...au itamkubatia fisadi na kuthibitisha kwamba chama hicho ni chama cha mafisadi? Tutege sikio
Nape Vs Lowassa
na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
SUALA la utata katika mradi wa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), ni miongoni mwa ajenda zinazotarajiwa kuwasha moto mkali wa hoja wakati wa kikao cha Kamati Kuu ya CCM, kinachokutana jijini Dar es Salaam leo.
Kikao hicho kitakachokuwa chini ya Uenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete, pamoja na mambo mengine kinakusudia kupitia mkataba wa mradi huo ambao katika siku za hivi karibuni, umezua maneno mengi ndani ya chama hicho tawala.
Kuibuka kwa mjadala huo kulianzishwa na kada wa chama hicho, Nape Nnauye, ambaye ni mmoja wa vijana wanaogombea nafasi nyeti ya mwenyekiti wa UVCCM, ambayo kihistoria imekuwa ikiibua ushindani mkali.
Kwa mara ya kwanza Nape alitoa hoja yake hiyo saa chache tu baada ya kuchukua fomu za kugombea nafasi hiyo inayompa fursa mshindi ya kuwa mjumbe wa vikao vya kimaaamuzi vyenye nguvu kubwa ndani ya chama hicho tawala, Kamati Kuu (CC) na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC).
Katika madai yake, Nape alimshutumu moja kwa moja Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa umoja huo, Edward Lowassa na viongozi wengine wa juu wa UVCCM kwa kuingia katika mkataba huo ambao alisema hauna masilahi yoyote ya maana kwa umoja huo.
Tangu Nape atoe tuhuma hizo, hali ya mambo ndani ya CCM na hususan katika UVCCM imekuwa ni ya vuta nikuvute, ikiwagawa viongozi waandamizi ndani ya chama hicho tawala katika makundi mawili.
Kundi la kwanza ni lile linalomuunga mkono Nape, likijumuisha wakongwe kadhaa wa siasa za CCM (majina tunayo), ambao wanakiona kitendo cha mwanasiasa huyo kijana kuwa ni cha kijasiri na ambacho kinapaswa kuungwa mkono na kila mwanachama wa chama hicho.
Miongoni mwa watu wanaomuunga mkono Nape katika siku za hivi karibuni wanadaiwa kuwa wamekuwa wakifanya kila linalowezekana ili kuhakikisha kwamba; ‘kijana wao' huyo anashinda uteuzi wa uenyekiti wa UVCCM kwa gharama zozote.
Kundi la pili katika msigano huo ni lile linalomuunga mkono Lowassa, likiwajumuisha wanasiasa kama Makamba, ambao wamekuwa wakimtaja Nape kuwa kijana anayejaribu kujenga hoja ili kujihalalishia ushindi kwa gharama zozote zile.
Habari kutoka ndani ya CCM zinaeleza kuwa, wanasiasa wanaounda kundi hili ambalo Mwenyekiti wa Taifa wa Umoja wa Vijana, Emmanuel Nchimbi, anatajwa kuwa mmoja wao, tayari wameshaanza kupanga mikakati ya kuhakikisha wanamuengua Nape katika mchuano huyo.
Wana CCM hao ambao baadhi yao wamepata kufanya mahojiano na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti, wamekuwa wakimuelezea Nape kuwa mwanasiasa mzushi na mtu anayetumiwa na kundi la wazee kadhaa wa ndani ya chama hicho wenye lengo la kuhakikisha wanawaengua watu wote walio karibu kisiasa na Rais Jakaya Kikwete, ambaye ndiye atakayekuwa mwenyekiti katika mchakato huu wa leo.
Habari ambazo Tanzania Daima imezipata kutoka kwa watu wa kundi hili la pili zinaeleza kwamba, kikao cha leo cha Kamati Kuu kinatarajia kuridhia kupitishwa kwa mkataba huo pamoja na kuwapo kwa wana CCM wengi wanaomuunga mkono Nape katika hoja yake.
Kwa sababu hiyo basi, iwapo kweli, Kamati Kuu itaridhia kupitishwa kwa mradi huo, upo uwezekano mkubwa kwamba, nafasi ya Nape katika mchuano wa kuwania uenyekiti wa UVCCM itakuwa shakani.
Katika hoja ya Nape, mbali ya Lowassa, wanasiasa wengine anaowahusisha katika mkataba huo ni Nchimbi, na aliyekuwa Katibu Mkuu wa UVCCM, ambaye sasa ni Mweka Hazina wa CCM, Amos Makalla.
Katika hoja zake, Nape amenukuliwa akisema kwamba mkataba huo ulipitishwa kinyemela hata kabla haujafikishwa kwenye vikao vya juu vya CCM, kwa maana ya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu (NEC) ya chama hicho ili kupata baraka za mwisho.
Vipengele vingine ambavyo Nape analalamikia ni kuhusu uhai wake, kwani kimojawapo kinasema mwekezaji ataendesha mradi huo milele, huku jumuiya hiyo ikipata asilimia 25 na mwekezaji asilimia 75.
Kasoro nyingine anazozitaja Nape katika tuhuma hizo ni pamoja na ile ya kukiukwa Sheria ya Ardhi (Kiwanja), kuhamishwa kwa wabia kabla ya shughuli yoyote ya ujenzi kuanza.
Utaratibu ni kwamba, kabla hatua hiyo haijachukuliwa, sharti Kabidhi Wasihi Mkuu wa Serikali, atoe kibali kwa ajili ya uhamisho wa aina hiyo.
Mkataba wa mradi huo unaosomeka kwa kichwa kisemacho ‘Development Agreement', ulisainiwa Januari 2 mwaka 2007 kati ya UVCCM na makampuni mawili ya M. M. Integrated Steel Mills (MMISML) na Estim Construction Company Limited (ECCL).
Mkataba huo pia hauelezi kiasi cha uwekezaji kutoka kwa wabia, ambacho kinaweza kutumika kuelezea mgawo wa asilimia 25, ambayo inadaiwa UVCCM watachukua.
Aidha, mkataba huo hauna ufafanuzi wa matumizi na mapato hatua kwa hatua, jambo ambalo linaonyesha kutokuwa makini au kuashiria ghiliba katika mahusiano ya wabia.
Vilevile mkataba hauelezi iwapo ubia ni wa miliki ya pamoja au itaundwa kampuni tofauti ya kuendesha kitega uchumi.
Mbali na kujadili suala la mradi huo, kikao hicho pia kitapitia majina ya waombaji wanaowania uongozi wa jumuiya za chama hicho, ambazo mbali ya UVCCM, pia itajadili majina ya wanaoomba uteuzi wa Jumuiya ya Wanawake (UWT).
Mbali ya Nape, waombaji wengine katika uchaguzi huo wa UVCCM unaoendelea kuvuta hisa za watu kila kukicha ni Jerry Slaa, Hamad Masauni, Issa Haji Ussi, Anthony Mtaka, Said Mtanda, Haule Pangisa, Samuel Marero, Stephen Deya, Geofrey Mwankenja, David Manoti, Mussa Mnyeti, Edson Lubua, Mwamini Lusingu, Asmah Kalokola, Marco Zablon Allute, Harold Adamson, Adila Hilal Vuai, Ashura Ismail, Rashid Masalaka na Raha Ahamada.
Wanaowania uteuzi wa nafasi ya makamu mwenyekiti ni Happy Mahava, Raha Ahamada Ally, Riziki Pembe Juma, Michael Bundala, Rabia Hamid Shaka, Nuru Mohammed Ahamed na Twaha Ally Muhaji.
Taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, ilisema chama hicho kitajadili masuala yanayokihusu chama, ikiwemo jumuiya zake pamoja na jamii kwa ujumla.
Katika taarifa hiyo, CCM inasema miongoni mwa ajenda hizo ni kupokea na kujadili taarifa kuhusu hali ya kisiasa nchini.
Makamba alizitaja ajenda nyingine kuwa ni ile inayohusu kupokea na kujadili taarifa ya maendeleo ya uchaguzi mkuu wa jumuiya za CCM, unaofanyika nchini kote mwaka huu, na nyingine ni kuziba nafasi za uongozi zilizo ndani ya chama hicho tawala.
"Mkutano huo pia utapokea taarifa kuhusu maandalizi ya CCM ya kushiriki uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata 34 Tanzania Bara," alisema.
Kikao hicho kitafuatiwa na kikao kingine cha Halmashauri Kuu (NEC) kinachotarajiwa kufanyika Septemba 9 hadi 10 mjini Dodoma.