Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 21*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Ndio, nipo tayari,” Darren akajibu. Basi mwanamke yule akanyanyua kisu kile na kukichomeka kwanguvu mezani. Kisu kikachimba meza na kusimama dede. Darren akazidi kuhofu.

Basi mwanamke yule akaanza kusimulia kwa sauti yake inayofanana na kasuku. Akiwa ameongea sentensi mbili tu, upepo ukapuliza dirishani na kupeperusha pazia kama bendera. Darren akatazama huko upesi akiwa mjawa wa mashaka.

ENDELEA

Mwanamke yule akiwa anamtazama Darren machoni akasema ya kwamba yeye hana majibu ambayo Darren alikuwa anayauliza, ila tu amefurahishwa sana na uwepo wa Darren hapo. Lakini inawezekanaje hilo na ingali Darren hajuani na mwanamke huyo?

Darren alipouliza, akatahamaki mwanamke yule anabadili rangi ya macho yake na kuwa nyeusi kama bendera. Alafu mwanamke huyo akachomoa kisu chake toka mezani na kumrukia Darren akitaka kumchoma.

Ilikuwa ni swala la kufumba na kufumbua tu, nyumba ile ikawa ghofu kabisa. Paa lake lilijawa na tando za buibui na madirisha yakiwa yamepotea yasionekane. Kulikuwa giza, mwanga hafifu rangi nyekundu ikiwa inatambaza kwa mbali.

Ilikuwa ni ajabu namna gani ambavyo mambo yalbadilika kwa upesi namna ile! Nyumba iliyokuwa ni nzuri ikageuka na kuwa nyumba ya mizimu, nyumba ya majini! Harufu ya damu ilitawala na mifupa huku na kule.

Kwa Darren yalikuwa ni kama mazingaombwe ama maigizo! Hakuwa anaelewa kinachoendelea hapa. Kila kitu kwake kilikuwa ni kama amerukwa na akili. Kitu pekee alichokuwa ana kijua na kupambana nacho ni kuokoa nafsi yake dhidi ya umauti uliokuwa unataka kumkumba.

Hakujua alikuwa amezama. Tena amezama kwenye lindi zito la kifo. Ameshikwa kwenye tego kali la kummaliza.

Akapambana kumzuia mwanamke yule asimkite na kisu, na alipofanikiwa kufanya hivyo baada ya kumtwanga mwanamke huyo kichwa cha puani, akakimbilia mlango afungue na kwenda, lakini alipofika mlango haukufunguka abadani! Haikujalisha ni nguvu kiasi gani alitumia, mlango ukamtazama kodo pasipo mafanikio.

Yule mwanamke akacheka sana. Akanyanyuka toka chini huku akijitoboatoboa na ncha ya kisu kana kwamba godoro. Ilikuwa ni ajabu kwamba ahisi maumivu? Akavuja damu na kujichafua haswa lakini hakuwa anajali hata kidogo.

Alimtazama Darren kwa macho ya matamanio, alafu akalamba kisu chake kana kwamba mtoto na mche wa ‘ice-cream’, alafu kufumba na kufumbua akamkimbilia mwanaume huyo akammalize. Mwendo wake ulikuwa wa kasi sana, lakini kabla hajafika aendapo, kumbe Darren alikuwa ameshakamata stuli kwa mikono yake miwili, akamkandika kwanguvu mno! Puuh!!! Mwanamke huyo akasombwa na kubwagwa ukutani, kisha kukawa kimya!

Darren, akiwa anahema kwa hofu, akamtazama mwanamke yule kwa jicho la tahadhari. Bado mikononi akiwa ameshikilia ile stuli yake endapo lolote litajiri. Ikapita dakika ya kwanza kukiwa kimya. Dakika ya pi… akasikia mlango unafunguliwa! Akatupa macho yake kupambana na kiza kilichopo apate kuona.

Hakuona kitu!

Moyo wake ulikuwa unamwenda mbio sana. Kwasababu kulikuwa na ukimya wa kufanya masikio yawe kiziwi, Darren alikuwa anaweza kusikia mapigo yake ya moyo kwa uzuri kabisa. Angeliweza kuyahesabu pasipo matatizo kabisa.

Kidogo, akapata wazo la kutumia stuli ile kubomolea mlango. Akabondea hapo mara kadha wa kadha. Akaponda na kubonda lakini mlango haukufunguka. Ulikuwa ni migumu kama ile ya kasri ya mfalme. Ulikuwa ni mgumu kana kwamba malighafi yake ni chuma na metali! Badala ya mlango kukongoroka, ni stuli ndiyo ikaanza kuwa dhoofu na kuanza kumomonyoka!

Mwishowe Darren akabakiwa na vipande tu vya stuli mkononi mwake ingali mlango ukiwa madhubuti.

Akainama kwa kuchoka. Akahema sana akivuja jasho. … lakini nyuma yake kule kulipotoka sauti ya mlango kulikuwa na nini? Kama ungetazama vema, kwa kuyafinya macho na kusisitiza maono yako basi ungeliona kuna kiumbe kilikuwa kinatembea gizani kumjongea.

Miguu ya kiumbe huyu ilikuwa inakanyaga sakafu taratibu. Kwasababu ya kiza, hakikuwa kinaonekana vema.

Kilisonga kwa hatua ya karibu lakini harakaharaka.

Darren alihisi kitu, upesi akageuka na kuangaza koridoni, kizani. Hakuwa anaweza kuona kitu. Japo alikodoa bado hakuwa na uwezo wa kuona jambo. Alipomtazaa yule mwanamke aliyemsomba kwa kumkita awali, akamwona bado amelala palepale. Sasa ni nini hicho anahisi? Akajiuliza.

Kufumba na kufumbua, Darren akastaajabu kuona kitu juu ya paa. Hajakaa vema wala kujitengenezea, kiumbe hicho kikamvamia na kumwangusha chini kikimkaba na kumng’ata shingoni!

Mdomo wake ulikuwa wa baridi sana. Meno yake yaliyochongoka yalikita kwenye mishipa ya shingo ya Darren na kisha koo lake likawa linamnyonya damu!

Kwa ubaridi wa kinywa hicho, Darren akahisi mwili wake umezamishwa kwenye dimbwi la barafu. Alihisi baridi toka kwenye nyayo yake mpaka utosini. Lakini baridi hili likiwa linakera! Baridi linalotisha.

Pumzi ya kiumbe hicho ilisabahi shingo yake na kuzidi kumtia hofu na kimuhemuhe.

Kheri Darren bado alikuwa na vipande vile vya stuli mkononi. Kama mtu aliyepandwa na kichaa, akatumia vipande hivyo kwanguvu na pasipo mafikirio kumshabulia kile kiumbe kilichomshikilia.

Akamtoboatoboa kiasi kwamba hata yeye akajiumiza. Kile kiumbe kikapiga kelele na kuangukia chini. Kabla Darren hajamtazama mvamizi wake huyo akagundua kuwa shingoni alikuwa anachuruzwa na kimiminika cha moto. Alipojipapasa akagundua ni damu! Alikuwa anchuruzwa na damu nyingi na akihisi maumivu makali.

Alimtazama kiumbe kile alichoadhibu na kubaini alikuwa ni yule mtoto aliyemkaribisha na kumfungulia. Alikuwa amejilaza akiwa ametulia na kuvuja damu. Alipotazama kule ambapo alikuwa amelala yule mwanamke aliyemwadhibu mwanzoni, ajabu hakuona kitu!

Akiwa ameweka kiganja chake shingoni kuzuiza damu zinazotiririka, akajongea na kuangaza pale alipokuwa amemwona mwanamke yule mwanzoni. Lah! Hakuwapo. Hapo akapata hofu sana. Kutokuwapo kwa mtu huyo kulikuwa ni ishara mbaya kwa usalama wake.

Akatazama kushoto na kulia, juu na chini asione kitu! Moyo wake bado ulikuwa unadunda kwa kasi, na damu bado zamchuruza kufurika vidole vyake. Ni wazi alikuwa ana muda mfupi wa kuwa hai kama jeraha hilo lisingepata huduma ya upesi.

Aliendelea kuangaza na kuangaza. Kidogo akahisi upande wake wa kulikuwa na kiumbe. Alirusha macho yake upesi akikodoa. Mkono wake wa kuume alikuwa amebebelea kipande cha stuli na ule wa kushoto ukiwa umehifadhi jeraha.

Baada ya muda kidogo, akaona kuna kitu chenye rangi nyeupe ya kufifia mule kizani. Alipojaribu kukaza macho yake atazame, akashindwa. Alikuwa ameanza kuishiwa na nguvu na macho yake yakijawa na ukungu.

Aliona kiza kimeongezeka maradufu … Mkono uliobebelea silaha nao ukaanza kupwaya.

Kidogo akaona kitu kile chenye rangi nyeupe kikisogea zaidi karibu yake. Alikuwa ni mtu lakini alishindwa akumtambua kutokana na macho yake kudhoofu. Na hata alipotaka kumshambulia mtu huyo kwa kutumia silaha yake, hakuweza. Hakuwa na nguvu hiyo tena. Jeraha lilishamzidi nguvu.

Akazabwa kofi shavu lake la kulia na kudondoka chini. Hata hakuhisi maumivu tena. Kitu pekee ambacho kilikuwa hai kwenye mwili wake ni macho yake yaliyokuwa yamekodoa na kuoa ukungu. Aliona tu kiza, kiza na yeye.

Na jambo la mwisho ambalo alilielewa ni kushikwa shati lake na kuburuzwa. Kidogo tu akapoteza fahamu kabisa.

Yalikuwa yamekwisha.

***
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 22*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akazabwa kofi shavu lake la kulia na kudondoka chini. Hata hakuhisi maumivu tena. Kitu pekee ambacho kilikuwa hai kwenye mwili wake ni macho yake yaliyokuwa yamekodoa na kuoa ukungu. Aliona tu kiza, kiza na yeye.

Na jambo la mwisho ambalo alilielewa ni kushikwa shati lake na kuburuzwa. Kidogo tu akapoteza fahamu kabisa.

Yalikuwa yamekwisha.

ENDELEA

Hakuelewa kinachoendelea hata kidogo. Alikuja kupata ufahamu wake akiwa kwenye gari, viti vya nyuma. Alikuwa amechoka mno, kichwa kinamuuma. Mwili wake anauhisi dhaifu viungio vyote vikiwa vinapwita.

Alijaribu kunyanyuka, akashika kiuno kwa kulalama. Alijikaza akanyanyuka vivyo hivyo na kisha akatupa macho yake kwenye kioo cha mbele cha gari. Ajabu alipotazama hapo akaona kipande kile cha gazeti chenye taarifa juu ya mwanamke yule aliyekumbwa na mikasa kama yake. Kipande kilekile cha gazeti ambacho kilimwelekeza kwenda kule kwa watu wa ajabu.

Akashtuka baada ya kukumbuka mkasa alopitia. Hakika haukufaa kusimulia. Kidogo gazeti lile likapeperushwa na upepo na punde akaonekana mtu akiwa amekaa kwenye kiti cha pembeni ya dereva. Mtu huyo ametulia tuli akitazama mbele.

Darren akashtuka kumwona mtu huyo maana hakumwona hapo awali. Hakujua wapi ametokea. Akaita kwa woga na kuuliza ni nani? Kidogo mtu huyo akageuka na kumwangazia Darren. Kumbe alikuwa ni Melissa.

“Melissa!” Darren akafoka. “Kumbe ni wewe?”

Alipandwa na hasira sana. Alijikuta ananyanyuka toka kwenye kiti chake na kumvamia Melissa. Akamkaba na kumtwanga ngumi mfululizo kwa hasira akiwa anafoka, “Niache na maisha yangu! Niache wewe mpuuzi! Niache! Niache!”

Melissa akajikinga na mashambulizi makali ya Darren, lakini alipoona yanamzidia, akamtupia mwanaume huyo nyuma ya gari! Alimnyanyua kana kwamba usufi. Na Darren, kama mfuko wa saruji, akadondokea vitini na kulalamikia maumivu ya kiuno chake.

“Niskize Darren!” Melissa akapaza sauti yake kali. Vioo vikachipua nyufa. “Kwanini hautaki kunielewa?” akauliza akiwa anamtazama mwanaume huyo kwa macho mekundu. “Kwanini unakuwa na moyo mzito na kichwa kigumu?”

Akaongea sana lakini Darren asijali. Alikuwa anagugumia maumivu ya kiuno huku akiwa anamtazama Melissa kwa jicho la mbali. Melissa alipomaliza kujichosha kwa kuongea, Darren akamwambia kwa sauti ya chini akiwa anachuruza chozi jicho lake la kushoto, “Toka kwenye gari langu. Ondoka mbele yangu Melissa.”

Melissa akamtazama Darren kwa sekunde nne pasipo kusema jambo. Macho yake yalidondosha machozi. Alifungua mlango wa gari na kujiondokea, Darren akashusha pumzi ndefu. Alikuwa anazidi kumwaga machozi aking’ata meno. Mwishowe alishindwa kabisa kujizuia, akalia kilio kikuu.

Akalia sana akiwa anajiona yupo kwenye lindi kubwa la matatizo. Akalia haswa akihitaji kusafisha kifua na kichwa chake. Mwishowe alipojiona kuwa yu sawa, akasonga kwenye kiti cha dereva na kuwasha gari lake aondoke.

Akiwa njiani akawaza sana namna gani aenende. Aliwaza sana nini afanye kujiondokea na matatizo, hata akawaza kujiua, lakini akifanya vivyo nani atakaye mwangalia mtoto wake? Mkewe alishafariki.

Aliendesha akiwa anamwaga tu machozi. Alipofika nyumbani akajilaza kitandani kwake pasipo kumtazama mwanaye. Alikuwa anawaza sana. Ilipofika majira ya usiku, Isabel alimpigia na kumwomba waonane.


**

Usiku wa saa tatu ….

Kulikuwa kumetulia kabisa, ungeweza kusikia mdomo wa Isabel ukitafuna. Mwanamke huyo aliyekuwa amevalia suti rangi ya zambarau alikuwa ameshikilia sambusa mkononi mwake na glasi ya sharubati ikiwa mezani.

Mbele yake alikuwa ameketi Darren akiwa na glasi ya mvinyo mwekundu pekee. Hakutaka kula maana hakuwa na hamu wala kujisikia kufanya hivyo, uso wake ulikuwa umepoa, mara nyingi akitazama watu wanaoingia na kutoka eneo hilo walilopo. Hakuwa sawa.

Kidogo Isabel akamshtua na kumuuliza, “Utakuwa kwenye hali hiyo mpaka lini, Darren?”

Darren akaminya lips zake asiseme kitu. Alitazama glasi yake ya kinywaji kwa mawazo.

“Inabidi uniruhusu nikusaidie Darren. Tafadhali.”

Bado Darren hakusema jambo. Isabel akanywa sharubati yake na kisha akajifuta mdomo kwa ‘tissue’.

“Darren ukiendelea hivi utashindwa kufanya kazi zako. Maisha yako yatapotea. Serious, inabidi ubadilike. Niambie nini tatizo.”

Darren akanywa kwanza mafundo mawili alafu akashusha pumzi ndefu kabla hajasema, “Unajua hapa karibuni nimepitia mambo makubwa sana. Nadhani badi sijapata muda wa kutulia. Bado akili yangu haijakaa sawa.”

“Najua, Darren,” akasema Isabel. “Najua umepitia milima na mabonde hapa karibuni. Lakini inabidi uache vitu viende, sawa? Hauwezi kuishi hivi milele? Hauoni namna unavypungua kwa mawazo? Inatosha Darren. Mfikirie mwanao. Vipi kama ukipatwa na tatizo, atakuwa kwenye hali gani?”

Darren akakosa majibu. Alifikicha macho yake akashika tama.

“Sikia, Darren. Ningependa niwe karibu zaidi na wewe. Naomba uniruhusu,” Isabel akapendekeza.

“Ukaribu kiasi gani, Isabel?” Darren akauliza. “Kwani hapa hatuko karibu?”

“Tuko karibu lakini nataka kuwa karibu zaidi. Naomba uniruhusu Darren. Nataka kuwa karibu na wewe zaidi.”

Wakatazamana kwa kama sekunde tano. Kulikuwa na kitu machoni mwa Isabel.

“Unaweza ukaja kuishi kwangu,” Isabel akapendekeza. “Naishi mwenyewe pamoja na wafanyakazi. Nadhani nitakuwa na wigo mpana wa kukusaidia. Mtoto wako pia hatapata shida. Unasemaje Darren?”

Darren akabinua mdomo wake. Akanyanyua glasi ya kinywaji na kupiga mafundo mawili tena kisha akamtazama Isabel machoni.

“Hapana, Isabel. Haiwezi kuwa haraka kiasi hicho.”

“Nini tatizo?” Isabel akauliza kwa kujiamini. Macho yake makali yalikuwa yanamtazama Darren barabara.

“Si kwamba kuna shida,” Darren akajibu. “Ila tu sijajiandaa kufanya hivyo. Hauoni kama ni hatari?” Isabel akatikisa kichwa.

“Kwa upande wangu, sioni kama kuna shida. Sijajua kwako.”

“Nipe muda nifikirie zaidi juu ya hilo. Siwezi harakisha.”

“Sawa. Muda gani unakutosha kufanya vivyo?”

“Nitakutaarifu, usijali.”

Lakini jibu hilo halikumridhisha Isabel. Alipokunywa fundo moja kumalizia kinywaji chake akauliza, “Kwanini usinipe muda halisia, Darren. Huoni unaweza kuningojesha milele kwa kauli hiyo?”

Basi Darren kwa kulazimika, akasema mpaka juma lijalo atakuwa tayari ameshampatia jibu. Angalau Isabel akafurahi. Wakamalizia maongezi yao kwa kuongea biashara juu ya ile nyumba ya bibi yake Darren kule ‘countryside’, wakaafikiana mpaka bei, ambapo ilikuwa pesa kubwa sana.

Kwa mawazo ya Darren aliona ni kheri akamuuzia Isabel nyumba hiyo kwani haikuwa na faida tena kwake, lakini zaidi apate kiasi cha pesa kitakachomwezesha kuwa na makazi mapya, makazi ambayo yatakuwa salama kwake na familia yake. Aliwaza pengine akihama, anaweza akapata pumziko la kichwa chake.

“Kwahiyo utaingiza lini hiyo pesa?” Akauliza.

“Kesho mchana,” Isabel akamjibu. Kidogo Darren akashangazwa, kilikuwa ni kiasi kikubwa cha pesa kupatikana haraka namna hiyo!

“Kuna shida, Darren?”

“Hapana. Hamna tatizo kabisa.”

“Sawa. Kesho tazama akaunti yako kuanzia majira ya saa sita mchana.”

Wakakubaliana hilo na basi kama alivyomleta, Isabel akamrejesha Darren nyumbani kwake, lakini kabla hajashuka, akamshika mwanaume huyo mkono wake wa kushoto na kumtazama kidogo.

“Kama kutakuwa na tatizo nijulishe Darren.”

Darren akatikisa kichwa chake kuafiki alafu akashuka toka kwenye gari na kwenda ndani. Kulikuwa ni kimya. Alishangaa kukuta hali hiyo. Akamwita dada wa kazi mara tatu pasipo majibu. Akapata shaka kidogo. Akanyanyuka na kwenda vyumbani, akakagua kila chumba lakini hakumwona dada wa kazi wala mtoto wake. Hapa shaka lake likakua zaidi.

Akajaribu kupiga simu ya dada wa kazi, ikaita, ila alipotulia na kuskiza vema akagundua simu hiyo inaitia ndani. Alipoenda chumbani kwa dada huyo akabaini simu ilikuwa imefunikwa na shuka. Sasa ameenda wapi na mtoto?

Tumbo likaanza kumsokota.

Alitoka ndani kwake akaenda kuuliza majirani kama wamemwona msichana huyo na mtoto wake lakini hakupata kitu. Alihisi kuchanganyikiwa. Alirejea ndani akaketi akiwaza na kuwazua. Muda ukaenda mpaka majira ya saa tatu usiku.

Sasa akaona ni vema atoe taarifa polisi kwa uchunguzi zaidi. Akatoa kila taarifa aliyoifahamu na polisi wakaanza kazi yao. Lakini kwenye majira ya saa nne usiku, dada wa kazi akarejea akiwa na mtoto.

Dada huyo mkononi alikuwa amebebelea vitu vya mtoto na kwa kutumia kibebeo maaulum alikuwa amembelea mtoto kifuani mwake. Darren akafurahi sana kumwona mwanae. Akamkumbatia kwanguvu na kumuuliza dada wa kazi wapi alikwenda kwa muda wote huo.

“Nilienda kumchukulia mtoto mahitaji yake,” dada akajitetea. “Lakini nilikutana na msongamano mkubwa wa magari sababu ya ajali. Samahani sana.”

Baada ya maelezo hayo, dada huyo akaenda chumbani kwake akimwacha Darren na mwanaye pale sebuleni. Darren akatoa taarifa polisi juu ya kumpata mwanaye.

“... Nashukuru sana, nitakuwa mwangalifu zaidi siku nyingine.”

Alipokata simu ndipo akagundua kuna kitu kwa mwanaye.


***
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 23*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Baada ya maelezo hayo, dada huyo akaenda chumbani kwake akimwacha Darren na mwanaye pale sebuleni. Darren akatoa taarifa polisi juu ya kumpata mwanaye.

“... Nashukuru sana, nitakuwa mwangalifu zaidi siku nyingine.”

Alipokata simu ndipo akagundua kuna kitu kwa mwanaye.

ENDELEA

Nyuma ya mgongo wa mwanaye, chini kidogo ya bega la kushoto, aligundua kuna chapa fulani ndogo. Chapa hiyo ilikuwa nyeusi yenye ishara kama ya msalaba lakini ikiwa na mikono miwili.

Hakujua maana ya chapa hiyo lakini alijikuta akiwa na wasiwasi nayo. Alijaribu kuifuta kwa kutumia kidole chake, haikufutika. Akajaribu kumfuta na kitambaa bado napo haikufutika, ilikuwa ni alama ya kudumu!

Upesi akamuuliza dada wa kazi apate kujua nini kimemtokea mtoto. Lakini dada, akiwa ameparamiwa na uso wa hofu, akajitetea sana. Hakuwa anafahamu lolote. Hakuwa anajua hata kama mtoto ana chapa hiyo? Amemwogesha jana yake na hata siku hiyo asubuhi lakini hakuona alama kama hiyo.

Darren akatingwa na maswali lakini pia na hofu. Hakuhisi kama mwanaye yuko salama. Kila mara alitazama alama hiyo na kujiuliza maswali mengi kichwani. Mwishowe aliona ni kheri akafanya jitihada zaidi kung’amua chapa hiyo na hapo ndipo akazama kwenye mtandao na kusaka alama ile baada ya kuiweka kwenye mashine yake.

Baada ya muda kidogo akapata kuona taarifa chache juu ya chapa hiyo ikiwa inahusishwa na habari za zamani sana kuhusu huko Uajemi tena ni ishara aghalabu ya majini!

Alipotafuta sana akabaini kuwa mwanawe hakuwa mtu wa kwanza kuwa nayo, takribani watu watatu walikuwa nayo, ila mwisho wao wote ilikuwa ni kifo! Alipohangaika zaidi kutafuta mengineyo, akapata kukutana na mwanamke mmoja ambaye mwanaye alikuwa na chapa hiyo. Alituma hilo swala mtandaoni kuomba ushauri.

Basi hilo likawa kama neema kwa Darren. Alitafuta zaidi taarifa za mwanamke huyo akafanikiwa kupata anwani yake, akapanga kesho yake akamtafute amwambie zaidi kuhusu hiyo chapa.

Alihofia sana juu ya mwanaye. Na kwa hofu hiyo akataka alalae nae ndani ya chumba chake.

Ulipofika usiku wa manane, Darren akiwa amelowea kwenye usingizi mzito, na pia nyumba ikiwa imetulia tuli sawa sawa na mtaa mzima, taratibu mlango wa chumba alalacho dada wa kazi, ulifunguliwa na kisha ukatuama pasipo lolote kutokea.

Kulikuwa kimya.

Zilipopita kama sekunde tano, ndipo mkono uliobebelea kisu ukatoka kwenye mlango huo. Bada ya punde, ukafuatia na mguu na kisha mtu mzima kabisa. Alikuwa ni yule dada wa kazi.

Aliyatoa macho yake akikodoa. Alitazama kushoto na kisha kulia, alafu akauendea ule mlango wa chumba cha Darren. Alipoufikia, hakugonga, lah! Akapindua kitasa taratibu na mlango huo ukafunguka. Alipousogeza vya kutosha, akatulia hapo akisimama.

Zikapita kama sekunde nne. Basi taratibu akazamisha mguu wake ndani ya chumba, na taratibu sana, akaweka nyayo zake sakafuni akisonga. Alimwendea mtoto na kumpakua toka kwenye kitanda chake. Lakini mikono yake ilikuwa ya baridi sana. Alipomshika mtoto tu, akaanza kulia.

Akakodoa kumtazama Darren. Darren alikuwa amelala bado fofofo. Lakini sauti ya mtoto iliyokuwa inaendelea kupaza na kupaza ilimshtua sasa akaamka na kuangaza.

alipotazama kwenye kitanda cha mtoto, hakukuwa na kitu. Kitanda kilikuwa tupu kikianza kujenga ubaridi! Akachanganyikiwa sana. Alitazama kushoto na kulia kwake asione kitu, mlango ulikuwa umefungwa, ila sauti ya mtoto bado akiisikia!

Sauti hiyo ilikuwa ikiishilia!

Haraka akatoka kitandani na kudaka korido. Akatazama na kupekua kwa macho yake, kidogo, masikio yake yakamwambia kuwa sauti ya mtoto inatokea kwenye chumba cha dada yake wa kazi!

Akauendea mlango huo na kubisha kwa kuutwanga ngumi. Akaukandika na kuukandika lakini haukufunguliwa. Mtoto bado aliendelea kulia!

Akiwa amepandwa na akili za ukichaa, Darren akaubamiza teke kali mlango huo na kuuvunjia mbali. Alipotazama, akamwona dada wa kazi akiwa amemkabia mtoto kitandani kwa kutumia mkono wa kushoto na ule wa kulia ukiwa umeshikilia kisu akitaka kumchoma.

“Tafadhali, usimuue mwanangu!” Darren akapaza sauti akimtazama dada wa kazi kwa imani. Dada akatabasamu na kusema, “Lazima afe, Darren. Hata kama nisipomuua mimi!”

“Kwanini?” Darren akalia. “Kwanini afe? Sina kitu kingine mbali na huyo mtoto. Nambie unataka nini nitakupatia!”

Dada akatabasamu almanusura kucheka. Alimtazama mtoto kisha akayarudisha macho yake kwa Darren na kusema, “Sitaki chochote Darren. Kama ningekuwa nataka chochote kile basi ningekitafuta na kukichukua mwenyewe. Kwa sasa ninachotaka ni roho ya huyu kiumbe tu, si kingine!”

“Lakini amekukosea nini?” Darren akauliza. Macho yake yalikuwa mekundu yakikaribia kudondosha chozi.

“Hajafanya kitu,” Dada akajibu akitikisa kichwa. “ila si mali yako tena. Huyu ni mali ya majini, na ni wa kufa tu!”

Dada aliposema hayo akamkandika mtoto kisu cha kifuani, chote kikazama na kutosha kumfanya mtoto mfu. Darren akalia sana. Akakurupuka toka kitandani mwake na kumtazama mwanaye pembeni. Nalikuwa ni ndoto. Mtoto alikuwa yu kwenye kitanda chake ila akilia sana.

Upesi akamnyanyua na kujitahidi kumbembeleza … sh!-sh!-sh!-sh!-sh!-sh! … lakini alipotazama dirishani akabaini kuwa li wazi. Akalisongea na kutazama nje kama kuna lolote lile, hakuona jambo. Mtaa ulikuwa umetulia sana. Ni upepo wa baridi ndio ulikuwa ukipuliza tena kwa mbali.

Akalifunga dirisha hilo, bado mtoto akilia, alipomaliza akasikia hodi mlangoni mwake. Kidogo mapigo yake yakaruka. Akiwa amemshikilia mtoto wake vema, akapaza sauti kuuliza,

“Nani?”

“Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni. Kidogo akajawa na mashaka.

“Unataka nini?”

“Nimemsikia mtoto analia. Vipi kuna shida?”

“Hapana. Hamna shida.”

“Naweza kukusaidia kumbembeleza?”

Darren akasita kwanza.

“Hapana, ahsante. Nitambembeleza mwenyewe.”

Baada ya hapo sauti ya dada haikusikika tena bali mtoto akiwa analia tu. Darren akaendelea kumbembeleza mwanaye akimsihi anyamaze kwani usiku umekuwa mkubwa na yeye amechoka sana. Kwa kama lisaa limoja, mtoto akaendelea kulia tu, akipunguza sauti na kurudi tena upya.

Darren akachoka sana kumbembeleza, mikono ikawa inamuuma, macho yanamsaliti kwa kuwa mazito, kichwa nacho kinachoshwa na sauti kali ya mtoto.

Mlango ukagongwa tena.

“Nani?” akauliza kwa sauti ya uchovu.

“Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni.

“Unataka nini?”

“Mtoto ana shida gani?”

“Amekurupuka tu toka usingizini, usijali. Unaweza kulala.”

“Naweza kukusaidia?”

“Hapana! Usijali, nitambembeleza mwenyewe mpaka alale.”

Basi baada ya hapo sauti ya dada wa kazi haikusikika tena, Darren akaendelea kumbembeleza mtoto. Kwa kama nusu saa akawa anafanya zoezi hilohilo tu. Kila alipojaribu kumweka mtoto kitandani ambembelezee hapo, ikawa tabu zaidi, mtoto aliongeza kilio.

Hakujua sasa cha kufanya. Kila mtindo alitumia lakini haikusaidia. Ilifikia kipindi akawa anapitiwa na usingizi ingali amesimama. Alimweka mtoto kitandani kwa kulazimisha akaendelea kumbembeleza hapohapo, kidogo akapitiwa na usingizi.

Kama baada ya dakika mbili akakurupushwa na hodi ya tatu mlangoni mwake. Akauliza, “Nani?”

“Dada wa kazi!”

“Unataka nini?”

“Mtoto anasumbuliwa na nini?” dada akauliza.

“Si nilishakwambia!” Darren akafoka kidogo.

“Naomba nimbembeleze,” sauti ya dada ikaomba.

“Nimesema nambembeleza mwenyewe. Hukunielewa?”

Kukawa kimya kidogo.

Punde sauti ya dada ikasema tokea mlangoni, “Utanipa nimbembeleze ama nije nimchukue mwenyewe?” mara hii sauti ilikuwa na amri ndani yake.
.
.
.
***
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 24*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Si nilishakwambia!” Darren akafoka kidogo.

“Naomba nimbembeleze,” sauti ya dada ikaomba.

“Nimesema nambembeleza mwenyewe. Hukunielewa?”

Kukawa kimya kidogo.

Punde sauti ya dada ikasema tokea mlangoni, “Utanipa nimbembeleze ama nije nimchukue mwenyewe?” mara hii sauti ilikuwa na amri ndani yake.

ENDELEA

Darren akajawa na hofu. Akamnyakua upesi mtoto wake na kumfichama kwenye mikono yake akiwa anatazama mlango kwa hofu. Punde mlango ukaanza kubamizwa kwa nguvu na kwanguvu! Darren akajaribu kuteka simu yake atoe taarifa polisi lakini hakuiona. Kwa muda alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa. Hakujua cha kufanya.

Mlango ukaendelea kubamizwa na kubamizwa. Mwishowe ukaanza kudhoofu na kubomoka. Vipande vyake viliruka huku na huko. Ilikuwa ni ajabu mbomoaji alikuwa anatumia nyenzo gani kufanyia zoezi lake hilo.

Darren alichofanya ni kutwaa kipande kidogo cha mbao ya mlango na kubebelea kama silaha. Ni ajabu kama mtu ameweza kubomoa mlango atamzuiaje kwa kipande cha mbao, lakini alikuwa na imani.

Mkono wake uliobebelea kipande hicho cha mbao ulikuwa unatetemeka. Macho yamemtoka na paji lake la uso linatiririsha jasho.

“Ni nani wewe?” Darren akauliza kwa sauti yenye kusita. Hakujibiwa. Kilichokuwa kinafanyika ni mlango kubamizwa tu! Tena kubamizwa kwanguvu mno.

Kidogo, kwasababu ya hofu na kukurupushwa usingizini, mtoto naye akaanza kulia. Alikuwa analia kwanguvu haswa kiasi cha kumchanganya Darren. Ingawa Darren alimsihi anyamaze, haikusaidia kitu.

Mwisho wa siku mlango wote ukawa upo chini na mlangoni akiwa amesimama mwaname anayechuruza damu mikononi. Mwanamke huyo si mwingine bali dada wa kazi. Mikono yake ilikuwa imejeruhiwa vibaya mno kwa kubamiza mlango hata kuvunjika. Macho yake yalikuwa makubwa yanayong’aa, uso wake umepauka kuwa mweupe.

Alimtazama Darren kisha akainamisha shingo yake kwenda kushoto na kulia, kisha kulia na kushoto. Akamnyooshea kidole Darren pasipo kusema jambo. Alafu kama mtu aliyegandishwa na barafu, akaanza kupiga hatua kumwendea Darren.

Darren akamtisha na kipande chake cha mbao, “Kaa mbali!” akafoka. “Kaa mbali na mimi!” lakini mwanamke yule hakuwa anasikia wala kujali, akaendelea kusonga kumfuata Darren, na alipomkaribia akanyoosha mikono yake yote miwili na kisha akasimama.

Kukawa kimya kidogo. Darren akamtazama mwanamke huyo kwa hofu na maulizo. Naye mwanamke huyo akawa anamtazama Darren kwa macho ya kumpembua. Kidogo akashusha macho yake kwa mtoto na kumtazama kwa sekunde kadhaa, alafu akasema kwa sauti ya kukoroma, sauti ya chini, “namtaka huyo mtoto.” alafu akahema kwanguvu na kusema kwa sauti ya hewa, “Nipatie, nami nitaenda nisirudi nyuma!”

“Wewe ni nani?” Darren akauliza akiwa anamshikilia vema mwanaye. Alikuwa amejiminyia kwenye kona akitamani kutoboa ukuta atokee nje.

Yule kiumbe akamtazama Darren alafu akapindishia shingo yake kushoto. Aliporejesha shingo yake kulia, akasema, “Mimi Melissa.”

“Melissa!” Darren akastaajabu. Hakujua alipata wapi nguvu ila alijikuta akisimama huku akitusi na kulaani. “nimekwambia kaa mbali na mimi Melissa!” punde akazabwa kofi lililomtupia ukutani yeye na mwanaye. Kwa muda kidogo akashindwa kuelewa kinachoendelea. Kwa mbali alisikia sauti ya mwanae ikilia sana lakini hakuwa anaweza kufanya kitu.

Kama baada ya dakika tano, akiwa ameanza kupata nguvu, akasikia sauti yaita,

“Hey! Helloooow!” kidogo mwanga ukatua kwenye macho yake yalofumba, akayafinya na kuyafumbua akiwa anajikinga na mkono wake wa kuume.

“Upo sawa?” alisikia sauti inauliza. Kidogo akabaini sauti hiyo inatokea dirishani. Walikuwa ni majirani, wanaume wawili. Mmoja alikuwa amebebelea bunduki kubwa na mwingine amebebelea gongo kubwa na kurunzi. Walikuwa wamesikia zile kelele na walikuja kutazama jirani yao amepatwa na nini.

Kabla Darren hajajibu kitu, alitazama kwanza kando yake kumtafuta mwanaye. Akamwona akiwa amelala kama hatua tatu tokea alipo. Alikuwa kwenye ukimya wa mbao. Na dada wa kazi alikuwa amelala kwa pembeni yake naye akiwa kimya.

Upesi akamfuata mwanaye na kumtazama. Hakuwa na dalili ya uhai. Alimwita na kumwita lakini ikiwa bure, mtoto hakuitika kwa kucheka wala kulia. Darren akapatwa na hofu kubwa sana ya kumpoteza mwanaye. Alimtikisatikisa aone kama ataamka lakini napo haikusaidia. Mtoto alikuwa amenyamaza. Alikuwa amenyazama milele.

Darren akapiga magoti na kugugumia kwa kilio. Alipata hasira sana. Alinyanyuka kama mbogo akamwendea dada wake wa kazi na kumvuta kwanguvu akimuuliza amemfanya nini mtoto wake, lakini dada naye alikuwa kimya. Hakuweza kuongea wala kujitetea kwa njia yoyote ile.

Darren asijali, akaanza kumuadhibu dada huyo kwa kumkandika mateke. “Shetani! Shetani! Shetani mkubwa wewe! Nitakuua!”

Kama si majirani kuvunja mlango na kuja kumshika, sijui hatma ilikuwa ni nini. Waligundua dada wa kazi alikuwa yu mzima, ila kama mtu aliyekuwa kwenye ‘coma’, hali mfu ya kupoteza fahamu, ila mtoto alikuwa amekwishafariki.

Basi dada wa kazi akawahishwa hospitali kwa matibabu zaidi. Mtoto naye akapelekwa huko kuhifadhiwa kwa ajili ya mazishi, na Darren pia, kwakuwa alihisiwa anaweza akawa si mzima, naye akapelekwa hospitali.


**

Baada ya juma moja …

Darren alikuwa ameketi kwenye kingo ya bahari. Alikuwa amevalia bukta na miguu yake ikiwa tupu pasi na viatu.

Upepo ukimpuliza taratibu, alikuwa anatazama bahari kwa umakini. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani ingawa macho yake yalikuwa yanatazama mawimbi ya bahari. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea mchanga, ila akiwa ameuminya kana kwamba anataka kuukosesha hewa.

Macho yake mekundu yalitazama mbali na karibu ya bahari. Yalitazama kushoto na kisha kulia ya bahari alafu akashusha pumzi ndefu. Akanyanyuka na kuanza kurandaranda.

Alitembea akiwa anawaza na kuwazua kichwani mwake. Kila alipofunga macho alimwona mwanae, alimwona mkewe. Ilikuwa ni ajabu na ghafla kwake. Kuna muda hakuwa anaamini kama Josephine hakuwapo naye, wala mtoto wao. Ilikuwa inamuwia ugumu sana kuamini kuwa yu mwenyewe hatimaye.

Alihisi maisha yake yanaparanganyika kama kioo kilichobondwa na jabali. Alikuwa anahisi hana umuhimu wowote maishani hivi sasa. Alikuwa anajihisi mfu anayetembea.

Alikunja ngumi yake akiendelea kutembea. Aling’ata meno yake na kutazama bahari tena, alafu punde akasema, “Melissa!” kwa sauti ya kufifia. Akarudia tena, “Melissa. Melissa. Melissa!” alafu akaapa, “Nitakumaliza kwa mkono wangu mwenyewe. Nitakumaliza Melissa!” alipomaliza kusema maneno hayo macho yake yakawa yanamwaga machozi. Alishindwa kujizuia kuumia. Moyo wake ulikuwa unavuja damu.

Jua likiwa linaanza kuwa kali kumaliza asubuhi, Darren akajirejesha kwenye gari lake na kutimka kuelekea upande wa magharibi. Alitembea kwenye gari kwa takribani masaa matatu kabla ya kuja kukomea kwenye nyumba kubwa namba 4089 kibaoni. Nyumba ya mwanamke yule aliyemwona mtandaoni kwa swala la mtoto wake kuwa na chapa mwilini.

Kabla hajashuka na kuzama humo, akalipekua kwanza jengo hilo kwa macho yake mepesi, kisha akashuka na kuliendea. Alipogonga kidogo akafunguliwa na mlinzi, akajitambulisha na mlinzi akamruhusu kuingia ndani maana alikuwa na miadi na mwenye nyumba.


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom