Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

***SURA YA SABINI NA SITA***



(MSIMU WA 02)




MTUNZI: Stevie Mollel



No: 0685 758 123







Baada tu ya mlango wa chumba kufungwa, Rajul alijaribu tena kuita jina la Stanis mara tatu pasipo majibu. Alichungulia kwenye kitundu lakini hakuona kitu kwa sababu ya giza lililokuwepo kwenye chumba cha Stanis.
Alipiga piga tena ukuta, mara hii Stanis akashituka, ila hakutoa sauti yoyote.
“Stanis! … Stanis upo?” Rajul alinong’oneza baada ya kusikia sauti ya mtu akisogea.
“Eeeiiigh …” Stanis aliitikia kwa kukoroma. Rajul akatabasamu.
“Stanis, inabidi utoroke, la sivyo utauwawa. Unanisikia?”
“Eeeeiggh …”
“Inabidi uondoke humo kwa njia yoyote. Inabidi tutoroke la sivyo, Kim atafanikiwa adhma yake.”
“Eeeeiigghhh …”
“Ili Kim afanikiwe anahitaji damu. Na endapo nikimwambia hilo basi atakufanya sadaka. Akikufanya sadaka, atapata nguvu. Akipata nguvu, hakutokuwa na wa kumzuia tena.”
“Eeeigggh …”
“Una wazo lolote la kutoroka?”
“Eeeiigggh …”
“Stanis, huwezi kuongea neno lolote?”
“Eeeiiggh …”
“Mungu wangu!” Rajul alijibamiza kichwa akaegemea ukuta.
“Nifanye nini sasa? … Nifanye nini?”
Aliwaza na kuwazua kwa dakika kadhaa, mara akatikisa kichwa na kusema:
“Hii sasa ndio njia. Hii ndio njia pekee.”
Aligeukia kwenye kitundu, akamuita Stanis.
“Stanis, nina njia ya kututoa humu. Upo tayari?”
“Eeeiggh …” Stanis akaitikia kwa kukoroma kama ada.

***

Sauti kubwa ya mlio wa pembe la ng’ombe ililia na kumshitua Vitalis aliyekuwa amelala.
Ilikuwa ni asubuhi sasa ya saa kumi na mbili hata jua halijasimama. Vitalis alimtizama Kaguta aliyelala upande wake wa kushoto akamuona yu hoi usingizini. Asimsumbue hata, akanyanyuka na kutoka nje atizame kunani. Huko akakutana na Bernadetha, Bakari na Miraji, wote walikuwa wametoka nje kushangaa. Kama wehu, wenyeji wao walikuwa wanatoka kwenye makazi yao wakikimbia kuelekea msituni sauti inapotokea. Wakiwa wamebung’aa wasipate hata mtu wa kumuuliza, wakamuona kiongozi. Upesi, Vitalis alimkimbilia akamwambia:
“Unajua ni wewe tu ndiye unayeongea lugha tunayoielewa.”
Kiongozi akaitikia kwa kutikisa kichwa.
“Kuna nini?” Vitalis aliuliza. “Mbona watu wanakimbia?” Kiongozi akatabasamu.
“Kuna taarifa ya mateka wamekamatwa mtegoni.” Alisema. “Usiwe na hofu.”
Kauli yake hiyo ikafungwa kwa kuingizwa kwa mateka hao ndani ya kijiji wakiwa wamewekwa chini ya ulinzi mkali. Vitalis alimuona Mamba pamoja na wenzake, akajikuta anatabasamu na kusema:
“Mungu mkubwa. Amenipa nafasi ya kutimiza ahadi yangu.”
“Vitalis!” Mamba alishangaa kumuona adui yake. Alijikuta anacheka kwanza kisha ndiyo akaendelea kunena:
“Sikujua kama ulikuja kuomba msaada wa watu hawa washamba ... wa kale ... wasiojua ulimwengu unaendaje.”
Alicheka tena alafu akaendelea:
“Sikujua kama wewe ni muoga kiasi hiki. Sikujua kama wewe ni mwanamke kiasi hiki. Vitalis, watu wanavyokudhania huko nje ni tofauti na ulivyo. Hawajui jinsi gani ulivyo mtu wa kujificha na kukimbia kama panya."
Mamba aliongea kwa kejeli akiupindisha mdomo wake. Vitalis akamuuliza:
"Unakumbuka ahadi yangu niliyoiweka mbele yako kule kiwandani?"
"Ahadi gani wewe mwanamke?" Mamba akauliza pia. Vitalis akamsogelea karibu zaidi.
"Nilikuambia siku nikikutia mikononi nitahakikisha nakuharibu mpaka mama yako mzazi ashindwe kukutambua. Siku yenyewe ndiyo leo."
"Karibu!” Mamba alisema akimuita Vitalis kwa ishara ya ulimi. “… sasa nitapambanaje na nimefungwa kama mzigo wa msafiri?" Akauliza. Vitalis akamuomba kiongozi ampatie mtu huyo, kiongozi akaridhia. Mamba alifunguliwa kamba, wakapewa uwanja.
La haula, kabla Vitalis hajajiweka sawa, Mamba alijitosa hewani akamgawia teke zito lililomzoa na kumbwaga chini mwanaume huyo.
Upesi Vitalis aliamka kwa sarakasi akajiweka sawa kisha akatulia kungojea tena shambulizi.
Mamba akatuma tena teke, mara hii likadakwa na mkono wa kuume wa Vitalis. Teke hilo likavutwa karibu kisha Vitalis akaruka na kujigeuza akimtandika Mamba kisigino cha taya. Mithili ya mzigo, Mamba akarushiwa kando.
Aliponyanyuka kwa hasira aonyeshe ubabe wake, akaula tena wa chuya, kila ngumi na teke alilorusha zikakwepwa kisha akazawadiwa ngumi nzito chini ya kifua, akacheua damu.

Mamba alifuta damu yake kwa kiganja kisha akaguna. Alikimbia kumfuata Vitalis, ila Vitalis akamkwepa haraka na kumuwekea goti la mguu wa kushoto mwanaume huyo aliyegota hapo kama gari la mwendo kasi. Kama haitoshi, Vitalis akarusha mguu wake wa kulia na kumkita nao Mamba shingoni. Sasa Mamba akadondoka chini ila akiwa katikati ya miguu ya Vitalis. Miguu ikabanwa kwanguvu na kumnyima Mamba hewa. Alirusha ngumi kwa fujo ajiokoe, Vitalis akakamata mikono hiyo na kuivunja kisha akavuta jabali lililokuwa pembeni akaponda uso wa Mamba mpaka pale ulipokuwa chapati.
Damu zilimrukia Vitalis kwa fujo. Shati lake lote na hata suruali vilichafuka damu. Wakati anafanya tukio hilo la kuponda kila mtu alimshangaa. Ni kama vile alikuwa anaponda mawe kumbe kichwa cha mtu. Hakuwa na roho ya ubinadamu hata kidogo muda huo bali ya shetani, tena shetani mwekundu. Hakuacha hilo zoezi mpaka pale alipokuja kutolewa na Kiongozi aliyemvutia pembeni na kumtaka apunguze jazba.
Aliwatizama wenzake na Mamba akawaambia:
“Nyie ndio mnafuata!”
Watu hao, isipokuwa chotara, walimtizama Vitalis kana kwamba wanatizama pundamilia akimla simba. Chotara yeye alikuwa hoi asijali hata kinachoendelea. Alisimama kama mgomba ulioelemewa na mkungu wa ndizi. Alikuwa ametota jasho mdomo ukiwa mkavu mno. Macho yake yalikuwa yamelegea yakiwa mekundu ya kutisha.
Vitalis alijikwamua toka mikononi mwa Kiongozi akajiendea ndani asiwaone watu hao. Mateka walitundikwa mitini, watu wakaendelea na shughuli zingine kama ada. Baada ya muda mfupi, Bakari aliwafuata hao mateka waliotundikwa mitini akawapekua mifukoni. Miongoni mwa mmoja wao alikuta simu. Aliitia mfukoni mwake akawauliza:
“Mmetumwa na nani?”
Mateka wale watatu, walio wazima wa afya, wakatabasamu.
“Usitegemee kupata jibu lolote toka kwetu.” Mmoja alijibu.
Bakari alimfuata chotara akamtizama kwa karibu. Aliona mishipa ya shingoni ya mwanaume huyo imegeuka kuwa rangi ya kijani. Alimfungua macho akamtizama, napo akaona macho ya mwanaume huyo yakiwa na umbijani kwa mbali, akaishia kutikisa kichwa na kusema:
“Mwenzenu atakufa muda si mrefu.”
“Tunaomba umsaidie.” Mmoja akasema. “Tafadhali naomba umsaidie.”
Bakari akatabasamu.
“Usitegemee kupata msaada wowote toka kwangu.”
Alisema kisha akajigeuza aondoke. Akaitwa.
“Tafadhali msaidie. Tutakuambia unayoyataka.”
“Vipi kama mkiniambia alafu ndiyo niwasaidie?” Bakari alisema akisogea karibu kwa aliyemuita.
“Hapana! Tutajuaje kama unatulaghai?”
“Na mimi nitajuaje kama mtanilaghai?”
“Hatuwezi kufanya hivyo. Tukikulaghai, tutaondokaje na mmetufungia mtini?”
“Siwezi jua. Ila ingekuwa vema kama mngeniambia upesi ili mwenzenu apate tiba upesi, yupo kwenye hali mbaya. Si mnamuona?” Bakari alimtizama chotara.
Alikatizwa zoezi lake hilo na sauti ya Bernadetha iliyomuita. Aliaga akaahidi kurudi upesi kumalizana nao. Aliondoka, Kaguta akasogea karibu na mateka. Muda wote Bakari aliokuwepo hapo, Kaguta alikuwa akimtizama kwa karibu.
Sura yake ilikuwa imekunjamana. Macho yake yalikuwa yamevimba na mekundu. Mdomo wake ulibinuliwa kwa kebehi ama hasira. Nyuma ya mgongo wake alikuwa amefichama mkono uliobebelea kisu. Aliwatizama mateka akawaambia kwa sauti ya chini:
“Nimekuja kudai uhai wenu.”
Bakari aliporejea baadae kwa mateka hao, akawakuta wote wamekufa. Kila mmoja alikuwa anachuruza damu kifuani mwake akiwa na matundu ya visu si chini ya mawili.
“Samahani kwa kuingilia maongezi yako.” Sauti ya Kaguta ilimfikia Bakari na kumshitua. Aligeuka akamkuta Kaguta nyuma yake.
“Kwanini umewaua?” Bakari aliuliza. “Kuna taarifa muhimu walikuwa wanataka kunipa!”
“Unadhani wangekuambia kitu?” Kaguta aliuliza. “Kama ulitegemea kitu toka kwa watu waliokula viapo vya kutosema lolote, pole sana. Hawa watu hawastahili huruma yoyote.”
Baada ya kusema hivyo Kaguta aliondoka akaelekea ndani ya kijumba. Alinyofoa mtungi wa pombe uliokuwepo chini ya kitanda cha ngozi alaliacho, akamwagia kinywaji hicho ndani yake mpaka pale alipozima akalala. Hakutia tumboni kitu chochote isipokuwa pombe hiyo ya kienyeji. Hata pale jioni alipoamka, aliamkia na pombe hiyo. Ni Vitalis ndiye aliyekuja kumuokoa toka kwenye hiyo shughuli.
“Inatosha!” Vitalis alisema akimpokonya Kaguta mtungi wa pombe kwanguvu.
“Unadhani itasaidia?” Vitalis aliuliza. “Haitosaidia zaidi ya kutuongezea msiba mwingine, Kaguta!” Alifoka. Aliweka kituo akapunguza sauti.
“Tuna maongezi. Tunakungojea nje, fanya uje.”
Alitoka ndani ya chumba, Kaguta akamfuata baada ya muda mfupi.
Wakiwa watano, WAGENI, wamekaa kwenye benchi refu, waliteta:
“Sasa ni muda wa kwenda kumalizana na adui yetu mkubwa.” Vitalis alifungua maongezi. “Kila tunachokihitaji tunacho. Hatuna tena muda wa kungoja.” Alimtizama Bakari, Bakari akachukua zamu:
“Nilifanikiwa kwenda town kuchaji simu. Bahati nzuri baada ya simu kuwaka, barua pepe toka kwa Mr Kim ziliingia. Nilichat naye nikijifanya mimi ni mtumishi wake, nikapata taarifa muhimu za kutufikisha alipo.”
“Basi twende!” Kaguta aliropoka. “Tunangoja nini?”
“Tulia Kaguta.” Vitalis akasihi. “Si tu kwenda, tupange kwanza. Unajua tutafikia wapi? Unajua tutafanyaje kumpata Mr Kim?”
“Haya, tuendelee.”
Kaguta alisema kwa sauti ya chini isiyoridhia.

***


☆Steve
 
Asante sana Steve. Inaonyesha inakaribia ukingoni.kama una nyengine baada ya hii. Wewe tuwekee tu
 
***SURA YA SABINI NA SABA***




(MSIMU WA 02)



MTUNZI: Steve Mollel







Hamilton, Bermuda.

Milango iliyokuwa imewafungia ndani wafungwa wawili, Stanis na Rajul, ilikuwa wazi. Pembeni ya milango hiyo ilikuwepo miili miwili ya wanaume waliokufa.
Taarifa hiyo ya vifo, ama kutoroka kwa wafungwa hao, haikuwa imesambaa popote pale. Hakuna yeyote ndani ya jengo hilo kubwa aliyefahamu kilichojiri isipokuwa tu akili za wafu waliolala hapo, akili zisizo na umuhimu tena juu ya ulimwengu wa walio hai.
Muda uliposonga, ukawadia wasaa wa Stanis kupokea adhabu yake ya muendelezo. Ndani ya muda huo ndipo taarifa ikatapakaa – Wafungwa wametoroka.
Kim alikuwa ameketi kwenye kiti chake kikubwa akiwa tayari kushuhudia tena mgongo wa mwanaume aliyejaribu kumpindua ukifumuliwa na mijeledi. Akiwa anakunywa Vodka iliyotunzwa kwenye chupa ndogo yenye urembo wa kuvutia, mtumishi wake alifika mbele yake akamnong’oneza. Kim alimsukuma mtumishi huyo kisha akanyanyuka upesi na kwenda huko wahifadhiwapo wafungwa.
Kama vile milango ilivyokuwa wazi, naye mdomo wake ukabaki wazi aliposhuhudia. Alitoa macho ya butwaa. Aliuliza waliokuwa zamu ya lindo, wote wakaitwa mbele yake. Aliagiza wanaume hao wafungwe kamba na waadhibiwe mpaka kifo. Pasipo huruma, wanaume hao wanne wakafungwa na kuchapwa mijeledi ya nguvu. Kama vile haitoshi, Kim akafumua bongo zao na bunduki kisha akawaita wanaume wake watano wa kazi, akawaagiza wawatafute wafungwa hao.
“Kwa njia yoyote, kwa gharama yoyote ile, nataka hao watu warudi hapa!”
Wanaume hao watano walijipaki kwenye gari wakatoka nje ya uzio wa jengo tayari kwenda kuwatafuta Rajul na Stanis kwa udi na uvumba.

***

Basi lilisimama wakashuka wanaume wawili, Stanis na Rajul. Stanis alikuwa hoi kutembea mwenyewe asiweze ila kwa msaada wa Rajul alijikokota kwa mwendo wa kinyonga wakielekea upande wa kaskazini mwa barabara.
Kwa mazingira ya eneo walilopo, haikuhitaji elimu kung’amua ni ya kijijini. Japokuwa nyumba zilikuwa nzuri na za kuvutia, zilikaa mbali mbali huku zikiambatana na maghala ya chakula ama zizi la ng’ombe au farasi. Mashamba yalikuwa mengi yakizunguka makazi. Na ndani ya mashamba hayo walikuwepo watu wakichakarika kutimiza majukumu.
Baada ya mwendo wa dakika kumi, Rajul na Stanis walifika mbele ya nyumba nyeupe saizi ya kati. Rajul aligonga mlango wakafunguliwa na mwanamke mzungu mzee, Kelly, ambaye alishangazwa na hali ya wageni wake.
“Rajul, kuna nini?” Mwanamke huyo aliuliza.
“Naomba niingie ndani kwanza.” Rajul akasema. Mwanamke huyo akasaidiana na Rajul kumshikilia Stanis mpaka ndani walipomlaza mwanaume huyo kifudifudi. Rajul alimvua shati Stanis, Kelly akafunika mdomo wake na kiganja.
“Oh my God!” Kelly aliduwaa.
“Naomba umsaidie.” Rajul akamwambia mwanamke yule mzee.
“Amefanyaje?”
“Ni stori ndefu. Usijali, nitakuambia.”
“Ni bora ungempeleka hospitali, Rajul. Sio kwangu.”
“Hapana. Hospitali ni hatari kwake na kwangu pia.”
“Kivipi?”
“Nimekuambia ni stori ndefu, nitakuambia. Msaidie kwanza.”
“Nitamsaidiaje, Rajul?”
“Vyovyote. Ulishawahi kuwa nesi, tumia ujuzi wako.”
“Nilikuwa nesi kitambo.”
“Najua … najua. Ujuzi haufutiki, Kelly. Msaidie.”
Kelly alinyamaza kwa sekunde chache alafu akasema:
“Ok, ningojee hapa.”
Aliondoka akaelekea chumbani. Alirejea akiwa na kiboksi chekundu kilichoandikwa ‘First Aid’, akakifungua na kutoa pamba na chupa mbili za dawa.
“Hizo dawa za nini? Rajul aliuliza. Kelly akatabasamu.
“Tatizo umezoea dawa zako za mitishamba. Nashangaa huyu hujaenda kumtibia na madawa yako.”
“Ni stori ndefu, Kelly.”
“Ok ok … Mr. stori ndefu. Ni dawa ya kumsafisha na kumkausha majeraha. Hawezekani kushonwa tena huyu.”
“Ahsante sana kwa kumsaidia.”
“Usijali. Unajua wewe ni rafiki yangu, na ulijua kabisa nisingeweza kukukatalia kukusaidia ndio maana ukaja.”
“Ndio. Mume wako yupo wapi?”
“Ameenda kunywa … kama kawaida yake.” Alijibu Kelly akimshughulikia mgongo wa Stanis.
“Pole.” Rajul alimwambia Kelly. Kelly akamtizama mwanaume huyo kisha akarudisha macho yake mgongoni mwa Stanis.
“Pole ya nini na ni wewe ndiye ulitaka niishi maisha haya.”
“Hapana, Kelly.”
“Hapana nini? Kama ungelikubali kunioa na kuwa na mimi, nisingeishia kwenye mikono ya huyu mlevi. Lakini kwasababu uliona dini yako ni bora kul …”
“Ishia hapo Kelly.” Rajul alimkatisha Kelly maneno. “Tafadhali tusianze kujadili yaliyopita. Hatuwezi kuyabadilisha abadani.”
Kelly hakutia tena neno. Alitikisa kichwa akaendelea na zoezi lake la kucheza na majeraha ya Stanis.


***


☆Steve
 
***SURA YA SABINI NA NANE***




(MSIMU WA 02)




MTUNZI: Stevie Mollel







“Hatujafanikiwa, mkuu.” Alisema mwanaume mmoja wa kazi. “Tumetafuta jiji zima lakini hatujampata kabisa.”
“Mnasemaje?” Kim aliuliza akiwatizama watumishi wake watano. “Hamjawapata kivipi?”
“Tumetafute kote mheshimiwa. Kote!”
Kim alibamiza meza kwanguvu, akafoka:
“Hamjatafuta vya kutosha! Nendeni mkatafute kwa mara nyingine. Haraka!”
Wanaume wale walitizama kisha wakatoka ndani ya ofisi ya bwana Kim na kwenda kwenye gari lao. Kwa mara ya pili walizunguka jiji zima wakitumia picha za watu wanaowatafuta kuulizia kila mahali lakini wasifanikiwe kabisa. Mpaka jua linazama na usiku unautwaa ulimwengu, walikuwa kapa. Walirejea ofisini kwa mkuu wao wakampasha habari – Rajul na Stanis hawapo jijini.
“Naombeni mnipishe.” Kim aliwaambia watumishi wake. Walitoka ndani ya ofisi wakamuacha mkuu wao akiwaza na kuwazua.
Baada ya muda mfupi aliwaita wanaume hao wa kazi, akawapatia ujumbe na kuwataka waupeleke makao makuu ya polisi. Ujumbe huo ulipofika, matangazo yakaanza kurushwa redioni na kwenye chaneli za televisheni yakiambatana na picha za Rajul na Stanis.
‘Watuhumiwa hawa wa mauaji wanatafutwa na jeshi la polisi. Popote watakapoonekana tafadhali tunaomba utoe taarifa kwenye namba zifuatazo: Zawadi zitatolewa kwa yeyote atakayefanikisha kutoa taarifa sahihi.’

***

“Fungua mlango wewe mbwa jike!” Sauti ya nzito ya kiume ilipaza toka mlangoni.
Kelly alitazama saa ya ukutani akaona ni saa saba usiku. Alijinyanyua toka kwenye kochi alipokuwa amelala akauendea mlango na kufungua.
“Nini kilichokufanya uchelewe kufungua mlango?” Aliuliza mwanaume huyo aliyefunguliwa. Alikuwa ni mzee wa makadirio ya miaka sitini na mbili mpaka na tano. Alivalia kapelo iliyochoka. Mkononi alibebelea chupa ya bia. Macho yake yalikuwa mekundu yanarembua. Alikuwa hawezi kusimama vizuri bali anayumba yumba kana kwamba miguu imepoteza balansi.
“Nimekuuliza kwanini umechelewa kufungua mlango?”
“Johnny, nilikuwa nimelala.”
“Umelala?” Mwanaume huyo aliuliza alafu akacheka. “Umelala na mumeo hajarudi nyumbani?”
Kelly hakusema kitu. Alitoka hapo mlangoni akaenda kukaa kwenye kochi.
“Kwahiyo ninayoyaongea siyo ya maana, umeamua uondoke?”
“Tafadhali, nakuomba unyamaze.” Kelly alisema kwa upole.
Mwanaume yule akaingia ndani pasipo kufunga mlango. Alimsogelea Kelly akamuuliza:
“Unaniambiaje we mwanamke?”
Kelly kimya.
“Unaniambia ninyamaze? Kwangu?”
Mwanaume huyo alimzaba kibao Kelly, Kelly akapiga kelele kali za maumivu. Kelele hizo zilimshitua Rajul toka usingizini akaketi na kutega sikio lake. Aliendelea kusikia kelele za kilio za Kelly, mwishowe uvumilivu ukamshinda akaenda huko sebuleni.
“Inatosha!” Rajul alifoka akimtizama mume wake Kelly, Johnny.
“Wewe ni nani? Na unafanya nini nyumbani kwangu?” Johnny aliuliza.
“Mimi ni Rajul. Nimekuja kwa rafiki yangu Kelly kumuomba msaada wa kitabibu. Nimekuja na rafiki yangu anaumwa.”
“Oooh Rajul!” Johnny alisema kwa kebehi kisha akamtizama Kelly.
“Kumbe huyu ndio Rajul? Naona amekufata sasa, unh? Umeamua kumleta huyu malaya wako mpaka nyumbani!”
Kelly kimya.
“Sina mahusiano yoyote na Kelly.” Rajul alijitetea. “ Ni rafiki yangu tu!”
“Naona!” Johnny akasema. “Naona kweli ni rafiki yako.”
Alinyanyua mkono wake ampige Kelly ila ghafla akavamiwa na Rajul akamwagiwa chini. Walipambana wakirushiana huku na huko. Kelly aliwataka waache kupigana lakini hakuna aliyemsikia, waliparangana mpaka pale Johnny alipotulia kimya kama mtu aliyekufa.
“Rajul, umemuua?” Kelly aliuliza.
“Hapana.” Rajul akamjibu. “Atakuwa amepoteza fahamu tu.”
“Sasa?”
“Itabidi niondoke kabla hajazinduka.”
“Utaenda wapi usiku huu?”
“Popote pale.”
“Hapana. Kaa hapa hapa mpaka asubuhi ndio uende.”
Kelly aliposema hayo alimkumbatia Rajul kwanguvu akambusu shavuni.
“Ahsante.” Alisema.
“Karibu.” Rajul akamjibu. “Nenda kalale sasa.”
Kelly na Rajul walienda kwenye vyumba vyao wakafunga mlango na kuzima taa.
Baada ya masaa kadhaa, Johnny aliamka akishikilia kichwa chake kwa maumivu. Alijikokota akaenda chumbani kwake alipogonga mlango pasipo majibu. Alirudi sebuleni akawasha televisheni na kujilaza kwenye kochi. Kabla usingizi haujamkomba, akaona tangazo la Rajul na Stanis.
‘Watuhumiwa hawa wa mauaji wanatafutwa na jeshi la polisi. Popote watakapoonekana tafadhali tunaomba utoe taarifa kwenye namba zifuatazo: Zawadi zitatolewa kwa yeyote atakayefanikisha kutoa taarifa sahihi.’
Macho yalimtoka kwa mshangao, akajilamba kwa tamaa.
“Mungu wangu. Huyu atakuwa Rajul na mwenzake bila shaka!”
Haraka alifuata simu ya mezani akatia namba alizoziona kwenye kioo cha televisheni na kuweka simu sikioni.
“Nimewaona hao watu mnaowatafuta … wapo nyumbani kwangu …”
Alipomaliza kutoa taarifa zote muhimu akarudi kwenye kochi na kujilaza. Alitabasamu muda wote kila alipokumbuka lile donge nono la pesa lililoahidiwa. Hata pale alipolala aliota yu tajiri haswa, akitapanya pesa anavyotaka.
Alikunja kushtushwa na hodi mlangoni ikiwa ni majira ya saa moja asubuhi. Alinyanyuka upesi akauendea mlango na kufungua, akakutana na wanaume watano wa bwana Kim.
“Bila shaka ni wewe uliyetoa taarifa polisi.”
“Ndio! Ndio mimi.”
“Wapo wapi?”
“Wapo chumbani. Twendeni.”
Waliongozana mpaka chumba cha wageni wakafungua mlango na kuingia ndani.
“Wapo wapi?”
Aliuliza mwanaume mmoja akimtizama Johnny.
“Walikuwepo humu.” Johnny alisema. “Watakuwa wametoroka.”
Mwanaume mmoja aliona tone la damu sakafuni, alichuchumaa akafuta tone hilo na kidole chake kisha akailamba.
“Wapo karibu.” Aliwaambia wenzake. “Damu bado fresh, hawajatoka muda mrefu.”
Haraka wanaume hao wakatoka ndani ya chumba, Johnny akawaita.
“Pesa yangu?”
Wanaume wale watano wakatazamana kisha mmoja akajiteua na kumfuata Johnny.
“Unasema?”
“Pesa yangu.” Johny alirudia kauli. “Si nimewapa taarifa.”
Mwanaume yule alimzawadia Johnny teke zito la kifua. Johnny akarushwa na kujibamiza ukutani kwanguvu. Alidondoka chini damu zikimtoka mdomoni na puani. Kifua kilikuwa nyang’anyang’a.
Wanaume wale watano walitoka ndani ya nyumba hiyo wakagawana pande za kusaka watu wao. Kwa kutumia pua kunusa kama wanyama, kwa kutumia mbio zao kama simba, walitawanyika kutekeleza walichoagizwa.
Umbali wa nusu kilomita wa mwanaume aliyeelekea upande wa mashariki ndipo alipokuwepo Rajul, Stanis na Kelly. Walikuwa wanatembea taratibu wakimsaidia Stanis kutembea. Walikuwa kwenye barabara nyembamba ikomeayo baharini baada ya mwendo wa kama dakika thelathini.
Wakiwa wamebakiza mwendo wa robo saa kufikia maji ya bahari, mlio wa bunduki uliwashitua, mlio huo ulienda sawia na kilio cha Kelly. Risasi ilikuwa imekita kwenye mgongo wa mwanamke huyo. Alidondoka chini akiachama mdomo. Rajul alipotizama ilipotokea risasi hiyo, akamuona mwanaume mmoja wa kazi akija kwa kasi.
“Ondoka, Rajul!” Kelly alipaza sauti. “Nenda, nitakuwa sawa.”
“Hapana siwezi nikakuacha hapa.” Rajul alisema akimtizama Kelly kwa huruma.
“Rajul, kama wakikukuta hapa nini itakuwa juhudi zako zote hizo tokea mwanzo?” Kelly aliuliza. “Nenda. Najua hawanihitaji mimi bali wewe na mwenzako. Nenda uttizame chini ya mnazi mrefu kuliko yote utaona mtumbwi. Nenda!”
Kishingo upande Rajul akaondoka. Alimbeba Stanis mgongoni akakimbia naye mpaka baharini akipunyuliwa na risasi. Huko alivuta mtumbwi na kujiweka na Stanis akawasha mashine na kuanza kukata maji.
Mwanaume wa Kim alifika ukingoni mwa bahari akiwa amechelewa. Alirusha risasi lakini hazikusaidia, Rajul na Stanis walilala ndani ya boti hivyo wakawa salama. Hata pale risasi zilipolenga kuitoboa boti hiyo, ilishindikana kwa kwenda kando.
Mwanaume huyo aliposhindwa kumalizana na kazi yake hiyo aligeuza shingo yake akamtazama Kelly. Upesi alimrudia mwanamke huyo. Kelly alijivuta akirudi nyuma. Aliomba aachiwe uhai wake lakini haikumsaidia. Alimiminiwa risasi na mwanaume huyo pasipo tone la huruma, hiyo ikawa salamu kwa Rajul aliyeishia kutoa machozi akitizama tukio hilo kwa mbali.
Mwanaume huyo akachomoa simu yake mfukoni na kuwataarifu wenzake upande walengwa wao walipoelekea. Hakuchukua tena muda hapo, akajiondokea.
Ndani ya muda mfupi, kundi la wanaume watano wa Kim likawa tayari limewasili kwenye mwambao wa bahari unaoshukiwa kuwapokea wageni wanaowatafuta – Rajul na Stanis. Waliona boti iliyowasafirisha watu hao lakini ndani hakukuwa na mtu isipokuwa tu mabaki ya damu yaliyotapakaa sehemu mbali mbali. Walijigawa wakaelekea pande tofauti kwa ajili ya kuwatafuta watu hao, ila mpaka yafika jioni hakukuwa na matokeo mazuri – wanaowatafuta hawakuonekana popote.



***

☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom