SEHEMU YA 16
Siku hiyo alipanga kwenda huko kwa ajili ya kuhubiri, alijua ni kwa jinsi gani washirika wake walikuwa wamemkumbuka kwani katika kipindi chote alichokuwa akikaa nyumbani, alikuwa akipigiwa simu na kuuliziwa maendeleo yake.
Siku hiyo alipoonekana kanisani, kila mshirika alikuwa na furaha, wiki tatu ambazo hakuonekana kabisani hapo zilionyesha kila dalili kwamba kanisa hilo lingepwaya sana na hatimaye lingeweza kupotea kabisa.
Ujio wake ukaibua ari ya washirika wake na hatimaye kuendelea na huduma kama kawaida. Kwa kumwangalia, usingeweza kuamini kwamba jana usiku alishinda klabu ya muziki, alionekana mchangamfu na hata macho yake hayakuonyesha kabisa kama alikuwa mtu aliyekesha.
Japokuwa alikuwa akihubiri na kuwabariki watu waliokuja na watoto wao kanisani hapo lakini mara alipokumbuka kwamba Irakoze alitaka kuzungumza naye asubuhi ya siku hiyo, ghafla amani ikakatika.
Hakukuwa na kitu alichokiogopa kama kuambiwa kwamba mtu fulani alitaka kuzungumza naye.
Hakujua ni kitu gani kiliendelea lakini mwisho wa siku akataka kukaa chini na msichana huyo ili kumsikia alikuwa na jambo lipi la kuzungumza.
Ibada ilipokwisha, hakutaka kukaa kanisani na kuwasalimia washirika, alichokifanya ni kuondoka na kuelekea nyumbani kwake.
Alipofika huko, kama ilivyokuwa siku nyingine, alipokelewa kwa mahaba mazito mpaka chumbani, hata kabla hajafanya lolote, akavuliwa joho na kupigwa mabusu mfululizo, ndani ya dakika tatu tu, alibaki kama alivyozaliwa.
Kilichofuata ni kilekile kilichokuwa kikitokea siku zote, walifanya dhambi kwa takribani masaa matatu na ndipo kila mmoja akaridhika na kutulia pembeni ya mwenzake.
“Aya niambie ulitaka kuniambia nini asubuhi,” alisema padri Benedicto.
“Una moyo?”
“Ninao. Hebu niambie wala usinitishe.”
“Usiogope, nafikiri ni baraka kutoka kwa Mungu.”
“Ipi?”
“Nina mimba yako!”
“Unasemaje?” aliuliza padri huku akionekana kushtuka.
“Nina mimba yako!”
Padri Benedicto akasimama na kuanza kumwangalia Irakoze, hakuamini kile kilichokuwa kimeongelewa mahali hapo, alimwangalia msichana yule, ndiyo kwanza alikuwa akitabasamu kwa furaha, hakuonekana kujua ni kwa jinsi gani padri alijisikia moyoni mwake.