*UNA NINI LAKINI MELISSA? -- 25*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Jua likiwa linaanza kuwa kali kumaliza asubuhi, Darren akajirejesha kwenye gari lake na kutimka kuelekea upande wa magharibi. Alitembea kwenye gari kwa takribani masaa matatu kabla ya kuja kukomea kwenye nyumba kubwa namba 4089 kibaoni. Nyumba ya mwanamke yule aliyemwona mtandaoni kwa swala la mtoto wake kuwa na chapa mwilini.
Kabla hajashuka na kuzama humo, akalipekua kwanza jengo hilo kwa macho yake mepesi, kisha akashuka na kuliendea. Alipogonga kidogo akafunguliwa na mlinzi, akajitambulisha na mlinzi akamruhusu kuingia ndani maana alikuwa na miadi na mwenye nyumba.
ENDELEA
Baada ya punde kidogo alionana na mwanamke aitwaye Charlie, mwanamke mrefu mwembamba mwenye nywele fupi nyeusi. Alikuwa mjawa ukarimu na mwenye wingi wa tabasamu ila uso wenye hisia. Mwanamke huyo alimkarimu Darren kwa namna iliyomfanya Darren ahisi angalau ahueni.
Ndipo akamwambia yale yaliyowahi kumtukia. Namna alivyohangaika na mtoto wake katika namna ya ajabu.
“Nilipata shida sana. Nilitafuta kila namna lakini haikusaidia. Na nakumbuka vema ikiwa ni usiku wa manane, nikampoteza mwanangu wa pekee!”
Darren akataka kujua zaidi kumhusu mwanamke huyo. Mbali na mtoto je yeye alishawahi kukumbwa na kadhia yoyote ile? Basi mwanamke yule akaeleza kuwa kwa kitambo kifupi baada ya mama na baba yake kufariki, ndipo alipoanza kuona mambo fulani ya ajabu ndani ya mji wao. Mwanzoni alikuwa anadhani anawehuka na labda ana laana na ule mji, hivyo akafanya kuhama aende mbali.
Alipoenda huko, akatuama na kuanzisha familia ambayo iliishi kwa amani mpaka pale mambo yalipokuja kuibukia katika namna ambayo hakuwa anaweza kuelewa vema.
“Ninachokumbuka ni kwamba, baada ya tetemeko kubwa la ardhi lilitokea miaka mitano nyuma, maisha yangu yakaanza kubadilika kwa wepesi sana. Sikuwa tena mtu wa amani bali kuona vituko na viroja. Mtu wa kuona mambo ya ajabu yasiyokuwa na mithili. Ajabu ni kwamba, baada ya mtoto wangu kufariki, mambo hayo yalipotea mpaka sasa.”
“Na vipi kuhusu mume wako?” Darren akadadisi. Charlie akatabasamu kwanza ila macho yake yakiwa kinyume. Alitazama chini kwa sekunde chache kabla hajabinua kinywa chake na kusema, “Alikuwa mwanaume niliyekuwa namhitaji. Mwenye kujali na kujua kupenda. Nilijihisi nimekamilika nilipokuwa naye. Alinifanya nisahau kifo cha wazazi wangu kwa muda kwani alikalia sehemu tupu ambayo iliachwa wazi.”
Akadondosha chozi. Akalifuta kwa kidole chake onyeshi kabla hajaendelea kuongea, “nilimpoteza kwenye ajali!” akapandisha mabega yake akisema, “sijui nini kilitokea lakini aliacga daraja na kutumbukia baharini. Waokozi walipokuja kumtazama, hakuwa hai tena.”
“Gari lake lilipata hitilafu?” Darren akauliza.
“Sidhani,” Charlie akajibu. “Gari lake lilikuwa sawa kabisa isipokuwa tu sehemu ambayo iligonga daraja. Sijajua kumhusu yeye. Sijajua alikuwa kwenye hali gani. Ila kwa mujibu wa shuhuda wa tukio, mume wangu alibamiza kioo chake cha pembeni kwanguvu kabla gari halijapoteza mwelekeo na kudumbukia.”
Kwa namna moja Darren akaona simulizi ya huyo mwanamke inawiana na ya kwake. Kwa kutaka kuhakikisha zaidi, akamuuliza Charlie, “Kuna mtu yeyote ambaye ulikuwa naye kwenye mahusiano kabla ya mumeo? Namaanisha mpenzi wako wa kwanza?”
Charlie akafikiri kidogo kabla hajasema, “Niliwahi kuwa naye. Ila ni kipindi cha zamani za utotoni. Sichukulii mahusiano yale kama yalikuwa serious.”
“Je haujawahi kumwona mwanaume huyo uliyewahi kuwa naye kwenye mahusiano? Yaani baada ya kuoana na mumeo? Au kipindi chochote kwa namna yoyote?”
“Hapana,” Charlie akakataa. “Sijawahi kuonana naye tangu kipindi hicho.”
Hapa kidogo Darren akajiona ni wa tofauti na Charlie. Mbona yeye anasumbuliwa na Melissa? Basi akaamua naye kumshirikisha Charlie kuhusu habari zake. Alipomaliza kumweleza kila kitu, Charlie akamuuliza Darren, “Unapajua anapokaa huyo Melissa?”
“Ndio, napajua,” Charlie akajibu.
“Naweza nikaonana naye?” Charlie akauliza akiwa ametoa macho kidogo.
“Unahitaji kuonana naye?”
“Ndio, kama itawezekana.”
Darren akanyamaza kidogo kisha akasema, “Si mtu mzuri kama unavyoweza kudhani.”
“Najua,” Charlie akamkatiza. “Sitegemei awe mtu mzuri, ila ningependa kuonana naye.”
“Kwanini? Huoni utakuwa umejiweka kwenye hatari?”
“Hatari ipi, Darren? Nimepoteza mume na mtoto wangu, kuna hatari nyingine zaidi ya hiyo?”
Kimya kidogo. Charlie akaendelea kuzungumza, “Nadhani kuna maswali yangu atakuwa na majibu nayo.”
“Yapi hayo?”
Hapa Charlie akamweleza Darren kuwa anahisi mama yake alikuwa ni mtu mwenye agano tokea nyuma. Mara kwa mara mama yake alikuwa anamwambia kuwa maisha yake hayatakuwa ya furaha kwakuwa yeye ni kizazi cha shetani. Damu yake inachembechembe za majini. Alipotaka kujua zaidi, mama yake hakumweleza kwa kumwambia muda bado mpaka pale utakapowadia na basi atajua.
“Una picha ya mama yako?” Darren akauliza. Charlie akafungua simu yake na kumwonyesha Darren picha ya mama yake, “huyu hapa wa kwanza upande wa kulia.” darren alipotazama vema, akagundua sura ya mama huyo haikuwa ngeni. Ilikuwa ni sura anayoijua. Aliionea wapi? Akajiuliza akirusha macho huku na kule.
“Vipi, Darren?” Charlie akamuuliza.
“Nahisi namjua huyu mtu,” Darren akajibu akiendelea kufikiri na punde akakumbuka. Sura hiyo aliionea kwenye ile picha ambayo aliipata kwenye jengo la bibi yake! Akamweleza Charlie habari hiyo.
“Kweli?” Charlie akastaajabu.
“Ndio, ni kweli!” Darren akaapa. Basi Charlie akafikiria kwa udogo na kusema, “Darren, nadhani sasa utakuwa unaona kuna haja gani ya kuonana na Melissa. Yeye anaweza kutueleza mambo haya kwa undani.”
Darren akashika kichwa, “Lakini Melissa si mtu mzuri hata kidogo. Ameyfanya maisha yangu yawe magumu kupita kiasi. Sikutaka kabisa kuhusiana naye.”
Charlie akauweka mkono wake begani mwa Darren, “sikia, Darren. Hatuna machaguzi hapa. Na kati ya wewe na mimi, hakuna mwenye maelezo ya kumtosha mwenzake isipokuwa huyo Melissa. Hima twende tukamwone!”
Darren akafikiri kidogo kabla hajanyanyuka na kumpakia Charlie kwenye gari yake, safari ikaanza. Walitembea kwa muda wa kama nusu saa pasipo kuzungumza. Charlie ndiye alikuja kuuvunja ukimya kwa kumuuliza Darren, “Ulimpenda Melissa?”
Darren akanyamaza kwanza kama mtu anayepangilia jibu kichwani kisha akasema kwa ufupi, “Ndio.”
“Na yeye alikupenda?” Charlie akauliza akimtazama Darren anayatazama mbele.
“Sidhani,” Darren akajibu.
“Haudhani?”
“Ndio. Kama angekuwa ananipenda basi angeniweka bayana kila kitu,”
“Kila kitu kama kipi Darren? Kuwa yeye ni jini aliyeishi na bibi zetu tuokea huko nyuma? … ungemwelewa? Ungeendelea kuwa naye?”
“Charlie, sijui haya mambo yaendavyo. Ila nisingeweza kuishi na Melissa zaidi. Unawezaje kufanya hivyo punde unapohisi kuwa uliyenaye si binadamu?”
Charlie akanyamaza asinene tena. Wakaumaliza huo mjadala. Kwenye majira ya saa tano za usiku wakawa wamewasili kwenye makazi ya Robson. Hapo waliposhuka, Charlie akauliza, “Hapa ndipo kwake?”
“Hapana, bali kwa mpenzi wake! Nadhani atakuwapo hapa,” Darren akaji bu wakisonga.
“Na vipi kama hatokuwapo?” Charlie akauliza.
“Basi mpenzi wake atakuwa anajua alipo,” Darren akamalizia kauli na kubisha hodi mara tatu. Punde akafunguliwa na Robson ambaye alishangaa kumwona Darren hapo wakati huo.
“Vipi, Darren?”
“Naweza kuonana na Melissa?” Darren akaenda moja kwa moja kwenye lengo lililomleta.
“Vipi, kuna tatizo?” Robson akauliza.
“Ndio, lipo,” Darren akajibu na kisha akarudia tena kauli yake, “Naweza kuonana na Melissa?”
Robson akawafungulia mlango wakaingia ndani. Ila walipoketi, simu ya Darren ikaingiwa na ujumbe. Alipoutazama kuusoma, ulikuwa unatokea kwa Melissa.
“Sipo hapo. Nikuteni fukweni,” ujumbe ulisoma.
***