SURA YA KUMI NA MBILI
Muziki ulisikika kwenye simu kubwa nyeupe iliyokuwa imelala juu ya meza ya plastiki ya kampuni ya Serengeti. Bwana Raheem aliyekuwa amekaa peke yake kwenye kona ya bar maarufu jijini Dar aliitizama simu hiyo kiooni akaona jina la Mtemvu. Alisonya kisha akaendelea kunywa kinywaji chake kilichokuwa ndani ya glasi ndefu yenye kiuno chembamba.
Simu ilipiga muziki mwishowe ikakata. Ila baada ya muda kidogo, ikapiga tena muziki. Raheem aliitizama kwa jicho la hasira kabla hajaamua kuipokea ili kumuepushia usumbufu zaidi.
Alifoka:
“Nini!” Akiwa amekunja sura. Ila baada ya muda alinywea na kuwa mtulivu zaidi akiubinua mdomo wake.
“Muda gani? ... Kwahiyo mpo wapi kwa sasa? ... Ok, nitakuwa hapo muda si mrefu!”
Aliirudisha simu juu ya meza akakuna ndevu zake.
“Hiki kijamaa kina matatizo sana!” Aliongea mwenyewe. Alikunywa kinywaji chake mafundo kadhaa kisha akaendelea kuteta kama vile kuna mtu anamsikiliza.
“Kwanza kioga kama mwanamke! ... Sijui kilienda wapi huko kikabinuliwa na lori!”
Akanywa tena mafundo mengine na kumaliza kabisa knywaji chake.
“Najuta sana kufanya kazi na hawa watu waoga hivi. Kama ningelijua mapema lile dili nisingeliwashirikisha kabisa. Hivi inakuaje kumuua mtu mmoja tu inakuwa ishu kubwa hivi? Suush! Huu ni wakati wangu muafaka wa kujutia kumtupilia mbali na kumlaghai bwana Kim. Najua asingenisumbua katu! Uoga wangu waniponza vibaya sana.”
Alipiga kichwa chake kofi akiing’ata lips.
Ni miezi kadhaa tu huko nyuma alikuwa mtu wa kwanza kushirikishwa wazo adhimu la kuua tembo na kuwapokonya pembe ili wapate zisafirisha kwenda Asia kwa kupitia madalali wa ulaya. Wazo hilo lilikuja mezani kwake pale alipokuwa anaperuzi barua pepe akakuta ametumiwa kipande kidogo cha habari kutoka kwa bwana Kim, kikieleza faida kinaganaga za pembe za tembo huko mashariki ya mbali.
Kwa mara ya kwanza alipuuzia ujumbe huo ambao haukuambatana na maneno mengine yeyote, ila baada ya bwana Kim kumshawishi zaidi kwa kumtumia namba za madalali hao wa ulaya akiweka wazi pesa nono za biashara hiyo, Raheem akadakwa uchu.
Kwa siri, tena kubwa sana alisuka mpango huo na bwana Kim ya kwamba atumie dhamana ya cheo chake kizito bandarini kufanikisha hilo. Ila alikuja kugundua asingeweza kufanikisha kazi hiyo mwenyewe. Angekwapuaje pembe hizo za tembo huko mbugani kwa wepesi? Ilimlazimu amtafute na amshirikishe bwana Pius wa TANAPA.
Kuhusu usalama wake na wa bidhaa alimtafuta Mtemvu wa jeshi la polisi huku usafirishaji wa bidhaa hiyo mpaka ulaya akimshirikisha Filbert na K square kwa kutumia kampuni zao kubwa za usafirishaji wa bidhaa baharini.
Tamaa hulevya. Raheem aliona mgao wa bwana Kim wa asilimia sitini na tano ni mkubwa mno, angepata pesa ndogo. Alihamishia biashara yote kwa wenzake kwa makubaliano kwamba atachukua asilimia arobaini na tano na itakayobaki atawapa wagawane, makubaliano yakapita. Bado pesa ilikuwa ni nyingi mno.
Raheem alitikisa kichwa chake akijitahidi kufuta kumbukumbu hiyo akilini. Aliiona ni kama jinamizi linalomuandama na sasa lataka kumtoa roho. Alilipia kinywaji akanyanyuka kufuata gari lale la kisasa aina ya Jaguar. Alitokomea eneo hilo kwa mwendokasi mkubwa akifurahia mlio wa nguvu unaotoka kwenye gari lake uliofanya wapita njia na madereva wengine wamtizame.
Furaha hiyo ya majigambo ilikuja kukoma pale kwa kutumia kioo cha dereva alipomuona mtu kwenye viti vya nyuma. Haraka aligeuza shingo kutizama asione chochote, aliporudisha uso mbele akamkuta mtu yule kwenye kiti cha mbele alafu kufumba na kufumbua akapotea!
“Shit! What the ***!”
Raheem alitoa macho. Alipoteza umakini, gari likayumbayumba. Alijitahidi kulimudu na kulirudisha mstarini akafuta uso na kiganja chake kama mtu ambaye haamini alichokiona. Alishusha pumzi ndefu akakung’uta kichwa chake kofi.
“Na mimi naanza kuwa kama wale wapumbavu!”
Akasonya. Mapigo yake ya moyo na pumzi vilirejea katika hali ya kawaida lakini macho yake bado yalikuwa yanarandaranda yakitizama kila upande. Ndani ya dakika zisizopungua tatu, simu yake ikaita. Ilikuwa imejilaza kwenye kiti jirani. Alishituka. Kutizama ni nani akaona namba mpya. Alinyakua simu na mkono wake wa kushoto akaibandika sikioni.
“Haloo! … Ndio mimi, nani mwenzangu? ... Mgeni yupi? … Shenzi!” Alikata simu akasonya kwa hasira.
“Pumbavu kweli! Unadhani mimi wa kuchezewa chezewa enh? Kawatishe haohao!”
Alipomaliza tu, ujumbe ukaingia kunako simu. Mlio ulimjulisha hilo, akaiteka simu na kiganja cha mkono wake wa kushoto akaibia kuusoma ujumbe.
‘Tizama kushoto.’ Ujumbe uliagiza. Raheem pasipo kujiuliza mara mbili akageuza uso kutizama alipoelekezwa. Aliona Lori lililobeba mawe makubwa laja kwa kasi likitokea barabara ya kuchepukia iliyokuwepo hatua kadhaa kwa mbele. Haraka alisinya breki kwanguvu zote bila ya mafanikio – gari lilizidi kwenda. Nalo lori lilipiga honi kali likiendelea kutiririka kana kwamba breki zimefeli.
Gari la Raheem ghafula lilizima hatua kadhaa tu mbali na lori linalokuja kama faru aliyejeruhiwa. Moyo wa mwanaume huyo ulidunda kama ngoma ya mtaa. Milango haikufunguka wala gari halikusonga. Hakuwa na la kufanya zaidi ya kufunga macho yake angojee kifo.
Muda ulipita asihisi chochote. Alifungua jicho moja kwa uwoga akatizama, hakukuwa na lolote lile lililotukia. Sauti za honi na za watu zilisikika tokea nyuma ya gari lake.
"Wewee sogea bwana unatuchelewesha!"
Pipiiiii! Pipiiiiiii!
Foleni ya dharura ilikuwa tayari ishajiri. Raheem akiwa hajielewi, alikanyaga mafuta akaduwaa gari lasonga mbele. Kwa muda kidogo akili yake iliganda akabaki ameachama. Alikuja kushtushwa na muziki wa simu lakini hakuthubutu kupokea wala kuitizama mpaka pale aliposikia mlio wa ujumbe, akainyakua simu asome.
'Pole muheshimiwa, mengi yaja. Hautofaidi hizo pesa kamwe!'
Raheem akang'ata meno na kupiga ngumi usukani. Kwa pupa aliajiri vidole vyake juu ya vibonyezeo akaandika akibonyeza kwanguvu.
"Wewe ni nani?"
Ujumbe haukwenda. Raheem akalaani kwa tusi. Alifungua kidroo kilichopo pembeni ya usukani akatoa bunduki yake ndogo.
***
Muendelezo soma hapa