Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? -- 27*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Akamshtua Darren atazame. Darren akapayuka kuuliza, “Melissa, nini kinatokea?” akiwa amemshika mkono mwanamke huyo. Melissa akatazama miguu yake inayomomonyoka na kisha akamtazama Darren na kusema, “Hii ndiyo gharama yangu kwa kusema haya. Yanipasa niende Darren. Maisha yangu yamekwisha hapa duniani.”

“Hapana Melissa, si una kito cha kuishi milele?” Darren akauliza.

“Sina kitu chochote Darren,” Melissa akasema akilaza kichwa chake kifuani mwa Darren, “Yote nimeyatoa kwa ndugu zangu kama sadaka ya kukubakiza wewe hai.” kisha akamtazama Darren na kumwambia, “lakini haikusaidia na wamenigeuka. Wanataka maisha yako, wanataka maisha yenu. Wanataka kila ambacho bibi yako alikuwa anamiliki. Siwezi kuwazuia tena, Darren. Sina nguvu hiyo.”

Melissa alipomaliza kauli hiyo, mwili wake ukawa umeshapukutika mpaka kufikia tumboni. Mwili uwake ulikuwa kichuguu cha mchanga. Akamwaga Darren, “Kwaheri, mpenzi”

ENDELEA

“Melissa!” Darren akaita akimshika Melissa vema. “Usiondoke, Melissa! Tutawezaje kupambana wenyewe? Tafadhali usituache!” Lakini tayari sasa mwili wa Melissa ulikuwa umepukutika zaidi mpaka kifuani. Maneno pekee ambayo aliyasema kabla hajamalizika kabisa ni haya,

“Kuna kitu kwenye jeneza la bibi yako,” alipotaka kunena zaidi, kichwa chake kikamomonyoka na hatimaye akawa mchanga kabisa. Darren na Charlie wasiamini macho yao wakautazama mchanga ule wa bahari.

“Amejitoa sadaka kwa ajili yetu,” akasema Charlie akimtazama Darren kisha akauliza, “sasa tunafanyaje?” Darren alipohakikisha kuwa kweli Melissa ameenda, akamwambia Charlie waende kule kwa bibi yake. Lakini muda ulikuwa umeenda sana.

“Vipi tukadamka asubuhi?” Charlie akapendekeza.

“Hapana,” Darren akatikisa kichwa. “Huoni ni hatari zaidi tukiendelea kungoja?” kweli Charlie akaafiki, lakini sasa wangefanyaje na muda ulikuwa umewatupa mkono?

Wakiwa wanafikiri namna ya kufanya, simu ya Darren ikaita, alikuwa ni Isabel. Alipokea na kumjulia hali mwanamke huyo.

“Upo wapi, Darren?” Isabel akauliza. Darren akamtazama Charlie na kujibu, “Nipo mbali.”

“Wapi? Tafadhali waweza kuniambia?” Isabel akasisitiza, lakini kabla Darren hajajibu akamtazama kwanza Charlie, mwanamke huyo akamtikisia kichwa. Darren akakata simu.

“Darren, usimwamini mtu yeyote kwa sasa hivi,” Charlie akamwambia akiwa amemkazia macho.

“Kwanini? Huyu nafahamiana na--”

“Hapana!”

Punde simu ikaita tena, Darren akamtazama Charlie. Ajabu mwanamke huyo akampoka simu hiyo na kisha akaikata na kuizima. “Tuondoke, Darren!”

Basi upesi wakalifuata gari lao na kujikwea. Charlie akamwambia Darren waelekee kwake alafu ndiyo waende huko waendako, Darren akatii. Walipofika kwa Charlie wakapakia silaha kadhaa ndani ya gari, Charlie akabeba na pesa, wakaanza safari ya kwenda kwenye nyumba ya marehemu bibi yake Darren.

Wakatembea kwa muda mrefu sana mpaka pale ambapo usiku sasa ukawa mkubwa. Wakiwa kwenye majira ya saa tano usiku, wamebakiza kama kilomita ishirini kuwasili wanapoelekea, Charlie akahisi kuna gari linawafuatilia. Alimshtua Darren na kumtaka aongeze mwendokasi.

Darren alipojaribu kutazama kwa kutumia vioo akaliona gari hilo wanalolishukia. Halikuwa ngeni machoni mwake. Alipoenda mbele zaidi na kulitazama vema, akagundua kitu,

“Isabel!” alijikuta akinena mwenyewe.

“Unamaanisha yule mwanamke?” Charlie akauliza. “Yule aliyekuwa anakupigia simu?”

“Ndio!” Darren akajibu. “Ndiye yeye!”

Charlie akatazama nyuma kuliangazia gari hilo. Lilikuwa linakuja kwa kasi. Alihofia sana.

“Darren, sasa tunafanya nini?”

“Sijui!” Darren akatikisa kichwa akiwa ametoa macho kukodolea kioo cha juu ya kichwa chake. Alikanyaga pedeli ya mafuta zaidi, gari likakimbia. Punde lile gari linalowafuata likatokomea wasijue limeenda wapi!

“Unaliona?” Darren akamuuliza Charlie.

“Hapana, silioni!” Charlie akajibu akiwa anaendelea kukagua. Kwa muda kidogo akaendelea kutazama asilione tena gari lile linalowafukuza, basi wakaendelea na safari yao mpaka waelekeapo. Walipofika wakajitua toka kwenye gari na kabla hawajaenda mbali sana, wakatupa macho yao kukagua.

Ilikuwa ni nyumba iliyomezwa na kiza. Kulikuwa kimya sana. Kwa namna moja ama nyingine kulikuwa kunatisha.

Wakiwa wanaendelea kutazama, Charlie akagundua kitu. Akamwita Darren na kumuuliza, “Nini kile? Ni gari ama macho yangu?” Darren alipotazama akaona gari kwa mbali upande wao wa kulia. Gari hilo lilikuwa limeegeshwa kwa ukimya. Lilikuwa ni lile gari waliloliacha barabarani. Gari ambalo Darren hudhania ni la Isabel.

“Umeliona likiingia muda huu?” Darren akauliza.

“Hapana,” Charlie akajibu na kuongezea, “Nimeliona likiwa tayari limeegeshwa.” kisha akauliza, “atakuwa amefika kabla yetu?”

Darren hakuwa na majibu, upesi akamwamuru Charlie wachukue kila kinachohitajika kwenye gari na waelekee eneo la kaburi upesi. Walipofanya hivyo, mara gari lile likawasha taa zote kwa pamoja, pap! likawamulika na kuwaumiza macho!

Upesi wakakimbia kule kaburini na kuanza kuchimba kwa maelezo ya Darren. Wakiwa wanaendelea kuchimba, Charlie akamwona mtu kwa mbali akija kwenye mwelekeo wao. Hakuweza kumwona vema maana alikuwa yu mbali, kitu pekee alichoweza kubaini ni kuwa mtu huyo ni mwanamke kutokana na umbo lake na mwendo pia.

Mikono yake iliyokuwa tupu ilikuwa ikienda mbele na kurudi nyuma sababu ya mwendo.

“Chimba, Charlie! Chimba!” Darren akabweka. Wakafukua kana kwamba sungura udongoni na mtu yule alipokaribia, Darren akamsihi Charlie aendelee na zoezi ilhali yeye akamkabili mtu huyo anayekuja.

“Darren, una uhakika?” Charlie akauliza kwa mashaka.

“Usijali, endelea,” Darren akasema akitoka shimoni na kupiga hatua kadhaa kusonga mbele. Alipomfikia mtu yule ndipo akabaini kweli alikuwa ni Isabel.

“Isabel,” Darren akaita na kuuliza, “Ni nini unataka hapa?”

Isabel akatabasamu na kuuliza, “Darren mbona haupokei simu yangu?” kabla Darren hajajibu, akauliza tena, “Kwani kuna tatizo lolote baina yetu?”

Darren akamtazama kwanza Isabel kwa namna ya kumtilia mashaka. Alikuwa anahisi kuna kitu hakipo sawa.

“Isabel, unataka nini hapa?”

Isabel akatazama nyumba kubwa iliyokuwa kando yao, “Ni nyumba kubwa. Nimeipenda sana Darren. Vipi ile ofa yangu, waweza kuniuzia?”

“Siuzi tena!” Darren akajibu.

“Kwanini? Auhitaji pesa tena?”

“Sihitaji pesa zako, Isabel.”

Isabel akamtazama Darren na kumsogelea karibu zaidi.

“Tangu lini umeanza kukataa pesa zangu, Darren?”

“Kuanzia leo. Sihitaji tena. Na pia sihitaji kukuona pia!”

Isabel akakunja shingo yake kutazama kule shimoni. “Naona umepata mwanamke mpya.”

“Hayakuhusu, Isabel. Hicho ndicho kimekuleta?”

“Hapana, Darren,” Isabel akajibu akiweka mkono wake begani mwa Darren. “Kilichonileta hapa ni kuchukua kilicho changu tu.”

“Kipi chako hapa?” Darren akauliza.

“Vyote unavyoviona hapa,” Isabel akajibu na kuongezea, “Vyote ni urithi wangu. Na kwakuwa haukutaka niuchukue kwa amani, basi nitatumia nguvu!”

“Ebu tumia nione!” Darren akasema akimkazia Isabel macho.

“Una uhakika?” Isabel akauliza akipandisha nyusi yake moja. Punde Darren akaanza kuhisi maumivu makali ya kichwa.



**
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- MWISHO*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Hayakuhusu, Isabel. Hicho ndicho kimekuleta?”

“Hapana, Darren,” Isabel akajibu akiweka mkono wake begani mwa Darren. “Kilichonileta hapa ni kuchukua kilicho changu tu.”

“Kipi chako hapa?” Darren akauliza.

“Vyote unavyoviona hapa,” Isabel akajibu na kuongezea, “Vyote ni urithi wangu. Na kwakuwa haukutaka niuchukue kwa amani, basi nitatumia nguvu!”

“Ebu tumia nione!” Darren akasema akimkazia Isabel macho.

“Una uhakika?” Isabel akauliza akipandisha nyusi yake moja. Punde Darren akaanza kuhisi maumivu makali ya kichwa.

ENDELEA

“Darren nisingependa nitumie nguvu dhidi yako. Nitakumaliza. Kwahiyo kwa kunusuru maisha yako, songa kando nifanye kilichonileta.”

Japo Darren alikuwa anasikia maumivu makali bado hakuwa radhi kumruhusu Isabel atende kile alichokuwa amekusudia. Basi akamvamia akimtupia maneno makali lakini alichoambulia hakikuwa kinasimulika vema. Alitupiwa mbali tena kwa mkono mmoja tu. Akaangukia tumbo na kulalama kwa maumivu makali!

Isabel akapiga hatua nzito kumfuata Charlie. Alipomfikia akanyoosha mkono wake kumnyaka mwanamke huyo, ila upesi Charlie akatumia kifaa alichokuwa anachimbia kumwadhibia Isabel! Alimchana na kumvujisha damu!

Isabel akautazama mkono wake unaovuja damu kisha akakunja ndita akimtazama Charlie. “Umekwisha!” akafoka na kujitupia ndani ya shimo. Charlie alipotaka kumwadhibu tena Isabel, nyenzo yake ikadakwa na mkono wa Isabel wenye nguvu.

“Kamwe usijaribu!”

Isabel akampokonya Charlie dhana hiyo na kisha akataka kumbamiza nayo kichwa. Kheri kabla hajatimiza adhma yake hiyo, nyenzo ikadakwa na mtu nyuma. Isabel alipogeuka kutazama, alikuwa ni Darren. Na kabla hajafanya jambo, mwanaume huyo akamwadhibu kwa kumzamishia ncha za reki usoni mwake! Kilikuwa ni kitendo cha kinyama ambacho Darren amewahi kufanya tangu azaliwe.

Hata wakati Isabel anaanguka chini, Darreb alikuwa ameachana asiamini kama amelitenda hilo. Basi upesi, wakishirikiana, wakamtoa Isabel ndani ya shimo na Darren akamburuza kwa hatua kadhaa mbali na shimo kisha wakaendelea kuchimba kaburi.

Walipofanya hivyo kwa takribani dakika sita, mara Isabel akanyanyuka akiwa na reki lake usoni. Si Darren wala Charlie aliyemwona. Mwanamke huyo akachomoa reki usoni na kulitupia kando. Alikuwa anachuruza damu lakini hakuwa anajali. Upande wake wa kushoto ulikuwa umefunikwa na damu inayotiririka kama bomba.

Alipotupia reki kando ndipo Darren na Charlie wakasikia na kuhisi. Darren alipotazama na kubaini hilo akahofia sana. Hata Charlie vilevile. Ni mtu wa aina gani angenyanyuka baada ya kadhia ile? Lakini kwa ujasiri Darren akatoka ndani ya shimo baada ya kumwambia Charlie aendelee kufukua.

“Darren!” Charlie akaita kwa hofu. Aliogopa. Aliona Darren angeenda kufa. Lakini Darren asijali akajiendea kifua mbele. Alipomfikia Isabel akasema, “Nitakuua!” naye Isabel akamwambia, “Karibu tena!” kisha akamnyaka shingo yake kwa nguvu na kumnyanyua juu juu!

“Ndiyo kwanza tupo kwenye moja, Darren. Unadhani binadamu kama wewe anaweza kuniua?” Darren akarusharusha miguu akijitahisi kujinasua toka kwenye mikono ya Isabel. Hakika asingeweza kwani mikono ya mwanamke huyo ilikuwa imeshiba nguvu haswa. Ilikuwa inaminya uhai toka kwenye mwili wa Darren.

Darren akapapatika sana pasipo mafanikio. Akarusha na mateke ambayo mengine yalikwenda hewa na mengine kumkita Isabel lakini haikusaidia, mwanamke huyo alikuwa mithili ya gogo kavu!

Basi Darren aliyekuwa anaelekea kufa alipoona amefanya kila jambo pasipo mafanikio na sasa anaelekea kufa, akamtazama Isabela akilenga kumtusi ama kumlaani. Ni kheri katika hilo akabaini jeraha alilokuwa nalo Isabel mkononi, lile jeraha ambalo Charlie alimsababishia. Basi kama simba aliye na njaa, Darren akadaka kwa mikono yote jeraha hilo na kuliparua sana. Isabel akashindwa kuvumilia na hatimaye akamwachia Darren aliyejidondokea chini akikohoa.

Darren alikuwa anahisi kifua kinambana, shingo nayo imeziba. Alikuwa anahema kwa tabu. Koo lake bado halikuachia. Alikohoa mara kadhaa akiwa anahangaika kumeza mate.

Hakukaa sana akamwona Isabel akimfuata kwa hasira. Alipotaka kuamka akimbie, Isabel akamwendea kwa kasi sana na kumdaka. Darren akajitahidi kurusha ngumi na kutumia nguvu zake za kibinadamu lakini akashindwa kabisa! Isabel alikuwa ana nguvu mno!

Mwanamke huyo pasipo kujiuliza mara mbilimbili, akadidimizia kucha za mkono wake wa kushoto kwenye tumbo la Darren, na hakufanya vivyo mara moja bali mara tatu! Darren akalalamika sana kwa maumivu. Isabel akamtupia mbali akiwa amemalizana naye.

Darren, akiwa amelala kama mtu anayengoja kifo akiwa ameshika tumbo lake linalovuja, akamtazama Isabel. Akamwona mwanamke huyo akiwa anaenda kumfuata Charlie kule shimoni. Basi akapaza sauti kuu kumwita Isabel. Halikuwa zoezi rahisi, alikuwa anahisi maumivu makali sana lakini alifanikisha adhma yake hiyo.

Isabel alipogeuka kumtazama, Darren akapaza sauti kumtusi na kumkebehi mwanamke huyo. Kitendo hicho kikamkasirisha sana Isabel, akaamua kuachana na Charlie akammalize mwanaume huyo kabisa. Basi akamjongea kwa madaha akiwa anamwambia ni kwa namna gani atakapofurahi akiona roho yake inaenda.

“Kama bibi na mama yako, nawe utaenda hukohuko!” akasema Isabel. “Mwana usiwe na haya ukatembea na bibi yako. Hujui Melissa ni sawa na bibi yako, ati Darren?”

“Na mbona na wewe ulikuwa unanitaka?” Darren akaguguma kuuliza. Saa hii kinywa chake kilikuwa kinachuruza damu pia. Isabel akacheka akiwa anazidi kujongea, “Mimi? Darren mpenzi nilikuwa nataka tu kukumaliza na si kingine. Unadhani mimi ni kama yule mpofu Melissa? Mjinga kama yule?”

“Ni wewe ndiye mjinga, si Melissa!” Darren akafoka.

“Pole sana, Daren,” Isabel akasema akiwa anamalizia hatua yake moja kumfikia Darren. “Mpumbavu wako ameenda, nani atakulinda sasa?” akauliza na kucheka. “Kwa akili yake amejitoa uhai kwa ajili yako. Wewe binadamu. Kwa sababu tu ya kukwambia yote yale ambayo hupaswi kuyajua. Shenzi kabisa!”

Alipomaliza kusema hayo akamnyakua Darren na kisha anyanyue mkono wake ili apate kumkita tena tumboni kama alivyofanya hapo awali. Lakini mara hii kabla hajafanya vivyo, akastaajabu kuona mpini wa reki ukitokezea tumboni mwake! Hamaki alikuwa ni Charlie nyuma yake!

Basi akamwacha Darren na kisha akapiga magoti akiwa anatazama chuma kile kilichomtoboa tokea mgongoni mpaka tumboni na kisha akadondoka puh! Na kutulia tuli,

Charlie akamjulia hali Darren.

“Niko sawa,” Darren akamjibu na kisha akamuuliza, “Umefanikiwa?”

“Bado kidogo!” Charlie akajibu. Akatazama tumboni mwa Darren, kulikuwa kunamwaga damu sana. Akashikwa na imani, “Darren, nikuwahishe hospitali!” alisema akitaka kunyanyuka akaendee gari lakini Darren akamdaka mkono na kumwambia, “Hapana, Charlie. Nenda kamalizie kwanza ile kazi!”

“Darren, nitaendeleaje na upo kwenye hali hii?” Charlie akauliza.

“Hapana! Hapana! Nenda kwanza, tafadhali nenda!” Darren alisisitiza na basi kwa shingo upande, Charlie akaenda zake. Akazama shimoni na kufukua zaidi na zaidi, ndani ya dakika tano akawa amefikia jeneza, akafunua na humo ndani akakuta maiti ya bibi yake Darren ikiwa mifupa.

Alipotazama vema akabaini kulikuwa na kito rangi ya asamawati, basi akakibeba na kupaza sauti, “Darren, nimekipataaaa!”

Haraka akatoka ndani ya shimo na kumkimbilia Darren. Lakini alipofika akabaini Darren hakuwa anasogea wala kuashiria kama mzima. Alipotazama vema akabaini pia mwili wa Isabel ulikuwa umesogea kidogo toka pale alipouacha, na kama haitoshi, reki halikuwa tumboni, bali kwenye kichwa likiwa limemtoboa!

Hapo Charlie akabaini ya kuwa Darren na Isabel walipambana kwa mara nyingine. Akapata hofu zaidi juu ya uhai wa Darren. Akamwita sana na kumtikisa, kwa mbali Darren akafungua macho yake kumtazama. Alikuwa ana mjeraha kooni na kifuani. Karibia mwili wake wote ulijawa damu.

“Umepata?” Darren akauliza kwa kunong’ona.

“Ndio, nimepata!” Charlie akajibu kwa kitete. Macho yake yalikuwa mekundu yakitaka kumwaga machozi. “Twende nyumbani, sasa!” akasema akijaribu kumnyanyua Darren.

“Hapana, Charlie,” Charlie akasema na kuongezea, “Hapa ndiyo nyumbani kwangu, sina pengine. We nenda mimi utaniacha hapa.”

“Nitakuachaje Darren? Tumekuja wote hapa! Nyanyuka tafadhali twende!”

Charlie alipoona ni ngumu kumnyanyua Darren basi akaenda zake asogeze gari karibu. Alipojipaki kwenye gari, akaendesha upesi sana kumrudia Darren. Alipoliweka gari tenge akashuka na kumwendea Darren, ila kwa muda huo hakuwa Darren tena bali mwili tu.

Akapambana kumweka kwenye gari, lakini kabla hajawasha gari Isabel akanyanyuka na reki lake kichwani! Mwanamke huyo akakaa mbele ya gari akimtazama Charlie kwa macho ya kukodoa.

Charlie akastajabu sana. Akahangaika kuwasha gari, kabla hajafanikiwa, Isabel akawa tayari amezama ndani na kumkaba shingo kwanguvu! Charlie akaweweseka sana kujiokoa.

Ajabu wakiwa kwenye zoezi hilo, wakasikia mtu akigonga kwenye kioo cha dirisha. Isabel alipotazama, akabaini ni Melissa! Akastaajabu akiwa ameachama mdomo!

“Ina -- inawezekanaje?”

“Unadhani nilikuwa mjinga, sio?” Melissa akauliza.

Kufumba na kufumbua akafungua mlango wa gari na kumnyaka Isabel. Kwa mikono yake akamnyofoa mwanamke huyo koo na kisha akamtupia mbali kana kwamba kitenesi!

“Melissa!” Charlie akaita kwa kustaajabu. Akamkumbatia Melissa kwanguvu na kisha akamwambia kumhusu Darren. Walipomtazama wakabaini mwanaume huyo alikuwa amekwisha kufa.

Basi Melissa akachukua kile kito ambacho Charlie alikipata kwenye jeneza la bibi yake Darren kisha akakitazama na kusema, “Nilikuwa nayajua yaliyo mbele yangu hata kuhifadhi sehemu ya maisha yangu kwenye jeneza lile.” aliposema hayo, akamtazama Charlie na kumwambia, “Utakapokutana na Darren mwambie nampenda sana. Hatimaye amekuwa huru. Hatimaye mmekuwa huru.”

Aliposema hayo akaingiza kile kito kinywani mwa Darren na kisha kumfumba mdomo. Charlie akamuuliza, “vipi kuhusu yule Isabel, hatarejea tena?”

Melissa akamjibu hatorejea tena kwa roho zake zimekwisha. Ndani yake alikuwa na roho kadhaa na kadiri walivyokuwa wanamuua ndivyo walivyozimaliza mpaka kubakia moja aliyoimaliza yeye muda si mrefu.

“Umejuaje?” Charlie akamuuliza.

“Kwasababu isingekuwa rahisi kummaliza kama nilivyofanya,” Melissa akamjibu na kisha akamuaga. Moja kwa moja akaenda kwenye shimo la kaburi na kudmbukia humo. Punde, Darren akaamka. Alikuwa mzima wa afya kabisa asiye na jeraha.

Charlie alipomweleza kila lililotokea, upesi akakimbilia kwenye kaburi kumtazama Melissa. Akamkuta mwanamke huyo akiwa ana uhai amekwishakufa. Akamwita na kumwita pasipo mafanikio, Melissa alikuwa ameenda.

Melissa hakuwapo tena.

Basi wakamfukia kwenye kaburi hilo na kwenda zao.


***
 
Haya hatudaiani, si ndio? Nashukuru kwa kuwa pamoja nami kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Kama nilivyosema awali Riwaya hii ni fupi, japo kuna watu roho zitakuwa zimewauma kuisha [emoji23]
 
Haya hatudaiani, si ndio? Nashukuru kwa kuwa pamoja nami kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Kama nilivyosema awali Riwaya hii ni fupi, japo kuna watu roho zitakuwa zimewauma kuisha [emoji23]
Aisee hapa inabidi Darren na Charlie waoane hapa roho yangu itasuuzika.. #
 
Daah asilimia kubwa ya wasomaji walikuwa wanisoma hii story mchana[emoji3][emoji3][emoji16]..bravo steve mzigo ulikuwa poa sana tena bila arosto.makofi mengi kwako.
 
Asante sana tivu Mungu azidi kubariki kazi ya mikono yako nakupenda [emoji8]
Haya hatudaiani, si ndio? Nashukuru kwa kuwa pamoja nami kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Kama nilivyosema awali Riwaya hii ni fupi, japo kuna watu roho zitakuwa zimewauma kuisha [emoji23]
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom