Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 13*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Basi akafungua macho taratibu sasa aangaze kule ambapo sauti inatokea. Ilikuwa ni dirishani. Alipotazama huko akamwona Melissa akiwa amesimama kando. Mkono wake ameuweka kwenye kioo cha dirisha na macho yake yanamtazama!

Kinywani akahisi Melissa akiita, “Darren … Darren …” alafu mwanamke huyo akatabasamu na kupunga mkono wake.

ENDELEA

Darren akajikuta akikodoa zaidi. Bado Melissa yupo palepale. Akafikicha macho yake na kuangaza tena, bado Melissa yupo palepale! Akatahamaki. Mapigo yake ya moyo yakamwenda mbio sana. Mwishowe akapoa tu na kumtazama Melissa kwa macho ya pole.

“Melissa,” Darren akaita kwa kunong’ona. Melissa kule kiooni dirishani akatikisa kichwa chake kuitikia. Ilikuwa ni ajabu ni kwa namna gani amesikia. Na kwa kujibu akasema kwa kupanua mdomo wake pasipo kutoa sauti. Umbo la kinywa chake kikisema, “Nimekumiss Darren. Nakupenda.”

Kisha mwanamke huyo akavujisha machozi na kujiondokea. Darren akaangaza pale kiooni pasipo kuona mtu tena. Akafikicha tena macho yake na kuyatupa. Hakuona jambo! Akabaki akihema na kujiuliza.

Kile alichokiona ni cha kweli ama ni macho yake ndiyo humdanganya? Akajiuliza sana. Kichwa kikaanza kumuuma tena, na damu zikaanza kumtoka puani.

Kidogo maumivu yakawa kama mionzi inayomkata kichwa. Mwishowe akashindwa kustahimili na kujikuta akipoteza fahamu! Baada ya kama dakika nane tangu alipopoteza fahamu, daktari akaja na kumkuta kwenye hali hiyo mbaya. Upesi akamsaidia kitaalamu na kisha akampatia mwanya wa kupumzika.

Ila daktari akapata maswali juu ya hali hiyo. Imekuwaje mgonjwa akarejea tena kwenye hali ya mwanzo na ingali alikuwa anaendelea vema hapo kabla? Hakujua kuwa mgonjwa wake alirejea kwenye rundo la mawazo kwa mara nyingine tena.

Basi asubuhi ilipowadia, ile ya saa kumi na moja. Josephine akarejea hospitali akiwa amebebelea juisi aliyomtengenezea mume wake. Si kwamba juisi hizo hazikuwa zikipatikana hospitali na maeneo ya karibu, lah, alitaka tu mumewe atumie kitu alichotengeneza kwa mikono yake mwenyewe. Alihisi hicho ndicho kitu sahihi. Kitu anachotakiwa kukifanya.

Alipotazama hakumwona Roby. Akamuuliza nesi juu ya uwepo wa bwana huyo, akaambiwa ya kuwa aliondoka usiku wake, hata hakulala hapo. Josephine akaghafirika sana. Hata akajilaumu kwanini hakubaki na mumewe. Alihisi ni yeye peke ndiye anajua umuhimu wa mume wake.

“Kwanini Roby alifanya hivyo?” akajiuliza. “Kama hakuwa anaweza kulala hapa, si angeliniambia nikajua cha kufanya!” ila mwishowe akashukuru tu kwa kumkuta mumewe ni mzima wa afya. Hilo ndilo la muhimu.

Kidogo, kwenye majira ya saa mbili asubuhi, Roby akafika hospitali akiwa ameshika kichwa chake na mkono wa kuume. Mwendo wake ulikuwa wa kasi sana, na uso wake ukiwa mithili ya mtu aliyechanganyikiwa.

Alipomwona Josephine, akasita. Akamtazama mwanamke huyo kwa muda kidogo akijiuliza kisha akaamua kusonga na safari yake. Alipomfikia Josephine akamsalimu, naye Josephine akamuitikia na kunyamaza kimya.

“Mgonjwa anaendeleaje?” akauliza kwa aibu.

“Anaendelea vema,” Josephine akajibu akimtazama mwanaye aliyekuwa amemlaza mapajani.

“Samahani, Josephine. Hai --”

“Usijali, Roby. Wa kuomba msamaha ni mimi kwa kukupatia majukumu makubwa.”

“Usiseme hivyo Josephine. Haikuwa dhamira yangu kufanya hayo. … yani siwezi hata … kuelezea. Nisamehe tu Joephine. Najua nimekukosea. Nimemkosea pia na Darren.”

“Nimekusamehe, Roby. Hamna shida.” baada ya Josephine kusema hayo, hakurudia tena kusema kingine. Akanyamaza akihangaika na mtoto wake. Roby akaenda kumtazama mgonjwa na kisha akarejea tena pale sehemu ya mapumziko. Kidogo Daktari akaja na kuwapa taarifa juu ya kile kilichotokea majira ya usiku, lakini akawapa moyo.

“Sidhani kama kitatokea tena. Kama hali yake itaendelea kuwa kama ilivyo sasa mpaka majira ya jioni, basi tutamruhusu aende nyumbani.”

Basi baada ya muda kidogo, Roby akamuaga Josephine kuwa anaenda kazini kutazama mambo kadhaa lakini baadae atarejea tena kumjulia hali Darren. Alipoondoka hapo akaenda kwanza nyumbani kuonana na Melissa kabla hajaendelea na kazi zake.

Akamlaumu sana Melissa kwa kitendo chake alichofanya usiku kwani amefanya mpaka akashindwa kurudi hospitalini mapema. Melissa hakujali sana kuhusu Roby. Hakuwa anamskiza. Akiwa amejilaza kitandani, alikuwa akitazama dari kwa kujawa na mawazo.

Roby alipomaliza kuongea, akamuaga Melissa kuwa anaenda zake, wataonana baadae. Hapo ndipo Melissa akamtazama na kumuuliza kumhusu mgonjwa. “Ameshatolewa hospitali?”

Roby akaghafirishwa. “Ina maana yote niliyokuwa naongea yalikuwa upuzi?”

“Nani kasema ya kipuzi? Sikukuskiza? Au ulikuwa unataka nifanye nini?”

Roby akashusha pumzi ndefu. “Sitaki kugombana na wewe, Melissa.”

“Nani anataka kugombana nawe, Roby?” Melissa akauliza. Roby asijibu, akauendea mlango aende zake. Lakini kabla hajatoka, Melissa akapaza sauti yake. “Nimeuliza mgonjwa ameshatoka hospitali?”

Roby akamtazama Melissa kwa kama sekunde tano na kisha akajibu, “Hapana.” alafu akajiendea. Huku nyuma Melissa akapaza mlango ukiwa umeshafungwa, “Akitoka utanambia!”

Roby hakujali, akatembea kuendea gari lake. Na alipotia moto akanyoosha mpaka kazini. Huko akakaa kwa kama masaa mawili na alipoona kila kitu kipo sawa, akafungafunga ofisi apate kwenda kumwona Darren hospitalini. Lakini kabla hajajiendea, Isabel akafika hapo akiwa ameongozana na mbwa wake. Baada ya kusalimiana, akamuulizia Darren.

“Darren amelazwa hospitali. Ni siku ya pili hivi sasa,” Roby akaeleza. Basi Isabel akaguswa sana na jambo hilo, naye akataka kuongozana na Roby kwenda huko hospitali kumwona Darren.

Pasi na kipingamizi, wakaongozana kwenda huko. Kila mtu alitumia usafiri wake. Walipofika, Roby akamtambulisha Isabel kwa mke wa Darren, Josephine, na kisha mwanamke huyo akapata fursa ya kumwona mgonjwa.

“Ni nini kilimpata?” akauliza Isabel. Uso wake ulikuwa umejawa na mashaka. Alimtazama Darren kwa uso wa huruma na kuguswa mno. Roby akamweleza kwa kadiri alivyokuwa anajua. Isabel akauliza, “Kuna shida nyingine yoyote?”

“Hapana,” Roby akajibu akitikisa kichwa. Isabel akamtazama na kumwambia, “Kama kutakuwa na shida yoyote, basi naomba mnijuze nijue kwa namna gani naweza kumsaidia, sawa?”

“Sawa, hamna shida.”

Basi Isabel akaendelea kumtazama Darren kwa kitambo kidogo. Mara Darren akafungua macho yake na kumtazama. Isabel akafurahi sana. Akamjulia hali Darren kwa tabasamu kubwa na kumpatia pole. “Utapoa, Darren.” kisha akamuuliza, “Ni nini unawaza hivyo? Kuna shida yoyote naweza kukusaidia?”

Darren akatikisa kichwa. “Hamna,” akajibu kwa kunong’ona. Isabel akamuaga na kumwahidi atakuja kumwona tena, aidha hospitali ama nyumbani.

Tangu alipoondoka, Darren akabakia akiwa amefungua macho. Akateta na kujisogeza. Afya yake ilionekana kuimarika. Basi ilipofika jioni, daktari akamruhusu aende zake nyumbani. Huko mkewe akampikia chakula apendacho kisha akamlisha mpenzi wake kwa mahaba.

Lakini kuna kitu Darren alikuwa anataka kuongea na Roby. Na kitu hicho si kingine bali ni kumhusu Melissa. Alishindwa kabisa kumsahau Melissa. Kila alipotuliiia, picha ya mwanamke huyo ikawa inamjia kichwani!

Alitamani kumpigia Roby aje nyumbani kwake lakini akaona hakuna haja hiyo. Aliamini ataonana naye kesho na basi atamweleza.

Lakini tofauti na matarajio hayo, mara mlango ukagongwa. Na Josephine alipoufungua, Roby akazama ndani pamoja na Melissa. Kitu cha kwanza ambacho Darren alikifanya, ni kukutana macho kwa macho na Melissa.

Akajihisi kutetemeka.


**

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 14*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Alitamani kumpigia Roby aje nyumbani kwake lakini akaona hakuna haja hiyo. Aliamini ataonana naye kesho na basi atamweleza.

Lakini tofauti na matarajio hayo, mara mlango ukagongwa. Na Josephine alipoufungua, Roby akazama ndani pamoja na Melissa. Kitu cha kwanza ambacho Darren alikifanya, ni kukutana macho kwa macho na Melissa.

Akajihisi kutetemeka.

ENDELEA

Huu ulikuwa ni ugeni asioutarajia kabisa. Japo ugeni ni baraka, kwa Darren huu ulikuwa ni laana. Alijihisi anakosa amani.

Josephine aliwakaribisha wageni kwa bashasha na kuwapatia chakula pamoja pia na vinywaji, pia akawaambia wageni namna Darren aendeleavyo tangu atoke hospitali.

Kukawa kumejawa na matabasamu hapo sebuleni. Hata Darren alitabasamu lakini moyo wake ukiwa wa zambarau. Alikuwa anajibana sana, mwishowe akashindwa na kuomba ruhusa aende chooni, lakini hakwenda huko na badala yake akaenda chumbani na kujilaza kitandani.

Alikuwa anawaza sana. Alikaa hapo akatafakari yaliyopita kumhusu Melissa. Moyo ukamuuma sana. Macho yakajawa na machozi na hata kulowanisha kitanda. Alishindwa kujizuia kabisa na hakuwa anajua kwanini alishindwa kujizuia.

Kidogo mkewe akaja na kumkuta hapo kitandani. Ndani ya chumba kulikuwa na kiza lakini alimwona mumewe akiwa amejilaza hapo. Akashangaa. Pasipo kuwasha taa akamjongea Darren na kumuuliza, “Darren, shida nini? Mbona umejilaza huku peke yako na kuna wageni wamekuja kukuona?”

Darren hakusema kitu. Hakutaka mkewe ajue kuwa analia au amekubwa na shida au hofu yoyote ile. Akasafisha koo lake na kusema hamna tatizo.

“Lakini mbona ukajilaza?” mkewe akauliza akiweka kiganja chake mgongoni.

“Sikuwa najisikia vizuri kwa muda kidogo,” Darren akalaghai. “Nilitoka ili nipate unafuu alafu nitazamie kurudi.”

Josephine akapata mashaka. “Kuna haja ya kurudi hospitali?”

“Hapana!” Darren akawahi kujibu akitikisa kichwa. “Sijajisikia hovyo kiasi hicho. Siwezi nikakuficha mpenzi.”

“Sawa. Kwahiyo utakuja muda gani?” Josephine akauliza kwa sauti yake ya upole.

“Muda si mrefu,” Darren akajibu akiwa anageuzia uso wake kando. Basi mkewe akanyanyuka na kujiondokea zake. Darren akaendelea kujilaza hapo kitandani kwa muda kidogo kabla hajasimama na kuendea dirisha. Akalifungua na kutazama nje.

Akatazama huko kwa muda akiwa anawaza mambo kadhaa kichwani. Alihisi anahitaji hewa zaidi, akafungua dirisha na kuendelea kusimama na kutazama kwa muda.

Kidogo mkewe akarejea tena chumbani. Mara hii alipoingia tu, akasema, “Darren twende sasa sebuleni. Wageni wanataka kuondoka!” Darren hakusema kitu. Macho yake yaliendelea kuzurura huko nje. Mkewe akamjongea karibu. “Darren, kuna shida yoyote?” akawasha taa na kumtazama mumewe usoni. Akamwona akiwa na macho mekundu yaliyolowana.

Mwanamke huyu akapata shaka. Huenda Darren ana jambo asilotaka kumweleza. Akamtazama ndani ya macho yake na kumuuliza, “Una nini mpenzi?”

Darren akamtazama mkewe kwa sekunde kadhaa pasipo kusema jambo. Alafu akamshika shavu na kumweleza, “Ni bora usifahamu kitu, Josephine.” kisha akambusu shavuni, na mara chozi likamwanguka.

Mkewe akamfuta na kumkumbatia kwanguvu alafu akasema kwa kunong’ona, “Napenda kujua, Darren. Pengine naweza kusaidia.”

Darren asiseme kitu, akamtazama mkewe kisha akashusha macho yake chini.

“Niambie,” Josephine akamsihi. Bado alikuwa ananong’ona. Darren akazidi kudondosha machozi. Akafungua kinywa chake na kumwambia Josephine, “Nakupenda sana. Jua hivyo, sawa?” Josephine akatikisa kichwa chake. “Najua, mpenzi.” Kisha akashauri, “twende kwanza sebuleni, si vema kuwakalisha wageni peke yao. Wakiondoka tutateta.”

Basi Darren akajivuta machozi na kusafisha koo lake asije onekana anaongea kama mtu aliyetoka kubanwa na kilio alafu akaongozana na mkewe mpaka sebuleni.

“Kila kitu kipo sawa?” Roby akauliza.

“Yah!” Josephine akadakia kwa tabasamu la wongo. “Kila kitu kipo sawa. Hamna shida.”

Kwa muda ambao Darren alikuwa amekaa ndani, wageni walishamaliza kula na hata kunywa. Muda huo walikuwa wanajiandaa kuondoka tu.

Melissa akamtazama Darren na kusema, “inabidi upate muda wa kupumzika zaidi, Darren. Nashauri kama ingewezekana, hata kwa juma moja ukae nyumbani pasi na kujishughulisha.”

Roby akamuunga mkono. “Kweli. Usijali kabisa kuhusu kazini. Tulia kwanza urejeshe utimamu wako rafiki yangu.”

Darren akashukuru pasipo kutia neno lingine na basi wageni wakaaga kwenda zao. Wakapeana mikono ya kwaheri, Melissa akamminya Darren mkono.

“Ilikuwa furaha kukutana nanyi,” Melissa akasema kwa tabasamu pana. “Nitakuwa nawatembelea kama hamtojali.”

“Karibu sana,” Josephine akamkarimu, wakaenda zao. Baada ya Josephine kutoa vyombo na kusafisha meza, akaenda kuoga na mumewe na kisha wakajiweka kitandani.

Hapo akambembeleza mumewe amweleze ni nini kinamsumbua, nini haswa ambacho kinamtoa chozi, lakini Darren hakuwa radhi kusema. Alimsihi mkewe kuwa hayupo kwenye ‘mood’ ya kuteta muda huo. Asiijali. Pindi atakapokuwa sawa, atamweleza kila kitu.

Basi Josephine kwa moyo mzito, akaridhia. Akajilaza pembeni ya mumewe na kidogo akapitiwa na usingizi. Alikuwa ana furaha maana siku hiyo hakuwa kitandani mwenyewe. Jana yake kitanda kilikuwa kikubwa na cha baridi, lakini kwa upande wa Darren ilikuwa ni kinyume. Hakupata usingizi kabisa. Alijawa na mashaka.

Sasa Melissa ameshajua wapi yalipo makazi yake, je atasalimika? Mwanamke huyo hatoacha kumsumbua? Na hofu yake kubwa haikuwa kwake bali kwa mke wake na mwanaye.

Basi usiku ukaenda akiwa anakodoa macho darini akilala chali. Akawaza sana na sana na hatimaye naye usingizi ukaanza kumnyemelea. Lakini akiwa bado hajalowea usingizini, akashtusha kusikia kioo cha dirisha kikigongwa kwanguvu, “Tih!” akakodoa kutazama huko na wala hakuona kitu, ila akagundua dirisha lilikuwa wazi. Akaogopa. Ila alipofikiria kidogo ndipo akakumbuka kuwa dirisha hilo alilifungua mwenyewe muda ule na kusahau kulifunga.

Akanyanyuka na kuliendea. Alipofika akatazama kwanza kama ataona jambo nje, kwa chini akaona tawi dogo la mti likiwa limedondokea hapo. Upepo ulikuwa mkali sana. Pasipo shaka tawi hilo lilikuwa limeangushwa na pepo kali.

Basi akafunga dirisha na kurudi kulala. Upepo ulikuwa unaendelea kupuliza sana. Hakujali. Akafunga macho yake akijaribu kuvuta usingizi.

Akiwa ameyafumba kwa kama sekunde kumi, dirisha likagongwa tena. Akatahamaki. Moyo wake ukamlipuka na pumzi yake ikaanza kwenda mbio. Alianza kuhisi kuna tatizo. Akanyanyuka na kuendea dirisha alafu akatazama huko nje.

Chini … juu … kushoto … kul--- akaona kitu cheusi kwenye mti! Macho yakamtoka akiachama. Baridi kali likampitia tokea unyayoni mpaka kichwani ghafula!

Alipokaza macho yake kutazama, akaanza kujikosoa. Huenda anachokihisi, sicho! Labda ni matawi, akajisema kifuani. Labda ni matawi yamefungamana. Akajilazimisha aamini vivyo.

Lakini …

Punde kidogo hicho kitu cheusi kikasogea toka chini kupanda juu. Hapo Darren akatingwa na hofu kali. Moyo wake ukaitikika ‘gup!’ kisha ukaanza kwenda mbio sana ‘gup!-gup!-gup!-gup!-gup!’

Haraka akafunga dirisha kwa kushusha pazia alafu akabaki akisimama hapo kama ataona kitu. Na kweli, baada ya muda kidogo akaona kivuli cha mtu dirishani. Kivuli cha mwanamke mwenye nywele ndefu zinazopepezwa na upepo.

Lakini mtu huyo hakubaki hapo kwa muda, akanyooshea kidole chake upande wa kushoto. Darren hakuelewa. Ila punde akapata maana baada ya ghafla mtoto kuanza kulia.

Chumba cha mtoto kilikuwa upande wake wa kushoto!


**

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 15*

*Simulizi za series*



ILIPOISHIA

Haraka akafunga dirisha kwa kushusha pazia alafu akabaki akisimama hapo kama ataona kitu. Na kweli, baada ya muda kidogo akaona kivuli cha mtu dirishani. Kivuli cha mwanamke mwenye nywele ndefu zinazopepezwa na upepo.

Lakini mtu huyo hakubaki hapo kwa muda, akanyooshea kidole chake upande wa kushoto. Darren hakuelewa. Ila punde akapata maana baada ya ghafla mtoto kuanza kulia.

Chumba cha mtoto kilikuwa upande wake wa kushoto!

ENDELEA

Akahisi kuwehuka. Upesi akatoka chumba chake na kukimbilia kule kwenye chumba cha mtoto. Alipofika huko akamkuta mtoto akiwa chini na ingali kitanda chake kidogo kikiwa kitupu na kinachocheza kwa upweke.

Akamnyanyua mwanaye na kumbembeleza, lakini akiwa anaangaza akitaka kujua ni wapi alipo mtu ambaye alimweka mwanaye chini toka kitandani.

Alitazama na kutazama lakini hakuona jambo. Hakukuwa na mtu humo. Alipotazama vema ndipo akagundua ya kwamba dirisha lilikuwa wazi. Basi akajongea taratibu na kulitazama dirisha hilo. Hapo, alipotazana vema, akapata kuona mabaki ya damu!

Akamkagua mwanaye kama kuna mahali popote ameumia lakini hakuona jambo. Hakuwa na jeraha wala mchubuko. Sasa ile damu ilitokea wapi? Akatazama nje ya dirisha, kushoto na kulia. Kulikuwa kimya tu zaidi ya upepo uliokuwa unapuliza kwa fujo kiasi.

Basi akafunga dirisha lile na kisha akamrejesha mwanaye kitandani. Alikuwa anaelekea kulala sasa. Alikuwa salama. Ila kwa upande wa Darren bado alikuwa mtu aliyejawa na mashaka sana. Alisita kuondoka katika chumba hicho akimwacha mwanaye papo.

Akangoja akiskizia kama kuna lolote litakalotokea. Hakukuwapo na kitu. Dakika ya kwanza mpaka ya kumi. Bado kulikuwa na kimya. Je pashakuwa salama? Akasema na nafsi yake. Japo mazingita yalionyesha kupo salama, bado bwana Darren hakuwa anaafki.

Kuna hisi fulani alikuwa nayo. Ushawahi kuhisi kuna mtu anakutazama mahali? Yaani umekaa ama umesimama lakini unahisi haupo mwenyewe? Ndivyo Darren alivyokuwa anahisi.

Alihisi chumba kina uzito fulani hivi. Ule uzito wa kutokuwa mwenyewe, japo macho yake hayakuweza kuthibitisha hilo jambo.

“Tafadhali,” Darren akasema kana kwamba kuna mtu anazungumza naye. “Naomba uiache familia yangu katika hili! Si mke wangu wala mtoto wangu wenye makosa. Naomba muwaache! Tafadhali naomba.”

Kukawa kimya. Kidogo upepo ukapuliza sana mpaka kutikisa kioo ha dirishani. Darren akatazama huko upesi, kwa woga. Akahisi huyo mtu azungumzaye naye atakuwapo huko.

Akasonga kwenda akiendelea kusema, “Naomba umwache mwanangu. Yeye hana makosa!”

Alipofika kiooni akagundua mabaki yale ya damu yalikuwa yameongezeka. Na si tu kuongezeka, bali yalikuwa yamepanda kwa matonetone kuchafua kioo. Mwanzo Darren hakuwa anaelewa, ila alipotazama vema matone hayo akabaini yalikuwa yameandika ujumbe.

‘WEWE NI WETU. NA YEYE HUYO MTOTO NI WETU PIA.’

Alipomaliza tu kusoma huo ujumbe, ghafla mtoto akalia kwanguvu! Darren akashtuka sana na kujikuta yu kitandani kando kidogo ya mkewe.

“Darren, una shida gani?” mkewe akakurupuka kwa hofu. Macho alikuwa ameyatoa na mdomo wake ameachama. Kwa kumtazama tu ungelijua mwanamke huyo alikuwa amepaliwa vipi na woga.

Darren akahema sana. Mpaka anakuja kutambua kwamba alikuwa ndotoni tayari ameshapitia shida sana, hata kwa mkewe pia. Kitu cha kwanza alichokifanya ikawa ni kutoka kitandani na kwenda moja kwa moja kwenye chumba cha mwanaye.

Alipomkuta yu salama, akashusha pumzi ndefu na kushika kichwa chake akiweka tama. Kidogo mkewe akaingia ndani ya chumba hicho.

“Darren unaweza kunambia kuna nini?” mwanamke akafoka. Alikuwa amechoshwa sasa na vitimbwanga vya mumewe. Darren, pasipo kutoa maelezo, akamnyanyua mtoto na kumpatia mkewe kisha akabeba kitanda cha mtoto na kusema, “tutakuwa tunalala na mtoto chumba kimoja!”

Akanyookea chumbani kwake na kukiweka kitanda cha mtoto pembeni na cha kwao.

Josephine akamwita, “Darren.” kisha akamtazama na kumuuliza kwa ustaarabu, “Nini kinakusumbua?”

“Mtoto hayupo salama, Jose!” Darren akabwatuka. Akashika kichwa chake na kukiacha, alafu akakishika tena. “Inabidi tuwe tunalala naye. Tutafanya hivyo kuanzia leo hii!” alikuwa kama mtu aliyewehuka. Mkewe alipatwa na hofu sana juu yake.

Akamweka mtoto ndani ya kitanda na kisha akamfuata mumewe na kumuuliza nini kinamsibu. Mbona amekuwa si mtu wa kueleweka hivi karibuni?

Basi Darren akanyamaza kwanza kwa muda wa kama dakika moja kabla hajasema kuwa hawapo salama. Hakuelezea sana. Alichomwambia mkewe ni kuwa hawapo salama na basi inawalazimu kuwa makini.

“Sasa si tutoe taarifa polisi?” Josephine akashauri. Alikuwa anamtazama mumewe kana kwamba mama anayemtazama mtoto ampendaye akiwa anamkanya,

“Polisi hawatasaidia kitu,” akasema Darren kwa sauti ya chini. Macho yake yalionyesha kukata tamaa. Yalionyesha hofu ndani yake. Mkewe alipomuuliza kwanini hawawezi kutoa taarifa polisi, Darren akasita kusema. Hakutaka kumtengenezea mkewe hofu zaidi. Alidhani kwa kumweleza mkewe zaidi na zaidi kungefanya apatwe na woga na hivyo kuharibu kabisa maisha yake.

Alitumai huenda akapata suluhisho la matatizo yake pasipo kumhusisha mkewe kwenye shida zake. Ila alikuwa sahihi? Alijikuta akijiuliza hilo swali mwenyewe pasipo kupatia majibu. Kichwa kilikuwa kinamuuma.

Kesho yake asubuhi na mapema, kinyume kabisa na alivyokuwa amekubaliana na Roby, akajiandaa na kwenda kazini. Altumai kwa kufanya kazi kungemfanya awe ‘busy’ na kujisahaulisha matatizo yake.

Alipofika akamweleza Roby kuwa hajiskii vema anapokuwa nyumbani. Mwili umekuwa wa kizembe sana na angependa kujishughulisha zaidi. Basi Roby akakosa maneno mengine ya kusema zaidi ya kumkaribisha Darren kazini, lakini akimpa angalizo, “Utakapoona hali inabadilika, basi utanambia. Sawa?”

Darren akachapa kazi kama kawaida mpaka majira ya saa sita mchana. Akiwa anapata mapumziko, ndipo akamwona Melissa, toka kwenye ghorofa ya pili aliyomo, akiwa anaingizana eneo hilo.

Mwanamke huyo alikuwa amevalia shati jeupe na sketi nyeusi ya kitambaa. Kabana nywele zake na shingoni amevalia skafu ya zambarau. Alikuwa na miadi na Roby. Na amini usiamini, mwanamke huyo hakuwa anafahamu kama Darren yu kazini.

Lakini uwepo wake huo ukamfanya Darren akose amani. Upesi alinyanyuka na kwenda kufunga mlango wa ofisi yake kwa ufunguo kisha akaketi kitini akitazama mlango kana kwamba anataraji kuna majambazi wanaweza kuuvunja.

Zikapita kama dakika ishirini. Dakika zote hizo Darren akiwa hafanyi kitu bali kutazama mlangoni na dirishani kama Melissa amekwenda zake. Ikiwa inaelekea dakika ya ishirini na moja, Darren akaanza kusikia sauti za watu zajongea mlangoni.

Kidogo hodi ikabishwa na sauti ya Roby ikapaza, “Hey Darren, una mgeni!” kisha kicheko kikafuatia kidogo. Darren akanyamaza kimya kama hajasikia.

Kidogo tena hodi ikagongwa, “Darren!” sauti ya Roby ikaita. Darren kimya. Kidogo, Roby akasikika akisema, “Ukute amepatwa na matatizo!” wakajaribu kufungua kwa kitasa, mlango haukufunguka. Wakajaribu tena na tena, majibu hamna. Kidogo Darren akasikia Melissa akishauri, “Tuvunje mlango, Roby!” kisha akalalama, “Kwanini ulimruhusu afanye kazi na unajua si mzima?”

Hapa Darren akapata mashaka. Mlango ukivunjwa itakuwa si jambo jema tena haswa akikutwa ni mzima wa afya. Basi upesi akanyanyuka na kuuendea mlango, akaufungua.

“Darren, vipi?” Roby akatahamaki kumwona mwanaume huyo. “Kuna shida? Mzima?”

Darren akawaondoa hofu kabisa kwa kusema yu mzima. Alikawia tu kufungua mlango sababu ya kutingwa na kazi fulani. Lakini ni wazi wageni wake walitilia shaka hilo jibu japo hawakutaka kulisema.

“Melissa hapa alikuwa anataka kukusalimu,” Roby akasema kwa tabasamu. Melissa na Roby wakapeana mikono. “Unaendeleaje Darren?”

“Niko vizuri, nashukuru. Karibu.”

“Ahsante. Nimefurahi kusikia upo vizuri. Ni habari njema.”

“Nashukuru, Melissa.”

Basi Melissa na Roby wakaaga waende zao. Na ni punde tu damu ikamchuruza Darren puani na kuchafua shati lake jeupe. Bahati damu hiyo haikuvuja zaidi. Ilikata. Darren akaketi na kuwaza afanyeje.

Akiwa anawaza ndipo akakumbuka kuhusu habari za yule jamaa aliyemsaidia mama yake toka kwenye shida za kuandamwa na mambo ya ajabu. Habari ambazo baba yake alimweleza muda mfupi baada ya mamaye kufariki.

Hapo Darren akaanza kuona kuna haja ya kumtafuta mtu huyo kwa udi na uvumba.

Atampatia wapi?


**

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 16*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akiwa anawaza ndipo akakumbuka kuhusu habari za yule jamaa aliyemsaidia mama yake toka kwenye shida za kuandamwa na mambo ya ajabu. Habari ambazo baba yake alimweleza muda mfupi baada ya mamaye kufariki.

Hapo Darren akaanza kuona kuna haja ya kumtafuta mtu huyo kwa udi na uvumba.

Atampatia wapi?

ENDELEA

Baada ya kufikiri kidogo, akaona kuna haja ya kwenda kule kwenye makazi ya wazazi wake marehemu, huenda akabahatika kupata chochote kitu huko cha kumpa angalau mwanga.

Akaaga na kujiendea zake akiwa amemaliza kazi. Alipofika akatafuta sana kila mahali mwishowe akaishia kushika simu ya baba yake na kuanza kukagua majina yalokuwemo humo aone kama atabahatisha.

Akasaka pasipo mafanikio, hatimaye akakata tamaa. Akarejesha simu ya baba yake na kujilaza kochini akiwa anawaza afanye nini zaidi.

Lakini akiwa hapo, kama ajali tu, akawa anapepesa macho yake ndani ya nyumba hiyo pweke. Aliporusha macho yake kule jikoni, akagundua kuna mabaki ya chakula yalikuwapo chini. Akakunja uso wake kwa kufikiri. Akanyanyuka na kuendea huko akatazame ni nini kilikuwapo.

Basi alipofika akakuta ni kweli kuna mabaki ya chakula hapo chini. Na si kidogo, mengi tu. Mabaki hayo yalikuwa yametokea kwenye sufuria iliyokuwapo kwenye kitako cha jiko.

Akashangazwa kidogo. Kitu pekee anachokumbuka kuhusu nyumba hii ni kwamba aliiacha ikiwa safi kabla hajajiondokea hapo na kutokurudi tena mpaka siku hiyo. Sasa nani alimwaga mabaki yale ya chakula?

Akafunua na sufuria. Alipotazama ndani, akaona chakula kikiwa kimejaa kede. Na ajabu ni kwamba chakula hicho bado kilikuwa cha moto. Na hata kitako kile cha jiko bado kilikuwa na vuguvugu la joto kumaanisha kimetoka kutumika muda si mrefu.

Hapa Darren akapata shaka sana. Akakagua tena nyumba kwa undani zaidi na kuja kugundua kuwa nyumba ile haikuwa pweke kama alivyokuwa anadhani. Kulikuwa na ishara za mtu humo.

Bafu lenye maji sakafuni. Vyombo vimehamishwa eneo. Makabati yapo wazi. Vitanda vimeezuliwa. Maana yake nini?

Alihofu huenda mwizi aliingia na kuiba, lakini alipotazama kila kitu humo ndani hakuhisi kama kuna lolote lililopungua. Kila kitu kilikuwapo ila kikiwa kimehamishwa ama kuvurugwa. Akahofu sana. Hata akaona inabidi atoke humo ndani upesi awezavyo.

Akakusanya vitu vyake na kuuendea mlango. Alipoufungua, ukagoma. Akajaribu tena na tena, mlango ukagoma. Akajipapasa mfukoni atoe ufunguo, alipoupata akauchomeka kwenye kitasa na kujaribu kufungua japo alikuwa anaamini hakuwa ameufunga mlango huo kwa ufunguo.

Alipotekenya ufunguo, mlango ukatoa mlio kidogo, na mara ukafunguka! Akashusha pumzi ndefu. Upesi akatoka na kuurejesha mlango kama alivyoukuta. Haraka akashuka ngazi na kuendea gari lake na kujitia humo.

Kabla hajaliwasha, akafikiri kwanza yale aliyoyaona kule. Kwa kama dakika mbili kichwa chake kikiwa kinavuruga. Hakujua ni nini kinatokea, na pengine hakuwa anataka kujua. Akawasha gari na kuadhimia kutorudi tena hapo.

Lakini ngoja. Akasimamisha gari lake baada ya kukumbuka jambo - simu za wazazi wake! Yampasa aende nazo! Basi akazima gari na kurudi kule ndani upesi ili abebe simu hizo na asiwe na sababu nyingine tena ya kurejea hapo.

Bado alitumai akiwa na simu zile huenda akapata majibu ya maswali yake.

Akafungua mlango na kuzama ndani akitupa macho. Akatazama sebuleni, hazikuwapo. Sasa aliziweka wapi? Akawaza. Kidogo akakumbuka ni jikoni alipokuwa anashangaa mabaki yale ya chakula. Haraka akaenda huko akatazame, lakini alipofika huko hakuona kitu chochote kile.

Sasa wapi? Akajikuta anajiuliza mwenyewe kwanguvu. Akiwa anaangaza hapo jikoni, akagundua mabaki yale ya chakula aliyoyaona muda ule, hayakuwapo tena! Akastaajabu.

Akafungua sufuria ile nayo aitazame kama ina chakula, hamaki akaikuta ni tupu! Hapo moyo wake ukaanza kusikika masikioni ukikimbia. Upesi akatoka humo jikoni na kwenda chumbani kuangaza kama ataona simu hiyo, na basi atakapoziona azikwapue na kuondoka upesi.

Akafika huko na kuangaza, akakuta vitanda vikiwa vimetandikwa kwa usafi! Macho yakamtoka na moyo ukamkimbia zaidi. Akatazama aone kama kuna simu, hamna! Hakukuwa na alama yoyote ile ya simu.

Sasa zimeenda wapi?

Akiwa anawaza, mara akasikia mlio wa simu! Akatega sikio akikodoa. Inalia wapi? Akadhani sauti hiyo itakuwa inatokea sebuleni. Haraka akaenda huko na kusaka, akafunua makochi na kusaka. Hakuona simu.

Simu ikaendelea kuita. Alipotega sikio vema, akahisi inalilia jikoni, upesi akaenda huko akaone. Napo alipofika akasaka sana pasipo mafanikio. Ila bado simu inaita.

Alipotega tena sikio kwa kadiri awezavyo, akabaini sauti hiyo inatokea chumbani. Hapa sasa ndiyo akaona huu ni mchezo tu. Huko chumbani ndipo alitoka, mbona hakuisikia sauti hiyo akaisikia sebuleni?

Akaona aondoke hapa upesi, hata simu hiyo aiache. Akaachana na kila kitu na kuuendea mlango. Alipoufungua ukagoma. Akachomeka ufunguo na kutekenya kitasa, napo pia mlango ukagoma!

Hapa akatoa macho kana kwamba kitenesi. Akavuta mlango kwanguvu sana lakini haukutii amri. Akavuta tena kwanguvu zake zote, mwishowe kitasa kikang’oka akadondoka chini, Puh!

Aligonga kichwa kwanguvu na kujisababishia maumivu makali. Akadaka kichwa akiugulia. Aaaaghhshhhh! Akajizungushia kushoto na kulia akigugumia.

Alipofungua macho yake kutazama kwa kuyafinya, akaona miguu ya mtu nyuma ya kochi. Miguu hiyo ilikuwa meusi na mipana. Basi upesi Darren akaketi kitako na kutazama nyuma ya kochi kama kuna mtu. Hakumwona!

Akasimama akiwa ameshika kichwa chake. Akatazama sebuleni na hata koridoni, hakumwona mtu. Kote kulikuwa kupweke. Na pia kimyaa kwani simu zilikuwa zimezima.

Lakini aliposkiza zaidi akagundua hakukuwa kimya kama alivyokuwa anawaza. Kwa mbali kulikuwa na sauti za vishindo vya mtu. Kwa mbali vishindo hivyo vilikuwa vinapapasa sakafu.

“Wewe ni nani?” akapaza sauti kuuliza.

Hakuna aliyemjibu. Ni sauti yake tu ndiyo ilimrejea. Akauliza tena, “Unataka nini kwangu? Unataka nini hapa?”

Napo hakuna aliyemjibu. Kadiri alivyokuwa anakaa hapo, moyo wake ukawa unazidi kumwenda mbio.


**

“Una uhakika uliipenda?” aliuliza mwanaume mmoja aliyekuwa anakatiza na mwanamke wakiwa wameshika mkono. Wote walikuwa wamevaa makoti ya kujikinga na baridi na nyuso zao zikiwa na furaha.

Uso wa mwanamke ulikuwa na miwani ya kumsaidia kuona, na ule wa mwanaume ulikuwa mrefu ukipambwa na tabasamu.

“Nimependa sana,” akajibu mwanamke akimtazama yule mwanaume, na kisha wote wakacheka. Wakatembea zaidi kwa kama hatua kumi, kidogo mwanamke akapaza sauti akimvuta mkono huyo mwanaume, “Tazama!” Alinyooshea kidole juu ghorofani. Macho yake yalikuwa yamekodoa haswa!

Mwanaume yule akatazama upesi kule alipolekezewa, na hamaki akamwona mtu akiwa amejishkiza dirishani, ananing’inia!

“Anataka kujitupa!” akaropoka yule mwanamke.

‘Inabidi tumsaidie!” akasema mwanaume kisha akatazama kushoto na kulia kwake aone ni namna gani anaweza kutoa msaada.

Mtu yule aliyekuwa ananing’inia dirishani alikuwa ni Darren! Mikono yake ilikuwa inavuja damu.


**

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom