono huo ndio ulivyomkita Brewster kwa chupa mpaka kumuua. Akasema, “sikumbuki ni roho ya namna gani ilinivaa. Nahisi nami nilikuwa mnyama kama yeye. Sikujiuliza mara mbili, hata sasa nashangaa.
.
.
Kitu pekee nilichokuwa nataka kukiona ni yeye akidondoka na kuwa mfu. Nikamtifua shingo yake …” Brian akaeleza akiwa mbali kifikra. Ni kama vile alikuwa anshuhudia anachokisema. “… nilimtifua kana kwamba plau inavyotafuna ardhi hata akalegea na kudondoka chini … akawa mfu.”
.
.
Wisconsin akamwekea mkono begani na kumminya kidogo, akasema, “Wewe ni shujaa, Brian.” macho yake yalikuwa yanamaanisha anachokisema. “Kecie hakukosea kukuchagua wewe. Aliona kipi kipo ndani yako.”
.
.
Mama Brian akamkumbatia mwanae kwa mara nyingine kisha akambusu mara mbili kwenye paji la uso. “Najivunia kuwa nawe, Brian.” akamtazama mwanaye kwa macho yanayolenga machozi. Wisconsin naye akamfariji na kisha kumwambia, “Inabidi niende huko kwenye hiyo nyumba.”
.
.
“Kufanya nini?” Mama Brian akatahamaki. Akajigeuza vema amtazame Wisconsin.
.
.
“Inabidi niende, kuna kitu nataka kutazama,” akasema Wisconsin kisha akasimama asiseme kitu gani champeleka huko. Akafungua mlango na kujiendea zake akimwacha Mama Brian kwenye bumbuwazi. Mwanamke huyo aliona kwenda huko ni kujitakia maswaibu kama yale ya Brian. Aliogopa.
.
.
Basi sasa tangu Wisconsin alipoyoyoma, akawa anahesabu masaa na dakika. Akawa anatazama saa yake mara kwa mara na hata njia kuangaza kama bwana huyo anarejea. Mpaka kufikia majira ya saa mbili usiku, hakuonekana. Mama Brian akapata shaka sana, hata Brian alitia doa imani yake.
.
.
“Atakuwa salama kweli?” Mama akamuuliza Brian. Alishika tama macho yake yakiwa yamejawa na ndita za woga. Brian akamjibu, “Anajua kujitazama. Haina haja ya kuhofia sana.”
.
.
Punde kidogo mlango ukagongwa, Mama akadamka upesi kwenda kutazama. Hakuwa Wisconsin, bali jirani tu.
.
.
“Habari?”
.
.
“Salama.”
.
.
“Samahani kwa usumbufu, vipi runinga yako yafanya kazi vema?” akauliza jirani. Mwanamama mwenye nywele nyeupe na mashavu mekundu. Kwenye nyonga yake alikuwa amembebelea mtoto mdogo wa kike makadirio ya miaka miwili.
.
.
“Sijajua, acha nitazame,” akasema Mama Brian alafu akaendea runinga yake na kuiwasha. Ilikuwa ajabu runinga hii haikuwa imewashwa mpaka sasa, pengine ni kwasababu hakukuwa na mtu mwenye mpango nayo. Kila mmoja alikuwa anamuwazia Wisconsin. Labda Olivia angelikuwa sebuleni, angeliwasha.
.
.
“Naona kuna matatizo,” akasema Mama Brian. Runinga haikuwa inaonyesha kitu isipokuwa chenga nyeupe tu. Hakujali sana, akaweka rimoti juu ya runinga na kumrudia mgeni wake.
.
.
“Naona kuna matatizo, haionyeshi kitu!”
.
.
“Ni ajabu,” mgeni akasema akitikisa kichwa chake kisha akabinua lips zake nyembamba.
.
.
“Vipi, kuna lolote?” Mama Brian akadadisi.
.
.
“Yah!” Jirani akaitikia kwa uhakika. “Walikuwa wanamwonyesha mtoto mmoja aliyepotelea msituni na kupatikana!”
.
.
“Kweli?” Mama Briana akakodoa macho.
.
.
“Ndio!” akajibu yule jirani. “Ni ajabu. Ni yeye pekee ndiye aliyefanikiwa kurudi baada ya kupotea. Simulizi yake hakika ilikuwa inasisimua! Ila sikufahamu nini kimetokea maana runinga ilizima picha nikadhani ni kwangu tu.”
.
.
“Haukusikia chochote kile?” Mama Brian akauliza. Habari hii ilimvutia. Kwa muda akasahau kuhusu swala la Wisconsin. Hata Brian aliyekuwa ndani naye akasimamisha masikio kuskiza.
.
.
“Sikusikia jambo la maana,” akajibu jirani. “Kabla ya mtoto huyo kuongea, basi runinga ikakata mawasiliano mpaka sasa.”

“Umemtambua mtoto huyo?” Mama Brian akauliza. Jirani akatikisa kichwa. “Hapana. Si wajua Boston ni kubwa!”
.
.
Basi akaendaze, huku nyuma Mama Brian na mwanae wakabakiwa na maswali. Walitamani kumwona mtoto huyo, au kusikia taarifa zake kwani kwa namna moja ama nyingine walikuwa wanazihitaji.
.
.
Brian akasema, “Nadhani kesho naweza kuzipata taarifa hizo vizuri.”
.
.
“Wapi?” Mama akauliza.
.
.
“Shuleni,” Brian akajibu na kuongezea, “Shule ni kubwa, sidhani kama atakosekana mtu mwenye habari hizo kwa undani.” Wazo hilo likajenga hoja kichwani kwa Mama. “Itakuwa vizuri ikiwa hivyo!” akanyanyuka na kwenda jikoni kufanya utaratibu wa chakula. Baada ya muda, chakula kikawa tayari.
.
.
“Brian, unahitaji chakula kwa sasa?”
.
.
“Hapana. Namngoja kwanza bwana Wisconsin.”
.
.
Mama akenda chumbani kumwita Olivia, punde akarejea naye, Olivia alikuwa amelewa usingizi, akampatia chakula, kisha akaketi kitini.
.
.
“Hauli?” Brian akamuuliza. Akatikisa kichwa chake na kusema, “Hapana, Sijisikii. Acha tumngoje Wisconsin kwanza.”
.
.
Kukawa kimya kidogo. Ni Olivia ndiye aliyevunja ukimya kwa kuomba atazamae runinga.

“Haionyeshi, mpenzi!” Mama akamjibu, ila akanyanyuka na kuendea rimoti ili athibitishe maneno yake kwa Olivia. Akawasha runinga. “Ona! Haionye--”
.
.
Hajamalizia, akashangaa picha zaonekania kideoni! “Brian, tazama!” Mama akapayuka. “Inaonyesha hivi sasa!”
.
.
Brian akauliza, “Ni chaneli gani ilirusha ile habari?” Mama naye hakuwa anajua. Wakapata kibarua cha kukagua chaneli zote kwa wepesi. Hawakuona kitu. Chaneli zote zilikuwa zaonyesha mambo mengine. Ila kuna moja bado ilikuwa giza.
.
.
“Ebu ngoja!” Brian akamtaka Mama yake asubiri kwanza hapo penye giza. “Hamna kitu!” Mama akasema.
.
.
“Hapo huwa ni chaneli gani?” Brian akauliza. Mama akapandisha mabega. “Sijui! Nitajuaje na haionyeshi?” Olivia akasema, “Ven 24! … inaitwa Ven 24.”
.
.
“Umejuaje?” Mama akauliza.
.
.
“Kwasababu ndiyo chaneli inayofuata baada ya kutoka Kids Date,” Olivia akajibu akiwa anatafuna.
.
.
“Najua zilipo studio zao,” Brian akasema, “Kesho nitaenda huko kuwauliza. Nadhani tutapata jambo.”
.
.
“Ila Brian,” Mama akatilia shaka. “Ni saa tatu sasa yaelekea na nusu, vipi kuhusu Wisconsin?” Kabla Brian hajajibu, Mama akaamka na kuuendea mlango, akafungua na kuchungulia nje. Hakukuwa na mtu, barabara ilikuwa nyeupe. Akafa matumaini.
.
.
“Inabidi tufanye jambo, Brian,” Mama akashauri.
.
.
“Niende kumfuatilia?” Brian akauliza. Mama akabanwa na
kigugumizi.
.
.
“Sidhani kama ni wazo jema. Pengine tuwataarifu polisi.”
.
.
“Unadhani kweli hilo ni wazo jema?” Brian akauliza na kuongezea, “Kumbuka ni mauaji!”
.
.
***
 
*ROHO YAKE INADAI --- 37*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Inabidi tufanye jambo, Brian,” Mama akashauri.

“Niende kumfuatilia?” Brian akauliza. Mama akabanwa na kigugumizi.

“Sidhani kama ni wazo jema. Pengine tuwataarifu polisi.”

“Unadhani kweli hilo ni wazo jema?” Brian akauliza na kuongezea, “Kumbuka ni mauaji!”

ENDELEA

Mama akakosa la kusema. Hakujua nini afanye. Bahati ndani ya muda mfupi wakasikia mlango unagongwa na mara Wisconsin akaingia ndani. Wakalipuka kwa furaha wakimkaribisha kwa hamu tele ya kutaka kujua nini hicho kimemkalisha muda mrefu hivyo mpaka wakapata hofu kubwa.

Kabla Wisconsin hajasema jambo, akaomba aletewa chai ya moto ajipashe mwili. Akanywa mafundo matatu ya chai hiyo na akiwa ametuama kwa fikra kisha akasema akimtazama Brian, “Brewster ameenda. Ulifanya jema sana kumuua akiwa katika mwili wake wa ulimwengu mfu. Endapo angekufa akiwa kwenye mwili wake wa kawaida basi mtihani ungekuwa mkubwa kwenye ulimwengu wa kiroho. Bado angalikuwa hai.”

“Lakini kwanini ukakawia hivyo?” Brian akauliza. Wisconsin akamjibu, “Kwasababu kulikuwa kuna mambo mengi ya kutazama.” kisha akamuuliza, “Unamjua vema bwana mwenye nyumba ile?”

“Dkt Hamill?”

“Ndio. Unamjua vizuri mtu huyo?” Wisconsin akauliza.

“Siwezi kusema namjua sana, sikupata muda mrefu wa kukaa naye,” Brian akajibu. Wisconsin akamuuliza, “Kwa muda huo ukamfahamu ni mtu wa aina gani?”

“Ni mtu mkarimu … pia mpweke,” Brian akajibu. Wisconsin akanyamaza kwa sekunde tatu, bado akimtazama Brian, kisha akamuuliza, “Una uhakika?”

Brian akatikisa kichwa. “Ndio, nina uhakika. Alinifanyia sana ukarimu. Siwezi kumsahau.”

“Sawa,” Wisconsin akasema na asiseme tena lingine. Brian akauliza, “Vipi kuna lolote?” Wisconsin akamtazama na kutikisa kichwa. “Hamna kitu. Tutaongea zaidi kesho, nahitaji kupumzika hivi sasa.”

“Ngoja basi ule,” Mama Brian akashauri. “Hapana,” Wisconsin akajibu. “Sijiskii njaa, nitakula kesho.” alafu akaenda zake.

Akiwa anaenda, Brian akagundua Wisconsin alikuwa na alama ya damu kwenye nguo yake. Akataka kuuliza lakini akaona ni stara kunyamaza. Wisconsin hakuwa kwenye hali ya kuongea, pengine kesho atafunguka zaidi.

“Vipi kuhusu yule mtoto wa kwenye runinga?” Mama akauliza. “Unadhani kuna haja ya kumwambia?”

“Ndio,” Brian akajibu na kuongeza, “lakini si kwa sasa. Unamwona hayupo kwenye mandhari hayo. Kesho nikitoka shule, nitateta naye vizuri.”

Basi Mama na Olivia nao wakaaga wanaenda kulala, Brian akabakia mwenyewe sebuleni akitazama runinga. Hakuwa mtazamaji mzuri wa runinga ila aliguswa tu kutazama kwa muda huo akidhani pengine anaweza kuona jambo kuhusu yule binti aliyekuwa anahojiwa.

Akaweka chaneli hiyo na kutazama, kulikuwa bado ni kiza. Si sauti wala picha yoyote ambayo ilikuwa inaonekana ama kusikika. Akatazama kwa sekunde kadhaa kisha akasimama na kuisogelea runinga. Akaendelea kutazama kwa makini. Baada ya muda kidogo, akahisi amesikia sauti ya kitu.

Akatazama kushoto na kulia kwake, hakukuwa na kitu. Alipotulia ndipo akajua ya kuwa sauti hiyo inatokea kwenye runinga. Ilikuwa ni sauti ya watu wakiruruma kwa chinichini. Brian akatazama runinga kwa macho ya ndita. Bado hakukuwa na picha, na sauti hii ilikuwa inaendelea kusikika. Ni ya nini?

Brian akaongeza sauti asikie lakini ajabu sauti hiyo haikuwa inaongezeka, ilibakia vilevile japo iliongezwa! Brian akalazimika kuegesha sikio lake kwenye spika za runinga. Akatulia tuli akisikiza kwa umakini…

“ … ruruma rurururuma … zizizissiiizii … vitiviikiviiizz … shishshishizz … trrriikk … chiiichiiib …” sauti ilinguruma pasipo kueleweka. Ilikuwa ni sauti nzito ya kiume. Brian alijitahidi sana kuisikiza aone kama atapata kitu lakini hakuambulia jambo. Akiwa anataka kuachana na sauti hiyo, mara akasikia sauti ya kike! Akatulia tena na kuskiza kwa umakini …

“tiiipttiiiiifff … reeegghaaatt … katkatgushik … chat,chat,chat … sssshhhhhh…” sauti ya kike ilinong’ona na kuendelea kunong’ona. Brian akajitahidi kuiskiza ili aone kama ataitambua sauti hiyo lakini hakufanikiwa. Ilikuwa ni ngeni kabisa.

Baada ya muda kidogo sauti hiyo ikakoma na kukawa kimya. Brian akatazama runinga kama kuna picha. Hakuona kitu. Akarudisha tena sikio lake kwenye spika ya runinga na kuskiza. Hakusikia kitu. Akakaa kwa kama dakika tatu kungoja kama kuna sauti ama picha itaonekana, hakuona wala kusikia kitu. Basi akaona ni kheri akazima runinga akalale.

Akaminya kitufe chekundu cha rimoti na kisha akaweka rimoti juu ya runinga, akageuka na kwenda zake azime taa kisha aende kulala. Alipofikia ‘switch’ kabla hajazima, akasikia sauti tena. Akageuka na kutazama runinga kwa hofu. Hakuona jambo ila sauti iliendelea kusikika.

Akiwa hapohapo ameduwaa, sauti ile ya runinga ikaendelea kuongezeka zaidi na zaidi mpaka kufikia kikomo chake cha mwisho na kuwa kelele kali! Haraka Brian akawahi rimoti na kujitahidi kupunguza mpaka kuwa sauti ndogo kabisa, kisha akatahamaki. Mbona nilizima runinga hii?

Akaiwasha tena na kuizima wa uhakiki. Akaiwasha tena kwa mara ya pili na kuizima kwa uhakiki zaidi alafu akaweka rimoti juu ya runinga na kuiendea ‘switch’ azime taa ya sebuleni.

Akazima taa, kukiwa kimya na salama. Kabla hajaelekea chumbani akaitazama tena runinga. Ilikuwa kimya na nyeusi. Hakukuwa na kiashiria chochote cha shaka. Basi akaelekea chumbani mwake akapumzike.

Akiwa amepiga hatua tano koridoni ambapo kiza kilikuwa kimetawala kwa taa kuzimwa, mara akaona mwanga hafifu ukimulika ukuta. Akasimama na kutazama akijiuliza mwanga huo unatoka wapi.

Alipotazama vema akagundua kuwa unatokea sebuleni. Haukuwa mwanga wa taa, bali runinga! Moyo wake ukakita fundo. Nani amewasha runinga na hakumwacha mtu sebuleni? Akajiuliza aende kutazama ama aachane nayo aende zake chumbani ajifungie na komeo?

Akapiga hatua mbili kusogelea mlango wake, akaona mwanga ule wa runinga ukiwa unachezacheza kuonyesha kwamba kuna kitu kinachorushwa kwenye kideo, kioo cha runinga kinaonyesha matangazo ya picha! Hapa akasita na kujiuliza, moyo wake ukiwa unaelekea kuchanganyia mwendo.

Aende kutazama ama aelekee chumbani mwake afunge mlango na kujifunika shuka gubigubi?

Akadaka komeo la mlango wa chumba chake. Akaminya komeo mlango ukafunguka. Kabla hajaingia, akasikia sauti ya runinga! Akatuliza vema masikio yake kuhakikisha. Ni kweli, ni sauti ya runinga. Kwahiyo sasa haikuwa picha pekee, bali pia na sauti yake!

Sauti hii Brian alipoisikiliza vema akagundua ni ya mahojiano kati ya mtangazaji na binti mdogo wa kike. Ilikuwa ya mahojiano yale ambayo waliyakosa sababu ya mtandao wa chaneli kuzimika. Basi akaona ni stara kukakata shauri akasikize, au angalau achungulie kinachoendelea.

Akarudishia mlango wake wa chumbani kisha taratibu akaanza kusonga kwenda sebuleni. Kwa mwendo wake wa majeraha, taratibu taratibu.

Alipofika kwenye kingo ya korido, akarefusha shingo yake kuchungulia. Kwenye runinga akamwona mtangazaji na binti mdogo wa kike akihojiwa. Uso wa mtangazaji aliuona, ila sura ya yule binti hakuiona kwani alikuwa ameipatia mgongo kamera. Kilichokuwa kinaonekana ni nguo na nywele zake alizobana mafungu mawili.

Mbali na runinga, Brian akatazama kukagua sebule nzima kama kuna mtu aliyewasha na kutazama runinga. Hakuona mtu. Sebule ilikuwa tupu na pweke, basi akahamaishia macho yake runingani kuendelea kutazama. Wakati huo moyo wake bado haujatulia. Hata kichwa chake kinamgonga kuashiria mambo hayako vile yanavyotakiwa kuwa.

“ … Ni nani alikuwa anakuitia msituni?” Mtangazaji akauliza. “ … ulimwona kwa sura?”

Binti yule runingani akatikisa kichwa na kusema, “Nilimwona.”

“Yupoje?” Mtangazaji akauliza. “Unaweza kumwelezea kwa umbo na sura yake?”

Kabla binti huyo hajajibu, Brian akashtushwa na hodi mlangoni! Moyo wake ukapiga bampa na kuanza kwenda kasi maradufu. Alihisi hofu sana. Miguu yake ilianza kutetemeka mpaka kugongana.

Hodi ikapigwa tena, na mara hii anayegonga akasema, “Heey!”

Ilikuwa ni sauti ya kike. Brian akajaribu kuwaza ni ya nani, upesi akili yake ikamkumbuka yule jirani. Ni yeye ndiye alikuja akagonga mlango muda ule alafu akasema heey!

Ina maana amekuja tena? Brian akawaza. Muda huu?

“Tafadhali,” sauti ikasema mlangoni. “…Naweza kuja kuangalia hicho kipindi?”


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom