Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

* SURA YA SITA *

Upepo mwanana wa bahari na kinywaji laini kilichokuwa kinakanda koo lake kavu, vilimbembeleza akasinzia kwenye kiti. Baada tu ya muda mfupi akili yake ilianza kumrejeshea yale yaliyopita.

Miezi kadhaa tu nyuma akiwa kwenye kikao cha siri pamoja na wenzake wanne: Bwana Pius Mbwambo, Raheem Victor, Filbert Waziri na Katende Katende, almaarufu kama K square.

“Mzigo umeshafika Rome, sasa tunafanyeje?” Sauti nyepesi ya bwana Katende iliuliza jopo. “Inabidi mmoja aende huko.” Mtemvu akashauri na kuongezea, “Mimi nimeshamaliza kazi yangu ya kuhakikisha usalama, tumteue mmoja akasimamie zoezi hilo.”

Bwana Pius akagonga meza.
“Nani akubali kwenda huko?” Aliuliza akitoa macho. “Kusema ukweli mimi sipo tayari! Hili jambo ni hatari sana!”

Raheem akatabasamu. “Sasa mnadhani ni nani atakayeamua kujitoa sadaka?” Alidhihaki. “K square upo tayari? ... Filbert upo tayari? ... Pius upo tayari? ... Mtemvu je? ... Si unaona? Hakuna anayekubali.

Tulifanya ujinga sana kuanza kufanya hii kazi kabla ya kupanga nani atakayesimamia hilo swala kwa uaminifu mkubwa. Unaona sasa inavyotugharimu? Tumepewa taarifa mzigo umewasili, then what is next? Tutawaachia wale wazungu?”

Kimya kikatwaa umati kwa dakika kadhaa kabla ya bwana Filbert Waziri kutia neno: “Kwani hatumuamini Amerigo? Tumuache asimamie tu!”

“Hapana!” Mtemvu akapayuka. “Unadhani hii ni biashara ya nyanya? ... What if akatudhulumu? Unaenda kushtakia wapi? Unampatia wapi? Hatujafikia kiasi cha kumuamini kina hiko.” Mtemvu alitema cheche, bwana Pius na wengineo wakamuunga mkono.

“Ni kweli!” Alisema K square. “Hatuwezi kumuamini kirahisi rahisi hivyo, haswa kwenye biashara kama hii. Tunamuhitaji mtu mwingine mbali na sisi kwasababu ya usalama. Mtu tutakayemuamini, mtu ambaye tunajua anatokea wapi na tutampatia wapi akileta ushenzi. Au nyie mnaonaje?”

“Ila tutampatia wapi huyo mtu wa kumuamini kiasi hiko?” Filbert Waziri aliuliza. Baada ya mafikirio kidogo, Mtemvu alipendekeza:
“Bwana Malale!”
Wenzake wakamtizama na macho yaliyotaka kufahamu zaidi.

Bwana Malale … Bwana Malale … Bwana Malale … Sauti ya kunong’oneza ilisikika ikififia masikioni mwa Mtemvu. Alikurupuka toka usingizini. Alitizama pande zake zote nne kisha kashusha pumzi ndefu akitikisa kichwa chake kwa masikitiko. Alichoropoa simu yake mfukoni akapiga.

“Haloo! Yes Pius, unaweza ukaja Palace hotel mara moja? Ni muhimu sana.” Alipokata simu akamuita pia Katende na Filbert pamoja na Raheem ambaye yeye alitoa udhuru. Baada ya dakika chache tu, wakawa tayari wamewasili kuitikia wito.

“Niambie Pius! Vipi huko mbugani wanyama wanasemaje?”
“Aaah safi tu!” Alijibu Pius kisha haraka akaeleza hofu yake: “Vipi, mbona ghafula? Kuna chochote au una dili jipya?”

Muhudumu alikuja akawahudumia. Mvinyo na nyama choma ziliteka meza na kufanya iwe ndogo kuliko uhalisia. Ilikuwa ni Pius, Filbert na K square tu ndio waliokuwa wanakula, Mtemvu alitumia maji pekee baada ya kumaliza glasi yake ya sharubati.

“Samahani sana kwa kuwaharakisha na wito wangu wa ghafula. Nina tatizo linanikabili. Can you imagine ndani ya usiku mmoja wamekufa watu watatu nyumbani kwangu katika mazingira ya kutatanisha?”

Swali hilo likateka nyuso za wenzake walioguswa kwa namna moja ama nyingine. Waliacha kula wakamtizama Mtemvu.
“Bro, are you serious?” Filbert aliuliza. Mtemvu aliminya mdomo wake alafu akanena kuonyesha ametingwa.

“Ndani ya usiku mmoja.” Mtemvu alianza kufafanua, “Dereva wangu amekufa na wafanyakazi wawili wa ndani. Vifo vyao mpaka sasa hivi sielewi nini kimesababisha. Nimewakuta wakiwa wanamwaga tu madamu huku anayetenda hayo asionekane kabisa! Sielewi kuna nini! Mbali na hapo nimekuwa nikiona mauzauza! Nahisi kuna mtu ananifuatilia! Si bure kanisa!”

Kabla ya kutia neno Filbert Waziri alitazamana na wenzake kwa bumbuwazi kisha akaguna akimtizama Mtemvu.
“Mtemvu, are you serious or unatutania? Mbona leo sio sikukuu ya wajinga brother?” Mtemvu akatizama chini akikuna kiwaraza chake. Alikunywa kwanza fundo moja la maji ndipo akaendeleza soga yake ya kutisha.

“Sio kwamba nawatania ndugu zangu. Nawaeleza ukweli, ukweli ulio uchi kabisa! Hamjapata kusikia lolote juu ya hayo kwasababu tu ya cheo changu huko usalama, la sivyo sijui!” Akaweka kituo anywe maji.

“Ila kama nilivyowaeleza, dereva wangu: Mustafa, pamoja na wafanyakazi wangu wa ndani wameuwawa. Simjui muuaji ni nani na sijui anataka nini. Sijui ametumwa na nani?”

Zaidi tu ya kushtukiza, kila mtu akatandwa na hofu. Chakula hakikulika tena wala vinywaji havikugusa koo. Nyuso zenye taharuki na ukakasi wa mawazo zilitungwa wakiwa wanajaribu kufumbua fumbo lililoonekana ni gumu sana kung’amuliwa. Kabla lisaa halijamegeka, daktari wa Mtemvu alifika hotelini.

“Bwana Mtemvu, wakati unanipigia ndio nilikuwa namalizia ile shughuli. Kusema ukweli nimeshangazwa na hivyo vifo vingine. Kwa mujibu wa chunguzi, Mustafa amekufa kutokana na kupasuka kwa mishipa ndani ya mwili wake hivyo kupelekea damu kuvujilia ndani kwa ndani mpaka kifo.

Na kuhusu wafanyakazi wako wa ndani, vifo vyao ni vya kufananana – kutobolewa na kitu kirefu chenye ncha kali shingoni mwao. Lakini ajabu sijaona michubuko wala chochote kuashiria kama walipitia purukushani zozote kabla ya vifo vyao. Inaonyesha muuaji ni mtu mwenye utaalamu wa hali ya juu. Bado sijajua alitumia mbinu gani!”

“Si unaona!” Mtemvu alishadadia. “Niliwaambia mimi, kuna tatizo jamani!”
“Sasa tunafanyaje?” Filbert akauliza kwa hofu. Macho yalikuwa yamemtoka ndita za woga zikijichora kwenye paji la uso. Hakuna kingine walichokiamua zaidi ya kuimarisha ulinzi maradufu, wawe macho zaidi na lolote litakalotokea wajulishane.

Kikao kilifungwa wakatawanyika. Mtemvu alielekea kuichukua miili ya marehemu na hatua za mazishi zikafanyika zikichukua siku mbili tu baada ya miili ya marehemu kurudishwa kwenye makazi yao huko vijijini. Habari hazikusambaa hata kidogo. Hakuna aliyejua nini kilijiri ndani ya uzio wa nyumba ya bwana Mtemvu isipokuwa daktari, marafikize na polisi.

Kwa siri alipeleka miili hiyo huko vijijini akitoa pesa taslimu kufanikisha na kumaliza zoezi. Siku ya tatu aligeuka kurudi nyumbani kwake. Kwakuwa Mama Beatrice alikuwa bado yupo nyumbani kwa dada yake ilimlazimu siku hiyo akae peke yake nyumba nzima, hakuwa na jinsi.

Alipiga moyo konde akijiaminisha ya kuwa yeye ni mwanaume na yupo radhi kupambana na adui yake. Mkononi akiwa ameshikilia bunduki yake ndogo alijipumzisha kwenye kochi atizame televisheni.

Kwakuwa alikuwa amechoka mno na purukushani za msiba na hakupata muda wa kupumzika huko vijijini, usingizi haukupata vizingiti kumtwaa haraka; macho yalifumba mdomo ukaachama akilegea na kuacha bunduki yake ikae mbali. Muda mfupi tu baada kuanza kukoroma, akapata mgeni.

Hakuwa mgeni wa kawaida! Kilikuwa ni kivuli kilichopita kwenye mwanya wa mlango kisha kikajisogeza mbele kabisa ya Mtemvu na kusimama papo. Baada ya muda si mwingi, Mtemvu alijikuta akiwa amelala bafuni. Hakuwa na nguo yoyote, na kwenye kioo cha bafu aliachiwa ujumbe uliosomeka:

‘Mpaka pale wasaa utakapowadia’

*****

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA SABA:

Usiku bado haukuisha. Ulizidi kuwa mweusi kadiri muda ulivyozidi kukua na kukua. Mwezi ulijifinya ukawa mdogo. Mawingu meusi yaliuficha mwezi huo na muda mwingine ukawa hauonekani kabisa.

Ni kama vile mvua ilitaka kunyesha kutokana na uweusi wa mawingu na upepo wa baridi uliokuwa unapuliza muda huo. Kulikuwa kimya. Vimilio vya mbwa kubweka ndivyo viliharibu sare hiyo baadhi ya maeneo.

Nyumba kubwa ya bwana Pius, afisa mkubwa wa serikali kwenye shirika la maliasili TANAPA, ilikuwa imetulia kando kando kidogo tu mwa barabara ya vumbi ielekeayo kanisa kubwa la katoliki.

Haikuwa imepakana na nyumba zingine kwa karibu sana isipokuwa umbali wa hatua kadhaa uliofanya nyumba hiyo kuwa pweke na ndogo haswa wakati huu wa usiku ambapo giza lilikuwa limemeza sehemu kubwa ya nyumba hiyo haswa upande wake wa nyuma.

Bwana Matata, mzee wa miaka hamsini aliyekuwa ndani ya sare za walinzi, mdomoni mwake alikuwa amepachika sigara akiivuta kwa madaha macho yake yakiranda randa huku na huko ndani ya jengo la bwana Pius. Hakuwa na kitu cha kuhofia.

Kwa miaka kadhaa sasa yupo hapo analinda na hakuna hata siku moja ambayo aliwahi kukumbana na purukushani zozote zile. Waya za umeme juu ya kuta ndefu za nyumba ya bwana Pius zilimfanya aheme na kuwa na amani nyeupe, zaidi ya yote, bobby, mbwa wake mweusi anayetisha kwa ukali na mwili wake mpana na mrefu alimpa faraja na kujiona ya kwamba kulinda eneo hilo ilikuwa ni kama kumsukuma mlevi.

Kuna ugumu gani ukizingatia mkuu wake alimpenda na alipata chakula safi kila siku?
Hakujua.

Bwana Matata hakujua ya kwamba usiku ule ulikuwa tofauti na alizowahi kuzipitia. Akiwa ameketi kwenye kiti chake ndani ya kijumba kidogo cha mlinzi, alisikia bobby akibweka kwanguvu akielekeza uso wake getini.

Bwana Matata alirusha macho yake kumtizama bobby alafu akampuuza, ni kama vile alijua mnyama huyo atanyamaza tu kwani huwa anabweka na kutulia. Ila haikuwa hivyo, bobby aliendelea kubweka kwanguvu na kwanguvu mwishowe bwana Matata alinyanyuka akaenda kutizama hicho anachobwekea mbwa wake.

Hakukuta kitu, alighafirika akambwekea bobby:
“Embu acha kunipigia kelele!”

Kisha akasonya na kurudi alipotokea. Bobby alinyamaza kwa muda kidogo kabla tena hajaanza kubweka kwanguvu. Mara hii aliusogelea mti wa mtiki uliokuwa umesimama bustanini. Hakudumu hapo, ghafula akanyamaza na kufyata mkia. Alikimbilia kwenye kijumba cha mlinzi akajificha nyuma ya mlango.

“Afadhali umeamua ulale. Kumbe usingizi ndio ulikuwa unakusumbua eenh?” Aliroroma Bwana Matata kwa kejeli. Sentensi yake hiyo ilipokoma, ghafula umeme ulikata kukawa giza totoro.

Bobby alibweka kwanguvu kwa mara ya mwisho. Hakusikika tena. Sekunde chache mbele umeme ulirudi ukawakuta Bobby na Bwana Matata wakiwa tayari maiti zilizoachwa zikivuja damu! Kivuli cha mtu asiyeonekana kilitoka nje ya jengo hilo kikaelekea upande wa nyuma ya nyumba.

Si tu kwamba Pius na mkewe hawakuwa wanafahamu kinachoendelea huko nje, bali hawakudhani wala kubashiri jambo kama hilo. Kila mtu alikuwa kwenye shughuli yake ndani ya nguo nyepesi walizokuwa wamevaa. Bwana Pius alikuwa akiandika barua pepe kwenye tarakilishi mpakato wakati mke wake akiperuzi riwaya ya Stephen King: ‘Under the dome’.

Ndani ya chumba kulikuwa tulivu kiyoyozi kikipuliza kwa mbali. Ilikuwa ni hivyo mpaka pale Bwana Pius aliposikia sauti ya kugonga dirishani akaacha shughuli yake na kusogelea dirisha afungue pazia kushuhudia. Hakuona kitu. Alisonya kana kwamba amejidharau, alirudi na kuendeleza shughuli yake, ila haikuchukua muda mrefu dirisha likagongwa tena … Kap! Kap! Kap! Bwana Pius akasonya akimtizama mkewe.

“Hivi huyu Matata, anan’tafuta nini?”
Mkewe akamtizama asijue kinachoendelea. Alirudisha macho yake kwenye karatasi za riwaya kana kwamba hajasikia lolote.
Kap! Kap! Kap! - Tena!

“Pumbavu!” Pius akafoka. Alinyanyuka kwa hasira akafuata dirisha na kutizama akitumbua macho. Hakuona kitu. Ila kabla hajafunga dirisha kwa pupa, kuna kitu aliona. Kulikuwa kuna maandishi kiooni yakiwa yameandikwa kwenye mvuke ulioshika kioo kutokana na ubaridi wa kiyoyozi. Bwana Pius alisogeza uso wake karibu akasoma maandishi hayo:

“Kuna mgeni aliyetumwa kuchukua roho yako.”
Alifunga dirisha haraka akamtizama mkewe na kumtaarifu. Mke akaja kutizama ila ajabu hakukuta chochote, maandishi hayakuwepo tena. Kioo kilikuwa kisafi kama vile kimepigwa maji na kufutwa na dekio.

“Kwani kuna nini, mbona mie sikuelewi?”
Mwanamke aliuliza huku kidole chake kikiwa ndani ya riwaya asije akapotea alipoishia.

“Kwani wewe ulikuwa husikii kuna mtu anagonga dirisha?”
“Sijasikia chochote mie. Nilikuwa nakuona tu unavyohangaika.”

Bwana Pius alidhani labda mkewe hakusikia sauti hiyo kwasababu ya utamu wa riwaya, ila ni kweli hakusikia kitu. Ni yeye peke yake ndiye aliyekuwa anasikia sauti hiyo ya kugongwa kwa dirisha, na ni yeye peke yake pia aliyeyaona maneno yale juu ya kioo. Wakati mke wake akijirudisha kitandani aendelee na riwaya yake, yeye alifungua kioo cha dirisha amuite mlinzi. Aliita pasipo mafanikio moja kwa moja akajua mlinzi amelala.

Hiyo si mara yake ya kwanza, alijisemea mwenyewe. Ila na mbwa je? Amelala? Mbona hajabweka? Pius alipata shaka kidogo. Alitwaa bunduki yake ndogo akatoka nje ya nyumba aelekee kwenye kibanda cha mlinzi. Kabla hajafika huko aliona damu zilizochuruzika tokea kwenye kibanda hicho.

Haraka bwana Pius alikumbuka kisa cha Mtemvu – macho yakamtoka. Aliona sasa leo ni zamu yake. Alihisi mwili wake umepitiwa na mtetemeko ghafula na ubaridi wa ajabu. Bunduki yake mkononi haikumpa ujasiri ijapokuwa alikuwa kaielekezea mbele mithili ya mwanajeshi aliyekuwa vitani.

Aliita kwa hofu:
“Bwana Matata!”
Huku akiwa amesimama na uso wake usitulie kwa kutizama huku na huko. Alishusha pumzi ndefu akajongea taratibu kwenda kibandani. Moyo wake ulikuwa unafukuta kwa mapigo.

Hatua zake za kutetemeka zilimfikisha ndani ya kibanda akaona jambo ambalo alizoea kuliona kwenye tamthilia. Bwana Matata pamoja na mbwa wake wote walikuwa wamelala chini damu zikitoka kwenye matundu ya puani, mdomoni na masikioni.

Pius akiwa hapo anashangaa, ghafula alisikia mtu amekatiza nje ya kibanda kwa kukimbia. Alitoka nje ya kibanda lakini hakukuta mtu huko nje. Alirusha macho yake huku yakienda huko. Akahisi kwenye mti wa mtiki ndipo alipo muuaji. Basi taratibu akaanza kuufuata mti huo akielekezea bunduki yake.

“Toka mwenyewe kabla sijakushushia mvua ya risasi!” Pius alitishia. Kijasho chembamba kilikuwa kinamchuruza. Mkono wake uliokuwa umebebelea bunduki ulikuwa unatetemeka. Kama kuna siku aliomba Mungu awe karibu na binadamu, basi ilikuwa ni hiyo. Roho ilikuwa mkononi!

Kinyume kabisa na mategemeo yake kwamba muuaji yupo mtini, alisikia vishindo vya miguu nyuma yake. Kwa pupa aligeuka na kufyatua risasi zilizoenda bure. Haikupita sekunde akasikia tena vishindo nyuma ya mgongo wake. Aligeuka akafyatua risasi hovyo mwishowe zikaisha. Sasa vishindo vya miguu vikakoma, sauti ya vicheko visivyojulikana ni wapi vinatokea vikaanza kumnyima raha masikioni.

Pius alichachawa, kwa muda akawa kama mtu asiyejua nini anataka kufanya mpaka pale alipoona mlango wa nyumba yake ukiwa wazi akaanza kuukimbilia. Mlango ulijifunga na komeo la ndani. Haukufunguka abadani pamoja na kwamba Pius alitumia nguvu zake zote akipiga makelele ya kilio na kuubonda mlango huo kana kwamba umemfanyia makusudi.

Alipoona hapo hakuna matumaini, upesi alikimbilia dirisha la chumba chake akapiga kioo akimuita mkewe aliyekuwa anamuona kwenye kauchochoro ka pazia akiwa anaendelea kusoma riwaya yake.

Hamaki mwanamke hakusikia kitu kabisa! Hakusikia dirisha likigongwa wala kumuona mtu dirishani. Alifungua tu karatasi za riwaya na macho yaliyozidiwa utamu.

Pius akiwa hapo dirishani asiwe na la kufanya, alishuhudia mlango wa kabati la chumbani mwake ukifunguka akatoka mwanaume wa ajabu. Mwanaume mrefu kwenye umbo la moshi mweusi ti. Mwanaume mwenye mwili mpana macho yake yakiwa mekundu kama moto.

Pius alipiga kelele kumshitua mkewe pasipo mafanikio. Mbele ya macho yake alishuhudia mwanaume huyo akijitapanya akawa moshi kisha akamuingilia mke wake kwa kupitia matundu ya pua, masikio na mdomo.

Mbele sekunde chache tu, mke alitapatapa damu zikimtoka mdomoni, puani na masikioni. Ndani ya muda mfupi mke akawa marehemu. Aligeuka historia tena mbele ya macho ya mume wake aliyekuwa hana msaada wowote zaidi ya kushuhudia.

Pius aliishiwa nguvu. Alibakia akiwa amesimama kama mnara wa babeli. Hakujua nini cha kufanya. Uso wake ulikuwa umeduwaa macho yakibubujika machozi. Alijikuta akiuliza kwa sauti ya chini kana kwamba kuna mtu anamsikia:
“Wewe ni nani?”

Majibu yake akayapata kwenye kioo cha dirisha yakijiandika na damu.
‘Mimi ni mgeni wako niliyetumwa roho yako. Tatizo sina haja ya kuwahi kukupeleka kuzimu.’
Pius akajikuta akidondoka chini na kupoteza fahamu.

Muendelezo soma hapa
 
Namie nipo tuu

Haya tunasubiri Kiongozi .........

Nimekaa kiti cha Mbele kuisubiria..... Ngoja tusubirie Mkuu.

Angalia usifikie katikati ukaanza kuweka restrictions zingine.


Naisubiri tu kwa shauku hiyo simulizi ya baradhuli hyo


Haya twendelezeni sura zingine mpya.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom