Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

***SURA YA SABINI***



(MSIMU WA 02)








“Mamba yupo mtaani.” Vitalis alijikuta akitabasamu. Alirushia chini gazeti alilokuwa analisoma akitikisa kichwa.
“Ndio.” Kaguta alidakia, “Amerejea uwanjani, hatujui ni nini atakuwa amepanga kufanya sasa hivi.”
“Ila nani kamuokoa?” Bakari aliuliza. “Hawezi akajiokoa mwenyewe toka kwenye mikono ya polisi!”
Kaguta akaeleza: “Mpango wao huo ulisukwa vema tokea polisi kwenyewe. Kwanza, vurugu iliyotokea huko jela ilikuwa ni ya kupanga ili kufanikisha hili. Pili, baada ya hiyo vurugu na mpango huo wa kuhamishwa kufanikiwa, taarifa ikatolewa kwa hao waokozi juu ya wapi gari litaelekea, hivyo wakajipanga na kumuokoa mtu wao.”
“Lakini kwanini wameamua kumuokoa Mamba?” Miraji alistaajabu.
“Swali zuri sana, Miraji.” Vitalis akateka zamu. “Hawa watu waliobebelea mchoro wa simba migongoni mwao sio watu wa hapa nchini, unaweza ukaona hata makazi yao ni kwenye hoteli za kitalii. Ni wageni, hivyo wanatafuta mwenyeji anayeielewa vema ardhi hii. Kwao uchaguzi bora wa mwenyeji ukawa ndio huu, Mamba. Wanajua fika wakiwa na Mamba itakuwa rahisi kukamilisha misheni zao.”
“Kwa njia yoyote ile, Mamba na wenzake inabidi watawanyishwe haraka iwezekanavyo.” Kaguta alisisitiza. “Tukivuta tu muda zaidi, watafanya jambo ambalo litagharimu nchi nzima.”
“Ni kweli.” Vitalis aliridhia, akamgeukia Bakari. “Kuna vitu ambavyo Bakari amevipata toka kwenye ile simu tuliyoiopoa kule hotelini … Bakari, unaweza ukatushirikisha sasa.”
Bakari akatikisa kichwa kuafiki. Alivuta mkoba wake ulioketi pembeni akafungua na kuchoropoa tanakilishi. Aliingiza tena mfuko mkobani humo akatoa karatasi nyeupe iliyobebelea maandishi kadhaa. Alifungua tanakilishi hiyo akabofya baadhi ya vitufe akifuatisha namba fulani kwenye karatasi yake, baada ya muda kidogo akasema:
“Kuna mojawapo ya namba ambazo mwenye hii simu alikuwa anazoza nazo. Hiyo namba wakati natizama hapo awali … naona kwa sasa mtandao unasumbua sana … ilikuwa nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam, karibu kabisa na Bahari Beach Resort.”
Bakari aliachana na namba hiyo akaenda kwenye maandishi mwengine karatasini.
“Lakini pia kwenye rekodi ya mawasiliano, nimekuta namba yenye ‘code’ 441. Namba hii ni ya nchini Bermuda. Nilipofuatilia zaidi kwa mujibu wa ujumbe, nikagundua ni namba ambayo ilipewa taarifa ya tukio lile la kuvamiwa. Zaidi kuna picha kadhaa ambazo mnaziweza mkaziona …”
Bakari aliwakabidhi wenzake simu wakawa wanatizama kwa zamu.
“Huyu ni mmojawao wa wale tuliowaua.” Vitalis alisema akioneshea kidole simuni. Mpaka zoezi hilo na kuonesheana picha linakoma, wanaume wote waliomalizwa Whitesands Hotel siku ile walionekana. Lakini pia na zaidi wakiwepo wanaume wanne ambao walikuwa wapya machoni.
“Hawa wanne ndio watakuwa wamehusika na kumuokoa Mamba.” Vitalis alisema kama mtu mwenye uhakika, kisha akamuuliza Bakari:
“Kuna lingine zaidi ya hayo?”
“Yapo, ila sidhani kama yanaendana na shughuli yetu.”
Kabla hawajafanya lolote zaidi ndani ya banda lao kubwa jipya lililoezekwa na kusukwa vema na majani ya minazi, papo hapo wakiwa kwenye viti vilivyoundwa kiustadi na miti mikavu na meza ndogo katikati, walisikia sauti ya mtu anayegugumia huko nje. Punde mlango ukafunguliwa akaingia Bernadetha akiwa kamshikilia Sandra anayetembea kwa kuchechemea.
Kaguta alinyanyuka upesi akawafuata wanawake hao na kumtwaa Sandra akimbebelea.
“Kuna nini?” Aliuliza.
“Amejichoma na mti huko porini tukitafuta kuni.” Bernadetha alijibu akifuata kiti na kuketi. Alikuwa anavuja jasho haswa.
“Amejichoma sana?” Bakari aliuliza.
“Kiasi chake.” Bernadetha akajibu kisha akamtizama Kaguta. “Mpeleke chumbani nakuja kumshughulikia.”
Kaguta akatii amri. Alichukua hatua kuelekea chumbani akirusha macho kwenye mguu wa kushoto wa Sandra unaochuruza damu.

****


☆Steve
 
***SURA YA SABINI NA MOJA***




(MSIMU WA 02)








Hamilton, Bermuda: Saa kumi na mbili asubuhi.

Stanis alitizama saa yake ya mkononi mara mbili kisha akatizama kushoto na kulia kwake. Ni kama vile abiria anayesubiria ‘treni’ la mwendo kasi akiwa anadhani aidha litakuwa limemuacha. Hakutulia.
Dakika kumi mbele akaungana na wanaume wanne: Gog, Fraud, Nun na Adrian. Bila ya kupoteza muda wakaanza kujongea kuelekea upande wao wa kaskazini.
“Wengine wapo wapi?”
“Wametangulia.” Fraud alijibu. “Tumeona kuongozana kwa wingi itapelekea kugundulikana kwa urahisi.”
“Ila hayo hayakuwa makubaliano yetu.” Stanis alitamba. “Sikupanga twende wote ila kuna baadhi tu ya mambo ningependelea kuyaweka sawa.”
“Kwani kutakuwa na shida yoyote kubwa kwa wao kutokuwepo hapa muda huu?” Gog aliuliza.
“Inaweza ikawepo, inategemea na huko tuendako.” Stanis akajibu.
“Ila sisi tupo, unaweza tu ukatujuza hayo mambo.” Gog alipendekeza. Stanis akatikisa kichwa chake.
“Tuachane nayo. Tuzingatie tu yale tuliyoyapanga awali.”
Walitembea kwa muda wa dakika ishirini kamili mpaka kufikia kwenye jengo lao la kazi. Palikuwa kimya na tulivu. Wakati wanaingia, Stanis aliwatizama wenzake na kuwapa ishara ya ngumi akinong’oneza:
“Kama tulivyokubaliana.”
Gog na wenzake wakamuacha Stanis aende mbele wakati wao wakijigawa kushoto na kulia kwenda kukutana na wengineo ambao walikuwapo kwenye mkutano siku iliyopita.
Stanis asiwe na hofu bali papara, akatembea akiwa amepachika macho yake kwenye mlango wa ofisi ya Kim. Hatua zake ndefu zilimuwia muda mfupi tu kumkutanisha na mlango huo ambao aliugonga kistaarabu, akatulia kusikiliza majibu.
“Ingia!”
Sauti toka ndani ikamkarimu. Alitabasamu kwanza kabla hajazungusha komeo na kuzama ndani alipomkuta Kim akiwa ameketi kwenye kiti chake kikubwa akibembea kwa kwenda kushoto na kulia.
“Karibu, Stanis. Vipi mbona mapema hivi?” Kim aliuliza na uso wenye hamu ya kufahamu. Kabla Stanis hajajibu, Kim alidaka simu yake ya mezani akamuita mhudumu.
“Kuna jambo nimekuja kumalizana na wewe.” Stanis aligamba.
“Jambo lipi tena hilo? Kuna lolote jipya?” Kim aliuliza.
Kabla Stanis hajajibu, mhudumu akaingia ndani akibebelea vikombe viwili ya kahawa. Alivisambaza vikombe hivyo kisha akaondoka zake.
“Fukuza uchovu na kahawa, Stanis.” Kim alimkaribisha mgeni wake baada ya kunywa mafundo mawili.
Stanis akanyanyua kikombe apeleke kinywani, ila alipofikisha nusu safari akashindwa. Alisikia maumivu makali ya kichwa akarejesha kikombe mezani.
“Vipi, kuna tatizo?” Kim aliuliza akitabasamu.
Stanis alinyanyua mkono wake akitaka kumkamata Kim, lakini zoezi lake hilo likashindikana haraka. Kichwa kilimgonga mithili ya nyundo akabaki akilaumu huku akipapasa papasa kichwa chake mithili ya mama kipofu anayejitahidi kumgundua mwanaye kwa kutumia viganja.
Kadiri muda ulivyozidi kusogea, maumivu yakazidi.
“Stanis … Stanis … Stanis. Unadhani ni rahisi kiasi hiko? Yani ulale tu na kuamka utake kunipindua? Unajua ni kwa nguvu gani nilitumia kujenga hiki unachokiona sasa? Unajua imenigharimu kiasi gani kuwepo hapa? … Hakika nakwambia, njia zangu si rahisi hivyo. Kiatu changu ukitumbukiza mguu basi hautoweza kuunyanyua.”
Maneno hayo yalikuwa kama mwangwi kwenye masikio ya Stanis, aliyasikia yakijirudufu kana kwamba yumo ndani ya chungu. Hata macho yake sasa hayakuona vema, yalimuona Kim wakiwa wanne tena akielea elea kama mtu anayeogelea.
“Nini kinatokea?” Stanis alijiuliza akitetema maneno kama ‘teja’.
“Unasema?” Kim aliuliza akijinywea kahawa.
“Nini … nini kinan’tokea mwilin … mwangu.” Stanis aliongea kwa shida. Si kichwa kilikuwa kinauma sasa bali kilikuwa kizito kama vile amebebelea kichwa cha gari moshi.
“Pole sana. Ulikosea. Kaa ukijua siku zote waweke marafiki zako karibu, ila maadui zako karibu zaidi. Nilitambua wewe ni adui yangu tokea siku ya kwanza ulipokuja ofisini kwangu kulaumu. Niliona ndani ya macho yako ari na matamanio makubwa, hivyo nikakuweka karibu zaidi nijue kila unalofanya, kila ulipo. Hatimaye kama unavyoona, nimefanikiwa.”
Kim alikunywa fundo moja la kahawa kisha akanyanyua mkonga wa simu yake na kupiga simu, punde Fraud na Gog wakaja ofisini.
“Mpelekeni anapostahili. Nina maongezi naye baadae.”
Fraud na Gog wakambeba Stanis kwa kumburuza mpaka kwenye chumba kimoja kilichojitenga kikitawaliwa na giza totoro. Humo wakamrushia Stanis na kuufunga mlango.



***


Masaa kadhaa huko nyuma …

“Nimekuja kukufikishia habari kama ulivyoniagiza, mkuu. Leo pia anataka tukutane naye.” Gog alisema kwa kujiamini akimtizama Kim.
“Unataka tufanye nini? Sema nasi tutafanya … tummalize?” Fraud aliuliza. Kim akatikisa kichwa.
Aliwatizama kwanza wanaume wake wa kazi, Gog na Fraud kisha akasema:
“Hapana. Nataka nimmalize kwa mikono yangu mwenyewe. Fanyeni kama aliyowaagiza, ila hakikisha na mimi nasikia kila kitu kwenye hayo maongezi.”
Kim alifungua droo akatoa kifaa kidogo rangi ya zambarau akamkabidhi Gog. Gog na mwenzake wakanyanyuka na kuaga. Nje wakakutana na Nun na Adrian walioongozana nao mpaka kwa wenzao wengine walioongea nao kwa dakika kadhaa kabla ya kukubaliana jambo kwa kutikisa vichwa vyao na kupeana mikono.
Baadae jua lilipozama na hata kusahau lilipotokea, wanaume hao wakaongozana kwenda kukutana na Stanis maeneo ya ufukweni. Hapo wakati wote wakiwa wanalonga, Kim akawa anasikia kila jambo kwa kifaache.
Stanis asiwe na hili wala lile, aliagana na wenzake akaenda. Wenzake walizunguka nyuma na kukutana. Gog akawasiliana na Kim.
“Nadhani umesikia yote yaliyopangwa, mkuu.”
“Nimeyasikia yote. Umefanya kazi njema, kapumzike sasa tukutane kesho.”
“Sawa, mkuu. Ila unaonaje tukarahisisha kazi zaidi?” Aliuliza Gog kabla hajamuelewesha Kim nini wamedhamiria kufanya.
Baada ya maongezi hayo, Gog alimteua Fraud kwa ajili ya kazi ya ziada. Alimpatia chupa kubwa ya kijani akisema:
“Hakikisha anakuwa salama. Ulisikia mkuu anataka ammalize kwa mkono wake mwenyewe.”
Wakati wenzake wanaelekea kwenye makazi yao, Fraud akashika njia kwenda kwa Stanis. Kwa kunyata na kwa uangalifu mkubwa alifuata dirisha la chumba alalacho Stanis akapulizia dawa humo taratibu akiwa amejifunga kitambaa kuziba mdomo na pua.

****


☆Steve
 
mzee wa ado ado...mkuu..!!...poa mkuu,bakisha mtiririko wa kesho....
 
***SURA YA SABINI NA MBILI***




(MSIMU WA 02)



MTUNZI: Stevie Mollel.


No: 0685 758 123








“Mwili wake unachemka sana. Hajisikii kula wala kunywa chochote. Kama kuna uwezekano, apelekwe hospitali.” Bernadetha alishauri akiwatizama wanaume waliomzingira.
“Yote haya ni kwasababu ya kujichoma na mti?” Kaguta aliuliza.
“Ni ajabu lakini kweli.” Bernadetha akajibu. “Hakuwa hivi kabisa kabla ya hiyo ajali … embu tizameni hapa …”
Bernadetha alifungua jeraha la Sandra akawaonyeshea wanaume. Jeraha lilikuwa limezungukwa na rangi ya kijani. Hata damu iliyokuwa imetapakaa kwenye bandeji hiyo nyepesi iliyofunga jeraha ilikuwa ni ya kijani.
“Kuna mtu yeyote aliyewahi kuona kitu cha aina hii?” Bernadetha aliuliza. Wote wakatikisa vichwa vyao – kilikuwa ni kitu kigeni machoni.
“Unadhani inaweza ikawa ni nini?” Vitalis aliuliza.
“Itakuwa alikanyaga mti wa sumu.” Miraji akadakia. “Kuna aina ya mimea yenye sumu, ila inatofautiana kwenye utapakaaji wake mtini na madhara yake mwilini. Kuna baadhi ya miti matunda yake yana sumu, mengine mbegu, mengine mizizi, na mengine kila kitu kinakuwa na sumu mfano mti wa ‘manchineel’. Tunda lake tu laweza kuua watu wazima ishirini, au endapo tu mtu atakapogusana na unyevu au maji tu ya mvua yaliyogusa mti huo, atapata malengelenge makali papo. Sasa hatujajua atakuwa amekanyaga mti wa aina gani.”
“Sasa tunafanyaje?” Bakari aliuliza. “Tumpeleke hospitali?”
“Sidhani kama hilo la hospitali ni jema kwa sasa.” Alisema Vitalis akitizama saa yake ya mkononi. “ Sasa hivi ni saa tano kasoro usiku na kama tunavyojua njia yetu ni kwenye maji, inaweza ikawa hatari zaidi. Tumpe tu huduma tunayoweza alafu asubuhi na mapema tudamkie hospitali.”
Baada ya mabishano madogo wakakubaliana juu ya hilo. Walizima moto waliokuwa wanautumia kama taa ndani ya banda lao kisha wakajilaza tayari kwa ajili ya kuvuta pumzi na nguvu za kutosha kwa siku inayofuata ambayo ilionekana itakuwa ndefu sana kwa majukumu.
Katikati ya usiku huo mpevu, watu wa ajabu, wakiwa wamevalia ngozi zilizositiri sehemu zao za siri tu, walikuja na kuzingira makazi ya ‘wageni’. Watu hao walikuwa ni wale waliokuja siku moja nyuma. Walikuwa wamejichora chora mwilini. Mikononi mwao walibebelea mikuki, marungu na mishale. Kwa idadi walikuwa wanaume mia moja.
Mwanaume aliyevalia kishungi cha manyoya kichwani, alisogea mbele zaidi akikodoa macho kana kwamba anatafuta funguo gizani. Alitizama kushoto na kulia kwake akaupeleka mkono wake wa kushoto nyuma ya kiuno na kutoa kibuyu kidogo.
Alikitizama kibuyu hiko kama vile anatafuta jambo la kukosoa. Kisha akakitikisa na kumkabidhi mmojawao ambaye alizunguka makazi ya ‘wageni’ akinyunyuzia yaliyotoka kibuyuni. Alipozunguka mara tatu alirejesha kibuyu kwa aliyempa naye akakirudisha nyuma ya kiunoche kisha akaelekezea kichwa chake kwenye makazi yale. Wanaume kumi wakafuata makazi ya wageni na kutoka na wote waliokuwemo ndani kisha hao wakatokomea nao msituni wakiimba nyimbo za ajabu wakicheza na kuruka kwa furaha.




****


Hamilton, Bermuda.

Mlango wa chumba hicho kilichokuwa giza totoro kilifunguliwa na kuruhusu angalau mwanga upenye na kummulika Stanis aliyelala chini kama goigoi.
Kim akiongozana na wanaume watatu, miongoni mwa wale waliokunywa damu ya Sultan, alisogea karibu kabisa na Stanis akachuchumaa. Mwanga uliongia tokea mlangoni ulimfanya amuone Stanis vema, huku Stanis akibughudhiwa na ukali wa mwanga huo mgeni machoni, akajitahidi kuukinga na mkono yake.
“Unaendeleaje Stanis?” Kim alichombeza kwa kebehi.
Stanis alisogeza pembeni mkono wake umkingao na mwanga akajitahidi kumtazama Kim.
“Unajulia hali yangu yanini? Niue upate kuridhika!” Alisema kwa jazba. Kim akatabasamu.
“Tatizo siwezi kukuua haraka haraka hivyo. Nataka nitengeneze somo zuri sana kwa wenzako wote wajue ya kwamba kunisaliti mimi si kitu wanachotakiwa kukiota kamwe. Nitakutengenezea ratiba nzuri sana ya mateso ya kila siku washuhudie …. Washuhudie jinsi mwili wako unavyovuja damu, jinsi unavyolia kwa uchungu na kumwaga machozi … washuhudie jinsi ilivyo chungu njia ya kwenda kombo na mimi. Nataka kifo kiwe kitu cha mwisho kabisa kwako baada ya kupata kila aina ya maumivu ninayoyataka. Baada ya hapo nitakutupa uliwe na mbwa wangu kama chakula cha mchana.”
Baada ya kusema hayo Kim alisimama akawatizama wanaume wale wa kazi aliokuja nao. Wanaume hao wakasogea na kumnyanyua Stanis, wakambeba na kumpeleka upande wa nyuma wa jengo lao kubwa. Huko wakamfungia kwenye mstimu mkubwa mweusi kisha akaadhibiwa kwa kutandikwa mijeledi ya nguvu iliyotumwa vema na mwanaume mmoja wa kazi.
Wakati hayo yanajiri, wafuasi wote wa Kim, pamoja na yeye mwenyewe, walikuwa wanashuhudia.
Macho yao yaliona damu zinavyoruka kwa hasira toka mgongoni mwa Stanis. Masikio yao yalisikia vema jinsi mwanaume huyo anavyolia kwa uchungu kana kwamba mtoto. Mgongo wake wote uliharibiwa ukawa mwekundu kwa majeraha yanayomwaga damu kwa mashindano.
Hakuachwa kutandikwa, mpaka pale alipopoteza fahamu kwa kushindwa kuhimili maumivu anayoyapata. Hapo ndio Kim akasimama na wote wakahamishia macho kwake.
“Hakuna jambo linalofanywa kwa bahati mbaya ulimwenguni hapa. Kila jambo lina sababu na msukumo wake … kama pia mnavyoliona hili lililotukia mbele yenu.”
Kim aliweka kituo akiwatizama wafuasi wake kwa macho makali na uso uliokunjamana. Akaendelea kulonga:
“Wote mnajua ni wapi nilipowatoa … jinsi mlivyokuja kwangu na nikawapokea kwa mikono yangu miwili tukiapa kutunzana na kamwe kutosalitiana. Je, kinatokea nini pale mmoja wetu anaposaliti maagano?”
“Kifo!” Wote wakajibu.
Kim akatikisa kichwa chake kuafiki.
“Kifo! … ndio, ni kifo. Na hicho ndicho anachostahili mtu huyo.” Alisema hayo akimtizama Stanis mstimuni.
“Mtoeni na mumrudishe kwenye makazi yake. Kesho tutakutana tena hapa kuendeleza yale anayostahili.”
Stanis alibanduliwa mstimuni akiwa hajitambui akapelekwa kwenye chumba chake cha giza. Alitupiwa humo kama mzigo, mlango ukafungwa na komeo, nje ya mlango wakasimama wanaume wawili kumlinda mgoigoi huyo asije kwenda popote kabla hajakutana na kifo chake.
Lakini ndani ya chumba hicho cha giza, Stanis akiwa amelala akichuruza damu na fahamu zake zikiwa ng’ambo, kuna sauti ilimuita mara tatu kwa kunong’oneza pasipo na majibu.
Kumbe kwenye ukuta upande wa kulia, palikuwa na tobo dogo lililotokezea chumba cha pili. Ndani ya chumba hicho, palikuwa na mtu … ndani ya chumba hicho palikuwa na Rajul.
Naye alikuwa amefungiwa humo pakiwa ni giza haswa. Hata hali yake ya mwili bado haikuwa imetengemaa toka kwenye mateso na adha alizozipata tempo kwa utovu wake wa nidhamu.

****



☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom