***SURA YA ISHIRINI***
(MSIMU WA 02)
Ndani ya asubuhi ya saa mbili na nusu, Kaguta akawasili kwenye nyumba ya inspekta Vitalis Byabata. Alipiga honi akatoka mama Miraji, ama Bernadetha kwa jina alilopewa na wazazi wake. Wakasalimiana kwa bashasha la furaha kisha Kaguta akamuulizia inspekta.
“Hayupo, ametoka muda si mrefu. Nilidhani mmewasiliana.”
“Hapana. Atakuwa kaenda wapi?”
“Ameniaga anaenda hospitali kwenda kumuona dokta Rajesh Deepti wa Royal Hospital.”
“Kuna tatizo lolote?”
“Hapana. Ni ameenda kufanya tu upelelezi wake. Dokta Rajesh ndiye alikuwa daktari wa mume wangu, na yeye ndiye alikuwa anaujua ukweli wote kuhusu kifo cha mume wangu kabla ya kuupotosha umma kwa sababu zisizojulikana.”
“Sawa. Vipi mtoto ameenda shule? Yani leo nilipitiwa na usingizi kama mzoga.”
Bernadetha alicheka kidogo kisha akajibu;
“Usihofu. Vitalis ameenda naye alipoamka tu asubuhi.”
“Afadhali. Sasa acha mie niende huko hospitali nikaonane naye.”
“Safari njema.”
Kaguta aliwasha gari, ila kabla hajasogea, Jombi alitokezea tokea ndani.
“Aaaah bwana Kaguta, kweli unataka uondoke hata hatujasalimiana?”
Kaguta alicheka kwanza ndio akajibu.
“Aisee. Samahani sana ndugu yangu. Si unajua tena, haraka haraka! Vipi lakini?”
“Safi tu. Wewe je?”
“Aaah … Nipo njema tu!”
“Nadhani sasa ni bora ukashuka unywe chai kabisa.” Bernadetha alishauri.
“Najua hujatia chochote mdomoni, Kaguta. Wala usifikirie kunipiga sound zozote.” Bernadetha alisisitizia. Kaguta akabakia bila ya maneno, alishuka akaungana na Jombi na Bernadetha wakaenda ndani.
Huko ndani ya Royal hospital kwenye sakafu ya tano, Vitalis alikuwa mbele ya mlango mpana ulioandikwa jina la Doctor Rajesh Deepti. Chini ya jina hilo kulikuwa na ratiba ya maonano, Vitalis aliitizama kisha akagonga mlango.
“Who is it?”
Sauti iliuliza ikitokea ndani. Vitalis hakujibu. Alitulia kama vile hakusikia hilo swali.
“Ingia.”
Vitalis akafungua mlango na kuingia ndani.
“Nani wewe? Taka nini hapa jaona ratiba ka mlango?” Mtabibu aling’aka.
Vitalis aliketi taratibu kisha akamtizama daktari aliyekuwa na uso na nywele za kihindi usoni akiwa na miwani ya macho.
“Naitwa Inspekta Vitalis Byabata.” Inspekta akaonyeshea kitambulisho chake. “Nina maongezi na wewe.”
“Maogezi bhanaa … Taka nini kwangu?”
“Unamjua huyu?” Vitalis alitoa picha ya Malale akamuonyeshea mtabibu. Mtabibu akashtuka.
“Sijui mimi!”
Vitalis akatabasamu kwa dharau.
“Mbio zako hazitokupeleka popote, dokta. Ni bora ukaeleza ukweli bila shuruti.”
“Kweli gani nataka phephe? … Sijui kitu. Toka kwa ofisi yangu bhana niko bhize. ”
Vitalis alinyanyuka akaufuata mlango akaufunga na komeo. Mtabibu Rajesh akawahi kuchukua simu yake ya mezani, kabla hata hajasema lolote, Vitalis akawa tayari ameshamfikia na kumpokonya simu kisha akatoa bunduki yake na kumuonyeshea.
“Kwanini uliongopa juu ya kifo cha Malale?”
Uso wa Vitalis ulibadilika na kuwa mchungu ghafula, hakuonyesha masikhara hata punje. Rajesh alikuwa mpole ghafla, macho yalimtoka na pumzi yake ilikuwa inapanda na kushuka kwa haraka.
“Usiniue, takwambia … takwambia kila kitu!”
“Sema kabla sijakupa tiketi chap ya kwenda jehanam!”
“Nilitumwa! Kama singalifanya. Ingeniua!”
“Nani?”
“Temvu … Temvu na wenzhake.”
Vitalis alishusha mkono wake wenye bunduki akaketi.
“Si nimeshaambia wewe. Nenda bhasi.”
“Inabidi twende wote kituoni. Una mashtaka ya kujibu.”
“Hapana! Hapana kwenda kituoni mimi.”
“Embu tusipotezeana muda bwana mzee. Simama twende kituoni, si mpaka tulazimishane.”
Japokuwa Vitalis alitia msisitizo, Rajesh hakuwa tayari kwenda popote. Ilibidi nguvu itumike. Vitalis alimnyanyua mtabibu kwa nguvu kwa mtindo wa kukwida akamburuzia mpaka mlangoni.
Akiwa katika purukushani ya kutaka kuufungua mlango, Vitalis akaona kitu kiunoni mwa mtabibu baada ya shati la mtuhumiwa wake kupanda. Aliona tattoo! Tattoo ile ile ambayo yeye anayo ikiwa imefunikwa na shati lake la kitenge.
“Umenidanganya, sio? Wewe ni nani?”
Vitalis aliuliza kwa sauti ya kufoka. Huku akimuonyeshea bunduki mtabibu Rajesh.
“Si ameshaambia wewe. nini taka kwangu?”
“Wewe ni mfuasi wa Mr Kim. Si ndio? … Hiyo tattoo umetoa wapi?”
Rajesh akashikwa na kigugumizi. Alichomekea shati lake akatengenezea miwai yake iliyokaa upande.
“Taka nini kwangu phephe?”
“Jibu swali langu, upesi!” Vitalis aliamuru. Kufumba na kufumbua, Rajesh alinyanyua mguu wake wa kuume akatandika mkono wa Vitalis uliobebelea bunduki. Bunduki ikarukia kando. Haraka kama upepo, Rajesh akaruka teke na kumsigina Vitalis kifuani, Vitalis akadondokea chini kama fuko la marando. Rajesh akavua koti lake la utabibu akaliweka juu ya meza.
“Si unataka vita, acha uipate sasa.”
Alisema Rajesh tena kwa lafudhi nzuri tu tofauti kabisa na ile ya mwanzoni aliyokuwa anaigiza.
Vitalis alichumpa kwa kutumia mikono yake akanyanyuka na kumtizama Rajesh. Wote wakakunja ngumi kwa mtanange.
Rajesh alirusha teke akiwa hewani, Vitalis akakwepa, lle kujiweka tu sawa, zikarushwa ngumi zingine mbili za haraka, Vitalis akaipangua moja na kuikwepa nyingine ambayo ilienda na kurudi kama kiwiko haraka kikambatua inspekta kichwani. Rajesh akatabasamu. Vitalis akaguna.
“Umemaliza?” Vitalis aliuliza. Vuup! Likaja teke lingine likifuata tumbo la Vitalis, Vitalis akajiweka ubapa haraka, teke likapita kama gari moshi. Rajesh alipolirejesha teke lake kwa mfumo wa goti, Vitalis akadaka goti lile na kulisukumia kando. Rajesh akaja tena kwa pupa, mara hii akitishia kurusha teke la mguu wa kulia ingali anataka kuleta la kushoto.
Vitalis akamtangulia Rajesh hatua mbele, akauwahi mguu ule wa kushoto kwa kuukanyaga kama mtu anayepiga breki ya gari na ule wa kulia uliokuwa unatishia akaudaka na kuurejesha chini.
“Kuna jipya? Au nianze na mimi kushambulia?”
Vitalis aliuliza. Upesi, Rajesh akachukua waya wake wa vipimo uliokuwa mezani akautuma umchape Vitalis usoni. Bahati haikuwa yak wake kwani Vitalis aliinama, waya ukapita kisha akapiga ngumi mkono wa Rajesh mbele kidogo ya kwapa, Rajesh akapigwa na ganzi paaap! Waya ukadondoka chini.
“Mi naona twende tu kituoni. Tunachoshana hapa!”
Vitalis alisema huku akitengenezea shati lake na kuigiza kama mtu afutaye vumbi. Rajesh alimtizama kwa hasira, akajaribu tena kushambulia kwa kupiga sarakasi atue na miguu kichwani mwa Vitalis, ila haraka mikono yake ikatenguliwa na miguu ya Vitalis akadondoka chini!
Vitalis akasonya kisha akaanza kuifuata bunduki yake. Alipoikota na kuiweka kiganjani akasikia mlio mkali wa kioo. Alipotizama, hakumuona tena Rajesh! Haraka akakimbilia dirishani kuchungulia, akamuona Rajesh kwa chini akiyoyoma.
“Shit!”
Vitalis alifoka. Alipepesa pepesa macho yake huku na huko ndani ya ofisi, akaona simu kubwa LG nyeusi akaitwaa na kuiwasha. Ubaya akashindwa kutambua pattern iliyowekwa, ila hakuiacha, aliiweka mfukoni akaondoka zake. Baada ya dakika ishirini akawa yupo nyumbani. Alikutana na Bernadetha ama mama Miraji akamueleza kila jambo alilokumbana nalo huko.
“Kama ilivyokuwa msaada wa Jombi kwa Miraji. Daktari naye aliwasaidia wakina Mtemvu ili wamalizane wenyewe kwa wenyewe bila wao kujua. Nimeona ile tattoo kiunoni mwake, ina maana ni mfuasi wa bwana Kim.”
Alisema Vitalis kwa kujiamini.
“Mmmh … huyu bwana Kim ananitisha kusema ukweli. Inspekta, najua kwako ni vigumu, ila kama waweza naomba uachane naye tupate kuishi maisha yetu tu ya kawaida. Ni kama vile tunapambana na bahari, ni mkubwa mno.”
“Hapana, mama. Siwezi kumuacha. Embu fikiria ni wangapi amewaumiza kwa biashara zake haramu? … Vijana wengi huko mitaani wanakufa kwasababu yake. Nchi yetu i mashakani na dhambini kwa ajili yake. Najua yeye ni goliath ila nasi tutajitahidi tuwe Daudi.”
“Sawa. Nakuombea kila siku Mungu akupe salama. Sitaki kukupoteza, kila unapotoka na kurudi nyumbani salama ni ahueni kwangu.”
“Nashukuru sana kwa kujali. Umekuwa mama yangu wa pili sasa.”
Bernadetha alicheka kidogo akamtizama Vitalis.
“Kujali ni jukumu mojawapo la mwanamke.”
Vitalis akatabasamu na kutizama chini. Kwa muda usiopungua wala kuzidi dakika mbili kukawa kimya. Vitalis alimtizama Bernadetha machoni, naye Berna akafanya vivyo hivyo. Ni kama vile kuna kitu walikuwa wanakiona sisi tusikione. Vitalis alinyanyua mkono wa kuume wa Bernadetha akaushika kama vile anataka uvalisha pete. Aliupeleka mkono huo kinywani akaubusu. Bernadetha akatabasamu.
“Nashukuru kwa yote unayonifanyia.” Vitalis alisema kwa sauti ya chini. Bernadetha hakusema jambo, aliacha macho yake makubwa yaseme kila kitu kwamba anafurahi kusikia vile. Labda ndio kilikuwa kipindi muafaka naye akajihisi mwanamke tangu mumewe afariki.
Kwa muda wakaendelea kutizamana wasione lolote linaloendelea ulimwengu mwingine. Huko nje ya nyumba, Kaguta aliwasili. Alikuwa amewekelea earphone masikioni kichwa chake kikidunda kama kitenesi. Alipopanda kibarazani kabla hajagonga mlango macho yake yaliruka ndani, na humo akamuona Vitalis akiwa na Bernadetha katika mkao ule wa mtizamano. Kaguta akatabasamu, na bila ya kusema lolote akageuza na kunyata taratibu akaondoka eneo lile.
Vitalis aliuteka mkono mwingine wa Bernadetha akaushikilia, sasa mikono yote akawa nayo. Taratibu akapeleka mdomo wake kinywani mwa Bernadetha akambusu mwanamke pap na kuacha kama vile alikuwa anataka kusikilizia mtendwa atasemaje.
Bernadetha akawa kimya zaidi alitabasamu. Vitalis akapeleka tena mdomo wake kwa Bernadetha, Bernadetha akaupokea mdomo wa Vitalis kwa kuufunda. Ila mara wakasikia mlango wa chumbani unafunguliwa, zoezi lao likakomea hapo. Punde Jombi akawa amefika sebuleni na kusalimia.
“Hivi mnajua leo ni siku ya ripoti ya Miraji?”
Jombi aliuliza. Vitalis na Bernadetha wakatizamana. Bernadetha akatabasamu.
“Najua. Naenda huko jioni hii. Acha nikajiandae.” Bernadetha alisema kisha akatoka na kuelekea jikoni akawaacha wanaume wale wawili watete mawili matatu. Vitalis akamueleza Jombi yale yaliyotukia hospitali. Jombi akaonekana kushtushwa na taarifa hizo.
“Bwana Rajesh ni coordinator wa bwana Kim kwa wahindi wote walipo hapa nchini. Kumpata kwake ni mojawapo ya hatua japo ya mbali ya kumpata bwana Kim.”
“Una maanisha nini kusema coordinator wa wahindi.”
“Ni hivi, kila race iliyopo nchini ina coordinator wake, ama tuseme muwakilishi kwa mr Kim. kwa watu weusi, coordinator ni bwana Isaac Makongo. Kwa wahindi ni huyo, Rajesh Deepti. Na kwa wazungu ni bwana Wayne Ford. Si rahisi kuwapata hao watu. Wana viapo vya binafsi.”
“Unaweza ukaniambia nitawapata wapi?”
“Kusema ukweli, sijui. Hawana makazi ya kudumu yanayojulikana. Ni watu wa kuhama hama pia kusafiri huku na kule.”
Inspekta alishusha pumzi ndefu akashika tama. Ni wazi aliona kuna mlima mkubwa mbele yake anaotakiwa kuusogeza. Kazi haikuwa nyepesi hata punje. Alinyanyuka akaaga, akaenda kuoga kisha akashika tanakilishi yake na kuitia modem, akaanza kuperuzi mtandaoni.
Aliandika jina kamili la bwana Kim na kubonyeza kitufe cha kutafuta, paap majibu kadhaa yakaja. Bwana Kim akatambulishwa kama mfanyabiashara mkubwa wa mambo ya mawasiliano kwa kupitia kampuni yake ya Bartel yenye makao yake Barmuda.
Zaidi ya hapo, picha mbalimbali za bwana Kim zikarushwa na hata makampuni ambayo ana ubia nayo, hadi ambazo ameweka hisa zake kwa wingi; makampuni ya vinywaji laini, makampuni ya bidhaa za wanawake, makampuni ya kilimo na kadhalika. Mitandao ikaendelea kumwaga maneno juu ya bwana Kim kuwa ni mfanyabiashara mkubwa na mwenye nguvu katika bara la Afrika na Amerika ya kaskazini.
Inspekta aliporidhika na taarifa alizozipata, akafunga tanakilishi yake na kujilaza kitandani. Alikuja kuamshwa baadae na sauti ya Kaguta. Ilikuwa ni jioni, jua limeanza kupoteza nguvu zake. Inspekta alinyanyuka akaenda sebuleni kukutana na Kaguta ambaye alikuwa amekaa na Jombi kwenye kochi. Wakasalimiana na kujuliana hali, Kaguta akaanza kueleza alichokipata toka kwa Sandra, mpaka kumtambulishwa kwake kwa bwana Isaac Makongo.
Inspekta na Jombi wakashtushwa na taarifa za bwana Makongo, nao huo ukawa mwanya mzuri kwao kuanza kumtafuta mtuhumiwa wao huyo baada ya inspekta naye kueleza ni wapi alipogumana nalo hilo jina.
“Kwa mujibu wa maelezo ya Sandra, Isaac Makongoanaishi kurasini, nyumba namba 898. Picha zake hizi hapa. Anapendelea sana kutizama mpira, na maeneo yake ni Samaki Samaki mbezi beach.” Kaguta alimwaga maelezo huku akiwa kazitandaza picha juu ya meza.
“Basi hatuna tena muda wa kupoteza, nadhani ni muda wa kuanza kufanya kazi. Tupange ni jinsi gani tunaweza kumpata huyu wakala haraka iwezekanavyo.” Inspekta alisihi.
“Kweli, ila inabidi tuwe waangalifu mno. Huyu mtu si wa kawaida.” Jombi naye akasisitiza.
“Kabisa!” Kaguta akadakia na kuendeleza maneno, “Inabidi tuanze pole pole. Kesho kutakuwa na mechi kubwa ya UEFA, najua hatokosa maeneo yake hayo. Alimradi najua sura yake, nitamfuatilia. Niacheni hiyo kazi.”
“Hakuna shida. Ila hakikisha unatupasha kila kinachotukia huko.” Inspekta alisema.
“Nitafanya hivyo.” Kaguta akamtoa hofu.
“Mbali na hayo, kuna baadhi ya taarifa nimezipata toka mtandaoni; makazi ya bwana Kim.” Inspekta alieleza. Jombi akatikisa kichwa chake huku akipunga mkono kama vile mtu anayeaga,
“Hakuna kitu cha ukweli huko. Hakuna mtu anayejua makazi ya bwana Kim hata wafanyakazi wake. Mitandao yenyewe haina data halisi juu ya huyo bwana.”
“Sasa ni wapi tutapata taarifa zake?” Inspekta akauliza.
“Ni kuzitafuta tu. Otherwise hakuna lolote.” Jombi alishauri. Inspekta na Kaguta wakawa kama wamekamatwa na kabutwaa.
“Kwanza, hakuna aneyejua sura halisi ya bwana Kim. Sura ambazo zimewekwa mitandaoni si za kwake, ni bandia na za kutengenezwa. Ni watu wachache mno wanaomjua the real Kim, watu wake wa karibu mno, kama vile familia yake.”
“Sasa hata hiyo familia yake tutaikotea wapi?” Kaguta aliuliza.
“Hapo ndipo kwenye shida. Kama nilivyosema mwanzo. Hakuna mtu anayejua haswa maelezo ya karibu ya bwana Kim. Ni kazi ya kutafuta hayo.”
“Hakuna linaloshindikana. We shall do it.” Inspekta Vitalis alisema kwa kujiamini. Kaguta akatikisa kichwa kumuunga mkono.
Baada ya muda mfupi, simu ya inspekta ikaita. Alipigiwa na Bernadetha, alipokea akaweka simu sikioni;
“Hallo … Hospital? … Haya sawa, nitakuwa hapo muda si mrefu.”
Simu ilipokata akawatonya wenzake;
“Miraji ameruhusiwa kutoka. Inabidi niende nikamtoe, si unajua tena mambo ya utaratibu.”
“Twende!” Kaguta akatamka.
“Na mimi naomba niende.” Jombi naye akatia neno. Wakajiandaa na kujipakia kwenye gari, wakaelekea hospitali na kurudi na Bernadetha pamoja na Miraji. Miraji alionekana kuchoka. Macho yake yalikuwa yanafunguka na kufunga. Ni kama vile alikuwa amelemewa na usingizi mzito.
“Daktari amesema anahitaji mapumziko. Asifanye kazi yoyote ngumu kwa sasa zaidi ya mazoezi madogo madogo.” Bernadetha alilonga.
Jombi akishirikiana na inspekta Vitalis wakamshusha Miraji na kumpeleka moja kwa moja kitandani kwenye chumba alalacho Jombi.
“Mungu mkubwa. Sikujua kama kuna siku mwanangu atatoka hospitali.” Bernadetha alisema kwa tabasamu.
“Atapona tu, na atarudi katika hali yake.” Inspekta akamtia moyo mwanamama.
*****
☆Steve