Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

mmh... .... jamaa wanajiona kiama kitoto .... ... ...kazungukwa!
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? -- 25*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Jua likiwa linaanza kuwa kali kumaliza asubuhi, Darren akajirejesha kwenye gari lake na kutimka kuelekea upande wa magharibi. Alitembea kwenye gari kwa takribani masaa matatu kabla ya kuja kukomea kwenye nyumba kubwa namba 4089 kibaoni. Nyumba ya mwanamke yule aliyemwona mtandaoni kwa swala la mtoto wake kuwa na chapa mwilini.

Kabla hajashuka na kuzama humo, akalipekua kwanza jengo hilo kwa macho yake mepesi, kisha akashuka na kuliendea. Alipogonga kidogo akafunguliwa na mlinzi, akajitambulisha na mlinzi akamruhusu kuingia ndani maana alikuwa na miadi na mwenye nyumba.

ENDELEA

Baada ya punde kidogo alionana na mwanamke aitwaye Charlie, mwanamke mrefu mwembamba mwenye nywele fupi nyeusi. Alikuwa mjawa ukarimu na mwenye wingi wa tabasamu ila uso wenye hisia. Mwanamke huyo alimkarimu Darren kwa namna iliyomfanya Darren ahisi angalau ahueni.

Ndipo akamwambia yale yaliyowahi kumtukia. Namna alivyohangaika na mtoto wake katika namna ya ajabu.

“Nilipata shida sana. Nilitafuta kila namna lakini haikusaidia. Na nakumbuka vema ikiwa ni usiku wa manane, nikampoteza mwanangu wa pekee!”

Darren akataka kujua zaidi kumhusu mwanamke huyo. Mbali na mtoto je yeye alishawahi kukumbwa na kadhia yoyote ile? Basi mwanamke yule akaeleza kuwa kwa kitambo kifupi baada ya mama na baba yake kufariki, ndipo alipoanza kuona mambo fulani ya ajabu ndani ya mji wao. Mwanzoni alikuwa anadhani anawehuka na labda ana laana na ule mji, hivyo akafanya kuhama aende mbali.

Alipoenda huko, akatuama na kuanzisha familia ambayo iliishi kwa amani mpaka pale mambo yalipokuja kuibukia katika namna ambayo hakuwa anaweza kuelewa vema.

“Ninachokumbuka ni kwamba, baada ya tetemeko kubwa la ardhi lilitokea miaka mitano nyuma, maisha yangu yakaanza kubadilika kwa wepesi sana. Sikuwa tena mtu wa amani bali kuona vituko na viroja. Mtu wa kuona mambo ya ajabu yasiyokuwa na mithili. Ajabu ni kwamba, baada ya mtoto wangu kufariki, mambo hayo yalipotea mpaka sasa.”

“Na vipi kuhusu mume wako?” Darren akadadisi. Charlie akatabasamu kwanza ila macho yake yakiwa kinyume. Alitazama chini kwa sekunde chache kabla hajabinua kinywa chake na kusema, “Alikuwa mwanaume niliyekuwa namhitaji. Mwenye kujali na kujua kupenda. Nilijihisi nimekamilika nilipokuwa naye. Alinifanya nisahau kifo cha wazazi wangu kwa muda kwani alikalia sehemu tupu ambayo iliachwa wazi.”

Akadondosha chozi. Akalifuta kwa kidole chake onyeshi kabla hajaendelea kuongea, “nilimpoteza kwenye ajali!” akapandisha mabega yake akisema, “sijui nini kilitokea lakini aliacga daraja na kutumbukia baharini. Waokozi walipokuja kumtazama, hakuwa hai tena.”

“Gari lake lilipata hitilafu?” Darren akauliza.

“Sidhani,” Charlie akajibu. “Gari lake lilikuwa sawa kabisa isipokuwa tu sehemu ambayo iligonga daraja. Sijajua kumhusu yeye. Sijajua alikuwa kwenye hali gani. Ila kwa mujibu wa shuhuda wa tukio, mume wangu alibamiza kioo chake cha pembeni kwanguvu kabla gari halijapoteza mwelekeo na kudumbukia.”

Kwa namna moja Darren akaona simulizi ya huyo mwanamke inawiana na ya kwake. Kwa kutaka kuhakikisha zaidi, akamuuliza Charlie, “Kuna mtu yeyote ambaye ulikuwa naye kwenye mahusiano kabla ya mumeo? Namaanisha mpenzi wako wa kwanza?”

Charlie akafikiri kidogo kabla hajasema, “Niliwahi kuwa naye. Ila ni kipindi cha zamani za utotoni. Sichukulii mahusiano yale kama yalikuwa serious.”

“Je haujawahi kumwona mwanaume huyo uliyewahi kuwa naye kwenye mahusiano? Yaani baada ya kuoana na mumeo? Au kipindi chochote kwa namna yoyote?”

“Hapana,” Charlie akakataa. “Sijawahi kuonana naye tangu kipindi hicho.”

Hapa kidogo Darren akajiona ni wa tofauti na Charlie. Mbona yeye anasumbuliwa na Melissa? Basi akaamua naye kumshirikisha Charlie kuhusu habari zake. Alipomaliza kumweleza kila kitu, Charlie akamuuliza Darren, “Unapajua anapokaa huyo Melissa?”

“Ndio, napajua,” Charlie akajibu.

“Naweza nikaonana naye?” Charlie akauliza akiwa ametoa macho kidogo.

“Unahitaji kuonana naye?”

“Ndio, kama itawezekana.”

Darren akanyamaza kidogo kisha akasema, “Si mtu mzuri kama unavyoweza kudhani.”

“Najua,” Charlie akamkatiza. “Sitegemei awe mtu mzuri, ila ningependa kuonana naye.”

“Kwanini? Huoni utakuwa umejiweka kwenye hatari?”

“Hatari ipi, Darren? Nimepoteza mume na mtoto wangu, kuna hatari nyingine zaidi ya hiyo?”

Kimya kidogo. Charlie akaendelea kuzungumza, “Nadhani kuna maswali yangu atakuwa na majibu nayo.”

“Yapi hayo?”

Hapa Charlie akamweleza Darren kuwa anahisi mama yake alikuwa ni mtu mwenye agano tokea nyuma. Mara kwa mara mama yake alikuwa anamwambia kuwa maisha yake hayatakuwa ya furaha kwakuwa yeye ni kizazi cha shetani. Damu yake inachembechembe za majini. Alipotaka kujua zaidi, mama yake hakumweleza kwa kumwambia muda bado mpaka pale utakapowadia na basi atajua.

“Una picha ya mama yako?” Darren akauliza. Charlie akafungua simu yake na kumwonyesha Darren picha ya mama yake, “huyu hapa wa kwanza upande wa kulia.” darren alipotazama vema, akagundua sura ya mama huyo haikuwa ngeni. Ilikuwa ni sura anayoijua. Aliionea wapi? Akajiuliza akirusha macho huku na kule.

“Vipi, Darren?” Charlie akamuuliza.

“Nahisi namjua huyu mtu,” Darren akajibu akiendelea kufikiri na punde akakumbuka. Sura hiyo aliionea kwenye ile picha ambayo aliipata kwenye jengo la bibi yake! Akamweleza Charlie habari hiyo.

“Kweli?” Charlie akastaajabu.

“Ndio, ni kweli!” Darren akaapa. Basi Charlie akafikiria kwa udogo na kusema, “Darren, nadhani sasa utakuwa unaona kuna haja gani ya kuonana na Melissa. Yeye anaweza kutueleza mambo haya kwa undani.”

Darren akashika kichwa, “Lakini Melissa si mtu mzuri hata kidogo. Ameyfanya maisha yangu yawe magumu kupita kiasi. Sikutaka kabisa kuhusiana naye.”

Charlie akauweka mkono wake begani mwa Darren, “sikia, Darren. Hatuna machaguzi hapa. Na kati ya wewe na mimi, hakuna mwenye maelezo ya kumtosha mwenzake isipokuwa huyo Melissa. Hima twende tukamwone!”

Darren akafikiri kidogo kabla hajanyanyuka na kumpakia Charlie kwenye gari yake, safari ikaanza. Walitembea kwa muda wa kama nusu saa pasipo kuzungumza. Charlie ndiye alikuja kuuvunja ukimya kwa kumuuliza Darren, “Ulimpenda Melissa?”

Darren akanyamaza kwanza kama mtu anayepangilia jibu kichwani kisha akasema kwa ufupi, “Ndio.”

“Na yeye alikupenda?” Charlie akauliza akimtazama Darren anayatazama mbele.

“Sidhani,” Darren akajibu.

“Haudhani?”

“Ndio. Kama angekuwa ananipenda basi angeniweka bayana kila kitu,”

“Kila kitu kama kipi Darren? Kuwa yeye ni jini aliyeishi na bibi zetu tuokea huko nyuma? … ungemwelewa? Ungeendelea kuwa naye?”

“Charlie, sijui haya mambo yaendavyo. Ila nisingeweza kuishi na Melissa zaidi. Unawezaje kufanya hivyo punde unapohisi kuwa uliyenaye si binadamu?”

Charlie akanyamaza asinene tena. Wakaumaliza huo mjadala. Kwenye majira ya saa tano za usiku wakawa wamewasili kwenye makazi ya Robson. Hapo waliposhuka, Charlie akauliza, “Hapa ndipo kwake?”

“Hapana, bali kwa mpenzi wake! Nadhani atakuwapo hapa,” Darren akaji bu wakisonga.

“Na vipi kama hatokuwapo?” Charlie akauliza.

“Basi mpenzi wake atakuwa anajua alipo,” Darren akamalizia kauli na kubisha hodi mara tatu. Punde akafunguliwa na Robson ambaye alishangaa kumwona Darren hapo wakati huo.

“Vipi, Darren?”

“Naweza kuonana na Melissa?” Darren akaenda moja kwa moja kwenye lengo lililomleta.

“Vipi, kuna tatizo?” Robson akauliza.

“Ndio, lipo,” Darren akajibu na kisha akarudia tena kauli yake, “Naweza kuonana na Melissa?”

Robson akawafungulia mlango wakaingia ndani. Ila walipoketi, simu ya Darren ikaingiwa na ujumbe. Alipoutazama kuusoma, ulikuwa unatokea kwa Melissa.

“Sipo hapo. Nikuteni fukweni,” ujumbe ulisoma.


***
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 26*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Vipi, kuna tatizo?” Robson akauliza.

“Ndio, lipo,” Darren akajibu na kisha akarudia tena kauli yake, “Naweza kuonana na Melissa?”

Robson akawafungulia mlango wakaingia ndani. Ila walipoketi, simu ya Darren ikaingiwa na ujumbe. Alipoutazama kuusoma, ulikuwa unatokea kwa Melissa.

“Sipo hapo. Nikuteni fukweni,” ujumbe ulisoma.

ENDELEA

Upesi Darren na Charlie wakaelekea huko ufukweni ambapo Melissa alikuwapo, na kweli wakamkuta akiwa ameketi mchangani akitazama maji ya bahari. Mbali na hivyo kulikuwa kimya sana isipokuwa upepo.

Darren akamwita Melissa akiwa anamtazama, naye Melissa akamtazama na kumkaribisha, “Nadhani hapa ni eneo zuri la kufanyia maongezi.” Darren na Charlie wakaketi wakimweka Melissa katikati yao.

“Ulimwambia Robson kama nipo huku?” Melissa akauliza.

“Hapana, hajui hilo,” Darren akajibu kisha akamuuliza Melissa kama anamjua mwanamke yule aliyekuja naye, yaani Charlie. Pasi na kumtazama, Melissa akasema anamfahamu hata kabla hajaja hapo.

Aliposema hayo akamtazama Darren. Macho yake yalikuwa tayari yameelekea kuwa mekundu. Akamshika mkono na kumuuliza kwa upole, “Darren, utasadiki nitakayokuambia?”

Darren alipojibu swali hilo, Melissa akamuuliza na Charlie swali hilohilo. Alipolijbiwa ndipo akaanza kunena. Darren na Charlie wakawa wametega masikio yao vema kabisa. Japokuwa upepo ulikuwa unapuliza, bado sauti ya Melissa ilisikika vema.

“Pengine mimi naweza nikawa mtu mbaya sana kwenye vichwa vyenu. Hamtaki kuniona na sifai kuwa hai wala kuwa mbele yenu hapa nilipo. Ila …” alipokomea hapo akamtazama Darren, “Kama si upendo wangu kwako, Darren. Basi usingalikuwa hai mpaka sasa. Haujui ni makovu mangapi umenisababishia kwa maneno yako lakini sikuwahi kuacha kukupenda.”

Aliweka kituo na kutazama bahari kwa sekunde kama sita akiwa kimya. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani mwake. Na basi alipojiona yu tayari ndipo akaendelea kunena ya kuwa hapo zamani kabisa ya miaka takribani mia tatu iliyopita, walikuwa kwenye familia kubwa ya bwana Roddeth. Bwana huyo alikuwa ni mtu mwenye nguvu kubwa na mwenye kuhofiwa sana.

Alikuwa na nguvu za ajabu. Watu wangekusanyika kwake awasaidie matatizo mbalimbali lakini kwa sharti la kutoa sadaka. Alikuwa si mtu wa kawaida bali jini, lakini alistahimili kuishi miongoni mwa binadamu. Na kwa uzao wake basi akapata watoto watano wa kike ambao kwa mujibu wa maelezo ya Melissa, mmoja wa hao watoto alikuwa ni yeye, na wengine ni pamoja na bibi yake Darren na Charlie na wengineo wawili.

Walikuwa ni watu wapendanao mpaka pale siku moja baba yao alipokufa na kugawa mali zao pasi na usawa. Walichukiana na kila mmoja akaelekea upande wake. Lakini kwasababu Melissa alikuwa ni kipenzi kikubwa wa baba yao basi ingali baba yupo kwenye kitanda chake cha kifo alimkabidhi mwanaye huyo kito cha moja ya mkufu wake akimwambia, “Utaishi milele, mimi safari yangu naona ikomee hapa.”

Alificha kito hicho kwa namna zote ili ndugu zake wasije kukiona na kumpokonya. Na kwake haikuwa ngumu sana kwani walikuwa tayari wameshatengana na kila mmoja akaenda njia yake binafsi.

Basi miaka ikapita kila mmoja akiwa na chuki na mwenzake na uadui pia. Kila mmoja akapata kuishi kwa namna ajuavyo huko mbali. Wengine wakafikia kuanzisha maisha kwa kuwa na mahusiano na binadamu.

“Halikuwa jambo jema. Baba yetu wakati yu hai alikuwa akitusisitiza juu ya hilo. Endapo tutakapokuwa kwenye mahusiano na binadamu basi si kwamba tutawafanya watoto waingie kwenye damu yetu isiyo ya kawaida, bali damu hiyo itawawinda na kuwaangusha,” alisema Melissa.

Lakini kwasababu za mapenzi, wenzao wawili walizaa na binadamu. Na kama ilivyokuwa neno la baba yao, watoto hao wakawa wanasumbuliwa kwa kutokewa na mambo ya ajabu wasiyoweza kuyaeleza. Mengine hata yakitishia uhai wao.

Kutokana na hayo ndipo binadamu hao wakawa wanatafuta tiba ya kujikinga dhidi ya maajabu waliyokumbana nayo. Na kila tiba walipoipata wakaifungia kwenye vitabu walivyovihifadhi maeneo ya mbali kabisa na makazi yao. Maeneo salama ambayo hayafikiwi na binadamu.

Vitabu hivyo vilikuwa ni vifungo vya kufunga yale yote yaliyokuwa yanawasumbua, na wakafanikiwa kufanya vivyo kwa muda.

“Shida ni kwamba, vitabu hivyo vinakuwa si vifungo tu bali hubeba roho za wale vinavyowalinda. Hivyo pale vinapopata madhara, basi na wale waliokuwa wanavimiliki hufa kwa aina hiyohiyo ya kifo,” maneno hayo ya Melissa ndiyo yakamkumbusha Darren kifo cha mama yake kilivyorandana na moto wa msitu. Akamuuliza naye Charlie akasema kuwa mama yake alikufa kwa kuzama maji ingali alikuwa chumbani mwake! Ikiwa ni muda mfupi baada ya tetemeko la ardhi kutokea.

“Baada ya hapo basi ndipo matatizo yenu yakaanza upya,” Melissa akaendelea soga, “Kwakuwa vifungo vilikuwa vimeenda basi ndiyo maana mambo ya ajabu yakaanza kuwatokea upya kwenye familia zenu, na itakuwa vivyo mpaka pale damu mliyobeba itakapotulizwa.”

Darren akamuuliza Melissa, “Mbona maisha yangu yalikuwa yametulia kabla ya kuja kukutana na wewe? Mbona kila mara ninapoonana na wewe huwa nakutana na jambo baya?”

Melissa akamtazama Darren akiwa anadondosha chozi, “Darren kamwe hautokuja kuelewa ni mangapi nilikuwa nayapitia kwasababu yako. Maisha yako kutuama kabla ya kuja kukutana na mimi haikuwa inamaanisha kuwa utakuwa sawa, lah! Na hilo halikuwa kwako peke yako bali pia kwa Charlie.

Mambo yalianza kubadilika si kwasababu ulikutana na mimi bali kwasababu ulikuwa umepata mtoto. Kama vilevile ilivyokuwa kwa Charlie. Mlikuwa mmefufua upya agano lenu, Darren,” Melissa alisema kwa sauti ya chini alafu akatazama chini kabla hajaendelea kunena, “Kila ulipokuwa unakutana na baya lolote, nami nilikuwapo pembeni, na ndiyo maana ulikuwa unatoka ama kushinda hai. Isingalikuwa hivyo, ungeshakufa muda mrefu Darren.”

“Na vipi kuhusu ile siku nilipoenda kwenye ile nyumba iliyotangazwa kwenye gazeti? Ilikuwa ni kweli ama ndoto kukuona pembeni ya gari yangu?” Darren akauliza. Melissa, bado akiwa anamtazama mwanaume huyo, akamjibu, “Yote yalikuwa ni uhalisia, Darren. Na ni mimi ndiye nilikurudisha pale kwenye gari lako upesi baada ya kuzidiwa na wale wadhalimu. Lakini uliponiona pembeni yako haukunipa muda nikajitetea, bali ukanijaza shutma na kunifukuza!”

“Kwanini hukuniambia yote hayo, Melissa?” Darren akauliza.

“Kwasababu haukunipa muda huo Darren. Maisha yako yote umekuwa ukinichukulia kama adui yako. Mtu ninayekusababishia mabaya na nuksi,” Melissa akieleza hayo machozi yakamtiririka zaidi. Na Charlie akagundua kuwa mwanamke huyo alikuwa akimomonyoka miguu yake kuwa udongo.

Akamshtua Darren atazame. Darren akapayuka kuuliza, “Melissa, nini kinatokea?” akiwa amemshika mkono mwanamke huyo. Melissa akatazama miguu yake inayomomonyoka na kisha akamtazama Darren na kusema, “Hii ndiyo gharama yangu kwa kusema haya. Yanipasa niende Darren. Maisha yangu yamekwisha hapa duniani.”

“Hapana Melissa, si una kito cha kuishi milele?” Darren akauliza.

“Sina kitu chochote Darren,” Melissa akasema akilaza kichwa chake kifuani mwa Darren, “Yote nimeyatoa kwa ndugu zangu kama sadaka ya kukubakiza wewe hai.” kisha akamtazama Darren na kumwambia, “lakini haikusaidia na wamenigeuka. Wanataka maisha yako, wanataka maisha yenu. Wanataka kila ambacho bibi yako alikuwa anamiliki. Siwezi kuwazuia tena, Darren. Sina nguvu hiyo.”

Melissa alipomaliza kauli hiyo, mwili wake ukawa umeshapukutika mpaka kufikia tumboni. Mwili uwake ulikuwa kichuguu cha mchanga. Akamwaga Darren, “Kwaheri, mpenzi”



**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom