Sikujua Ungenisaliti Mpenzi

Sikujua Ungenisaliti Mpenzi

Madame S

JF-Expert Member
Joined
Mar 4, 2015
Posts
17,190
Reaction score
34,526
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (1)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

*****
HALI ya hewa ilikuwa ya baridi sana asubuhi hiyo, mvua za rasharasha ziliendelea kunyesha na hapakuwa na dalili ya kukatika! Kwa mji wa kibiashara kama Dar es Salaam, mvua hizo zilikuwa kero kubwa sana kwa wakazi wake.
Ziliharibu kila kitu, wengi walisikika wakilaumu kwanini ilinyesha mjini badala ya Bagamoyo! Ni mvua ambayo ilikesha usiku kucha ikinyesha hadi asubuhi hiyo bila kukoma. Mavazi makuu sasa yakabadilika, yakawa ni makoti, masweta na majaketi!
Mvua ilikuwa kero!
Lakini kwa wenye nazo, haikuwa kero kubwa sana, kwani waliamua kupumzika majumbani mwao wakifurahia fedha na mali walizonazo. Lakini kuna ambao walizidishiwa zaidi maumivu na mvua hizo; wagonjwa waliolazwa katika hospitali mbalimbali.
Ndani ya wodi ya majeruhi, katika Hospitali ya Amana, Ilala jijini Dar es Salaam, hali haikuwa shwari kwa kijana huyu! Kwa mwonekano wake, alikuwa anavutia sana. Ana macho makubwa meupe, yenye mboni nyeusi. Mpangilio wa nyusi zake ndiyo unaowachanganya wanawake wengi. Kifua chake cha mazoezi ni kati ya vitu vinavyozidisha mwonekano wake wa kimahaba.
Hakuna nguo ambayo anaitia mwilini inamkataa. Kila anachovaa anapendeza sana, huyu ni Bruno. Utanashati wake, mvuto wake wa kimahaba, uchangamfu na kila kitu, vyote vimepotea! Sasa Bruno amekuwa mpya! Amebadilika kwa kila kitu.
Hana tabasamu tena!
Hana furaha tena!
Maisha yake sasa yametawaliwa na huzuni na hofu tupu. Amelala kitandani akionekana kuwa na mawazo na kukata tamaa kabisa. Hana tumaini tena, kila kitu kimeshaharibika. Macho yake yamezingirwa na machozi, anaonekana hana amani wala matumaini ya kuishi muda mrefu baada ya pale.
“Mimi ni mzoga tu,” alijikuta akitamka kwa sauti huku mvua ya machozi ikianza kunyesha machoni mwake.
Msichana mrembo aliyekuwa akipita jirani yake, aliumizwa sana na machozi yake; akajua lazima alikuwa na jambo zito lililokuwa likimtatiza. Akapiga hatua za taratibu, macho yake yakiwa yanamwangalia sawia Bruno.
“Pole!” Akatamka msichana huyo kwa sauti ya chini, lakini kwa haraka kidogo.
“Nashukuru sana!”
“Pole utapona tu!”
“Ahsante sana.”
“Naitwa dada Vanessa, sijui wewe!”
“Bruno.”
“Pole sana Bruno, Mungu atakupa afya njema. Jipe moyo!”
“Ahsante sana!”
“Umepatwa na nini?”
“Ajali, nimepoteza mguu mmoja dada yangu!”
“Masikini pole sana.”
“Nashukuru.”
“Mimi pia nina mgonjwa wangu, mjomba wangu amelazwa hapa. Ndiyo nimetoka kumwangalia!” Akasema Vanessa.
“Pole sana, anaendeleaje sasa?”
“Ana nafuu kidogo, anaweza kuruhusiwa kesho kama siyo kesho kutwa.”
“Pole sana dada yangu!”
“Usijali, wewe ndiyo unatakiwa kupewa pole nyingi zaidi kutokana na matatizo uliyoyapata.”
“Nashukuru kwa wema wako.”
“Usijali...samahani, kuna jambo nataka kukuuliza...sijui utaniruhusu?”
“Uliza tu!”
“Kuna mtu anayekuja kukuangalia hapa hospitalini?”
“Unamaanisha nini?” Bruno akauliza angali macho yake ameyakaza usoni mwa Vanessa.
“Namaanisha mtu wa kukuletea huduma muhimu, mathalani chakula na mambo mengine!”
Lilikuwa swali baya kwa Bruno, swali lililotibua mambo yaliyojificha ndani ya moyo wake! Vanessa akashindwa kuelewa kwamba swali lile lilikuwa sawa na mwiba wa samaki ndani ya moyo wake!
Ghafla, macho ya Bruno yakalowana!
Mvua nyingine ya machozi ikaanza kumwagika machoni mwake, yakafunika kope zake...aliumia sana moyoni. Hakupenda kabisa lile swali.
Vanessa hakuyapenda machozi ya Bruno, kwa kumtizama tu, akafahamu kwamba, lazima alikuwa na kitu kingine kinachomwumiza zaidi. Bruno akazidi kulia, Vanessa akaketi kitandani kisha akatoa leso yake na kumfuta machozi.
“Samahani sana Bruno kama nimekukosea...” Vanessa akamwambia Bruno kwa sauti tulivu sana.
“Hapana dada, hakuna kitu!”
“Lakini umeanza kulia baada ya kukuliza kama kuna mtu anayekuja kukuangalia...samahani sana kama nimekukosea, siyo dhamira yangu!”
Bruno akazidi kulia.
“Nyamaza tafadhali, wewe ni mwanaume, hakuna tatizo kubwa kwa mwanaume, jikaze na utulize moyo wako.”
“Sawa, nimekuelewa...” Bruno akasema akijitajidi kunyamaza.
“Yaani Tunu?!!!” Hatimaye neno hilo likamtoka Bruno kinywani mwake.
“Tunu? Ndiyo nani?”
“Ni habari ndefu sana dada’ngu, siwezi kuzungumza kitu kwasasa, lakini fahamu hakuna mapenzi ya kweli duniani!” Bruno akamwambia Vanessa ambaye alionekana kushtuka sana.
“Hakuna mapenzi ya kweli, kivipi Bruno?”
“Fahamu tu, kwamba hakuna mapenzi ya kweli duniani!” Bruno akasema akianza kulia tena.
“Kwani hayo mapenzi yana uhusiano wowote na hii hali uliyonayo sasa?”
“Tena kwa asilimia mia moja!”
“Kivipi?”
“Siwezi kuongea chochote sasa hivi, sitaki kujiumiza zaidi ya hapa, nahitaji muda wa kupumzika zaidi, samahani kama nimekuudhi, lakini siku tukionana kwa majaliwa ya Mungu, nitakusimulia kisa kizima!”
“Sawa. Sasa unaweza kujibu swali langu?”
“Uliuliza nini vile?”
“Kama kuna mtu anayekuja kukuangalia na kukupa mahitaji yote ya muhimu?!”
“Kifupi hakuna!” Bruno akajibu baada ya kujikaza sana.
“Pole sana, kama hutajali, naomba kuanzia sasa nianze kukuangalia, sijui utaniruhusu?” Macho ya Vanessa yalikuwa ya huruma sana wakati akizungumza maneno hayo.
Bruno hakujibu!
Alibaki akimwangalia Vanessa.
“Tafadhali naomba unikubalie, usikatae Bruno nakuomba sana.”
Bado hakujibu!
Ghafla matone ya machozi yakaanza kumiminika tena machoni mwake. Ikawa machozi ni kitu cha kawaida kwa kijana huyu mtanashati. Kila kitu analia! Kila swali analoulizwa jibu lake ni machozi!
Machozi!
Machozi!
Machozi!
Vanessa akaogopa sana, akashindwa kuelewa ni kwanini kila anapomwambia kitu lazima alie! Akilini mwake kukajengeka kwamba lazima alikuwa na matatizo makubwa sana.
Ni kweli siku zote alikuwa mtu wa kusaidia watu, moyo wake ulikuwa wa huruma sana, hakupenda kumwona mtu akiwa katika hali ya shida na matatizo halafu amwache, kama anaweza kumsaidia alifanya hivyo.
Kwa kijana huyu aliyelala hoi kitandani, akionekana kukosa faraja kabisa, akionekana kukata tamaa ya maisha kabisa. Akionekana kupoteza hamu ya kuishi.
Aliyepoteza dira!
Ambaye havutii kwa chochote!
Hatamaniki kwa lolote!
Mlemavu!
Moyo wake ulikuwa na zaidi ya huruma, alishawishika kwa kiasi kikubwa sana kumsaidia, alishindwa kuelewa ni kwanini alijikuta akihisi hali hiyo, lakini moyo wake ulishaamua na alikuwa tayari kumsaidia kwa namna yoyote na kwa gharama yoyote.
“Tulia Bruno, lazima ujikubali kwanza jinsi ulivyo. Najua una mawazo mengi sana lakini unatakiwa kujitahidi uyaondoe, kwani hayatakusaidia kitu.
“Nahisi unavyoumia, naona unavyoteseka. Najua...nafahamu utakuwa na maumivu mengi sana kwa wakati mmoja. Nahisi unavyoungua na moto, lakini hayo yote ni sehemu ya maisha.
“Kumbuka matatizo hayakimbiwi Bruno, matatizo yanakabiliwa. Yanatatuliwa. Hayakimbiwi. Kwanza huwezi kuyakimbia. Utakimbia mpaka wapi? Utajificha wapi? Utalia mpaka lini? Nyamaza tafadhali...” sauti ya Vanessa ilikuwa ya kusihi kuliko kawaida.
Ilikuwa sawa na msumari wa moto ambao uliingia moyoni mwa Bruno kabla haujapoa vyema. Maumivu juu ya maumivu. Vanessa hakujua kinachomliza Bruno. Hakulia kwa sababu ya maumivu na mateso pekee.
Hakulia kwasababu sasa alishakuwa mlemavu. Alilia kwa sababu nyingine zaidi. Sababu kubwa kuliko kawaida, kubwa ingawa kwa mtu mwingine ingeweza kuonekana ndogo!
Mapenzi...
Hiyo ndiyo sababu kubwa iliyomfanya kila wakati awe analia. Akajuta kuyafahamu mapenzi, akajuta kumfahamu mpenzi wake aliyesababisha awe katika hali ile.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (2)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Sijui ni kwanini nilikutana na Tunu katika maisha yangu? Najuta kukutana na mwanamke yule, kwanza si mwanamke ni shetani, amekuwa maumivu katika maisha yangu. Mwiba na sumu kali ya kuulia mamba! Amepoteza dira yangu, amenipa machungu na mateso. Najuta...najuta kukutana naye...” Bruno anawaza akilini mwake, akiwa ameshasahau kabisa kwamba anazungumza na Vanessa.
“Bruno, naomba unijibu basi...” sauti hii tamu ndiyo iliyomnasua mawazoni.
“Unasema?”
“Mungu wangu! Sijui kwanini unaruhusu maumivu katika moyo wako? Unajua unaweza kujiona huna thamani tena, huna umuhimu tena au hakuna mtu ambaye ataona thamani yako, hayo yanaweza kuwa mawazo yako ya machoni, lakini ndani yako lazima ujitengenezee ushindi, ujijenge wewe mwenyewe kuwa ni mshindi na huna tatizo kubwa.
“Thamani hiyo ndogo ambayo unajipa sasa, wapo watu wengi sana ambao wanakuhitaji kwasababu wanakuona una thamani kubwa sana kwao. Acha kijipangia maisha, amini kila kitu kinawezekana, mimi mwenyewe naamini bado hujashindwa. Wewe ni mshindi Bruno.
“Tafadhali futa machozi yako na kila fikra mbaya iliyopo kichwani mwako. Tatizo ulilonalo halimaanishi kuwa mwisho wa maisha yako umefika. Bado una nafasi kubwa sana Bruno,” yalikuwa maneno makali sana yaliyotoka kinywani mwa Vanessa kwa sauti laini sana ya kusihi.
Bruno akamwangalia Vanessa kwa macho ya huruma, alikuwa mtu pekee aliyempa faraja baada ya kuikosa kwa muda mrefu sana. Alianza kuiona thamani yake ikirejea taratibu, alianza kuona utu wake.
“Nashukuru sana Vanessa dada yangu, wewe ni mwanamke wa aina yake, unanifanya nianze kuwa na furaha sasa, ahsante sana,” Bruno akasema.
“Usijali Bruno, napenda kuona furaha yako na siyo machozi.”
“Ahsante, nashukuru kusikia hivyo.”
“Naamini sasa umenikubalia kwa moyo mmoja, usiwe na mashaka na jambo hili tafadhali.”
“Usijali, nipo tayari. Sijui nikushukuru vipi, lakini Mungu wangu wa Mbinguni ndiye anajua shukrani iliyopo moyoni mwangu. Ahsante sana Vanessa.”
“Nimefurahi kusikia hivyo, mimi naenda kwenye mihangaiko yangu, jioni nitakuja kukuona tena, kuwa huru sasa, sawa?”
“Sawa.”
“Samahani naweza kuchukua namba zako za simu?” Vanessa akamwuliza.
“Sina.”
“Ok, baadaye. Ugua pole.”
“Ahsante.”
Vanessa akaondoka.
***
Kama Vanessa alivyoahidi, jioni alikwenda tena hospitalini kumuona Bruno. Alimpelekea chakula kizuri sana, ndizi nyama pamoja na matunda. Akamlisha kwa upendo huku akimtania.
Bruno anatabasamu!
Anacheka!
Muda mfupi kabla hajaondoka, Vanessa anatoa simu kwenye pochi na kumkabidhi Bruno.
“Ya nini?”
“Yako Bruno, ukiwa na tatizo lolote nifahamishe. Tayari nimeshakuwekea vocha na nimeshaingiza jina langu, so tuwasiliane wakati wowote ukiwa na dharura sawa?”
“Ahsante sana Vanessa, lakini kwanini unanifanyia mambo yote haya?”
“Sisi wote ni binadamu na tunaishi katika sayari moja Bruno, lazima tupendane. Hilo tu, hakuna kingine!”
“Nimefurahi sana kusikia hivyo. Nakushukuru sana.”
“Usijali. Mi nakwenda, nitakuja kukuona tena asubuhi.”
“Ahsante, usiku mwema.”
“Nawe pia...usitegee kunywa dawa Bruno.”
“Kwa hilo usijali, nakuahidi.”
Wakaagana.
***
SAA 3:00 za usiku, Vanessa alikuwa anapiga honi getini kwake, lakini msichana wake wa kazi hakutoka kumfungulia. Kwa dakika tatu nzima aliendelea kufanya hivyo bila mafanikio.
Akiwa ndiyo kwanza amefungua mlango akitaka kushuka ili akafungue geti mwenyewe, geti likafunguka. Akaingiza gari huku akifoka. Akaegesha.
Wakati anamalizia kushusha mguu wa pili kutoka kwenye gari, akiendelea kufoka, akakutana na kibao cha nguvu shavuni mwake. Kilikuwa kibao kizito alichohisi maumivu makali sana. Hakupata shida kugundua kwamba kilikuwa kibao cha mwanaume.
Lilikuwa kofi moja tu, la nguvu lililompotezea mwelekeo. Akiwa anatafakari namna ya kukabiliana na aliyempiga ambaye bado hajamuona, akakutana na kibao kingine!
Akaanguka chini!
Akagaagaa chini akiwa haelewi kinachoendelea, moyo wake ulishabadilisha mapigo na kwenda kasi kuliko kawaida. Akayatoa amcho yake kumwangalia aliyekuwa akipambana naye.
Haikuwa rahisi kuamini!
Alikuwa ni Emma!
Emmanuel!
“Emma?! Ni wewe mpenzi wangu? Kwanini unanipiga?”
“Nyamaza!” Emma akasema kwa ukali.
“Kwanini unanipiga?” Vanessa akasema akizidisha kilio.
Hakuona kosa la kupigwa na mpenzi wake, kila alipojaribu kuvuta picha kama kuna mahali alikuwa amemkosea, hakuona.
“Amka uende ndani haraka sana,” Emma akamuamrisha.
Vanessa akajizoa-zoa pale chini na kuamka, akaanza kupiga hatua za kivivu, akiwa ameshika shavu lake moja akiugulia maumivu makali. Akaenda moja kwa moja hadi chumbani kwake. Akajitupa kitandani. Muda mfupi baadaye, Emma akaingia akiwa anakazana sana.
“Umeanza umalaya siyo?” Emma akauliza kwa sauti iliyojaa ukali.
Ni swali lililomshutua sana Vanessa, akabaki kimya kwa muda akitafakari. Alihisi huenda alimfuatilia hospitalini na kumuona akiwa na Bruno. Hata kama alimuona, alikuwa na uhakika gani kwamba Bruno ni mpenzi wake? Hata hivyo Bruno si mpenzi wake.
“Sasa kwanini ananiuliza swali hilo?” Akawaza kichwani mwake.
“Si naongea na wewe?” Emma akasema, akionesha kujiandaa kumwangushia konde lingine.
“Mbona unanifanyia hivi lakini? Majina gani hayo unayoniita? Na kwanini unasema mimi ni malaya?”
“Ulikuwa wapi?” Emma akauliza tena.
“Mara ya mwisho kuongea na wewe kwenye simu nilikwambia naekea wapi?”
“Sitaki kujua mambo ya mara ya mwisho, nakuuliza sasa hivi umetokea wapi?”
“Hospitalini kumwona Anko!”
“Kumwona Anko siyo?”
“Ndiyo!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo!”
“Kwanini nakupigia simu hupokei?”
“Umenipigia saa ngapi jamani?”
“Hebu toa simu yako.”
Vanessa akatoa simu yake kwenye pochi, hakuamini alipokutana na missed calls 12 zote za mpenzi wake Emma.
“Mungu wangu sikuona calls zako Emma. Lakini ndiyo sababu iliyokufanya unipige kiasi hiki?”
“Umeona ni sababu ndogo siyo?”
“Sijasema ndogo, lakini action uliyochukua ndiyo kubwa kuliko tukio lenyewe.”
“Sasa niambie kwanini hukupokea simu?”
“Sikuona Emma, unajua nilipokuwa naingia hospitalini, niliweka simu silence ili nisisumbue wagonjwa, nilipotoka sikukumbuka tena kuirudisha kawaida.”
“Nakuambia kwa mara ya mwisho...sitaki kuona napiga simu zaidi ya mara mbili hupokei...nitakuja kukuvunja taya siku moja...” Emma alisema kwa sauti kisha akabamiza mlango na kuondoka.
Vanessa akabaki analia peke yake. Vituko vya Emma vilikuwa vimeshamchosha kwa kiasi kikubwa. Kila wakati alikuwa akimpiga, kosa dogo tu, ilikuwa lazima apigwe. Kilichomuuma zaidi ni kwamba, Emma alikuwa akimfanyia vurugu nyumbani kwake, ambapo analipia kodi mwenyewe.
Hakufurahia kabisa mapenzi na kijana huyu ambaye ni mkorofi kupindukia, ingawa moyoni mwake alishindwa kuelewa ni kwanini alikuwa akimpenda kwa kiasi hicho. Emma ni mwanaume ambaye alimwingia moyoni na kumchanganya sana moyo wake.
“Lakini lazima siku moja nifanye maamuzi, lazima nifanye kitu, siwezi kuwa katika penzi la kitumwa kwa muda wote huu. Mwanaume anafanya vituko vya kila aina. Hana mapenzi ya dhati, mkorofi, ananipiga, kwanini niendelee kumsumbukia mwanaume wa aina hii? Lazima nikubali kujitoa mikononi mwake, lazima...” Vanessa akawaza hayo kichwani mwake kisha akaamka haraka.
Akavua nguo zote na kujifunga taulo kifuani, akawa tayari kuingia bafuni, lakini ghafla akasita. Akarudi tena chumbani, akapiga hatua za taratibu kuelekea kwenye dressing table yake.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (3)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Akaiachia ile taulo yake, ikaanguka chini. Akayakazia macho yake katika umbo la mtu yule aliyekuwa kwenye kioo. Msichana huyo mrembo ambaye alikuwa na sifa zote. Aliyaacha macho yake kwa muda katika nywele zile zilizotengezwa na mtu ambaye anajua vyema kazi yake. Akarudi kutazama zile nyusi zilizochongwa vyema.
Akakaza macho yake katika macho ya kulegea ya mrembo yule, akamtamani. Alikuwa mwanamke mzuri sana. Akayashusha macho yake hadi kwenye matiti yaliyosimama wima ya mrembo huyo. Akashuka chini hadi kwenye kitovu kilichozungukwa na garden love iliyochanua vyema.
Hakuchoka, akatazama kiuno chake, akachanganyikiwa. Kiuno kile kilikuwa kimebebwa na hips pana za kutosha ambazo zilizidisha urembo wa mwanamke yule.
Akatabasamu!
Alikuwa mwanamke mzuri sana kwa kutazama, hakustahili kupigwa wala kunyanyaswa. Alikuwa mwanamke ambaye alitakiwa kutuzwa kwa kila hali, siyo kupigwa! Alitakiwa kubembelezwa kwa kila namna.
Mwanamke huyo ni Vanessa!
Yeye mwenyewe!
“Sitakiwi kunyanyaswa!” Akawaza kisha akachukua taulo lake chini na kuingia bafuni.
Akafungua bomba la mvua, akaanza kuoga!
***
“Tulia hivyo hivyo!” Tunu akamwambia Bruno ambaye alikuwa amelala kitandani chali, akiwa mtupu kabisa.
“Sawa mama, kwani mimi nina neno?!”
“Fuata masharti yangu, nataka kukuonesha kwanini naitwa Tunu mtoto wa Kitanga. Mimi nimefundwa kwetu Uziguani...” Tunu akasema kwa sauti laini, huku akiendelea kumpaka Bruno mafuta mwili mzima.
Raha aliyokuwa akiisikia ilikuwa siyo ya kitoto, kwani Tunu alikuwa akimpaka kwa staili ya kupapasa au kama ambaye alikuwa anatafuta kitu alichopoteza.
Alijihisi kama yupo katika kisiwa kizuri chenye burudani ya aina yake. Macho ya Tunu yalikuwa yanamchanganya sana Bruno aliyekuwa ametulia kitandani, huku miguno ya kimahaba ikisikika.
“Nakupenda sana Bruno wangu, nakupenda sana....”
“Nakupenda pia Tunu,” Bruno akasema akitabasamu...
***
“Nooooooooo....” Bruno akapiga kelele akiwa kitandani hospitalini.
Alishtuka kutoka katika ndoto ambayo hakupenda kuikumbuka kabisa. Tunu alikuwa mwanamke mbaya sana kwake. Huyo ndiyo sababu ya yeye kuwa hospitalini muda huu.
Kitandani!
Akiwa amekatwa mguu wake, kwa maneno mengine alikuwa ameshapata kilema cha maisha! Sababu kubwa ni Tunu. Machozi yakaanza kushuka machoni mwake.
***
Ni kama alikuwa anagopa kuharibu marumaru iliyokuwa chini wakati akitembea, alikuwa akitembea kwa mnyato, kama anaogopa kuumia miguu yake. Hata hivyo, si kama alijifanyisha, hiyo ilikuwa tembea yake. Anapiga hatua za taratibu, huku taulo ikiwa kifuani mwake.
Anafunga mlango wa bafuni na kuingia chumbani kwake, anajitupa kitandani, anahema kwa kasi kisha anasimama tena. Akabaki akiwa amesimama akiwa hajui ni kwanini alifanya hivyo.
“Nilikuwa nataka kufanya nini? Lazima kuna kitu kilinisababisha nisimame, ni nini?” Akawaza Vanessa akiwa hana jibu.
“Oh! Yeah, nimekumbuka!” Akasema kwa sauti akisogelea meza yake ya kujipambia.
Akaketi kwenye kiti kilichokuwa mbele yake. Akayatupa macho yake kwenye kioo na kumtulizia macho msichana yule mrembo ndani ya kioo. Ilikuwa ni taswira ya sura yake mwenyewe. Akaachia tabasamu la kivivu akiashiria kwamba anaukubali uzuri wa mwanamke yule mrembo aliyepo mbele yake.
Anajikubali.
“Mimi ni mrembo, sifa unajipa mwenyewe...” akawaza akitabasamu.
Siku zote usiku, huwa hana kazi kubwa sana kwenye dressing table yake, akachukua kofia yake yake ya plastiki na kuivaa kichwani. Akajipuliza na manukato mepesi kisha akatoka.
Hatua ya kwanza, hatua ya pili hadi sebuleni, akaketi kwenye sofa kubwa akitazama runinga. Pembeni yake alikuwa amekaa msichana wake wa kazi Amina.
“Shikamoo dada...” Amina akamsalimia.
“Marhaba...”
“Pole na kazi!”
“Ahsante. Nina maswali kidogo nataka kukuuliza.”
“Uliza tu dada.”
“Mimi ni nani kwako?”
“Bosi wangu!”
“Ukiachana na huo ubosi, ni nani kwako?”
“Dada.”
“Unamaanisha unachokisema Amina?”
“Ndiyo dada.”
“Hivi, unafahamu ni kwanini upo hapa?”
“Ndiyo!”
“Enheee...”
“Kwa ajili ya kufanya kazi za hapa nyumbani!”
“Unazijua vizuri?”
“Ndiyo dada!”
“Unaweza kunitajia?”
“Ndiyo, kusimamia mambo yote yanayohusu usafi, kupika na kazi nyingine ndogo ndogo.”
“Ok! Sasa kwanini wakati napiga honi getini hukutoka kunifungulia?”
“Shem Emma aliniambia nisitoke!”
“Unasemaje wewe? Hivi una akili kweli? Hii ni nyumba ya Emma au yangu? Emma ulimkuta hapa au alikukuta na ni mimi ndiye niliyekutambulisha kwake?”
“Alinikuta dada, lakini kutokana na wewe kunitambulisha kwake kama shemeji yangu, sikuona vyema kubishana naye, maana najua ni mchumba wako.”
“Sasa Emma amenipiga hapo nje, yote hayo ni kwasababu yako. Sasa natoa agizo, kuanzia leo unatakiwa kunisikiliza mimi kwa kila kitu, fuata kila ninachotaka na siyo Emma, umenielewa?”
“Ndiyo dada!”
Vanessa akainuka akiwa amefura, akaenda kwenye chumba cha chakula, akaanza kula. Hakuwa na raha ya kukaa sebuleni muda mrefu sana, akaingia zake chumbani kulala.
***
Usiku mzima aliishia kujigeuza-geuza kutoka upande mmoja wa kitanda kwenda mwingine, hakupata usingizi kabisa. Bruno alitawaliwa na maumivu makali sana, si maumivu ya jeraha la mguu, yalikuwa maumivu makali ya moyo.
Alikuwa akiumizwa na jinsi alivyotendwa na Tunu, mwanamke huyo ndiye chachu ya matatizo yote aliyonayo sasa hivi, ndiyo sababu ya yeye kuwa amelazwa. Kwanini ampende? Kwanini amuone mwema? Hakuwa mwanamke mwenye thamani kabisa, kwake alikuwa sawa na mbwa koko, ambaye hana maana yoyote, zaidi ya kufakamia vyakula jalalani!
Kumbukumbu za Tunu zilimsumbua sana. Asubuhi hii ndiyo anaanza kupata usingizi, baada ya kuteseka usiku mzima.
***
Honi mfululizo zilikuwa zikipigwa nyuma ya gari la Vanessa kwenye eneo la mataa ya Morocco, kwenye makutano ya Barabara ya Ali Hassan Mwinyi na Kawawa, hiyo ikiwa ni baadada ya taa ya kijani kuwaka, kuruhusu magari yanayotokea Msasani kuingia barabara inayelekea Posta.
Si kwamba, Vanessa hakuona ile taa, aliona vizuri sana, lakini muda wote tangu alipotoka nyumbani, alikuwa hajawa na uamuzi wa moja kwa moja kwamba aanzie ofisini kwake Posta ndipo aende Hospitalini au aende kwanza Hospitalini kisha aende ofisini. Akiwa yupo kwenye foleni na taa kuruhusu, alikuwa hajapata uamuzi wa moja kwa moja.
Akasita kwenye foleni.
“Niende wapi?” Akawaza kichwani mwake, lakini baadaye akapata jibu.
“Acha nianzie kwanza Hospitalini,” akajisemea mwenyewe, akiwa hana habari na zile honi.
Aliendelea kusubiri kwa muda mpaka taa ziliporuhusu kunyoosha moja kwa moja kufuata Barabara ya Kawawa. Akaondoa gari kwa kasi. Ndani ya robo saa tu, alikuwa anaegesha gari lake, ndani ya Hospitali ya Amana. Akaenda hadi wodini na kuingia.
Alipopita kwenye kitanda cha Bruno, akamuona akiwa amelala. Akasimama kwa muda akimtazama, akazidi kumuonea huruma. Akakata shauri kwamba aanzie kwanza kwa mjomba wake, ndipo arudi kumtazama tena Bruno.
Wazo hilo lilipita bila kipingamizi akilini mwake.
Akaenda kumuona mjomba wake, kwa bahati nzuri sana, ilikuwa ndiyo siku aliyoruhusiwa. Baada ya taratibu zote kukamilika, akamshika mkono, akimsaidia kutembea kuelekea nje. Kabla hawajaufikia mlango mkubwa, Vanessa akamwomba mjomba wake, amtambulishe kwa rafiki yake wa karibu.
“Ni nani?”
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (4)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Yule aliyelala pale!”
“Sawa.”
Walipofika, Vanessa akaanza kumuamsha Bruno aliyekuwa anaogelea katika usingizi mzito. Aliposhtuka, akakutanisha macho yake uso kwa uso na mjomba wake na Vanessa.
“What? Bryson?” (Nini? Bryson?) Bruno akapayuka.
“Bruno?” Mjomba wake Vanessa naye akamwita Bruno akionekana kushangaa sana.
“Bado unaendelea kunifuata? Hujaridhika tu? Unataka kuchukua na roho yangu kabisa?” Bruno akamwuliza, Vanessa akiwa kimya huku akichanganyikiwa kichwani mwake.
“....hivi, mnafahamiana?” Vanessa akawauliza.
Hakuna aliyejibu.
Pamoja na kwamba alikuwa katika hali ya kuugua, lakini Bruno alionekana kupata nguvu za ghafla. Alikuwa amefura sana pale kitandani akimwangalia Bryson kwa hasira isiyo ya kawaida. Vanessa yupo kimya akiwatazama kwa macho ya kuhoji. Anapatwa na maswali mengi sana kichwani. Mjomba wake anafahamiana na Bruno? Lilikuwa swali gumu sana. Hata hivyo halikuwa na ugumu mkubwa au mshangao wa ajabu. Kufahamiana ni jambo la kawaida sana, lakini alishangazwa sana na namna ya kufahamiana kwa watu hawa wawili!
Wanatishana!
Wanafahamiana kwa shari! Vipi mjomba wake awe mkorofi? Sawa, inawezekana akawa mkorofi, lakini si kwa kijana huyu mwenye macho yanasoma huzuni na simanzi tele machoni mwake.
“Wana nini hawa?” Akawaza kichwani akiwa hana amani kabisa.
Macho ya Vanessa yakaanza kuwaangalia watu hawa wawili ambao wamekaziana macho.
“Hivi mna nini nyie? Anko unamfahamu Bruno?”
Mjomba wake hakujibu.
“Bruno, kuna nini kati yako na mjomba?” Vanessa akauliza akiwa anawashangaa kwa jinsi tafrani ilivyokuwa kubwa.
“Huyu ndiyo mjomba wako?” Bruno akauliza badala ya kujibu.
“Yeah! He is my uncle.” (Ndiyo! Ni mjomba wangu.)
“Your uncle?” (mjomba’ko?)
“Yes!” (Ndiyo!)
“Ok! Sikiliza Vanessa, pamoja na misaada ambayo umekuwa ukinisaidia, naomba leo nikukosee heshima, huyu ni mjomba mpumbavu, tena hana maana yoyote kabisa. Huyu ni mpumbavu. Muuaji. Hafai. Kama utaona inafaa, sitisha misaada yako kwangu kuanzia leo,” Bruno akasema kwa hasira sana akionekana kutaka kuamka kitandani!
Haikuwezekana!
Alikuwa mgonjwa!
Mlemavu!
Hana ujanja wowote wa kuamka na kufanya kitu chochote. Anamwangalia Vanessa kwa macho yaliyoonesha kwamba yupo tayari kwa lolote na hajali kitu chochote. Baadaye akayarudisha macho yake tena kwa Bryson ambaye alionekana kuwa na hasira zaidi hata ya Bruno, lakini naye alikuwa na tatizo lile lile.
Hana nguvu!
Angali anaumwa!
“Kuna tatizo gani kati yenu?”
Hakuna aliyejibu.
“Mmedhulumiana?”
Kimya!
“Mbona nawauliza, halafu mpo kimya? Mna nini lakini mbona mnanichanganya sasa?” Vanessa akasema, lakini hakuna aliyezungumza chochote.
“Kwasababu hakuna anayetaka kuzugumza neno, Anko twende nyumbani, haya mambo nitazungumza na Bruno baadaye.”
Wote kimya!
Vanessa akamshika mkono mjomba wake na kuanza kuondoka hadi nje walipoingia kwenye gari na kuondoka. Njia nzima Vanessa alikuwa na mawazo, lakini katu hakuzungumza kitu na mjomba wake.
***
Bruno akayatoa macho yake kwa mshangao, akimwangalia mwanauume huyu anayeonekana kujazia vyema kifuani mwake. Hakuwa na sababu ya kutaka kuuliza mahali popote kama huyu bwana anafanya mazoezi. Yupo peke yake, akiwa amevalia suruali ya jeans ya rangi ya blue na fulana nyeupe ya kukata mikono.
Sura yake inatangaza vita!
Anaonekana dhahiri kudhamiria kuua mtu! Bruno akiwa bado yupo katika taharuki, anashangaa Tunu anapiga magoti kwa mwanaume huyu akilia na kuomba asamehewe! Woga wake haujifichi, analia na kumwangalia kwa huruma.
“Samahani mume wangu, naomba unisamehe, sikufanya kwa makusudi mpenzi, ni bahati mbaya. Naomba msamaha wako baby,” Tunu anazungumza kwa sauti ya kusihi mbele ya mwanaume huyu mwenye miraba minne!
“Tunu my wife? Why? Why? Why Tunu? Kwanini umenifanyia hivi?” Mwanaume huyo akazidi kulalamika akionekana kuwa na hasira kuliko kawaida.
“Please forgive me my husband, nisamehe mpenzi wangu tafadhali, usinitende hivyo, najua una hasira na unaweza kuniua, lakini nisamehe.”
“Nikusamehe?”
“Ndiyo?”
“Kwa usaliti huu?”
“Nisamehe baby!”
“Ndani ya nyumba yangu?”
“Bryson sweetie nisamehe.”
“Kitandani kwangu?”
“Najua ndiyo maana naomba msamaha. Najua kiasi kiasi gani una maumivu, nisamehe tafadhali mpenzi wangu.”
“No! No! No! I can’t, lazima nifanye kitu kama fundisho.”
“Hapana baby!”
Bryson hakutaka kusikiliza maneno ya Tunu, akachomoa bastola aliyokuwa ameichimbia kibindoni. Akaielekeza usoni mwa Tunu.
“Naanza na wewe, halafu namuua na huyo mshenzi mwenzako, huwezi kunisaliti Tunu, huwezi...” Bryson akasema akionekana kukasirika sana.
Muda wote Bruno alikuwa kama amenaswa na shoti ya umeme, lakini alipoona bastola, akachanganyikiwa. Mawazo yake ya mwanzoni kwamba, mambo yangeweza kuisha kwa kuzungumza na kumalizana kiume, yakatoweka kabisa, pale kifo kilikuwa kinanukia wazi wazi!
Lakini katika maajabu yote, hili lilikuwa la kwanza, kwasababu kwa kipindi chote cha miezi sita alichokuwa katika uhusiano wa kimapenzi na Tunu, hakuwahi kumwambia kwamba ana mume. Imekuwaje leo anapiga magoti mbele ya mwanaume huyu akisema ni mumewe?
Akamwangalia Tunu kwa mshangao, kisha akayarudisha macho yake kwa Bryson ambaye alionekana dhahiri kudhamiria kuua. Macho yake yalikuwa yanasoma huruma na kuomba msamaha!
“Tunu, si ulisema hujaolewa?” Bruno akauliza kwa uchungu sana huku woga ukiwa umemshika.
“Nyamaza Bruno, kikubwa hapa ni kuomba msamaha, kama ni kosa limeshatokea.”
“Pumbavuuuuuu...mnashauriana ujinga gani hapo? Kwanza inabidi nianze na wewe fala kwanza, kabla ya Tunu. Haya Sali sala zako za mwisho kabla ya kifo chako. Haraka...” Bryson akasema akionekana kutaka kuachia risasi...
***
“BRYSON, BRYSON, BRYSON.....Noooooooooo....” Bruno akajikuta akipiga kelele wodini, wazo la kwamba alikuwa wodini, lilishaondoka.
Mawazo yake yote yapo kwa Bryson, ambaye kwake ni kama sumu ya nyoka ukiwa porini bila dawa ya kuulia sumu hiyo. Ghafla akamwona mtu ambaye hakutarajia kumuona mbele yake. Alikuwa ni Vanessa.
“Umefuata nini?” Bruno akauliza kwa hasira.
“Nimefuata nini?”
“Ndiyo, umefuata nini hapa? Sitaki msaada wowote kutoka kwako!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Hebu niangalie machoni Bruno!”
Bruno akamwangalia.
“Haya sasa sema hutaki msaada wowote kutoka kwangu!”
Bruno hakuweza, kilichofuata ikawa ni machoni mwake. Alionekana kuwa na maumivu makali sana moyoni mwake.
Macho yake yalitangaza dhiki, sura yake ikaonesha huzuni na kinywa chake kikizidisha machungu kwa Vanessa aliyekuwa amesimama mbele yake. Kwa kumtizama tu Bruno, Vanessa aliweza kugundua kwamba, tayari Bruno alikuwa mbali sana kihisia, kwamba anaweza kufanya kitu tofauti kama hatapatiwa msaada wa ushauri kwa haraka!
Mara moja akaketi kitandani, akajivuta juu ya kitanda na kumuinua kidogo Bruno, kisha akamlaza miguuni mwake. Akayaacha macho yake yaoneshe nia yake ya kumuweka miguuni mwake.
Bruno akazidi kushangazwa na wema wa mwanamke huyu mzuri, mwenye sifa zote za kuwa mrembo! Kwa jinsi alivyokuwa amependeza asubuhi hiyo, kwa hakika hakustahili kabisa kukaa katika kitanda kile cha mgonjwa, ambacho si ajabu kulikuwa na unyevunyevu kutokana na Bruno kulala muda mrefu.
Lakini amekaa!
Amemlaza miguuni mwake akitabasamu!
Hana kinyaa!
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (5)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Ni mwanamke wa aina gani? Si kwamba ni vigumu mambo haya kufanyika, lakini kuwe na uhusiano mwema basi baina ya watu hawa wawili! Lakini ndiyo kwanza wanafahamiana, tena hapo hapo hospitalini! Lakini kubwa zaidi, ni kwamba, tayari Bruno anaonekana kuwa na tofuati na mjomba wake Vanessa, tofauti ambayo bado Vanessa hajaijua!
Anawezaje?
Bruno akamwangalia kwa jicho la kuhitaji huruma yake, ambaye naye alijibu kwa jicho la kupokea huruma hiyo. Kama ndoto ya mchana, tabasamu changa likachanua usoni mwa Bruno, Vanessa akajibu!
Kama ungefanikiwa kuwaona, usingekuwa na mashaka kwamba wale walikuwa wapenzi. Haikuwa hivyo! Walikuwa marafiki tu, tena wasio na umri mrefu. Hata mwezi hawana. Tena wana ugomvi uliosababishwa na mjomba wake Vanessa.
“Bruno...” hatimaye Vanessa akaita.
“Vanessa!” Bruno akaitikia kivivu akionesha kudeka kidogo.
“Kwanini una mawazo sana?”
“Matatizo Vanessa, matatizo.”
“Lakini siku zote, matatizo huwa hayakimbiwi Bruno, ni kuyakabili tu. Kwanini unakuwa mwoga wa kukabiliana na matatizo?”
“Siyo woga!”
“Bali nini?”
“Lazima uwe na hofu na jambo ambalo hujui mwisho wake Vanessa.”
“Najua Bruno, lakini si kwa kiwango ambacho wewe unayachukulia matatizo yako.”
“Kwanini unasema hivyo?”
“Mambo mengi sana, unayachukulia kwa ukubwa. Kama unakumbuka, siku ya kwanza kukutana na wewe nilikuambia najua unadhani huna thamani tena kutokana na tatizo lako.
“Unajiona huwezi kuwa na marafiki tena, huwezi kupata mtu wa kukujali, huwezi kukubalika, huwezi kupendwa. Huwezi kuwa na sauti na kadhalika lakini nataka kukuambia kwamba unawaza tofauti sana, kila kitu kinawezekana na unaweza kuondoa fikra hizo kichwani mwako ukawa Bruno mpya kabisa...” sauti ya Vanessa ilikuwa tulivu, ambayo aliitoa kwa mpangilio unaofaa.
“Ahsante sana Vanessa kwa kunipa moyo, kuanzia sasa naanza kuwaza upya.”
“Nimefurahi sana kusikia hivyo. Ok! Vipi hali yako sasa?”
“Dokta amepita round, ameniruhusu!”
“Hongera, nyumbani ni wapi?”
“Sina.”
“Huna mahali pa kukaa?”
“Ndiyo Vanessa.”
“Kwanini?”
“Sina nyumba hapa Dar.”
“Ndugu?”
“Sina!”
“Anyway, mambo mengine tutazungumza baadaye, lakini kwasasa hebu tumalize kwanza hili suala la makazi. Naomba nikusaidie kwa mara nyingine Bruno.”
“Nitashukuru sana.”
“Nitakutafutia sehemu ya kuishi kwa muda, ukipata huduma zote, halafu baadaye nitajua cha kufanya.”
“Sawa.”
“Nimefurahi sana Bruno, sasa amka upate mtori kwanza, halafu nitakuacha kwa muda ukiendelea kukamilisha taratibu za discharge ili nikaandae mazingira then nije nikuchukue.”
“Sawa.”
Bruno akainuka na kukaa kitako. Vanessa akamimina mtori na kuanza kumnywesha. Taratibu Bruno akawa anakunywa mpaka akashiba kabisa! Akamenya machungwa mawili na kumpa, akala na kumaliza.
“Good! Ukiwa na bidii ya kula hivi, uta-recover mapema zaidi.”
“Usijali Vanessa, kwenye kula wala usiwe na wasiwasi, mimi ni mkali sana kwenye eneo hilo!”
Wakacheka pamoja!
“Acha basi mi’ niondoke, ndani ya saa moja nitakuwa nimesharudi, halafu tutaondoka.”
“Sawa.”
Vanessa akatoka wodini na kwenda alipoegesha gari lake, akaingia na kuwasha. Safari yake iliishia Manzese Tip Top, alipotafuta hoteli nzuri na kupanga.
“Hiki chumba ni kwa ajili ya ndugu yangu, mgonjwa. Nahitaji apate huduma zote akiwa hapa, nitakuwa nakuja kumwangalia kila siku, lakini ningependa kama angekuwa anapewa uangalizi wa karibu zaidi,” Vanessa akamwambia dada aliyekuwa mapokezi.
“Kama vipi yaani!”
“Huduma muhimu, chakula, kufuliwa nguo n.k.”
“Hilo halina tabu, kama utanitoa itakuwa poa!”
“Kuhusu hilo, weka shaka pembeni, utafurahi. Sasa vipi ukiwa haupo?”
“Nitaacha maagizo kwa nitakayemuacha, naye nitamkatia chake mapema, kwahiyo atakuwa anafanya kama mimi, kifupi usiwe na shaka, atakuwa salama!”
“Nimefurahi sana kusikia hivyo, acha nikamchukue!”
“Ok!”
Vanessa akaondoka zake.
***
Vanessa alimkuta Bruno akiwa ameshakamilisha taratibu zote na alikuwa akimsubiri yeye! Bruno akampokea kwa tabasamu changa, lakini Vanessa akajibu kwa tabasamu lililochanua. Akamshika mkono, kisha Bruno kwa msaada wa gongo, akaanza kupiga hatua fupi fupi kuelekea gari lilipoegeshwa.
Vanessa alikuwa ameshika gongo moja na kumuachia Bruno moja, wakatembea taratibu sana. Watu waliowaona, waliweza kugundua upendo wa ndani kwa ndani walionao wawili hawa! Taratibu wanakwenda mpaka kwenye gari!
Vanessa akampandisha na kuyaweka magongo yake siti ya nyuma, akawasha gari na kulitoa getini taratibu. Alipofika barabarani, akakata kushoto akiifuata barabara inayokwenda kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.
Kwenye mataa ya Barabara ya Kawawa, akakata kushoto kuelekea Magomeni, alipofika kwenye mataa ya Usalama, akapinda kushoto, kuishika Barabara ya Morogoro hadi Tip Top, ambapo aliingia kushoto kwenye kituo kidogo cha daladala, akaifuata Barabara ya Kione.
Hapo akakatiza mitaa miwili mitatu na kuegesha gari lake nje ya hoteli. Akamsaidia Bruno kushuka na kutembea naye pole pole hadi Mapokezi.
“Huyu ndiyo yule mgeni wangu.”
“Ok! Karibuni sana. Ni ghorofa ya nne, chumba namba 502. Ngoja nikusaidie tumpelekea mgonjwa!” Yule dada wa Mapokezi akajibu akitabasamu.
Akatoka na kusimama kushoto mwa Bruno, Vanessa akasimama kulia, kisha wakakutanisha mikono yao, Bruno akakaa katikati, wakapandisha ngazi hadi ghorofa ya nne!
Wakaingia chumbani na kumkalisha kitandani, yule dada wa Mapokezi akarudi zake ofisini kwake, chumbani wakabaki Bruno na Vanessa. Vanessa akiwa amechoka kabisa, Bruno akiwa ametulia kitandani akimwangalia Vanessa.
“Lakini kwanini unafanya yote haya Vanessa?” Bruno akauliza kwa utulivu sana.
Lilikuwa swali muafaka kwa Vanessa lakini gumu kujibika! Ni kweli alikuwa na sababu ya kufanya yote yale kwa Bruno. Mwanzoni hakujua, lakini tayari ameshajua, kwamba anafanya yote kwa sababu ndani yake kulikuwa na mzigo mzito wa mapenzi!
Hilo alilijua!
Ndiyo ukweli wenyewe!
Lakini atasemaje?
Akabaki anamwangalia bila kujibu neno, ingawa kwa mbali, macho yake yalikuwa yanatoa majibu. Majibu mazito. Kwamba anampenda, lakini domozege!
Hisia za moyo wake zilishamhakikishia kwa asilimia mia moja kwamba, anampenda sana mwanaume huyu. Mwanaume huyu ambaye yupo mbele yake akisubiri jibu la swali alilomwuliza; kwanini anamfanyia wema wote ule?
Alitakiwa kutoa jibu moja jepesi sana....kwamba anafanya yote yale kwasababu ndani yake kuna mapenzi ya dhati, lakini Vanessa hawezi na amejikuta akishindwa kabisa kutoa jibu la swali hilo lililomchanganya kidogo.
Bado Bruno ameyatuliza macho yake usoni mwa Vanessa na alichokuwa anasubiri ni jibu tu!
“Niambie basi,” Bruno akaomba.
“Kwanini umeniuliza hivyo Bruno?”
“Sina nia mbaya, nataka kujua tu!”
“Kila kitu kina sababu Bruno, najua hata wewe una sababu za kuuliza hilo, hebu niambie ni nini?”
“Umenifanyia mambo makubwa sana, umekuwa muungwana mno kwangu, lazima nihisi huenda kuna sababu.”
“Kama ipi Bruno?”
“Sijui.”
“Bruno.”
“Nakusikia Vanessa.”
“Hakuna sababu kubwa sana, lakini lazima utambue kwamba wewe ni binadamu mwenzangu, moyo una nyama Bruno...hivyo nilivyokuona upo katika mateso, sikupenda, nikaona ni vyema kukusaida. Sidhani kama kuna sababu kubwa zaidi ya hiyo...” Vanessa akasema akionekana wazi kabisa kuacha sababu nyingine ya msingi zaidi nyuma ya maneno yale.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (6)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Kama ndivyo nashukuru, lakini nina swali nataka kukuuliza.”
“Uliza tu.”
“Uliona tafrani kidogo kati yangu na mjomba wako?”
“Ndiyo!”
“Unahisi kuna nini kati yetu?”
“Sijui!”
“Alipata kukuambia chochote?”
“Hapana.”
“Najua hawezi kukuambia!”
“Kwanini?”
“Tuachane na hayo, lakini hujachukia au kukwazwa na jinsi ambavyo hatuna maelewano, ingawa hujajua ni nini?”
“Hapana, siwezi kuumizwa na kitu ambacho sikijui, ingawa najua kipo. Unaweza kuniambia?”
“Ndiyo!”
“Ni nini?”
“Si leo. Tunahitaji muda zaidi!”
“Hapana, tafadhali naomba uniambie leo.”
“Nitafurahi sana kama utaheshimu hili, naahidi kukuambia, lakini si leo. Muda ukifika nitakujulisha, shaka ondoa.”
“Hapana, nataka uniambie leo.”
“Leo haitawezekana.”
“Kwanini isiwezekane?”
“Nina sababu zangu, lakini naomba uwe mvumilivu, muda ukifika nitakuambia.”
“Naona sasa hatutaelewana, kwanini wewe unakuwa msiri sana? Hutaki nijue mambo yako, kuna nini?”
“Kwa hili, nipo tayari kwa lolote Vanessa, lakini sitakuambia.”
“Lakini una nini?”
Bruno hakujibu kitu!
Machozi yakaanza kumtoka machoni!
***
Wakati anashuka kwenye basi katika Kituo Kikuu cha Mabasi ya Mikoani jijini Tanga, akitokea Arusha, mvua kubwa ilikuwa ikinyesha. Mbaya zaidi simu ya mpenzi wake Tunu ilikuwa haipatikani. Mara ya mwisho aliwasiliana naye akiwa Hale, akimuahidi kwenda kumpokea stendi.
Aliposhuka aliangaza macho huku na huko lakini hakumuona. Akajaribu kumpigia kwa mara nyingine tena, lakini bado jibu lilibaki kuwa lile lile, haipatikani! Akachanganyikiwa kidogo. Alikuwa na haki ya kuchangangikiwa, maana ilikuwa usiku, halafu sehemu aliyokuwa akiishi Tunu mwanzo Mabawa alikuwa amehama na alipohamia hakupafahamu.
Ilikuwa saa 4:25 hivi za usiku, mvua ikianza kupungua kidogo na kuwa manyunyu, akachepuka kidogo na kuifuata taxi iliyokuwa mbele yake na kuingia akijikinga na mvua.
“Wapi kaka?” Dreva taxi akamwuliza.
“Sikumbuki vizuri eneo, lakini ni Chuda, kuna Gesti moja nzuri sana niliwahi kulala pale. Ndipo ninapotaka kwenda,” Bruno akajibu akiwa na mashaka kidogo.
“Chuda?”
“Ndiyo.”
“Naijua sehemu unayosema, kuna eneo moja lina Gesti nyingi sana, lakini nzuri zaidi ni Flowers Hotel.”
“Hiyo hiyo.”
“Ok! Twen’zetu!”
Dereva akaingiza gia na kuondoa gari taratibu. Dakika mbili tu, ikiwa ndiyo kwanza wanazunguka kutoka eneo la kituo cha mabasi, simu ya Bruno ikaita, alipotazama namba kwenye kioo, ilikuwa ngeni. Akaamua kupokea.
“Nani mwenzangu?” Ndiyo neno la kwanza Bruno kuongea.
“Tunu!”
“Tunu?”
“Ndiyo Tunu, samahani mpenzi, simu yangu imeisha charge ghafla, upo wapi?”
“Ndiyo natoka stendi, nipo kwenye taxi naelekea Gesti.”
“Sikia, mwambie huyo dereva wako akulete Nguvumali, akifika Denare Hotel, asimame hapo ni jirani na nyumbani nilipohamia, unijulishe.”
“Sawa, nakuja sasa hivi.”
Bruno akamgeukia dereva wake na kumpa maelekezo aliyopewa, dereva akageuza gari na kuondoka. Muda mfupi baadaye walikuwa nje ya Hoteli ya Denare. Bruno akashuka na kumlipa dereva, akaingia mle hotelini. Alipotulia akatoa simu yake na kumpigia Tunu.
“Umeshafika hapo?”
“Siyo kufika tu nimeshashuka, nimeingia humu hotelini.”
“Nakuja mpenzi wangu.”
Bruno akaagiza kinywaji akiwa na shauku kubwa ya kukutana na mpenzi wake Tunu. Hakuchelewa, akafika haraka na kuondoka naye hadi kwenye makazi yake mapya. Alipofika tu na kukaa kwenye kochi, Bruno akaonekana kuwa na mawazo sana. Tunu akagundua tofauti hiyo na kumuuliza...
“Vipi baby, mbona kama una mawazo?”
“Ni kweli, bado nafikiria sana kama ni kweli hunisaliti mpenzi wangu nikiwa sipo. Hivi huna mpenzi yeyote kweli baby?!”
“Bruno acha wivu dear, utakufa kwa presha.”
“Kweli?”
“Mmmmh!” Tunu akaitikia kimahaba na kumsogelea Bruno aliyekuwa hoi kwenye kochi.
Akambusu na kuamsha hisia zake zilizokuwa zimejificha. Kilichofuata ilikuwa ni kuanza kufungua vishikizo vya shati na kumuamuru avue nguo zote. Bruno akatii. Akampa taulo na kumwongoza bafuni. Akamwogesha!
***
“TUNU NOOOO...” Bruno akasema kwa sauti kuu akizidi kulia.
Vanessa akashindwa kuelewa Bruno alikuwa na tatizo gani, ni mara ya pili sasa anataja jina la Tunu na kila anapomwuliza, anakuwa hana jibu la maana. Tunu akazidi kumchanganya.
Vanessa akayatuliza macho yake usoni mwa Bruno akiwa na simanzi tele moyoni, ni mwanaume ambaye moyo wake ulikubali kumuhifadhi katikati ya kiota cha huba. Kuona machozi yake ilikuwa ni kidonda kibichi kabisa. Hakutaka kukiona kikiendelea kutoa maji!
Alitamani sana kipone!
Akamwangalia Bruno kwa macho yanayozungumza, tena kwa uwazi sana. Kwamba alikuwa akiteswa na matatizo aliyokuwa nayo. Kwamba alikuwa akiumia sana na jinsi ambavyo hataki kuwa mkweli juu ya huyo Tunu ambaye alikuwa akimtaja kila siku. Vanessa aliumia sana.
“Lakini Bruno una nini?”
“Acha tu!”
“Kwanini?”
“Vanessa kama ni kweli unatamani niishi kwa furaha naomba tuache kuzungumza juu ya hili!”
“Napenda sana uishi kwa furaha Bruno, ndiyo maana nafanya yote haya kwa ajili yako. Tafadhali naomba uniambie tatizo ni nini, unajua hakuna kitu kibaya kama kukaa na kitu kichwani na kukitolea maamuzi peke yako, unaweza kufanya maamuzi mabaya sana, kwahiyo ni vyema ukaniambia ili tushirikiane pamoja, tafadhali Bruno naomba uniambie!”
“Vanessa, Tunu ni mwanamke mbaya sana. Ni adui namba moja katika maisha yangu.”
“Kivipi?”
“Na namba mbili ni Bryson!”
“Bryson?”
“Ndiyo!”
“Mjomba’ngu?”
“Off course!”
“Ok! Niambie basi wamekufanyia nini?”
“Umeshawahi kusikia jina la Tunu?”
“Hapana.”
“Basi kwa leo tuishie hapa na naomba sana iwe hivyo kweli, nakuahidi kuzungumza na wewe siku nyingine!”
“Kweli?”
“Niamini.”
“Poa.”
Mazungumzo yakahama, wakaanza kuongelea mambo mengine kabisa. Jioni, Vanessa akaaga na kwenda zake nyumbani. Akamwacha Bruno mwenyewe hotelini.
***
Ni saa 4:45 za usiku, macho yake kwa mbali yalianza kuwa mazito, lakini hakutaka kulala. Kichwani aliendelea kusumbuliwa na kijana Bruno. Ni mara nyingi sana alijiuliza sababu za kumpenda Bruno, lakini hakuzijua.
Alikuwa mwanaume asiyejiweza, hana fedha na anayemtegemea kwa kila kitu. Kubwa zaidi alikuwa mlemavu!
Haina maana kwamba mlemavu hana haki ya kupendwa, lakini huyu hakuwa mlemavu kabla. Amepata kilema baada ya ajali, tena akiwa amemkuta hospitalini amelazwa, alijihoji mwenyewe kwa muda mrefu sana, lakini jibu alilolipata ni kwamba alikuwa akimpenda sana Bruno.
“Lakini nitaanzaje kumwambia?” Anawaza Vanessa akikosa majibu.
“Anyway, labda naweza, lakini vipi kuhusu huyo Tunu? Kwanza ni nani na ilikuwaje wakawa hawana maelewano mazuri na Anko? Hapo napata na maswali ambayo hayana majibu ya kuridhisha, lakini naamini kama nikiendelea kuwa karibu na Bruno ataniambia ukweli...” anawaza Vanessa.
Akiwa bado yupo kwenye lindi la mawazo, simu yake inaita. Anaichukua na kutazama kwenye kioo, jina linalotokea ni la mpenzi wake Emma. Anasita kupokea na kuitupa simu pembeni. Simu inaendelea kuita mpaka inakatika!
Baada ya muda inaanza kuita kwa mara nyingine tena. Vanessa anaiangalia kwa muda na kuachana nayo. Iliendelea kuita zaidi ya mara tano, hakupokea. Ilipokatika, akaizima kabisa na kuiweka kwenye chaji, akazima taa na kujilazimisha kulala.
Kiasi cha nusu saa mbele, akasikia geti likigongwa na honi kwa fujo, akajua kwa vyovyote vile atakuwa ni Emma. Hakujigusa. Lakini baada ya muda mfupi akasikia muungurumo wa gari likiingia ndani, kumbe msichana wake wa kazi alikwenda kumfungulia. Baada ya muda, Emma alikuwa chumbani kwake akiwa amefura!
“Umeshamtoa huyo mwanaume wako?” Emma akauliza akionekana kuwa mkali sana.
“Mwanaume gani?”
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (7)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Emma hakuongea kitu, akamzaba kibao cha nguvu kilichotua vyema usoni mwa Vanessa.
“Lakini kwanini unanipiga? Kwanini unaninyanyasa? Kwanini unanitesa kiasi hicho? Kwani nimekukosea nini hadi unipe adhabu kubwa kiasi hicho? Kwani mimi ni ngoma? Mbona unaninyima raha?” Vanessa alisema akilia.
“Huo umalaya wako hautakusaidia kitu we’ mwanamke. Haya kwanini ulikuwa hupokei simu yangu?”
Vanessa hakujibu!
Emma akafungua mkanda wake kiunoni na kuanza kumchapa nao Vanessa, Emma hakuwa na huruma kabisa. Alimpiga mpaka aliporidhika akaacha na kuvaa mkanda wake.
“Nitakuua wewe mwanamke, unaleta tabia zako za kimalaya hapa? Nitakuja kukuua siku moja, mimi siyo wa kuchezewa...” Emma akasema na kubamiza mlango kwa nguvu.
Kitambo kidogo, mlio wa gari ukasikika nje, alikuwa anaondoka zake.
Vipigo vya Emma vimekuwa vikimnyima raha kabisa Vanessa, pamoja na mapenzi yake yote, lakini alijikuta akianza kumchukia. Emma hakuwa na mapenzi ya kweli, siku zote alimfanya Vanessa ngoma, jambo ambalo lilimuumiza sana.
“No, muda wa kuachana naye umefika. Kuanzia sasa simtaki tena Emma na kinachofuata ni kuhakikisha Bruno anakuwa hapa. Lazima iwe hivyo, lazima...” akawaza Vanessa moyoni mwake huku akilia kwa uchungu.
Akavuta shuka na kujifunika, akisaka usingizi. Alikuwa mchovu sana, mchovu wa vitu viwili; pilika-pilika na mapenzi!
***
Kila alipogeuza macho yake na kutazama meza ya jirani yake, jicho la mwanamke yule mrembo liliendelea kumkodolea. Jicho lenye uzuri wote wa kike. Lililopambwa kwa wanja na kila aina ya vikorombwezo! Jicho lililochongwa nyusi vyema na kulifanya lizidi kuvutia!
Mbali na yote, lilikuwa legevu kama linataka kuanguka. Bruno hakuzoea macho ya aina hiyo, Mwanza hakuna macho ya aina hiyo. Pamoja na kuwa mzaliwa wa Mwanza, lakini alitembelea sehemu nyingi kikazi, ila jicho lile hakukutana nalo.
Si Mwanza, Moshi, Arusha, Dodoma, Mombasa, Shinyanga, Iringa, Mbeya na mikoa mingine yote, hakukutana na jicho lile. Leo hii anakutana nalo Tanga! Moyo ukamzizima! Akashawishika kuzidi kuliangalia, lakini alifanya hivyo kwa kuibia!
Hakutaka kuonekana wakuja, akalitizama kwa kujificha kwa mtindo wa siri yake. Akiwa ameyarudisha macho yake kwa marafiki zake, akamwona Mhudumu anakuja mpaka alipokuwa amekaa. Akamkabidhi karatasi na kumwonesha yule msichana aliyekuwa akimwangalia kwa jicho lake tamu!
“Nimepewa na yule dada pale,” yule Mhudumu akasema akisonza kidole kwa yule dada.
Kile ki – memo hakikuwa na maneno mengi. Kiliandikwa hivi; Karibu sana Tanga. Kama hutajali, ningependa niwe mwenyeji wako. Namba zangu ni 0841 17074512. Tunu.
Moyo wake ukapasuka, akageuza macho yake na kumtazama yule msichana. Akampokea kwa tabasamu pana. Tabasamu mwanana. Tunu alikuwa tunu kweli, tabasamu lake likamwongezea uzuri wake.
Tunu toto la Kitanga!
Bruno hoi!
***
Kuachana na Emma ndiyo wazo alilolala nalo Vanessa, pia wazo hilo hilo aliamka nalo kichwani mwake. Hakutamani kabisa kuwa na Emma, mwanaume mkorofi, anayempiga kila siku, anayemnyanyasa, anayemuonea! Hakuwa na thamani tena katika maisha yake.
Aliapa kumuacha!
“Lazima niachane naye, lazima,” akatamka kwa sauti ya chini akionekana kuwa na uchovu mwingi wa usingizi.

Mara moja, akachukua simu yake iliyokuwa mezani, kisha akabonyeza jina la Bruno haraka. Alitamani sana kuzungumza naye, akiamini angekuwa msaada mkubwa wa mawazo tele aliyokuwa nayo kichwani mwake. Muda si mrefu, sauti ya upande wa pili ilisikika; alikuwa ni Bruno akiongea kwa sauti ya taratibu.
“...umeamkaje Bruno?”
“Salama, vipi wewe?”
“Sijambo kabisa.”
“Yeah, ndiyo nimeamka muda huu, nikafikiria naweza kufanya kitu gani kama cha kwanza kwa leo, nikaona bora nikupigie wewe, nikusalimie, hili ndiyo jambo nililoamua kulifanya la kwanza kwa leo.”
“Nashukuru sana Vanessa, naweza kukuuliza jambo?”
“Yeah!”
“Kwanini umenichagua mimi kuwa wa kwanza kuanza ratiba zako za leo?”
“Tupo karibu Bruno, sisi ni marafiki wakubwa sasa, marafiki wa karibu sana Bruno.”
“Hakuna kingine?”
“Kipi? Au wewe unacho?”
“Sidhani, lakini kama ndivyo, nashukuru sana maana naona nitakuwa nina nafasi kubwa sana kwako.”
“Ni kweli kabisa, ipo nafasi kubwa sana moyoni mwangu kwa ajili yako. Ipo.”
“Ahsante sana.”
“Basi nikutakie, asubuhi njema, baadaye nitakuja kukuangalia.”
“Nashukuru sana, ahsante sana Vanessa, nawe nakutakia kila la kheri katika siku yako ya leo. Mungu awe taa yako!”
“Nashukuru kwa baraka zako.”
“Ok!”
Wakakata simu zao.
Vanessa akavuta pumzi ndefu sana kisha akazishusha taratibu kabisa, akatabasamu. Taratibu akamvuta Bruno kichwani mwake, akamwangalia akiwa amesimama mbele yake; naam! Alikuwa mwanaume thabiti kwake. Anayejiheshimu, mwenye mapenzi ya dhati, mwenye upendo wa ndani, mvumilivu na kila sifa njema, akammiminia Bruno.
Akatabasamu tena.
“Yeah! Yule ndiyo mwanaume, mwenye kauli njema na kujua kubembeleza, najua nikimsogeza kwangu, nitakuwa na amani. Ninazo fedha, lakini sina amani. Nahitaji amani ya moyo wangu. Naamini ipo kwake, nitajitahidi sana niipate,” anawaza Vanessa akiwa amesimama na kanga moja kifuani.
Anatoka nje na kusaidiana usafi na msichana wake wa kazi.
***
Alishasahau kabisa kwamba mkononi mwake ameshika glasi yenye kinywaji, aliulegeza mkono wake, macho yake yakiwa bado yanamwangalia yule msichana aliyemtumia kikaratasi chenye ujumbe. Akarudia kusoma kwa mara ya pili, halafu akarudisha macho yake tena kwa yule msichana.
Akakaribishwa na tabasamu mwanana kabisa. Naye akajibu. Wakatazamana wakitabasamu. Punde kile kinywaji ndani ya glasi, kikaanza kumwagika!
“Oyaaa vipi mkubwa, unanichafua!” Alikuwa ni rafiki yake aliyekaa meza ya jirani.
“Oh! I’m sorry kaka, sikukuona.”
“Usijali, lakini kuwa mwangalifu.”
“Poa.”
Kazi ikaendelea kuwa ile ile, lakini muda kidogo, akiwa kama amegutuka hivi, akaiandika ile namba ya simu kwenye simu yake, kisha akaihifadhi. Alichokifanya ni kwenda kwenye sehemu ya kuandka ujumbe mfupi, kisha akaandika ujumbe na kutuma kwenda katika ile namba.
Ulisomeka hivi; “Ahsante Tunu, nimefurahishwa sana na ukarimu wako.”
“Nami pia, nimevutiwa sana na wewe. Naomba usitafsiri vibaya, nimevutiwa na wewe....” Tunu akamtumia.
“Ahsante kwa hilo, unaishi maeneo gani kwa hapa Tanga?”
“Mabawa.”
“Ni mbali sana kutoka hapa?”
“Hapana...sijui mwenzangu unaitwa nani?”
“Bruno.”
“Najua ni mgeni, unatokea wapi?”
“Kiukweli hapa Tanga siyo mgeni sana, kwani ni mara ya sita sasa nakuja hapa.”
“Ni mfanyabiashara?”
“Hapana ni mfanyakazi wa mfanyabiashara!”
“Sawa, karibu sana Bruno, kama nilivyokuambia, nimependa sana kampani yako...kama hutajali ningependa ulale kwangu kwa kipindi chote utakachokuwa hapa.”
“Nilale kwako?”
“Ndiyo...nina nyumba kubwa Bruno, hata chumba cha wageni pia ninacho, nadhani kitakufaa.”
“Nitashukuru....acha niongee kwanza na wenzangu, halafu nitakujulisha.”
“Sawa.”
Bia zikaendelea kunyweka, huku Bruno akichati na Tunu, baadaye Tunu akahamia kwenye meza ya akina Bruno kabisa, wakaendelea kukata maji kama kawaida. Muda wa kuondoka, Bruno akaomba kwenda kulala na Tunu. Hakuna aliyemzuia, kila mtu alikuwa amelewa.
“Sasa Tunu, twende zetu,” Bruno akamwambia Tunu ambaye aliitikia kwa kutingisha kichwa huku akijitahidi kuamka kwa kuyumba kidogo.
Wakashikana mikono na kwenda kwenye taxi. Wakaingia na kuketi wote siti ya nyuma. Mabusu ukawa ndiyo wimbo mzuri kwako kwa usiku huo.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (8)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

***
Waliingia kwenye chumba kimoja kizuri chenye mpangilio wa kuridhisha. Kilikuwa chumba kimoja chenye kila kitu ndani, choo na bafu vilikuwa ndani. Ile kuingia tu, Tunu akavua nguo zote harakaharaka, akamsogelea Bruno na kuanza kumvua.
“Vipi?” Bruno akauliza, pombe ikianza kumtoka.
“Nataka twende bafuni.”
“Si ulisema kuna chumba changu?”
“Acha ujinga, utaniaibisha mwanaume. Hebu vua nguo twende bafuni, tuoge tuje tulale.”
Bruno akawa mpole, akapelekwa bafuni na kuogeshwa kwa maji ya karafuu. Starehe zote alizisikia. Neno moja tu, lilimponyoka; “Hivi Tunu hujaolewa?”
“Bado, kwani unataka kunioa?”
“Nitakuwa muongo, nilitaka tu kujua.”
“Sijaolewa.”
“Huna bwana anayekuja hapa?” Swali hili aliuliza akionekana kuwa na mashaka kidogo.
“Sina, kwanini una mashaka sana? Unadhani mimi ni mwanamke mpumbavu wa kiwango gani nikulete kwenye nyumba ambayo ina mmiliki wake? Bruno jiamini,” Tunu akasema, akimbusu midomoni mwake, kisha akamsukuma kitandani.
Akazima taa.
***
Alitulia kitandani kwa muda, akijitahidi kujisahaulisha kumbukumbu za nyuma, lakini ilishindikana. Hakutaka kuendelea kumkumbuka Tunu, kikubwa kwake kwa wakati ule ilikuwa ni kupona kwanza, halafu kisasi kingefuata baadaye.
Ilikuwa lazima afanye kitu kwa ajili ya Tunu, kumuacha hivi hivi haikuwa ndoto yake hakika. Lazima amkomeshe. Lazima.
“Ndiyo, nitamkomesha, nitaanza na Tunu, halafu nitamaliza na Bryson, lakini wote lazima niwaachie maumivu kama ambavyo wao wameniachia mimi maumivu. Siwezi kukaa kimya wakati naumia, nimeteswa, nimenyanyaswa! Siwezi na kweli siwezi na sitaruhusu hilo kabisa,” anazidi kuwaza Bruno.
Anaamka kwa kujikongoja kidogo, kisha anaingia bafuni kujiswafi. Anarudi na kuvaa nguo zake, anachukua gazeti la Championi lililokuwa mezani na kuanza kuperuzi. Alikuwa anapenda sana kusoma hadithi.
Macho yake yametulia kwenye hadithi ya The Devil’s Smile (Tabasamu la Shetani) iliyotungwa na mtunzi mashuhuri katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati Eric Shigongo, ambaye anasifika sana kwa vitabu vyake vya President Loves My Wife (Rais Anampenda Mke Wangu) na The Last Days of My Life (Siku za Mwisho wa Uhai Wangu), akasoma akiwa ametulia, mstari kwa mstari. Utulivu huo ukamfanya asisikie mlango uliokuwa ukigongwa!
Baadaye mgongaji akazidisha kasi, akagonga kwa kasi zaidi...
Akashtuka sana!
“Nani?” Akauliza.
“Jane, vipi umelala?”
“Hapana, ingia.”
Akaingia.
“Vipi?”
“Salama, za asubuhi?”
“Njema. Mbona umechelewa kuitika?”
“Bwana, sikusikia, akili yangu yote ipo kwa Shigongo, napenda sana hadithi zake!”
“Ok! Kumbe wewe ni mpenzi sana wa hadithi?”
“Sana!”
“...sasa vipi, nikuletee nini?”
“Hata sijui dada’ngu, unaweza kunichagulia?”
“Sema chochote utakacho.”
“Kwani mna nini na nini?”
“Kama kawaida, supu zote, maziwa, chai rangi na mtori.”
“Nadhani leo ninywe mtori, utaniwekea na chapati mbili, mchana ugali samaki.”
“Sawa.”
Jane akaondoka, huyu ni dada maalum ambaye alikuwa akimhudumia kwa kila kitu pale Hotelini na malipo yote hufanywa na Vanessa. Pamoja na kwamba alikuwa mgojwa, lakini sasa afya yake ikaanza kuimarika.
Akazidi kuvutia!
***
Anatazama maji yanavyopiga kwa kasi baharini, yupo katika Ufukwe wa Coco, akipunga upepo. Vanessa aliamua kwenda ufukweni kwasababu mbili; alihitaji kumpumzisha akili yake, lakini pia alitamani sana kupata jibu la uhakika kuwa anampenda nani kati ya wanaume wawili. Emma na Bruno!
Alihitaji kupata jibu moja yakinifu ambalo lina maana, hakutamani kupata maumivu ya moyo, ufukweni ni sehemu ambayo akili yake huhiyari kutulia na kuchanganua mambo vyema, kwahiyo aliamini kwa vyovyote vile angepata jibu la moja kwa moja.
Akiwa katika tafakari, mkononi mwake akiwa na boksi la juice, mara simu yake ikaita. Mara moja akatazama kwenye kioo cha simu, akakutana na jina la Emma. Moyo wake ukashtuka sana.
Ni Emma!
Emma mpigaji!
Anayeugeuza mwili wake ngoma kila siku. Ni kweli alikuwa anampenda sana, lakini yeye hajali wala kuthamini penzi lake, kazi yake imekuwa kumshushia kipigo kila siku, jambo linalomuumiza sana.
Akaiangalia ile simu ikiita mpaka ikakatika! Ikaanza kuita tena, baadaye ikakatika. Ikaita kwa mara ya tatu; akaamua kupokea.
“Unasemaje Emma?” Vanessa akasema kwa hasira mara tu alipopokea simu.
“Acha hasira mpenzi.”
“Emma, naona mwisho wetu sasa umefika.”
“Najua sweetie, najua...na ndiyo maana nimekupigia simu...” Emma alikuwa akizungumza kwa sauti ya taratibu sana, akionesha upole wa hali ya juu.
Haikuwa kawaida yake kabisa. Emma si mtu wa kumbembeleza Vanessa, siku zote alikuwa wa kutukana na kumpiga. Leo anazungumza taratibu?
Anabembeleza?
Amestaarabika?
Maajabu haya!
“Hivi ni Emma mwenyewe nazungumza naye au kuna mtu ameiba simu yake?” Vanessa alisema akijitahidi kuisikiliza vyema sauti ya Emma.
“Najua ni vigumu kuamini, umeshazoea kelele zangu, si kawaida yangu kuzungumza hivi, lakini leo nimejua thamani na maana ya mapenzi, nimegundua kwamba nilikuwa nakutesa sana mpenzi wangu, sipendi iwe hivi na ndiyo maana nimekupigia...nahitaji kuonana na wewe mpenzi!”
“Leo una nini?”
“Kwanini?”
“Mbona siku nyingine ukinihitaji umekuwa ukija moja kwa moja nyumbani, leo mbona unaomba ruhusa, una nini Emma?”
“Nimezaliwa katika ulimwengu mpya wa mapenzi, ndiyo maana kila kitu kimebadilika, nakupenda Vanessa...” Emma akazungumza kwa sauti ya taratibu sana, iliyojaa ustaarabu.
Vanessa akachangayikiwa sana, yalikuwa maneno makali sana yaliyomchoma, alikuwa katika wakati mgumu wa kuaga penzi la Emma, lakini inakuwaje leo hii anampigia na kumwambia anamhitaji, anampenda na anataka kuwa mpenzi mpya kwake?
Alisisimka mwili!
Moyo wake ukaenda mbio, kisha akakata simu na kuizima kabisa! Akaketi chini akijilazimisha kuwa katika hali ya kawaida. Hakuweza. Mvua ya machozi ikaanza kumiminika machoni mwake.
Ufukweni pale, hapakuwa mahala pazuri tena kwake, akainuka pale chini, kisha akapiga hatua za kivivu kwenda alipoegesha gari lake. Akaingia na kuwasha, akaondoka kwa kasi.
***
Hakuangalia sehemu yoyote baada ya kuegesha gari lake nyumbani kwake. Vanessa akapiga hatua za taratibu akiufuata mlango wa kuingilia ndani. Hakusikia hata sauti ya msichana wake wa kazi akimsalimia pale sebuleni.
Mguu wa kwanza, mguu wa pili hadi chumbani. Hamad! Anakutana na Emma, akiwa ametulia kitandani. Alikuwa na dalili zote kwamba alikuwa akimsubiri yeye tena kwa mazungumzo muhimu.
“Usishtuke mama, pole na mihangaiko yako. Karibu ndani mpenzi...kama nilivyokuambia kwenye simu, nahitaji kuzungumza na wewe, nataka sana kuzungumzia penzi letu, nahisi linayumba sasa!” Emma akasema akisimama taratibu na kumvuta Vanessa ndani.
Akaingia akionesha woga. Akambusu na kumkalisha kitandani. Mazungumzo yakaanza, Emma mtulivu kuliko kawaida. Walikuwa kama wapenzi waliokutana kwa mara ya kwanza. Wakaingia bafuni na kuoga pamoja. Wakarudi chumbani na kujitupa kitandani.
Moyo wa Vanessa ukaingiwa na ubaridi, akishindwa kuwa na msimamo nani awe wake. Kwa unyonge akanyoosha mkoko wake na kushika bed switch akazima. Akiwa analala sawasawa, simu ya Vanessa ikaita.
Kwakuwa Emma alikuwa karibu nayo, akaichukua na kumpa Vanessa.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (9)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Oh baby...someone is calling you!” (Oh mpenzi, kuna mtu anakupigia) Emma akasema kwa upole, haoneshi wivu kabisa.
Vanessa alipoichukua, akashtuka sana.
Alikuwa ni Bruno.
“Pick up the phone baby!” (Pokea simu mpenzi!)
Vanessa akaganda!
Haikuwa kawaida ya Emma kuchukulia kwa wepesi kama vile, kwake yeye ilikuwa maajabu sana. Yaani Emma anampa simu yake na kumwambia kuna mtu anapiga? Amebadilika kiasi gani?
Muungwana kiasi gani?
Hakika yalikuwa maajabu ya aina yake. Lakini hakutaka kuongea na Bruno, ingawa hawakuwa na mazungumzo mabaya. Alijikuta akiwa hayupo tayari kuzungumza naye tu! Akabaki anaingalia ile simu kwa muda mrefu, mpaka ilipokatika.
“Kwanini hupokei darling?” Emma akamwuliza akionekana kuwa na kauli nzuri sana kwa mpenzi wake.
“Hapana...sijisikii kuongea na mtu saa hizi.”
“Sasa si bora upokee na kumwambia akupigie kesho!”
“Achana naye darling, asikusumbue kichwa.”
“Ni nani?”

“Bwege mmoja hivi, si muhimu sana kumjua.”
“Ok!”
Vanessa akazima simu na kuirudisha mezani. Bado anashindwa kuelewa ni kwanini Emma amebadilika kiasi kile.
“Lakini sweetie, nina maswali kidogo kwako.”
“Uliza.”
“Ni kweli umebadilika?”
“Nadhani matendo yangu yanaweza kuongea zaidi kuliko mimi.”
“Ni kweli dear, lakini nataka kusikia kauli yako.”
“We’ unaonaje?”
“Kweli naona mabadiliko katika mapenzi yetu, lakini siamini kama yatakuwa ya kudumu!”
“Kwanini huamini?”
“Siamini tu!”
“Kwanini mpenzi wangu? Kila kitu kina mwanzo na mwisho wake, unajua wakati mwingine mtu unaweza kufanya makosa kwa muda, lakini ghafla ukagundua makosa yako na kubadilika. Huyo ndiye mimi. Nimegundua na nimeona ni bora nibadilike, ni vibaya baby?”
“Hapana.”
Pamoja na kuhisi kama ndoto, lakini siku hiyo ndiyo aliyofaidi zaidi penzi la Emma. Wakaufurahia vilivyo usiku huo. Kila mmoja akiwa mpya kwa mwenzake.
***
Emma alikuwa wa kwanza kuamka asubuhi, akamwamsha Vanessa na kumbusu mashavuni mwake, ikawa asubuhi nyingine njema tena kwa Vanessa. Anaamshwa?
Anapigwa busu?
Alikuwa na haki ya kushangaa, huyu si Emma wa miezi sita iliyopita. Sasa ni Emma wa kimahaba anayeonekana dhahiri kufahamu umuhimu wa mapenzi. Vanessa akafurahi sana moyoni mwake.
Akaanza kujiona naye ni mwanamke kati ya wanawake bora wanaofurahi jijini Dar es Salaam. Si mwenye simanzi tena, si mwenye kilio tena. Ni mwanamke mwenye amani ya moyo ambaye tabasamu kwake ni wimbo wenye nafasi kubwa zaidi.
“Darling, kweli umebadilika. Ahsante sana kwa kunipenda, nakupenda pia Emma.”
“Usijali mpenzi wangu, natambua uliumia sana, muda wa kuumia umeshapita, furahi pamoja nami mpenzi.”
“Ahsante sana, sasa mbona asubuhi hivi?” Vanessa akauliza akiachia tabasamu mwanana kabisa usoni mwake.
“Mbona umekaa kimya muda wote!”
“Nilishasahau mwenzio, nimenogewa na penzi jipya!”
Wakacheka tena.
“Nawahi kazini mama.”
“Lakini si kawaida yako!”
“Ni kweli, ila kuna jamaa nakutana nao asubuhi hii, nikiwakosa tu, dili linaharibika.”
“Haya baba umeshinda.”
“Sasa?”
“Nini tena zaidi ya kuondoka?”
“Nenda basi bafuni kwanza ujimwagie maji ndiyo uende.”
“Unadhani ni rahisi kutoka bila kuoga?”
“Lakini kama mkeo nina wajibu wa kukumbusha mpenzi wangu!”
“Sawa, ahsante sana mama,” akasema Emma na kumuangushia busu lingine la nguvu.
Emma akaingia bafuni.
***
Macho yake yalitosha kabisa kufikisha ujumbe wa kile kilichopo moyoni mwake, alikuwa akitazama kwa macho ya huruma, huku akionesha wazi kwamba anahisi anadhauriwa.
Bruno alikuwa ameshaanza kuhisi kwamba amekuwa mzigo kwa Vanessa, kitendo cha kutokupokea simu kilitosha kabisa kuthibitisha hisia zake hizo. Kabla hajafungua kinywa chake kusema chochote, Vanessa akamuwahi!
“Sijui nitumie kauli gani Bruno, sijui nizungumzeje Bruno, lakini nataka kukuomba msamaha kwa yote yaliyotokea jana,” Vanessa akasema kwa sauti ya kulalamika.
“Najua unanisaidia Vanessa, lakini kama nakusumbua ni bora uniambie.”
“Hapana Bruno, samahani!”
“Lakini kwanini hukupokea simu yangu?”
“Ndiyo maana nimekuomba msamaha!”
“Kama nilikuwa na tatizo kubwa?”
“Bruno please elewa, naomba unisamehe kwa hilo.”
Kimya cha muda mfupi kikapita. Kila mmoja akitafakari kivyake. Bado Bruno alionekana mwenye mawazo mengi, huku akifikiria maisha yake ya baadaye. Mwonekano wake ulionesha wazi kwamba sasa hana imani tena na Vanessa.
“Lakini nimekuja na wazo,” Vanessa akasema.
“Wazo gani?”
“Naomba uhamie kwangu, nataka kuishi na wewe nyumbani kwangu!”
“Hapana,” Bruno akajibu haraka.
“Kwanini?”
“Sitaki tu!”
“Kila kitu kina sababu!”
“Hujaolewa?”
“Bado, lakini nina mchumba ambaye huwa anakuja nyumbani kwangu!”
“Sasa itakuwaje?”
“Niachie mimi, nitamwambia wewe ni mjomba wangu, kazi ya kuongea naye ni juu yangu,” akasema Vanessa.
“Hapana, roho yangu inakataa kabisa kukubaliana na hilo...kama msaada wako umeishia hapa niambie, nitakachokuomba ni nauli tu ya kunipeleka kwetu basi!” Bruno akasema akionekana kutokubaliana kabisa na mawazo yake.
Vanessa ni kama alikuwa njia panda, maana alipata wazo la kumuhamishia nyumbani kwake ili amtunze na ikiwezekana baadaye awe mpenzi wake, kwani mabadiliko ya Emma hakuyaamini sana.
Bado alihisi penzi lake lipo kwa Bruno.
Akaampa kumsogeza kwake!
Alihitaji sana kuishi naye nyumbani kwake, aliamini kufanya hivyo, kutakuwa kunamsogeza karibu yake zaidi. Hilo ndilo lililounguruma zaidi ubongoni mwake. Akamwangalia Bruno kwa macho ya ushawishi, lakini Bruno alionekana kukosa furaha ghafla.
Alionekana wazi kutofurahishwa na uamuzi wa Vanessa, ndani ya moyo wake alifurahi sana kuona jinsi mwanamke yule mwenye upendo ambaye alijitoa kwa ajili ya maisha yake, lakini hakuwa na wazo kwamba Vanessa alikuwa akiyafanya yote yale kwasababu ya penzi lake la dhati. Hilo hakulijua kabisa.
Anazidi kumwangalia...
Macho yake yanaongea...
Hata uso wake nao unasoma kitu fulani, kitu ambacho kipo ndani kabisa ya moyo wake.
“Sikiliza Vanessa najua una nia ya kunisaidia, hilo nalijua kabisa...”
“Sasa?”
“Ingekuwa rahisi mimi kukubaliana na wazo lako, lakini mazingira hayaruhusu!”
“Mazingira kivipi Bruno?”
“Najua unapenda kunisaidia.”
“Enhee!”
“Pia nafahamu huna nia mbaya na mimi!”
“Ni kweli.”
“Lakini tayari umeshaniambia kwamba unaye mchumba na huwa anakuja nyumbani kwako mara nyingi!”
“Hujakosea kitu Bruno!”
“Sasa unadhani akinikuta atajua kuwa mimi ni rafiki yako na siyo wapenzi akaridhika kirahisi?”
“Kwani tuna nia nyingine mbaya?”
“Najua hatuna.”
“Hata siku moja kuna mmoja wetu aliyezungumza au kuonesha ana nia tofautio na mwenzake?”
“Hapana!”
“Sasa wasiwasi wa nini Bruno?”
“Yule ni mpenzi wako Vanessa, ana haki ya kuwa na mashaka na kuhoji kama kitu hakipo sawa, huoni kwamba nitakuwa navuruga mapenzi yenu?”
“Unavuruga kivipi?”
“Nimeshakuambia kila kitu Vanessa, sioni kama kuna jambo jipya ambalo sijakuambia.”
“Ok! Nimekubaliana na yote kama unavyotaka, lakini unakumbuka nimekuambia nini mwanzoni kabisa? Nitamwambia wewe ni mjomba wangu, hana mamlaka ya kunihoji zaidi, isitoshe hawajui ndugu zangu wote. Maswali mengine niachie mimi.”
Bruno akaonekana kukaa kimya akizidi kutafakari. Akavuta pumzi ndefu sana, kisha akazishusha taratibu, midomo yake ikaanza kutingishika. Ni dhahiri alikuwa anaongea...
“Nimekuelewa vizuri sana, lakini nina jambo lingine nataka kukuuliza.”
“Uliza tu!”
“Vipi kuhusu Bryson?”
“Bryson?”
“Ndiyo Bryson!”
“Unamaanisha nini?”
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (10)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Vanessa nazungumza kuhusu mjomba wako.”
“Hafahamiani naye.”
“Sijasema anafahamiana naye, lakini si unajua kuwa nina matatizo naye.”
“Sasa kwani hayo matatizo yako na Anko Bry, yanahusiana vipi na mimi?”
“Unaona hayakuhusu?”
“Kivipi sasa?”
“Kama nakuja kuishi kwako, nyumbani kwa mtoto wa dada yake, si huwa anafika pale? Nitamwambia nini wakati nina uadui naye.”
“Halafu huwa unanichanganya sana, hivi una matatizo gani na Anko lakini?”
“Muda ukifika nitakuambia.”
“Kwanini kila siku huwa unasema hivyo na huniambii kitu?”
“Siku ya kukuambia itafika na lazima nitafanya hivyo. Hebu nikuulize kitu kimoja.”
“Niambie.”
“Unamfahamu Tunu?”
“Tunu?”
“Ndiyo Tunu wa Tanga.”
“Hapana simfahamu, lakini nimekuwa nikikusikia sana ukimtaja kila ninapokuuliza kuhusu chanzo cha matatizo yako. Ni nani?” Vanessa akauliza akiwa ameyatuliza macho yake kwa Bruno.
Ikawa kama amemwambia Bruno alie, macho ya Bruno yakaanza kubadilika rangi taratibu na kuwa mekundu, ghafla mvua ya machozi ikaanza kumiminika machoni mwake. Vanessa akazidi kupata utata.
“Kwanini unalia Bruno?” Vanessa akauliza akijisogeza jirani na alipoketi Bruno.
Bruno hakujibu!
Machozi yalijibu!
“Niambie Bruno. Una tatizo gani?”
“Tunu!” Akasema mara moja na kunyamaza.
“Amekufanya nini?”
“Bryson!”
“Mbona maneno yako yamejaa mafumbo sana, nieleze basi niweze kufahamu, kwanini unanifumba kiasi hicho Bruno?”
Akazidi kulia.
Hilo ndilo jibu pekee alilokuwa nalo. Ghafla akaonekana kuyaelekeza macho yake juu ya dari, akayagandisha huko. Akaonekana kuwaza jambo fulani zito, machozi yakizidi kulowanisha mashavu yake. Alikuwa katika lindi la mawazo. Lindi lenye mawazo mazito ya kutesa!
Ya kuumiza moyo!
Akazidi kulia...
***
Ni usiku wa tatu analala kwenye chumba hiki kizuri, chenye vitu vizuri, akiwa na mwanamke mzuri. Mrembo. Anayevutia. Mwenye macho ya kulegea, anayejua mapenzi, aliyeweza kumchanganya mtima wake.
Tunu!
Bruno aliona kama dunia nzima ni mali yake kwa manjonjo aliyokuwa akiyapata kutoka kwa Tunu. Mwanamke huyo alikuwa na kila aina ya ufundi wa kimapenzi. Alikuwa anajua anachokifanya anapokuwa na mwaume faragha. Anajua kiu ya mwanaume inavyokatwa! Tunu anajua kumfanya mwanaume atulie na kusikiliza kila atakachokiagiza faragha kwa raha na kauli zenye kuvutia masikioni.
Tunu alifanikiwa kumnasa mapenzini. Akakumbuka swali alilomuuliza asubuhi ya siku hiyo, hakukumbuka vizuri idadi ya swali hilo kwa Tunu, lakini kwa kukukisia, aliweza kugundua kwamba alimuuliza kwa zaidi ya mara kumi na tano. Swali gumu kwa muulizaji, lakini jepesi sana kwa anayetakiwa kujibu.
“Hivi ni kweli hujaolewa?” Alimwuliza, akimtazama usoni.
“Nikuambie mara ngapi sina mume?”
“Tunu kweli?”
“Sema nifanye nini ili uniamini!”
“Basi nakuamini, lakini napenda sana kujiridhisha, huwa sipendi matatizo yasiyo ya lazima. Enhee, huna hata mchumba?”
“Sina Bruno.”
Hayo ni mazungumzo waliyoongea asubuhi ya siku hiyo, ambayo yalizidi kumpa matumaini kwamba hayupo katika penzi la wizi. Hilo aliliamini kwa asimilia mia moja!
Yupo kitandani mtupu, akiwa anacheza michezo ya kimahaba na Tunu, mara mlango unagongwa! Mgongaji anagonga kwa kasi zaidi.
Anamwangalia Tunu ambaye alikuwa anahema kwa kasi akiwa ameyatoa macho. Akachukua upande wa kanga na kusogea mlangoni.
Akafungua!
“Mume wangu!” Tunu akapiga kelele.

Bruno akabaki anatetemeka akiwa hajui la kufanya. Alikuwa ameingia kwenye matatizo mapya. Alijua vizuri adha ya kufumaniwa.
Mara akaingia mwanaume mwenye miraba minne, akiwa anaonekana dhahiri kupigwa na butwaa na alichokiona.
Alikuwa ni Bryson.
***
“Sikiliza Vanessa, sitaki kwenda kuishi kwako!” Bruno akasema kwa hasira akimwangalia Vanessa usoni bila kupepesa macho.
“Kwanini?” Vanessa akauliza kwa mshangao.
“Nimesema sitaki tu!”
“Sawa hutaki, kuna nini?”
“Mbona huelewi, sitaki!”
Macho ya Bruno yanaonesha kilichomo ndani ya moyo wake, yanasema na kuweka kila kitu bayana. Anaonekana kuwa katika bahari kubwa yenye mateso na simanzi, yupo katikati ya msitu wenye wanyama wakali wasio na huruma!
Yanasema...
Kwamba mzigo alionao ni mkubwa kuliko nguvu zake. amelemewa sana, lakini mbaya zaidi ni kwamba, hayupo tayari kutua mzigo huo na kumpa mwingine amsaidie, na kama anafaya hivyo ni kwa kupunguza kilo moja moja wakati mzigo alionao ni wa kilo elfu moja!
Machozi machoni!
Huzuni moyoni!
“Lakini Bruno, kwanini unakuwa hivyo?” Vanessa akamwuliza tena.
“Nateseka!”
“Na nini?”
“Naumia.”
“Kivipi?”
“Nanyanyasika!”
“Sawa sema basi kwa namna gani?”
“Tutazungumza siku nyingine!”
“Kwanini kila siku huwa unasema hivyo na hujawahi kutimiza hiyo ahadi?”
“Kwasababu hiyo siku haijafika, ikifika nitafanya hivyo!”
“Bruno...” Vanessa akaita kwa sauti ambayo sasa ilisema.
Alishaamua kuonesha kitu tofauti kidogo, sauti yake ilikuwa ya kimahaba yenye kusihi na kuomba kukubaliwa ombi lake. Ni sauti hiyo ndiyo iliyonasua mgando akilini mwa Bruno na kuanza kuhisi kitu kingine zaidi katika msaada wa mrembo yule!
Yeye si mjinga!
Si mshamba!
Ni mwerevu!
Tena aliyeerevuka na kufahamu mambo yanavyokwenda! Kwahiyo hata hapo alijua kuna kitu. Kitu ambacho kinaweza kuwa kizuri na wakati huo huo pia kinaweza kuwa kibaya. Kipo kitu. Alijua kabisa kwamba sasa Vanessa alikuwa anaelekea kwenye mapenzi!
Akakaa vizuri kitandani, akiyatazama macho ya Vanessa yanavyotazama. Naam! Yalikuwa yanatazama kimapenzi, hata midomo yake, ilikaa kimapenzi. Kila kitu kilikuwa kimapenzi-mapenzi. Akaamua kurahisha mambo...
“Najua unachotaka kuniambia...” Bruno akasema kwa kujiamini.
“Ni nini?”
“Ni juu ya kwenda kuishi kwako!”
“Kweli kabisa, hakuna ulichokosea.”
“Ninalo swali moja.”
“Uliza.”
“Unanihakikishia usalama wa maisha yangu?”
“Kabisa.”
“Utahakikisha unamfanya mchumba wako aamini kwamba mimi ni mjomba wako?”
“Ndiyo!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Ok, nimekubali kwenda kuishi na wewe!”
“What?”
“Mbona umeshtuka, kwani ni ajabu sana?”
“Tumetumia muda mrefu sana kujadili jambo hili na wewe umeendelea kukazania kwamba hutaki, lazima nishtuke, ahsante sana kwa kukubaliana na mimi. Nashukuru kwa hilo.”
“Usijali, Tuondoke au?”
“Ndiyo, kwani kuna nini tena?”
Wakacheka pamoja. Kilichofuata ilikuwa ni kukusanya nguo zote na kuweka kwenye begi, kisha Vanessa akapiga simu Mapokezi, waliokuja kumsaidia kumshusha Bruno hadi chini na kumpeleka kwenye gari. Akaketi kushoto kwa dereva.
“Ahsanteni sana...” Vanessa akawashukuru wale dada wa Mapokezi, akiondoa gari taratibu.
“Karibuni tena...” mmoja wao akasema.
Bruno akatoa mkono wake dirishani na kuwapungia. Kwa muda mfupi aliokuwa akiishi pale hotelini, walikuwa wameshazoeana sana.
***
Ilikuwa nyumba nzuri ya kuvutia, yenye maua yaliyopandwa katika mpangilio wa kupendeza. Kila kitu kilikuwa kizuri kwake, kuanzia getini, alikuwa akifurahia uzuri wa rangi. Sasa anaingizwa sebuleni, anakutana na sofa za kisasa zilizonakshiwa na vitambaa vizuri juu yake!
Bruno akawa anashangaa kila kitu, ilikuwa nyumba nzuri ambayo si rahisi kuamini kwamba ilimilikiwa na mwanamke. Lakini ndivyo ilivyokuwa.
“Karibu sana Anko, jisikie huru...” Vanessa akamwambia Bruno mara baada ya kuingia ndani.
“Ahsante sana mpwa wangu, umejitahidi sana...hongera!”
“Kawaida, nashukuru lakini kwa pongezi Anko!”
“Ok!” Akajibu akiendelea kutembeza macho yake kila kona ya nyumba ile nzuri yenye samani za kupendeza ndani!
“Amina...huyu ni mjomba wangu, alipata ajali na kuvunjika mguu, kwa bahati mbaya amekatwa. Tutakuwa naye hapa nyumbani akiendelea kujiuguza!” Vanessa akamwambia msichana wake wa kazi.
“Sawa dada...” akaitikia kwa heshima na kumsalimia Bruno: “Shikamoo Anko!”
“Marhaba!”
“Anko huyu ni Amina, ananisaidia kazi hapa nyumbani!”
“Ok, nimefurahi kumfahamu.”
Kilichofuata ilikuwa ni kupelekwa chumbani na kuoneshwa chumba chake cha kulala. Kilikuwa na kila kitu ndani.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (11)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

“Hiki kitakuwa chumba chako cha kulala, kuna kila kitu ndani!” Vanessa akamwambia Bruno.
“Ahsante sana Vanessa, nashukuru sana kwa kunijali.”
“Usijali.”
Akamwacha chumbani kwake, akarudi sebuleni. Chakula kilipokuwa tayari akaenda kumwita, wakaungana pamoja sebuleni na kupata chakula. Baada ya hapo ikawa ni kuangalia filamu za kibongo, stori za hapa na pale zikiendelea.
***
Saa 5:30 za usiku Emma alikuwa akipiga honi getini mwa nyumba ya Vanessa, Amina akatoka na kwenda kumfungulia. Akaingiza gari ndani na kushuka akielekea sebuleni.
Macho yake yakakutana na Bruno. Akapigwa na butwaa, moja kwa moja aliamini kwamba mwanaume yule alikuwa na uhusiano na Vanessa.
Hakumsalimia mtu pale sebuleni, akapita moja kwa moja hadi chumbani. Vanessa akasimama na kumfuata nyuma. Alipobamiza mlango wa chumbani, naye akaufungua na kuingia.
“Umeshaanza umalaya wako, umeona kuwa naye huko nje hakutoshi, sasa umemuhamishia nyumbani kabisa, eneheeeee....” Emma akafoka kwa hasira.
“Ndiyo salamu yako?” Vanessa akajibu akionesha kutojali.
Emma hakuongea kitu chochote zaidi ya kuinua mkono na kushusha kibao kizito shavuni mwa Vanessa. Kibao kimoja tu, kilimdondosha Vanessa chini, Emma akavua mkanda kiunoni, akijiandaa kuendelea kutoa kipigo!
Emma alidhamiria kumuumiza Vanessa, alikuwa hachagui mahali pa kupiga, alivua mkanda kiunoni na kuendelea kumchapa kila kona ya mwili wake, pamoja na kilio alichokuwa akitoa Vanessa, lakini Emma hakuonekana kujali!
“Wewe unajifanya malaya, sasa nitakukomesha!”
“Nani malaya Emma, nani malaya?”
“Wewe!”
“Umenifumania?”
“Huyo mwanaume hapo sebuleni ni nani? Unaniletea wanaume hadi nyumbani, leo nitakuua!” Emma alisema na kuendelea kumpiga Vanessa ambaye alizidi kuomba aachwe lakini Emma ni kama aliweka pamba masikioni mwake.
Baadaye Emma akaacha kumpiga na kukaa kitandani, Vanessa naye kwa taabu sana akaketi kitandani akizidi kulia.
“Kwanini unanipiga bila kosa Emma?”
“Unataka kosa gani lingine zaidi ya hili la kuniletea wanaume nyumbani?”
“Una uhakika gani kuwa yule ni mwanaume wangu!”
“Nina uhakika!”
“Kivipi?”
“Unafikiri mimi sijui kinachoendelea?” Emma akasema.
Kidogo Vanessa akashtuka, akiamini huenda Emma alikuwa anajua kila kitu.
“Unajua nini?”
“Najua sana...najua kila kitu!”
“Sasa kwa taarifa yako yule ni Anko wangu!” Vanessa akasema kwa kujitahidi kidogo, maana alikuwa anadanganya!
“Nani?”
“Mjomba!”
“Ni mjomba wako yule?”
“Kwahiyo hujanisikia au hujapenda?”
“Nataka kujua!”
“Tena anaumwa, alikuwa nyumbani na sasa amekuja kwangu kujiuguza, maana huku Hospitali nyingi!”
“Kweli?”
“Nina utani na wewe?”
Emma akanyamaza kimya, akaonekana kuanza kuingiwa na maneno ya Vanessa, tayari ndani ya nafsi yake kulishaingiwa na huruma pamoja na kujilaumu!
Mjomba wake?
Halafu anasema ni bwana’ke?
Aibu kiasi gani?
Uonevu kiasi gani?
“Baby, ni kweli unayosema?” Emma akamwuliza akiwa na sauti ya kimahaba ambayo ilikuwa inahitaji msamaha.
“Nashukuru kwa kunipiga bila kosa...”
“Siyo hivyo, ni mapenzi tu baby!”
“Mapenzi ya kupigana?”
“Sasa nilijua ni mwanaume wako, ndiyo maana nikachukia na kushikwa na hasira!”
“Sasa umegundua nini?”
“Ni mjomba wako!”
“Baada ya kunipiga siyo? Kwani ungeuliza kabla ungepungua wapi?”
“Nisamehe!”
“Umeshaufanya mwili wangu ngoma, kila siku unaudunda unavyotaka, kwanini unanifanyia hivi lakini? Kwanini unaninyanyasa? Ni lini nitakaa kwa amani?”
“Vanessa ndiyo maana nimekuomba samahani mpenzi wangu!”
“Samahani wakati nimeshaumia?”
“Najua baby, lakini bado nahitaji msamaha wako!”
“Kwahiyo kosa langu ni kukupenda siyo?”
“Sina maana hiyo!”
“Emma naona huu uwe mwisho wetu, kama unaweza kunitukana na kusema natembea na mjomba wangu, naona haya mapenzi yetu yafikie tamati, hatuwezi kwenda kwa staili hii. Inaniuma sana, kila siku unanipiga, sina amani na haya mapenzi, naona tufikie mwisho.”
“Hapana sweetie,” Emma akasema, lakini Vanessa akamkatisha haraka.
“Sitaki Emma, naona umeona mwili wangu ngoma, sikutaki tena!” Vanessa alisema akionesha kuwa na hasira kuliko kawaida.
Kazi ya Emma kumbembeleza Vanessa ilikuwa kubwa sana, lakini hapakuwa na dalili za kuelekea kwenye makubaliano. Vanessa aliendelea kushikilia msimamo wake, lakini moyoni alikuwa na lengo lingine kabisa. Alitaka kuachana na Emma ili aanzishe uhusiano mpya na Bruno.
***
“Vipi mbona kama nasikia zogo?” Bruno akamwuliza Amina pale sebuleni.
“Ni kweli mjomba, hujasikia vibaya!”
“Wanagombana au?”
“Ndiyo...lakini ni kawaida yao, baada ya muda mfupi utashangaa wakiwa kimya kabisa!”
“Sababu ni nini?”
“Sijui na sijawahi kufahamu hata mara moja, kwasababu mambo yao ya ndani wanayajua wenyewe!”
“Ok! Nimekuelewa!”
Mara wakiwa wanaendelea kuzungumza, Vanessa akatamalaki sebuleni, nyuma yake akija Emma. Vanessa akaketi kwenye kiti akionekana kuwa na mawazo sana. Akili yake haikuwa sawa, hakupendezwa na tabia ya Emma ambayo ilikuwa ni kumuangushia kipigo kila wakati.
“Emma, huyu ni mjomba wangu, anaitwa Anko Bruno!” Vanessa akasema akionekana kupoteza furaha yake kabisa.
“Nimefurahi kumfahamu!” Emma akasema.
“Hata mimi pia!” Bruno naye akadakia.
“Anko, huyu ndiye mchumba wangu, anaitwa Emma!”
“Ok! Nimefurahi kukutana naye!”
“Na mimi pia.”
Ulikuwa utambulisho usio na furaha, ambao kila mmoja aliweza kugundua hilo, hivyo mazungumzo hayakuwa mengi sana, walikwenda kulala.
***
Usiku Vanessa aliamka kwa siri na kufungua mlango kisha akatoka nje, akiwa varandani, akaanza kupiga hatua za taratibu kuelekea kwenye mlango wa kuingia kwenye chumba cha Bruno.
Ni saa nane usiku!
Akagonga kwa hadhari, Bruno akafungua!
“Vipi usiku huu, kuna nini?” Bruno akauliza akitetemeka kwa hofu.
“Shiiiiiiii....” Vanessa akamnyamazisha.
Vanessa akaingia. Kwa Bruno alitamani kila kitu kiwe ndoto, lakini hilo halikuwezekana, ilibaki kuwa kweli, kwamba Vanessa ameingia chumbani kwake usiku huo, akimuacha mwanaume wake ambaye ni mkorofi! Hiyo ilikuwa ishara mbaya kwa Bruno, ambaye alianza kuona matatizo ya wazi kabisa mbele yake!
Papo hapo, kumbukumbu asizozipenda zikamrudia tena, kumbukumbu za Tunu, mwanamke wa Kitanga ambaye ndiye chanzo cha ulemavu aliokuwa nao.
“Vanessa rudi chumbani kwako!”
“Nyamaza Bruno, please tulia, Emma asije akasikia!”
“Kwanini unafanya hivi lakini?”
“Usijali, nina jambo la muhimu kidogo!”
“Jambo la muhimu?!”
“Ndiyo!”
“Kwanini tusizungumze kesho!”
“Hapana, nimechagua muda huu!” Akajibu Vanessa kwa kujiamini.
Bruno akapata wakati mgumu sana, hapo akagundua kuwa, Vanessa aliamua kumfanyia hivyo baada ya kuwa tayari yupo katika himaya yake, lakini hapo alipata picha ya wazi kwamba Vanessa alikuwa anampenda na ndiyo maana akamfanyia wema wote ule!
Yes, alimpenda!
Hakuwa mwanaume mjinga wa kiwango hicho, mwanaume asiyeweza kujua hisia za mwanamke. Kwanini amsaidie kiasi kile. Kwanini aoneshe uungwana zaidi kwake. Kwanini?
Hakuwa ndugu yake!
Hakuwa rafiki yake!
Nini basi kilimsukuma kumsaidia kwa kiwango kile? Hapo akapata jibu moja tu, mapenzi! Ni kweli yalikuwa mapenzi maana anajijua jinsi alivyo na mshawasha wa kimahaba. Lakini kichwani alikuwa na mawazo sana, yawezekana vipi yeye apendwe leo?
Haikuwa ajabu zamani zile, enzi za utanashati wake! Enzi za kuzungumza kwa sauti ya kuremba, sauti iliyonakshiwa na tungo na semi za kimjini! Haikuwa ajabu! Lakini si leo!
Akiwa mlemavu!
Asiye na kitu!
Apendwe?
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (12)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Akazidi kuchanganyikiwa. Vanessa alikuwa amemuacha mwanaume mtanashati zaidi yake chumbani, tena mwanaume wake wa kila siku ambaye ana wivu na anamwonesha mapenzi motomoto. Akamfuata yeye. Kwake bado alikuwa anahisi kama yupo ndotoni.
Alitakiwa kujiridhisha kama ni kweli hakuwa ndotoni. Akaketi kitandani, akajikongoja hadi kwenye switch ukutani. Akawasha taa! Macho yake yakakutana na umbo la mwanamke mrembo sana. Alikuwa ni Vanessa.
Vanessa usiku huo alikuwa amevalia gauni la kulalia, gauni jepesi ambalo liliweza kuonesha vizuri sana bikini yake iliyokuwa imeshikiliwa na mikanda midogo! Bruno akachachawa! Hapo akagundua kwamba kumbe Vanessa alikuwa mzuri zaidi ya vile alivyokuwa akifikiria.
Kwamba alikuwa akimwangalia kwa wasiwasi na huyu aliyepo mbele yake, alikuwa Vanessa halisi. Vanessa mrembo. Vanessa mwenye umbo namba nane. Vanessa mwenye rangi ya asili. Vanessa mwenye kiuno chembamba. Vanessa mwenye hipsi za kutosha. Vanessa mwenye miguu ya kuvutia.
Vanessa!
Alikuwa Vanessa original!
Moyo wake ukaenda kwa kasi sana, akaona kabisa jinsi ambavyo angekwenda kufanya kitu ambacho moyo wake haukuwa tayari. Aliona hatari hiyo. Haraka akabadilisha hisia zake, akamng’akia Vanessa...
“Vanessa ni hatari sana kuwa hapa muda huu, akija bwana’ko unadhani itakuwaje?”
“Najua Bruno, lakini miye nimekuja kwa ajili ya jambo moja tu!”
“Jambo gani?”
“Mh! Bwana, mbona unakuwa mkali hivyo? Twende polepole.”
“Nakuwa mkali kwasababu naona unataka kunisababishia matatizo!”
“Acha utoto, wewe ni mtu mzima sasa, unamwogopa nani? Kumbuka hapa ni kwangu, si kwa Emma!”
“Hata kama!”
“Sikiliza Bruno, kubali basi nilichojia!” Sauti ya Vanessa ilikuwa imepoa sana, lakini macho yake nayo yalitoa taswira nyingine mpya.
Vanessa alikuwa anataka penzi!
“Nini, sema basi!”
“Busu!”
“Busu?”
“Ndiyo nimekuja hapa kwa ajili ya kupata busu lako tu, tafadhali sana naomba unibusu, halafu nitaondoka!”
Maneno ya Vanessa yakamchanganya Bruno, ni muda mrefu sana hajambusu mwanamke. Kumbukumbu zake zilimwambia kwamba, mwanamke wa mwisho yeye kumbusu alikuwa ni Tunu, ambaye ndiye alikuwa mwanzo wa yeye kuanza kuwachukia sana wanawake. Leo hii anahisi afanye hivyo. Anaona anapoteza kitu muhimu sana.
“Busu tu!” Akatamka Bruno kwa haraka, lakini kinywa chake kikionekana kushindwa kuhimili vyema kutamka maneno yale.
“Yes, only kiss!”
“Haya sogea!”
“Sogea wewe!”
Wakabishana sana, kila mmoja akimtaka mwenzake asogee, lakini mwishowe, Vanessa akamsogelea, akapeleka shavu lake kwa Bruno, akambusu, baadaye naye akambusu. Wakanata kwa muda wakiangaliana, mara Vanessa akamvamia Bruno. Akaupeleka ulimi wake kinywani mwake.
Bila kutegemea, Bruno akaupokea. Wakaanza kunyonyana ndimi. Ni zoezi hilo ndilo lililosababisha wote kujikuta wameingia kwenye dimbwi la mapenzi. Emma akiwa chumbani kwa Vanessa. Hakujua yaliyokuwa yakifanyika chumbani kwa ‘Anko Bruno!’
***
Anatembea kwa hadhari kubwa sana kwenye korido, anaufikia mlango wa chumba chake. Vanessa akaganda kwa muda akimsikilizia Emma kama alikuwa ameamka! Kama ingekuwa hivyo, asingekuwa na ujanja, maana kama ni choo, kilikuwa chumbani!
Akafungua mlango taratibu sana, kisha akaubana kwa kitasa! Alivyokuwa anamalizia kufunga, akashtushwa na sauti ya Emma akikohoa. Alipogeuza shingo, akakutana na macho maangavu ya Emma!
Hofu tupu!
Emma akazidi kumwangalia Vanessa kwa macho yanayoonesha kwamba alishajua kila kitu. Vanessa akaingiwa na woga wa ghafla. Isingekuwa rahisi kujitetea.
Ametoka wapi?
Swali hilo lingetosha kumbana, maana hata nguo aliyokuwa amevaa ni ya kulalalia. Vanessa alikuwa na wakati mgumu sana wa kujitetea.
“Baby vipi?” Vanessa akajibaraguza.
“Nikuulize wewe!” Emma akajibu.
“Kivipi?”
“Kwani kuna nini?”
Vanessa akaketi kitandani kivivu, kisha baadaye akaamua kulala kabisa. Akamsogelea Emma na kumkumbatia! Kwa muda mfupi sana aliweza kugundua kwamba Emma alikuwa hajafahamu kinachoendelea!
“Ulienda wapi?”
“Toilet sweetie, kwani vipi?”
“Nothing, nilitaka kujua!”
“Poa!”
Emma hakujua kilichoendelea, lakini wasiwasi wa Vanessa ulianza kumtia mashaka kidogo. Alianza kuhisi kwamba kuna kitu kilichokuwa kikiendelea kimya kimya!
Kitu gani?
Hakujua!
Wakalala kila mmoja akiwa na lake kichwani, Vanessa akijipongeza kwa kumzidi akili Emma wakati Emma akiwa na mawazo kidogo kuhusu Vanessa. Mashaka yake yalisababishwa na hali ya ghafla aliyokuwa nayo Vanessa.
Hata kama ungekuwa ni wewe, lazima ungehisi kitu fulani kinaendelea.
“Ana nini?” Akawaza, lakini jibu bado lilikuwa gumu kupatikana.
***
Bruno alibaki na makovu moyoni mwake, hakuwa tayari kulala na Vanessa, lakini kwasababu ya ushawishi akajikuta ameingia kwenye mtego. Vanessa alipoondoka mle chumbani na Bruno kupata muda wa kutafakari zaidi, aliweza kugundua kwamba alifanya kitu cha hatari sana.
Alikuwa mlemavu, halafu anafanya vitu vya hatari kama vile, chumbani kwa mtu, tena mwenye mali akiwa chumbani kwake, lilikuwa kosa kubwa sana.
Kwa mara nyingine tena, Bruno akaingia kwenye kumbukumbu za mateso, kumbukumbu zile zile ambazo hapendi kuzikumbuka kila wakati.
Kumbukumbu za majonzi!
***
Alipoinua macho yake juu, akakutana na sura ngumu ya mwanaume huyu wa miraba minne. Alionekana dhahiri kutaka kufanya kitu kibaya sana. Mwanaume huyu ambaye hana huruma.
Mwanaume wa shoka!
Alikuwa ni Bryson!
Akayarudisha macho yake na kumwangalia mwanamke aliyekuwa naye chumbani. Mwanamke huyu alikuwa akilia sana miguuni mwa Bryson!
Alikuwa ni Tunu, ambaye alikuwa akilia chini ya miguu ya Bryson, akiomba asamehewe!
“Nisamehe mume wangu, ni shetani tu alinipitia!” Tunu akasema akilia.
Alikuwa akilia machozi, tena bila kutania. Bruno anajua vizuri sana adha ya kufumaniwa. Anajua vizuri sana hasira za wafumaniaji. Kwahiyo pale alikuwa amefumaniwa na mwenye mali, ambaye alionekana kuwa na hasira ambayo si ya kutafuta!
Bryson alikuwa amevimba!
“Samahani bro...” Bruno akaanza kujitetea.
“Samahani ya nini? Una nini cha kuniambia we’ mwanaharamu?!”
“Ninacho brother, ni vyema unisikilize kwanza.”
“Kwanza nafanya makosa sana kuzungumza na ninyi bila mashahidi. Ngoja kwanza nikachukue mashahidi ndiyo tuzungumze vizuri, lakini unatakiwa kufahamu, leo nitakufanya kitu kibaya sana ambacho hujawahi kufanyiwa katika maisha yako yote. Hilo nakuhakikishia!”
“Usifanye hivyo bro!”
“Pumbavu, nyamaza wewe. Mi’ naongea na wewe unaongea. Umekuwa nani? Nani wewe?” Bryson akafoka kwa hasira.
Ghafla akasimama na kuufuata mlango, kisha akaubamiza kwa nguvu, kabla ya kuufunga kwa kitasa!
“Lakini Tunu mbona hukuwahi kuniambia kama umeolewa?” Bruno akamwuliza Tunu akizidisha uoga.
“Nyamaza Bruno!”
“Ninyamaze kivipi? Unadhani huyo mumeo atanifanya nini hapa kama siyo kuniua?”
“Tunatakiwa kujadili tatizo, sio kulaumiana saa hizi!”
“Lakini kwanini unanisababishia matatizo ambayo si ya lazima?”
Tunu akakaa kimya.
Wakiwa wapo kwenye mabishano, wakasikia mlango ukifunguliwa, baadaye kidogo, sura za watu wanne zikatamalaki mle ndani. Sura hizi zilikuwa mbaya kuliko kawaida. Siyo ubaya wa sura wala mtazamo, ila zilikuwa sura ambazo zimejiandaa tayari kwa lolote!
Sura za kazi!
Walikuwa ni vijana watatu wakiongozwa na Bryson.
“Ndiyo huyu?” Mmoja wao akauliza.
“Ndiyo!” Bryson akajibu.
“Sasa bro, wanawake wote huko barabarani hukuwaona mpaka ukaona utembee na mke wa mshkaji wetu!”
“Siyo hivyo ndugu zangu, huyu hakuniambia kama ameolewa!”
“Hiyo ni hoja dhaifu sana kueleweka na kama unadhani utaeleweka, nataka kukuambia kwamba umeongea kitu cha kipumbavu kuliko kawaida,” akasema mmoja wa vijana wale.
“Kwanini?” Bruno akauliza akionekana kuwa na mashaka sana.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (13)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Hakusikia jibu lolote kutoka kwa mmoja wao zaidi ya kibao kikali kilichotua usoni mwake barabara!
“Mbona mnanipiga!”
“Fanyeni kazi...” Bryson akasema.
Muda huo huo, wakaanza kumvua nguo Bruno, wakiwa na nia ya kutaka kumfanyia mchezo mchafu! Walionekana kupania kweli kufanya upuuzi ule. Kwa lazima Bruno akajikuta amevuliwa nguo na alikuwa katika hatua za mwisho kabisa kabla ya kufanyiwa ufirauni!
“Wewe si umeona raha kutembea na mke wangu, sasa ngoja hawa jamaa nao wakufanyizie ili uwe na adabu na wake za watu!” Bryson akasema kwa hasira.
“Tafadhali, nipo tayari kutoa kiasi chochote cha fedha, msinifayie hivi jamani, nawaombeni sana.”
“Sema shilingi ngapi?” Bryson akauliza haraka akionekana ndicho kitu alichokuwa akikisubiria kwa hamu!
“Milioni moja!” Bruno akatamka kwa haraka, akitaka kujinasua katika mikono ya wanaume wale hatari.
“Unasemaje?” Bryson akauliza kwa dharau.
“Nitatoa milioni moja brother.”
“Wakubwa, endeleeni na zoezi lenu, naona huyu hajui mimi ni nani! Fanyeni kazi niliyowaitia,” Bryson akaagiza.
Wale vijana wakawa tayari kumkabili!
It’s not fair!
Bruno alikuwa akiingia katika historia mbaya zaidi kutokea katika maisha yake. Hakuwahi kufikiria kuingiliwa kinyume na maumbile, kwake yeye lingekuwa tukio ambalo lingeharibu kabisa taswira ya maisha yake.
Akawaangalia watu wale ambao hawakuonekana kuwa na huruma kabisa, ambao walikuwa wanavutana naye ili watimize lengo lao.
Tunu alikuwa akilia machozi, wakati akimuona Bruno akijitahidi kutumia nguvu zake zote kuhakikisha hawatimizi lengo lao. Vibao vilikuwa halali ya Bruno usoni mwake. Alilia sana, lakini hakuna aliyekuwa tayari kumsikiliza.
“Weee...unajifanya mjanja siyo? Nitakuua, nimekuambia nitakuua sasa hivi, acha kucheza na akili yangu wewe mjinga!” Bryson alifoka akivua mkanda wake kiunoni kwa ajili ya kumkabili zaidi Bruno.
“Mnanionea, mtaniua bure jamani!” Akasema Bruno lakini hakuna aliyemsikiliza.
Hakuna aliyetaka kupoteza muda wake kumsikiliza, mkanda ukatua mgongoni mwake na kumsababishia maumivu makali zaidi ya awali.
“Jamani mimi ni mwanaume mwenzenu, nawaombeni mniambie mnachohitaji ili muache kunitenda hivi,” alisema Bruno.
“Unatuambie sisi, kwani hujui uliyetembea na mkewe?” Mmoja wa wale vijana akasema.
Bruno akageuza uso wake na kumuangalia Bryson, macho yake yalikuwa yanatoa ujumbe mzito sana kwake. Hakutaka kufanya unyama ule. Ulikuwa unyama mbaya sana...
“Brother najua ni kiasi gani unaumia, najua nimefanya makosa, lakini naomba msinitende hivi, nipige faini yoyote nitalipa.”
“Milioni kumi unazo?!” Bryson akauliza akiwa hapepesi macho yake.
“Sitakuwa nayo kaka!”
“Una ngapi?”
“Naweza kupata milioni tano, nisaidieni tafadhali.”
“Milioni tano, haiwezekani.”
“Nisaidieni.”
“Mwisho saba, vinginevyo kazi iendelee.”
“Sina, ninazo tano.”
“Acha ujinga wewe, nitawaruhusu waendelee.”
“Hapana kaka, usifanye hivyo.”
“Haya sita.”
“Lakini sina zote kwa hapa, naweza kuwapa kwa awamu.”
“Kivipi?”
“Hapa nina milioni tatu, nitawakabidhi hapa hapa, halafu mbili twendeni kwenye ATM, halafu moja nikikusanya madeni kesho, nitamalizia.”
“Lakini kwanini ukaamua kutembea na mke wangu? Au ulikuwa unataka kupima watu?”
“Ndiyo maana naomba msamaha.”
“Sawa, nadhani nikubaliane na wewe kwakuwa umeomba sana, lakini unaweza kunitoroka na hizo tatu zilizobakia. Mimi ninayo kamera, kaeni hapo mkiwa watupu niwapige picha, hizi ndizo zitakazokufanya unilipe, ndiyo ushahidi wangu. Tukishalipana, nitazifuta. Kama upo tayari sema.”
“Sawa, nipo tayari,” Bruno akatamka haraka akiwa na shauku ya kuachiwa mikononi mwa wale watu wasio na huruma.
Muda ule ule, kamera ikatolewa na Tunu kulazimishwa kuvua nguo zote. Akavua. Bruno hakuwa na haja, maana tayari alikuwa mtupu.
Wakapigwa picha nyingi sana, kisha Bruno akatoa fedha mfukoni na kuanza kuhesabu hadi kufikia milioni tatu akamkabidhi Bryson.
“Ok! Sasa twende kwenye ATM tukamalizie nyingine ziliobakia.”
“Sawa.”
Bruno akavaa, wakatoka nje akiwa ameongozana na wale wanaume wanne na Bryson. Wakaingia kwenye gari na kwenda hadi kwenye mashine ya kutolea fedha.
“Ila jamani kama mnavyojua, mashine haiwezi kutoa zaidi ya milioni moja kwa siku!”
“Kwahiyo? Umeanza uswahili?”
“Hapana, ni hali halisi?”
“Kwahiyo unasemaje?”
“Nitachukua hizo milioni moja na kuwapatia, halafu ikifika saa sita kamili za usiku, turudi tena kuchukua nyingine.”
“Sawa.”
Wote wakakubaliana. Bruno akaingia kwenye mashine akiwa ameongozana na Bryson, akatoa fedha na kumkabidhi. Wakarudi kwenye gari na kuondoka zao. Safari yao iliishia Nguvumali kwenye moja ya baa maarufu, wakatafuta sehemu tulivu na kukaa pamoja.
“Tutakunywa hapa mpaka saa sita turudi kwenye ATM, usije ukajidanganya kwa kupiga kelele. Utakuwa umejiharibia mwenyewe. Nategemea sana utulivu wako kwa kila kitu.
“Kuwa huru kuagiza kitu chochote, ule utakavyo na unywe utakavyo. Hatutapenda kuona unafanya vurugu ya aina yoyote, ukijaribu tutakuua. Mimi nina roho mbaya kuliko unavyofikiria,” Bryson akasema kwa kumaanisha, maana ni kweli alikuwa hatanii katika kauli yake.
“Sawa.”
Mbuzi ikachomwa, kuku zikakaangwa na bia zikashuka mezani. Walikuwa wakipiga stori kama wote walikuwa marafiki. Bruno alipotaka kwenda chooni, alisindikizwa, hakwenda mwenyewe. Ilikuwa hivyo mpaka ilipofika saa 6:12 za usiku, ndipo Bryson alipogutuka.
“Oya muda tayari,” akasema akimtazama Bruno usoni.
“Twendeni,” mwingine akadakia.
Hakuna aliyeona umuhimu wa bia tena, wakaachana na vinywaji na kuingia kwenye gari na kwenda kuchukua zile pesa nyingine kwenye ATM. Hapo Bruno akaachiwa huru, akiamrishwa kupeleka mwenyewe milioni iliyobaki kesho yake.
“Ahsante sana kaka, nawashukuru sana,” Bruno akasema kwa woga.
Pesa kwake haikuwa kitu tena, kwa muda ule, thamani yake kama yeye ndiyo ilikuwa kitu cha kwanza.
“Ole wako usilete hiyo pesa!”
“Nitaleta.”
“Kumbuka picha zako tunazo.”
“Najua kaka.”
“Ok! Kesho,” Bryson akasema.
Bruno akaondoka muda ule ule, alikuwa akielekea gesti kutafuta mahali pa kulala, kichwani akiwa na mawazo yasiyo na kikomo.
***
“Nooooooooo....” Bruno akapiga kelele usiku huo, baada ya kukumbuka tukio lile ambalo si rahisi kufutika katika maisha yake.
Akiwa bado anaendelea kuwaza pale kitandani, akijilaumu kwa kufanya mapenzi na Vanessa, mchumba wa mtu, tena mwanaume wake akiwa pale nyumbani usiku ule, alisikia mlango wa chumba chake ukigongwa!
Taa za hatari zikawaka ubongoni mwake.
Msala!
Mshtuko alioupata Bruno, ulikuwa hauelezeki. Kwa vyovyote vile, alijua aliyekuwa anagonga mlango alikuwa ni Emma, mpenzi wake na Vanessa. Emma yule yule ambaye anasifika kwa ukorofi na ukali!
Emma ndiye anayegonga mlangoni.
“Anko...” sauti ya kiume ikasikika mlangoni.
Hapo akajua ni kweli alikuwa Emma anagonga...
“Vipi?” Bruno akaongea kivivu huku moyo ukimdunda kwa woga.
“Fungua...” Emma akasema kama anayeamrisha.
Moyo wa Bruno ukaongeza kasi, akili yake ikajua kwa vyovyote vile kulikuwa na hatari iliyokuwa inakuja mbele yake. Hatari ambayo kwa hakika hakutamani kabisa. Lakini hakuwa na jinsi, tayari alikuwa ndani ya nyumba ya watu, akawa tayari kwa lolote.
“Nakuja,” akajibu tena, safari hii akijitahidi kushusha mguu mmoja chini na kuchukua gongo linalomsaidia kutembea na kujivuta mlangoni.
Akafungua mlango akitweta na kutetemeka kwa woga. Akakutana na uso wa Emma, ambaye hakuwa na maswali zaidi ya kuonesha ishara kwamba anataka kuingia ndani. Bruno akampisha. Emma akaingia na kuketi kwenye kiti pekee kilichokuwa ndani.
Uso wake ulionekana kusema jambo, lakini hakuweza kulitoa moja kwa moja. Akamtulizia macho usoni kama anayejifunza jambo fulani. Bruno akaketi kitandani kimya akionekana kuwa na wasiwasi kidogo
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (14)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

Emma akavuta pumzi ndefu sana kisha akazishusha taratibu kabisa...kinywa chake kikaonekana kuanza kutingishika na kuonekana dhahiri alitaka kuongea lakini hakuwa na hiyari ya maneno gani ayatoe kinywani mwake.
“Pole sana,” akaponyokwa na maneno yale, akionekana kama anawaza kukosea kutoa maneno yale.
Bruno hakujua pole ilikuwa ya nini, kwahiyo alibaki kimya akimtazama, lakini baadaye akaamua kuonesha ushirikiano ingawa hakujua pole ilikuwa ya nini, akaamua kuitikia kwa kutingisha kichwa!
“Pole sana Anko!”
“Samahani...pole ni ya nini?” Kwa mara ya kwanza Bruno alitamka maneno hayo.
“Nimesikia kama umepiga kelele?”
“Mimi?”
“Ndiyo!”
“Umesikia vibaya!”
“Hapana...nimesikia vizuri sana ukipiga kelele, ukisema nooooo....nikashindwa kuelewa ni kwanini, lakini nilihisi labda maumivu ya mguu yanakusumbua!”
Bruno akahema kwa kasi tena, angalau sasa alishajua ni kwanini alikuwa anapewa pole, maana mwanzoni alikuwa njia panda, kwasababu hakujua ni sababu gani hasa iliyomfanya ampe pole.
“Ni kweli, nilikuwa kwenye mawazo, kwenye kumbukumbu za hatari, nikajikuta nimepiga kelele!”
“Pole sana Anko!”
“Nashukuru.”
“Ni kumbukumbu za nini?”
“Acha tu Anko wangu, siku nikiwa na muda nitakusimulia, kwasasa nenda kapumzike!”
“Ok! Usiku mwema.”
“Nawe pia.”
Emma akatoka na kumuacha Bruno mwenyewe ndani, akaamka haraka na kwenda kufunga mlango, akarudi kitandani akiwa anahema. Haamini kilichotokea. Kwamba Emma hakugundua kwamba muda mfupi uliopita, alilala na mpenzi wake. Kwamba yeye si mjomba wa Vanessa bali ni rafiki tu!
Rafiki ambaye tayari mchezo wa hatari umeshaanza!
Akajichukia ghafla!
Akavuta shuka na kujitahidi kuusaka usingizi. Haikuwa kazi ndogo, lakini hatimaye akafanikiwa kupata usingizi. Akalala fofofo.
***
Asubuhi na mapema Emma aliamka na kwenda zake kwenye mihangaiko yake, akamuacha Vanessa kitandani mwenyewe. Ilikuwa asubuhi ya saa kumi na mbili! Mapema kabisa, kabla nuru haijalinyang’anya giza nafasi.
Vanessa akachepuka haraka na kwenda mlangoni kwa Bruno, akamgongea. Bruno akashtuka sana, akajua lazima alikuwa ni Emma amemfuata tena. Moyo wake ukapiga kambi kwa mshtuko!
“Nimepatikana...” akawaza akifungua mlango.
Tofauti na matarajio yake, mlango ulipofunguka, akakutana na uso wa Vanessa ukiwa umeachia tabasamu la nguvu! Hakusubiri kukaribishwa, akaingia mwenyewe na kujitupa kitandani. Alikuwa na upande mmoja wa kanga, kwahiyo aliuvua na kubaki mtupu! Akawa anamwangalia Bruno kwa macho yanayosema.
Macho yalikuwa yanazungumza jambo moja tamu; kwamba anahitaji mapenzi. Bruno akaogopa sana. Hakuwa tayari kufanya kitu chochote.
“No! No! No!”
“Acha ujinga Bruno, njoo bwana!”
“Sitaki!”
“Please naomba uje, Emma ameshaondoka!”
“Lakini sijapendezwa na hii tabia yako!”
“Usiwe hivyo bwana!”
“Sikia, mimi ni kweli nina shida, lakini huwezi kunifanyia hivi.”
“Vipi?”
“Utumwa! Unataka kunifanya mimi mtumwa wako wa mapenzi.”
“Sijasema hivyo, mimi nina mapenzi ya dhati kwako!”
“Hata kama, lakini wewe una mwanaume wako.”
“Ni kweli lakini hapa ni kwangu, au hujui?”
“Hata kama Vanessa, mimi sitaki!”
“Bruno kweli hutaki kuthamini yote niliyokufanyia?”
“Lakini si kwa njia hii, huku ni kuninyanyasa.”
“Nimekwambia ni mapenzi tu, si manyanyaso.”
“Hapana Vanessa.”
“Mimi nina nia njema na wewe, nataka kubadilisha maisha yako.”
Bruno akakaa kimya kwa muda akimsikiliza...
“Najua maisha yako yameshabadilika, nataka kukusaidia kukunyanyua tena. Kwanza kabisa nitahakikisha unapata mguu wa bandia, mzuri ambao utakusaidia kuachana na gongo kabisa!”
Zilikuwa habari njema kwa Bruno, akaendelea kuwa kimya akimpa nafasi Vanessa aendelee kuzungumza.
“Tena kama huamini, sema wiki ijayo nikupeleke India, ukirudi hapa unatembea mwenyewe na nitahakikisha nakupa mtaji wa kufanya biashara. Nataka uweze kujitegemea tena. Yote haya ni kwasababu nakupenda.”
“Kweli Vanessa?” Bruno akaponyokwa na maneno hayo akiwa ameyatuliza macho yake usoni mwa Vanessa.
“Sijawahi kukudanganya Bruno!” Vanessa akasema akimsogelea Bruno.
Hakuhitaji kupewa ruhusu tena!
Hakuhitaji kukubaliwa!
Macho ya Bruno yaliongea wazi wazi...yalikuwa yanasema, nimekubali! Kwa mara nyingine tena, wakazama kwenye dimbwi la mahaba mazito. Bruno alikubali kufanya yote hayo kwa ajili ya maisha yake, alitamani sana siku moja atembee tena.
Ndoto ambayo ilikuwa inanukia!
Vanessa alijisikia mshindi maana alijua wazi kwamba, kwa ahadi aliyoitoa Bruno asingeweza kuchomoka kabisa. Akamsogelea akiwa anahema kwa kasi, Bruno akawa hana hiyari tena na kitu chochote.
Vanessa akamkalisha Bruno kitandani, kisha akayatuliza macho yake usoni mwake, akatabasamu. Bruno akawa anaangalia kwa macho yaliyojaa huruma, alikuwa ndani ya penzi la kitumwa, maana ndani ya moyo wake hapakuwa na alama yoyote ya mapenzi kwa Vanessa.
Ni kwa vile hakuwa na ujanja wa kufanya jambo lolote, lakini ukweli ni kwamba hakuhisi kumpenda Vanessa. Akamwangalia kwa jicho la kuhoji kitu; Vanessa akagundua kwamba Bruno alikuwa na mashaka na jambo fulani au alikuwa anataka kuuliza kitu lakini akawa anasita.
“Sema Bruno, nahisi kama kuna kitu unataka kuniuliza ni kweli?”
“Ndiyo!”
“Hebu niambie ni nini?”
“Nataka kufahamu nia yako hasa kwangu ni nini?”
“Mapenzi Bruno!”
“Halafu?”
“Sijakuelewa.”
“Mapenzi ya aina gani?”
“Nataka kufunga ndoa na wewe!”
“Haiwezekani!”
“Kwanini?”
“Sababu zipo mbili, kwanza wewe una mchumba wako Emma, na mimi nina mke wangu yupo Mwanza!”
“Una mke?”
“Ndiyo!”
“Umefunga naye ndoa?”
“Hapana, ila nimezaa naye watoto wawili!”
“Sasa kumbe hujafunga naye ndoa, wasiwasi wako wa nini? Unashindwa vipi kuoana na mimi wakati hata ndoa bado hamjafunga?”
“Basi tu!”
“Kwanini?”
“Na Emma?!”
“Kwani nimefunga naye ndoa? Emma yupo chini yangu, hana ujanja wowote kwangu, mimi ndiye ninayemlea kwa kila kitu. Kumbuka hapa ni kwangu, hana uwezo wa kufanya lolote.”
“Thubutu! Na ukorofi wake wote ule? Siamini kabisa!”
“Hayo ya Emma achana nayo, jambo la msingi ni kuangalia moyo wako! Kwani wewe unaonaje, unanipenda?”
Bruno akakaa kimya!
“Unanipenda Bruno?”
“Nakupenda ndiyo!”
“Sasa wasiwasi wa nini?”
Bruno akabaki kimya!
“Kama ni kweli unanipenda, hayo mengine yaache kama yalivyo, we’ angalia mapenzi, kila kitu kitakuwa juu yangu!”
“Vipi kuhusu mguu?!”
“Wiki ijayo twende India.”
“Sawa, nitashukuru sana.”
Vanessa akamsogelea Bruno kisha akamwonesha ishara apande kitandani. Bruno akafanya hivyo, kilichofauta baada ya hapo ilikuwa kazi nzito sana iliyowafanya wote wawe hoi baadaye.
WIKI MBILI BAADAYE
Mambo hayakuwa mepesi kama Vanessa alivyokuwa akifikiria mwanzoni, alitarajia kusafiri na Bruno baada ya wiki moja, lakini hilo halikuwezekana. Utaratibu wa hospitali aliyokuwa anakwenda ulikuwa wa tofauti kidogo.
Kwanza aliwasiliana na Uongozi wa Hospitali ambayo ingemshughulikia Bruno, baadaye akaunganishwa na daktari wake ambaye alisema alikuwa na wateja wengi, hivyo akawataka waende baada ya wiki mbili.
Maandalizi yote yalikuwa tayari, Emma alipewa taarifa kwamba ‘mjomba’ wake na Vanessa alikuwa anapelekwa India kwa ajili ya kuwekewa mguu wa bandia, hakupinga!
“Nawatakieni safari njema.”
“Tunashukuru sana Anko, ubaki salama!”
“Ahsante sana, nawaombea kila lililo jema!”
“Tunashukuru!”
Emma akawasindikiza hadi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, wakaagana kwa mara nyingine tena. Bruno akatembea kwa kutumia gongo lake akimfuata vanessa aliyekuwa ametangulia.
Wakaingia kwenye sehemu yenye maandishi yaliyosomeka WANAOONDOKA. Vanessa akageuka nyuma na kumpungia Emma.
Wakaingia.
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (15)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

***
Baada ya saa kadhaa angani, ndege waliyokuwa wakisafiria ilitua kwenye ardhi ya nchi ya India jijini New Delhi. Kila kitu kilikuwa kimeshapangwa! Walipokuwa wakitoka waliona bango kubwa lililoandikwa kwa maandishi makubwa; BRUNO AND VANESSA FROM TANZANIA, YOU ARE WELCOME TO INDIA.
Lilikuwa bango lilibebwa na wahudumu wawili wa Hospitali wanayofikia kwa ajili ya matibabu. Vanessa na Bruno wakawafuata watu hao. Nao walivyowaona, Bruno akiwa akiwa anatembea na gongo, waliweza kugundua kilichoendelea. Walijua ndiyo wageni wao.
“Hello, I hope you are from IPRO Hospital!” (Habari, naamini mnatoka Hospitali ya IPRO!) Vanessa akauliza alipowafikia.
“We are fine! Yes, we are coming from there. Are you Vanessa and Bruno?” (Hatujambo! Ndiyo tunatokea kwenye hospitali hiyo. Ninyi ndiyo Vanessa na Bruno?) Mmoja wao akauliza.
“Yeah!” (Ndiyo!)
“You are all welcome to New Delhi!” (Karibuni sana New Nelhi)
“Thank you!” (Ahsante) Vanessa akaitikia.
Baada ya hapo wakandoka na kwenda kuingia kwenye gari lililoandikwa IPRO HOSPITAL tayari kwa safari ya kwenda hospitalini. Kila kitu kwa Bruno kilikuwa kipya, alihisi kama yupo kwenye ndoto ndefu sana ya kupendeza, lakini haikuwa hivyo!
Ilikuwa kweli, kwamba yupo India kwa ajili ya kuwekewa mguu wa bandia!
Furaha kiasi gani?
Kila kitu kilikuwa kipya kabisa kwa Bruno, ambaye alikuwa ametulia kimya kwenye kiti akitazama nje, akijionea mandhari ya mji ule. Hakuamini kama kweli siku chache baadaye alikuwa akienda kutupa gongo na kutembea kwa miguu yake mwenyewe kama zamani.
Hilo lilimpa furaha sana, hapo akaona jinsi Vanessa alivyokuwa na mapenzi ya kweli kwake. Si jambo jepesi hakika atokee mtu wa kukusaidia katika kiwango kile. Bruno alikuwa na furaha sana.
“Mh! Vanessa,” Bruno akaita.
“Bee!”
“Ahsante sana!”
“Nini tena?”
“Ahsante kwa kila kitu Vanessa, sasa ndiyo naamini kwamba nakwenda kutembea tena.”
“Unatakiwa kuendelea kuamini hivyo Bruno, nimeshajitoa kwa ajili yako mpenzi, amini kwamba nakupenda ndiyo maana nafanya yote haya kwa ajili yako!”
“Nashukuru sana Vanessa, ahsante sana.”
“Usijali dear!”
Safari ikaendelea hadi walipoingia katika geti la hospitali ile, iliyokuwa na mandhari nzuri ya kuvutia. Nje ya hospitali hiyo kulikuwa na bango kubwa lililoandikwa IPRO HOSPITAL, gari likaingia na kwenda kwenye maegesho, likaegesha.
Mlango ukafunguka wenyewe!
“Karibuni sana!” Mmoja wa wahudumu wale akasema kwa lugha ya Kiingereza.
“Tunashukuru sana.”
“Nifuateni.”
“Ok!”
Wakaanza kumfuata Mhudumu yule aliyekuwa akikatiza kwenye barabara ndogo zilizozungukwa na maua mazuri ya kuvutia. Walipita ofisi nyingi, baadaye wakaingia kwenye mlango mmoja wa kioo.
Macho yao yakakutana na daktari mwenye asili Japan, akiwa ameketi kimya kitini. Alipowaona akaachia tabasamu.
“Karibuni sana!” Akawakaribisha.
“Ahsante sana,” wote wakaitikia.
“Dokta, hawa ndiyo wageni wetu kutoka Tanzania,” yule Mhudumu aliyewaleta akasema.
“Ok! Nashukuru sana, nilijua ndiyo hawa...habari za Tanzania?” Daktari yule aliyejitambulisha kwa jina la Dk. Lives aliuliza akitabasamu.
“Tanzania ni kama unavyotuona, tuna shida dokta,” Vanessa akajibu kwa unyonge.
“Hapana usijali, huna sababu ya kuwa mnyonge kiasi hicho dada yangu, mgonjwa wako anakwenda kutupa gongo muda si mrefu sana. Mmeshafika hospitalini sasa, hapa ndiyo sehemu pekee itakayomrejeshea ndugu yako furaha yake!”
“Nashukuru kusikia hivyo!”
“Ok! Kama tulivyoongea kwenye simu, kila kitu kipo tayari, tumeshakuandalia sehemu ya kufikia, kwahiyo ondoa shaka. Huyu mgonjwa mwache hapa, taratibu nyingine zitaendelea. Kesho kutwa asubuhi asubuhi utakuja kuchukuliwa hotelini, kazi ikiwa imeshakamilika!” Dk. Lives akasema.
“Sawa.”
“Ok! Sabina, mpeleke hotelini tafadhali, hakikisha mnampatia huduma nzuri.”
“Bila shaka dokta!”
Sabina akaongozana na Vanessa hadi kwenye gari lile lile walilokuja nalo kutoka uwanja wa ndege. Wakaingia, dakika moja baadaye, dereva alifika na kuwapeleka hotelini. Hoteli haikuwa mbali sana na Hospitali, hivyo mwendo wa robo saa tu baadaye gari lilikuwa linaingia kwenye geti lililoandikwa HOTEL IPRO.
Wakashuka na kuongozana pamoja hadi Mapokezi. Vanessa akatambulishwa kama mteja wao aliyefika na mgonjwa wake hospitalini. Akapewa chumba kizuri na huduma zote.
***
“Room no. 207 ghorofa ya nane!” Ndivyo Vanessa alivyosema mara baada ya kupokea simu iliyokuwa chumbani kwake, iliyoita kwa muda mrefu.
“Ndiyo nimepiga hapo kutoka Mapokezi, naitwa Martinah, habari za asubuhi?”
“Salama, naomba nikusaidie!”
“Ok! Nilipenda kujua utapenda tukuandalie nini kama kifungua kinywa chako kwa leo?”
“Mh! Mbona leo mmenipigia mapema sana? Ni saa moja kasoro za asubuhi sasa, bado nimelala. Sijajua bado.”
“Nafahamu, lakini saa 3:00 utakuja kuchukuliwa na wahudumu wa Hospitalini ukamuone mgonjwa wako!”
“Ok! Sasa nimekuelewa, kuhusu kifungua kinywa, niandalieni maziwa fresh na mayai ya kukaanga!”
“Utapenda kawaha au majani?”
“Majani!”
“Robo saa ijayo, vitakuwa chumbani mwako.”
“Nitashukuru sana.”
Kama alivyoahidiwa ndivyo ilivyokuwa, robo saa baadaye Mhudumu alifika chumbani mwake na kumpelekea kifungua kinywa. Tayari alikuwa ameshaoga, hivyo aliingia mezani na kuanza kula.
Saa 3:00 za asubuhi alipigiwa simu, gari la Hospitalini lilikuwa limeshafika. Akatoka na kwenda kwenye lifti, akaingia na kushuka hadi chini. Akaingia kwenye gari na kupelekwa Hospitalini.
***
“Kila kitu kimeshakamilika, kilichobaki kwasasa ni mazoezi tu. Nitakuruhusu uende naye Hotelini, lakini kila siku asubuhi atafuatwa na kuletwa hapa kwa ajili ya mazoezi yatakayomchukua wiki moja, kabla ya kuwaruhusu mrudi Tanzania!” Dk. Lives alimwambia Vanessa muda mfupi baada ya kuingia ofisini kwake.
Mbele yake alikuwa ameketi Bruno akiwa hana gongo tena! Furaha aliyokuwa nayo ikamfanya ashindwe kudhibiti machozi yake. Bruno akaanza kulia.
“Usilie Bruno, hongera sana...nyamaza tafadhali!” Vanessa akajitahidi kumtuliza.
“Siamini Vanessa, siamini kabisa kama ni kweli nimepona!”
“Nimeshakuambia usijali, kila kitu kinawezekana, tulia Bruno!”
Bruno akanyamaza, Vanessa akamgeukia dokta na kumwambia:
“Ana furaha, haamini kama angeweza kutembea tena.”
“Ni kawaida, lazima awe katika hali hiyo, lakini msijali!”
“Tunashukuru sana Dokta, nadhani sisi sasa twende.”
“Sawa, pole sana Bruno.”
“Ahsante dokta.”
Bruno na Vanessa wakatoka, Bruno akitembea mwenyewe, ingawa bado alikuwa akichechemea, lakini angalau alikuwa na mguu wake bandia.
Ilikuwa siku mpya kwa Bruno.
Vanessa akamshika mkono na taratibu wakaongozana hadi kwenye gari aina ya Toyota Hiace iliyoandikwa kwa maandishi makubwa ubavuni, IPRO HOTEL, wakaingia na kuketi vitini. Bado Bruno alionekana kujawa na mawazo sana kichwani mwake.
“Usiwaze sana!” Vanessa akasema.
“Nashindwa kujizuia!”
“Najua, lakini usiruhusu sana!”
“Nimekuelewa!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Lakini kwanini unakuwa hutaki kukubaliana na kilichotokea?”
“Nahisi ni kama maumivu yaliyo ndani ya furaha, unajua si rahisi kuamini kilichotokea, lakini ndiyo hivyo tena sina namna lazima nikubaliane nalo. Ahsante sana Vanessa, nakushukuru sana!”
“Usijali mpenzi wangu, lazima ufahamu kwamba nimefanya yote hayo kwasababu ya penzi langu la dhati lililojificha moyoni mwangu, nashukuru kwa utambuzi huo, naomba nikushukuru sana Bruno kwa namna ambavyo wewe unaona thamani hiyo!”
“Usijali Vanessa, sasa naamini kuwa unanipenda mpenzi!”
“Siku zote hizo, ulikuwa hujui?”
“Nilijua, lakini leo imethibitika zaidi!”
Gari liliondoka Hospitalini pale kwa mwendo wa taratibu hadi Hotelini ambapo wote walishuka na kuingia kwenye lifti kisha wakaenda zao chumbani kwao.
Walizungumza mengi sana, lakini kubwa zaidi ilikuwa ni juu ya mapenzi yao na jinsi ambavyo Bruno aliachana na gongo na kutembea mwenyewe!
 
RIWAYA: SIKUJUA UNGENISALITI MPENZI (16)
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
SIMU: 0762 458590
EMAIL: joeshaluwa@gmail.com
FACEBOOK: Joseph Shaluwa
INSTAGRAM: josephshaluwa

***
Ilikuwa siku ya sita ya mazoezi ya Bruno, ikiwa ni siku moja kabla ya kumaliza mazoezi Hospitalini hapo na kuanza safari ya kurejea Tanzania. Tayari Bruno alishaanza kuzoea kutembea na mguu wake bila kuchechemea.
Hakuamini kama mguu ule wa bandia angeweza kuuzoea na kutembelea kama wake. Yalikuwa maendeleo makubwa sana kwa Bruno.
Bado Vanessa alikuwa akiteswa na vitu vingi sana kichwani mwake, kwanza aliwaza kuhusu mjomba wake Bryson, kwanini alikuwa anasema alikuwa mbaya kwake, pia kitu kingine kilichokuwa kikiutesa zaidi ubongo wake ni Tunu, kwanini alikuwa akimtaja kama mwanamke mbaya katika masha yake?
Akapanga lazima azungumze naye ili aweze kumweleza ukweli halisi...
Alikuwa na maendeleo mazuri sana katika mazoezi, aliendelea vizuri sana na uwezo wake ulishakuwa mkubwa kabisa wa kutembea mwenyewe. Vanessa hakutaka kukubali kuendelea kuwaza mambo ambayo hayajui kichwani mwake, ilikuwa lazima aulize ili aweze kuujua ukweli.
“Kuna kitu kinanichanganya sana Bruno, natakiwa kuzungumza na wewe,” Vanessa akamwambia Bruno ambaye alipigwa na butwaa na kauli hiyo.
“Ni nini hicho? Unaweza kuniambia tu!”
“Usinifikirie vibaya Bruno, nataka tu, kufahamu ukweli.”
“Sawa, nakusikiliza!”
“Nataka kujua mambo mawili!”
“Ni mambo gani hayo?”
“Kwanza ni kuhusu Anko Bryson, halafu nataka pia kujua kuhusu Tunu!”
“Hatuwezi kuzungumza siku nyingine?”
“Nahisi leo ni siku nzuri zaidi.”
“Bryson ni mtu mbaya sana kwangu!”
“Sawa, ulishaniambia!”
“Hata Tunu pia...”
“Najua, lakini sijafahamu sababu bado.”
“Lakini nahisi kama hapa si mahali sahihi sana pa kuzungumza.”
“Hapana Bruno, nakuomba sana kama ni kweli unanipenda, niambie ili niweze kujua ukweli.”
“Lakini ni kumbukumbu za majonzi sana, ambazo huwa sipendi kuzikumbuka kila wakati.”
“Najua, lakini naona kama zitazidi kukutesa kila siku kichwani mwako, kwanini usiniambie tu mpenzi wangu?”
“Hapana!”
“Au hunipendi?”
“Nakupenda sana Vanessa, tayari nimeshatoa moyo wangu kwa ajili yako!”
“Please naomba uniambie basi.”
Bruno alikaa kimya akionekana kuanza kukumbuka kila kitu juu ya watu hao wawili, alionekana kuwa na mambo ya kuumiza sana aliyofanyiwa na Tunu pamoja na Bryson, kimya cha dakika mbili kilipita wakiwa pale bustanini, lakini baadaye akaanza kuzungumza...
“Mimi ni Msukuma, kwetu ni Mwanza. Nilikuwa nafanya kazi katika Kampuni ya Sangara Distributors ya jijini Mwanza, kama Afisa Mauzo. Kazi yangu ilikuwa kusafiri na gari lenye samaki wa maji baridi na kupeleka Kanda ya Kaskazini, nikimaanisha, Manyara Arusha, Kilimanjaro na Tanga.
“Nilikuwa msimamizi wa kila kitu katika gari. Tulishusha mizigo kila mkoa na mimi ndiye niliyekuwa nabaki na mauzo yote. Nyumbani Mwanza nina mke, ingawa sijafunga naye ndoa, lakini nimezaa naye watoto wawili kama nilivyokuambia awali ambao tunaishi nao katika nyumba ya kampuni.
“Bosi wangu alikuwa ananipenda sana na alikuwa akinipa kila kitu. Nilifanya kazi kwa uaminifu mkubwa, nikipata mshahara mzuri na marupurupu ya kutosha, lakini siku moja tu, ndiyo iliyoharibu kila kitu katika maisha yangu. Ni siku ambayo nilikutana na Tunu. Siku hiyo nilikwa nimekaa na marafiki zangu kwenye baa moja huko Tanga, tukiwa tunakunywa na kuendelea na stori za hapa na pale.
“Nikamuona Tunu...ni kweli nilihisi kumpenda, lakini hata yeye alionekana kuvutiwa na mimi na kusema kweli yeye ndiye aliyenitongoza. Nikazungumza naye na kumwambia nimekubaliana na ombi lake, lakini nilisisitiza kumuuliza kama hana mume, akasema hana!
“Basi nikaenda nyumbani kwake, nikalala naye kwa siku mbili mfululizo, usikuwa wake, akaja mwanaume mmoja ambaye ndiye huyo mjomba wako Bryson, akasema ni mume wake. Nikapigwa, nikaumizwa sana na baadaye nikapigwa picha akiwa na vijana wengine wahuni. Ili mambo yaishe, nikakubaliana nao niwape shilingi milioni sita!
“Kwanza nikawapa milioni tatu, baadaye nikaenda kutoa milioni moja kwenye ATM kisha tukasubiri hadi saa sita usiku nikaenda kuchukua milioni nyingine moja na kuwapatia kwa ahadi ya kuwapatia milioni moja asubuhi baada ya kukusanya madeni kwa wateja wangu!” Alisema Bruno akionekana kuwa na huzuni sana.
“Enhee ikawaje?”
“Kweli asubuhi yake nikakusanya madeni na kupata ile milioni moja, nikawa nawatafuta ili niwapatie ili picha zangu zisisambazwe, nikagundua kitu cha ajabu sana. Sikuamini kabisa!” Akasema Bruno huzuni yake ikizidi kuongezeka.
“Uligundua nini?”
“MJOMBA WAKO NI TAPELI, TUNU HAKUWA MKEWE ILA WALIAMUA KUNITAPELI YEYE NA TUNU! KILA KITU NILIELEZWA, HAPO UKAWA MWANZO WA KUPATA ULEMAVU!”
“Kivipi?” Vanessa akauliza akionekana kuwa na shauku ya kutaka kujua.
Bruno hakuweza kuongea kitu tena, zaidi ya machozi machoni mwake kuanza kuchuruzika kama maji ya mfereji!
***
Bruno alidamkia sokoni kwa ajili ya kudai madeni ya wateja wake aliowauzia samaki. Hazikuwa fedha zake, lakini alitaka kwanza amalize matatizo katika mkoa wa watu ili awe huru. Tayari aliamini kwamba alikuwa ameshajifunza kutokana na kosa alilolifanya!
Hakutamani kabisa, picha zake za utupu zisambazwe! Angeficha wapi uso wake? Angemweleza nini mkewe? Vipi kuhusu wazazi wake na marafiki zake? Alikuwa katika wakati mgumu sana.
Haikuwa kazi kubwa kupata milioni moja aliyokuwa anaihitaji! Hadi kufikia saa 4:00 za asubuhi tayari alikuwa na milioni kibindoni! Akakodisha taxi na kwenda zake mitaa ya Sahare, ambapo Bryson alimwelekeza azipeleke hizo fedha.
Hakuwa mwenyeji wa mitaa hiyo, kwahiyo alipoona salon moja ya kiume jirani na eneo aliloelekezwa...
“Paki hapo kaka!”
“Wapi?”
“Mbele ya hiyo salon hapo!”
“Poa.”
Dereva akapunguza mwendo na kuegesha sehemu aliyoelekezwa. Akashuka na kupiga hatua za taratibu kwenda kwenye ile salon, akaingia ndani.
“Mambo vipi washkaji?” Bruno akasalimia.
“Poa mwana, shwari?” Kinyozi wa pale akaitikia.
“Poa.”
“Sema, karibu kiti mkubwa!”
“Siyo mkaaji, ila kuna mshkaji mmoja namwulizia, alinielekeza mitaa hii!”
“Anaitwa nani?”
“Bryson!”
“Bryson?!!!” Sauti za watu wawili zikasikika na wote wakamkazia macho kwa mshangao!
Bryson anajulikana mtaa mzima kwa tabia zake za utapeli, si mwaminifu na mara zote amekuwa akifanya utapeli hata kwa watu wa mtaani kwao kabisa.
Kumtaja jina lake, kulikuwa na maana mbili; ama ameshatapeliwa au anamtafuta kwa ajili ya mazungumzo ambayo mwisho wake ungekuwa utapeli.
“Mbona mmeshtuka washkaji?” Bruno akawauliza, tayari kichwani mwake alishaanza kuingiwa na mashaka kidogo.
“Ni ndugu yako?” Mmoja akamwuliza.
“Hapana!”
“Unamtafutia nini?”
“Nina ishu naye muhimu, kwani vipi washkaji, mbona mnanitisha jamani?”
“Siyo tunakutisha, tunataka kujua ili baadaye tusilaumiane.”
“Tulaumiane kwa lipi tena? Mimi namuulizia tu ndugu zangu, mambo mengine nitajua mwenyewe!”
“Poa, hesabu nyumba tatu kutoka hii, mkono wako wa kushoto, utaona nyumba yenye geti jekundu, ni hapo!”
“Ok! Poa wakubwa, ahsanteni sana.”
“Hamna noma!”
Bruno akatoka kwa mwendo wa taratibu sana, akionekana kuanza kuingiwa na mashaka kidogo na akina Bryson. Huku nyuma aliacha mzozo...
“Washkaji, yule jamaa atakuwa anakwenda kulizwa, kwanini tusimsaidie?” Dulla akawaambia wenzake.
“Unamjua Bryson au unamsikia?”
“Atajuaje?”
“Kama wewe mwema sana, nenda kamsaidie bwana!”
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom