*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 23*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Baada ya maelezo hayo, dada huyo akaenda chumbani kwake akimwacha Darren na mwanaye pale sebuleni. Darren akatoa taarifa polisi juu ya kumpata mwanaye.
“... Nashukuru sana, nitakuwa mwangalifu zaidi siku nyingine.”
Alipokata simu ndipo akagundua kuna kitu kwa mwanaye.
ENDELEA
Nyuma ya mgongo wa mwanaye, chini kidogo ya bega la kushoto, aligundua kuna chapa fulani ndogo. Chapa hiyo ilikuwa nyeusi yenye ishara kama ya msalaba lakini ikiwa na mikono miwili.
Hakujua maana ya chapa hiyo lakini alijikuta akiwa na wasiwasi nayo. Alijaribu kuifuta kwa kutumia kidole chake, haikufutika. Akajaribu kumfuta na kitambaa bado napo haikufutika, ilikuwa ni alama ya kudumu!
Upesi akamuuliza dada wa kazi apate kujua nini kimemtokea mtoto. Lakini dada, akiwa ameparamiwa na uso wa hofu, akajitetea sana. Hakuwa anafahamu lolote. Hakuwa anajua hata kama mtoto ana chapa hiyo? Amemwogesha jana yake na hata siku hiyo asubuhi lakini hakuona alama kama hiyo.
Darren akatingwa na maswali lakini pia na hofu. Hakuhisi kama mwanaye yuko salama. Kila mara alitazama alama hiyo na kujiuliza maswali mengi kichwani. Mwishowe aliona ni kheri akafanya jitihada zaidi kung’amua chapa hiyo na hapo ndipo akazama kwenye mtandao na kusaka alama ile baada ya kuiweka kwenye mashine yake.
Baada ya muda kidogo akapata kuona taarifa chache juu ya chapa hiyo ikiwa inahusishwa na habari za zamani sana kuhusu huko Uajemi tena ni ishara aghalabu ya majini!
Alipotafuta sana akabaini kuwa mwanawe hakuwa mtu wa kwanza kuwa nayo, takribani watu watatu walikuwa nayo, ila mwisho wao wote ilikuwa ni kifo! Alipohangaika zaidi kutafuta mengineyo, akapata kukutana na mwanamke mmoja ambaye mwanaye alikuwa na chapa hiyo. Alituma hilo swala mtandaoni kuomba ushauri.
Basi hilo likawa kama neema kwa Darren. Alitafuta zaidi taarifa za mwanamke huyo akafanikiwa kupata anwani yake, akapanga kesho yake akamtafute amwambie zaidi kuhusu hiyo chapa.
Alihofia sana juu ya mwanaye. Na kwa hofu hiyo akataka alalae nae ndani ya chumba chake.
Ulipofika usiku wa manane, Darren akiwa amelowea kwenye usingizi mzito, na pia nyumba ikiwa imetulia tuli sawa sawa na mtaa mzima, taratibu mlango wa chumba alalacho dada wa kazi, ulifunguliwa na kisha ukatuama pasipo lolote kutokea.
Kulikuwa kimya.
Zilipopita kama sekunde tano, ndipo mkono uliobebelea kisu ukatoka kwenye mlango huo. Bada ya punde, ukafuatia na mguu na kisha mtu mzima kabisa. Alikuwa ni yule dada wa kazi.
Aliyatoa macho yake akikodoa. Alitazama kushoto na kisha kulia, alafu akauendea ule mlango wa chumba cha Darren. Alipoufikia, hakugonga, lah! Akapindua kitasa taratibu na mlango huo ukafunguka. Alipousogeza vya kutosha, akatulia hapo akisimama.
Zikapita kama sekunde nne. Basi taratibu akazamisha mguu wake ndani ya chumba, na taratibu sana, akaweka nyayo zake sakafuni akisonga. Alimwendea mtoto na kumpakua toka kwenye kitanda chake. Lakini mikono yake ilikuwa ya baridi sana. Alipomshika mtoto tu, akaanza kulia.
Akakodoa kumtazama Darren. Darren alikuwa amelala bado fofofo. Lakini sauti ya mtoto iliyokuwa inaendelea kupaza na kupaza ilimshtua sasa akaamka na kuangaza.
alipotazama kwenye kitanda cha mtoto, hakukuwa na kitu. Kitanda kilikuwa tupu kikianza kujenga ubaridi! Akachanganyikiwa sana. Alitazama kushoto na kulia kwake asione kitu, mlango ulikuwa umefungwa, ila sauti ya mtoto bado akiisikia!
Sauti hiyo ilikuwa ikiishilia!
Haraka akatoka kitandani na kudaka korido. Akatazama na kupekua kwa macho yake, kidogo, masikio yake yakamwambia kuwa sauti ya mtoto inatokea kwenye chumba cha dada yake wa kazi!
Akauendea mlango huo na kubisha kwa kuutwanga ngumi. Akaukandika na kuukandika lakini haukufunguliwa. Mtoto bado aliendelea kulia!
Akiwa amepandwa na akili za ukichaa, Darren akaubamiza teke kali mlango huo na kuuvunjia mbali. Alipotazama, akamwona dada wa kazi akiwa amemkabia mtoto kitandani kwa kutumia mkono wa kushoto na ule wa kulia ukiwa umeshikilia kisu akitaka kumchoma.
“Tafadhali, usimuue mwanangu!” Darren akapaza sauti akimtazama dada wa kazi kwa imani. Dada akatabasamu na kusema, “Lazima afe, Darren. Hata kama nisipomuua mimi!”
“Kwanini?” Darren akalia. “Kwanini afe? Sina kitu kingine mbali na huyo mtoto. Nambie unataka nini nitakupatia!”
Dada akatabasamu almanusura kucheka. Alimtazama mtoto kisha akayarudisha macho yake kwa Darren na kusema, “Sitaki chochote Darren. Kama ningekuwa nataka chochote kile basi ningekitafuta na kukichukua mwenyewe. Kwa sasa ninachotaka ni roho ya huyu kiumbe tu, si kingine!”
“Lakini amekukosea nini?” Darren akauliza. Macho yake yalikuwa mekundu yakikaribia kudondosha chozi.
“Hajafanya kitu,” Dada akajibu akitikisa kichwa. “ila si mali yako tena. Huyu ni mali ya majini, na ni wa kufa tu!”
Dada aliposema hayo akamkandika mtoto kisu cha kifuani, chote kikazama na kutosha kumfanya mtoto mfu. Darren akalia sana. Akakurupuka toka kitandani mwake na kumtazama mwanaye pembeni. Nalikuwa ni ndoto. Mtoto alikuwa yu kwenye kitanda chake ila akilia sana.
Upesi akamnyanyua na kujitahidi kumbembeleza … sh!-sh!-sh!-sh!-sh!-sh! … lakini alipotazama dirishani akabaini kuwa li wazi. Akalisongea na kutazama nje kama kuna lolote lile, hakuona jambo. Mtaa ulikuwa umetulia sana. Ni upepo wa baridi ndio ulikuwa ukipuliza tena kwa mbali.
Akalifunga dirisha hilo, bado mtoto akilia, alipomaliza akasikia hodi mlangoni mwake. Kidogo mapigo yake yakaruka. Akiwa amemshikilia mtoto wake vema, akapaza sauti kuuliza,
“Nani?”
“Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni. Kidogo akajawa na mashaka.
“Unataka nini?”
“Nimemsikia mtoto analia. Vipi kuna shida?”
“Hapana. Hamna shida.”
“Naweza kukusaidia kumbembeleza?”
Darren akasita kwanza.
“Hapana, ahsante. Nitambembeleza mwenyewe.”
Baada ya hapo sauti ya dada haikusikika tena bali mtoto akiwa analia tu. Darren akaendelea kumbembeleza mwanaye akimsihi anyamaze kwani usiku umekuwa mkubwa na yeye amechoka sana. Kwa kama lisaa limoja, mtoto akaendelea kulia tu, akipunguza sauti na kurudi tena upya.
Darren akachoka sana kumbembeleza, mikono ikawa inamuuma, macho yanamsaliti kwa kuwa mazito, kichwa nacho kinachoshwa na sauti kali ya mtoto.
Mlango ukagongwa tena.
“Nani?” akauliza kwa sauti ya uchovu.
“Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni.
“Unataka nini?”
“Mtoto ana shida gani?”
“Amekurupuka tu toka usingizini, usijali. Unaweza kulala.”
“Naweza kukusaidia?”
“Hapana! Usijali, nitambembeleza mwenyewe mpaka alale.”
Basi baada ya hapo sauti ya dada wa kazi haikusikika tena, Darren akaendelea kumbembeleza mtoto. Kwa kama nusu saa akawa anafanya zoezi hilohilo tu. Kila alipojaribu kumweka mtoto kitandani ambembelezee hapo, ikawa tabu zaidi, mtoto aliongeza kilio.
Hakujua sasa cha kufanya. Kila mtindo alitumia lakini haikusaidia. Ilifikia kipindi akawa anapitiwa na usingizi ingali amesimama. Alimweka mtoto kitandani kwa kulazimisha akaendelea kumbembeleza hapohapo, kidogo akapitiwa na usingizi.
Kama baada ya dakika mbili akakurupushwa na hodi ya tatu mlangoni mwake. Akauliza, “Nani?”
“Dada wa kazi!”
“Unataka nini?”
“Mtoto anasumbuliwa na nini?” dada akauliza.
“Si nilishakwambia!” Darren akafoka kidogo.
“Naomba nimbembeleze,” sauti ya dada ikaomba.
“Nimesema nambembeleza mwenyewe. Hukunielewa?”
Kukawa kimya kidogo.
Punde sauti ya dada ikasema tokea mlangoni, “Utanipa nimbembeleze ama nije nimchukue mwenyewe?” mara hii sauti ilikuwa na amri ndani yake.
.
.
.
***