*ROHO YAKE INADAI --- 04*
*Simulizi za Series za Steve*
ILIPOISHIA
“Lipi hilo?” Dkt akauliza. Brian akamtajia yale maneno aliyoyasoma toka kwenye kingo ya kitanda cha Faris. Dkt akamuuliza akimkazia macho, “Umeyaona wapi hayo maneno?”
ENDELEA
Brian akafikiria kidogo. Pengine hakuona tabu yoyote kuhusu hayo maneno lakini muitikio wa Dkt Hamill ukamfanya apate mashaka. Dkt aliyekuwa katika mpango wa kuondoka, akarejea na kusimama mbele ya Brian kungoja majibu.
“Niliona tu mahali,” akajibu Brian. Hakutaka kusema uhalisia kwa kuhofia pengine anaweza kujikuta amemwingiza Faris na familia yake kwenye matatizo.
Dkt akaketi juu ya meza, kisha akauliza kwa sauti ya upole, “Unaitwa nani kijana?”
“Brian Woodgate.”
“Brian,” Dkt akaita. Alikuwa anamtazama Brian kwa macho ya umakini. “Kuwa muwazi, sawa? Sina mpango wa kukudhuru bali kukusaidia … umeyaona wapi hayo maneno?”
“Kwenye kitabu,” Brian akajibu.
“Hakuna maneno hayo kwenye kitabu changu,” akasema Dkt Hamill.
“Si kwenye kitabu chako,” Brian akajitetea. “Ni kitabu kingine kabisa nilichokutana nacho kule maktaba.”
“Una uhakika?” Dkt akauliza akifinya ndita.
“Ndio,” Brian akajibu akitazama chini. Dkt akatazama saa yake ya mkononi kisha akanyanyuka na kusema, “Muda wangu wa kuwapo hapa umekwisha. Nina kazi nyingi za kufanya nyumbani kwangu. Kama hutojali, kesho majira ya saa tano asubuhi, ufike ofisini, tutaongea mambo kadhaa.”
Dkt akaondoka zake na kumwacha Brian akiwa mpweke darasani. Akiwa na mawazo kadhaa juu ya maneno yale ya Faris na namna ambavyo Dkt alivyoyapokea. Naye hakudumu muda, akaweka begi lake mgongoni na kwenda zake nyumbani.
**
Saa mbili usiku …
Brian alikuwa na mama yake sebuleni mahali pa kupatia chakula. Mbali na sauti ndogo ya redio iliyokuwa inasikika kwa mbali, hakukuwa na sauti nyingine kubwa zaidi ya midomo inayotafuna.
Walipomaliza kula, mama alitoa vyombo, na kabla Brian hajaondoka mama akamweleza kuwa kuna jambo anataka kuongea naye, basi akangoja kitini wakati mama anamalizia kazi kadhaa jikoni. Kichwani mwake akijaribu kubashiri ni kitu gani ambacho mama anataka kumweleza.
Hapa akajikuta akili yake yote inakimbilia kwa Wayde. Pengine baba wa binti huyo atakuwa amekuja kumweleza mama yake kuhusu mahusiano yao. Kidogo akapata shaka, akapanga namna ya kulikabili hilo endapo mama yake atakapomhabarisha.
Ni hivi, yeye hajui lolote kuhusiana na hilo jambo, anasingiziwa tu, akapanga vivyo.
“Brian,” mama akaita akiketi. Alimtazama Brian katika namna ambayo ilimfanya ajue kuna mushkeli kwenye kauli ijayo.
“Jana usiku ulikwenda wapi?” mama akauliza, na kabla Brian hajajibu akatahadharisha, “Usijaribu kuniongopea chochote, Brian. Ni kwa ajili yako.”
Brian akapatishwa shaka na kauli ya mama yake. Hapa akawa njia panda kujua ni kipi haswa mama yake anakiongelea, kwenda kule kwa wakina Faris ama kwenye tafrija pamoja na wakina Wayde? Kutaka kujua hilo, akauliza, “Kwani kuna nini, mama?”
“Brian, nimekuuliza,” mama akapandisha sauti. “Nahitaji majibu na si maswali.”
“Nilienda kutembelea familia ya Garett!”
“Alafu?”
“Nikaenda kwenye tafrija ya kumbukumbu ya kuzaliwa ya mwanafunzi mwenzetu.”
“Ukiwa na nani?”
Hapa Brian akaanza kuhakikisha kuwa mawazo yake ya awali yalikuwa sahihi. Wanaenda kujadili lile swala la Wayde, mtoto wa seneta.
“Nikiwa na marafiki zangu … watu ninaosoma nao darasa moja! Kuna ubaya kwenye hilo?”
“Alafu ulipotoka hapo ukaenda wapi?”
Hapa Brian akapata shaka, pengine alivyokuwa anawaza sivyo. Akajiuliza zaidi ni nini mama yake anajua kabla hajafungua mdomo wake aidha kuongopa ama kusema ukweli.
“Tulipotoka hapo tukarudi nyumbani,” akajibu. “Hivyo ndivyo ilivyokuwa, hamna cha ziada.”
Mama akanyamaza akimtazama kwa sekunde kadhaa kisha akamuuliza, “Haukwenda kwa wakina Faris?”
Moyo wa Faris ukaruka pigo. Akahisi mstari wa baridi umempitia mwilini kwa wepesi. Mama amejuaje hilo?
“Brian,” mama akaita. Akashusha pumzi ndefu na kutikisa kichwa chake taratibu. “Wewe ni mwanangu wa pekee, sina mtoto mwingine yeyote yule. Tangu baba yako alipofariki, wewe ndiye familia pekee niliyobaki nayo. Sitaki kukupoteza.”
“Kivipi?” Brian akauliza.
“Sitaki maswali, Brian!” mama akafoka. “Kuanzia leo hii sitaki kukusikia wala kukuona ukienda kwa Garett tena. Sitaki kusikia ukienda kwa wakina Faris pia. Tumeelewana?”
Mama alikuwa amebadilika rangi. Uso wake ulikuwa unatisha. Macho yake yalikuwa mekundu yamekodoa.
“Sawa, mama,” Brian akajibu kwa hofu. Mama akanyanyuka na kwenda zake chumbani akitembea upesi na kwa hasira. Alimwacha Brian akiwa na maswali, mama amejuaje kama alienda kwa wakina Faris?
Aliwaza sana lakini hakupata jibu. Alijaribu kutengeneza kichwani namna ambavyo mama yake aling’amua safari hiyo, akashindwa. Akaona ni stara, siku ambapo mama yake atakuwa amepungukiwa na hasira, amuulize apate kujua.
Basi akaendaze kulala.
Baadae katikati ya usiku, kwenye majira ya saa nane ya saa yako, akasikia mlango wa chumba chake ukigongwa. Akafungua macho na kuweka shuka kando, akajiuliza kwa muda mfupi kabla hajapaza sauti,
“Nani? - mama?” Hakukuwa na majibu. Hodi ikagongwa tena. Basi akanyanyuka na kwenda mlangoni kufungua. Hakuona mtu. Alitazama kushoto na kulia, patupu! Kabla hajatoka hapo mlangoni, akasikia tena hodi nyingine. Akashangaa!
Alitega sikio lake kwa umakini, akagundua hodi hiyo ilikuwa inatokea kwenye mlango wa sebule. Akakunja ndita za mashaka, lakini akapata hamu ya kujua. Akanyanyua nyayo zake kuuendea mlango … alitembea taratibu, hakukuwa na vishindo vyovyote … sakafu yao ya mbao ilikuwa ya baridi … aliufungua mlango kwa upole na kutupa macho nje.
Hakukuwa na mtu. Akaufungua mlango zaidi kutazama. Alitupa macho yake upande wa maghariki. Barabara ilikuwa pweke na upepo wa baridi ulikuwa unapuliza. Nyumba zote zilikuwa kimya. Hakukuwa na sauti ya kitu chochote isipokuwa ya matawi ya miti punde yakipulizwa na pepo.
Alipotazama upande wa mashariki, moyo wake ukapiga fundo kubwa. Kwa mbali alimwona mtoto mdogo wa kike akiwa amesimama katikati ya barabara. Mtoto huyu alikuwa kwa umbali wa hatua thelathini toka kwenye nyumba yao. Alikuwa amevalia gauni jeupe linalokomea juu ya magoti, mkononi akiwa amebebelea mdoli.
Moyo wa Brian ukaanza kwenda upesi.
“Kecie! …” akajikuta anatamka. “Kecie, ni wewe?” alikuwa anauliza kwa sauti ya chini kana kwamba mtoto yule yupo kando yake. Bado kichwa chake hakikuwa sawa. Alikuwa anawaza ni nini anachokiona mbele yake. Ni jinamizi ama mzimu?
“Kecie!” akaendelea kuteta, sasa akitoka nje ya mlango. “Ni wewe, Kecie? … ni wewe kweli?”
Akapiga hatua mbili kuuacha mlango, macho yake yakimtazama yule mtoto amwonaye. Kwakuwa alikuwa mbali na kulikuwa kiza barabarani, hakupata kumwona uso wake vema. Ila yule mdoli, lile gauni, lilikuwa kweli ni la Kecie.
Brian hakuwa na kumbukumbu kiasi hicho cha kuweza kukumbuka sawasawa kitu kilichopita miaka kumi, ila ndani ya chumba chake kuna matangazo yote ya kutafutwa kwa Kecie. Matangazo yaliyokuwa yanaelezea ni nini Kecie alivaa siku anapotea.
Basi akaendelea kupiga hatua kumfuata yule mtoto, sasa hatua tano toka mlangoni. Ila mara, kwa mbali, akasikia sauti ya kike inamwita. … Briaaan! … Briaaan! … kana kwamba mtu yupo ndani ya chungu.
Lakini kabla hajaitikia sauti hiyo, kwa macho yake, akashuhudia yule mtoto akigeuka na kuanza kwenda zake. Akapaza sauti kumwita. Mtoto hakusikia, akaendelea kwenda zake. Mara mtoto huyo akaanza kukimbia. Brian akiwa anashuhudia, japo kwa uhafifu wa uwezo wake wa macho, akamwona yule mtoto amesimama ghafla, na alipofinya macho yake kumtazama kwa umakini, akagundua kuna mtu pembezoni yake. Na mara mtu huyo akaanza kuondoka naye wakitokomea gizani!
Alijitahidi kumtazama mtu huyo, hakubahatika kabisa kumwona. Alikuwa mweusi kufanana na giza. Akataka kuwafuata, ila aliponyanyua mguu, akahisi amedakwa mkono wake wa kuume, akavutwa kwanguvu!
“Brian!” Kutazama alikuwa ni mama yake. Akatazama kule alipomwona mtoto, hakukuwa na kitu. Taa zilikuwa zinamulika barabara iliyokuwa nyeupe pe.
“Brian, nini shida?” Mama akauliza. Bado Brian alikuwa haelewi kinachoendelea. Hakuwa anajua hata cha kusema. Basi mama akamrejesha ndani na kisha akaufunga mlango.
“Brian!” mama akaita, na kuuliza, “Umeanza lini kuota ukiwa unatembea?”
Kumbe yale yote ambayo Brian alikuwa anayafanya alikuwa usingizini. Lakini akiwa katika hali hiyo, akafungua mlango na kwenda mpaka nje ya nyumba.
Akamweleza mama yake kilichojiri, nini aliona na kusikia.
“Unafikiri mno kuhusu Kecie … Kalale, Brian. Tutaongea kesho.” mama yake akambusu kwenye paji la uso na kisha akaenda zake chumbani kulala. Brian naye akanyanyuka na kwenda kujitupia kitandani mwake bado akiwa na hofu. Aliwaza sana juu ya kile alichokiona. Kilimnyima raha na kumpatia maswali mengi ambayo hakuona dalili ya kupatia ufumbuzi.
Ila akiwa hapo, anajibuabidua kutafuta usingizi, akatazama dirishani na kuona kitu. Kulikuwa kuna maandishi kwenye kioo cha dirisha. Alisonga kwa ukaribu na kutazama vema. Ni kweli alichokiona. Kulikuwa na maandishi yaloandikwa kwa herufi kwa kutumia kidole dhidi ya unyevu uliojishika kiooni.
‘NIOKOE, BRIAN’
Maandishi yalisomeka vivyo.
***