Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Kwa hii network kubwa na ushirikina wa hili genge la Mr. Kim
Sidhani kama kuna uwezekano wa Inspekta Vitalis, Jombi & Kaguta kuuproot hili Genge la Mr. Kim
 
***SURA YA ISHIRINI NA SITA***





(MSIMU WA 02)





Ndani ya mida ya jioni jua likiwa tayari limezama na kilichobakia ni miale yake ya njano tu, inspekta Vitalis alijirudisha nyumbani kwake akiwa kabebelea mkoba wa ngozi. Alipoingia sebuleni aliutupia mkoba juu ya meza akaketi kwenye sofa.



“Jombii!”
“Yeeeah!”




Sauti ya mwanaume iliitikia kwa ndani, punde Jombi akaja sebuleni wakasalimiana.




“Afadhali umekuja. Simu yako imenisumbua siku nzima ya leo.” Jombi alianzisha mada.
“Simu yangu ipi?” Inspekta Vitalis aliuliza kwa mshangao.
“Hii hapa!” Jombi akatoa simu kubwa nyeusi aina ya LG. Inspekta akaachama mdomo kwa bumbuwazi. Aliikwapua simu toka mkononi mwa Jombi akaitizama.
“Hii ni simu ya dokta Rajesh! … Gosh! … Umeionea wapi?”
“Chumbani kwangu, chini ya uvungu. Imeita sana.”
“Aisee, nilikuwa nimeisahau kabisa!”





Inspekta alinyanyuka akaubeba mkoba wake na kwenda chumbani. Aliwasha taa kisha akailaza simu ya dokta Rajesh kuhakisi mwanga wa taa kwenye kioo cha simu, akaona alama za michoro. Akaweka kidole chake kwenye kioo na kuchora, simu ikafunguka.





Alifungua mkoba wake akatoa note book na kalamu akaanza kupitia missed calls. Miongoni mwazo akaona ina jina la Wayne Ford, nyingine I. Makongo. Akaziandika hizo namba kwenye note book yake. Baada ya hapo akaanza kupitia jumbe zilizokuwemo ndani ya simu. Moja ya jumbe ikakamata hisia zake.




“Kumbuka unadaiwa damu ya watu kumi na mbili. Hakikisha leo unauwa watu hao na kuleta damu hiyo. Its urgent.”






Inspekta aliandika kwenye note book namba iliyotuma huo ujumbe kwa dokta na kwenye simu ya dokta ilikuwa imeseviwa ‘Sahayoogee’. Inspekta akaanza kufuatilia conversation kati ya Sahayoogee na dokta Rajesh Deepti.






Alipomaliza, akaendelea kutizama jumbe zingine, akakutana na jumbe moja kati ya dokta Rajesh Deepti na mtu aliyeseviwa Svaamee Math. Kabla hajaendelea, inspekta alichukua simu yake akatafuta maana ya neno ‘Svaamee’ akagundua ni neno la kihindi lenya maana ya mkuu. Sasa likabakia neno ‘Math’ maana yake nini? Wakati inspekta anafikiria alikumbuka maneno mawili yanayoishia na hilo neno, akayatamka:




“Rosemath stationary chini ya Mikmath company”





Akafikiria tena kwa muda, taratibu akaanza kulinyambua neno ‘Mikmath’, hapo akapata kutambua neno Mik maana yake ni Kim likiwa limegeuzwa kwa kinyume. Sasa akarudi tena kwenye jumbe kati ya Svaamee Math na dokta Rajesh. Akakuta jumbe nane tu:





“Let us meet in Delhi.”
“Let us meet in Barmuda … urgent.”
“Let us meet in Dar es salaam, at Serena Hotel after 30 minutes.”
“If there’s any problem, consult me.”




Hizo zote zikiwa zimetumwa na Svaamee Math, na jumbe nne zilizobakia zikiwa ni za kujibu hizo jumbe nne kwa neno moja tu lililojirudia.




“Yes, master.”




Mara simu ya dokta ikaita, bwana Isaac Makongo akiwa ndiye mpigaji. Inspekta alitizama kioo cha simu kwa dakika moja akaamua kupokea.




“Mbona ulikuwa hupokei simu, Rajesh?”
“Ilikuwa mbali. Lete habari.” Inspekta aliongea huku akijitahidi kuiga sauti ya Rajesh.
“We have to meet kesho asubuhi saa tatu maeneo ya masaki, Mr Wayne Ford atakuwepo pia. Ni kuhusu our spreading propaganda.”





Baada ya hayo maneno, simu ikakata. Inspekta Vitalis akabakizwa na maswali: Masaki sehemu gani wanapoenda kukutana? Baada ya muda kuna kitu kikamjia kichwani … namba 898. Inspekta akatabasamu na kutikisa kichwa chake. Alinyanyua simu yake na kumtaarifu Kaguta habari nzima. Wakapanga kesho waende huko Masaki.




Masaa yakaenda na asubuhi ikawasili. Inspekta na Kaguta walikutana na kujiweka kwenye gari mpaka masaki, taratibu na kwa tahadhari wakakaa umbali wa mita kadhaa mbali na jumba kubwa lililobebelea namba 898. Wakiwa hapo wakarusha macho yao eneo la tukio, punde wakaonamagari matatu meusi aina ya benzi yanaingia ndani ya lile jengo kisha geti likafungwa.






Inspekta Vitalis na Kaguta wakashuka garini na kuanza kusonga kufuata nyumba ile kubwa. Hatua kama saba, ghafla likatokea gari aina ya van nyeusi, mlango ulifunguliwa akatokeza mwanaume mmoja aliyebebelea bunduki kubwa SMG, kabla wakina inspekta hawajafanya lolote, mwanaume yule aliyebebelea bunduki alimimina risasi kadhaa zikamlenga Kaguta kifuani na inspekta Vitalis miguuni. Wote wakadondoka chini. Van ikaondoka kwa kasi na kupotea.





Inspekta alimtizama Kaguta akamuona yu kimya. Alimtikisa huku akimuita jina lakini Kaguta hakusema neno lolote. Alikuwa kimya tuli kama maji mtungini. Mara machozi yakaanza kujaa kwenye macho ya Vitalis. Alikuwa amekodoa kama vile haamini kinachotokea. Aliita kwa sauti kubwa lakini haikuleta tofauti yoyote, Kaguta alikuwa kimya.





Inspekta alinyanyuka, huku miguu yake ikivuja damu, alimbeba mwenzake akampeleka mpaka kwenye gari walilokuja nalo kisha akawasha gari na kuondoka eneo hilo mpaka maeneo ya ufukwe mwa bahari. Alizima gari na kumtazama Kaguta aliyekuwa amekaa nyuma ya kiti akiwa amelala kama mfu kisha akaegemea usukani mwa gari akaanza kuangua kilio kama mtoto. Ni kama vile ndoto, tena ya jinamizi mbele ya macho ya inspekta. Hakutaka kuamini, kila mara aligeuka na kumtizama Kaguta labda atakuwa amefungua macho lakini wapi.







Mwishowe alitoka ndani ya gari akasogelea maji ya bahari akayachota na kiganja chake akanawa uso. Akiwa hapo alitizama maji ya bahari yakicheza kwa kwenda mbele na kurudi nyuma. Alitizama meli na boti kwa mbali zikipita. Alitizama watu aliowaona kwa mbali wakiwa ufukweni wakifurahia mandhari hayo, wakati huo yeye alikuwa anamimina machozi ambayo hayakuonyesha yatakatika muda gani na huku suruali yake ikiwa imelowa damu maeneo ya mapajani.





Anayelala na mgonjwa ndiye anayejua miugulio. Haikuhitaji shahada kujua Vitalis amekwazika hisia, amebeba gululi la majonzi ndani yake. Neno ulikataalo, ndilo Mungu apendalo jama, inspekta alisema na nafsiye. Baada ya kutizama bahari kwa muda na uso wake pozo, alisema kama vile anamwongelesha mtu anayemuona:





“I am sorry my friend: nimekuleta kifoni.”






Maneno hayo yalisindikizwa na machozi yenye kina kirefu. Ijapokuwa aliyafuta kwa kutumia vidole vyake bado yaliendelea kutiririka kiasi kwamba akawa haoni tena mbele.





Alikamua macho yake kwa kuyabinya kwanguvu kisha akageuka na kulifuata gari, muda huu alitembea akiwa anachechemea na uso wake ukipokea hilo jambo kwa kukunjamana. Aliwasha gari akaanza safari, alichojoa simu yake mfukoni akampigia Bernadetha.






“Naomba uje nyumbani muda si mrefu. Nakuhitaji.”





Aliongea maneno hayo tu kabla ya kurejesha simu yake mfukoni na kuendelea na safari. Mara ghafla akasikia mtu akikohoa nyuma ya gari. Alirusha macho yake mekundu kwenye kioo cha gari kilichoketi juu ya kichwa chake akamuona Kaguta akijinyanyua.





Inspekta Vitalis akatoa macho ya tahamaki. Haraka alipeleka gari kando kulipaki kisha akageuza uso wake na kutizama nyuma. Alaa! Akamuona Kaguta akiwa kakaa sasa amekunja uso wake na kiganja chake chaperemba kichwa kama mtu anayehisi maumivu.




“Kaguta!” Inspekta Vitalis aliita, uso wake ukiwa umechangamana hisia za mshangao na furaha.
“Nini kimetokea, Vitalis?” Kaguta aliuliza, “mbona kichwa chaniuma hivi?”
“Ulipigwa risasi kifuani ukadondoka! … How come upo mzima?” Vitalis aliuliza huku akitizama maeneo ya kifuani mwa Kaguta. Kaguta alitabasamu kidogo akauliza:
“Mbona macho yako mekundu, umelia?”





Inspekta Vitalis alitabasamu kama mtu ambaye hakuwa na mpango wa kufanya hivyo. Alitikisa kichwa chake akauliza:





“Kaguta, tell me imekuaje?”
“It’s proof. Nilivaa bullet proof, Vitalis.” Kaguta alijibu huku akibinya kifua chake na kidole.
“Usiniambie hukugundua hilo, Vitalis.”
“Sikugundua, labda kwakuwa umevaa koti jepesi.”
“Hapana. Ni kwakuwa ulimezwa na hofu yako.”
Inspekta Vitalis alitabasamu akashika usukani gari likaondoshwa.



*****
☆Steve
 
***SURA YA ISHIRINI NA SABA***





(MSIMU WA 02)






“Nadhani ni kwasababu alidondoka akajigonga kichwa.” Bernadetha alisema huku akimtizama inspekta Vitalis aliyekuwa amejilaza kwenye kochi.
“Nilidhani amekufa. Really!”



Kaguta na Bernadetha walicheka baada ya hiyo kauli, Bernadetha akatia neno:
“Hakuwa mbali sana na kufa. Ni uzi mwembamba sana unaotenganisha uhai na kifo pindi unapokuwa hauna fahamu.”
“Usihofu, Vitalis. Mi bado nipo sana tu.” Kaguta alisema kwa sauti yenye kubeba utani ndaniye. Wote wakacheka.
“Una bahati sana we kima. Sijui nani alikuambia uvae bullet proof leo!” Inspekta Vitalis alinena kisha akauliza huku akimtizama Bernadetha:
“Na vipi kuhusu mimi, nesi?”




Bernadetha akapasua mdomo wake kwa tabasamu kabla hajajibu.





“Inabidi uende hospitalini. Kutoa risasi mwilini bado hakutoshi, huenda ukawa umevunjika ama jeraha likawa na madhara zaidi.”
“Aaah! … Kwenda hospitali? Nachukia sana kwenda hospitali.”
“Itabidi uende tu. Hivyo vidonda ni vikubwa.”
“Nitaangalia.”
“Tafadhali usizembee katika hilo.”
“Sawa, nesi.”
“Naweza nikaenda? Nimemuacha Jombi peke yake na Miraji.”
“Mbona unawahi? … Ngoja basi tule.”
“Kweli!” Kaguta alidakia, “Itakuwa si vizuri endapo ukiondoka bila kula. Jombi yupo na mgonjwa, usihofu. They are bestfriends.”




Bernadetha akaridhia. Alienenda jikoni akapika chakula: Wali nyama na mboga za majani, akapakua na kuweka chakula mezani, akawakaribu Kaguta na Jombi. Wakati wanakula wakaendeleza soga:





“Kwahiyo, vipi kazini?” Bernadetha alimuuliza Vitalis.
“Nitawapa taarifa kesho.” Vitalis alijibu.
“Hakutakuwa na shida yoyote?”
“Sidhani. Nimepata ajali kazini.”
“Sasa utaendaje kuwapa taarifa?” Kaguta aliuliza.
“Nitawapigia simu. Au utan’saidia kwenda kutoa taarifa?”
“Sio mbaya. Kama ukin’taka nifanye hivyo, nitafanya.”
“Nitashukuru sana.”





Baada ya maongezi hayo madogo na kula, Bernadetha aliaga. Alimbusu Vitalis shavuni akaenda zake. Kaguta akabaki na inspekta.





“Ujue wewe Vitalis ni mjinga?”
“Kivipi?”
“Unajua kabisa wewe sasa hivi ni kilema alafu unamwachia Bernadetha anaondoka bila ya kumsisitizia aje hapa awe anakuhudumia. Unadhani mie nitaweza kukaa hapa muda wote? Nitaenda saa ngapi kunywa kidogo na watoto?”
“Nani kakuambia siwezi kujihudumia?”
“Maiti haiulizi sanda, ndugu.”
“Naweza kujihudumia mwenyewe. Wewe nenda unapotaka kwenda wala usijibane.”
“Hapana! Siwezi kukuacha mwenyewe hapa. Ila zingatia ushauri wangu, brother.”




Inspekta Vitalis hakusema tena kitu. Alijinyamazia kama mjinga.





*****
☆Steve
 
***SURA YA ISHIRINI NA NANE***





(MSIMU WA 02)








Mlango wa nyumba ulipofunguliwa, Miraji na Jombi walirusha macho yao wote kuona nani anaingia. Hakuwa mwingine bali Bernadetha, mama Miraji, aliingia ndani akatengeneza tabasamu usoni.




“Mnaendeleaje?”
“Safi tu. Vipi huko utokako?” Miraji aliuliza.
“Kwema tu.”
“Kweli?”
“Ndio. Kwema.”
“Sidhani kama ni kwema. Gauni lako lina damu.”




Bernadetha akashtuka kusikia hivyo, alitizama gauni lake kwa chini kweli akaona alama za damu. Macho yakamtoka.





“Mama, hakuna haja ya kunidanganya. Najua umetoka kwa inspekta. Vipi ana jeraha?”




Bernadetha alishusha pumzi ndefu akatikisa kichwa chake kama mtu akubaliye jambo. Akasema:




“Ndio, ana jeraha. Umefurahi?”




Hakusubiria jibu. Alienenda zake kwa mwendo wa haraka kuelekea chumbani. Miraji na Jombi wakamsindikiza kwa macho mpaka anazama.





“Naomba niondoke, Miraji. Inaelekea kuna tatizo huko nyumbani.”
Jombi aliaga. Miraji akanyanyuka na kumtoa mpaka nje.
“Kwaheri, Jombi.”
“Kwaheri. Hakikisha unazingatia na kuyatafakari yale niliyokuambia.”
“Sawa.”




Jombi alishika njia akaondoka. Miraji alirudi sebuleni akajilaza kwenye kochi. Baada ya muda mama yake akaja na simu na daftari akaketi papo, akawa anapiga mahesabu ya biashara zake. Kwa muda kama dakika kumi, hakuna aliyeongea na mwenzake mpaka pale mama alipofunga daftari lake la mahesabu.





“Mama, mbona umetoa picha ya baba sebuleni?” Miraji aliuliza. Mama akamtizama bila ya kumjibu, akaendelea kubofya simu yake.
“Mama, nimeuliza. Mbona umetoa picha ya baba sebuleni?”
“Kwani umeona leo?”
“Ndio, nimeona leo haipo.”
“Embu wacha nikuulize. Hii nyumba ya nani?”
“Ya kwetu.”
“Ulitoa hata sumni kuijenga?”
“Si alijenga baba yangu.”
“Mpumbavu wewe! Funga bakuli lako. Kwa kazi gani ya maana aliyokuwa nayo baba yako ajenge nyumba kama hii peke yake? Hii nyumba tumejenga mimi na baba yako, tukijibana na kujinyima kadiri tulivyoweza. Baba yako amefariki, hii nyumba ni ya kwangu, usinipangie nini cha kufanya. Umesikia?”
“Mama, jua mimi ni mwanao …”
“Kama ungekuwa unalijua hilo, ungekuwa na adabu na mimi. Umekuwa mtoto wa ajabu sana. Adabu huna, unanipandishia sauti kama vile unaongea na housegirl. Umekuwa wa kunchagulia wapi pa kwenda, kipi cha kuongea. Nikitoka uniulize nikirudi uniulize, naishi mahakamani?”
“Mama nafanya yote hayo kwa ajili yako.”
“Nimekuomba? Wakati unaumwa umelala kitandani hujielewi kwa lolote, nani alikuwa ananilinda? Mimi sio dada yako, mama yako!”
“Mama yote hayo ni kwa ajili ya …”
“Funga mdomo wako! Ishia hapo hapo.”





Macho ya Bernadetha yalikuwa mekundu. Alifura kama simba aliyejeruhiwa. Alikuwa anahema juu juu. Alikwapua daftari lake kama kibaka akarudi chumbani.





Zilipita siku tatu mwisho wa wiki ukabisha hodi. Bernadetha akatimiza ahadi yake kwa mwanae, Marietta, aliongozana naye kwenda kumtembelea inspekta Vitalis. Huko wakamkuta inspekta akiwa amekaa kwenye kiti cha matairi, Jombi akiwa ndiye dereva wake akimpeleka huku na huko.






“Hukuenda hospitali, Vitalis.” Bernadetha alitamka akiwa na uso usio na utani.
“Ndio, sikwenda.”
“Kwanini?”
“Nimeshindwa kwenda.”
“Umeshindwa? … Kivipi?”




Inspekta Vitalis hakupewa muda wa kujibu, Marietta alikuja haraka akitokea nje akamrukia Vitalis.





“Mariettaaa, si nimekuambia uncle anaumwa? Nenda nje kacheze.” Bernadetha alifoka. Marietta akasimama na kunywea ghafla.
“Muache bana. Njoo Marietta.” Vitalis alimvuta Marietta akamshika mkono. Marietta akamuangalia Vitalis kwa tabasamu.
“Utapona lini uncle uje kwetu?” Marietta aliuliza.
“Muda si mrefu napona. Ila ukitaka nipone haraka uwe unakuja kun’tembelea.”
“N’takuja kila siku.”
“Nitafurahi kweli. Haya shika hii kanunue chocolate. Si unapenda chocolate?”
“Ndio.”
“Haya kanunue.”






Inspekta Vitalis alitoa elfu moja mfukoni akampatia Marietta. Marietta alishukuru kisha akatoka ndani akawaacha Bernadetha na inspekta Vitalis. Wakaendelea kuteta:






“Tokea nimetoa taarifa kazini hakuna lolote ambalo nimefanyiwa. Hakuna hatua yoyote ambayo wameichukua. Sina pesa, Bernadetha.”
“Una uhakika taarifa imewafikia?”
“Exactly. Nimepiga mpaka na simu, wameishia kunipatia kiti tu cha matairi.”
“Labda wapo kwenye process. Nina uhakika watafanya jambo, Vitalis.”
“Lini? Hali yangu haisubiri.”
“Naamini hawatokuacha. We usichoke kuwasumbua kuwapa taarifa.”
Kinyume kabisa na alivyosema Bernadetha, majuma yakazidi kukata bila ya inspekta Vitalis kupokea mkono wowote wa msaada toka kazini kwake.






Mara kwa mara Bernadetha alikuwa anakuja kumuona na kumjulia hali, vile vile Kaguta. Hata inspekta alipokwenda kazini akiwa kwenye kiti cha matairi, hakuna alichoambulia zaidi ya ahadi tu. Mwishowe alikata tamaa. Kama haitoshi, akatumiwa barua ya kufukuzwa kazi.





“Siwezi amini kama haya ndio malipo ya kazi yote ile niliyofanya.” Vitalis alimwambia Kaguta kwa sura ya uchungu.
“Nilijitolea kwa hali na mali kupambana na kutimiza majukumu yangu, leo hii naishia kuwa fukara kilema?” Vitalis alitabasamu huku akitizama chini. Kaguta akamshika bega na kumpa moyo:
“Yote ni maisha, Vitalis, usinononeke sana. Mimi nipo, hakuna litakalo kwenda kombo.”





Vitalis akageuka mlevi. Kila siku alitaka aletewe pombe na Kaguta, na hata pale ilipokosekana kabisa alidiriki kumtuma Jombi kiroba hata cha mia tano apate kunywa.





Hakuweza kulala akiwa na akili timamu bali pombe. Hakuwa na hamu ya kula, Bernadetha alijitahidi kumpikia ila akiondoka tu, anaacha papo hapo. Hata afya yake ikaanza kuzorota. Miguu yake ikalemaa kabisa kutokana na kutokula wala kutotaka kufanya mazoezi. Hakuwa tena Vitalis yule, bali Vitalis aliyekuwa hajipendi wala kujijali tena.





“Naomba ukakae nae, hakuna tena jinsi. Yupo stressed sana, hali yake inaweza ikawa mbaya zaidi.” Kaguta alimwambia Bernadetha. Bernadetha alitizama chini kama mtu anayefikiria, uso wake ulikuwa umenyong’onyea mno. Alinyamaza kwa muda kidogo machozi yakambubujika.
“Nitajitahidi kulifanyia kazi, Kaguta.”
“Please. Vitalis anakuhitaji sana kwa sasa.”
“Nitajitahidi Kaguta.” Bernadetha alisisitizia. Kaguta alinyanyuka akaaga. Bernadetha akabaki mwenyewe sebuleni na uso wake uliopoa. Kwa muda wote waliokuwa wanaongea na Kaguta Miraji alikuwa ametega sikio mlangoni akisikiliza.





Kaguta alipoondoka, Miraji akafungua mlango na kwenda kumkuta mama yake sebuleni. Aliketi kando akamtazama mama yake aliyekuwa anabubujikwa na machozi, akamshika mkono.




“Mama.” Miraji aliita. Mama akageuza uso na kumtizama.
“Mara yangu ya mwisho kukuona katika hali uliyopo ni kipindi kile baba alipokufa. Haukuwa na raha. Ulikonda kwa mawazo. Hukutaka kuongea na mtu yeyote zaidi ya kulia kila uchwao. Na yote hayo ni kwakuwa ulimpoteza mtu uliyempenda. Siwezi kukuona ukipitia katika hali ile kwa mara ya pili kwa mana najua jinsi ninavyojisikia nikikuona hivyo. Nakuomba futa machozi mama. Nenda kapiganie maisha ya unayempenda.”





Miraji alisema kwa sauti ya chini na punde machozi yalimtoka. Mama yake alimtizama huku naye machozi yakimbubujika. Alimvuta mwanaye akamkumbatia kwanguvu na kumwambia:





“Ahsante. Wewe ndiye Miraji niliyekumis kwa muda wote huo tangu ulipodondoka.”
Miraji alitabasamu, akasema:
“Nisamehe mama kwa kukatili moyo wako kwa muda wote huo. Sasa naelewa ni jinsi gani Vitalis anamaanisha kwako.”



Alimfuta machozi mama yake kwa kutumia vidole vyake, akamwambia:
“Nenda mama.”
Mama akamjibu:
“Nataka twende wote.”
Miraji akatikisa kichwa.


*****
☆Steve
 
Mi naona sasa OCD anahusika na mateso ya inspector Ila wamemgusa mbogo sehemu nyeti ngoja huo mguu upone waone watakavyokula mateke mpaka watajuta na ndo ivo tatuu imechomwa na pasi sipati picha wallah
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom