*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 17*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
“Anataka kujitupa!” akaropoka yule mwanamke.
‘Inabidi tumsaidie!” akasema mwanaume kisha akatazama kushoto na kulia kwake aone ni namna gani anaweza kutoa msaada.
Mtu yule aliyekuwa ananing’inia dirishani alikuwa ni Darren! Mikono yake ilikuwa inavuja damu.
ENDELEA
Upesi watu wakaongezeka na kufanya namna za kumsaidia Darren. Walikuwa ni wanaume watano wenye nguvu, wakakinga mikono yao kumdaka. Na kheri Darren akajiachia na kudakwa.
Alikuwa amechoka sana. Mikono yake ilikuwa imechanjika viganjani kwa kung’ang’ania kingo za dirisha. Basi kwa kumpatia huduma ya kwanza, wakamwahisha hospitali kupata huduma.
Huko Darren akatiwa dawa kwenye majeraha na kufungwa bandeji kisha akaondoka zake kurudi nyumbani. Alipofika mkewe akastaajabu kumwona mumewe yu kwenye hali ile ya kuchoka na majeraha. Alipomuuliza nini kimetokea, Darren akasihi ni ajali.
“Haukutakiwa kwenda kazini, Darren,” mkewe akalalamika. “Muda mwingine uwe unasikia.”
Darren hakusema jambo. Alipopata chakula akajiendea chumbani na kujilaza. Akawaza sana. Nini kile alichokiona kwenye nyumba ya wazazi wake? Ni nani yule ambaye hakumfahamu?
Akiwa anawaza, simu yake ikaita. Akatazama na kukuta ni namba mpya. Ni nani? Akapokea na kuweka simu yake sikioni. Akasikia sauti ya kike ikimwita kwa sauti ya chini, “Darren!”
“Yes,” akaitikia kwa tahadhari. “Ni nani mwenzangu?”
“Melissa,” sauti ikajibu. Mara kukawa kimya kwa sekunde tatu kabla Darren hajasema, “Melissa, tafadhali naomba uachane na maisha yangu. Sawa?” kisha akakata simu.
“Ni nini mwanamke huyu anataka kwangu?” Darren akauliza akitoa chozi. “Ni nini nilimkosea? Kumpenda kwangu?”
Hakupata majibu. Mara ujumbe ukaingia kwenye simu. Akanyanyua simu yake kuutazama, ‘Darren, tafadhali naomba tukutane tuongee. Usiwe mwepesi wa jazba,’ ujumbe ulisomeka vivyo,
Darren hakujali, akazima simu na kuiweka kando akijilalia. Alijilaza hhapo kitandani mpaka mke wake alipokuja na kumwita kumwamsha. Japokuwa Darren alisikia sauti ya mke wake, hakuitika. Alinyamaza kimya kwani alifahamu kuwa mkewe atamuuliza maswali mengi ambayo yeye hakuwa radhi kuyajibu.
Basi mkewe baada ya kudhani mumewe amelala, akaachana naye kwenda sebuleni. Kidogo akarejea na kuzima taa, kisha akalala.
Baada ya kama masaa manne ya mwanamke huyo kulala, akiwa tayari ameshalowea usingizini, Darren akafungua macho na kutoka kitandani. Alielekea sebuleni akakaa hapo akiwa anawaza sana. Nini haswa afanye? Akawasha simu yake na punde jumbe kama nne zikaingia kwa mkupuo.
Zilikuwa ni jumbe za Melissa.
‘Darren, najua unaniwazia mabaya. Biado nakupenda. Kuna siku utalifahamu hilo,’ ujumbe wa kwanza ulisomeka vivyo.
‘Nina mengi ya kuongea nawe Darren. Tafadhali fanya jitihada tukutane,’ huo ulikuwa ni ujumbe wa pili.
‘Unajua wapi pa kunipata Darren kama ukinihitaji,’ ujumbe wa tatu na wa mwisho ukasema, ‘Kwaheri.’
Darren akasonya na kufuta jumbe zote hizo, na kabla ya kufungia namba ya Melissa akamwandikia ujumbe mwepesi, ‘Sitaki kukutana na wewe kamwe!’ kisha akalaza kichwa chake kwenye kiti akiendelea kuwaza na kuwazua. Mwishowe usingizi ukampitia na akalala fofofo hapohapo.
Hakujielewa mpaka majira aliyokuja kushtuliwa na mkewe. “Darren! Wewe Darren!”
Alipofungua macho akabaini ni asubuhi sasa. Aliwezaje kulala hapo mpaka asubuhi? Alifikicha macho yake, akapiga mihayo na kujinyoosha kisha akamsalimu mkewe.
Lakini,
“Mbona umelala hapa na ulikuwa chumbani?” Josephine akamuuliza.
“Aaahm …” Darren akajiuma, “niliamka usiku wa manane baada ya usingizi kukata. Nilipoketi hapa, sijui nini kilitokea, nikapitiwa na usingizi.”
Josephine hakumuuliza tena mumewe badala yake akampa pole na kumuuliza hali yake, “Auhisi kuumwa viungo vya mwili?”
“Kidogo,” Darren akajibu na kuongezea, “Mgongo na shingo vyauma kwa mbali. Nadhani vitakuwa sawa kadiri muda utakavyoenda.”
“Na vipi kuhusu majeraha yako?” Josephine akaongezea swali.
“Nayo yapo sawa,” Darren akajibu na kusema, “Baadae nitabadili bandeji na kutia dawa.” kisha naye akauliza, “Mtoto anaendeleaje?”
“Yupo sawa,” Josephine akamjibu kwa tabasamu alafu akaenda zake jikoni akapate kuandaa chai kwa ajili ya familia. Wakanywa na kukaa pamoja mpaka majira ya saa saba mchana ambapo walipata ugeni. Alikuwa ni bibie Isabel akija kumjulia hali Darren.
Mwanamke huyo alikuja na gari la thamani akiendeshwa na mwanaume mzee ndani ya suti nyeusi. Akiwa amevalia suti rangi ya ugoro na viatu mchuchumio, alikuwa amependeza haswa. Nywele zake alizozilazia pembeni zikipeperushwa na upepo.
Japo mwanamke huyu alikuwa mtu mzima kidogo, narudia tena, alikuwa na mvuto wa ajabu kwa mwonekano wake. Alijua kupendeza na kujivesha kutokana na mwili wake.
Alipoonana na familia ya Darren akatabasamu sana ingali aliteta nao machache na alipotimiza haja ya kumuulizia hali mgonjwa, akaomba aonane na Darren faragha, kwenye gari. Darren pasipo kusita akaongozana naye mpaka ndani ya gari, huko akiwa yeye, Isabel na dereva.
Dereva ambaye hakuonekana kujali kama nyuma yake kuna watu wanateta.
“Darren,” Isabel akaita akisonga karibu na mwanaume huyo. “Niambie kama kuna tatizo lolote linalokusumbua.”
Kidogo Darren akashtushwa na swali hilo. Aliwaza pengine Isabel anajua anachokipitia ama? Lakini hapana, akasema na nafsi yake. Haiwezekani!
“Sina tatizo, Isabel,” Darren akasema akitikisa kichwa chake.
“Kweli?” Isabel akauliza akimtazama Darren machoni. Macho yake yalikuwa ni makali, Darren akashindwa kuvumilia, akatazama chini.
“Ni kweli. Sina tatizo, Isabel.”
“Sawa,” mwanamke akajibu na kuweka mkono wake kwenye paja la Darren. “Basi mimi nina tatizo.”
Darren akautazama mkono wa Isabel kabla hajauliza, “Tatizo gani?”
Isabel akanyamaza kwanza akingoja Darren amtazame usoni. Darren alipofanya hivyo, Isabel akasema, “Nataka kuwa karibu na wewe zaidi, Darren.”
Darren akashtushwa na kauli hiyo. “Una maana gani, Madam Isabel?”
Isabel akatabasamu. “Nini ambacho hujaelewa, Darren? Anyway, hii nyumba unayokaa sasa, sijapendezwa nayo. Umeona nyumba ya mwenzio Roby?”
Kabla Darren hajajibu, Isabel akaendeleza maneno, “Nataka na wewe uwe na nyumba kama ile. Kubwa na ina nafasi kidogo. Sawa?”
“Lakini sina tatizo na nyumba yangu hii,” Darren akajitetea.
“Najua, najua, Darren. Hauna tatizo kabisa na nyumba yako hii, lakini nimekuomba tu uhame hapa. Tafuta nyumba kubwa zaidi. Usijali, nitasimamia kila kitu. Sawa?”
Darren hakujibu, badala yake akatazama chini. Hakuwa ameafiki wazo hilo. Isabel akafungua pochi yake ndogo na kutoa kipande cha gazeti lenye picha kisha akamkabidhi Darren. Ilikuwa ni picha ya jengo la bibi yake kule kijijini.
Akamuuliza, “Unajua nyumba hiyo?”
“Ndio,” Darren akawahi kujibu. “Ni nyumba ya marehemu bibi yangu.”
“Roby aliniambia hivyo,” Isabel akamhusia na kumuuliza, “Je, naweza nikaiununua?”
“Nani alikwambia inauzwa?” Darren akauliza.
“Kwenye gazeti ilikuwa inasema hivyo. Wamekosea?”
Darren akafikiri. Pengine wazazi wake waliweka matangazo hayo wakiwa hai. Sasa vipi? Akawaza. Aibakize ile nyumba ama aiuze tu?
“Ngoja ntakujibu,” akamwambia Isabel.
“Sawa. Utakapokuwa tayari utaniambia,” Isabel akasema akifunga pochi yake. “Nitakulipa pesa taslimu, Darren.”
“Sawa.”
“Kwaheri. Nitakuja kukuona siku nyingine.”
Kabla Darren hajatoka ndani ya gari, Isabel akambusu shavuni na kumuaga kwa kumnong’oneza, “Kwaheri, Darren.”
Darren hakusema kitu akatoka zake na kwenda ndani. Alipoketi sebuleni, mkewe akatokea chumbani akiwa amembebelea mtoto. Macho yake yalikuwa yanatiririsha machozi.
“Darren,” Josephine akaita na kuuliza, “Unaniletea mwanamke wako nyumbani kwangu. Kweli?”
Darren akakodoa.
**