*ROHO YAKE INADAI --- 16*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
.
.
Kulikuwa na korido ndefu sana. Sakafu yake haikuwa inaonekana kwani imetwaliwa na moshi. Kutani kulikuwa na fremu za picha na kwa mbali kulikuwa kunasikika sauti nzito ya mwanaume ikinena na hata kucheka.
.
.
ENDELEA
.
.
Brian akapata shaka na walakini. Akatazama nyuma kumwangalia Kecie, Kecie akamnyooshea kidole huko huko mbele. Lakini Brian hakuwa anajua cha kufanya. Alinyanyua miguu yake kwenda mbele akiwa hafahamu anaenda kukutana na nani.
.
.
Sakafu ilikuwa ya baridi kupita kiasi. Ilimfanya atetemeke na akunjekunje vidole vyake kila alipokuwa anakanyaga. Kwenye kuta, zile picha zilizokuwa zimetundikwa, zikawa zinanyamaza na kumtazama Brian alipokuwa anapita.
.
.
Picha hizo zilikuwa ni za sherehe. Zilikuwa ni za vifijo cha kipindi kile ambapo Helo alikuwa anatumbuiza. Bado picha hizo zilikuwa hai. Watu walikuwa wanafurahia na kushangilia mazingaombwe ya Helo, lakini Brian akitazama zilikuwa zinaganda na kuwa picha kamili!
.
.
Brian akazitazama akisonga. Moyo wake ulikuwa unapiga kusema hofu iliyomtawala. Kadiri alivyokuwa anasonga kwenda mbele, ndivyo sauti ile aliyokuwa anaisikia kwa mbali ikawa inamjongea na hata kuleta maana.
.
.
Kuna muda ilikuwa ni wimbo waimba. Na kuna muda kulikuwa na sauti ya mwanaume ikifoka ama kuteta. Mwanaume huyo ni nani? Na wimbo huo - ngoja! Atakuwa ni Helo. Brian alikuwa na kikao kichwani mwake. Na huyo anayemfokea ni nani?
.
.
Hakukuwa na majibu zaidi ya yeye kusonga na kutazama kwa macho yake. Japo alikabwa na woga, hakika alitaka kujua. Alipofika kwenye mwisho wa korido, taratibu, akachomoza kichwa chake kuchungulia sebuleni.
.
.
Kwa macho yake akamwona mwanaume fulani mzito aliyekuwa amevalia kofia ndefu kichwani yenye michirizi mekundu kwenye kingo zake. Mwanaume huyo alikuwa amevalia nguo za sherehe, zinazometa na kuvutia.
.
.
Koti jeusi la kumbana, suruali iliyoshika mapaja na nyonga zake kisha kubwaga huko chini. Miguuni ana viatu vyenye visigino virefu na kuchongoka kwa mbele. Mikononi amevalia glovu nyeusi malighafi ya ngozi.
.
.
Vitu vyote hivyo ambavyo vimetajawa vilikuwa vyametameta kana kwamba nyota angani!
.
.
“Helo!” Brian akajikuta ananong’ona mwenyewe akistaajabu. Mbele ya macho yake alikuwapo mwanaume ambaye amekuwa akisikia tu simulizi zake. Mwanaume aliyewahi kutikisa Boston na Massachusetts nzima!
.
.
Bado mwanaume huyo alikuwa amevalia nguo zake alizokuwa anatumbuiza nazo, hata picha zake huko ukutani zilikuwa zamwonyesha hivyo.
.
.
Hakika alipendeza na basi ungetamani umwone akiwa anatumbuiza. Lakini endapo ungekumbuka kuwa mtu huyu ni mfu, ungepoteza hamu yote! Mtu aliyechomwa moto miaka iliyopita na hata nyumba yake kutiwa pia motoni, leo yu hai, mzima na anacheza!
.
.
Pembeni yake kulikuwa na santuri ya kale iliyokuwa inamimina muziki wa bluzi. Hakika muziki huu ulikuwa unamkonga moyo wake, alikuwa akiimba pamoja nao na muda mwingine akijikuta anapiga kelele kali za nguvu!
.
.
Lakini sura yake haikuwa inaonekana. Alikuwa amempa mgongo Brian. Kichwa chake anakitikisatikisa na mkono wake uliopo ndani ya glovu unatengeneza ala kwa vidole.
.
.
Brian atamfanya nini mtu huyu? Akatazama nyuma, akakutana uso kwa uso na Kecie. Kecie hakusema jambo, bali akaendelea kumnyooshea kidole huko mbele, yaani sebuleni. Brian alipotazama tena kule sebuleni, Helo hakuwapo! Kiti pekee kilikuwa kinachecheza.
.
.
Moyo wa Brian ukalipuka kwa woga sana. Akapepesa macho yake kule na kule, hakumwona Helo. Hakujua wapi ameenda, tena ‘hafla hivyo! Kurudisha uso kwa Kecie, hapo akamwona mwanaume mrefu akiwa amesimama! Mwanaume mzito aliyeshiba.
.
.
Uso wake haukuwa unaonekana kwa kufichwa na kivuli cha kofia. Nguo zake zilikuwa zametameta, zang’aa, kana kwamba vito vya almasi vimeshikiziwa kwenye shuka.
.
.
Alikuwa anatisha kwa urefu wake. Brian alitetemeka na akatamani kupiga kelele kwanguvu sana. Mwili ulimuisha nguvu. Mkojo ulimbana, maungio ya mwili yalipata ganzi!
.
.
Kecie alijificha nyuma ya mwili wa mwanaume huyo, naye pia akiwa na uso wa hofu kuu.
.
.
“Unafuata nini kwenye himaya ya walio wafu?” sauti nzito ikauliza.
.
.
Brian hajajibu, akazabwa kofi kali sana. Akapaa juu na kwenda kujikita ukutani na kupoteza fahamu papo hapo! Hakujua tena kilichoendelea. Alipokuja kufungua macho, hajui hata majira, akajiona yu sebuleni kwao. Kichwa kilikuwa kinamuuma sana, haswa upande wake wa kulia.
.
.
“Mama!” akaita.
.
.
“Brian!” mama yake akamjongea upesi kumtazama. “Brian, mwanangu. Unaendeleaje?”
.
.
“Kichwa kinaniuma sana …” Brian akatazama kushoto na kulia kwake, akamwona Mrs Garett na Olivia. Akaita, “… Olivia.” kabla hajaongeza neno, kichwa kikamgonga sana, akakunja uso wake kus’kizia.
.
.
“Pumzika, Brian,” mama yake akamsihi. “ulipoteza fahamu ghafla.”
.
.
“Mlikuta Olivia?” Brian akauliza.
.
.
“Ndio. Olivia alikuwa ndani. Tulistaajabu kukuona wewe ukikimbia kwenda huko nje.”
.
.
“Alikuwa ndani? Mbona sikumwona? Wote hatukumwona!”
.
.
“Sisi tulimwona, alikuwa amelala kitandani. Tulikuambia lakini hukutuelewa. Tulistaajabu unakimbilia nje. Tulipokufuata tulikukuta ukiwa umezirai, umelala barabarani!”
.
.
Brian akaduwazwa na hayo maelezo. Yule hakuwa Olivia? Mbona alimwona vivyo? Basi na ilikuwa ni njia ya Kecie kumpeleka kule kwenye ulimwengu mwingine. Ulimwengu ambao Helo aliuita wa wafu.
.
.
Hakuwa anaota. Ulimwengu huo ni wa dhati. Maumivu ya kofi zito alilozabwa, bado alikuwa anayasikia sana yakiathiri sikio lake la kulia. Akawaza, atamwokoaje Kecie kule? Na je baada ya yeye kuondoka huko, Helo atamfanya nini Kecie?
.
.
**
.
.
Saa nane mchana.
.
.
.
Hakukuwa na shule siku hiyo, wanafunzi wote pamoja na wafanyakazi wa shule walikuwa wamehudhuria msiba wa Dkt Hamill. Shule ilikuwa pweke. Makaburi ya Boston yalikuwa yamefurika watu waliovalia sare za wanafunzi.
.
.
Hakukuwa na ndugu, jamaa wala rafiki wa marehemu. Kwa heshima za wafanyakazi wenzake, shule ikiwa imesimamia kila jambo, Dkt Hamill akaagwa na kuzikwa.
.
.
Watu walipotawanyika, Brian akaenda nyumbani kwa Dkt Hamill moja kwa moja. Alikuwa ndiye mtu mwenye ufunguo wa nyumba hiyo, pamoja pia na wa gari yake.
.
.
Alipofika, akaitazama nyumba hiyo kana kwamba ni kitu anachokijua ila kilipotea kwa muda mrefu. Akaikagua sana kwa nje, kila kona, akajikuta anajawa na machozi machoni mwake. Aliingia ndani na kuendelea kupekua. Akatazama picha za Dkt Hamill na familia yake. Akapata maswali sana kichwani,.
.
.
Familia hii ilipotelea wapi? Kwanini Dkt Hamill amekufa akiwa mpweke. Hana ndugu wala rafiki? Ni maisha gani hayo aliyokuwa anaishi? Alitamani sana kujua.
.
.
Akiwa anaendelea kupekuapekua, akiwa kwenye ghorofa ya juu, kwa chini nje ya uzio, akamwona mwanaume mmoja akiwa amesimama … amesimama anamtazama!
.
.
Mwanaume huyo alikuwa amevalia koti refu jeusi. Kichwa chake amekihifadhi ndani ya kofia na mikono yake ameidumbuliza kwenye mifuko ya koti.
.
.
Brian akastaajabu kuwa mwanaume huyo amemwonaje akiwa juu huko? Na kwanini amesimama kana kwamba mnara akimtazama? Ni nani?
.
.
Alipotazama vema akagundua mwanaume huyo ni Brewster! Mwanaume kikongwe ndani ya mji wa Boston. Mzee huyo anafanya nini hapo? Brian alishangazwa na namna ambavyo Brewster amekuwa wa kumfuatilia.
.
.
Akashuka upesi toka ghorofani, akaendea geti na kutazama nje. Hakumkuta mtu! Brewster hakuwepo. Alikimbilia kaskazini mwa barabara na kusini lakini hakumwona mzee huyo. Haikujulikana wapi alielekea.
.
.
Basi Brian akaona shughuli imetiwa doa, akafunga kila kitu na kwenda zake nyumbani, akiwa na maswali juu ya Brewster.
.
.
Alipofika, kwakuwa alikuwa na njaa, akaendea jikoni na kupakua chakula. Alimkuta Olivia pekee sebuleni anatazama televisheni.
.
.
“Wapo wapi hawa?” akamuuliza akitafuna.
.
.
“Wametoka,” Olivia akamjibu kwa ufupi.
.
.
Hapa ndipo Brian akakumbukua kuwa gari halikuwapo nje.
.
.
“Wameenda wapi?”
.
.
Olivia akapandisha mabega juu pasipo kutia neno, hakuwa anamtazama Brian. Basi Brian akaendelea kula, lakini ghafla kuna kitu kikamjia kichwani. Hakujua kwanini, ila alijikuta akikumbuka tukio la ajali ya Mr Garett!
.
.
Aliyakumbuka yale maneno ya Mrs Garett kuwa bwana wake alimwambia kuwa Kecie anawinda roho yao kabla hajafariki, punde ndogo baada ya kupata ajali ya gari.
.
.
Basi Brian akajikuta anakosa amani. Hata chakula hakukimaliza, akakiweka kando.
.
.
“Wametoka muda mrefu?” Akauliza.
.
.
“Tangu asubuhi,” Olivia akajibu, bado akiwa anatazama televisheni. Ila sauti yake ilikuwa tofauti kidogo. Hili kwa kiasi likampa mashaka Brian. Akaita, “Olivia!”
.
.
Olivia akaitikia. Hakumtazama Brian. Uso wake ulikuwa umeng’ang’ania kutazama televisheni.
.
.
“Olivia, nitazame.”
.
.
Olivia akakaa kimya. Hakutikisika wala kupepesuka. Brian akarudia kumwambia akimtaka ageuke. Mara hii Olivia akajibu kwa swali, “Kwanini nigeuke?”
.
.
Sasa mara hii sauti yake ndiyo ilikuwa tofauti kabisa. Sauti nzito ya kiume! Brian akajikuta akishtuka mno.
.
.
.
***