Sehemu ya 24.
Katika hilo sikutaka kumshirikisha mtu yeyote kwa kuhofia yale ambayo yalimtokea Glory.
Siku zilikatika, siku ya jumapili ilipowadia nikaondoka zangu vizuri kuelekea katika kanisa la Praise na Worship lililokuwepo maeneo ya Mwenge.
Siku hiyo nakumbuka nilipanda daladala vizuri mpaka kufika Mwenge, kitu cha kushangaza baada ya kufika na kutaka kwenda katika kanisa hilo sikuliona.
Nilishangaa sana, nikahisi labda nimesahau mahali lilipokuwepo kwa sababu sikuja muda mrefu, ni hapa ambapo nilimsimamisha jamaa mmoja ambaye baada ya kumsalimia nilimuuliza;
“Samahani kaka nilikuwa naulizia kanisa la Praise and Worship nimesahau sijui lipo maeneo gani kwa hapa?”
“Kanisa la Praise and Worship?” aliniuliza huku akinishangaa.
“Ndiyo, lipo wapi?” nilimjibu kisha nikamuuliza.
“Mbona hapa Mwenge hakuna kanisa kabisa,” alinijibu.
“Hakuna kanisa?”
“Ndiyo hakuna kanisa hata moja sasa nashangaa unaponiuliza hilo kanisa la Praise and Worship sijui umelionea wapi?”
“Kivipi?”
“Kwani dada wewe umeulizia nini?”
“Kanisa.”
“Nimekwambia halipo,” aliniambia jamaa huyo kisha akaamua kuondoka zake.
Sikutaka kuamini, nilihisi labda jamaa huyo alikuwa ni mgeni na eneo hilo, nilichokifanya nikatafuta mtu mwingine wa kumuuliza, huyu alikuwa ni mwanamke mtu mzima kidogo.
“Shikamoo,” nilimsalimia.
“Marahaba hujambo,” aliiitika.
“Sijambo, samahani.”
“Bila samahani.”
“Nilikuwa naulizia kanisa la Praise and Worship sijui lipo maeneo gani kwa hapa Mwenge maana nimesahau.”
“Umesema kanisa gani?”
“La Praise and Worship.”
“Mbona hilo kanisa sijawahi kuliona.”
“Hujawahi kuliona?”
“Ndiyo.”
“Je, hakuna kanisa lingine unielekeze?”
“Kwa kweli kwa hapa Dar hakuna kanisa lolote nitakudanganya, kote utakapoenda utasumbuka bure,” alinijibu mwanamke huyo, nikazidi kupigwa na butwaa.
Je nini kitaendelea?