***SURA YA THELATHINI NA MOJA***
(MSIMU WA 02)
Ikiwa ni asubuhi ya saa mbili watu walikuwa wamejazana kwenye kijiwe cha magazeti kilichokuwa kimejiweka pembezoni mwa barabara kuu ya lami. Walikuwa wanateta juu ya vichwa vya habari pasipo kuonekana hata mmoja akiwa amebebelea gazeti mkononi.
Kundi hilo lililokuwa na watu wanne liliongezeka baada ya Kaguta kusogea na kurusha macho yake kwenye vichwa vya habari, gazeti moja likakamata macho yake.
‘SIMANZI: KIJANA MMOJA AUWAWA KINYAMA KWA RISASI KUMI’
Kichwa cha habari kilijieleza kikiambatana na picha ya kijana huyo ambaye alikuwa amechafuka damu. Kaguta alitoa shilingi elfu moja mfukoni mwake akampatia muuzaji na kumnyooshea kidole gazeti atakalo, muuzaji akampatia.
Kaguta akalisogeza gazeti machoni na kuanza kuitizama ile picha ya muhusika aliyeuwawa kwa risasi kumi. Mara mmoja wa wale waliokuwa wanajadili vichwa vya habari akaanza kuhororoja:
“Unamtizama huyo jamaa? … Unaweza ukamuona huruma ila mshenzi kama nini!”
Mara mwenzake akauliza:
“Nani huyo?”
“Si Roby!” Jamaa akajibu. Basi majadiliano yote yakahamia kwenye lile gazeti alilonunua Kaguta.
“Muuaji kauwawa hatimaye. Ila nani atakuwa kamuua?”
“Watakuwa wameuana wenyewe hao. Si unajua hawa madili yao ya madawa?”
“Kweli, hata mimi nahisi hivyo. Unakumbuka siku ile huyu jamaa alipita na gari kwa kasi tulipokuwaga kule magomeni?”
“Alikuwa anaendesha Prado?”
“Ndio, nyeusi hivi.”
“Eeeh … nakumbuka!”
“Sasa pale si alikuwa anaenda kwa yule Niga c. He! Baadae nakuja kusikia Niga c kauwawa na risasi mwanangu!”
“Walimuua yule!”
“Ndio mana yake, cha kushangaza hata mshkaji hakufuatiliwa wala nini!”
Kaguta alifunga gazeti lake akaondoka lile eneo. Alielekea hospitalini kwenda kumjulia hali Vitalis, alipomkuta mlengwa wake kalala alifungua gazeti lake akawa anasoma habari ya Roby. Alizama gazetini mpaka pale alipokuja kushtuliwa na Bernadetha.
“Umekuja saa ngapi?”
“Muda si mrefu sana. Vipi unaendeleaje?”
“Safi tu. Mbona hujamuamsha Vitalis?”
“Sijataka kumsumbua, mwache tu apumzike.”
“Hapana. Anatakiwa aamke anywe chai saa hivi.”
“Iko wapi?”
“Namletea hivi punde.”
Bernadetha alimuamsha Vitalis akaketi kitako. Baada ya kujuliana hali, Kaguta alimuonyesha Vitalis gazeti aliloninunua, Vitalis akapitia yaliyomo, alipomaliza Bernadetha naye akalichukua na kulisoma.
“Nani atakuwa kamuua?” Vitalis alimuuliza Kaguta kwa mshangao.
“Watakuwa ni wakina Isaac Makongo.” Kaguta alijibu.
“Umejuaje?”
“Hujaona pale kwenye gazeti?”
“Sijaona sehemu iliyosema kauwawa na wakina Isaac.”
“Kauwawa maeneo Oysterbay na huo mtaa naujua. Pembezoni mwake mbele kidogo kuna nyumba kubwa ina namba 898.”
“Ila Isaac anaishi Kurasini.”
“Basi jua kati ya yule muhindi ama yule mzungu, Ford, atakuwa anahusika na kifo hiko.”
“Ila kwanini wamuue?”
“Hapo ndipo kuna la kutafuta. Inabidi tufanye utafiti.”
“Tufanye? … mmh mmh hapana! Sijihusishi tena na mambo ya hao watu. I am done, Kaguta.”
“You are done kivipi, Vitalis?”
“Sitaki tena kujihusisha na mambo yoyote ya upelelezi. Sasa hivi mimi ni mwananchi wa kawaida, acha iwe hivyo tu. Kama Mungu akinijalia nikatoka hapa, basi nitaenda kufanya biashara zangu basi.”
Kaguta alimtizama Bernadetha, Bernadetha akapandisha mabega. Kaguta alishusha pumzi ndefu kisha akanyanyuka.
“Nitakuja baadae mida ya jioni. Ila Vitalis, fikiria maamuzi yako mara mbili.”
Kaguta akatoka. Bernadetha akamtizama Vitalis na kutabasamu.
“Mbona unatabasamu?”
“Nimefurahi.”
“Umefurahishwa na nini?”
“Kujua kuanzia sasa utakuwa salama.”
Vitalis alitabasamu akaunyanyua mkono wa Bernadetha na kuuweka kifuani kwake.
****
Gari la Kaguta lilipaki pembezoni mwa baa iliyobebelea jina la Karunde. Ni mida ya saa mbili ya usiku. Kaguta alishuka akiwa kavalia suruali nyeusi ya kadeti, shati jeupe la kubana na koti single button rangi nyekundu aliyoifananisha na viatu vyake vya kuchomeka.
Alinyookea glocery akaagiza kinywaji, alibebelea glasi akapeleka mdomoni na kuria mafundo mawilikabla hajatoa simu yake mfukoni na kutuma ujumbe kwa Sandra.
‘Nipo hapa bar karibu na kwako njoo basi’
Alimaliza kinywaji chake lakini bado Sandra hakutokea. Alinyanyuka akalipa akatoka nje ya bar mpaka kwenye gari lake, akarusha macho yake barabarani pasipo kuomuona mtu. Alianza kutembea taratibu taratibu mpaka nyumbani kwa Sandra.
Aligonga mlango lakini hakuruhusiwa aingie ndani. Aligonga na kugonga lakini hakukuwa na majibu yoyote. Alizunguka nyuma ya nyumba akachungulia kupitia dirishani, akaona miguu ya Sandra ikiwa imelala chini. Alijitahidi auone mwili mzima lakini haikuwezekana, pazia la dirisha lilimkinga.
Haraka Kaguta alirudi mlangoni, alichomoa earphone ya simu mfukoni akaing’ata na kutengeneza waya mnene kiasi alioupenyeza kwenye kitasa akadondosha ufunguo uliokuwemo humo. Akautoa waya na kuupindisha alama ya saba, akaungiza ndani ya tundu ya kitasa na kuuchezesha, mara ikasikika sauti ‘tas!’ mlango ukafunguka.
Kaguta aliingia ndani akamkuta Sandra uchi wa mnyama, pembezoni mwake kulikuwa na pakti ya madawa ya vidonge, mashavu yake yalikuwa na alama nyekundu za vidole, uso umevimba na kuvijilia damu na mdomo wake ulikuwa una mabaki ya mapovu.
Kaguta alikimbilia kabatini akatoa gauni. Alimvika Sandra kisha akambeba na kumkimbizia garini kwake haraka. Aliondoa gari mpaka hospitalini ndani ya dakika mbili tu, alishuka akambeba Sandra na kumuingiza ndani. Alitolewa nje ya chumba cha wagonjwa akaambiwa angoje majibu nje.
Aliketi kwenye mabenchi, akawa amefungamana mikono yake na kuiweka mbele ya mdomo wake. Alikaa hapo kwa muda, hakuna dokta aliyekuja kumpa majibu. Mwishowe alilala kabisa. Alikuja kuamshwa na daktari usiku ukiwa mzito.
“Mgonjwa wako amekunywa madawa: alikuwa anafanya jaribio la kujiua. Na inaelekea alipta kipigo kabla hajachukua maamuzi hayo.”
“Anaendeleaje kwa sasa?”
“Anaendelea vizuri. Tumempa huduma ya kwanza tu. Tunaomba uende kituo cha polisi ukaripoti, hatuwezi mtibia bila hivyo.”
Kaguta alitoa kitambulisho chake cha kazi akamuonyesha daktari. Daktari akasema:
“Okay. Ameomba aonane na wewe.”
Daktari aliposema tu hivyo, Kaguta alianza kutembea. Daktari alimshika mkono akamwambia:
“Fanya haraka. Inabidi apumzike.”
Kaguta alitikisa kichwa akaendelea na safari yake. Alipoingia chumba cha Sandra alikutana macho kwa macho na mwanamke huyo. Sandra akaanza kulia. Kaguta alimsogelea akambembeleza anyamaze.
“Niambie nani kakufanyia hivi?”
Sandra akiwa amekabwa na kilio alisema:
“Isaac … Isaac Makongo. Amemuua Roby, amenipiga na kusema hatambui ujauzito nilio nao. Hataki kuniona tena! Sikudhani kama angekuja kunifanyia unyama kiasi hiki!”
Baada ya hayo maneno, Sandra aliangua kilio kama aliyefiwa. Kaguta alitikisa kichwa chake akamvuta Sandra na kumkumbata. Ila punde, Sandra alizirai. Kaguta alikimbia kwenda kumtafuta dokta akaja naye upesi, daktari alimtoa Kaguta nje afanye kazi yake, baada ya muda daktari alitoka chumbani akampasha Kaguta habari.
“Amezirai tu. Nadhani sasa ni muda wa kumuacha apumzike.”
Kaguta alitoka hospitali akaeleka bar. Alinunua chupa moja kubwa ya konyagi akaiweka mezani taratibu akawa anamiminia kooni kwake kwa pozi. Kabla ya chupa kufika nusu, Bhoke alisogea eneo alilopo Kaguta. Alitabasamu kisha akapaza sauti yake laini:
“Mambo handsome!”
Kaguta alimtizama Bhoke kisha akapandisha nyusi zake.
“Poa, karibu.”
Bhoke alivuta kiti akaketi.
“Niambie, handsome. Kitambo sijakuona.”
Kaguta alitabasamu tabasamu lililo kinyume na macho yake. Alikunywa fundo moja kisha akajibu:
“Mbona nipo tu. Mambo yamebana.”
“Nimekumisi sana. Nichukue kinywaji.”
“Chukua.”
Bhoke aligeuza shingo yake akatazama kaunta.
“We Mishiii naomba castle nyongaa!”
Haraka mhudumu alikuja na sahani inayobebelea castle, akaiweka mezani na kuifungua. Bhoke akaidaka castle akaipeleka mdomoni na kunywa mafundo manne kama vile maji.
“Sasa, leo twaenda wote ama?”
“Hapana!”
“Kwanini? … Umepata mwanamke mwingine baba?”
“Hapana. Nimechoka tu.”
Baada ya kusema hivyo, Kaguta alisimama akamiminia kinywaji chake mdomoni kama vile si konyagi bali juisi au energy drink, alafu akaaga:
“Sasa mi naenda. Tutaonana.” Alisema huku akitoa pesa kwenye pochi yake na kuilaza mezani. Bhoke akabaki akimtizama Kaguta kama mtu anayeshuhudia mtu akimla simba.
Kaguta akautoa mwili wake pale bar na kufuata gari lake, wakati yu njiani kwenye lami mara simu yake ikapokea ujumbe. Mkono moja ulibeba simu na kuipeleka usoni wakati mwingine ukiwa umeshikilia usukani, akausoma ujumbe:
“Hi Peltridge! ts me Rhoda from hospital.”
Kaguta alisonya akaitupia simu yake kwenye kiti cha kando.
****
☆Steve