Simulizi: Roho yake inadai

Simulizi: Roho yake inadai

*ROHO YAKE INADAI --- 21*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Brian na Olivia wakapiga kelele kali. Wakawashtua watu wote waliokuwepo kwenye sala. Wote wakakoma kusali na kuwatazama kwa mshangao.

“Brian! Olivia! Mmekumbwa na nini?” mama Brian akauliza. Brian kabla hajajibu kitu, akarusha macho yake kwa Padri Alfonso na Dada Magdalena. Dada Magdalena akatabasamu.

ENDELEA

Brian akalipuka kwa hofu. Akamnyooshea kidole Dada Magdalena na kusema, “Ni mashetani!”

“Unasemaje Brian?” Mama akauliza akiduwaa.

“Ni mashetani!” Brian akalia. Aliwanyooshea kidole Padri Alfonso na Dada Magdalena. “Hawa ni mashetani! Mashetani! Tokeni nyumbani kwetu. Mashetani!”

Ikawa vurugu asitake kusikia wala kuambiwa kitu akaelewa. Aling’ang’ana Padri Alfonso na Dada Magdalena ni mashetani, watoke nyumbani kwao! Waende zao.

Basi sababu ya vurugu hii, Padri Alfonso na Dada Magdalena wakaaga waende zao. Mama Brian akawaomba radhi kwa yote yaliyotokea.

“Usijali,” Padri Alfonso akasema akiufuata mlango. Nyuma yake Dada Magdalena akimfuatia. Wakaenda zao na amani ikarejea kwa muda kwenye nyumba ya wakina Brian. Ila walezi wakiwa hawajui liendealo. Kwa namna moja wamechanganyikiwa, wamejawa na maswali pia hofu.

“Brian, Olivia, mnaweza mkatuambia nini shida?” mama aliuliza. Sebule ilikuwa imetulia tuli. Taa zimewashwa na hata madirisha yamefunguliwa.

“Ni mashetani!” Brian akasema akitazama chini kama mtu anayateswa na fikira. “Nimewaona kwa macho yangu. Tumewaona! Padri Alfonso na Dada Magdalena ni mashetani! Si watu wa dini!”

“Mmewaona wapi?” Mrs Garett akauliza.

“Kule kanisani!”

“Lini?”

“Leo! Leo wakati tunasali!”

Mrs Garett na Mama Brian wakatazamana. “Brian, ulienda kanisani muda gani na wakati ulikuwapo hapa?” waliwaona Brian na Olivia ni watu waliochanganyikiwa. Maelezo yao yalikuwa hayawaingii akilini. Yalikuwa ni ya kufikirika. Vitu visivyowezekana!

“Sijui huu mji unaelekea wapi? …” akasema Brian kwa sauti ya pole. Macho yake yalikuwa pole. Anatazama meza akiwandawanda mawazoni. “ … Naogopa sana. Sijui ni wangapi ni binadamu kama sisi, nyumba ngapi zimetwaliwa na kukaliwa na mashetani … Inatisha…”

Brian aliposema hayo, akanyanyuka akitaka kwenda zake chumbani.

“Ngoja, Brian,” mamaye akamshika mkono. “Ulimwona Brewster?” Brian kusikia hivyo, akaketi chini. “Ndio, nimemwona.”

“Alikuja kwa ajili yako.”

“Kukuambia kuwa nimevunja nyumba yake?”

“Umevunja nyumba yake?” Mama akashangaa. “Hapana, si hilo!”

“Amekuambia nini?” Brian akauliza akimtazama mamaye kwa mshangao.

“Amenipa onyo tu kama ilivyo kawaida yake … Brian, ulienda kwenye nyumba ya marehemu?”

“Marehemu?”

“Mkuu wenu wa shule aliyefariki majuzi!”

“Dkt Hamill! … Brewster amekuambia nini?”

“Jibu, ulienda huko?”

Brian akanyamaza kidogo.

“Ndiyo nilienda. Jana.”

“Ulienda kufanya nini huko na mwenyewe hayupo? Amekwishafariki!”

“Mama, Dkt Hamill alikufa mbele ya uwepo wangu. Nyakati zake za mwisho alikuwa na mimi. Kuna ubaya ga--?”

“Brian! … tafadhali unaweza ukakaa mbali na matatizo kwa muda?”

Brian akakuna kichwa chake akikitikisa. “Mama, nimechoshwa na hili! … ina maana umemweka Brewster awe ananifuatilia si ndio?”

“Mimi na wewe tunajua hilo haliwezekani. Umemsikia Padri Alfonso alivyokuwa anamwongelea Brewster. Sipendi kumwona, lakini haimaanishi nisimsikilize anachoniambia! Na ni kweli aniambiayo.”

“Kwanini ananifuatilia? Kwanini mimi?”

“Na hilo ndilo linalonipa hofu. Brian, kaa mbali na mambo ya ajabuajabu. Tafadhali.”

Brian akakaa kimya. Alikua anawaza kichwani mwake. Mbona Brewster anamfuatilia? Lakini zaidi, mbona hakumwambia mama yake kuwa amevunja nyumba yake kuingia ndani? Ina maana hajajua kuwa ni yeye?

Hapana. Kama anajua vitu ambavyo hudhani yu mwenyewe, ataacha kujua jambo kama hilo la kwenda kwake? Ilikuwa haiingii akilini.

Brian akanyanyuka na kwenda chumbani. Akatulia kitandani mwake akiwaza juu ya yale mambo aliyotoka kuyaona. Yalikuwa ni mambo mengi ya kumuumiza kichwa. Mengi ya kumuogopesha. Aliwaza nini yatakuwa mwisho wa yote hayo?

Alinyanyuka akaendea dirisha la chumba chake na kutazama nje. Alitazama nyumba za jirani zilizopo karibu mpaka zile zilizokuwapo mbali. Akawaza sana. Je katika nyumba hizo, kuna watu kama wakina ‘Padri Alfonso?’. Alipata hisia za kumwogopa kila mtu sasa, lakini zaidi Brewster. Kwanini mwanaume huyo anamfuatilia kiasi hiko? Na kule kwenye handaki lake ….

Aliendelea kutazama nje kana kwamba mtu atazamaye runinga kisha akasombwa na mawazo. Alikaa hapo kwa takribani dakika tano, akashusha pumzi ndefu, na kugeukia kitanda chake. Akapiga hatua tatu kukifuata, ila kabla hajakifikia, akasikia dirisha linagongwa!

Haraka akageuza shingo yake kutazama. Hakuona kitu! Akasonga kulifuata dirisha na kutazama nje. Hakuona kitu. Akatikisa kichwa na kurudi kitandani. Akanyaka ile nyaraka ya Dkt Hamill ambayo bado hajaimaliza, akaiweka machoni apate kuendelea kuisoma.

Kabla hajaanza akasikia sauti ya dirisha likifunguka. Haraka akatupa macho yake kutazama. Akaona dirisha likiwa wazi, kioo kimefunguliwa. Akatazama kwa kama sekunde tano, hakuona jambo. Ila kidogo, akaanza kusikia sauti ya watoto.

Akaweka nyaraka yake pembeni na kunyanyuka taratibu kufuata dirisha atazame. Alipofika, akachomoza kichwa chake nje ya dirisha. Akatazama barabarani upande wa kushoto. Hakukuwa na kitu. Upande wa kulia. Hakukuwa na kitu!

Kabla hajarudisha kichwa chake ndani, mara kioo cha dirisha kikashuka chini na kukaba shingo yake. Akapapatika upesi kujinasua toka kwenye dirisha. Alipojinasua, akabaki anahema kwanguvu na kushika shingo yake kwa maumivu makali.

Hata mate aliona hayapiti kooni. Alipata woga, kila saa akitazama dirishani.

**


Baada ya kuzima bomba la maji mvua, Mrs Garett alitoka bafuni alimokuwa anaoga. Alifunga vema taulo lake kifuani na moja kwa moja akaendea sinki kwa ajili ya kusugua meno akamilishe zoezi lake la usafi.

Alitia dawa kwenye mswaki na kuanza kujisafisha. Hakuwa na hili wala lile. Macho yake yalikuwa yanatazama kioo muda wote akijikagua uso. Kumbe bado alikuwa kijana, alijiona. Kumbe bado anaweza kupata mwanaume mwingine na kuwa na familia, aliwaza kichwani.

Aliposafisha meno yake na kutema povu la dawa, akainua uso wake kutazama kioo. Ajabu akamwona Kecie nyuma yake! Akapiga kelele za woga macho yakiwa yamemtoka. Haraka akatazama nyuma, hakumwona mtu! Aliporudisha uso wake kwenye kioo, akakutana uso kwa uso na Kecie! Akapiga kelele kali za kumshtua kila mtu ndani ya nyumba.

Ndani ya dakika tatu, Mama Brian na Brian wakafika bafuni. Ila walikuwa wamechelewa. Mrs Garett alikuwa tayari amekwishakufa. Kichwa chake kilikuwa kimepondwapondwa kwenye sinki, sinki lote limekuwa jekundu kwa kujawa na damu!

“Mungu wangu!” Mama Brian akatahamaki akiwa ameziba mdomo wake. Muda si mrefu macho yake yakawa mekundu na kutiririsha machozi. Alimkumbatia mwanae na kuendelea kulia.

Brian akambembeleza mamaye akiwa anatazama mwili mfu wa Mrs Garett. Ila akiwa anatazama vema, akaona maandishi yakiwa yameandikwa kwa damu karibu na dirisha la bafuni! Alipoyafinya macho yake kutazama vema, akauona maandishi hayo yakisomeka, “Tazame vema mji wenu!”


**


Baada ya siku mbili tangu Mrs Garett azikwe … saa saba mchana.


Brewster akiwa amebebelea karatasi kadhaa mikononi mwake na mashine ya chuma ya kubania makaratasi hayo, alionekana akiwa anatembea kwa pole barabarani.

Alijongea kufuata mstimu mmoja pembezoni ya barabara, akabandika picha tatu tofauti za watoto waliopotea. Mmmoja alikuwa wa kike, wawili wa kiume. Alipofanya hivyo, akaendelea na mwendo wake wa taratibu kufuata mstimu mwingine kutimiza majukumu yake.

“Umeona matangazo ya wale watoto waliopotea?” aliuliza Mama Brian akiwa amesimama dirishani anamtazama Brewster akiishilia. Brian akanyanyuka upesi na kwenda dirishani kuangaza. Hakuona vema, akatoka kwenda nje kuufuata mstimu uliobandikiwa tangazo aone vema.

Akasoma matangazo yote hayo matatu na kugundua kuwa miongoni mwa wale waliopotea, mmoja wao anamfahamu fika. Alikuwa ni Silvia! Silvia rafiki yake mkubwa na Wayde. Wayde mtoto wa seneta wa Massachusetts!

Akaachama kwa mshangao. Nini kinaendelea?


**
 
*ROHO YAKE INADAI ---- 22*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Akasoma matangazo yote hayo matatu na kugundua kuwa miongoni mwa wale waliopotea, mmoja wao anamfahamu fika. Alikuwa ni Silvia! Silvia rafiki yake mkubwa na Wayde. Wayde mtoto wa seneta wa Massachusetts!
.
.
Akaachama kwa mshangao. Nini kinaendelea?
.
.
ENDELEA
.
.
Akarudi ndani na kumwambia mama yake kuwa mmoja wa wale waliopotea anamjua kwani wanasoma naye darasa moja. Na basi kutaka taarifa zaidi, akajipaki kwenye baiskeli yake, hakuweza kungoja, akaenda moja kwa moja kwa wakina Silvia.
.
.
Huko akamkuta Wayde akiwa ameketi kibarazani. Akamsalimu na kumuuliza nini kimejiri. Wayde alikuwa anachuruza machozi. Pua yake imekuwa nyekundu kwa kuifikicha.
.
.
“Silvia amepotea, Brian!” Wayde akalia. Akamkumbatia Brian na kuendelea kulia. Brian akapata kibarua cha kumbembeleza binti huyo kwa muda kidogo kabla hajatulia na kuendelea na maongezi yao.
.
.
“Ni jana tu, Brian!” akasema Wayde akiwa amebanwa na kwikwi. “Ni jana tu amepotea katika mazingira ya kutatanisha! Yaani siamini, Brian! Siamini kabisa! Nimejawa na hofu sana.”
.
.
“Ilikuwaje akapotea? Unaweza ukaniambia mazingira ya kupotea kwake?” Brian akauliza akimtazama Wayde usoni.
.
.
“Brian, usiku wa kuamkia juzi, wakati tukiwa tunaenda klabu, Silvia aliniuliza kuhusu ndoto za ajabu! Sikumwelewa, na sikutilia sana maanani. Najuta kwanini nilifanya hivyo. Aliniambia Wayde, nimeota naitwa usiku wa manane. Kuna mwanaume ananiita. Kuna mtoto ananiita. Watu hao wamesimama mlangoni, wamesimama dirishani!”
.
.
“Ni wakina nani? Aliwatambua?”
.
.
“Hapana. Aliniambia ni kama vivuli tu. Ajabu ni kwamba walikuwa wanamuitia kwenda kutazama mazingaombwe!”
.
.
“Ikawaje akanusurika siku hiyo?” Brian akadadisi.
.
.
“Wakati anatoka chumbani kwake, katika hali ya kutojielewa, akakutana na mama yake koridoni! Mama yake alimkurupusha na kumuuliza nini alikuwa anafanya, lakini hakuwa anajua kitu! Hakujua hata alifikaje pale koridoni. Kitu pekee alichoweza kumbuka ni kuitiwa kwenda kutazama mazingaombwe na wale watu!”
.
.
“Kwahiyo ndiyo haohao watakaokuwa wamemchukua?”
.
.
“Ni nani mwengine, Brian? … asubuhi ya leo, wazazi wake walikuta chumba chake kikiwa wazi, pia mlango wa sebuleni. Na skafu yake imeokotwa huko msituni.” machozi yakabubuja macho ya Wayde. “Silvia ametokomea huko!”
.
.
“Polisi wanasemaje?” Brian akauliza.
.
.
“Wamesaka msitu wote tangu asubuhi. Hakuna walichopata zaidi ya skafu yake.”
.
.
Brian akashusha pumzi na kushika tama akitazama barabara. “Brian, kuna lolote unajua?” Wayde aliuliza. Brian akatikisa kichwa akibinua mdomo. Akasema, “ni ajabu. Watu watatu wapotea ndani ya siku moja! Si jambo la kawaida hata kidogo.”
.
.
“Ni lazima kutakuwa na kitu,” Wayde akaunga mkono hoja. “Ngoja tuone ripoti ya polisi itasemaje. Ila …” Wayde akabinua mdomowe. “Sidhani kama kutakuwa na cha maana.”
.
.
“Kusipokuwa na cha maana utafanya nini?” Brian akamtazama Wayde. “Kuna kitu unaweza kufanya kwa ajili ya rafiki yako?”
.
.
“Chochote kile,” akasema Wayde akitikisa kichwa. “Kwanini unaniuliza hivyo Brian?”
.
.
“Nimetaka tu kujua,” Brian akajibu kisha akasimama na kumuaga Wayde. “Ningependa kukaa na wewe lakini unajua ku--”
.
.
“Unamwogopa baba yangu, sio?”
.
.
Brian hakutia neno.
.
.
“Usijali, Brian. Naelewa. Unaweza kwenda, lakini utakapopata kitu kuhusu Silvia, usisite kunijuza.”
.
.
“Ni mwanafunzi mwenzagu. Najali pia,” akasema Brian kabla hajajiweka kwenye baiskeli yake na kwenda zake.
.
.
.
**
.
.
Saa mbili usiku …
.
.
Baada ya ukimya mdogo wakiwa wanatazama runinga, Brian akamtazama mama yake na kumwita. Akamwambia kwa sauti ya chini, “Mama, Kecie ameanza kuua watu!”
.
.
“Kwanini unasema hivyo, Brian?”
.
.
“Nimekaa nikafikiri sana. Sasa ndiyo nimepata maana ya ujumbe ule ambao tuliukuta bafuni baada ya Mrs Garett kuuawa … unaukumbuka ujumbe ule?”
.
.
“Ndio.”
.
.
“Naona vitakuwa na mahusiano na huku kupotea kwa watu. Kwanini alituambia tutazame mji wetu?”
.
.
Mama akabaki kimya.
.
.
“Lakini kwanini muuaji huyo alituambia hivyo? Kwanini ametupa ujumbe huo baada ya Mrs Garett kuuawa?”
.
.
Hakuna aliyekuwa anajua. Walijawa na hofu. Hawakufahamu kama kupotea huko kwa watu kutakoma ama kutaendelea tena kesho yake. Lilikuwa ni swala la muda tu.
.
.
Basi baada ya muda kidogo, Brian akanyanyuka na kwenda zake chumbani. Alikuwa anataka kulala. Siku mbili za nyuma amekuwa akishughulika sana, haswa kutokana na msiba wa Mrs Garett, hivyo hakupata muda wa kupumzika vema.
.
.
Lakini basi kuvutia usingizi, akanyaka nyaraka ya Dkt Hamill aendelee kuisogeza karatasi kadhaa. Hakuwa ameipitia nyaraka hiyo tangu majuzi. Hakuwa na huo muda.
.
.
Alifungua alipoishia akaendelea kupekua kwa macho tangu pale ambapo mtumwa Jasmine alikuwa ameuawa na baba yake mzazi kisha kutupiwa ndani ya jengo ghofu la Helo.
.
.
“ … nakumbuka siku hiyo, ilikuwa ni usiku nikiwa chumbani mwangu, nikasikia sauti kali ya mama yangu. Haraka nikanyanyuka na kwenda chumbani kwake. Nilidhani ni baba ndiye anampiga mama, lakini nilipofika nikakuta habari tofauti. Mama alikuwa analia kwa woga wa kumwona mfu!
.
.
‘Kuna nini?’ nikamuuliza. Alikuwa amesimama kwenye kona ya chumba chake na bado sikuwa nimeona wapi baba alipo. Mama alikuwa anamimina machozi na ndita amezikunja haswa.
.
.
Akaninyooshea kidole nyuma yangu, yaani nyuma ya mlango. Nilipotazama nikauona mwili wa baba ukiwa umelala unachuruza damu nyingi mno. Nikaogopa haswa. Nikamuuliza mama nini kimemuua baba, akanijibu, ‘Jasmine!’
.
.
Nikastaajabu. Jasmine atakuwaje amemuua baba ingali amekufa?
.
.
‘Nimemwona kwa macho yangu!’ akasema mama akiwa ametoa macho ya woga. ‘Nimemwona Jasmine na amesema amerudi kulipa kisasi!’
.
.
Habari hizi zikaniogopesha kweli. Kesho na keshokutwa yake tukafanya utaratibu na baba akazikwa. Ila mambo bado yakaendelea kutokuwa shwari. Baada ya baba kufa, sasa watumwa wakaanza kupotea mmoja mmoja tukiambiwa ameelekea msituni! Ni kama mchezo, mwishowe wote wakapotea asibaki hata mmoja. Kwenye eneo zima, nyumba yote, tukabaki wawili tu mimi na mama yangu.
.
.
Hapo ndipo nilipogundua ya kuwa msitu ule umelaaniwa. Na aliyeulaani msitu ule ni yule ambaye anaishi humo. Helo. Kama vile alivyouawa kwa hatia, na kutupiwa huko, basi wote wale wanaouawa kwa hatia na kutupiwa humo msituni, huamka tena na kwenda kuwaangamiza wale waliosababisha vifo vyao.”
.
.
Brian alipofikia hapo, akafunga nyaraka na kujiuliza maswali juu ya hiko alichokisoma. Ina maana kile kilichotokea kwa Jasmine ndicho ambacho kinatokea kwa Kecie saa hii? Kama ilivyokuwa kwa Jasmine, Kecie aliuawa na kwenda kuzikiwa huko msituni. Kama pia ilivyokuwa kwa Jasmine, naye Kecie akawamaliza wazazi wake waliomuua.
.
.
Alafu kama ilivyokuwa kwa Jasmine, baada ya kumuua mtu aliyemuua, watumwa wenzake wakaanza kupotelea msituni, navyo kwa Kecie baada ya kuua wazazi wake, watu wameanza kupotelea msituni!! Ajabu. Ina maana Kecie alikuwa anajua kitakachofuatia baada ya yeye kummaliza mama yake? Ndio. Na ndiyo maana akaacha ujumbe wa kutazama mji?
.
.
Briana akapatwa na maswali haswa. Ina maana Kecie alikuwa anawatahadharisha? Kwanini afanye hivyo? Ina maana si yeye anayewapoteza hao watu msituni, bali Helo!
.
.
Helo anamtumikisha Kecie kufanya mambo yake ya kupoteza watu. Kecie hataki, na ndiyo maana anataka Brian amwokoe? Brian akajikuta anaketi akichakata mawazo haya. Sasa alipata picha kamili juu ya kinachoendelea. Ila bado hakuwa anajua cha kufanya. Atafanyaje kumwokoa Kecie?
.
.
Mara akasikia hodi mlangoni! Akashtuka haswa akikodoa macho.
.
.
“Nani?” Akauliza. Hakukuwa na majibu, akasita kwenda kufungua. Hodi ikapigwa tena. Akaamua kunyanyuka na kuusogelea mlango. “Nani?” akauliza tena. Hakukuwa na majibu. Brian akaamua kufungua mlango na kutazama nje.
.
.
Hamaki, kule sebuleni akauona mlango ukiwa wazi! Na kama haitoshi, akamwona Olivia akiwa anaishia, anaenda zake!
.
.
“Olivia!” Brian akapaza sauti. Haraka akatoka chumbani na kukimbilia nje.
.
.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 23*

*Simulizi za series*



ILIPOISHIA
.
.
“Nani?” Akauliza. Hakukuwa na majibu, akasita kwenda kufungua. Hodi ikapigwa tena. Akaamua kunyanyuka na kuusogelea mlango. “Nani?” akauliza tena. Hakukuwa na majibu. Brian akaamua kufungua mlango na kutazama nje.
.
.
Hamaki, kule sebuleni akauona mlango ukiwa wazi! Na kama haitoshi, akamwona Olivia akiwa anaishia, anaenda zake!
.
.
“Olivia!” Brian akapaza sauti. Haraka akatoka chumbani na kukimbilia nje.
.
.
ENDELEA
.
.
Alimuwahi Olivia na kumsimamisha. Binti hakuwa anajitambua. Brian alijaribu kumwamsha toka usingizini pasipo mafanikio. Bado Olivia alikuwa anataka kwenda, anataka kusonga mbele! Macho yake yalikuwa yamepandisha kiini cheusi juu kupotea!
.
.
“Olivia, amka! Oliviaa!” Brian aliita akimtikisa Olivia kwanguvu. Akaita pasipo kuchoka, hatimaye Olivia akarejewa na fahamu! Alikuwa anahema kana kwamba ametoka kukimbizwa. Alitazama kando na kando akaitaajabu kwanini yupo hapo.
.
.
“Olivia, upo sawa?” Brian akauliza. Olivia akatikisa kichwa. Uso wake ulikuwa umejawa na woga. “Nipo wapi hapa Brian?” akauliza.
.
.
“Upo nje! Ulikuwa umetoka, unaondoka!” Brian akamjibu akimtazama mtoto huyo kwa matumaini. Lakini ghafla, Olivia akatazama nyuma ya Brian na kuduwaza macho. Akaachama mdomo na kumuuliza Brian, “Ni nani yule?”
.
.
Brian akageuza shingo kutazama. Ajabu akamwona mwanaume mrefu mweusi aliyekuwa anaongozana na mtoto akija kwa kasi kuwafuata. Moyo wake ukaruka pigo. Haraka akamnyakua Olivia na kuanza kukimbia naye haraka!
.
.
Alitupa miguu kadiri alivyokuwa anaweza. Kila alipotazama nyuma akaona mwanaume yule akimjongea kwa kasi ya ajabu. Alikuwa anakimbia kana kwamba upepo!
.
.
“Wanatufikiaa!” Olivia akapiga kelele. “Brian, wanatufikiaa!” Olivia akalia. Lakini nini afanye Brian? Alikuwa anakazana kadiri ya uwezo wake wa mwisho. Alikimbia haswa. Alikuwa amebakiza hatua chache tu kufikia mlango wa nyumbani, ila ajabu napo, mlango huo ukaanza kujifunga wenyewe taratibu!
.
.
Kwa mahesabu ya wazi, Brian asingeweza kuufikia mlango huo kabla haujajifunga.
.
.
“Tafadhali, usifunge!” Brian akalia. Hakuwa anaweza kuongeza tena kasi kwani hapo alikuwa tayari kwenye kikomo. Alichokifanya, alipoukaribia kidogo mlango, wazi akiona unaelekea kufunga, akaruka hewani kuuparamia.
.
.
Akadondokea chini kama mzigo, Olivia akiangukia upande mwingine. Lakini kabla hajaugulia maumivu, akaukita mlango kwa mguu wake wa kuume, mlango ukafunga! Haraka akanyanyuka na kuutia komeo kisha akasimama hapo akiskiza nini kitaendelea.
.
.
Punde akasikia kishindo cha mtu mlangoni. Mlango ukagongwa mara mbili na sauti ikanong’ona, “Heeeeeyy! … wataka kucheza?” Brian hakusema kitu. Alikuwa amesimama hapo kuugandamizia mlango akiwa amejawa na woga.
.
.
“Najua unataka kucheza, sivyo hivyo Brian?” sauti iliendelea kunong’ona. “Najua unapenda kucheza … njoo basi, twende tukacheze … eti?”
.
.
Brian hakusema kitu, akaendelea kuwa kimya. Naye Olivia alikuwa ametulia akimtazama Brian.
.
.
Wakasikia kishindo kile cha miguu kikisonga kwenda mbali na mlango na kisha kurudi karibu. Kwenda mbali na kisha kurudi karibu. Mara kikakoma. Alafu sauti ile ikauliza, “Brian, hutaki kumwona Silvia?”
.
.
Brian akakodoa kwa mshangao.
.
.
“Yupo wapi?” akaropoka kuuliza.
.
.
“Yupo kule, twende ukamwone!” sauti ikamjibu. “Twende upesi!”
.
.
“Anafanya nini huko?”
.
.
“Anatazama mazingaombwe! Hutaki na wewe kuona?”
.
.
“Sitaki!” Brian akafoka. “Sitaki kukuona maishani mwangu. Sitaki uje kwetu. Kaa mbali na sisi!” Brian alisema machozi yakiwa yanamtoka. Mara kukawa kimya kwa sekunde tano, hakuwa anasikia kitu. Alitega masikio yake vema akiwa anatazama madirishani.
.
.
Mara akasikia sauti ya kike, “Brian, niokoe! Niokoea tafadhali!”
.
.
Brian akagutuka. “Silvia!” akajikuta anaropoka. “Silviaa!”
.
.
“Ndio, Brian!” sauti ya kike ikamjibu. “Naomba uniokoe Brian!” sauti ikalia. “Naomba uniokoe, tafadhali!” ikaendelea kulia na kulia. Brian akatamani kufungua mlango. Alitazama kitasa akitaka kukiminya, Olivia akapaza sauti, “Hapana, Brian!”
.
.
Brian akamtazama Olivia.
.
.
“Usifungue, Brian. Usifungue! Sio Silvia huyo.”
.
.
Mara mlango ukaanza kupondwa kwanguvu! Nguvu ya kuponda ilikuwa kubwa sana. Ukuta ulikuwa unatikisika. Bawaba zilikuwa zinalegea. Olivia akaenda kumsaidia Brian kuminya mlango lakini haikusaidia chochote kwani mlango uliendelea kupondwa kwanguvu sana. Ukaanza kutia ufa kana kwamba gogo lililooza likikitwa na ncha ya shoka kali.
.
.
Mara,
.
.
“Briaaaan!” sauti ya kike ikaita. Brian alipotazama koridoni akamwona mama yake akiwa amesimama, anawatazama kwa mshangao mkuu. Ni ghafla pia mlango ukaacha kupondwa na kukawa kimya kabisa kana kwamba hakuna kilichotokea!
.
.
“Brian, kuna nini?” mama akauliza akijongea. Brian alikosa cha kusema akabaki kimya. Mama alisonga karibu akatazama mlango. Ulichora ufa haswa. Bawaba zilikuwa zimetema nati zake. Ukuta ulikuwa umechimba mistari!
.
.
**
.
.
Mama alifikicha macho yake kisha akamtazama Brian aliyekuwa ameketi kwenye kiti pamoja na Olivia. Akashusha pumzi ndefu na kukuna kichwa chake kilichojawa na nywele.
.
.
“Hili ni tatizo kubwa mno, kila siku linazidi kukua. Kama tusipochukua hatua za mapema, linaweza kutugharimu.”
.
.
Kukawa kimya Mama aliponyamaza. Vinywa vilikuwa vizito. Akili zilipoa. Ni kama vile walikuwa wamenyeshewa mvua.
.
.
“Nadhani inabidi turudi kule kwa mtaalamu demonolojia,” Mama akaendelea kuteta. “Bila shaka yule ndiye mtu pekee aliyebakia wa kutusaidia.”
.
.
“Tutaenda lini?” akauliza Brian.
.
.
“Jua litakapochomoza,” mama akajibu na kuongezea, “Jiandaeni kabisa maana umebaki muda mchache kwenda huko … nadhani tutalala hukohuko.”
.
.
Mama aliposema hayo akaenda zake. Kweli jua lilipochomoza wakajikwea kwenye gari wakiwa wamebebelea mahitaji kadhaa tayari kwa ajili ya safari. Brian aliona ni stara kubeba zile nyaraka tatu za Dkt Hamill, alizitia garini akilenga kuendelea kuzisoma safarini.
.
.
Wakafunga nyumba, safari ikaanza.
.
.
Wakatembea kwa muda wa masaa mawili. Wakaacha mji wote nyuma na kuzama katikati ya misitu. Mwendo ulikuwa wa upesi maana safari ilikuwa ndefu. Basi Brian, ambaye alikuwa ameketi nyuma peke yake, akawa ameegamishia kichwa chake kwenye kiti akitazama miti irudiyo nyuma.
.
.
Alikuwa ametulia haswa. Alikuwa anawaza mambo yake kichwani. Lakini ukimya wake huo haukudumu kwa muda mrefu. Akiwa hana hili wala lile, mara akaanza kusikia sauti nyembamba ikimnong’oneza masikioni … “Brian, unataka kucheza?” akashtuka kidogo na kutumbua macho. Akatazama kila pande akiwa amekunja ndita.
.
.
Sauti ile masikioni ikacheka ikiishilia … “Wataka kuniona?” ikanong’ona. “Wataka kuniona Brian?” mara Brian alipotazama kushoto kwake akamwona mtu aliyevalia nguo nyeupe akikatiza ghafla kana kwamba radi! Akatoa macho kushangaa!
.
.
Akakunja uso wake kuangaza. Alitupa macho kwenye kioo cha nyuma cha gari lakini hakumwona mtu. Alishusha vioo vyote vya nyuma, akatazama pasipo mafanikio.
.
.
Basi punde, upepo mkali ukapuliza. Sijui ulikuwa umetokea wapi. Ulizama ndani ya gari kwakuwa vioo vvya nyuma vilikuwa wazi. Ajabu ukasomba zile nyaraka za Dkt Hamill na kuzimwagia nje!
ukazipeperusha huku na huko kutawanyika.
.
.
“Mama, simamisha gari! Simamisha garii!” Brian akawaka akimpigapiga mama yake begani. Mama akasimamisha gari upesi, na kumtazama Brian kwa taharuki. “Vipi?” Brian alitoka kwenye gari upesi kukimbilia nyaraka zake. Zilikuwa zinapeperushwa upesi na upepo kuzama msituni!
.
.
Aliikimbiza mojawapo lakini upepo ulizidi kuitokomeza. Mwishowe alisimama akadaka magoti yake akihema kwanguvu. Hakuamini macho yake, nyaraka zilikuwa zimepotea mbele ya macho yake!
.
.
Basi akiwa hapo, sura imemvurugika kwa kuchoka na mawazo, akaona mojawapo ya nyaraka yake ikiwa pembezoni mwa mti mkubwa umbali wa kama hatua kumi toka alipo kwa upande wa mkono wake wa kushoto.
.
.
Akasimama na kutazama vema. Ni kweli alichokuwa anakiona. Nyaraka ilikuwa imetuama hapo. Basi akakata shauri kuifuata. Alipopiga hatua tatu, akastaajabu kuona mkono ukitokea nyuma ya mti, ukaivuta ile nyaraka upesi!
.
.
Akakimbia kutazama, hakukuta kitu! Akabaki akiduwaa. Mara akasikia sauti ya makaratasi nyuma yake yakifunguliwa na upepo! Akageuka kutazama. Uso kwa uso akakutana na kiumbe ambacho hakuwahi kukiona wala kuja kukikumbuka. Asijue kinachoendelea, akadondoka chini na kupoteza fahamu!
.
.
.
.
“Briaaaaan!” mama aliita akiangaza huku na kule. Kandokando yake alikuwa pia Olivia naye akirusha macho kumtafuta Brian ndani ya msitu huu mkubwa.
.
.
“Briaaan!” mama aliendelea kuita. Macho yake yalishaanza kuwa mekundu akitaka kulia. Alipotembea kwa muda kidogo, akaona alama za miburuzo kwenye majani! Akajikuta analalama akiziba mdomo, “Mungu wangu, Brian!”
.
.
Alitazama kufuatilia alama hiyo ya miburuzo, kwa mbali akamwona mtu fulani akiishilia akiwa anavuta mwili wa Brian!
.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI -- 24*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Briaaan!” mama aliendelea kuita. Macho yake yalishaanza kuwa mekundu akitaka kulia. Alipotembea kwa muda kidogo, akaona alama za miburuzo kwenye majani! Akajikuta analalama akiziba mdomo, “Mungu wangu, Brian!”

Alitazama kufuatilia alama hiyo ya miburuzo, kwa mbali akamwona mtu fulani akiishilia akiwa anavuta mwili wa Brian!

ENDELEA

“Ni Brian!” mama akaropoka kwa kuduwaa. Haraka akaanza kukimbia kumfuata Brian. Nyuma yake Olivia alikuwa anamfuata kwa kasi. Ajabu alipokimbia kwa muda fulani, akampoteza yule mtu anayemburuta Brian! Hakuwa anaonekana tena.

Akaangaza kushoto na kulia, kulia na kushoto, hakuona kitu! “Briaaan!” akaita. “Briaaaan!” machozi yakamshuka haswa akiwa anapoteza matumaini ya kumpata mwanae. Ila ghafla akiwa anaangaza, mara akauona mwili wa Brian kwa mbali ukiwa umelala.

Akausogelea upesi. Akiwa amebakiza hatua chache, akasimama na kuangaza. Alihisi hayupo mwenyewe. Alihisi kuna mtu anamtazama mahali. Akageuka na kumwita Olivia. Akamdaka mkono binti huyo na kisha akasonga naye mbele taratibu na kwa tahadhari.

“Brian!” mama akaita akimtazama Brian ambaye bado hakuwa na fahamu. Alipomkaribia, akamtikisatikisa akimwita. Punde Brian akaamka. Akatazama kando na kando, akauliza, “Nipo wapi?”

“Amka twende!” mama akamwambia akimnyanyua. Wakaanza kutembea kurudi kwenye gari lao. Wakatembea kwa kama dakika kumi na tano kwakuwa walitembea pole.

Walipofika barabarani, kuangaza, gari halikuwepo! “Mungu wangu! Mungu wangu!” mama akalalama. Akakimbia kwenda huku na huko, gari halikuonekana. Hakufahamu ni kwamba limepotea ama limeibwa!

“Sasa tutafanyaje pasipo gari?” mama akauliza akishika kichwa chake kwa mawazo. Hakukuwa na mwenye majibu. Kila mtu alikuwa ameduwaa wasijue cha kufanya.

Baada ya muda wakakata shauri kutembea kwa miguu. Endapo litatokea gari lolote, wataomba msaada. Basi wakatembea kwa muda wa karibia lisaa limoja pasipo kuona gari lolote. Walichoka ila hawakuwa na budi kuendelea na matembezi. Wasingependa usiku kuwakuta humo katikati ya miti.

Wakatembea kwa robo saa zaidi ndipo wakasikia honi ya gari nyuma yao. Wakashtuka na kuangaza kwa furaha. Waliamini msaada sasa umewadia. Kweli kutazama lilikuwa ni gari, wakalipungia mkono kuliomba msaada. Gari likasimama na upesi wakaliendea.

Vioo viliposhushwa, wakawaona Padri Alfonso na Dada Magdalena! Mioyo yao ikawashtuka.

“Habari zenu?” Padri Alfonso akasalimu kwa tabasamu.

“Njema,” akajibu Mama Brian.

“Vipi, mbona msituni muda huu?”

“Aaaahm ni simulizi ndefu kidogo … vipi? Nyie mwaenda wapi?”

“Tunaenda kwenye huduma ya pamoja ya Massachusetts! Bila shaka mnahitaji msaada.”

Kabla Mama Brian hajaitikia, akamtazama Brian na Olivia. Wote wakamtikisia kichwa kutoafiki. Mama akarejesha uso wake kwa Padri kisha akatabasamu. “Nashukuru. Nyie mnaweza kutangulia tu.”

“Kweli?” Dada Magdalena akauliza.

“Yah! Tangulieni tu hamna shida.”

Padri Alfonso akamtazama Mama Brian kwa sekunde kadhaa kisha akaatia moto chombo na kuondoka. Mama Brian na wanawe wakabaki kutazama gari hilo likiishilia. Japo walihitaji msaada, waliamua tu liende.

Wakaendelea kutembea kwa miguu. Ikapita dakika kumi, wakaona gari jingine. Wakalipungia mkono kulisimamisha.

“Samahani tunaomba mtusogeze!”

Lilikuwa ni gari lenye nafasi kubwa kwa nyuma, wakajipaki na safari ikaendelea. Wakatembea kwa muda wa kama dakika kumi na mbili wakipulizwa na upepo huko nyuma.

Ila ghafla, Brian akamshtua mama yake. “Mama, tazama!” alikuwa amenyooshea kidole chake mbele. Kutazama, Mama akaona gari lao likiwa limejiegesha kando.

Akiwa haamini, akakodoa lakini bado kitu kikiwa ni kilekile. Ni kweli lilikuwa gari linalowahusu. Basi wakawaomba wale waliowasaidia wasimamishe ili washuke.

“Hapa?” akauliza dereva akiwa anashangazwa kidogo na ombi hilo. Gari lilisimama, wakashuka. Wakalifuata gari lao na kulikagua vema. Ndilo lenyewe! Hakukuwa na mtu ndani. Ni tupu.

Mama akafungua mlango wakazama ndani, akaliwasha wakaendelea na safari. Ila nani aliyelileta gari hilo hapo? Na aliwezaje wakati funguo hakuwa nayo? Hayo yalikuwa ni maswali ambayo hayakuwa na majibu.

Wakatembea kwa muda wa lisaa limoja kamili. Walibakiza sehemu ndogo tu kumaliza msitu huu. Wakiwa wanatafuna sehemu hiyo ya mwisho, wakakutana na gari lile lililokuwa limewabebelea Padri Alfonso na Dada Magdalena!

Gari hilo lilikuwa limesimama kando, limeharibika. Padri Alfonso na Dada Magdalena walikuwa nje wakihangaika nalo. Lakini walipoliona gari la wakina Brian, wakaacha shughuli yao na kulipungia mkono kulisimamisha.

“Habari?” Mama Brian akasalimu akitazama gari lile lililogoma kwenda.

“Habari si nzuri, tumeharibikiwa na gari letu,” akasema Padri Alfonso. “Vipi mnaweza kutusogeza tuendako?” Padri akauliza. Mama Brian akawatazama wanawe, wote wakampatia nyuso ngumu kama ishara. “Sidhani kama mtaenea humu. Kuna baadhi ya mizigo.”

Padri akatazama kulikagua gari kisha akauliza, “Hawezi kuingia hata mmoja wetu basi?”

Mama Brian akabanwa. Akawatazama wanae kabla hajajibu kitu. Alikosa namna ya kumkatalia padri basi akasema, “kwa mmoja … aahm … tunaweza kwenda naye!”

Padri akatabasamu. Akamtazama Dada Magdalena na kumwambia aingie ndani ya gari, yeye atangoja lingine lijalo. Basi Dada Magdalena akazama ndani na safari ikang’oa nanga. Wakatembea kwenda kumalizia msitu ule waende zao kwa mtaalamu.

Safari ikaenda na kuenda. Ndani ya gari kulikuwa ni kimya. Hakukuwa na soga yoyote ile. Wakakata lisaa limoja. Wakakata lisaa la pili. Bado wapo ndani ya msitu usio na kikomo.

Lakini mama Brian alitwaliwa na shaka. Makadirio yake ya muda yalikuwa kinyume kabisa na alichokuwa anakiona. Kwa ufahamu wake safari iliyobakia haikuwa ya kuchukua masaa mawili kuimaliza. Alistaajabu! Kila alipokanyaga mafuta, ni miti tu ndiyo ilikuwa mbele na nyuma yake. Miti pasipo kikomo!

Akasimamisha gari.

“Nahisi nimepotea!” akasema.

“Kwani unaelekea wapi?” akauliza Dada Magdalena akitabasamu kwa ukarimu.

“Naenda mbele. Nashangaa msitu haukomi!”

Dada Magdalena akatabasamu. “Pengine ni macho yako tu. Mbona tunasogea?”

“Najua barabara hii! Hii si mara yangu ya kwanza kupita. Haikuwahi kuwa ndefu kiasi hiki!”

“Vipi tukatumia sjia fupi basi?” akauliza Dada Magdalena.

“Njia ipi?”

“Kuna njia ya vumbi naijua. Mngependa tupite?”

“Hapana!” Brian akawahi kujibu. “Tutatumia njia hiihii!”

“Mafuta yanaelekea kuisha,” mama akasema. “Endapo tukiendelea kuzunguka humu, basi muda si mrefu gari litazimika lisiamke tena!”

Kukawa kimya kidogo. Ni kama vile watu walikuwa wanategeana kuongea. Brian akauvunja ukimya. “Dada Magdalena,” Brian akaita akimtazama Dada huyo usoni. “Tumekukosea nini?” akamuuliza.

Dada Magdalena akakunja uso kwa mshangao.

“Usin’tazame hivyo. Unajua ninachokiongea. Tunajua kuwa wewe si mwenzetu. Wewe ni jini. Jini miongoni mwetu binadamu! … mnaweza mkatupa kipindi cha amani kidogo tafadhali?”

Dada Magdalena akamtazama Mama Brian. “Anasema nini huyu?” akauliza.

“Anasema wewe ni jini!” Olivia akadakia. Uso wake ulikuwa umefumwa kwa hasira zaidi kuliko woga. “Wewe na Padri Alfonso ni majini. Tumewakosea nini? Tuacheni!” Olivia akamalizia kwa sauti ya chini iliyokaribu na kulia.

Dada Magdalena akaziba mdomo wake kwa mshangao. Akafanya ishara ya msalaba na kukutanisha viganja vyake kana kwamba anataka kusali. Macho yake yalikuwa yanaelekea kuwa mekundu kwa kutaka kulia.

“Sijui nini mnaongelea. Kwanini mnanisemea hivyo? Kuna lolote baya nimewatendea?”

“Dada Magdalena,” Mama Brian akashika hatamu ya kunena. Aligeuza shingo yake vema kumtazama anayemwongelesha. “Tafadhali. Sipendi kwenda mbali kwa maneno ambayo aidha nami naweza kuja kuyajutia hapo mbeleni … naomba ushuke twendelee na safari yetu.”

“Lakini mtaniachaje msituni?” akauliza Dada Magdalea kwa uso wa huruma.

“Nimekuomba,” Mama Brian akamsisitizia. “Nimekuomba ushuke toka kwenye gari yangu!”

Dada Magdalena akamtazama Mama Brian kwa sekunde kadhaa pasipo kusema jambo. Mara akaanza kubadilika. Mwili wake ukawa mweupe ukichomozwa na michirizi meusi kana kwamba mizizi ya miti. Macho yake yakabadilika na kuwa ya paka. Mdomo wake ukawa mweusi, kucha kama chui, meno kama simba!

Ghafla akamnyaka Brian aliyekuwa amekaa naye nyuma, akamnyonga kwanguvu akipanua kinywa chake kipana! Brian akahangaika kujitetea. Upesi Mama akamkita Dada Magdalena kichwani kwa kutumia ‘fire extinguisher’, Dada Magdalena akapata maruweruwe.

Hajakaa vema, Brian akamkita teke zito. Mama alishafungua mlango. Dada Magdalena akajikuta chini, gari likatimka kwa kasi!

Wakati Dada Magdalena anajikusanya chini, mara miguu ya mwanaume ikamjongea na kukoma mbele yake. Alikuwa ni Padri Alfonso. Alitazama mbele gari la wakina Brian likitokomea.



****
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom