Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

* SURA YA TATU *

Punde bwana Mtemvu aliposhuka kwenye gari, alitoa simu yake mfukoni akampigia mtu aliyemtunza kwa jina la Ninja. Aliongea naye kwa muda mfupi tu kisha akairudisha simu yake mfukoni akielekea kwenye kiti cha mgahawa mkubwa wenye jina la STEERS. Aliketi hapo akichezea simu yake kubwa nyeupe.

Ndani ya muda mfupi mhudumu alikuja na kumsikiliza, akahudumiwa. Ndani ya dakika zisizozidi kumi na tano magari mengine mawili yenye nembo za STK yakafika eneo la mgahawa. Watu wanne walishuka na kuelekea upande alipo mzee Mtemvu. Nao walisikilizwa na kuhudumiwa na wahudumu kisha maongezi yakachukua nafasi.

“Tujipongezeni jamani, hatimaye tumerudisha amani mioyoni mwetu … Cheers!” Mtemvu alibwabwaja wakagongesha glasi zao za mvinyo wakizisindikiza na matabasamu mapana usoni mwao. Waliongea maneno machache huku vicheko vikiwa vingi.

Baada ya muda waliagana na kutakiana kazi njema lakini mzee Mtemvu hakuondoka pale mgahawani. Baada ya dakika kadhaa alijumuika na kijana mmoja aliyekuwa anamuita kwa jina la Ninja. Alikuwa ni kijana mrefu mno mwenye misuli minene na kifua kikubwa kama makalio.

Alikuwa kavalia kombati la jeshi na macho akiyafunika kwa miwani kubwa ya jua. Alisalimia kisha akaketi wakaanza kuteta na mzee Mtemvu kwa sauti ya chini mno wakitazama usalama. Mzee Mtemvu aliingiza mkono mfukoni mwa koti akatoa shilingi milioni moja na kumkabidhi Ninja ambaye hakupoteza tena muda pale, akajiondoa.

Huko nyuma, mzee Mtemvu naye alitizama kushoto na kulia kisha akalifuata gari lake na kutokomea. Ila kulikuwa kuna mtu anamtizama muda wote akiwa pale mgahawani. Hakujua. Na si tu kumtizama, bali sasa alikuwa anamfuatilia hatua kwa hatua akiwa katika muonekano wa kivuli kilichoonekana pale tu mwanga wa jua ulipokiangazia.

Gari la Mtemvu, mtumishi mkubwa wa serikali, sasa liliacha lami likashika barabara ya vumbi iliyoelekea moja kwa moja na kukomea mbele ya geti kubwa jekundu lililojishikiza kwenye ukuta mrefu mnene wa rangi ya samawati. Hapo geti lilifunguka lenyewe gari likaingia na kisha geti likajifunga.

“Mpenzi, nimerudi nyumbani!” Mtemvu alipayuka baada tu ya kumaliza kuongea na dereva wake.

Nyumba ilikuwa kubwa na ya kuvutia; vigae vyekundu viliezekwa kwa juu, madirisha yake makubwa yalipachikwa vioo, chini kulitandikwa tiles, kuta zilipakwa rangi nyeupe, na bustani kubwa ya maua ya kupendeza ilitambaa mbele ya uso wa nyumba. Ilipendeza.

Mtemvu alifika mlangoni, mkewe: Mama Beatrice, akatoka na kumkumbatia.
“Karibu, mpenzi.” Alimbusu mumewe kwenye lips.
Japokuwa umri wao ulikuwa si haba, mapenzi yao hayakusita kujionyesha. Mtemvu alirudishia busu wakaingia ndani.

Walioga na kula wakajipumzisha sebuleni. Mtemvu alivalia bukta fupi rangi ya manjano na kaushi nyeupe huku mkewe, Mama Beatrice, akijisitiri kwa khanga pekee. Walikuwa wanapiga soga za hapa na pale haswa juu ya msiba wa karibuni. Watoto hawakuwepo hivyo walikuwa huru kushikana na hata kutomasana mara zingine.

Baada ya muda kidogo walinyanyuka kwa milengwa ya kueleka chumbani kujilaza. Ila kabla hajajitoa sebuleni, Mtemvu aliendea dirisha akafungua pazia na kuchungulia nje, akaliona gari lake. Alitahamaki.

“Mbona Mustafa hajaondoka?”
Alikunja sura.
“Si nimemwambia apeleke gari service?”

Mustafa, mwanaume wa makadirio ya miaka hamsini na mbili, ni miongoni mwa watu wapole wenye sauti ya chini. Ndiye mtu aliyekuwa anayempa kampani Mtemvu muda mwingi kwa kuwa naye garini.

Anamfahamu mkuu wake akiwa katika hali yoyote ile; anajua wakati ambao mkuu wake anamtaka aongee na wakati gani anaomtaka anyamaze. Zaidi ya yote anafahamu vyema siri za mkuu wake, pengine kuliko mkewe.

Mtemvu alipata shaka. Alitoka nje akalifuata gari, alipolifungua mlango akakuta Mustafa amelalia usukani. Alimuita lakini hakuitika. Alimshika begani akamvuta kumnyanyua.

La haula!

Mustafa alikuwa anamimina damu mdomoni na uso wake haukuonyesha kutojitambua. Moyo wa Mtemvu ulitetemeka na akajikuta anahisi hofu imemtambaza.

“Mustafa! Mustafa!” Aliita akimtikisa lakini Mustafa alikuwa kimya. Alimshusha kwenye gari akamlaza chini. “Mustafa! ... What is this? Mama Beatrice! Mama Beatrice!” Mtemvu aliita. Aliinamisha kichwa chake akakilaza kifuani mwa Mustafa: kifua kilikuwa kimya, tuli.

Aliponyanyua kichwa chake, mkewe – mama Beatrice – alikuwa tayari ameshafika, na msichana wa kazi – Habiba – alikuwa amesimama mlangoni. Mvulana wa kazi naye – Lupi – alikuwa amefika eneo la karibu.

“Nini baba?” Mama Beatrice alichuchumaa. “Nini kimetokea?”
“Sijui! Nimemkuta Mustafa hivi. Anatoka damu na mapigo yake ya moyo yamesimama!”
“Tumpeleke hospitali! … Au mpigie dokta wako!”
“Dada, embu niletee simu yangu hapo kwenye kochi.”

Dada, msichana mchanga mwenye umri kati ya 15 mpaka 18, aliyevalia gauni lake la pink iliyofifia na kiremba kichwani, mwembamba mrefu na mwenye uso wa upole, alielekea alipotumwa akarejea na simu ya bosi.

Mtemvu akampigia dokta.
Dokta aliwasili ndani ya dakika thelathini. Aliukagua mwili wa Mustafa kwa dakika kadhaa, akatikisa kichwa.

“Amefariki.”
“Nini kimemuua?” Mtemvu alidakia. Dokta akameza kwanza mate.
“Sijui, bado sijafahamu. Nahitaji kuufanyia uchunguzi zaidi.”
“Sawa. Acha basi nitoe taarifa polisi.”

Mtemvu alichukua simu yake akapigia polisi. Ndani ya muda mchache polisi walifika wakahoji na kufanya msako mwepesi bila ya matunda, mwili wa marehemu ulichukuliwa polisi wakaenda na daktari. Mtemvu pamoja na mkewe walirudi ndani tukio hilo bado likiwa kichwani na midomoni mwao. Walijilaza kitandani giza la usiku likazidi kudaka umri.

Ila Mtemvu hakupata usingizi.

***

Muendelezo soma hapa
 
* SURA YA NNE *

Alikuwa akijigeuza huku na kule kichwani akimrejelea Mustafa. Hivi ni kweli amekufa ama naota? Ilikuwa ngumu kuamini. Nani aliyemuua ama kipi kilichomuua? Hilo ndilo lililomuumiza haswa kichwa na kumkosesha amani.

Kuna muda alihisi kulala ndani ilhali jambo kama hilo limetukia ndani ya uzio wake ni uzembe. Vipi kama muuaji bado yu ndani anatafuta roho yake? Aamke akamsake? Hapana! Roho ilikataa. Kwakuwa mkononi alikuwa amelala na bunduki yake ndogo hivyo hakuwa na haja ya kuogopa, alijifariji.

Baada ya masaa kadhaa macho yake yaliyokuwa yanapepesa huku na huko yalichoka, yalifumba pasipo kupenda. Alijitahidi kupambana nayo lakini mwishoni alikuwa mshindwa akatwaliwa na usingizi mzito uliokuja kukatishwa kikatili asubuhi na mapema na sauti ya mkewe.

“Amka uende kazini, muda umewadia!” Aliamrisha Mama Beatrice. Ilikuwa ni mara yake ya nne akijaribu kufanya hilo zoezi pasipo na mafanikio na sasa alifaulu baada ya kuropoka.

Mtemvu aliuvuta mwili wake kivivu akaketi. Alitazamatazama kushoto na kulia asione bunduki yake. Mkewe alitikisa kichwa akamwambia:
“Imedondokea huko chini! … Sijui ulikuwa unamlinda nani na hiyo bunduki usiyojua hata ilipo.”

Mtemvu aliichukua bunduki yake akaitizama, kumbe hata ndani haikuwa na risasi!l Aliitupia kando akapiga mhayo wa nguvu. Alitikisa kichwa chake akanyanyuka aende bafuni akijitahidi kukaza macho yake mekundu yaliyokuwa yanafumba mara kwa mara pasipo ruhusa.

Alifuata kioo cha bafu akajitizama, aliteka mswaki na kuudumbukiza mdomoni aswaki. Alipiga mswaki chapuo la kwanza, akainama na kutema povu. Kimbembe alipoamsha sura yake atizame tena kioo; ajabu alikutana na sura ya mtu mwingine kiooni! –Sura ya mwanaume mweusi mno mwenye macho makubwa meupe na lips zenye nyama nene.

Mtemvu aliduwaa akadondosha mswaki. Moyo wake ulisimama kisha ukaanza kukimbia mbio mno. Alihisi mwili umekuwa wa baridi ghafla. Kufumba na kufumbua taswira yake ilirejea kwenye kioo, maandishi yakajichora:

‘Nadai roho yako ila sina papara nayo’
Alifikicha macho yake na kutizama tena. Maneno hayakuonekana!
“Iishh! Hivi naota au?”
Alinawa uso wake na maji aondoe maulevi ya usingizi. Alitizama tena kioo asione kingine chochote isipokuwa taswira yake. Aliishia tu kutikisa kichwa akamalizia kujihudumia na kutoka nje ya bafu.

***

Muendelezo soma hapa
 
* SURA YA TANO *

Mama Beatrice alikuwa ametoka ndani ya chumba lakini akiwa tayari ameshamuandalia mumewe nguo akiwa amezilaza kitandani. Kwa haraka Mtemvu alijiandaa akitizama saa yake ya mkononi mara kwa mara. Akiwa anavalia viatu vyake apate kuhitimisha zoezi hilo, mara alisikia sauti kali ya ukunga – sauti ambayo haikumchukua muda kuigundua kuwa ni ya mkewe, Mama Beatrice.

Kabla hajamaliza kuvuta pumzi, Mama Beatrice alikuwa tayari ameshafungua mlango kwanguvu. Alimtizama mumewe na sura iliyotepeta hofu. Aliongea kwa pupa la kigugumizi akionyeshea kidole alipotokea.

“Baba Bite! – mama yangu – kule! Twende ukaone! Twendee!”
“Kul – kule wapi? Kuna nini?” Mtemvu aliuliza kwa papara. Uso wake ulibadilika ukafanana na ule wa mkewe.

“Wamekufa!” Mama Beatrice aliropoka kisha akanyamaza ameze mate na kuvuta pumzi.
“Habiba – Lupi! Wameuwawa! Uwiiiiii! – Wote wamekufaa!”

Haraka Mtemvu alikwapua bunduki akaunyakua mkono wa mke wake wakaelekea huko tukioni. Hakukumbuka hata kama hiyo bunduki haikuwa na risasi japokuwa alishaitazama.

Walifika eneo la tukio, nje kibarazani, Mtemvu akatokwa na macho. Alishuhudia miili ya Habiba na Lupi ikiwa imelala kibarazani inaogelea kwenye dimbwi la damu nzito, damu zilitokea kwenye matundu mawili marefu yaliyotobolewa kwenye kila shingo ya marehemu. Kwa mujibu wa michoro ya damu ilikuwa ni wazi miili hiyo iliiburuzwa tokea vyumbani mpaka pale.

“Mtemvu, kuna nini kinaendelea?” Mama Beatrice alilia. “Kuna nini humu ndani? Kuna nani humu ndani?” Aliuliza Mama Beatrice akiwa karibu mno na mume wake. Mwili wake ulikuwa unatetemeka kwa baridi na akivuja jasho kwa muda huo huo. Moyo wake ulikuwa unaenda kasi na alihisi maumivu ya kichwa.

Mtemvu alijivika ujasiri akaanza kupekua nyumba nzima huku mkono wake uliobebelea bunduki ukiwa mbele kumlinda na kumuepushia shari, nyuma yake Mama Beatrice hakubanduka hata kidogo. Walimaliza nyumba nzima wasione kitu. Hakukuwa na mtu yeyote isipokuwa wao wenyewe!

“Wapigie simu polisi waje! … Mie siwezi kukaa hapa tena.” Mama Beatrice alisema kwa sauti ya chini akimtizama mumewe na macho yanayovuja machozi.

Baada ya nusu saa polisi walifika na kufanya upekuzi. Waliuchukua miili ya marehemu wakaongozana pamoja na Mtemvu na mkewe kwenda kutoa maelezo wakati huo miili ikitangulizwa hospitali. Baada tu ya dakika thelathini Mtemvu na mkewe wakatoka kituoni wakiwa wameongozana na polisi mmoja mrefu mwembamba ila mwenye mustachi mpana.

“Pole sana, Mkuu. Kama isingelikuwa wadhifa wako ungelikuwa matatani sana. Nakushauri umtafute inspekta Vitalis, huwezi jua maadui wako wamepanga nini mbele yako. Usalama wako u matatani sasa.” Polisi alishauri. Mtemvu akatikisa kichwa.

“Sahihi. Nadhani huo ni ushauri mzuri, nitaufanyia kazi lakini hakikisheni habari hizi hazienei popote pale. Hakuna sikio lolote litakalosikia hizi taarifa.”

“Halina shida hilo. Siku njema, mkuu.”
“Nanyi pia. Ila dokta anaweza akaja kuonana na nyie akitoka hospitali kuikagua ile miili. Endapo akija mumpe ushirikiano.”
“Sawa, Mkuu.”

Mtemvu alijiweka kwenye gari pamoja na mkewe wakahepa. Alimpitisha Mama Beatrice kwa dada yake Kigamboni, yeye akajipata pembezoni ya bahari, ndani ya hoteli moja kubwa ya kifahari akijaribu kufanya jitihada za kuburudisha akili yake dhidi ya tafrani lililotoka kumkabili.

***

Muendelezo soma hapa
 
So far so good.asante.ila usikae wee ukatuweka kwenye kusubiri
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom