*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 15*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Haraka akafunga dirisha kwa kushusha pazia alafu akabaki akisimama hapo kama ataona kitu. Na kweli, baada ya muda kidogo akaona kivuli cha mtu dirishani. Kivuli cha mwanamke mwenye nywele ndefu zinazopepezwa na upepo.
Lakini mtu huyo hakubaki hapo kwa muda, akanyooshea kidole chake upande wa kushoto. Darren hakuelewa. Ila punde akapata maana baada ya ghafla mtoto kuanza kulia.
Chumba cha mtoto kilikuwa upande wake wa kushoto!
ENDELEA
Akahisi kuwehuka. Upesi akatoka chumba chake na kukimbilia kule kwenye chumba cha mtoto. Alipofika huko akamkuta mtoto akiwa chini na ingali kitanda chake kidogo kikiwa kitupu na kinachocheza kwa upweke.
Akamnyanyua mwanaye na kumbembeleza, lakini akiwa anaangaza akitaka kujua ni wapi alipo mtu ambaye alimweka mwanaye chini toka kitandani.
Alitazama na kutazama lakini hakuona jambo. Hakukuwa na mtu humo. Alipotazama vema ndipo akagundua ya kwamba dirisha lilikuwa wazi. Basi akajongea taratibu na kulitazama dirisha hilo. Hapo, alipotazana vema, akapata kuona mabaki ya damu!
Akamkagua mwanaye kama kuna mahali popote ameumia lakini hakuona jambo. Hakuwa na jeraha wala mchubuko. Sasa ile damu ilitokea wapi? Akatazama nje ya dirisha, kushoto na kulia. Kulikuwa kimya tu zaidi ya upepo uliokuwa unapuliza kwa fujo kiasi.
Basi akafunga dirisha lile na kisha akamrejesha mwanaye kitandani. Alikuwa anaelekea kulala sasa. Alikuwa salama. Ila kwa upande wa Darren bado alikuwa mtu aliyejawa na mashaka sana. Alisita kuondoka katika chumba hicho akimwacha mwanaye papo.
Akangoja akiskizia kama kuna lolote litakalotokea. Hakukuwapo na kitu. Dakika ya kwanza mpaka ya kumi. Bado kulikuwa na kimya. Je pashakuwa salama? Akasema na nafsi yake. Japo mazingita yalionyesha kupo salama, bado bwana Darren hakuwa anaafki.
Kuna hisi fulani alikuwa nayo. Ushawahi kuhisi kuna mtu anakutazama mahali? Yaani umekaa ama umesimama lakini unahisi haupo mwenyewe? Ndivyo Darren alivyokuwa anahisi.
Alihisi chumba kina uzito fulani hivi. Ule uzito wa kutokuwa mwenyewe, japo macho yake hayakuweza kuthibitisha hilo jambo.
“Tafadhali,” Darren akasema kana kwamba kuna mtu anazungumza naye. “Naomba uiache familia yangu katika hili! Si mke wangu wala mtoto wangu wenye makosa. Naomba muwaache! Tafadhali naomba.”
Kukawa kimya. Kidogo upepo ukapuliza sana mpaka kutikisa kioo ha dirishani. Darren akatazama huko upesi, kwa woga. Akahisi huyo mtu azungumzaye naye atakuwapo huko.
Akasonga kwenda akiendelea kusema, “Naomba umwache mwanangu. Yeye hana makosa!”
Alipofika kiooni akagundua mabaki yale ya damu yalikuwa yameongezeka. Na si tu kuongezeka, bali yalikuwa yamepanda kwa matonetone kuchafua kioo. Mwanzo Darren hakuwa anaelewa, ila alipotazama vema matone hayo akabaini yalikuwa yameandika ujumbe.
‘WEWE NI WETU. NA YEYE HUYO MTOTO NI WETU PIA.’
Alipomaliza tu kusoma huo ujumbe, ghafla mtoto akalia kwanguvu! Darren akashtuka sana na kujikuta yu kitandani kando kidogo ya mkewe.
“Darren, una shida gani?” mkewe akakurupuka kwa hofu. Macho alikuwa ameyatoa na mdomo wake ameachama. Kwa kumtazama tu ungelijua mwanamke huyo alikuwa amepaliwa vipi na woga.
Darren akahema sana. Mpaka anakuja kutambua kwamba alikuwa ndotoni tayari ameshapitia shida sana, hata kwa mkewe pia. Kitu cha kwanza alichokifanya ikawa ni kutoka kitandani na kwenda moja kwa moja kwenye chumba cha mwanaye.
Alipomkuta yu salama, akashusha pumzi ndefu na kushika kichwa chake akiweka tama. Kidogo mkewe akaingia ndani ya chumba hicho.
“Darren unaweza kunambia kuna nini?” mwanamke akafoka. Alikuwa amechoshwa sasa na vitimbwanga vya mumewe. Darren, pasipo kutoa maelezo, akamnyanyua mtoto na kumpatia mkewe kisha akabeba kitanda cha mtoto na kusema, “tutakuwa tunalala na mtoto chumba kimoja!”
Akanyookea chumbani kwake na kukiweka kitanda cha mtoto pembeni na cha kwao.
Josephine akamwita, “Darren.” kisha akamtazama na kumuuliza kwa ustaarabu, “Nini kinakusumbua?”
“Mtoto hayupo salama, Jose!” Darren akabwatuka. Akashika kichwa chake na kukiacha, alafu akakishika tena. “Inabidi tuwe tunalala naye. Tutafanya hivyo kuanzia leo hii!” alikuwa kama mtu aliyewehuka. Mkewe alipatwa na hofu sana juu yake.
Akamweka mtoto ndani ya kitanda na kisha akamfuata mumewe na kumuuliza nini kinamsibu. Mbona amekuwa si mtu wa kueleweka hivi karibuni?
Basi Darren akanyamaza kwanza kwa muda wa kama dakika moja kabla hajasema kuwa hawapo salama. Hakuelezea sana. Alichomwambia mkewe ni kuwa hawapo salama na basi inawalazimu kuwa makini.
“Sasa si tutoe taarifa polisi?” Josephine akashauri. Alikuwa anamtazama mumewe kana kwamba mama anayemtazama mtoto ampendaye akiwa anamkanya,
“Polisi hawatasaidia kitu,” akasema Darren kwa sauti ya chini. Macho yake yalionyesha kukata tamaa. Yalionyesha hofu ndani yake. Mkewe alipomuuliza kwanini hawawezi kutoa taarifa polisi, Darren akasita kusema. Hakutaka kumtengenezea mkewe hofu zaidi. Alidhani kwa kumweleza mkewe zaidi na zaidi kungefanya apatwe na woga na hivyo kuharibu kabisa maisha yake.
Alitumai huenda akapata suluhisho la matatizo yake pasipo kumhusisha mkewe kwenye shida zake. Ila alikuwa sahihi? Alijikuta akijiuliza hilo swali mwenyewe pasipo kupatia majibu. Kichwa kilikuwa kinamuuma.
Kesho yake asubuhi na mapema, kinyume kabisa na alivyokuwa amekubaliana na Roby, akajiandaa na kwenda kazini. Altumai kwa kufanya kazi kungemfanya awe ‘busy’ na kujisahaulisha matatizo yake.
Alipofika akamweleza Roby kuwa hajiskii vema anapokuwa nyumbani. Mwili umekuwa wa kizembe sana na angependa kujishughulisha zaidi. Basi Roby akakosa maneno mengine ya kusema zaidi ya kumkaribisha Darren kazini, lakini akimpa angalizo, “Utakapoona hali inabadilika, basi utanambia. Sawa?”
Darren akachapa kazi kama kawaida mpaka majira ya saa sita mchana. Akiwa anapata mapumziko, ndipo akamwona Melissa, toka kwenye ghorofa ya pili aliyomo, akiwa anaingizana eneo hilo.
Mwanamke huyo alikuwa amevalia shati jeupe na sketi nyeusi ya kitambaa. Kabana nywele zake na shingoni amevalia skafu ya zambarau. Alikuwa na miadi na Roby. Na amini usiamini, mwanamke huyo hakuwa anafahamu kama Darren yu kazini.
Lakini uwepo wake huo ukamfanya Darren akose amani. Upesi alinyanyuka na kwenda kufunga mlango wa ofisi yake kwa ufunguo kisha akaketi kitini akitazama mlango kana kwamba anataraji kuna majambazi wanaweza kuuvunja.
Zikapita kama dakika ishirini. Dakika zote hizo Darren akiwa hafanyi kitu bali kutazama mlangoni na dirishani kama Melissa amekwenda zake. Ikiwa inaelekea dakika ya ishirini na moja, Darren akaanza kusikia sauti za watu zajongea mlangoni.
Kidogo hodi ikabishwa na sauti ya Roby ikapaza, “Hey Darren, una mgeni!” kisha kicheko kikafuatia kidogo. Darren akanyamaza kimya kama hajasikia.
Kidogo tena hodi ikagongwa, “Darren!” sauti ya Roby ikaita. Darren kimya. Kidogo, Roby akasikika akisema, “Ukute amepatwa na matatizo!” wakajaribu kufungua kwa kitasa, mlango haukufunguka. Wakajaribu tena na tena, majibu hamna. Kidogo Darren akasikia Melissa akishauri, “Tuvunje mlango, Roby!” kisha akalalama, “Kwanini ulimruhusu afanye kazi na unajua si mzima?”
Hapa Darren akapata mashaka. Mlango ukivunjwa itakuwa si jambo jema tena haswa akikutwa ni mzima wa afya. Basi upesi akanyanyuka na kuuendea mlango, akaufungua.
“Darren, vipi?” Roby akatahamaki kumwona mwanaume huyo. “Kuna shida? Mzima?”
Darren akawaondoa hofu kabisa kwa kusema yu mzima. Alikawia tu kufungua mlango sababu ya kutingwa na kazi fulani. Lakini ni wazi wageni wake walitilia shaka hilo jibu japo hawakutaka kulisema.
“Melissa hapa alikuwa anataka kukusalimu,” Roby akasema kwa tabasamu. Melissa na Roby wakapeana mikono. “Unaendeleaje Darren?”
“Niko vizuri, nashukuru. Karibu.”
“Ahsante. Nimefurahi kusikia upo vizuri. Ni habari njema.”
“Nashukuru, Melissa.”
Basi Melissa na Roby wakaaga waende zao. Na ni punde tu damu ikamchuruza Darren puani na kuchafua shati lake jeupe. Bahati damu hiyo haikuvuja zaidi. Ilikata. Darren akaketi na kuwaza afanyeje.
Akiwa anawaza ndipo akakumbuka kuhusu habari za yule jamaa aliyemsaidia mama yake toka kwenye shida za kuandamwa na mambo ya ajabu. Habari ambazo baba yake alimweleza muda mfupi baada ya mamaye kufariki.
Hapo Darren akaanza kuona kuna haja ya kumtafuta mtu huyo kwa udi na uvumba.
Atampatia wapi?
**
Sent using
Jamii Forums mobile app