MIMI NA MIMI 3
A Story by Elton Tonny
Familia, Urafiki, Mapenzi, Kazi, Siri, Tamaa, Hila, Usaliti, Ukatili, Mauaji, Mambo Yasiyotazamiwa
R-rated 18+
Enjoy!
★★★★★★★★★★★★★★★★★
SEHEMU YA KUMI NA NANE
★★★★★★★★★★★★★★★★★
Basi, ikawa hivi. Nilihitajika kumaliza chakula nilichowekewa hapo, kisha ningepangwa juu ya kilichotakiwa kufuata ambacho Bertha alitaka nifanye. Nikiwa bado ndani ya maumivu ya moyoni kwa kujua kilichowapata Miryam, Adelina, na Bobo, nikajitahidi kula chakula hicho baada ya baunsa mmoja wa mwanamke yule kurudi kunisimamia, na kisha niliponaliza, akaniongoza kuingia ndani ya bafu humo humo chumbani ili niusafishe mwili wangu aliponiondolea kamba zilizonifunga miguu. Sikuwa na nguvu nyingi lakini zilizokuwepo zilitoshea kujiongoza kuoga, maji yakiwa ya kunimwagikia tu, na nadhani nilikaa humo bafuni kwa saa zima nikiwa bado nasononeka tu mpaka nilipogongewa mlango na jamaa ili nitoke.
Nilipojitoa taratibu bafuni, nikamkuta mwanamke yule ambaye alitumiwa kumshikilia Miryam ile juzi, akiwa amesimama chumbani hapo na mfuko mkononi mwake. Nilikuwa mtupu kabisa, lakini sikuhangaika na jambo hilo na kubaki nimemtazama kwa njia yenye mkazo. Akiwa makini, akaurusha mfuko alioushika kitandani na kuniambia nifanye upesi sana kuvaa nguo na viatu, halafu yeye angenitengeneza zaidi; yaani vitu kama nywele na vingine vya kunipa mwonekano bora. Sikutoa jibu lolote kwa maneno isipokuwa vitendo tu, nikianza kwa kuufata mfuko huo na kutoa vilivyokuwemo, kisha nikaanza kuvaa huku baunsa na mwanamke huyo wakiwa hapo bado kunichunga.
Nilipomaliza kuvaa, mwanamke huyo akanikalisha kitini na kuanza kutengeneza nywele zangu vizuri, akizichana na kutumia mashine ndogo kuninyoa, kisha akanivisha vitu kama saa yangu mwenyewe, akaniwekea wallet yangu mwenyewe mfukoni, na vitu vyote ambavyo nilikuwa navyo siku waliyoniingiza mtegoni akasema ningevikuta ndani ya gari langu tukishatoka. Akanipatia na funguo za gari langu, halafu akasema hapo ndiyo tungepaswa kuondoka, mimi niondoke kwenye gari langu na kuelekea nyumbani kwetu. Hakuniambia kingine chochote, kwa hiyo sikuweza kuelewa kikamili ni nini hasa ningekutana nacho mbele ya safari hii. Ilikuwa ni kama wananiachia huru tu, lakini naelewa haikuwa hivyo kabisa.
Kwa hiyo kweli, mwanamke huyo akanitangulia, na mimi nikamfuata huku baunsa akiwa nyuma yangu. Nyumba hii ilikuwa na muundo kama zile lodge maridadi sana, tukapita vyumba vichache na sebule hadi tulipofika nje, na mwanga wa nje ulifanya niumie macho kiasi lakini nikaweza kuzoea hali upesi. Hapo nje kulikuwa na wanaume wengine watano, wenye mionekano ya kiulinzi yaani, na niliwatambua baadhi kuwa wale wa kwenye picha waliomtendea Adelina unyama ule. Magari mawili meusi ya Harrier yaliegeshwa kwa mbele, na moja ambalo lilikuwa la kwangu kando yao. Sikuona uwepo wowote wa Bertha sehemu hiyo wala yule mwanaume aliyetambulika kama mjomba wake, na mwanamke huyu aliyeniongoza sasa akaniambia niende kwenye gari na kuondoka haraka; akisema "usisahau." Hivyo tu.
Nilimwelewa vizuri sana. Sikutakiwa kusahau kwamba watu hawa walikuwa na macho kwangu, popote pale ambapo ningekuwa na mtu niliyemjali, wangekuwepo pia. Kwa hiyo ijapokuwa sikuelewa kwa asilimia zote wao kuniambia tu niende nyumbani ilimaanisha nini, najua ingekuwa wazi zaidi Bertha alitaka nini nikishafanya alichoagiza. Sijui ni nini tu kilikuwa kikiningoja huko. Ila sikutaka kuuliza chochote. Nikawapita watu hawa wakiwa wananiangalia kama vile wanataka kunitafuna, wachache wakishika bastola mikononi mwao nakwambia, na inaonyesha pesa za Bertha zilikuwa nene sana kwao kuwasukuma kufanya mambo mabaya bila kujali.
Nikafika kwenye gari langu na kufungua mlango, nikiingia ndani na kukaa kwa sekunde kadhaa kama vile nangoja jambo fulani. Ilikuwa kutoamini tu namna ambavyo maisha yalinifikisha hapa. Bado sikuelewa yaani ilikuwaje-kuwaje mpaka ikawa hivi. Na kwa muda huo mfupi niliokaa humo ndiyo nikatambua kwamba kuna simu iliwekwa kwenye dashboard pembeni, nami nikaivuta na kuiwasha. Hii haikuwa yangu, kwa sababu yangu ilipasuliwa na watu hawa. Lakini, nilichokuta ilikuwa ni simu zilizopigwa na jumbe nyingi sana kutoka kwa wapendwa wangu wote na marafiki. Laini zangu zote zilikuwa humu sasa.
Kuangalia siku hii, sasa ilikuwa ni Jumanne kwenye mida ya saa kumi jioni, na nilipopitia jumbe za watu kama mama yangu, mzee Manyanza, Ankia, Tesha, Bi Zawadi, Jasmine, Stella, nilijikuta nashikwa na kihoro kikali moyoni na kuanza kudondosha machozi. Wote walikuwa wakinitafuta sana, wakiniambia kuhusu taarifa za msiba wake Miryam, Bobo, na Adelina, na inaonekana kutokujua kwao nilikuwa wapi iliwatia hofu kubwa kwa kuwaza labda na mimi nilipatwa na mambo mabaya sana.
Sikujua nianze na nani, kumtafuta nani ili niongee naye kwanza. Hata askari Ramadhan alionekana kuwa amenipigia mara kadhaa, lakini kufikia sasa, sikujali lolote tena kwa upande wa askari huyo. Hapa nilichotakiwa kufanya ilikuwa kutii nilichoagizwa kufanya na Bertha, na mambo yote ambayo yaliendelea huko nyumbani ningeyajua huko huko nikishafika. Nikaweka simu pembeni na kujisawazisha kiakili, nikiikaza huzuni yangu na kuwasha gari, nami nikaanza kuligeuza kutoka hapo huku nikiwaona watu wake Bertha pale nje walivyokuwa wakinisindikiza kwa macho yao.
★★
Nikaliondoa gari ndani ya geti la nyumba hiyo na kuanza kuisaka barabara yoyote ambayo ningeweza kuifahamu, na huku ilikuwa ni kwenye eneo ambalo sikuwahi kufika, lakini nilijua palikuwa Dar bado. Nikapita hapa na kupita kule mpaka ilipokuwa wazi kwamba sehemu niliyokuwepo ilikuwa maeneo ya Bunju, nami ndiyo nikaendeleza mwendo kwa utambuzi zaidi kuweza kupafikia nyumbani. Nilikuwa nimechoka sana. Nilikaa tu hivyo na kuendesha gari lakini ilikuwa ni kama ninavuta kokoteni lenye mzigo mzito mno. Umakini wa kuendesha haukuwa wa hali ya juu kiasi kwamba zaidi ya mara tatu nilikaribia kuingia upande usio sahihi wa barabara, ikiwa ni kama Mungu tu nilikosa kujisababishia ajali kwa kugonga magari mengine.
Bado nilisongwa na hisia mbaya mwilini na moyoni, na hilo lilisababisha nikose kutambua kwamba kuna gari lililokuwa likinifuatiilia kwa nyuma huku likipiga honi mara kadhaa kama kutuma ujumbe fulani kunielekea. Sikuwa nimekazia fikira kelele zozote zilizoendelea za barabara, ila sasa ndiyo nikaangalia kwenye kioo na kutambua kwamba gari hilo, aina ya Harrier nyeusi, lilikuwa la maaskari, likitiwa POLISI pande za milango yake. Lilikuja upande wangu kwa ukaribu sana, ikiwa kama napewa amri nisimame upesi, nami nikawa sina budi ila kutii na kulisogeza gari upande wa pembeni wa barabara maeneo ya stendi ya mabasi Mwenge; hapo hapo gari hilo la maaskari likija na kusimamishwa kulitangulia langu.
Wakashuka maaskari wawili waliovalia nguo za kikazi na bunduki mikononi mwao, wakianza kuja kwenye gari langu, na jambo hilo naona lilivuta umakini wa wadau waliokuwa maeneo hayo kutazama nini kingeendelea. Nilihisi labda maaskari hao waliona aina fulani ya ukiukwaji wa sheria kutokana na uendeshaji wangu na hivyo wakahitaji kuja kunikagua, hivyo nikatoa wallet yangu upesi kuangalia kama leseni na vitambulisho vyote vilikuwemo, na kwa hakika kila kitu kilikuwepo. Nikiwa nimetengenezwa vizuri kimwonekano, najua hawangeona kwamba nilikuwa na maumivu mwilini, kwa hiyo nikataka kuhakikisha naonyesha kila kitu kipo sawa.
Walipokaribia milango ya gari langu, nikashusha vioo ili waweze kuniona vyema, na walikuwa wanaume watu wazima wenye sura makini kikazi. Kabla hata sijajaribu kuongea lolote, aliyesimama upande wangu wa mlango akatoa ishara kwa kiganja kuwa nishuke, nami nikatii hilo na kufungua mlango, nikishuka na kusimama mbele yake huku nikijitahidi kuonyesha utulivu.
"Shikamoo?" nikamwamkia askari.
"Marahaba. Hujambo?" akanisemesha kwa njia ya kawaida.
"Sijambo," nikamwambia.
Mwenzake alikuwa upande mwingine akiliangalia gari langu kwa umakini, kisha akaanza kuja tuliposimama.
"Unaitwa nani?" askari wa kwanza akaniuliza.
"Jayden," nikamwambia.
"Jayden nani?"
"Jayden Constantine Mria," nikamjibu.
"Unatokea wapi?" akauliza tena.
Nikatulia kidogo, kisha nikasema, "Nilikuwa maeneo ya Bunju kule."
Askari wa pili akanikaribia na kusema, "Umebeba vitambulisho?"
Nikamwangalia na kusema, "Ndiyo... hiv.. hivi hapa..."
Nikaanza kutoa wallet huku nikitetemeka viganjani kiasi, lakini askari wa kwanza akanyoosha kiganja chake kama kunizuia. Nikamwangalia usoni.
"Nataka uniambie ulikuwa unafanya nini Bunju. Tunajua wewe ni nani," akasema hivyo.
Nikabaki nikimtazama kana kwamba sikumsikia, na watu pembeni waliendelea kututazama.
"Umefanyaje mdomoni hapo, mbona umevimba?" askari wa pili akauliza.
"Aa... nilijiumiza kidogo tu..." nikasema hivyo na kuangalia chini.
"Ulienda Bunju huko lini? Ulikuwa unafanya nini?" askari wa kwanza akaniuliza.
Nilishindwa kujua cha kumjibu, ambacho kisingeleta utata kwa upande ambao naelewa ulikuwa mbaya kwangu. Yeye kusema ananijua inamaanisha kwamba hii haikuwa kusimamishwa ili kukaguliwa labda, bali kwa kuwa tayari maaskari hawa walifahamu mambo fulani yaliyoendelea kunihusu mimi mpaka kufikia hapa. Lakini kutokujua walifahamu nini ndiyo kulinipa kizungumkuti, na kwa kukosa cha kusema nikajikuta naangalia tu chini huku huzuni ikiwa inazidi kunikaba.
Askari wa pili akanishika begani, na nilipomtazama, alikuwa akinisogelea huku akiweka uso ulioonyesha aina fulani ya uelewa, kisha akasema, "Usijali kijana. Wewe ongea tu. Hauko kwenye shida. Tunataka kujua kama ulipatwa na jambo baya ama vipi... kwa hizo siku mbili ulizopotea."
Alizungumza kwa njia yenye upole, nami nikapata taswira kubwa sasa kwamba maaskari hawa waliagizwa kunitafuta, na wakawa wamenipata.
"Mara ya mwisho kabla hujaenda Bunju ulikuwa wapi? Jayden... tuambie," askari wa pili akauliza hivyo.
Nikafumba macho na kuegamia gari langu, nami nikasema, "Mtanisamehe kwa kweli. Nashindwa... nashindwa hata niseme nini yaani... maana... nina uchungu mwingi sana moyoni."
Niliposema hivyo, wakaangaliana kwa ufupi, kisha wakanitazama tena.
"Nime... nimefiwa. Nilikwenda mbali kidogo ili... hhh... ili niwe mwenyewe kwanza... maana bado nilikuwa na huzuni... huzuni kali... kwa hiyo..." nikazungumza huku pumzi zangu zikitetemeka.
"Pole. Tunajua kuhusu msiba wenu, na ndugu zako walikuwa wanakutafuta," askari wa kwanza akasema hivyo.
"Simu yako ilikuwa inabadili location sana tulipopewa assignment ya kukutafuta jana, ni kwa nini? Tungeona upo Kisutu, mara Ubungo, Masaki... kijana... kama kuna jambo lilitokea kabla ya...."
"Nani aliwapa hiyo kazi ya kunitafuta?" nikamkatiza askari wa pili.
"Baba yako," akasema askari wa kwanza.
Nikamwangalia na kutikisa kichwa kwa uelewa.
Askari wa pili akasema, "Ulikuwa umeshajua ajali iliyompata mchumba wako ndiyo ukaenda huko Bunju? Ulijuaje, yaani... taarifa ulizipataje... halafu..."
Nikainamisha uso tu kwa huzuni. Sijui walifikiri ni nini kilikuwa kimetokea kihalisi.
"... pia kuna marafiki zako wengine wamekufa siku moja baada ya ajali kutokea, ni ndani ya wakati mfupi sana hayo yote kutokea na wewe ukawa haupatikani. Ilizua tafaruku kwa wazazi na ndugu zako, walidhani na wewe utakuwa umepatwa na matatizo. Unaelewa ni kwa nini mambo hayo yametokea namna hiyo?" askari wa pili akaendelea kuzungumza.
Nikabaki nimetazama chini tu.
"Una... una taariffa zote juu ya vifo vyao?" akauliza tena.
Nikatikisa kichwa kuonyesha hakuna nilichojua.
Askari wa kwanza akasema, "Okay Thomas, inatosha."
Nafikiri alikuwa anamwambia mwenziye aache kuniuliza maswali mengi, naye akasogea nyuma kidogo.
"Hapa ndiyo ulikuwa unarudi nyumbani nafikiri," askari wa kwanza akasema.
Nikamwangalia na kutikisa kichwa kukubali.
"Sawa. Naona mambo bado ni mazito kwako, kwa hiyo tutatafuta muda mwingine tuongee zaidi. Tunampigia Mr. Manyanza kumjulisha umepatikana, halafu tunaenda pamoja nyumbani kwenu. Familia yenu yote... wapo huko, bado wanakusubiri. Ingia kwenye gari twende," askari huyo akaniambia hivyo.
Inaonekana hali ilionwa kwa utofauti na namna ambavyo mambo yalikuwa kihalisi, na ni taratibu kila jambo lingefunuka kwangu mpaka ningeelewa kwa nini kilichompata Miryam kilizungumzwa kuwa "ajali." Nikaingia ndani ya gari tena, maaskari hao wakirejea kwenye lao, nami nikawatangulia kwa mara nyingine tena na kuanza kuisaka barabara ya kuelekea Goba, ambako najua pindi yenye simanzi kuu iliningoja kwa hamu.
★★
Mwendo haukuwa mrefu sana, na katikati ya safari hiyo nilipigiwa simu na mzee wangu, Frank Manyanza, ambaye hatimaye niliweza kupokea simu yake leo hii. Bila shaka angekuwa amepewa taarifa na maaskari wale kuhusu kupatikana kwangu, na akionyesha kujali sana alianza kuniuliza nilikokuwa nimepotelea, akisema mama na wengine waliwaza mno juu yangu hasa kutokana na hali mbaya zilizokuwa zimetokea. Nikamwambia tu kwa ufupi nilikuwa njiani kwenda nyumbani, na huko tungekutana na kuzungumza zaidi juu ya mambo yote yaliyotokea. Mama pia alitaka sana tuzungumze kwa simu lakini nikamwomba mzee amwambie avute subira, si muda mrefu angeniona pia.
Huku maaskari wakifata nyuma yangu, nikafanikiwa kuingia mitaa ya Steve Nyerere na moja kwa moja kuielekea nyumba ya wazazi. Yaani nilikuta geti lote la uzio likiwa wazi, na nilipoanza kuliingiza gari ndani ningeweza kuona magari kadhaa hapo na idadi kubwa ya watu, mwonekano ulioleta maana halisi ya kuendelea kwa msiba. Sikujua ulimhusu nani mwingine kama isingekuwa ni Miryam, kwa kuwa kabla hata sijaegesha gari langu tayari niliweza kumwona Ankia, Tesha, na wengine wa familia yangu wakitokea kule ndani na kuja upande huu.
Nikaegesha gari langu na kubaki nimetulia humo kwa sekunde chache, nikiwa naona namna ambavyo mama alikuja upesi kunielekea, nami nikashuka taratibu huku maaskari nao wakiwa wanashuka kutoka garini kwao. Kabla hata sijafunga mlango wa gari, mama akawa amenifikia na upesi kunikumbatia kwa nguvu, akiwa analia kwa hisia sana. Nilibaki nimetulia tu, wengine pia wakiwa wamefika hapo, mzee, Simba, Deborah, Tesha, Ankia, Jasmine, Nuru, na watatu hao wa mwisho wakatusogelea pia kumuunga mama mkono kunikumbatia kwa pamoja. Nilibaki nimesimama huku nikimtazama Tesha machoni, kijana akiwa ameniangalia kwa uso ulioonyesha huzuni nzito mno, na chozi likaniponyoka jichoni baada ya huzuni yangu kunilemea pia.
Mama, akiwa karibu nami bado, akanishika usoni kwa mikono yote huku akiniangalia kwa hisia sana, nami nikamtazama pia huku machozi yangu yakiwa yanataka kuvuja kama mvua sasa. Sikuweza kujikaza. Wanawake wote wakaanza kutoa machozi, na mama akakosa maneno ya kusema na kunikumbatia tu tena. Nikajifuta tu machozi upesi na kujitahidi kujikaza, na mzee akasogea karibu nasi na kunishika begani kama kunitia nguvu. Maaskari waliposogea karibu nasi pia ikambidi mzee awageukie ili bila shaka wazungumze kwa ufupi, ndiyo mama akaniachia na kuniomba tuelekee ndani pamoja kwenda kuutafuta utulivu. Ikawa hivyo.
Dakika chache baadaye, sote tukawa ndani, na nilikuta familia yote ya Miryam wakiwa hapo; Mariam, Bi Zawadi, Bi Jamila, Shadya, Doris, mama yake, na Dina, wote walikuwepo pia. Nilifikia kukaa na binti Mariam, ambaye baada ya kuniona huzuni yake ilimsukuma anishikilie na kuning'ang'ania kwa nguvu tulipokaa pamoja. Uwepo wa familia yote ya Miryam hapa ulionyesha kwamba msiba wake uliletwa kufanyiwa huku kwanza, kwa sababu toka wapate taarifa za kifo chake mimi pia sikuwa nimepatikana. Na ni taarifa ambazo wapendwa wangu hawakujua zilikuwa za uwongo.
Nilipata kujua sasa kwamba, Miryam alisemekana kupoteza maisha baada ya gari lake kudondokea kwenye bonde refu "alipokuwa akielekea nje ya jiji." Yaani walikuja kulipata gari lake likiwa limeharibika na kuungua moto pia, na mwili wake Miryam ulipatikana humo ukiwa hautamaniki hata kidogo. Ni jambo lililonipa picha kwamba, Bertha, na watu wake, walitengeneza kisa bandia kwa namna hiyo, ionekane kwamba Miryam alipatwa na ajali, na mimi kwa sababu ya huzuni nikaenda mbali na kutotaka nipatikane kwa muda fulani. Ndiyo lililokuwa lengo la Bertha kuniachia nije nyumbani, ili nije kuipa "uhalisia" hali hii aliyoijenga huku, halafu ndiyo aendelee kuyafanya maisha yangu yawe mabaya kivyovyote alivyotaka kutokea hapa.
Haikuwa rahisi kwangu kufanya maigizo haya, kuwaangalia wapendwa wangu na kujifanya kutoelewa mambo yote yaliyokuwa yametokea, ama kukubaliana na yale waliyofikiria yametokea, lakini sikuwa na namna. Kila nilipokumbukia picha za Bobo na Adelina, sikuwa na namna. Na tena nilihitajika kumfariji Ankia wangu pia kwa sababu hakuomboleza kifo cha marafiki zake wawili wapendwa, bali na mpenzi wake ambaye alikufa kikatili sana. Alibeba huzuni nzito sana Ankia, pamoja na Tesha pia.
Mzee na mama walikuwa wameamua kuwaleta wote huku wakae kwanza kabla ya kwenda kufanya mazishi, kwa sababu kwa hatua zilizochukuliwa na maaskari kwenye uchunguzi wa matukio hayo, zingepita siku kadhaa hadi ije kuruhusiwa kwa miili hiyo kuachiliwa kwa ajili ya mazishi. Mambo hayo yalikuwa mazito mno, zilikuwa ni taarifa zilizozagaa jijini na mitandaoni hadi kufikia vyombo vya habari, jeshi la Polisi likiwa na ahadi za kutoa kuwakamata waliohusika na mauaji hayo ya kikatili sana. Lakini naelewa wasingefanikiwa kupata lolote. Bertha alikuwa makini sana. Sijui tu hata alikuwa akiwatoa wapi watu aliowatumia kufanya maovu yake, maana hata maaskari walipochunguza mwili wa Adelina ili kutambua watu waliomshika kabla ya kumuua, hawakuweza kubaini walikuwa nani.
Ilikuwa ngumu mno kwangu kujitahidi kujikaza, yaani, nisiseme niliwajua, nilizijua vizuri sura zao, lakini kila nilipokumbukia picha ya Evelyn ikionyeshwa kwangu na Bertha, JC sikuwa na ujanja. Angeweza kufanya lolote lile huyo mwanamke na hiki ndiyo kilikuwa kipimo kwangu aone ikiwa ningeweza kufuata aliyoyataka kama nilivyomwahidi kufanya. Aisee! Nilijiona fala mmoja mkubwa sana. Maaskari wangehitaji kunihoji kuhusiana na ishu ya Miryam, kwa sababu kuna mambo kutoka kwangu walihitaji kujua zaidi, na wakanipa muda wa kufanya mazungumzo nao kuwa kesho mida ya mchana; kwamba wangekuja nyumbani nikiwa nimeshatulia zaidi. Kulikuwa na ile heshima fulani kutoka kwa maaskari kwenda kwa mzee wangu kutokana na jina lake, kwa hiyo walionyesha aina fulani ya ustaarabu.
★★
Kwa hiyo ikawa ni kuendelea kukaa pamoja, usiku ukiwa umeingia baada ya maaskari kumaliza mawili matatu na mzee kisha kuondoka zao, nasi kama familia tukakaa sebuleni pamoja kutiana moyo. Deborah alikuwa hapa kwa sababu ya Jasmine, hiyo jana walipopata taarifa za kushtua za kifo cha Miryam walikuwa pamoja huko kutembeleana kufanya maandalizi ya Krismasi kwa ajili yetu sote, ndiyo akawa amekuja naye nyumbani ilipofahamika sikuwa napatikana.
Jasmine alikuwa pamoja na mapacha wake hapa ingawa 40 hazikuwa zimefika, na Deborah alisema Stella alikuwa hospitali pamoja na Evelyn, kwamba mtoto ndiyo alikuwa anarejea hali nzuri kiafya lakini mama yake alitaka awe huko kwa muda zaidi kisha ndiyo wangerudi nyumbani. Na yeye pia akiwa anajua yaliyotokea, Stella alisema angekuja huku kuniona pia wakati ambao angepata nafasi, na akawa ametuma salamu zake za pole kwetu sote.
Sikuwa na la kusema wengine walipojaribu kunisemesha kwenye kikao hicho kidogo cha kufarijiana. Mama aliketi karibu yangu na Mariam, huku wengine wakikaa pale au kusimama kule kusikiliza maneno ya hisia kutoka kwa mmoja na mwenzake. Bi Jamila aliongea kwa uchungu mwingi kuhusu binti yake mpendwa, akilia na kukumbatiwa na Bi Zawadi huku anauliza maswali yale yale tu; ni kwa nini ajali ile ilimpata binti yake? Kwa nini afe mapema namna hiyo? Ankia na Doris walijitahidi kuzungumza pia lakini walishindwa kutokana majonzi kuwajaa, na Tesha ndiyo akaongea kwa kujikaza, akisimulia namna ambavyo dada yake alikuwa baraka kwa maisha yao toka wazaliwe mpaka kufikia hiyo juzi. Hakuamini kama kweli aliwatoka.
Baada ya maneno hayo, mzee ndiyo akazungumza kwa kutufariji sote, akisema tulihitaji kuwa na nguvu kuvumilia kisa hiki chenye kusikitisha hata ingawa ilikuwa ngumu sana, kwa sababu tunajua Miryam angetaka tufanye hivyo kwa ajili yake. Aliongea kwa kuelekeza maneno mengi kwangu akisema anajua ni namna gani niliumizwa sana na kifo cha mwanamke niliyempenda sana, na akanifariji kwa kusema wote hapo walikuwa pamoja nami kunisaidia kuvumilia, kwa kuwa ingawa halikuwa jambo zuri, tukio hilo ndiyo lingeimarisha ukaribu wa familia zetu na kusonga mbele tukiwa tumeshikamana bila kuacha.
Nilikosa cha kuongea, hata ilipokuwa wazi kwamba wengine waliningojea nizungumze, sikuweza kabisa kufungua mdomo na kubaki nimeshusha macho chini tu, Mariam akiwa kwenye kumbatio langu. Wafanyakazi wa familia zetu walikuwepo pia kushughulika na maandalizi ya chakula kwa kusaidiwa na baadhi ya wanawake wengine hapa, na ilipokuwa ni mida ya saa tatu usiku wakaanza kutuletea vyakula kila mmoja ili tujumuike kushiriki mlo kwenye pindi hii yenye huzuni. Haikuwa rahisi kwa wengi kula chakula kizuri kilichoandaliwa kwa sababu ya hali mbaya za kihisia, lakini wakubwa wakajitahidi kuwatia moyo wengine wale ili kujipa nguvu kama mzee alivyoshauri.
Sikutaka kula hata kidogo, kichwa kilikuwa na mambo mengi mno bado, hivyo nikaamua kuanza kumlisha Mariam, ambaye hakutaka kabisa kula. Nilimshawishi hadi akawa akila huku analia, na wengine walishikwa na simanzi kwa sababu ya hili. Kulikuwa na ukimya fulani zaidi wakati huu, na mimi nilijikaza tu hivyo hivyo kuendelea kumlisha binti huku huzuni ikitawala moyoni mwangu, ndipo jambo jipya likazuka. Simu yangu, ikiwa pembeni sofani, ikaingiwa na ujumbe, lakini sikutaka kushughulika nayo mpaka nimalize kumjali Mariam, ndiyo mama akaivuta na kuniambia kuna ujumbe. Nilitaka kumtikisia kichwa kuonyesha aachane nayo, lakini, wazo lililoingia kichwani likanifanya niipokee tu na kuufungua ujumbe huo.
'Njoo barabarani. Dk 10. Usitumie gari.'
Ulisomeka hivyo. Nikiwa ndiyo nimeusoma tu bila kuelewa kwa upana zaidi maana yake, ujumbe huo ukajifuta wenyewe! Nilibaki kuitazama simu kwa umakini, naye mama akaonekana kuchungulia kuona nini niliangalia namna hiyo.
"Jayden..." mama akaniita.
Nikaangalia pembeni tu bila kumwitikia, na niliona kwamba wengine walikuwa wakinitazama sana.
"Jayden, vipi?" mama akauliza.
Nikajitahidi kuonyesha utulivu na kumwangalia, nami nikamwambia, "Natoka mara moja."
"Unaenda wapi?" mama akauliza.
"Hapo nje. Nahitaji fresh air," nikasema tu hivyo na kusimama.
"Nikusindikize?" Simba akaniuliza.
"A-hamna... na... nakuja muda siyo mrefu, nahitaji tu..." nikaishia hapo.
Wote waliniangalia kwa sura zenye kujali sana, yaani hii ndiyo iliyokuwa mara ya kwanza nimeongea toka maaskari waondoke.
Nikamwangalia Mariam, ambaye alinitazama kwa huzuni, nami nikasema, "Nahitaji dakika chache tu. Nakuja."
Mariam akaangalia tu chini na kutikisa kichwa kukubali.
Nikashika kichwa na nywele zake kwa kujali, kisha nikawavuka wengine na kuelekea mlangoni bila kugeuka nyuma hata mara moja. Nilitoka tu ndani hapo nikiwa nakumbuka vitu viwili; ujumbe niliotoka kutumiwa, na nilichokuwa kwa kipindi hiki na kuendelea. Mbwa wa Bertha. Sikuhitaji kuuliza mengi, nikitakiwa kufanya chochote alichotaka endapo kama sikutaka yeyote kati ya wale niliowaacha pale ndani wapatwe na jambo baya. Yaani! Sikujua ujumbe huo ulitoka wapi na ulijifutaje, lakini kama nilivyosema, najua Bertha alikuwa makini mno, kwa hiyo na mimi kwa upande wangu nilitakiwa kuwa makini kuhakikisha nawalinda watu niliowapenda.
Kwenda barabarani nikaenda, na nilijitahidi kutembea upesi ili hizo dakika kumi zisipite. Ilikuwa wazi kwamba nilipaswa kuifikia lami, na bila kutumia gari ningetakiwa nikimbie kidogo. Lakini sikuwa nimeifikia lami kabisa nami nikakutana na gari moja likiwa limeegeshwa usawa wa barabara hii changarawe iliyoelekea huko lami, aina ya Subaru Forester jeusi. Nilihisi kabisa kwamba lazima aliyetuma ujumbe alikuwa humo, nami nilipolikaribia nikasitisha mbio zangu na kusimama umbali mfupi kutokea lilipokuwa na kulitazama. Vioo vya mbele havikuonyesha kwa ndani na hapo kulikuwa na ugiza kabla ya kuifikia nyumba ya Steve kule mbele, ndipo mlango wa mbele wa gari hilo ukafunguka na mwanaume mmoja kushuka.
Sikumtambua, lakini alikuwa mweusi na mwenye mwili mpana ingawa si wa mazoezi sana, na alivalia kwa njia ya kitanashati kabisa. Hakutoa zile vibe za uhuni wala unoka, naye akasimama hapo hapo karibu na mlango wa gari na kubaki akiniangalia kwa njia makini. Alivalia kofia nyekundu kichwani. Mimi nilikuwa namtazama kwa subira tu, naye akatumia vidole viwili kunionyesha ishara ya kuniita ili nisogee karibu naye. Nikatii. Nikamsogelea mpaka karibu na kusimama mbele yake, akiwa ni mtu mzima kama Festo tu, naye akaangalia huku na kule upesi, halafu akaninyooshea kiganja chake kingine kwa chini. Nilipokiangalia, nikaona ameshika kitu kama laini ndogo, halafu kiganja chake kilivalishwa glovu nyeusi. Nikamtazama usoni.
"Shika," akasema hivyo.
Upesi nikaichukua laini hiyo, nami nikaendelea kumtazama tu.
"Alipokuita hotelini, ulifika ukakuta hayupo. Ulipoendelea kumtafuta hukumpata, kwa hiyo baadaye ukagundua alikuwa na wivu kwa sababu ulikuwa na Stella..." mwanaume huyo akasema hivyo.
Nilishangaa!
"Ulijaribu kumfatilia lakini hukumpata, ndiyo ukaja kusikia gari lake limepindukia bondeni. Labda ilikuwa ni ajali, ila labda kwa sababu alikuwa na huzuni, ndiyo maana akaona akatishe maisha yake. Ulijilaumu sana ndiyo maana ukaenda mbali kwanza, kwa sababu uliona ni makosa yako mpaka yeye kufa namna hiyo," akaongea hivyo.
Nilikunja uso kwa kutomwelewa kabisa, yaani aliongea kana kwamba ni roboti, nami nikauliza, "Nini?"
Akaangalia chini na kusema, "Hivyo ndiyo utakavyosema. Hiyo laini iweke kwa simu siku mbili baada ya leo. Usiku mwema."
Ih!
Kabla hata sijazungumza tena, mwanaume huyu akafungua mlango wa gari na kuingia, kisha akaliwasha. Nilibaki nimeangalia gari hilo kama vile silielewi yaani, lakini ni yeye ndiye aliyekuwa ameniacha na maswali kedekede kichwani. Hapo hapo tu gari hilo likaanza kuondoka, nikibaki kulisindikiza kwa macho tu. Kwa nini hawa watu walifanya hivi? Yaani, kuniacha na kizungumkuti cha kufikiria maneno hayo yangemaanisha nini sijui iliwapa raha sana? Alikuwa anamwongelea Miryam, au? Yaani, ni kama alikuwa ananipanga niseme maneno hayo. Lakini kwa nani? Na kwa nini iliwabidi wafanye hivi ili kunifikishia hii taarifa badala ya kuniambia yote kule kule nilikotoka leo? Ilimpa Bertha faida gani kutumia hizi gharama zote kuni... yaani, ah!
Nikaitazama laini hiyo niliyopewa na kuona ilikuwa ni ya TTCL, na nikiwa bado natafakari....
"JC?"
Nikashtuka sana na kugeuka nyuma upesi, baada ya kushikwa begani na sauti hiyo niliyoifahamu kuniita namna hiyo.
★★★★★★★★★★★
ITAENDELEA
★★★★★★★★★★★
Whatsapp +255 678 017 280