Simulizi: Roho yake inadai

Simulizi: Roho yake inadai

Yaani mkuu mastory yako kama unaangalia movie.....
picha liendelee..NEXT........
 
*ROHO YAKE INADAI -- 18*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Wasaa ulipowadia, nakumbuka ilikuwa ni kwenye majira ya jioni ya mapema, Jasmine akauteka mkono wangu na kutokomea nami msituni. Hakuna mtu aliyetuona. Hata watumwa wengine hawakuwa wanajua. Tukatembea upesi sana.
.
.
Njiani Jasmine akinieleza namna nitakavyofurahia mazingaombwe ninayoenda kuyaona!
.
.
ENDELEA
.
.
Basi kwasababu ya mwendo wetu huo, tukawasili eneoni mapema. Ilikuwa ni kama baada ya dakika sita tu! Tayari jengo ghofu lilikuwa mbele yetu. Lakini kabla hatujaingia humo, ajabu nikasikia sauti kali ya risasi! Nilishtuka mno!
.
.
Sikuwahi nimewahi kusikia sauti kali kama hiyo. Huwa nasikia risasi ila si kwa ukaribu kiasi kile. Nilipotazama kando, nikamwona Jasmine akiwa hatamaniki kwa damu! Uso wake wote ulikuwa umefumuliwa na risasi! Haki sikuwahi kuona picha ya kinyama kama ile.
.
.
Tundu kubwa lililopasua kichwa cha Jamsmine na kutapanya uso wake lilikuwa linachuruza damu kedekede. Nikatazama, kwa hofu, wapi ilipotokea risasi ile. Macho yalikua yamenitoka na moyo wanienda kwa pupa sana.
.
.
“Hey Hamill!” nikasikia sauti kavu ikiniita. Kutazama upande wangu wa kulia, nyuma, hatua kama arobaini na mbili, nikamwona baba yangu. Mkononi alikuwa amebebelea gobore kubwa alilokuwa amelitua. Kumbe ndi’ yeye aliyemuua Jasmine.
.
.
“Upo sawa?” akaniuliza akijongea. Nilikosa cha kumjibu. Nilipandwa na hasira mno. Nilimtazama kwa ghafira nikitamani kummaliza. Lakini yeye hakuwa anajali. Aliposonga karibu nami, akani ‘patipati’ kichwani na kumtazama Jasmine aliyekuwa maiti. Akamtemea mate.
.
.
“Kufa wewe malaya!”
.
.
Kwa hasira nikajikuta namshika baba yangu pindo lake la suruali na kumuuliza, “Kwanini umemuua Jasmine?” mara machozi yakaanza kunivuja. Nilishindwa kuuweka mdomo wangu sawa, ulipinda kana kwamba upinde wa mshale.
.
.
“Unasemaje?” baba yangu akafoka. “Alikuwa anakupeleka wapi huyu malaya?” akaniuliza. Asingoje hata jibu, akasema, “Nilimkanya mara kadhaa akae mbali na familia yangu, hakusikia! Kwa maana mgongo wake hausikii tena mijeledi, ngoja na tuone kama kichwa chake kinaweza kuwa sugu mbele ya risasi!” aliposema hivyo akaguna akibinua mdomo.
.
.
Akanyanyua mwili wa Jasmine na kuupeleka ndani ya ghofu. Akautupia humo na kukung’uta mikono yake kwa kumaliza kazi. “Twende!” akaniamuru.
.
.
“Siendi popote!” nikamwambia. Na nisimngoje aniambie kitu, nikakimbia nisijue wapi naelekea. Nikakimbia tu kwenda mbali na baba yangu. Nilimchukia sana. Nilimwona ni mtu asiyefaa kabisa.
.
.
Nikakimbia kadiri ya uwezo wa miguu yangu. Nilipochoka, nikalala chini na kulia sana. Pale nilipokuwa nimelaza kichwa changu pakalowana kwa machozi.

Nilikaa huko mpaka giza lilipoanza kumeza uso wa nchi. Niliogopa sana kuwa msituni nyakati za usiku ila niliona ni kheri kuliko kwenda nyumbani. Basi nikajikunyata kwa baridi na kulazimisha usingizi unitwae.
.
.
Ila kila mara nikawa nashtuka. Wanyama wakikatiza ama matunda yakidondoka ama miti ikisogezwa na upepo, nilikuwa nafungua macho na kuangaza. Nilikuwa naogopa. Sikuweza kudhani usiku ule ungekuwaje.
.
.
Nikiwa sijapata usingizi, nahangaika kufumba na kufumbua macho, nikasikia jina langu likiitwa kwenye miti! Nikanyanyua uso wangu haraka na kuangaza. Ilikuwa ni sauti ya kike. Punde kidogo nikaona mwanga wa taa kwa mbali. Haraka nikanyanyuka na kwenda kufichama nyuma ya mti kuchungulia.
.
.
Nikaendelea kuitwa. Mara ya tatu nikatambua kuwa sauti hiyo ni ya mama yangu, nikaguswa moyoni. Nikaitikia na kukimbia kwenda kumkuta mama. Alikuwa mwenyewe katikati ya msitu. Mkono wake wa kushoto ulikuwa umebebelea taa, na ule wa kulia ukiwa umebebelea gongo kubwa kumlinda.
.
.
Aliponiona akafurahi sana. Akanikumbatia kwanguvu akitupia taa kando. Akanibusu na kunikumbatia tena kwanguvu.
.
.
“Twende nyumbani!” Akasema akinishika mkono. Alikuwa ni jasiri wa namna gani. Alikuja mwenyewe msituni kunitafuta, akimwacha baba peke yake nyumbani akivuta tumbaku. Asingeweza kulala ndani mimi nikiwa nje. Kuna muda nilikuwa najiuliza, ilikuaje mama yangu akaolewa na mwanaume katili kama baba yangu? Ila niliamini watu wadhalimu huitaji zaidi malaika kama mama yangu kuliko wawahitajivyo wadhalimu wenzao.
.
.
Tukafika nyumbani salama, naye baba asiseme jambo, mdomo wake ulikuwa umetingwa na shughuli kubwa ya kunyonya tumbaku na kutemea moshi nje.
.
.
Siku hiyo nikalala kwa maruweruwe sana. Jua liliponyanyuka, nikashukuru. Nikaomboleza kifo cha Jasmine na hata ile safari yetu ya kwenda kwenye mazingaombwe. Ningeenda na nani na yeye ashakufa? Niliogopa kwenda mwenyewe ingawa eneo nalifahamu.
.
.
Basi nikaachana na mpango huo. Na sasa nikadhani ya kuwa Jasmine atakuwa ameenda milele. Nisingemwona wala kumsikia tena. Hakuna mtu anayemkumbuka mtumwa. Hakuna anayejali wala kutunza tarehe yake ya kifo, labda wenzake.
.
.
Ila nilikuwa mwongofu. Nilikosea kuwaza hivyo. Roho ya Jasmine haikwenda, ilirejea kudai haki yake ya uhai. Ilirejea ikiwa si ya yule Jasmine nimjuaye, mwenye upendo, mpole na mkarimu. Ilirejea ikiwa ya muuaji asiye na chembe ya huruma. Aliyejawa na kisasi kikubwa!”
.
.
Brian akaishia hapa kusoma. Macho yalikuwa yamechoka sasa na hakuweza kuendelea tena. Akaweka nyaraka ile kando na kuchukua muda kidogo kuyawaza yale aliyoyasoma, Hakuchukua muda, usingizi ukamkwapua asiamke mpaka asubuhi.
.
.
Hakukuwa na shule hivyo hakuwa na sababu ya kuwahi. Akajibandua kitandani majira ya saa tatu asubuhi, akaoga na kuosha uso alafu akajivuta sebuleni. Huko akamkuta mama yake, Mrs Garett na Olivia. Walikwishaamka na tayari wamejipatia kifungua kinywa.
.
.
“Brian, leo ndiyo siku ambayo Padri atakuja hapa. Naomba uwapo mapema nyumbani,” mama akakumbushia. Brian asionyeshe muitikio wowote, akaenda jikoni na kutwaa chakula cha asubuhi. Baada ya hapo, hakukaa sana nyumbani. Hakuona shughuli ya kufanya papo. Alipata wazo la kwenda kwa Brewster, kwakuwa ni asubuhi, aliamini atamkuta mzee huyo.
.
.
Aliamini ana mambo kadhaa ya kuteta naye ingawa mlengwa wake hakuwa mtu wa kuunga mkono. Mkimya. Na kwa namna moja ama nyingine, anatisha.
.
.
Kuna kitu alihisi hakipo sawa na mzee yule. Brian aliamini. Na pia alihisi kuna mambo ambayo mzee yule anayajua ila mdomowe kautia gundi.
.
.
Akaendea stoo na kuchukua baiskeli yake, akakwea na kwenda moja kwa moja nyumbani kwa Brewster. Kama ilivyo ada nyumba hii ilikuwa imetulia haswa. Ni kama vile hakukuwa na mtu aishiye hapa. Kunguru walikuwa wametandia kwenye paa, wakitazama huku na kule, huku na kule.
.
.
Brian akasonga karibu. Akaugonga mlango na kuita. Hakukuwa na majibu. Akachungulia ndani, hakumwona mtu. Sebuleni kulikuwa na kiti kimoja cha kucheza. Mbali na kiti hicho hakukuwa na samani nyingine. Sebule ilikuwa pweke, hodi ikibishwa inasikika na mwangwi.
.
.
Brian akashusha pumzi na kujiuliza kwa sekunde kadhaa. Akakata shauri la kwenda nyuma ya nyumba hiyo. Huenda Mr. Brewster akaja kumkutia huko kama ilivyokuwa siku ile.
.
.
Napo huko akakaa kwa muda mrefu akimtazama nguruwe wa Brewster. Mzee huyo hakutokea. Akawaza kuondoka, ila kabla hajafanya hilo, akapata wazo. Vipi akizama ndani ya nyumba ya mzee huyo na kutazama? Kupekua kidogo?
.
.
Huenda nikagundua mambo ambayo hataki kuniambia, akawaza. Akili yake ikatumikisha viungo vyake vya mwili kutenda wazo hilo la kidhalimu. Akauendea mlango wa nyuma na kufanya namna kwa kuufungua kwa ndani baada ya kusukuma dirisha.
.
.
Taratibu akaurudishia mlango huo na akarusha macho yake kukagua nyumba hiyo. Ilikuwa imejawa na tando za buibui kwenye kona zake. Kuta zilikuwa na ukungu. Harufu iliyokuwamo ndani haikuwa ya kuridhisha.
.
.
Brian aliwaza ni namna gani mzee huyo anaishi humo. Alifika sebuleni, akakagua. Uso wake ulikuwa umeumba ndita kwa kutopenda anachonusa. Alipomaliza kutazama sebuleni, akaendea korido kwenda kukuta vyumba viwili vya nyumba hii.
.
.
Ila kadiri alivyokuwa anapiga hatua kwenda huko, nayo harufu ikawa inazidi maradufu. Hakujua ni nini inanuka. Ilikuwa ni harufu kali ya kitu kilichooza.
.
.
Alijaribu kuusukuma mlango wa kwanza, ukafunguka. Akachungulia humo ndani. Kulikuwa na kitanda chakavu chenye godoro lililotobokatoboka. Akaangaza huku na huko. Hakuona kitu zaidi ya tando za buibui, nguo zikiwa zimezagaa huku na kule.
.
.
Akaachana nacho na kwenda kwenye chumba cha pili. Akajaribu kukifungua, mlango ukakubali. Harufu ile aliyokuwa anaisikia, sasa ikazidi mara tatu yake! Ilikuwa ni kali mno kiasi cha kuwa ngumu kuvumilika.
.
.
Brian akabana pua yake kwanguvu. Akaangaza huku na kule chumbani. Hakukuwa na kitu! Chumba kilikuwa kitupu. Kimejawa na nzi na kina kiza kiasi kutokana na kutofunguliwa kwa pazia.
.
.
Ila kabla Brian hajakiacha chumba hiki, akaona mlango mdogo kwa sakafuni. Kulikuwa na andaki kwenye chumba hiki. Na Brian akawaza kuwa huko ndipo kwenye kitu kitoacho harufu.
.
.
Akabaki njia panda, aende kutazama, ama ajiondokee upesi kabla hajakutwa?

.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 19*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Ila kabla Brian hajakiacha chumba hiki, akaona mlango mdogo kwa sakafuni. Kulikuwa na andaki kwenye chumba hiki. Na Brian akawaza kuwa huko ndipo kwenye kitu kitoacho harufu.
.
.
Akabaki njia panda, aende kutazama, ama ajiondokee upesi kabla hajakutwa?
.
.
ENDELEA
.
.
Akawaza kwa muda mchache, akaamua kwenda kutazama. Ila kabla hajatimiza adhma yake hiyo, akachungulia dirishani kukagua kama Brewster hayupo karibu. Alipojiona yu mwenyewe eneoni, akafungua mlango wa handaki na kutupia macho yake humo ndani.
.
.
Kulikuwa kuna giza hivyo basi hakuonekani. Brian hakuweza kuona chochote kile pasipo kujali namna gani alikodoa. Kutakuwa kuna namna, aliwaza. Akatazama huku na kule akitafuta taa ya kutazamia humo ndani. Juu ukutani akaona taa inaning’inia. Akaisongea na kuikwapua. Akaiwasha na kufungulia mlango wa handaki.
.
.Akanyooshea mkono wake ndani ya handaki. Kutazama akaona vitu kadha wa kadha vikiwa ndani ya mifuko ambayo imetandiwa na nzi. Handaki ilikuwa kubwa, asingeweza kuliona lote kwa juu.
.
.
Basi akashuka chini na kuendelea kuangaza. Kulikuwa na vitu vingi ambavyo vimefungashwa na kukalia hovyo. Vyote vilikuwa vinatoa harufu kali. Ndani humu kulikuwa na harufu na hewa nzito sana.
.
.
Brian akainama na kubinyabinya miongoni mwa mizigo iliyokuwamo humo. Akiwa anaangaza, mara akaona kichwa kikubwa cha mnyama. Akakisongea kukitazama vema. Kilikuwa ni kichwa cha mnyama paa. Kilikuwa kinaelekea kuoza sasa.
.
.
Ina maana kwenye mizigo yote ile kulikuwa na nyama za wanyama? Akajiuliza Brian. Ila bado roho yake haikuwa imeridhika. Alitaka kutazama kwenye mifuko ile mingine kulikuwa na nini pia.
.
.
Akatoboa mfuko mmoja. Kabla hajatazama vema, akasikia sauti ya kengele. Akashtuka. Kengele hii ilikuwa ni ya baiskeli! Nani amebofya baiskeli yake? Ina maana Brewster amefika? Akapatwa na maswali mengi lakini zaidi hofu sana!
.
.
Moyo wake ulianza kwenda mbio sana. Kichwa kiliwaka moto, je atoke upesi humo kwenye handaki ama abaki? Kwakweli hakuwa anajua cha kufanya. Alihisi kuchangayikiwa.
.
.
Haraka akapanda ngazi kuendea juu. Alipofika kwenye kamlango ka handaki, akasikia mlango unafunguliwa, na punde vishindo vya miguu! Akawaza upesi. Akitoka, humo chumbani hakuna mahali pa kujificha, itabidi aende chumba kingine. Ni wazi ataonekana.
.
.
Kwa upesi akawaza na kuamua kubakia humohumo ndani kwenye handaki. Akasimamisha masikio yake asikie kinachoendelea.
.
.
Brewster alisafisha koo lake na kuketi kitini. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea mfuko mweusi wenye kitu ndani. Alikuwa amechoka, lakini pia macho yake yalionyeshea mawazo fulani. Si makubwa. Hakuwa anahofia.
.
.
Kwenye koti lake akatoa kiko na kukiwasha. Akawa anavuta akiwa anachambua mawazo yake kichwani. Taratibu akawa anaenda mbele na kurudi nyuma, anaenda mbele na kurudi nyuma akibembea. Mdomo wake unanyonya kiko na kutemea moshi nje. Macho yake yanatazama dirisha, mlango, paa, korido, kila sehemu.
.
.
Baiskeli aliyoikuta nje. Nyayo za viatu. Mlango kuukuta wazi. Vyote vilikuwa vinatafuna kichwa chake kwa nafasi yake. Lakini ilikuwa ni ajabu kwani hakuonyesha hofu ambayo pengine mwanadamu mwengine angeonyeshea.
.
.
Alikuwa mtulivu.
.
.
Alipovuta kiko chake kwa dakika kumi pasipo kusikia jambo, akapaza sauti yake kusema, “Ni kheri ukaja sebuleni! Utakaa huko mpaka muda gani? Nimechagua amani badala ya shari na wewe.”
.
.
Sauti yake ilisikika kila eneo ndani ya nyumba yake. Alipolijua hilo, akaendelea kuvuta kiko chake akimpa muda mvamizi ajitokeze yeye mwenyewe. Akavuta tena kwa takribani dakika tano, bado kukawa kimya. Basi akazima kiko chake na kusimama.
.
.
“Kwakuwa umekuwa punda wa kulazimishwa kunywa maji ya mtoni, acha nikupe ukitakacho!” akasema kwa sauti kubwa. Akashika njia kuendea kile chumba chake cha kwanza. Mwendo wake ulikuwa wa kikakamavu mbali na umri wake. Bado alikuwa ana nguvu za kujisogeza, na hata kupambania maisha yake.
.
.
Alienenda kwa tahadhari na alipozama ndani ya chumba hicho, nyuma ya mlango akatoa gobore lake na kulitazama kama lina risasi humo ndani. Alipoliona li vema, akalikoki tayari kwa shambulizi.
.
.
“Toka na ujisalimishe kwa usalama wako!” Brewster akafoka. Akatoka kwenye chumba alichomo na kuendea kile chumba pekee kilichobakia. Bado alikuwa anatembea kwa tahadhari sana. Alipofika humo, akagundua ya kuwa, taa ile atumiayo kuzamia kwenye handaki haikuwapo!
.
.
Akatazama mlango wa handaki. Akapata sasa shaka kuwa mvamizi atakuwa humo ndani. Taratibu akauendea mlango huo, akafungua na kuonyeshea kinywa cha gobore humo.
.
.
Akajaribu kuangaza kwa macho yake ya kizee. Hakuwa anaona kitu! Ndani kulikuwa ni giza. Na pia kuingia humo pia ilikuwa ni hatari.
.
.
Brewster akawaza cha kufanya. Hakuwa mtu mwoga ila ilimlazimu achukue tahadhari hapa. Akafyatua risasi moja ndani ya handaki. Mwanga wa risasi ukalipuka na kuangaza humo. Kwa kiasi kidogo, Brewster akawa ameona sasa.
.
.
Akajiveka ujasiri na kuzama humo. Akashusha mguu kwa taratibu, akiwa anaangaza huku na huko ingawa haoni. Alipofika katikati ya ngazi, akafyatua tena risasi apate kuona lakini pia kumtisha mvamizi aliyekuwamo humo ndani.
.
.
Ila hakujua kuwa risasi hizo zilionyesha pia mahali yeye alipo.
.
.
Aliposonga hatua tatu, ghafla akastaajabu amedakwa mguu, akadondoka chini na kubiringita kwenye ngazi mpaka chini. Akapoteza fahamu kwa muda.
.
.
Haraka Brian akatoka ndani ya handaki, ndani ya nyumba, akajikwea kwenye baiskeli na kutokomea upesi akiwa na pupa sana! Hata hakuamini kama ametoka salama.
.
.
.
**
.
.
.

“Nadhani leo itakuwa vema tukipika mboga za majani!” Alipendekeza Mrs Garett baada ya kuulizwa na Mama yake Brian. Tangu amekuja kwenye nyumba hii, ni nyama tu ndiyo imekuwa ikitembelea jiko.
.
.
“Basi kama ni hivyo, sina haja ya kuanza kuandaa mapema,” akasema mama Brian kisha akaketi kochini. Hapo sebuleni walikuwa wote, hao wanawake pamoja pia na Olivia.
.
.
Baada ya Mrs Garett kutazama runinga kidogo, Mama Brian akamuuliza, “Ni nini mipango yako baada ya mumeo kufariki?”
.
.
Mrs Garett akaguna na kushusha pumzi ndefu. “Sijajua. Unajua sijapata muda wa kutulia tangu mume wangu afariki. Akili yangu inashindwa kuwaza mambo ya kujiendeleza, bali hofu hofu hofu tu!” aliposema hayo, akamtazama Olivia, alafu akapeleka sura yake kando na kusema kwa sauti ya chini.
.
.
“Likipita hili nitatuliza kichwa changu niangalie chakufanya sasa. Natumai kila kitu kitakuwa sawa.”
.
.
Mama Brian akamwekea mkono wake begani. “Kila kitu kitakuwa sawa, usijali.” Mrs Garett akatikisa kichwa chake kuitikia. “Hata wewe umewezaje kwenye hali hii?” akauliza. Mama Brian akatabasamu na kusema, “Nishazoea. Ni muda sasa nikiwa mwenyewe. Japokuwa mume wangu aliniacha na kiasi kidogo cha pesa, niliweza kukikuza.
.
.
Nilihangaika sana mwanzoni, kwa upweke na kwa kutokuwa na uzoefu. Ila kadiri na muda nikazoea. Niko sawa sasa,” akamalizia kwa kutabasamu. Mrs Garett naye akatabasamu.
.
.
“Nitashukuru sana mambo yatakapotulia.”
“Usijali. Kila kitu kitakuwa sawa. Ngoja padri Alfonso akija leo tuone nini kitatokea. Naamini atatusaidia.”
.
.
Mara mlango ukafunguliwa na Brian. Alikuwa anatiririsha jasho na anahema kwa pupa. Kila mtu akamshangaa kwa namna alivyokuwa. Hakusalimu, akaenda ndani upesi, ila mara akarudi na kusema, “Akija mtu yeyote kuniulizia, sipo!”
.
.
“Kuna nini Brian?” mama akauliza. Swali hilo lilimkutia Brian akiwa koridoni anazama ndani ya chumba chake. Alikuwa yu harakani mno. Mama hakuhangaika naye, wakaendelea na mambo yao.
.
.
Muda nao ukaenda mpaka kufikia jua kuzama na ilhali hakuna yeyote aliyekuja kumuulizia Brian. Ikiwa inaelekea majira ya saa mbili na nusu usiku, Padri Alfonso na dada Magdalena wakafika hapo nyumbani. Walikuwa wamekawia kwasababu ya kutingwa na shughuli fulani fulani za huduma huko kanisani.
.
.
Padri Alfonso alikuwa amevalia joho jeupe. Dada Magdalena amevalia gauni jeusi na kiremba cheupe, shingoni amebebelea rozari.
.
.
“Karibuni sana!” Mama Brian akasema kwa tabasamu pana akiwapa mkono wageni wake. “Nimefurahi sana mpo hapa. Najua mmeacha kazi zenu lukuki kuja kutuhudumia.” Hakika wanawake hawa wakafurahi sana. Ila si kwa Olivia. Yeye alikuwa ameketi kwa mbali, macho yake yakibeba hofu. Alikuwa anawatazama Padri Alfonso na dada Magdalena kana kwamba vinyago vitishavyo. Hakuwa na amani.
.
.
“Mngependelea chai?” akauliza Mama Brian.
.
.
“Hapana.” Padri Alfonso akatikisa kichwa. “Tunashukuru. Muda umeenda, nadhani tungeendelea tu na huduma yetu.”
.
.
“Olivia!” Mama Brian akaita. “Kamwite Brian aje sebuleni.”
.
.
Olivia akasimama na kwenda. Punde kidogo akarudi na Brian ambaye alisalimu na kisha kuketi. Aliketi karibu na Olivia, kochi moja.
.
.
Basi kidogo maongezi yakachukua nafasi mama akimtambulisha Brian na kutoa historia kidogo ya familia yake. Wakati huo Brian akatambua ya kuwa Olivia hakuwa sawa. Alikuwa anahofia. Macho yake yalikuwa yanamtazama padri Alfonso.
.
.
Brian akajaribu kutazama kile akitazamacho Olivia. Ilikuwa ni kwenye pindo la mfuko wa joho la padri. Hapo alipotazama vema, akaona kitu kama damu kwa ndani ya mfuko. Akapata shaka.
.
.
Akiwa kwenye hilo ombwe, mara mlango ukagongwa. Na sauti kavu ya kizee ikasema, “Hodi!”
.
.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 20*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Brian akajaribu kutazama kile akitazamacho Olivia. Ilikuwa ni kwenye pindo la mfuko wa joho la padri. Hapo alipotazama vema, akaona kitu kama damu kwa ndani ya mfuko. Akapata shaka.
.
.
Akiwa kwenye hilo ombwe, mara mlango ukagongwa. Na sauti kavu ya kizee ikasema, “Hodi!”
.
.
ENDELEA
.
.
Brian akatoa macho kwa mshangao. Aliogopa. Alihisi hiyo hodi haitomtendea jema.
.
.
“Brian, kafungue mlango,” mama akamwamuru. Brian akasita. Alimtazama mama yake kwa sekunde chache kisha akanyanyuka. Hata mama alihisi Brian hayupo sawa. Aliufungua mlango na uso kwa uso akakutana na Brewster!
.
.
Mzee huyo alikuwa amekodoa macho haswa. Kwenye paji lake la uso upande wa kulia alikuwa amevilia damu. Brian akamsalimu. Alikuwa anaogopa kwa namna ambavyo Brewster alivyokuwa anamtazama.
.
.
“Mama yako yupo?”
.
.
“Ndio, yupo. Karibu.”
.
.
Brewster aliingia ndani, akasalimu kila mtu. Kwakuwa kulikuwa na watu wengi humo, akaomba kuonana na mama Brian faragha. Basi Mama Brian akaomba radhi na kisha akaelekea nje pamoja na Brewster.
.
.
Huko wakakaa kwa muda wa kama dakika tano. Waliteta wakiwa hawasikiki na hata mmoja wa walioko ndani. Walipomaliza, Brewster hakurudi tena ndani hata kuaga, akaenda zake, Mama Brian akarudi ndani peke yake.
.
.
“Samahani kwa usumbufu.”
.
.
“Usijali,” akasem Padri Alfonso kisha akauliza Mama Brian akiwa anaketi kitini. “Unamjua yule mzee?”
.
.
“Aaahmm … ndio! Kiasi chake.”
.
.
Padri Alfonso akatikisa kichwa na kunyamaza asitie neno. Mama Brian akauliza, “Vipi kuna shida yoyote?”
.
.
“Ndio, ipo.”
.
.
“Ipi hiyo?”
.
.
“Watu wanasema si mtu mzuri. Hana marafiki wala mtu wa karibu. Ni mtu anayependa upweke. Mara kadhaa nimekuwa nikiletewa mashataka yake kanisani.”
.
.
“Umejuana naye lini?” Dada Magdalena akamuuliza mama Brian.
.
.
“Si muda mrefu sana.”
.
.
“Na tangu ulipojuana naye umemwona ni mtu wa namna gani? … Anakuletea habari gani?” Dada Magdalena akaendelea kuuliza. Kidogo Mama Brian akasita. Akamtazama Padri Alfonso na Dada Magdalena kisha na kusema, “Habari za kawaida tu. Hamna cha zaidi.”
.
.
“Hamna shida. Tulikuwa tuna hofu kutokana na historia yake. Nadhani sasa tunaweza kuendelea na huduma yetu,” akasema Padri Alfonso. Basi wote wakanyanyuka na kisha taa zikazimwa na kuwashwa mishumaa kwa maelekezo ya Padri.
.
.
Dada Magdalena akafukiza, na kumwagia maji maeneo mbalimbali ya nyumba. Maji ya baraka. Kisha wakafunga macho na sala ikaanza baada ya kuimba na kusema kwa pamoja vifungu kadhaa.
.
.
Wakasali kwa dakika sita mfululizo pasi na kukoma. Kwenye dakika ya saba, Brian akavutwa mkono wake wa kuume. Upesi akafungua macho na kutazama. Akamwona Olivia akiwa amejawa na hofu usoni. Macho yake yanatiririsha machozi.
.
.
“Nini, Olivia?” Brian akauliza kwa kunong’ona akitumia haswa uso wake kufikisha ujumbe. Olivia akaonyeshea koridoni. Brian kutazama hakuona kitu. “Kuna nini?” akauliza tena kwa mtindo uleule.
.
.
Olivia akatikisa kichwa. Kwa sura na mkono wake, akaonyeshea kulikuwa na kitu. Brian akamhimiza afunge macho, asitazame popote pale. Olivia akatazama tena kule koridoni kwa mashaka, kisha akafunga macho yake, Brian akafuatia.
.
.
Sala ikawa inaendelea. Baada tena ya dakika mbili, Olivia akamvuta Brian mkono. Brian akafungua macho yake kumtazama. Lakini kabla hajasema kitu, akaona mtu anaishia koridoni upesi. Olivia akanyooshea kule koridoni na kumwambia Brian kwa ishara ya kinywa, “Kuna mtu kule!” sasa hivi Brian hakuwa na haja ya kubisha kwani kwa macho yake alishuhudia.
.
.
Alikuwa nani yule?
.
.
“Kuna mtu kule!” Olivia alisema akiwa anachuruza machozi. Sauti yake ilikuwa inasikika kwa chini maana alikuwa ananong’ona. Basi Brian akatoka pale eneo la sala na kwenda koridoni kutazama. Alirusha macho yake, hakuona kitu! Ila mlango wa chumba chake ulikuwa wazi. Ulikuwa unachezacheza kuashiria umeguswa.
.
.
Akawaza. Mtu yule amekimbilia chumbani mwake? Basi akaanza kuchukua hatua kwenda huko kutazama. Olivia alikuwa anamtazama kwa hofu, ni kama vile alikuwa anataka kumzuia asifanye hilo.
.
.
Brian akasonga. Kulikuwa ni giza, ila kwakuwa nyumba za jirani na huko nje taa zilikuwa zinawaka, basi akaweza kuona akanyagapo. Taratibu akasonga na kusonga. Alipofikia mlangoni, akatazama ndani ya chumba chake. Hakuwa anaona jambo.
.
.
Akasonga kuzama ndani. Alikuwa ana hofu. Alikuwa anatembea kwa tahadhari macho yake akiyatupa kule na kule. Alipodumbukia kabisa ndani ya chumba, akasikia sauti ya kishindo cha mguu. Akapatwa na woga. Kutazama mlangoni alikuwa ni Olivia.
.
.
“Olivia, rudi sebuleni!” Brian akamwambia kwa kunong’ona. Olivia akatikisa kichwa na kusema, “yupo kule!”
.
.
“Wapi?” Brian akauliza.
.
.
“Jikoni!” Olivia akajibu akionyeshea kidole. Basi Brian, upesi, akatoka na kwenda jikoni akiongozana na Olivia. Walipofika huko hawakukuta kitu.
.
.
“Hamna kitu, Olivia.”
.
.
“Nilimwona! Alinichungulia na kisha akakimbilia huko!”
.
.
Brian akashusha pumzi ndefu. “Olivia, huyo mtu hataki tuwepo kwenye sala. Anatusumbua tusishiriki huduma. Turudi kwenye maombi na sasa tusitazame wala kuhangaika naye.”
.
.
Olivia akajibu kwa kumeza mate. Brian akautwaa mkono wake na kumrudisha sebuleni lakini binti huyo akitazamatazama huko nyuma, pembeni na kule aelekeapo.
.
.
Wakajiunga na sala. Wakafunga macho yao kwanguvu wakitulia. Kheri wale waliowaacha hawakutambua kama waliondoka. Au labda walitambua wakanyamaza.
.
.
Sala, kama walivyoiacha, ikaendelea. Sasa hivi wakadumu kwa dakika moja tu, na mara Brian akaanza kuhisi upepo kana kwamba wapo nje ya jengo. Akakunja uso wake kwa maulizo, ila hakufungua macho yake. Punde, sauti ya sala ikakoma!
.
.
Brian akiwa amefumba macho yake, yu gizani, akajitahidi kuskiza asisikie kitu. Muda kidogo akasikia sauti ya Olivia ikimwita! Akafungua macho kutazama, akamwona Olivia akiwa kando yake. Ila hawakuwa ndani bali nje! Kiza. Kimya.
.
.
“Olivia tuko wapi hapa?” Brian akauliza akitazama kila pande yake. Wote walikuwa wamejawa na hofu. Olivia alikuwa anachuruza machozi lukuki hata kunena hawezi.
.
.
Kutazama vema, wakagundua eneo walilopo ni la kanisa. Hapo palikuwa ni uwanjani. Hatua kama ishirini na nne mbele upande wao wa kaskazini kulikuwa na jengo kubwa la kanisa la Boston!
.
.
Wamefikaje hapa?
.
.
“Brian!” Olivia akaita. Akanyooshea kidole chake upande wa mashariki, huko, kwa mbali, Brian akamwona mtu akiwa amevalia nguo nyeupe. Mrefu, amesimama wima. Na kando ya mtu huyo, akamwona mwingine kama kivuli, ila kichwa chenye kiremba cheupe!
.
.
Punde watu hao wakaanza kuwasogelea! Mwendo wao ulikuwa ni kana kwamba watu wasio na maungio ama wamevunjika mifupa lakini wakitaka tu kutembea! Waliogofya. Na japo walikuwa mbali, macho yalikuwa yanang’aa kama taa ama paka awapo gizani.
.
.
“Kimbia!” Brian akaropoka. Upesi wakaanza kukimbia na Olivia kuelekea kule kanisani. Hawakuwa wanaona majengo mengine yoyote zaidi ya kanisa. Mbali na jengo hilo kulikuwa na misitu tu ikiwa imewazingira!
.
.
Wakakimbia kwa kasi na kukomea kwenye lango la kanisa. Wakajaribu kulifungua, haikuwezekana. Lilikuwa limetiwa ‘lock’, basi haraka wakaachana nalo na kuuendea mlango mwingine mdogo. Wakaujaribu, huo ukafunguka.
.
.
Wakazama ndani upesi na kuurejeshea. Wakiwa wanahema kwa pupa, macho yamewatoka, wakapata tulizo ya kuwa huenda sasa wakawa salama. Ila punde wakapata hisia tofauti! Ni kama baada ya sekunde sita tangu kuingia humo. Walihisi hawakuwa wenyewe, kuna watu wengine zaidi ya wao ndani ya jengo.
.
.
Kutazama kwenye ukumbi wa kanisa, vitini, kulikuwa na watu wameketi. Na walipotazama madhabauni, kulikuwa na padri, Padri Alfonso, akiongoza misa.
.
.
Nyuso za watu wote hawa hazikuwa za watu wa kawaida. Zilikuwa ni nyuso nyeupe zilizojawa na michirizi meusi kana kwamba vijito vya mito. Midomo meusi. Macho ya njano na nyekundu yaliyokuwa yanawatazama watu walioharibu misa yao, Brian na Olivia!
.
.
Kwa muda kidogo Brian akakosa la kufanya. Olivia akalia kwa hofu. Waliona huo ndiyo mwisho wa maisha yao. Waumini wote wakasimama na wakiongozwa na Padri Alfonso na Dada Magdalena wakawasogelea Brian na Olivia ambao hawakuwa na mahali pengine pa kukimbilia. Walijaribu kufungua mlango pasipo mafanikio.
.
.
Waliwapowasogelea kabisa, wakasimama wote na kusema kwa pamoja, “Unaona nini Brian?” kisha wakanyoosha mikono yao kuwadaka.
.
.
Brian na Olivia wakapiga kelele kali. Wakawashtua watu wote waliokuwepo kwenye sala. Wote wakakoma kusali na kuwatazama kwa mshangao.
.
.
“Brian! Olivia! Mmekumbwa na nini?” mama Brian akauliza. Brian kabla hajajibu kitu, akarusha macho yake kwa Padri Alfonso na Dada Magdalena. Dada Magdalena akatabasamu.
.
.
.
.
****
 
Dah hatujaona mazingaombwe na bi jasmine...ba Hamil nae roho mbaya tu
 
Steve big up simulizi nzuri.Ungechanganya na nyingine ya kikachero tuwe tunapiga double double mkuu!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom