Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Daaah. Huyu Miraji si amesomea uDR huyu? Mbona ghafla kawa Mafia!
 
mpk sasa kuna kuwekwa episode 4 kweli steve
 
SURA YA KUMI NA TISA

Asubuhi iliwasili. Siku ilikuwa kavu isiyo na dalili zozote za kunesha. Anga lilikuwa na rangi ya bahari, mawingu yakijitengeneza umbo la mawimbi.

Mbele ya nyumba ya Mtemvu, ilisimama gari dogo nyekundu Toyota Vitz. Mlango ulifunguliwa akatoka mzee mrefu mweusi mwenye ndevu nyingi na kiwaraza kikali akiwa amevalia kaunda suti ya kijivu, mkononi akibebelea rambo kubwa nyeusi. Moja kwa moja mzee huyo alifuata geti akabonyeza kengele.

Mlinzi alifungua kidirisha kidogo kilichopo kwenye geti akamtazama.

“Nikusaidie nini?”
“Samahani. Naitwa Ali wa Fatuma. Nina shida ya kuonana na mwenye nyumba.”
“Shida gani?”
“Za kibiashara.”
“Zipi?”
“Ni mambo binafsi.”
“Yapi?”
“Ndugu, ambacho hatuelewani ni nini? Mwambie bosi wako kuna mgeni anaitwa Ali wa Fatuma, yupo nje anamsubiri.”
“Ametoka.”
“Ameenda wapi?”
“Kwenye biashara zake.”
“Zipi?”
“Ni mambo binafsi.”

Ali wa Fatuma alitikisa kichwa akitabasamu.

“Wewe ni mgeni hapa, enh?” Aliuliza na kuendelea: “Si bure ndio mana huna adabu. Mwambie mama Mtemvu, Ali wa Fatuma yupo nje. Tusigombane bure.”

Mlinzi alimtizama mgeni yule kuanzia juu mpaka chini akatikisa kichwa. Aliondoka akimuacha Ali wa Fatuma nje ya geti, baada ya muda akarudi na Mama Beatrice.

“Ndio huyu hapa!” Mlinzi alimnyooshea kidole Ali wa Fatuma kana kwamba anamshtakia.
“Ooh Mtaalamu!” Mama Beatrice alilipuka kwa furaha. “Karibu! karibu sana!”
“Ahsante, mama.”
“Wewe! Ebu fungua geti!” Mama Beatrice alimuamuru mlinzi, haraka geti likafunguliwa mgeni akaingia.
Ali wa Fatuma alimtizama mlinzi na jicho kali asiseme kitu. Mlinzi alinywea kana kwamba amemwagiwa maji ya baridi.
“Mtaalam, umeacha gari leo?”
“Kuna mtu analitumia, amenishusha hapa na kwenda zake.”
“Oooh! Karibu bwana.” Mama Beatrice alisema akifungua mlango. Waliingia wakaketi sebuleni.
“Unapendelea kinywaji gani, mtaalam?”
“Nashukuru, wala usijichoshe mama. Mzee nimemkuta?”
“Hapana. Vipi hujawasiliana naye?”
“Simu yangu imeharibika kioo jana baada ya kuikalia hivyo nilishindwa kabisa kumtaarifu. Lakini anafahamu kwamba ningekuja, niliwaambia wasinifuate, nitawafuata mwenyewe.”
“Basi wacha nimpigie.”
“Itakuwa vema.”

Mama Beatrice alienenda chumbani baada ya muda kidogo akatoka akishikilia simu mkononi.

“Anakuja.” Alimpa taarifa Ali wa Fatuma ambaye alitikisa kichwa kwa mapokeo.

Ndani ya muda usiozidi robo saa, Mtemvu alitia mguu ndani. Tabasamu lake lilikuwa pana alipomuona mgeni, walikumbatiana kwa furaha wakaketi kwa karibu. Mwanamke akawapa faragha.

“Kama nilivyokueleza juu ya tatizo letu. Tumekuwa watu wa mikasa mikasa na sisi, hatupati usingizi vizuri, hatuli kikashuka kabisa!”

Ali wa Fatuma alicheka akitingisha mabega yake. Aliponyamaza aliweka uso wa kutisha kama vile si yeye aliyetoka kukenua.

“Tatizo lako limeisha!” Alisema kwa kujiamini, “Alimradi Ali wa Fatuma ameshafika, tatizo lako limekwisha!” alisema huku akitikisa kichwa kwa uhakika.
“Nitashukuru sana, Mtaalam. We niambie tu nini vinahitajika, mimi nitakupatia.”
“Sawasawa.” Ali wa Fatuma aliitikia.

Alifunua rambo lake akatoa vibuyu viwili, moja kikubwa na kingine kidogo. Alitoa mkia wa ng’ombe akauweka pembeni kisha akatoa na kaniki nyekundu na nyeupe zikifuatiwa na kioo cha saizi ya kati.

Alisimama akajivesha kaniki yake. Aliendea kona ya nyumba akasimama hapo mkononi akishikilia mkia wa ng’ombe ambao aliupeleka kushoto na kulia, kulia na kushoto. Baada ya hapo alipangusia makalio yake hapo na kusimama akiwa anarusha rusha macho yake kama vile anatafuta kitu kinachotambaa kwenye dari.

Alitikisa kichwa akisonya. Alifuata kioo chake akakipangusia na mkia wa ng’ombe, akawa anakitizama.

“Bwana Mtemvu, huyo mtu anayekusumbua ndie huyu?” Ali wa Fatuma aliuliza akimuoneshea Mtemvu kioo.
Mtemvu alitizama macho akajikuta akiropoka: “Ndiye yeye huyo huyo!”

Ali wa Fatuma akacheka.

“Matatizo yako yamekwisha. Nilikuambia.”
“Sasa mtaalam nilikuwa nataka kujua. Huyo mtu katumwa na nani?”
“Ili tupate kujua mengi inabidi tutoe kafara. Kuku mweupe anahitajika kwa ajili ya kujua nani kamtuma na mbuzi mweupe kwa ajili ya kumdhibiti.”
“Hilo halina shida. Lini sasa?”
“Hata leo kama inawezekana.”
“Sawa! Basi ningoje hapa mtaalam nika …”
Simu ya Mtemvu iliita. Aliitizama akapokea.
“Eeenh shem, habari yako? … Mmevamiwa? Usiku huu wa kuamkia leo? ... He! Wewe! … Nakuja nakuja! Sasa hivi!”
Alikata simu akamgeukia Ali wa Fatuma na uso wenye mashaka na woga akamtaarifu aliyopashwa kwenye simu.
“Naomba urudi kesho. Sina jinsi tena kwa sasa.”
Ali wa Fatuma aliridhia. Mtemvu alimkabidhi noti kadhaa nyekundu kisha akamuita mke wake na kumpa taarifa alizozipata. Akaaga na kwenda zake.
“Inspekta, upo wapi? ... Naelekea kwa Raheem, ameuwawa jana usiku na majambazi … Basi nakupitia hapo muda si mrefu … Sawa.”

Simu ikakatwa na kurushiwa kwenye kiti jirani.

Dakika chache kupita gari likazima katikati ya barabara. Mtemvu alishuka akafungua boneti asione tatizo. Alipiga tairi teke akilaani. Alifungua mlango wa gari akachukua simu yake. Alikuta ujumbe umetumwa na namba ngeni muda mfupi uliopita:

‘Sasa kuna mawakala wawili wa kifo. Jiandae vema kwa yeyote atakayekutangulia.’

Alimaliza kuusoma huo ujumbe, ghafula gari kubwa aina ya Scania likabamiza nyuma ya gari lake kwanguvu. Mtemvu alirushwa mbali vioo vikimfuata na kumchana chana.

Gari lake liliserereka kwa kusukumwa na Scania, likaenda kubamiza gari lingine kwa mbele.
Ni kama vile maigizo yakitukia mbele ya macho ya Mtemvu. Alijaribu kunyanyuka lakini ghafula mkono ulimzuia tokea nyuma.

“Tulia kwanza mzee.”
Alikuwa ni kijana mwembamba aliyevalia hovyo, mdomoni mwake akibebelea sigara.

Ndani ya muda mfupi, watu walisogea na kujaa eneo la tukio. Mtemvu aliwekwa katikati ya umati akidhaniwa amechachawa na ajali. Mashahidi walisogelea Scania kumtizama dereva ila hawakumkuta.

“Ameshakimbia!”
“Ametokea wapi?”
“Sijui! Labda dirishani!”
“Vipi mzee unajisikiaje?” Shahidi mmoja alimuuliza Mtemvu kama aliyeguswa.
“Ni mgongo tu unanivuta kwa maumivu.” Mtemvu alijibu akijikanda mgongo. Mara akajipapasa mifukoni.
“Simu yangu? ... Kuna yeyote amenionea simu yangu?”

Hakuna aliyejibu. Watu wengine walianza kuondoka eneo la tukio.

Mtemvu alinyanyuka akafuata gari lake akishikilia kiuno chake na kujikongoja. Kabla hajalifikia alirudishwa alipotoka na mlipuko mkali!

Gari lake liliwaka moto kama kifuu. Kwa haraka lilianza kuyaambukiza magari mengine yaliyo karibu – eneo likageuka tanuru. Makelele na mayowe yakarindima. Kila mtu alikimbilia alipopahisi yeye ni salama.

Hapo ghafula Mtemvu alikurupuka akihema kwa pupa. Kumbe alikuwa anaota. Bado alikuwa ndani ya gari lake lililozima.

Alitizama kwenye kochi la pembeni akaona simu yake, aliichukua akaitizama. Mara ikaita namba kwa namba ngeni. Mtemvu aliitizama bila ya kuipokea. Simu ikakata.

Iliita tena na tena, badala yake Mtemvu aliamua kuizima kabisa. Ajabu ikaita tena! Mtemvu alikodoa macho ya mshangao. Alitoa betri akaitenganisha na simu, ajabu simu ikaendelea kuita.

Aliinyanyua akairushia nje kisha akafunga kioo. Alihema juu juu macho akiyakodoa kwa kutoamini. Kama vile haitoshi, simu iliita tena! Mara hii sauti ikitokea viti vya nyuma.

Mtemvu aligeuza shingo kutizama akamkuta mtu mwesu ti akiwa amejivika joho. Mtu huyo alimdaka koo kwanguvu akamminya. Mtemvu akahangaika mno kutafuta hewa bila ya mafanikio. Macho yalimtoka na mishipa ikamsimama. Alijua sasa kifo chake kimewadia japokuwa bado alikuwa mgumu kukubali.

Ilikuwa ni kama bahati, Inspekta akawasili hilo eneo kana kwamba alitaarifiwa kinachoendelea. Alijaribu kufungua milango ya gari la Mtemvu kwa nguvu zake zote bila ya kufanikiwa. Alichungulia ndani akamuona Mtemvu anazidiwa na isingechukua muda zaidi ya dakika moja tu apoteze uhai.

Alipiga ngumi kioo cha mlango wa gari akakivunja kisha akafungua mlango kwa ndani. Mtu mweusi akapotea kufumba na kufumbua.

“Mkuu, upo sawa?”

Koh! Koh! Koh! Mtemvu alikohoa akijitahidi kutafuta hewa kwanguvu. Inspekta alitizama kushoto na kulia, nyuma na mbele. Honi za magari zilikuwa zinaita, magari mengine yaliwavuka yakipita pembeni.

Baada ya Mtemvu kuvuta hewa ya kutosha, Inspekta alimtazama akamuuliza:

“Nini kimetokea?”
Mtemvu alibung’aa kama mtu mtu aliyeshushwa katikati ya jiji asilolijua. Alifagia uso wake na kiganja mara mbili, akamtizama Inspekta.
“Tuondoke!” Aliropoka. “Tuondoke hapa, Inspekta!” Inspekta akamshika mkono.
“Naomba niendeshe, Mkuu. Tafadhali.” Inspekta alipendekeza. Alijiweka kwenye kiti cha dereva akakanyaga mafuta, gari likasonga mbele kinyume kabisa na hapo mwanzo lilipogoma.
“Tunaelekea kwa Raheem kama kawaida, Mkuu?”
“Ndio. Tuelekee huko.”

Kisha kimya kikatawala miongoni mwao.

Walifika kwenye nyumba ya Raheem wakakuta watu tayari wamejazana. Walishuka wakaungana na kadamnasi.

Mtemvu alimfuata mke wa Raheem kumuuliza kilichotukia. Muda mfupi, Pius na K square nao wakafika eneoni kuungana na jumuiya ya waombolezaji. Wakati huo Inspekta alikuwa ameketi, lakini macho yake yalikuwa yamesimama yanatembea huku na huko kutizama usalama.

Haukupita muda mrefu, Pius, K square na Mtemvu wakaitana kando kuteta. Ilikuwa siri, hata Inspekta hakuhusishwa. Macho yao yalikuwa yanazurura mara kwa mara kutizama na kuhakikisha kama kweli wapo wenyewe.

“Mke wake amesema walivamiwa na mtu wasiyemjua. Hajachukua chochote zaidi ya kumuulizia na kumuua Raheem.” Mtemvu aliwaambia wenzake.

“Mmmh.” K square akaguna. “Jamani, mbona tunaishi kwa hofu hivi? Huku mambo ya ajabu huku majambazi! Roho zipo mkononi! Tutapona kweli?”
“Vipi kumhusu mtaalamu?” Pius aliuliza. K square akatikisa kichwa kama mtu aliyependezwa na hilo swali.
“Mtaalamu yupo.” Mtemvu alijibu. “Nimemuambia aje kesho nyumbani. Alikuja leo lakini taarifa za msiba zikaingilia kati.”
“Hawezi akaja hata hiyo kesho!” K square alitamka. “Itabidi tuwe tunashughulikia mazishi ya Raheem. Labda umwambie aje keshokutwa.”

Baada ya mabishano kidogo, walikubaliana juu ya hilo.

“Ila mnahisi ni nani atakuwa kamuua Raheem? Kuna mtu yeyote aliyekosana naye?” K square aliuliza.
“Sijui!” Mtemvu akajibu. “Sina taarifa yoyote juu ya hilo. Una ufahamu wowote kuhusu hilo?” Mtemvu aliuliza huku akimtazama Pius.
“Hapana. Sina.” Pius alitikisa kichwa. “Unajua Raheem si mtu wa kuweka wazi sana mambo yake. Ni mtu wa kujivuna muda mwingine. Huwezi jua alikuwa na maadui gani.”
“Ila hao maadui hawana uhusiano wowote na sisi?” Mtemvu aliuliza. Walitizamana kwa macho ya viulizi. Hakuna mtu aliyejibu swali. Mwishowe walifikia makubaliano kama ya awali, kuongeza ulinzi miongoni mwao lakini mara hii wakingojea ya mtaalamu.

****

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI

Tip! Tip! Tip! Tip! Simu iliita. Iliketi juu ya kitanda cha Miraji. Mkono uliivuta simu hiyo na kuipeleka usoni mwa mwenye nayo. Ulikuwa ni ujumbe mfupi ukisomeka: ‘nipo nje nakusubiri.’

Miraji alinyanyuka akanawa uso. Alitoa begi lake kabatini. Alivalia nguo nyeusi kisha akatoka nje kupitia dirishani.

Ilikuwa ni usiku. Taa za majumba zilikuwa zimewaka. Kwa mujibu wa saa ya mkononi ya Miraji, ilikuwa ni saa nne kasoro.

“Twende!” Sauti ya Miraji ilisikika. Gari likachoropoka kwa kasi. Dereva alikuwa Jombi mdomoni akitafuna mirungi.
Walielekea moja kwa moja mpaka hospitalini. Walipofika walizima gari na kutulia humo ndani kwa muda.
“Chukua mfuko mweusi hapo nyuma” Jombi alielekezea kidole chake viti vya nyuma. Miraji akavuta mfuko na kuufunua, ndaniye akatoa joho refu jeupe.
“Vaa hilo.” Jombi alioda. Miraji alivaa hilo joho akatengeneza mithili ya daktari.
“Sasa uwe makini sana. Hakikisha hufanyi makosa. Baada ya dakika kumi na tano kamba itakuwa dirishani tayari.”
“Usihofu.” Miraji alisema akichomeka kisu nyuma ya kiuno chake. Alitoka ndani ya gari, kwa kujiamini akatembea akielekea ndani ya hospitali. Hatua zake zilitengeneza sauti kutokana na ukimya ulioanza kujijenga kwa mujibu wa muda mbali na hapo alitembea kwa ukakamavu akijazwa na dhamira.

Kabla asiingie ndani ya jingo la hospitali, sauti ya kuamuru iliita nyuma yake.

“Wee simama hapo!”

Walikuwa ni walinzi. Wawili kwa idadi. Walishikilia virungu vikubwa mkononi mwao. Miraji alijigeuza akawatizama.

“Samahani. Tunaomba kitambulisho chako.” Mlinzi mmoja alisema huku akinyoosha mkono.

Miraji alikaa kimya. Ni kama vile alikuwa amepigwa bumbuwazi. Alitumikisha akili yake ajue cha kufanya haraka iwezekanavyo kabla mambo hayajaharibika.

“Tunaomba kitambulisho chako, hujasikia?” Mlinzi mwingine alirudia swali.

Watu walitekwa na hilo tukio, walisogea, wengine waliopo mbali wakafuatilia kwa makini.
Miraji aliwatizama hao watu kisha akakunja sura akiwatizama walinzi.

“I do not understand you. What do you want? You are wasting my time, I have patients to look after.”
Miraji alisema kiingereza hiko kwa kujiamini. Walinzi wakatizamana.
“Umemuelewa?”
“Hapana!”
“Atakuwa daktari, tumeingia choo cha kike.”
“Muombe msamaha sasa.”
“Kwa kiingereza? ... Mie sijui!”
“Sorry dokta! … Sorry.” Mlinzi alijikomba kwa Miraji akijilazimisha kutabasamu. Miraji alitikisa kichwa chake kisha akaondoka. Alishusha pumzi ndefu akauweka mkono wake palipo na moyo.

Nusura nikamatwe, alijisemea mwenyewe akitabasamu.

Alitizama saa akaongeza kasi ya kutembea. Alipofika mlangoni mwa chumba alichokuwepo Filbert alimkuta mwanaume ameketi kwenye viti vya nje akichezea simu. Alimsalimia akaingia ndani.

Alifunga mlango na komeo akamuamsha Filbert akimuita jina lake mithili ya mtoto anayemuamsha babaye mpenzi.

“Shikamoo, mzee.”
“Marhaba.” Filbert aliitikia akistaajabu. “Wewe ni dokta mpya?”
“Ndio.”
“Mbona sikuambiwa kama amebadilishwa?”
“Watakuwa wamesahau.”
“Vipi, mbona umekuja muda huu?”
“Kuna ujumbe nataka kuufikisha kwako.” Miraji alisema kisha akatizama saa yake.
“Ujumbe wa nani?”
“Wa bwana Malale.”
“Bwana Malale?” Filbert alikodoa macho. Alijitahidi kunyanyuka maumivu yakamshinda.
“Bwana Malale yupi?”
“Malale mliyemuua wewe na wenzako.” Miraji alisema akitabasamu.

Filbert alitaka kupayuka haraka Miraji akamziba mdomo na mkono wake wa kushoto, wa kulia akachomoa kisu.

Mlangoni hodi ilibishwa. Mwanaume aliyekutwa kwenye kiti akichezea simu alibamiza mlango akitaka kuingia, mlango haukufunguka.

Aliita daktari daktari lakini hakukuwa na majibu. Aliita Filbert Filbert asisikie kitu. Aliita walinzi wakaja, mlango ukavunjwa. Ndani wakamkuta Filbert ametapaliwa na damu kifuani. Hakukuwa na mtu mwingine ndani ya chumba. Ila dirisha lilikuwa wazi.

“Kuna mtu aliingia humu! Alikuwa amevalia kidaktari!” Mwanaume aliwaambia walinzi.
“Rambo, washtue getini fasta!” Mlinzi mmoja alimwambia mwenzake. Mwenzake akanyofoa redio call kifuani mwake akaiweka mdomoni na kuwataarifu walinzi wa getini wazuie watu wote watokao.

Hawakufua dafu. Mtu waliyekuwa wanamtafuta alikuwa tayari ameshapotea eneo hilo kwa kasi kubwa ya gari.

Jombi aliondoa chombo kama chizi. Hakusimama wala kupunguza mwendo mpaka walipopotea kabisa maeneo ya karibu na hospitali. Kituo cha kwanza kilikuwa mbele ya nyumba ya wakina Miraji. Miraji aliagana na Jombi akanyookea dirishani kwake.

Alijaribu kufungua dirisha lakini hakufanikiwa, dirisha lilikuwa limefungwa ndani na komeo.

“Oh no!” Miraji alilalamika. Hakuwa na chaguzi lingine zaidi ya kuufuata mlango. Alijua wazi mama yake atakuwepo sebuleni na ni ngumu kukatiza asigundue.

Alipiga moyo konde akisema:

“Leo nitakuwa mwangalifu zaidi.”

Alitembea pole pole akaufungua mlango na kuurudishia taratibu. Alivuta pumzi ndefu akaanza kunyata akihakikisha hakuna mlio wowote unaotokana naye, alifanikiwa katika hilo.

Ila mlio wa alarm toka kwenye simu ya mama yake ukatia mchanga kitumbua. Bernadetha aliamka kutizama simu yake akamuona mwanae.

“Miraji, umetoka wapi?”

Miraji kimya. Bernadetha aliamka akamsogelea mwanae. Alimtizama usoni, Miraji akatizama chini.

Bernadetha alimtizama vema mwanae akaona ana damu mkono wake wa kuume. Kama mtu ambaye hakuamini, aliuliza:
“Miraji, nini hiki?”

Alipeleka pua yake akanusa kabla Miraji hajaupokonya mkono wake kwanguvu.

“Miraji, hiyo si damu?” Bernadetha aliuliza.
“Ndio.” Miraji akajibu.
“Umeitoa wapi?”
“Niliumia.”
“Wapi? … Lete nione.”

Miraji hakutoa mkono wake. Bernadetha alijikuta akinyanyua mkono wake wa kuume akamzaba kofi.

“Umetoa wapi hiyo damu?” Bernadetha aliendelea kuuliza Miraji asijibu kitu.
“Lete begi hilo.” Bernadetha aliwaka akivuta begi la Miraji.

Miraji alitoa mikono ya mamaye kwanguvu kwenye begi lake kisha akaelekea chumbani na kujifungia.

Bernadetha akaangua kilio. Alimuita Miraji lakini hakutoka. Alikaa mlangoni mwa chumba cha Miraji akililia hapo.

Miraji alijilaza kitandani pembeni yake akiweka picha ya marehemu baba yake. Sauti ya kilio cha mama yake ilimfanya ashindwe kujizuia, naye akajikuta analia. Ila roho yake ilimwambia anachofanya ni sahihi na alitegemea mama yake angekuja kuelewa hapo baadae.

***

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI NA MOJA

Siku tatu zilipita msiba wa Filbert ukivuma na kutika.

Haikuwa jambo jepesi kwa Mtemvu na wenzake ambao sasa walishapata jibu kamili kwamba huyo muuaji atafuata pia roho zao. Wazo lao kuongeza ulinzi likionekana kukosa mashiko, uhitaji wa mganga ukawa juu kuliko awali. Waliamini hata huyo jambazi anayeua atakuwa na mahusiano na mtu yule wa ajabu, mtu mweusi, hivyo kumzuia ingehitaji pia nguvu za giza.

Kwenye kikao cha dharura walichofanya baada ya mazishi ya Filbert, waliafiki mtaalamu, Ali wa Fatuma, afike siku inayofuata kwa gharama zozote, huku tayari wakijiandaa kwa mahitaji ya kuku na mbuzi weupe kungoja ibada.

Jambo ambalo hawakulijua ni kwamba usiku wa siku hiyo, mmojawao alikuwapo kwenye orodha ya mauaji ya Miraji, ilibidi afe asione jua lingine likichomoza. Hiyo siku ndio ilikuwa siku yake ya mwisho kuvuta pumzi ya ulimwengu.

Gari la Jombi lilisimama mbali kidogo na nyumba ya K square. Ndani yake walikuwapo Miraji na Jombi vidoleni mwao wakishikilia misokoto ya bangi wakijaza moshi mzito garini. Kwa mbali redioni muziki wa rege uliita, Bob Marley akitumbuiza na wimbo wake wa taratibu Redemption song.

Jombi alinyonya msokoto wake wa bangi akameza moshi akiutolea puani kisha akamtazama Miraji na macho yake mekundu kama nyanya.

“Upo mwake?” Aliuliza. Miraji akatikisa kichwa akinyonya msokoto. Alipopuliza moshi nje akajibu,
“Nipo fresh. Wewe tu.”

Jombi alivuta pafu la mwisho kisha akazima msokoto na kuuweka ndani ya droo ya gari. Humo drooni alitoa bunduki ‘mguu wa kuku’ akamkabidhi Miraji. Akatoa tena bunduki nyingine akaikoki na kuishika. Aliibusu akitikisa kichwa.

“Leo ndio leo.” Alisema akitabasamu.
“Sasa ni hivi. Walinzi wapo watatu. Wewe utaingilia nyuma mimi nitaingilia mbele. Fanya kama tulivyokubaliana. Tumia bunduki kama tu ukiona hakuna namna nyingine, tusije tukajaza watu mapema bure.” Jombi alielekeza.

Walivaa vinyago na mabegi madogo migongoni. Walitoka garini wakagawana njia. Mwingine alienda nyuma ya nyumba mwingine akafuata geti na kutulia hapo kama anayesubiria jambo.

Miraji alikwea mti mkubwa ulio karibu na uzio wa nyumba. Alipofika juu alijirushia ndani ya jengo akafikia kwa mtindo wa kuchuchumaa bila ya kutoa kelele.

Haraka alikimbilia nyuma ya jiko la nje ya nyumba akajificha. Alivua begi lake akatoa mfuko wa mkubwa uliobebelea vyupa akaanza kuzitandaza kwa haraka eneo linalomzunguka. Alitoa mshipi akaufunga upande moja mlango wa jikoni pande nyingine akaishikilia yeye akiwa amejificha kisha akatoa chupa ya bia begini na kuibamizia ukutani kwanguvu.

Walinzi walishituka. Wawili haraka walikimbilia eneo la tukio na kumuacha mmoja getini. Hapo ndio Jombi akaweka kifaa kidogo getini kikatoa sauti ya gari lipigalo honi.

Kwakuwa hakukuwa na sehemu ya uwazi getini, mlinzi aliyebakia akawa hana namna, aliburuza geti kando ili apate kuchungulia. Hilo likawa kosa.

Kutoa uso wake kulimpa mwanya Jombi aliyekuwa amejibanza getini. Alishika kichwa cha mlinzi na kubamiza kwanguvu ukutani. Mlinzi akazirai.

Jombi aliingia ndani akafunga geti.

Huko nyumba upande wa jikoni, mlinzi mmoja tayari alikuwa amelala juu ya vyupa akimwaga damu. Mwenzake alikuwa kando damu zikimvujilia kichwani, pembeni kukiwa na jiwe ukubwa saizi ya kati. Miraji aliwatemea mate akiwatizama kwa kinyaa. Alishamaliza kazi ya kuwateketeza ndani ya muda mfupi tu.

Aliachana na hiyo miili akakimbilia mbele ya nyumba huko akaungana na Jombi wakaingia ndani ya nyumba kwa kuvunja mlango wasikute mtu sebuleni.

Walitazamana wakapeana ishara ya kusonga vyumbani, wakaanza kupita chumba baada ya chumba. Walivunja milango na kujitenga pembeni kusikilizia. Katika vyumba vinne walivovunja hawakukuta mtu yeyote. Na sasa kilibakia chumba kimoja tu wamalize vyote.

Kabla ya kuvunja mlango wa hicho chumba, Jombi alifuata swichi kubwa ya umeme akakata umeme. Alivunja mlango kisha akawasha kurunzi moja na kuirushia ndani.

Risasi zikashambulia hiyo kurunzi kana kwamba kuna mtu ameibebelea. Hiyo ikawa nafasi mujarabu kwa Jombi ambaye alibashiri vema risasi hizo zinapotokea akalenga risasi nne, sauti kali ya maumivu ikamjibu.

Miraji alipomulika kurunzi wakamuona K square amelala anaugulia maumivu akishikilia tumbo lake linalovuja damu. Miraji alimsogelea K square akavua kinyago chake na kumtizama mwanaume huyo aliyekuwa anagugumia akiomba abakiziwe roho yake.

“Nadhani unaijua hii sura.” Miraji alimulika uso wake. “Sina muda wa kupoteza. Nimekuja hapa kuchukua roho yako kama vile mlivyoichukua ya baba yangu, mzee Malale. Kawakute wenzako jehanamu.”

Miraji alitoa bunduki yake akampiga risasi kichwani K square kisha akamtemea mate kana kwamba ananuka.

Haraka walitoka ndani wakafuata gari lao na kutimka.

Ila hawakufahamu, ndani ya kabati la chumba hicho kilichoshuhudia mauaji kulikuwemo na watoto wawili mapacha wa K square: Jeniffer na Jenister. Makamo yao ya umri kumi na tano.

Watoto hao walishuhudia kila kitu kilichofanyika kwa baba yao kupitia upenyo wa kabati. Majambazi walipoondoka watoto hao walitoka kabatini wakaulilia mwili wa baba yao wakimimina machozi na makamasi.

Jombi na Miraji wasifike mbali na gari lao lililoendeshwa kasi kama upepo wakakutana na gari la polisi konani. Lilikuwa limeziba njia polisi watano wakitanda na bunduki barabarani wakiwaamuru washuke na kujisalimisha.

“Shiit!” Jombi alipiga ngumi usukani. “Atakuwa alitoa taarifa polisi yule mshenzi!”
“Sasa tunafanyaje?” Miraji aliuliza akitizama kwa woga.
“Funga mkanda. Hatuwezi tukakamatwa kirahisi hivi!”

Jombi alisema kimajigambo. Aliweka gia na kukanyaga mafuta akavamia vichaka vya kando ya barabara akatokea upande mwingine kwa kasi kubwa mno. Polisi wakaanza kufukuzia kwa nyuma ving’ora vikiita.

Moyo wa Miraji ulikimbia kwa kasi mno. Jasho lilimvuja. Alimtizama Jombi akamuuliza:

“Tutafanikiwa kweli?”
“Hilo sio ombi.” Jombi akajibu kwa kujiamini. “Ni lazima!”

Miraji alihisi Jombi anatania kusema maneno hayo katika hali waliyopo. Alitikisa kichwa chake akitizama vioo vya pembeni vya gari akashuhudia polisi wanakuja kwa kasi. Moja kwa moja akaona picha moja akiwa jela, nyingine akiwa amefariki kabisa, hayo ndiyo machaguzi mawili aliyoyapata kichwani.

“Hamia siti za mbele!” Sauti ya Jombi ilimshitua Miraji toka fikirani.
“Nageuza gari muda si mrefu kurudi tulipotoka. Nikigeuza, fungua mlango wako, tutawamwagia risasi za kushtukiza hao mbwa kufumba na kufumbua.” Jombi alitoa maelezo, Miraji pasipo kuuliza akayafuatisha.

Gari lilipiga breki kali likageuka pasipo polisi kutegemea. Kabla polisi hawajajipanga, Miraji alishafungua mlango, Jombi akishusha kioo. Risasi zilimiminwa kuelekea kwenye gari la polisi ambao hawakuwa na la kufanya kwa muda huo zaidi ya wengine kujificha wengine wakisulubishwa na risasi.

Vioo vya gari la polisi vilivunjika matairi yakipasuliwa. Jombi na Miraji walitokomea kwa kasi wakiwaacha polisi wasijue la kufanya.

Walipita nyumba fulani isiyokaliwa na mtu, Jombi akapaki gari hapo. Walivua vinyago wakatumia daladala kama usafiri kurudi majumbani mwao.

Miraji aliamini ni Mungu tu ndiye aliyewaokoa, tena kwasababu ana dhamira safi ya kulipa damu ya baba yake iliyomwagwa pasi na hatia.

***

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI NA MBILI

Asubuhi ilikucha kwa Ali wa Fatuma. Kibanda chake kidogo mbavu za mbwa kilikuwa kinamimina moshi mzito ukitokea kwenye madirisha yake madogo.

Sauti ya kukohoa ilisikika ndani ya kibanda hicho, baada ya muda kidogo mlango ukafunguliwa akitoka mzee Ali wa Fatuma. Alikuwa kavalia kaniki nyeusi kiunoni. Mdomoni mwake alikuwa ana kijiti kirefu alichotumia kusafishia meno. Mkononi alishika kopo kubwa lililobebelea maji.

Alinawa uso. Asimalize, akatoka mwanamke mweupe mchanga, Chausiku, akaungana naye kufanya shughuli sawa.

“Chai tayari, mume wangu.”
“Ahsante. Yani leo nina kazi kubwa sana. Umentilia maziwa?”
“Ndio, kila kitu kama ulivyotaka. Hiyo kazi unayoniambia tangu jana, ni kazi gani?”
“We acha tu. Kwanza wateja wenyewe ni watu wakubwa, si unawajua wale mabosile wangu? ... Pili wanakabiliwa na janga kubwa. Kubwa, mke wangu!”
“Mbona unantisha sasa?”
“Wala! Ila ndio uhalisia huo. Nataka nipate chai nzito ya kun’toa jasho. Alafu nipakie kwenye mkoba vile vitu vyangu nilivyovitenga jana pembeni.”
“Sawa.”

Ali wa Fatuma alimaliza kunawa uso akaelekea bafuni na ndoo yenye maji. Chausiku, mwanamke mbichi ambaye unaweza dhani ni mwanae, alijirudisha ndani ya kibanda akatazama sufuria yenye chai ndani yake.

Miaka mitatu nyuma Chausiku alilazimishwa na wazazi wake kuolewa na Ali wa Fatuma kama malipo ya fadhila kwa mganga huyo ambaye aliwasaidia kumpa ahueni mama yake aliyekuwa mahututi. Ilimchukua muda mrefu mwanamke huyo kukubali hiyo hali ya kuwa mke wa mtu mwenye umri unaorandana na baba yake, ila mwishowe alizoea, maisha yakasonga.

Kiredio cha mbao kiliruruma kwa mbali kikiwa kimebandikwa dirishani. Taarifa ya habari ilisikika mtangazaji akiongea kwa sauti nzito na ya kushiba. Chausiku hakuvutiwa na taarifa hiyo ya habari, ilikuwa inaboa, mara zote kwake huwa hivyo.

Aliendelea kufanya shughuli zake kana kwamba hasikii chochote. Laiti kama isingelikuwa mume wake asingelikuwa anasikiliza taarifa ya habari hata kidogo. Kusikia taarifa ya habari hapo nyumbani ilikuwa ni alama tosha Ali wa Fatuma yupo nyumbani.

Ila siku hiyo ilikuwa tofauti. Ndani ya muda mfupi, kuna sauti ilitoka redioni ikateka hisia zake:
TAARIFA ZILIZOTUFIKIA HIVI PUNDE.

Chausiku aliacha shughuli zake akatega sikio.

“Mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya usafirishaji majini, AFRI CARGO, bwana Katende Katende amekutwa amefariki nyumbani kwake usiku wa kuamkia leo mwili wake ukiwa na idadi ya risasi tano. Wanaume wawili wasiojulikana wanatuhumiwa kuhusika na tukio. Kwa taarifa zaidi endelea kusikiliza redio wani … ”

Chausiku akaachama mdomo kwa kubung’aa.

“Katende?” Alijiuliza.
“Katende wa usafirishaji? ... Mmmh … Si ndo’ huyu wa mume wangu? Au nafananisha?” Chausiku alisimama kwa muda akitafakari. Alipuuzia akaendelea na shughuli yake. Ali wa Fatuma alipotoka bafuni, akampokea na swali:
“Mume wangu, hivi yule bosi wako wa mambo ya usafirishaji anaitwa nani?”
“Ushamsahau?” Ali wa Fatuma aliuliza akitabasamu. Ni kama vile alijivunia kuwa na mteja wa aina hiyo
“Anaitwa Katende Katende au K square.”
“Basi kafariki usiku wa kuamkia leo. Ameuwawa na majambazi.”
“Unasema?”
“Amefariki! Sasa hivi wametoka kutangaza brekingi nyuzi redio wani.”
“Embu nipatie simu yangu mara moja, haraka!”
Chausiku alikimbilia simu chumbani akamletea mumewe.
“Haloo, bwana Mtemvu. Nimesikia taarifa ya habari kuhusu Katende, vipi? ... Sawa, nakuja sasa hivi!”

Ali wa Fatuma alikata simu akamuhakikishia mkewe juu ya zile habari. Ilikuwa ni kweli. Alikunywa chai upesi akavaa na kujipakiza kwenye gari lake Vitz nyekundu tayari kwa ajili ya safari.

Alitoka kwa kasi. Alisahau kubeba mizigo yake aliyomwambia mkewe amwekee mkobani. Alifika barabarani ya lami akakumbuka. Aligeuza gari haraka akarudi nyumbani upesi.

Alipofika alipiga kelele kumuita mkewe amletee mkoba ila mke hakuitika wala kuonekana. Alishuka akaenenda ndani. Huko alimkuta mkewe amelala chini akimiminika damu toka shingoni kama mtu aliyechinjwa.

Alipigwa na butwaa. Alitizama huku na kule asione mtu. Alichuchumaa akamshika Chausiku. Alimuita machozi yakimlenga lenga lakini Chausiku hakuamka.

Ghafula upepo ulimpita mgongoni, akashituka. Alitizama asione kitu. Alishika mkoba wake pembeni akauvuta. Aliufungua ndani asikute kitu.

“Silaha zangu zimeenda wapi?” Aliduwaa.

Upepo ulimpitia tena nyuma yake, akashituka. Alinyanyuka akielekea mlangoni, mlango ukajifunga.
Ndani kulikuwa giza totoro. Sauti ya Ali wa Fatuma akihema kwanguvu ilisikika. Ghafula ikanyamaza. Sauti kali ya kelele ikapasuka:
Aaaaaaaaahh!

Mlango ulipojifungua, Ali wa Fatuma alionekana amelala chini, shingo yake imekatwa. Macho yalikuwa yamemtoka nje. Mdomo ulikuwa wazi. Muda mfupi nzi walimzonga kutafuta chakula.

Simu yake aliyoiacha kwenye gari iliita mpaka basi. Jina la Mtemvu lilishika kioo kumtafuta mganga pasipo matunda. Mganga alishageuka marehemu aliyemuua asijulikane.

***

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI NA TATU

Hakuna chombo cha habari kilichokuwa nyuma kurusha tukio la msiba wa bwana Katende. Kila chaneli na stesheni ilijitawaza kurusha matangazo moja kwa moja toka eneo husika.

Wananchi pia wasibaki nyuma, wengi wao walikodolea vioo vya televisheni ama kukinga masikio redioni wapate kupashwa habari juu ya kifo cha ghafula cha mtumishi huyo mkubwa na muhimu nchini, hamu yao kubwa ikiwa ni kufahamu nani alikuwa nyuma ya kifo hiko ukizingatia kwa muda wa karibuni kumekuwa na mfululizo wa vifo vya watu wazito.

Kila mtu alisema yake. Wengine waliamini watakuwa wamedhulumiana hivyo wanauwana wenyewe. Wengine walienda mbali wakidhani wanagombea hawara, lakini hakuna hata mmoja aliyediriki kubashiri kwa kutaja jina la Miraji, mtoto wa marehemu Malale.

Mambo yaligeuka pale ilipofikia mida ya saa saba kamili ya mchana. Picha ya muuaji ikiwa imechorwa ikaoneshwa kwenye televisheni. Jeniffer, mtoto wa K square, alitumia kipaji chake cha uchoraji akachora picha nzuri sana ya Miraji kwa mujibu wa kumbukumbu zake pale alipomuona muuaji huo akijimulika usoni.

“Ni nani huyo muuaji?”
Swali hilo lililoshika vinywa vya watazamaji lilijibiwa pale Mtemvu alipohojiwa.
“Ni mtoto wa kwanza wa aliyekuwa afisa wa serikali, bwana Malale Kombo.”
“Kwanini anafanya mauaji hayo ya watu ambao walikuwa karibu sana na baba yake kipindi chake cha uhai?”
“Ni kitu cha kushangaza kwanini anafanya haya mauaji. Sijui hasa lengo lake ni nini!” Mtemvu alijibu akipandisha mabega yake juu.

Japokuwa aliulaghai umma kwamba hana wazo lolote juu ya sababu za Miraji kuua, kichwani kwake alishapata jibu ni kwasababu ya kisasi cha marehemu baba yake. Mama yake atakuwa kampandikiza chuki, aliwaza. Alipata hofu endapo Miraji akikamatwa na kuhojiwa anaweza akamwaga mchele wote, aliendelea kuwaza.

Alitoa amri kwa mapolisi kumtafuta Miraji na kuhakikisha anataarifiwa punde tu atakapotiwa nguvuni. Na kuhusu mama wa mtuhumiwa, Bernadetha, naye akamatwe, asihojiwe na mtu mwingine yeyote isipokuwa yeye.

Wakati chaneli za televisheni zikiendelea kurusha matangazo hayo ya mauaji ya K square moja kwa moja, Bernadetha alikuwa analia tangu alipoona picha ya mwanae. Pembeni yake aliketi mtoto wake mdogo, Marietta, naye akilia kwa kumuona mama yake anafanya hivyo.

“Kwanini umefanya hivi, Miraji?” Bernadetha alilia sana akiuliza.
“Nitabaki na nani mimi? Kwanini hukutaka kunisikiliza? Unamuacha mama yako na nani sasa?”

Sauti hiyo ya kilio ilitosha kabisa kumsumbua jirani. Lakini haikudumu kwa muda mrefu ikamezwa na sauti kali ya king’ora cha polisi.

Magari mawili aina ya defender yalisimama mbele ya nyumba ya marehemu mzee Malale wakashuka askari sita waliovalia kofia na mavazi magumu wakibebelea bunduki mikononi mwao.

Haraka na kwa tahadhari waliingia ndani. Walimuweka chini ya ulinzi Bernadetha. Walivamia vyumbani kumtafuta Miraji lakini hawakupata kitu.

Bernadetha pamoja na mwanaye walichukuliwa kwa lengo la kusaidia polisi kwenye upelelezi. Nyumba ilibaki tupu. Televisheni peke yake ilibakia ikinena asiwepo mtu wa kuitizama.

Jua likazama.

Katikati ya usiku wa siku hiyo, ndani ya nyumba ndogo ikivutia kwa mapambo na mpangilio wake, sebuleni aliketi Jombi pamoja na Miraji. Mezani kulikuwa na chupa kubwa ya kilevi Johnny Walker na glasi ndogo mbili.

Vidoleni mwa watu hao wawili kulikuwa na misokoto ya bangi ikienda midomoni mwao zamu kwa zamu.
Baada ya kupiga pafu kadhaa za bangi, Jombi alikunywa fundo moja la kinywaji chake, akasema:
“Kwahiyo tunafanyaje sasa man?”

Miraji akanyonya kwanza msokoto wake wa bangi.

“Mpango wetu upo palepale.” Alisema kisha akaongezea. “Ila kwa sasa kuna wazo ninalo. Tutakapomvamia Mtemvu itabidi nichukue pesa za kutosha niende zangu nje, hapa si salama tena kwangu.”

Jombi hakuzingatia Miraji alichosema. Alifikiria kwa muda akaendelea na mazungumzo ya uvamizi kana kwamba hoja ya Miraji haina mashiko.

“Kazi iliyopo mbele yetu kwa sasa si ndogo kabisa. Ni vita kubwa sana. Inabidi tujipange haswa jombaa.”
“Niambie, nakusikiliza.” Miraji alisema kwa hamu.
“Tunahitaji silaha kubwa. Tunahitaji sniper gun ya kulenga masafa marefu.”
“Tutaipatia wapi hiyo, Jombi? Si pesa ndefu sana?”
“Tutaipata tu. Nipe leo na kesho itakuwa mikononi mwangu.”
“Kwahiyo tunahitaji hicho tu?”
“Hapana. Tunahitaji pia sumu.”
“Sumu?”
“Ndiyo. Tutahitaji sindano za sumu kama tatu hivi. Pia na mabomu ya moshi.”
“Tutayapata wapi yote hayo?”
“We tulia. Niachie mimi hiyo kazi.”
“Sawa, nakuaminia bro!”

Baada ya hivyo vitumaongezi, Jombi alinyanyua simu yake akampigia mtu aliyemtunza kwa jina la ‘Mkuu’. Simu ilipopokelewa akasogea pembeni kidogo.

“Samahani mkuu kwa kukupigia muda huu, nina shida … Kuna silaha nahitaji, bunduki ya kudungulia, mabomu ya moshi na sindano za sumu … Kesho? ... Sawa Mkuu … Kazi inaenda vizuri, wamebakia wawili tu … Hakuna mtu yeyote anayejua uwepo wetu, wote wanamjua ni Miraji tu analipa kisasi … Usihofu Mkuu, haitozidi majuma mawili waliobaki watakuwa jehanamu.”

Jombi alikata simu akamrudia Miraji. Waliendelea kuvuta na kunywa mpaka kila mtu alipozima ndani ya usingizi.

Jua liliamka likamkuta Miraji akiwa juu ya kitanda, Jombi asionekane alipo. Miraji alitazama huku na kule. Alijinyanyua akaandaa chai na kupata kifungua kinywa hiko akiwa anatazama uchambuzi wa magazeti kwenye televisheni.

Taarifa ya mauaji ya Katende pamoja na picha yake zilitawala vichwa vya kila magazeti ila hazikuonekana kumshitua sana Miraji. Macho yalimtoka pale habari juu kukamatwa kwa mama yake iliposomwa.

“Mama wa mtuhumiwa akamatwa, asema hajui sababu inayomfanya mwanae afanye mauaji.”

Chai ilikuwa chungu. Machozi yalibubujika juu ya uso wa Miraji. Alipiga ngumi juu ya meza kwanguvu akisaga meno. Alitafuta simu yake akampigia Jombi.

“Upo wapi? Wamemkata bim’kubwa … Sasa? ... Njoo basi, fanya haraka!”

Hazikupita dakika tano Jombi aliwasili. Alikuwa kabebelea mifuko miwili ya nailoni akaiweka mezani na kuketi kumsikiliza Miraji.

Akiwa na pupa ya jazba pamoja na macho yanayovuja machozi, Miraji alieleza kile alichokiona na kukisikia kwenye televisheni.

“Hakuna haja ya kuhofia, Miraji. Mama yako hatosema lolote. Mwishowe watamuachia tu.” Jombi alimpa moyo.
“Lakini huko polisi ndipo alipo Mtemvu!” Miraji alisema kiwoga.
“Na hiyo ndio sababu mama yako hatosema kitu chochote. Niamini. Tumalize kwanza kazi yetu, na tena sasa tuanze na huyo Mtemvu. Unaonaje?”
Miraji alifikiria kidogo kisha akasema:
“Sawa. Tufanye hivyo.”
Jombi akatabasamu na kumkumbatia.

****

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI NA NNE:

Zilipita siku nne tangu msiba wa K square uvume. Siku hiyo Mtemvu alikuwa na miadi ya kuonana na mheshimiwa Waziri Mkuu katika hoteli kubwa ya PWEZA LA VIDA maeneo ya posta kandokando na bahari ya hindi.

Akiwa katika maandalizi nyumbani kwake, Mtemvu alitazama kioo chake kikubwa akatabasamu mwenyewe. Suti ilikuwa imemkaa vema. Mama Beatrice naye alisogea kiooni akajitizama. Gauni lake lilimpendeza. Walikumbatiana wakapeana busu kisha wakaongozana kutoka nje walipomkuta inspekta Vitalis yu tayari anawasubiri.

Walipanda garini, safari ikaanza.

Hatua kama kumi na tano nyuma yao pikipiki kubwa iliwafuata. Iliwabebelea wanaume wawili wote wakiwa wamevalia kofia ngumu, makoti meusi yaliyobana miili yao na miwani ya jua. Mwanaume wa nyuma alibebelea begi kubwa jeusi mgongoni mwake.

Inspekta Vitalis aliona pikipiki hiyo ikiwafuata. Aliongeza kidogo mwendo kasi wa gari akiwakumbusha mkuu wake na mkewe wafunge mikanda kwa usalama.

Walikata kona ya pili, pikipiki ile kubwa ikapotea. Inspekta Vitalis alizururisha macho lakini hakuona kitu. Mpaka wanafika hotelini taswira ya pikipiki haikujiri machoni mwake.

Mtemvu na Mama Beatrice walishuka kwenye gari wakachukua hatua kwenda ndani. Kabla inspekta Vitalis hajawafuata alitizama kioo cha kando ya gari akamuona mwanaume akiwa amevalia koti jeusi, miwani na begi mgongoni anaingia kwenye jengo lililo karibu na hoteli. Uso wake ulikuwa umeelekea chini akitembea kwa haraka.

Inspekta Vitalis alishuka garini akamfuatilia mwanaume yule aliyemtilia shaka. Alitembea kwa haraka macho yake yakiwa makini kumtizama mhusika wake.

Japokuwa watu walikuwa wengi barabarani, aliwakwepa bila ya kutikisa macho na hata pale alipokumbana nao vikumbo hakusema jambo, aliwaacha wahanga waropoke yeye akiendelea kufanya kazi yake.

Huku hotelini, PWEZA LA VIDA, mwanaume wa pili akiwa kavalia koti jeusi na miwani aliingia ndani. Alitembea kwa haraka uso wake ukitizama huku na kule kana kwamba anamtafuta mtu. Alichukua lifti akaiamuru kwa kubonyeza vitufe impeleke sakafu za juu.

Juu, sakafu ya sita ndani ya hoteli, mambo yalishakwiva. Mtemvu, Waziri Mkuu pamoja na wake zao waliketi kwenye meza iliyopambwa sahani zenye vyakula na vinywaji vya gharama. Nyuma yao walisimama wahudumu wawili na walinzi, wanaume wawili warefu mwenye mwili mpana ndani ya suti nyeusi.

Waziri alitoa ishara kwa wahudumu na walinzi hao anahitaji faragha. Wakapishwa na kubakia watu wanne tu ambao walimimina vinywaji vyao kwenye glasi wakavigongesha na kuvimiminia mdomoni.

“Ni muda mrefu tangu tuonane, bwana Mtemvu. Mbona kimya hivyo?”
“Majukumu, mheshimiwa. Si unajua tena hizi kazi zetu za usalama.”
“Aaah bwana ndio uwe kimya kiasi hiko? Eti shemeji?”
Mama Beatrice alitabasamu asitie neno.
“Kazi tu mheshimiwa. Hakuna kingine.” Mtemvu alisema akitabasamu.

“Nafurahi sana kusikia hivyo.” Waziri Mkuu alisema na kuongezea, “Najua utakuwa umeshangazwa na taarifa ya ghafula juu ya kikao hiki. Ila nimekuita hapa kwa mambo makuu matatu. Mosi, ni kujuliana hali kama familia. Pili, ni kuhusu hali ya usalama kwa sasa. Mwisho, ni kuhusu uhakiki wa taarifa fulani ambayo nimeipata hivi majuzi juu yako.”
“Ndio, mheshimiwa.” Mtemvu aliitikia akiacha kula.

Waziri Mkuu alikata nyama iliyokuwepo kwenye sahani akaitia mdomoni. Aliwatizama wanawake kisha akanywa kinywaji kidogo.

“Mwaka jana, mwezi wa saba, kama nakumbuka vema, ndio ilikuwa mara yangu ya mwisho kukutia machoni wewe na shemeji. Ilikuwa ni Arusha, si ndio shemeji?”
“Ndio.”
“Mlikuwa mmeongozana na watoto, mbona leo hamjaja naoh?”
“Wapo shule.” Mtemvu alijibu mkewe akiongezea: “Wanasoma Afrika ya kusini huwa wanakuja huku likizo tu.”
“Ooh! Hongereni sana!”
“Vipi wakina Berham, wapo?” Mtemvu naye aliuliza. Mke wa waziri akawahi kujibu.
“Wapo! Sasa hivi wanamalizia mwaka wao wa mwisho chuoni Uingereza.”

Walijichekesha wakiendelea kula.

Kabla halijatiwa tena neno lingine, ilisikika sauti ya ndogo ya kioo ikipasuka Waziri Mkuu akipokea risasi mbili kifuani. Alitoa kelele za maumivu akidondoka chini kama mzigo.

Mtemvu aliamrisha wanawake walale chini haraka. Walinzi wa waziri walifungua mlango wakaingia ndani kwa pupa. Walipokelewa na risasi wakadondoka chini na kufa.

Risasi zote zilipitia kwenye kuta ya kioo zikiacha matundu na nyufa. Ziliendelea kufululiza zikishambulia hatimaye vioo vya hoteli vikapasuka pasuka katika vipande milioni.

Risasi zote hizo zilitokea sehemu moja, kwenye dirisha la jengo refu lililopakana na hoteli. Jengo kubwa ambalo lilikuwa bado halijamaliziwa. Humo alikuwa amelala mwanaume mwenye sura nyeusi akiwa na bunduki ndefu iliyosimamia miguu miwili. Mwili wake ulikuwa umeveshwa koti na miwani meusi.

Alimaliza kufyatua akaanza kuitengua bunduki yake aiweke kwenye begi. Kabla hajafunga begi na kuhepa, inspekta Vitalis aliingia eneoni akihema kwanguvu kwa kutoka mbioni. Mkononi alishikilia bunduki ambayo haraka aliinyooshea kwa mwanaume yule muuaji.

"Mikono juu!" Inspekta aliamuru. Mwanaume akatii haraka.
"Piga teke begi lije huku!" Inspekta aliamuru tena.

Mwanaume yule akatabasamu kwa mbali. Alivuta na kulinyanyua begi kama mpira akalirushia kando ya inspekta Vitalis.

Inspekta Vitalis alihamisha atensheni yake kwa kujaribu kudaka hilo begi. Mwanaume yule akajiangusha chini akitoa kifaa cheusi cha mviringo mfukoni akakibamiza chini, moshi ukafuka kwa haraka.

Inspekta alifyatua risasi mbili asimpate mlengwa wake aliyekuwa anajiviringita. Baada ya muda mfupi, moshi ulitapakaa kuonana ikawa shida.

Inspekta Vitalis akibung’aa kutafuta, alijikuta akipigwa teke tumboni akainama kwa kusikilizia maumivu. Kabla hajakaa vema, teke lingine lilimsomba kichwa na kumpeleka chini kama kiroba cha viazi.

Alifyatua risasi kadhaa akibashiri alipo mlengwa wake. Moshi ulipopungua makali, hakuona mtu. Aliachwa mwenyewe mwanaume muuaji akikaribia kumaliza jengo.

Alinyanyuka upesi akatazama upande wa jengo la hoteli. Aliona watu wamejazana ndani ya eneo walilokuwa wameketi Waziri Mkuu na Mtemvu. Alitizama chini barabarani akawaona wanaume wale wawili wakijichanganya kati kati ya umati wa watu wanayoyoma.

Haraka alishuka. Alitazama kushoto na kulia lakini hakuwaona walengwa wake. Aliendea gari akaliwasha, ila kabla hajatoka kwenda popote, ving’ora viliita. Magari mawili ya polisi yalifika eneo la tukio, wakashuka polisi wanne wakibebelea bunduki.

Baada tu ya muda mfupi, walisogea polisi wengine ndani ya defender. Walivalia makofia na miwani wakibebelea pia bunduki. Inspekta alitoka ndani ya gari akawafuata. Aliwaoneshea kitambulisho chake akiwauliza;
“Wakati mnakuja mlipishana na watu wawili juu ya pikipiki kubwa?”
“Ndio. Kona ya pili tu hapo.” Alisema dereva akielekezea kidole barabarani.

Haraka inspekta Vitalis alipanda gari la polisi akalitimua kwa kasi akielekea alipoelekezwa. Kwa kuwa aliwasha king’ora, magari na watu walimpisha barabarani, ndani ya dakika chache akawatia machoni wanaume wawili juu ya baja.

Aliongeza kasi zaidi na zaidi, sasa ikabakia umbali mdogo kuwakarabia walengwa wake.

“Man, ni muda wa plan B sasa.” Mwanaume aliyekuwa anaendesha alimshitua mwenzake aliyeketi nyuma.
Mwanaume wa nyuma alijigeuzia upande wanaotokea akatoa bunduki begini na kuelekezea kwenye gari la inspekta Vitalis linalokuja kwa kasi.

Risasi zilifyatuliwa kwa pupa kushambulia gari, pikipiki ikipenya penya ubavuni na kati ya magari mengine. Inspekta alijitahidi kukwepesha gari kwa kulipeleka kushoto na kulia. Ila mwishowe risasi zilipiga kioo cha gari kikawa nyang’anyang’a.

Kumaliza kabisa kazi, mwanaume muuaji alilenga matairi ya gari alilomo inspekta Vitalis, matairi yakapasuka, safari ya Inspekta ikakomea hapo hapo.

Inspekta alisaga meno kwa hasira. Kwake ilikuwa ni nafasi nzuri sana ya kumaliza kazi, na ameipoteza kizembe, aliwaza. Alilaza kichwa chake kwenye usukani akashusha pumzi ndefu.

Kupita dakika ishirini, ndani ya jumba kubwa lililoachwa solemba na mji, pikipiki ilipakiwa humo wakishuka wanaume waliotoka kufanya tukio.

Walivua sura bandia walizovaa, hapo ikajionyesha kumbe alikuwa Jombi na Miraji. Miraji akiwa mwanaume aliyebebelea begi lenye bunduki.

Walibadili pia na mavazi kisha wakatoka ndani ya jengo wakitumia gari dogo, Toyota Passo, ambayo vioo vyake vilikuwa vyeusi ti.

Muziki uliita kwa mbali ndani ya gari kwa muda watu wakiwa kimya. Baadae Jombi alisafisha koo akasema:
“Kazi inakuwa ngumu zaidi.”
Miraji akamtizama asitie neno.
“Kosa ulilolifanya la kulenga litatugharimu sana. Ilikuwa ni nafasi yetu nzuri mno.”
“Najua hilo.” Miraji alisema akitizama chini. “Ila nilikuambia, Jombi, mie sina utaalamu wa kulenga vizuri umbali huo.” Miraji alijitetea.
“Umbali haukuwa mkubwa ilibidi tu utulize mchecheto. Sikuwa na budi kukuachia wewe ufanye lile jambo, si ulisema unataka uwaue kwa mkono wako mwenyewe?”

Miraji kimya.

“Ulinipa kazi nikatafute wapi walipoketi, nikafanya na nikakujulisha. Lakini ukafanya uzembe!”
“I am sorry, Jombi. Mi mwenyewe imeniuma sana.”
Walinyamaza kidogo, Miraji akasema:
“Vipi sasa kuhusu hivyo vifaa vingine vya kumalizia kazi. Tutavipatia wapi?”
“Usiogope kuhusu hayo maswala, bro. Kila kitu niachie mimi.” Jombi alijigamba.
“Naogopa sitakuwa na pesa ya kukulipa vyote hivyo.” Miraji alisema kinyonge. Jombi akamshika bega.
“Umesahau wewe ni rafiki yangu? Usijali sana kuhusu pesa. Tufanye kazi kwanza.” Jombi alisema akitizama mbele.
“Ahsante sana, Jombi. Wewe ni rafiki wa kweli. Hakika Mungu atakulipa.”
Miraji alisema machozi yakimlenga.

***

Muendelezo soma hapa
 
Mkuu nipo. Nimesimama wima ili nisipitwe.

tym ndio hii steve

Shusha vitu jombi eeeh

Nadhani jamaa anajipanga vizuri

mkuu umepotelea wapi lete vituuzi tupunguze stress

Shusha Niko mubashara kabisa

mpk sasa kuna kuwekwa episode 4 kweli steve
Nimekuja wakuu. Nimerusha na za fidia kwa usumbufu!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom