Simulizi: Roho yake inadai

Simulizi: Roho yake inadai

*ROHO YAKE INADAI --- 10*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Akaanza kupiga hatua kumsogelea Olivia. Hatua zake zilikuwa nzito kinyume kabisa na mwili wake. Kila alipokanyaga chini ilisikika tih! Tih! Tih!

Olivia akajawa na woga mkubwa, akapiga kelele kali sana na kumshtua kila mtu!
.
.
ENDELEA
.
.
Kila mtu akaangaza. Hawakuona jambo. Wakamtazama Olivia na kumuuliza nini kimemsibu. Olivia akanyooshea mkono wake mlangoni.
.
.
“Ni nini, Olivia?” mama akauliza kwa ukali kidogo.
.
.
“Nimemwona mtu, mama. Nimemwona mtu mama!” akalia Olivia.
.
.
“Umemwona wapi?” akauliza mama akiangaza macho yake. Olivia akaendelea kunyooshea mkono wake mlangoni. Macho yake yalikuwa yanatema machozi. Uso wake umejawa na mashaka tele.
.
.
“Nimemwona pale mlangoni. Mtoto mdogo mwenye mdoli mkononi!”
.
.
Mama akashika mdomo wake. Akamtazama Padri Alfonso na dada Magdalena.
.
.
“Usijali, Mrs Garett,” akasema Padri. Akainama na kumshika mikono Olivia. Akamtazama kwa macho ya upole na tabasamu kwa mbali. “Mtoto mzuri Olivia, usiogope. Sawa? Sasa hivi tukienda kusali, usifumbue macho yako mpaka tutakapomaliza. Umesikia?”
.
.
Olivia akatikisa kichwa kukubali aliachoambiwa. Bado macho yake yalikuwa yanatoa machozi na uso wake ukisema hofu. Padri akamfuta machozi kwa vidole vyake kisha akambusu kwenye paji lake la uso. Akamkumbusha tena, “usifungue macho yako.”
.
.
Basi baada ya kumwambia hivyo, Padri akamtazama Dada Magdalena na kumpatia ishara ya kichwa. Dada huyo akachovya mkono wake kwenye maji na kukung’utia kule ambapo Olivia alisema amemwona mtu. Alipomaliza akajumuika na wenzake na kuanza kusali upya.
.
.
Zikapita dakika nne za sala. Watu wote walikuwa wamefumba macho yao. Ni sauti tu ya padri ndiyo ilikuwa inasikika hapa. Na mbali na mishumaa ile iliyokuwa imewekwa pale mezani, hakukuwa na chanzo kingine cha mwanga humu ndani.
.
.
Katika dakika hiyo nne ya sala, Olivia ambaye alikuwa ameyafumba macho yake kwanguvu akaanza kuhisi kitu. Alihisi kuna mtu anatembea akitokea kule koridoni kuja sebuleni. Akaogopa sana. Alinyamaza kimya na akijitahidi kutoyafungua macho yake kama alivyoelekezwa, lakini sikio lake la kushoto bado likaendelea kumfanya ahofie zaidi na zaidi.
.
.
Vishindo vya mtu vilikuwa vinasikika vikifika sebuleni, na kisha vinafifia kwenda koridoni. Vinakuja tena na tena vinarudi kwenda koridoni. Zoezi hili lilijirdia mara tatu. Mara ya nne, vishindo vya miguu vilipokuja sebuleni havikurudi tena koridoni. Vikabakia palepale sebuleni!
.
.
Hapa Olivia akahisi kubanwa na mkojo. Mwili wake ulisisimkwa sana. Alihisi baridi la ajabu linampitia na kila kinyweleo kilichopo kwenye mwili wake kimemsimama! Alitamani kukimbia. Alitamani kukaa. Alitamani kulia, alitamani kunyamaza. Alijikuta anatamani kila kitu!
.
.
Ila kwa muda kidogo akahisi kimya. Hakusikia tena vishindo vya mtu na basi akapata angalau ahueni. Huenda mtu huyo atakuwa ameondoshwa na maombi. Akatamani kufungua macho yake atazame, ila akaogopa. Aliona ni kheri asifumbue macho hayo kama alivyoelekezwa kwani anaweza kuona mambo atayoshindwa kuyastahimili.
.
.
Akaendelea na zoezi lake. Ila baada ya dakika moja, akaanza kusikia tena vishindo vile vya binadamu! Moyo wake ukaanza kupiga makasi. Ubaya ni kwamba vishindo hivyo vilikuwa vinamjongea! Na vilipomfikia karibu kabisa vikasimama. Kwa mbali sauti ya kike ikaita,
.
.
“Oliviiaaa …”
.
.
Sauti hii ilikuwa mithili ya upepo. Ilikuwa ni ya baridi sana. Ilipofika kwenye sikio la Olivia ilimfanya mtoto huyo ahisi baridi kali sikioni na shingoni. Alitamani kupiga kelele, lakini akajizuia. Ilihitaji moyo mkubwa sana kuvumilia haya.
.
.
“Oliviaaaa … amka, amka! … Oliviaaaa … amka! Njoo uone mchezo mzuri kule msituni, kweli utafurahia! …” sauti ya baridi ilipulizia sikioni mwa Olivia.
.
.
“Najua unataka kuuona … njoo, twende Oliviaa … twende upesi!”
.
.
Olivia akajitahidi sana kujikaza. Hakufungua macho yake kumwona mtu huyo anayemwongelesha, wala hakumjibu. Alikuwa amefunga tu macho na kinywa chake japo anahofia sana.
.
.
Basi baada ya mtu huyo kuona Olivia hasikii, akamsogelea karibu zaidi na kuanza kumshika! Kiganja chake cha baridi kilipapasa mkono wa Olivia, ukapandisha mpaka shingoni mwake. Ukapapasapapasa shingo ya Olivia, na kisha ukadumbukia mgongoni mwa mtoto huyo na kuendelea kumpapasapapasa!
.
.
Hapa Olivia akashindwa kubana mkojo, akajikuta analowanisha mapaja yake kwa woga. Akatetemeka kwa hofu kupita kiasi, na kama zoezi hili lingeendelea kama kwa dakika mbili mbele, Olivia angepiga kelele na kufumbua macho, ila bahati likakoma na akabaki salama!
.
.
Akahema kwanguvu. Akatazama kushoto na kulia, hakuhisi kitu. Akaendelea kuhema kwanguvu moyo wake nao ukipiga kwanguvu kwenda pole. Ikapita dakika moja kukiwa kimya.
.
.
Ikapita dakika ya pili kukiwa kimya.
.
.
Ikapita dakika ya tatu kukiwa kimya.
.
.
Kwenye dakika ya nne Olivia akaanza kusikia kitu ambacho kilimshangaza. Si vishindo vya mtu wala kiganja kikimpapasa, bali sauti ya Padri Alfonso na Dada Magdalena. Watu hao walikuwa wanateta na kucheka. Wanagonga mikono yao na pia kulia!
.
.
Olivia akaachama mdomo wake kwa kustaajabu. Hakuwa anaamini alichokuwa anasikia. Padri Alfonso na Dada Magdalena! Haiwezekani! Akatikisa kichwa chake. Hapana. Akatikisa kichwa chake. Hapana. Alikuwa haamini kitu alichokuwa anasikia. Alfonso na Magdalena walikuwa wanasali, ndivyo alivyokuwa anaamini na si vinginevyo.
.
.
Lakini masikio yake yalikuwa yanamwambia tofauti. Padri Alfonso na Dada Magdalena walikuwa wakipanga kuwamaliza. Alfonso na Magdalena walikuwa wanapanga kuwatupia kule msituni! Na walipoelezana hayo wakawa wanacheka kwanguvu. Wanacheka kishetani!
.
.
Olivia akafungua macho yake kwa mbali apate kutazama kama ni kweli alichokuwa anasikia. Alishindwa kuvumilia. Alitaka kushushudia namna ambavyo Padri na Dada walivyokuwa wanapanga madhalimu juu yao.
.
.
Alichokiona kikamtisha, na kikamfanya afungue macho kwa nguvu kukodoa asiamini. Alimwona Padri Alfonso akiwa na uso mweusi, macho mekundu yenye mboni mithili ya mbuzi, meno makali yaliyochongoka, masikio marefu na ulimi mrefu mwembamba.
.
.
Dada Magdalena alikuwa na uso mweupe pe wenye michirizi meusi. Macho yake yalikuwa mekundu na makubwa. Mdomo wake ulikuwa mweusi kana kwamba kunguru. Meno yake yalikuwa yamekaa hovyo na yenye rangi ya kuoza.
.
.
Punde Olivia alipokodoa macho yake, Padri Alfonso na Dada Magdalena wakamtazama wakiwa wamekodoa. Nyuso zao zilikuwa zimesimama tuli kana kwamba zimegandishwa. Mara ghafla shingo zao zikaanza kupinda na kupeleka vichwa vyao kushoto, kulia, juu na chini! Kushoto, kulia, juu na chini!
.
.
Olivia akamtazama mama yake kwa hofu. Mama alikuwa amefumba macho hajui kinachoendelea. Olivia akamwita na kumwita. Akamvuta mkono na kumtikisatikisa ila wapi! Mama hakufungua macho wala kumtazama.
.
.
Basi padri Alfonso na Dada Magdalena wakaanza kumjongea. Olivia akamvuta mamaye kwanguvu sana kumwamsha aone, ila jitihada zake hazikuzaa matunda. Mama alikuwa kwenye usingizi mzito sana. Ni kana kwamba ametiliwa kiasi kingi cha madawa ya kulevya!
.
.
Padri Alfonso na Dada Magdalena wakazidi kumsogelea Olivia wakitembea kama watu wasiokuwa na mifupa, wakijikunjakunja , wakijipindapinda, wakijikunjakunja na wakijipindapinda. Wakitazama kana kwamba watu wasiokuwa na kope.
.
.
Mdomo wa Padri Alfonso ukaanza kuchuruza damu iliyofika kidevuni mwake na kudondokea chini. Macho ya Dada Magdalena nayo yakaanza kuvuja damu, ikipita mashavuni mwake na kudondokea chini.
.
.
Walipomkaribia Olivia wakakunjua mikono yao yenye vidole vyembamba na kucha ndefu wakitaka kumyaka binti huyo. Olivia akapiga kelele kali sana akimkumbatia mama yake kwanguvu. Mara mama akafungua macho na kumtazama, “Una nini Olivia?”
.
.
Olivia akamtazama mama yake akiwa anahema kwa hofu, akamnyooshea kidole upande wa Padri Alfonso na Dada Magdalena.
.
.
“Kuna nini?” mama akauliza. Hakuwa anaona kitu. Hakukuwa na kitu. Padri Alfonso na Dada Magdalena nao wakaduwaa wakimtazama. Wote walikuwa kwenye hali yao ya kawaida.
.
.
“Nini, Olivia?” Padri Alfonso akauliza akimjongea mtoto huyo. Olivia akapiga kelele kali na kukimbilia nyuma ya mgongo wa mama yake kujificha. Akalia sana.
.
.
“Olivia,” Padri akaita. “Olivia, ulifungua macho?” akauliza kwa sauti ya chini akijaribu kumtazama binti huyo, ila Olivia hakutaka kabisa kumtazama Padri. Kadiri Padri alivyokua anasogea, ndivyo naye akawa anasonga mbali naye. Ila upande wa pili alipokuwa anaelekea akakutana na Dada Magdalena, naye akamuuliza, “Ulifungua macho?”
.
.
Olivia akapiga tena kelele kali. Mama akamnyanyua na kumbeba.
.
.
“Olivia, una nini?”
.
.
.
**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 11*

*Simulizi za series za Steve*


ILIPOISHIA
.
.
“Olivia,” Padri akaita. “Olivia, ulifungua macho?” akauliza kwa sauti ya chini akijaribu kumtazama binti huyo, ila Olivia hakutaka kabisa kumtazama Padri. Kadiri Padri alivyokua anasogea, ndivyo naye akawa anasonga mbali naye. Ila upande wa pili alipokuwa anaelekea akakutana na Dada Magdalena, naye akamuuliza, “Ulifungua macho?”
.
.
Olivia akapiga tena kelele kali. Mama akamnyanyua na kumbeba.
.
.
“Olivia, una nini?”
.
.
ENDELEA
.
.
Olivia akamtazama mama yake na kumwambia kuwa Padri Alfonso na Dada Magdalena ni watu wa ajabu. Ameona kwa macho yake na akasikia kwa masikio yake wakipanga kuwaua na kwenda kuwatupia msituni.
.
.
Mama akastaajabu. Akamwona Olivia amechanganyikiwa. Akajaribu kumtuliza na kumwambia alichokiona ni ndoto ama maruweruwe tu, si uhalisia.
.
.
“Hapana!” Olivia akatikisa kichwa akilia. “Ni majini, mama! Ni majini!” Olivia akafoka. Padri Alfonso akatazamana na Dada Magdalena kwa macho ya mshangao. Walikuwa wanajiuliza ni nini kimemtokea binti yule kiasi cha kuropokwa namna hiyo.
.
.
Lakini kila Padri Alfonso alipotaka kumjongea Olivia kumtuliza na kumsihi, Olivia akapiga kelele. Hakutaka mwanaume huyo amsogelee hata kidogo. Alimwogopa mno kama ukoma. Ikafikia kipindi mama ikambidi aende na Olivia chumbani.
.
.
“Tulia hapa, sawa?” mama alimweka Olivia kitandani. “Hautaona wala kuhisi chochote. Sisi tutaendelea na kusali na tutakapomaliza, nitakuja kulala na wewe, sawa Olivia?”
.
.
Olivia alikuwa anaogopa kuachwa mwenyewe, ila aliona ni kheri kuliko kwenda kule sebuleni kumwona Padri Alfonso na Dada Magdalena, basi akakubali japo kwa shingo upande.
.
.
“Hatutachukua muda mrefu,” alisema mama, Mrs Garett, kabla hajambusu Olivia kwenye paji lake la uso na kwenda zake. Kwa nje akaufunga mlango. Olivia akabaki mwenyewe akiwa amejilaza na kuukumbatia mto alioufinya kwanguvu.
.
.
Baada ya muda kidogo, akasikia sauti ya sala ikiwa inaendelea. Akiwa ametulia tuli, akawa anasikia kila kitu na kila jambo. Akafunga macho yake akitamani alale. Alitaka kutoka kwenye ulimwengu wake wa ufahamu kwa kuhofia pengine anaweza kuona mambo ambayo hataki kuyaona.
.
.
Basi baada ya jitihada zake hizo, usingizi mwepesi ukamsomba na kumpatia amani ya muda. Na amani hii ikawa upande wake mpaka sala ilipokwisha.
.
.
“Nashukuru sana,” Mrs Garett alimpatia Padri mkono wa shukrani. “Natumai hii haitakuwa mara yenu ya mwisho kuja hapa.”
.
.
“Usijali,” akasema Padri Alfonso akitabasamu. “Tumetumwa kazi hii, nitajitahidi kukusaidia kwa kadiri niwezavyo, Mrs Garett.”
.
.
Basi Mrs Garett akawasindikiza Padri Alfonso na Dada Magdalena mpaka nje ya nyumba yake na hatua kadhaa chache kisha akasimama akiwatazama wakitokomea.
.
.
Alipojiridhisha akarudi zake ndani na kwenda kumwona Olivia moja kwa moja. Akamkuta amelala. Akaona si stara kumsumbua, akambusu tena kwenye paji lake la uso na kisha akaenda kuoga.
.
.
Akiwa anaoga, akili yake ikawa inawaza yale yaliyokuwa yametukia kwenye sala. Maji ya kuoga yalikuwa ya moto na hivyo kumfanya apate starehe ya aina yake kwenye kuoga haswa kwenye mazingira ya baridi kama haya.
.
.
Akili yake ikawanda na kuwanda kwa kuwaza. Kwa namna moja akajihisi atakuwa ametua mzigo wa mambo yale ya ajabuajabu yaliyokuwa yanamtokea. Alikuwa na imani sasa mambo yatakuwa shwari kabisa. Na uzuri yote yalifanyika pasipo mume wake kujua kitu.
.
.
Ila akiwa hapa anaoga na kuwaza, mara bomba yake ya ‘maji ya mvua’ ikakata akiwa bado hajajiosha kuondoa sabuni mwili mzima. Usoni alikuwa ana sabuni hivyo aliogopa kufungua macho yake kutazama.
.
.
Akapapasa bomba na kulitikisa. Akakunja uso akinung’una ni nini kimetokea. Sasa hakuwa na namna bali kuogea maji ya baridi yaliyokuwako kwenye ndoo kubwa zilizopo humo bafuni.
.
.
Ila ndoo hizo zilikuwa mbali kidogo na yeye, konani mwa bafuni, kwahiyo ilimbidi afanye namna ya kuona ili azifikie. Basi kiuvivu, akafungua macho yake kwa mbali ajue tu uelekeo kisha afuate ndoo hizo. Ajabu alipofanya hivyo, akamwona mtoto mdogo kwenye kona! Akashtuka sana. Haraka alifuta sabuni kwenye macho yake kwa kutumia mkono na kisha akakodoa kuangaza.
.
.
Hakuona mtu! Macho yakawa yanawasha kwa kuingiwa na sabuni. Haraka akafuata ndoo na kujisafisha alafu akatazama tena huku na kule. Hakukuwa na mtu.
.
.
Akajimwagia maji akiwa na hofu. Ni kweli alimwona mtu ama mawazo yake? Hakuona mtu mpaka anmaliza kuoga. Sasa alikuwa anasikia baridi maana ameogea maji hayo. Haraka akaelekea chumbani kujikausha na kuvaa nguoze.
.
.
Alipomaliza akaenda kumkuta Olivia chumbani mwake, akamkumbatia na kufunga macho alale. Kabla hajapata usingizi akawaza kuhusu kile kitu alichokiona bafuni. Hakuwa anataka kiwe kweli kabisa kwani aliamini sala waliyofanya iliondoa kila jambo.
.
.
Akalazimisha akili yake kuwa kila jambo li shwari na hana haja ya kuhofia hata kidogo. Basi akalala na kukawa shwari mpaka asubuhi yake.
.
.
Kukiwa ni majira ya saa tatu, yupo na Olivia sebuleni, wakapata mgeni mmoja, mwanaume mfupi mnene aliyekuwa amevalia sare za kampuni afanyayo kazi Mr. Garett. Mwanaume huyo alijitambulisha kwa jina la Jeff kama afisa msaidizi wa mawasiliano wa kampuni ya DOGOUT TIMBERS.
.
.
Alisema ana haraka na hatokaa hapo muda mrefu. Ila uso wake ulikuwa umejawa na simanzi, hata tabasamu zake zilikuwa za kuongopa. Alipokunywa chai kidogo aliyolazimishwa na Mrs Garett akasafisha koo na kusema, “Nina habari mbaya, samahani sana kwa hilo.”
.
.
“Mume wangu amefanyaje?” Mrs Garett akawahi kuuliza akiwa ametoa macho. Alianza kuhisi mwili wake unapata joto, moyo wake unaanza kupiga makasia.
.
.
“Tafadhali, punguza munkari,” akasema Jeff akimshika Mrs Garett mkono. “Kila jambo litakuwa sawa, hapana shaka.”
.
.
“Naomba uniambie mume wangu amekumbwa na nini?” akasisitizia Mrs
Garett. Uso wake ulibadilika na kutisha kwa umakini.
.
.
Jeff akashusha pumzi kwanza, kisha akasema, “Amepata ajali akiwa safarini …”
.
.
Mrs Garett akaziba mdomo wake kwa mshangao.
.
.
“Tunashukuru maana yu salama. Hivi tunavyoongea amelazwa hospitali kwa matibabu zaidi.”
.
.
Machozi yakaanza kumtiririka Mrs Garett. Jeff akajitahidi kumpooza na kumfariji. “Atapona, usijali. Hatukutaka kukuletea habari hizi za kukuumiza ila hatukuwa na namna nyingine. Tangu alipofika hospitali, amekuwa akisema ukamwone kila anapopata nafasi finyu ya kuongea.”
.
.
.
***
.
.
Saa nne na nusu asubuhi …
.
.
“Huyu ndiye mke wake!” alisema Jeff akimwonyeshea daktari. Uso wa Mrs Garett ulikuwa umefumwa na mashaka. Alikuwa anatetemeka sana. Daktari alimtazama kisha akanyanyuka toka kwenye kiti chake na kumwambia Mrs Garett, “twende, nifuate!”
.
.
Mrs Garett akanyanyuka na kuongozana naye mpaka chumba alimwolazwa mumewe. Akamwona mume wake akiwa amefunikwa na P.O.P karibu mwili mzima. Ni uso tu ndiyo ulikuwa wazi. Basi akahisi moyo wake umezimama. Akakabwa na kilio cha uchungu. Haraka akamsogelea mume wake akiwa anatamani kumuuliza nini kimemsibu.
.
.
“Ni ajabu akatoka hai kwenye ajali ile mbaya,” alisema Daktari akimsogelea Mrs Garett. Akamwekea mkono wake begani. “Kama alitoka kwenye gari ile iliyokuwa nyang’anyang’a, basi atatoka pia na hapa hospitali … usijali.”
.
.
Tayari macho ya Mrs Garett yalikuwa yanatoa machozi kana kwamba mto. Alimwonea huruma sana mumewe. Hakukumbuka kuwa mwanaume huyo alitoka kumpiga na kumwaribu uso hapo nyuma, alichokuwa anajali ni uhai wake tu.
.
.
“Ila,” Daktari akasema akimtazama Mrs Garett. “Mumeo amekuwa akikurupuka na kukuita kila muda. Amekuwa akitaka kukuona tangu anafika hapa. Ni mke wangu ni mke wangu kila anapofungua macho. Inaonekana anakupenda sana.”
.
.
Mrs Garett akavuta makamasi asiseme jambo. Hawakujua ni namna gani ambavyo walimpatia maswali kumwambia habari hizo. Huo upendo wa mumewe umetoka wapi? Alihisi kuna kitu mumewe anataka kumwambia.
.
.
Punde mumewe akafungua macho. Jicho lake la kushoto lilikuwa limevilia damu, la kulia ndilo lilikuwa zima ila nalo lilikuwa jekundu kwa chumvi ya machozi ya maumivu.
.
.
“Mke wangu!” Mr Garett akaita. Akataka kunyanyua mkono wake amshike mkewe ila akashindwa. Daktari akamzuia na kumtaka atulie kwani mwili wake umejawa na majeraha ya kuvunjika.
.
.
“Mke wangu!” akaita tena Mr Garett. Macho yake yalianza kumimina machozi kwa wingi.
.
.
“Nini shida?” mkewe akamsogelea kwa karibu akimtazama kwa huruma.
.
.
“Kecie,” Mr Garett akajibu kwa sauti ya chini.
.
.
“Kecie? Amefanya nini? - nini Kecie amefanya?” akauliza Mrs Garett.
.
.
“Yupo hai,” akasema Mr Garett. “Kecie yupo hai … na anataka roho zetu!” aliposema hayo akanyamaza kimya, tuli.
.
.
“Umemwona wapi Kecie?” Mrs Garett akauliza, ila mumewe akawa kimya. Mke akarudia tena swali, “Umemwonea wapi?”
.
.
Hapa ndiyo akagundua kuwa mumewe alikuwa amefariki.
.
.
.
***
 
*ROHO YAKE INADAI --- 12*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
.
.
Yupo hai,” akasema Mr Garett. “Kecie yupo hai … na anataka roho zetu!” aliposema hayo akanyamaza kimya, tuli.
.
.
“Umemwona wapi Kecie?” Mrs Garett akauliza, ila mumewe akawa kimya. Mke akarudia tena swali, “Umemwonea wapi?”
.
.
Hapa ndiyo akagundua kuwa mumewe alikuwa amefariki.
.
.
ENDELEA
.
.
Ila hakuamini, akamtazama Daktari na kumuuliza nini kimetokea? Mbona mumewe haongei? Daktari akamtoa nje na kubaki mwenyewe ndani ya chumba. Baada ya muda akatoka na kumweleza Mrs Garett kuwa mumewe alikuwa amefariki, hakuna namna bali afanye taratibu za mazishi.
.
.
Siku ikawa mbaya sana kwa Mrs Garett. Akakabwa na uchungu mkubwa kifuani mwake. Hakutaka kuamini kama mumewe amefariki, mtu aliyemjua kwa miaka nenda rudi. Ama hakika kumbe kifo ni kitu chepesi tu!
.
.
Unavyokisikia na ukubwa wake unaweza dhani kinachukua miaka kutokea, kumbe ni sekunde moja tu na habari yote hubadilika, ikiwamo na cheo cha jina lako.
.
.
Basi Mrs Garett akiwa amekabwa na kilio na asijue cha kufanya, akaketi kwenye benchi ya hospitali akilia na kulia. Muda si mrefu akaja Jeff na kumpoza. Akamwambia kampuni itafanya jitihada zote kuhakikisha Mr Garett anapumzika salama, hivyo yeye watamchukua na kumrudisha nyumbani.
.
.
.
**
.
.
.
“Nini shida yako kijana?” Karani wa shule alimuuliza Brian aliyekuwa amesimama kandokando ya mlango wa ofisi ya mkuu wa shule, Dkt Hamill.
.
.
Karani huyo alikuwa ni mwanamama aitwaye Georgina, mwanamke mnene mfupi mwenye miwani kubwa ya kumsaidia kuona.
.
.
“Nahitaji kumwona mkuu wa shule,” akasema Brian. Georgina akamtazama na kumuuliza, “una shida naye gani?” Brian akabanwa na kigugumizi. iBahati, sauti ya Dkt Hamill ikaita tokea ndani kumtaka Georgina amruhusu mvulana huyo aingie kwani ana miadi naye.
.
.
Brian akazama ndani na kusalimu kisha akasema amekuja kama ambavyo walikuwa wamepanga kuonana. Dkt Hamill alikuwa mezani akiparangana na baadhi ya mafaili, akamtaka Brian amngoje kwa dakika kadhaa kisha wataongea.
.
.
Muda huo Brian akautumia kuzungusha macho yake ndani ya ofisi ya Dkt Hamill. Kulikuwa na picha kadhaa, ikiwemo zake na za familia. Alikuwa na watoto wawili na alivyokuwa kijana alikuwa mtanashati haswa. Mbali na picha hizo, kulikuwa kuna ofisi ndogo ya karani Georgina. Kwenye meza yake kulijawa na makaratasi mengi pamoja na mashine ya zamani ya ku - ‘type’.
.
.
Brian akiwa anaendelea kukagua ofisi hii, macho yake yakaangukia dirishani na basi kutazama nje ya ofisi alipokuwa anawaona wanafunzi kadhaa wakiwa nje kwa ajili ya mapumziko.

Huko nje akiwa anatazama, kwa mbali akamwona binti mdogo ambaye hakuwa amevalia sare. Binti huyo alikuwa ameshikilia mdoli mkono wake wa kuume na gauni lake lilikuwa limekomea juu ya magoti.
.
.
Binti huyo mdogo alikuwa anatazama hapo dirishani. Ni kama vile alikuwa anamwona Brian na pia anamfanyia mazingatio. Brian akamtazama vema binti huyo. Akili yake ikamwambia ndiye mtu aliyemwona kwenye ndoto siku ile. Akili yake ikamwambia kuwa binti yule ni Kecie!
.
.
Brian akafikicha macho yake kama mtu asiyesadiki. Alipotazama tena, bado akamwona binti yule! Alikuwa amesimama kama mstimu akimtazama, ila wanafunzi wengine walikuwa wanampita kana kwamba hamna kitu. Ina maana walikuwa hawamwoni!
.
.
“Kecie!” Brian akasema kwa kunong’ona. Ajabu binti yule akatikisa kichwa chake kuitikia, na taratibu akaanza kujongea kufuata dirisha alimo Brian.
.
.
Pale alipokuwa anakutana na wanafunzi wengine, Kecie akapita kana kwamba moshi ama kivuli. Macho yake yalikuwa yanatazama dirisha na macho ya Brian pekee. Hatua zake zilikuwa za taratibu ila zinazomfikisha kwa wepesi mno!
.
.
Brian akatoa macho.
.
.
“Kecie!” akanong’ona tena akiita. Moyo wake ulikuwa unapiga kwa kasi. Alisimama afuate dirisha kumtazama Kecie. Masikioni mwake alikuwa anasikia sauti ya kunong’ona, sauti ya kike, ikisema, “Niokoe, Brian … Niokoe, Brian.” Ila kabla hajafika dirishani, akashikwa mkono na kuvutwa.
.
.
“Brian!” alipotazama akakutana uso kwa uso na Dkt Hamill. Dkt alikuwa anamtazama kwa mshangao, na pia Georgina alikuwa ameduwaa kumwangalia.
.
.
“Nini shida?” Dkt Hamill akauliza. Brian akatazama kule dirishani, hakukuwa na mtu, hata wanafunzi walikuwa tayari wamesharudi kwenye madarasa yao.
.
.
Dkt Hamill akamtazama Georgina na kumwambia, “Naomba utupishe.” Georgina alipofanya hivyo, Dkt Hamill akamkalisha Brian kwenye kiti kisha na yeye akaketi mahala pake.
.
.
“Brian, niambie ulikuwa unaona nini dirishani?”
.
.
Brian akatazama tena dirishani, kulikuwa kweupe hamna jambo. Akaurudisha uso wake kwa Dkt na kumwambia kwa sauti ya chini, “Kitu cha ajabu!”
.
.
“Brian,” Dkt akaita. Akamtazama kwa macho ya udadisi na kumuuliza, “Kecie ni nani?”
.
.
Brian akanyamaza. Bado alikuwa kwenye ombwe la mawazo. Hakuwa anajua cha kusema.
.
.
“Brian, niambie kila kitu. Acha kunificha. Nitakusaidia.”
.
.
Brian akavuta kwanza pumzi ndefu. Akatazama chini akifikiri jambo kisha akaamua kukata shauri kusema kila kitu kwa Dkt Hamill. Basi asifiche kitu akaeleza kinaga ubaga. Simulizi yake ikamwacha Dkt akiwa ameachama.
.
.
“Brian, una kazi kubwa,” Dkt akasema na kisha akakuna kidevu chake. Akashusha pumzi ndefu na kupangilia vema maneno mdomoni.
.
.
“Kecie hajafa. Yupo mahali na anataka ukamwokoe.”
.
.
“Mahali gani?” Brian akauliza. Kabla Dkt Hamill hajajibu, akamwambia, “Brian, haitakuwa rahisi hata kidogo. Kecie sasa ni mali ya Helo!”
.
.
“Kivipi?”
.
.
“Michoro uliyoikuta kwa Faris kulikuwa na mwanaume kando yake, sio?”
.
.
“Ndio,” Brian akajibu.
.
.
“Maneno yale ambayo Faris ameyaandika kwenye kitanda ni yale aliyosema Helo pindi anakufa!”
.
.
“Kwahiyo ina maanisha nini?”
.
.
“Helo amerudi!” akasema Dkt Hamill. “Na ndiye huyo unayemwona akiwa anaongozana na Kecie.”
.
.
“Sasa tutafanyaje?” akauliza Brian kwa kimuhe.
.
.
“Bado sijajua, ila … kuna haja ya kwenda kuonana na Faris. Kuna mengi ya kujua toka kwake. Ni wazi yeye ndiye atakuwa daraja letu.”
.
.
Kukawa kimya kidogo. Dkt akasonya na kutikisa kichwa.
.
.
“Kwanini Helo hajaanza kuwamaliza watu wa mji huu?” akauliza akitazama dirishani. Hilo swali lilikuwa ni kubwa na lilimtafuna kichwa. Lazima kutakuwa kitu, aliamini.
.
.
.
**
.
.
Kesho yake majira saa sita mchana …
.
.
Watu kumi na wawili walikuwa makaburini wakiwa wamevalia nguo nyeusi. Walikuwa wameketi kwenye viti na mbele yao kukiwa na shimo refu lililofunikwa na jeneza.
.
.
Padri Alfonso akiwa amevalia nguo zake za kazi ndiye alikuwa anaendesha misa. Na alikuwa ukingoni. Alipomaliza jeneza lilishushwa chini na watu wakaanza kuweka udongo wakianza familia ya marehemu.
.
.
Wakatia pia maua na kisha watu wakaanza kuparanganyika kwenda majumbani mwao. Nyuma wakaachwa Mrs Garett, Olivia, Brian na mamaye.
.
.
Wageni wakawa wanateta kuwapoonza wafiwa. Wakatembea mpaka kufikia kwenye gari la Mrs Garett, hapo mama huyo akaomba kuonana na kuongea na Brian faragha. Kabla Mama Brian hajapisha, akamtazama mwanaye kisha akainamisha kichwa kuafiki. Akatangulia zake.
.
.
Brian akaingia kwenye gari la Mrs Garett akiketi viti vya mbele.
.
.
“Brian,” Mrs Garett akaita kisha akanyamaza kwa sekunde kadhaa. “Kuna kitu nataka kukuuliza na tafadhali naomba uwe mkweli.”
.
.
“Usijali, mama. Nitakuwa mkweli,” akasema Brian akianza kubuni kinachofuatia.
.
.
“Ushawahi kumwona Kecie?” mama akauliza. Kisha akamtazama Brian machoni.
.
.
“Kumwonaje, Mrs Garett?” Brian akauliza.
.
.
“Kwa vyovyote tu,” Mrs Garett akasema. “Tangu amepotea, ushawahi kumwona popote pale … akifanya lolote lile? Tafadhali naomba kuwa mwaminifu.”
.
.
Brian akanyamaza kidogo na kusema, “Nishawahi onana naye. Jana ilikuwa mara ya mwisho nikiwa shuleni.”
.
.
Jambo hili likaonekana kumshtua kidogo Mrs Garett, akauliza, “Unapomwona anakuambia nini? … kuna kitu chochote anakwambia?”
.
.
Brian akasita. “Kuna nini Mrs Garett?”
.
.
“Nataka tu kujua … niambie, Brian.”
.
.
Uso wa Mrs Garett ulionyesha mashaka ndani yake. Aidha kuna habari aliyokuwa anatarajia toka kwa Brian.
.
.
“Huwa ananiambia nimwokoe,” akajibu Brian. “Kila ninapomwona ananisihi nimwokoe.”
.
.
“Umwokoe?” Mrs Garett akastaajabu. Kwa akili yake alidhani Kecie atakuwa amemwambia Brian kuwa familia yake ndiyo imemuua. Hili swala la kuokolewa kwake lilikuwa jipya. Kecie anataka aokolewe na nini? Kutoka kwa nani?
.
.
“Umwokoe?” akauliza.
.
.
“Ndio,” Brian akajibu na kuongezea, “Pengine Kecie hajafa.”

Mrs Garett akatoa macho ya mshangao. “Brian, sikuelewi. Nini unasema?”
.
.
“Samahani, Mrs Garett. Ni simulizi ndefu kidogo na muda sina kwa sasa. Nakuahidi kuja kukuona baadae jioni. Kwa sasa kuna mahali natakiwa kwenda. Kuna mtu aningoja!”
.
.
Basi Brian akaaga na kwenda zake. Mpaka anayoyoma Mrs Garett akawa anamtazama kwa namna ya kubanwa na maswali. Brian alimtibua kabisa akili yake na kumwacha kwenye hamu kubwa ya kutaka kujua.
.
.
Hata bado hakumweleza kijana huyo ujumbe aliopewa na mumewe, Mr Garett, ya kwamba Kecie anawinda roho zao.
.
.
Mrs Garett akajikuta anaona mate ni mazito kuyameza.
.
.
.
***
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom