Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 17*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Anataka kujitupa!” akaropoka yule mwanamke.

‘Inabidi tumsaidie!” akasema mwanaume kisha akatazama kushoto na kulia kwake aone ni namna gani anaweza kutoa msaada.

Mtu yule aliyekuwa ananing’inia dirishani alikuwa ni Darren! Mikono yake ilikuwa inavuja damu.


ENDELEA

Upesi watu wakaongezeka na kufanya namna za kumsaidia Darren. Walikuwa ni wanaume watano wenye nguvu, wakakinga mikono yao kumdaka. Na kheri Darren akajiachia na kudakwa.

Alikuwa amechoka sana. Mikono yake ilikuwa imechanjika viganjani kwa kung’ang’ania kingo za dirisha. Basi kwa kumpatia huduma ya kwanza, wakamwahisha hospitali kupata huduma.

Huko Darren akatiwa dawa kwenye majeraha na kufungwa bandeji kisha akaondoka zake kurudi nyumbani. Alipofika mkewe akastaajabu kumwona mumewe yu kwenye hali ile ya kuchoka na majeraha. Alipomuuliza nini kimetokea, Darren akasihi ni ajali.

“Haukutakiwa kwenda kazini, Darren,” mkewe akalalamika. “Muda mwingine uwe unasikia.”

Darren hakusema jambo. Alipopata chakula akajiendea chumbani na kujilaza. Akawaza sana. Nini kile alichokiona kwenye nyumba ya wazazi wake? Ni nani yule ambaye hakumfahamu?

Akiwa anawaza, simu yake ikaita. Akatazama na kukuta ni namba mpya. Ni nani? Akapokea na kuweka simu yake sikioni. Akasikia sauti ya kike ikimwita kwa sauti ya chini, “Darren!”

“Yes,” akaitikia kwa tahadhari. “Ni nani mwenzangu?”
“Melissa,” sauti ikajibu. Mara kukawa kimya kwa sekunde tatu kabla Darren hajasema, “Melissa, tafadhali naomba uachane na maisha yangu. Sawa?” kisha akakata simu.

“Ni nini mwanamke huyu anataka kwangu?” Darren akauliza akitoa chozi. “Ni nini nilimkosea? Kumpenda kwangu?”

Hakupata majibu. Mara ujumbe ukaingia kwenye simu. Akanyanyua simu yake kuutazama, ‘Darren, tafadhali naomba tukutane tuongee. Usiwe mwepesi wa jazba,’ ujumbe ulisomeka vivyo,

Darren hakujali, akazima simu na kuiweka kando akijilalia. Alijilaza hhapo kitandani mpaka mke wake alipokuja na kumwita kumwamsha. Japokuwa Darren alisikia sauti ya mke wake, hakuitika. Alinyamaza kimya kwani alifahamu kuwa mkewe atamuuliza maswali mengi ambayo yeye hakuwa radhi kuyajibu.

Basi mkewe baada ya kudhani mumewe amelala, akaachana naye kwenda sebuleni. Kidogo akarejea na kuzima taa, kisha akalala.

Baada ya kama masaa manne ya mwanamke huyo kulala, akiwa tayari ameshalowea usingizini, Darren akafungua macho na kutoka kitandani. Alielekea sebuleni akakaa hapo akiwa anawaza sana. Nini haswa afanye? Akawasha simu yake na punde jumbe kama nne zikaingia kwa mkupuo.

Zilikuwa ni jumbe za Melissa.

‘Darren, najua unaniwazia mabaya. Biado nakupenda. Kuna siku utalifahamu hilo,’ ujumbe wa kwanza ulisomeka vivyo.

‘Nina mengi ya kuongea nawe Darren. Tafadhali fanya jitihada tukutane,’ huo ulikuwa ni ujumbe wa pili.

‘Unajua wapi pa kunipata Darren kama ukinihitaji,’ ujumbe wa tatu na wa mwisho ukasema, ‘Kwaheri.’

Darren akasonya na kufuta jumbe zote hizo, na kabla ya kufungia namba ya Melissa akamwandikia ujumbe mwepesi, ‘Sitaki kukutana na wewe kamwe!’ kisha akalaza kichwa chake kwenye kiti akiendelea kuwaza na kuwazua. Mwishowe usingizi ukampitia na akalala fofofo hapohapo.

Hakujielewa mpaka majira aliyokuja kushtuliwa na mkewe. “Darren! Wewe Darren!”

Alipofungua macho akabaini ni asubuhi sasa. Aliwezaje kulala hapo mpaka asubuhi? Alifikicha macho yake, akapiga mihayo na kujinyoosha kisha akamsalimu mkewe.

Lakini,

“Mbona umelala hapa na ulikuwa chumbani?” Josephine akamuuliza.

“Aaahm …” Darren akajiuma, “niliamka usiku wa manane baada ya usingizi kukata. Nilipoketi hapa, sijui nini kilitokea, nikapitiwa na usingizi.”

Josephine hakumuuliza tena mumewe badala yake akampa pole na kumuuliza hali yake, “Auhisi kuumwa viungo vya mwili?”

“Kidogo,” Darren akajibu na kuongezea, “Mgongo na shingo vyauma kwa mbali. Nadhani vitakuwa sawa kadiri muda utakavyoenda.”

“Na vipi kuhusu majeraha yako?” Josephine akaongezea swali.

“Nayo yapo sawa,” Darren akajibu na kusema, “Baadae nitabadili bandeji na kutia dawa.” kisha naye akauliza, “Mtoto anaendeleaje?”

“Yupo sawa,” Josephine akamjibu kwa tabasamu alafu akaenda zake jikoni akapate kuandaa chai kwa ajili ya familia. Wakanywa na kukaa pamoja mpaka majira ya saa saba mchana ambapo walipata ugeni. Alikuwa ni bibie Isabel akija kumjulia hali Darren.

Mwanamke huyo alikuja na gari la thamani akiendeshwa na mwanaume mzee ndani ya suti nyeusi. Akiwa amevalia suti rangi ya ugoro na viatu mchuchumio, alikuwa amependeza haswa. Nywele zake alizozilazia pembeni zikipeperushwa na upepo.

Japo mwanamke huyu alikuwa mtu mzima kidogo, narudia tena, alikuwa na mvuto wa ajabu kwa mwonekano wake. Alijua kupendeza na kujivesha kutokana na mwili wake.

Alipoonana na familia ya Darren akatabasamu sana ingali aliteta nao machache na alipotimiza haja ya kumuulizia hali mgonjwa, akaomba aonane na Darren faragha, kwenye gari. Darren pasipo kusita akaongozana naye mpaka ndani ya gari, huko akiwa yeye, Isabel na dereva.

Dereva ambaye hakuonekana kujali kama nyuma yake kuna watu wanateta.

“Darren,” Isabel akaita akisonga karibu na mwanaume huyo. “Niambie kama kuna tatizo lolote linalokusumbua.”

Kidogo Darren akashtushwa na swali hilo. Aliwaza pengine Isabel anajua anachokipitia ama? Lakini hapana, akasema na nafsi yake. Haiwezekani!

“Sina tatizo, Isabel,” Darren akasema akitikisa kichwa chake.

“Kweli?” Isabel akauliza akimtazama Darren machoni. Macho yake yalikuwa ni makali, Darren akashindwa kuvumilia, akatazama chini.

“Ni kweli. Sina tatizo, Isabel.”

“Sawa,” mwanamke akajibu na kuweka mkono wake kwenye paja la Darren. “Basi mimi nina tatizo.”

Darren akautazama mkono wa Isabel kabla hajauliza, “Tatizo gani?”

Isabel akanyamaza kwanza akingoja Darren amtazame usoni. Darren alipofanya hivyo, Isabel akasema, “Nataka kuwa karibu na wewe zaidi, Darren.”


Darren akashtushwa na kauli hiyo. “Una maana gani, Madam Isabel?”

Isabel akatabasamu. “Nini ambacho hujaelewa, Darren? Anyway, hii nyumba unayokaa sasa, sijapendezwa nayo. Umeona nyumba ya mwenzio Roby?”

Kabla Darren hajajibu, Isabel akaendeleza maneno, “Nataka na wewe uwe na nyumba kama ile. Kubwa na ina nafasi kidogo. Sawa?”

“Lakini sina tatizo na nyumba yangu hii,” Darren akajitetea.

“Najua, najua, Darren. Hauna tatizo kabisa na nyumba yako hii, lakini nimekuomba tu uhame hapa. Tafuta nyumba kubwa zaidi. Usijali, nitasimamia kila kitu. Sawa?”

Darren hakujibu, badala yake akatazama chini. Hakuwa ameafiki wazo hilo. Isabel akafungua pochi yake ndogo na kutoa kipande cha gazeti lenye picha kisha akamkabidhi Darren. Ilikuwa ni picha ya jengo la bibi yake kule kijijini.

Akamuuliza, “Unajua nyumba hiyo?”

“Ndio,” Darren akawahi kujibu. “Ni nyumba ya marehemu bibi yangu.”

“Roby aliniambia hivyo,” Isabel akamhusia na kumuuliza, “Je, naweza nikaiununua?”

“Nani alikwambia inauzwa?” Darren akauliza.

“Kwenye gazeti ilikuwa inasema hivyo. Wamekosea?”

Darren akafikiri. Pengine wazazi wake waliweka matangazo hayo wakiwa hai. Sasa vipi? Akawaza. Aibakize ile nyumba ama aiuze tu?

“Ngoja ntakujibu,” akamwambia Isabel.

“Sawa. Utakapokuwa tayari utaniambia,” Isabel akasema akifunga pochi yake. “Nitakulipa pesa taslimu, Darren.”

“Sawa.”

“Kwaheri. Nitakuja kukuona siku nyingine.”

Kabla Darren hajatoka ndani ya gari, Isabel akambusu shavuni na kumuaga kwa kumnong’oneza, “Kwaheri, Darren.”

Darren hakusema kitu akatoka zake na kwenda ndani. Alipoketi sebuleni, mkewe akatokea chumbani akiwa amembebelea mtoto. Macho yake yalikuwa yanatiririsha machozi.

“Darren,” Josephine akaita na kuuliza, “Unaniletea mwanamke wako nyumbani kwangu. Kweli?”

Darren akakodoa.


**
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 18*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Darren hakusema kitu akatoka zake na kwenda ndani. Alipoketi sebuleni, mkewe akatokea chumbani akiwa amembebelea mtoto. Macho yake yalikuwa yanatiririsha machozi.

“Darren,” Josephine akaita na kuuliza, “Unaniletea mwanamke wako nyumbani kwangu. Kweli?”

Darren akakodoa.

ENDELEA

Kidogo mkewe akajigeuza na kwenda zake ndani pasipo hata kuaga na huku akiwa anamwaga machozi. Hali hiyo ikamfanya Darren ajisikie vibaya sana. Moyo ukamnyong’onyea akiwa anajiuliza nini kimemsibu mkewe?

Hakuwa anajua kwamba mkewe alimwona wakati Isabel akimbusu kwenye gari, kioo cha gari kilikuwa chini hivyo ikapeleka kuonekana kwa urahisi na mkewe akiwa chumbani.

Akaketi pale sebuleni kwa kama sekunde tano kabla hajanyanyuka na kumfuata mkewe ndani kumjulia hali lakini kumuuliza nini shida. Alipofika, akamkuta mkewe akiwa amejilaza kitandani analia. Mtoto alikuwa amelala kwenye kitanda chake.

Akamwita, “Josephine!” mwanamke hakuitika. Akarudia kuita tena na tena lakini bado kukiwa kimya. Akaketi kitandani na kumshika bega.

“Mke wangu,” akaita kwa upole. Mwanamke bado akawa kimya. Ni sauti ya mafua tu ndiyo ilikuwa inasikika na miguno ya kilio.

“Nimekufanya nini?” Darren akauliza. “Niambie basi nini tatizo?” Darren akahisi huenda mkewe aliumizwa na kile kitendo cha mkewe kwenda kuonana na Isabel kando, basi akaomba msamaha huku akimhakikishia kuwa hakufanya jambo baya, lakini bado tu. Josephine aliendelea kulia asiseme jambo.

Zikapita kama dakika tano … sita … saba … bado Josephine kimya. Mwishowe Darren akaona ni staha akimwacha mwanamke huyo yeye aende sebuleni kutulia alafu baadae mwanamke huyo atakapokuwa sawa, aongee naye.

Akaketi sebuleni kwa kama lisaa. Kimya. Akawasha runinga na kutazama lakini akili yake yote ikiwa kwa mkewe. Akaitazama kwa kama nusu saa, bado kimya. He! Akashangazwa na hali hiyo. Akapatwa pia na mkanganyiko wa nafsi, je aende tena kumbembeleza mkewe au atulie hapo mpaka atakapokuja mwenyewe?

Akiwa anawaza, mara akasikia mlango ukifunguliwa na kisha vishindo vya mtu. Kidogo akamwona mkewe akifika sebuleni lakini akipitiliza moja kwa moja kwenda jikoni.

Akarusha macho kumtazama. Kidogo akahofu mkewe asije akawa ameenda kujidhuru. Akakodoa mpaka pale Josephine alipotoka huko jikoni na kutembea kudaka korido. Akamwita tena, mara hii Josephine akaitika kwa kumtazama.

Macho yake yalikuwa yamekauka machozi lakini yakiwa bado mekundu. Uso wake ulikuwa umesinyaa kwa huzuni na mdomo wake umevimba.

“Una nini Josephine?” swali hilo likafungua tena mifereji ya machozi. Josephine akabubujikwa na machozi na mdomo wake ukatetemeka akiumauma meno. Hakuwa anaweza kuongea. Kuna kitu alikuwa anahisi kinamkaba kooni. Mdomo ulikuwa ni mzito na kichwa chake kilikuwa kinagonga.

Hakuwahi kuwaza … hakuwahi kuwaza kabisa kama Darren anaweza kumsaliti kwa kuwa na mwanamke mwingine.

Kila alipotaka kuongea akajikuta taya zinagongagonga. Mdomo unajawa na uchungu usio wa kawaida. Akaamua tu kuondoka zake. Mumewe akamsindikiza kwa macho yenye itilafu mpaka alipozama ndani ya chumba kabisa, akaufunga mlango.

“Eh!” Darren akahema akijilaza kitini. “Kazi nnayo.”

Akabaki hapohapo akitazama runinga na kurudi mawazoni, akitazama runinga na kurudi mawazoni mpaka mwishowe akabebwa na usingizi kabisa. Ulikuwa ni usingizi mwepesi lakini uliomfanya akapata kidogo afueni ya rundo la mawazo alokuwa anapitia.

Lakini katika namna ya ajabu, ya ajabu kabisa, usingizi huo ukageuka kuwa mzito kupita kiasi! Darren akajikuta analala akikoroma kabisa, hata kumwaga udenda akiachama kinywa. Ni kama vile hakuwa amelala kwa juma zima, au amefanya kazi kubwa sana na hakupata muda wa kupumzika.

Akiwa ndani ya usingizi huo akazamia ndotoni ambapo alijiona yu ndani ya nyumba ya bibi yake, kule kijijini. Alikuwa sebuleni akifanya usafi akiwa anangojea ugeni muda si mrefu.

Kidogo akiwa anaendelea na kazi hiyo, mkewe akaja akiwa amembebelea mtoto. Mtoto alikuwa analia lakini punde akanyamaza. Josephine akaketi kwenye kiti na kumtazama Darren.

“Ungesogea kando kidogo na mtoto kwani kuna vumbi!” Darren akamwonya mkewe kisha akaendelea na kazi yake akijua mkewe atafanyia kazi ushauri wake. Lakini baadae alipokuja kutazama, akatahamaki mkewe alikuwa bado amekaa kwenye kiti!

“Josephine!” Darren akaita. Mkewe alikuwa bado anamtazama. “Si nimekwambia utoke hapo lakini? Huoni vumbi?”

Josephine akaendelea kumtazama tu. Hakuonyesha dalili yoyote ya kusikia anachoambiwa. Kidogo, mbele ya macho ya Darren, Josephine akachomoa kisu toka nyuma ya mgongo wake. Kilikuwa ni kisu kipana na kirefu. Kisu kinachometa kwa upya. Na ndani ya sekunde moja tu, kufumba na kufumbua, Josephine akamdidimizia mtoto kisu chote kifuani!

Darren akatoa macho haswa. “Mungu wang - Josephine! Nini unafanya?”

Josephine akamweka mtoto kando na kisha akanyanyuka kumfuata Darren akiwa amebebelea kisu chake mkononi. Darren akapiga yowe kali. Akashuka toka alipokuwa amekwa na kuanza kupambana kujiweka mbali na Josephine kwasababu za usalama wake.

Josephine akazidi kumjongea na kisu kinachochuruza damu. Uso wake ulikuwa umekengeuka kuwa wa ajabu. Macho yake yamekuwa ya kijani na mdomo wake unaapa kifo.

Hakuwa Josephine uliyemzoea, mkarimu, mpole na mwenye kutenda yaliyo mema. Alikuwa ni Josephine kutoka kuzimu. Josephine mwenye umbo la binadamu lakini roho ya shetani!

“Josephine! Hapana! Tafadhali usifanye hivyo!” Darren aliwaka kwa woga. “Tafadhali, Josephine. Mimi ni mume- ” hajamalizia, Josephine akamrukia na kunyanyua mkono wake wenye kisu.

Hapo ndipo Darren akaamka toka kwenye lindi zito la usingizi! Akiwa anahema kama mbwa, akatazama kushoto na kulia kwake. Macho yamemtoka na mdomo ameachama!

Kidogo tu, akasikia sauti kali ya mtoto ikilia. Haraka akanyanyuka na kukimbilia chumbani. Upesi akamwangalia mtoto, alikuwa yu kwenye kitanda chake analia haswa. Basi akamnyanyua na kujaribu kumbembeleza. Kitandani Josephine alikuwa amelala.

“Josephine,” Darrena kaita na kuuliza, “Hausikii mtoto analia?”

Kimya.

Darren akaita tena na kuuliza. Bado kimya. Basi akadhani bado Josephine ameendeleza mgomo wake. Lakini ndiyo mpaka kwa mtoto? Akajiuliza. Akatoka chumbani humo na kwenda mpaka sebuleni akiwa anambembeleza mtoto wake, hatimaye mtoto akalala.

Basi akaona ni vema akamlaze mtoto kitandani chumbani. Alipofanya hivyo, kabla hajatoka chumbani akamwita tena Josephine. Bado kimya. Saa hii akaamua kutoondoka mpaka pale atakapotimiza adhma yake, kuongea na mkewe.

Akamgusagusa na kumshtua. Akamsogezasogeza na kumwita. Kidogo ndipo akabaini ya kuwa mkewe alikuwa amemeza vidonge vingi, kumbe pale hakuwa mzima. Povu lilikuwa linamtoka mdomoni na macho yake yamekwisha panda juu!

Akachanganyikiwa haswa.

Uopesi akambeba mkewe na kumkimbizia kwenye gari, na pasipo kufunga mlango akatia moto gari na kuendesha kwa haraka amwahishe hospitali. Lakini kufika mbele ndipo akabaini hata na mtoto alikuwa amemwacha ndani!

“Mungu wangu!” akajikuta anatoka na maneno. Akarudi nyuma upesi na kujitengenezea vema kwenye barabara kisha akarudi nyumbani kwa kasi ya ajabu.

Alipofika akakimbilia ndani na kumbemba mtoto, akamweka ndani ya gari na kutimka kama kimbunga!

Laiti askari angemwona namna alivyokuwa anaendesha, asingeshani hata kama mwanaume huyo amembembelea mtoto na mwanamke ndani. Akili yote ya Darren ilikuwa imeruka! Alikuwa anamuwaza mkewe tu. Lakini pia akidhani huenda akawa amempoteza, au atampoteza akiwa njiani.

Kheri akafika hospitalini salama. Akamtua mke wake na kumwahisha kupatiwa huduma. Yeye na mwanaye wakakaa kitini kungoja taarifa ya daktari.

Darren akiwa amekaa hapo akawa anaomba kila aina ya sala mkewe anusurike.

Kama baada ya dakika tatu, Isabel akampigia simu.


**
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 19*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Kheri akafika hospitalini salama. Akamtua mke wake na kumwahisha kupatiwa huduma. Yeye na mwanaye wakakaa kitini kungoja taarifa ya daktari.

Darren akiwa amekaa hapo akawa anaomba kila aina ya sala mkewe anusurike.

Kama baada ya dakika tatu, Isabel akampigia simu.

ENDELEA

Akaitazama simu hiyo na kusonya, hakutaka kupokea, lakini ikaita pasipo kukoma, hatimaye, kwa kuepusha usumbufu, akapokea na kuiweka sikioni.

“Hey Darren,” Sauti ya Isabel ikasalimu na kisha kuuliza, “Kuna shida?”

Swali hili likamshtua kidogo Darren. Alijiuliza kama Isabel amemwona ama? Mbona ni mara ya pili hii akimuuliza swali hilohilo?

“Isabel,” Darren akaita na kuuliza, “Una maanisha nini kuniuliza hivyo?”

“Najua una matatizo, Darren,” Isabel akasema kwa kujiamini.

“Umejuaje kama nina matatizo?”

“Uso wako tu unaonyesha. Niambie ukweli Darren, hauna shida?”

Darren akawa kimya kidogo.

“Ni sawa, Darren. Kama utakuwa una shida basi unajua pa kunipata.” kisha Isabel akakata simu na kumwacha Darren akiwa kwenye lindi la mawazo. Ni kweli Isabel anayajua anayoyapitia ama anahisi tu? Je ni sahihi kwake kumshirikisha mwanamke huyo ama akaze kifua tu?

Alijiuliza pasipo na kikomo. Daktari akaja na kumshtua amwitaji ofisini. Alipoenda huko Daktari akamweleza maendeleo ya mkewe kuwa ameathirika sana na madawa aliyoyatumia. Kurudi kwenye hali yake itawachukua muda kidogo.

“Laiti ungemuwahisha, kazi ingekuwa nyepesi zaidi,” Daktari alisema vivyo na kisha kumpatia moyo bwana Darren, “Usijali, atapona tu. Japo yatupasa tuchukue muda kwa mwili wake kurejea kwenye hali ya kawaida.”

Basi Darren baada ya habari hizo, akajiendea kwenye benchi kuketi zaidi. Hapo akawa na mwanaye aliyekuwa anambembeleza. Mwanaye aliyekuwa anamwonea huruma kwa mama yake kuwa hoi kwa ugonjwa.

Alikaa hapo kwa masaa mawili kabla hajaona ni vema kumjuza Roby ili aje kumjulia hali. Punde kidogo, Roby akaja na angalau Darren akapata muda wa kutoa yaliyo kifuani mwake. Angalau akajihisi mwepesi kwa kunena yanayomsibu.

Kuongea napo ni tiba.

Roby akampa pole sana na kumfariji. Akakaa naye kwa muda mrefu kabla hajamuaga aende kupumzika nyumbani.

“Utaniambia kitakachotokea, Darren. Lakini nakushauri kwanza uende nyumbani ukapumzike na kumpatia mahitaji huyo mtoto,” alishauri Roby kabla hajajiendea zake. Darren akamsindikiza kwa macho akitamani kumwambia mwanaume huyo asimwambie Melissa chochote kile.

Alijua fika angemwambia hivyo Melissa basi mwanamke huyo angefika hapo ndani ya masaa machache. Hakutaka kabisa kuwa karibu na mwanamke huyo. Lakini angemwelezaje hivyo Roby?

Roby akaenda zake. Darren akajikusanya na kwenda nyumbani kumlisha mtoto na kuweka mambo mengine sawa. Alipohakikisha kila kitu kipo kwenye utaratibu, akaenda kuoga aondoe uchovu.

Alipotoka bafuni na kutazama simu yake akakuta ‘missed calls’ toka namba ya Roby. Baada ya kujiuliza kidogo akapiga na kupachika simu yake sikioni. Baada ya kuita kidogo, ikapokelewa. Ajabu likuwa ni sauti ya kike. Sauti ambayo si ngeni masikioni mwa Darren.

“Hujambo?”

“Sijambo. Nani?”

“Umeshanitambua, Darren. Najua namba yangu umeifunga.”

“Unataka nini Melissa?”

“Nimesikia una matatizo. Vipi upo sawa?”

“Ndio, nipo sawa. Kuna lingine?”

“Pole sana, Darren. Najua matatizo unayoyapitia hivi sasa. Usi--”

“Melissa! Naomba niskize vema, sawa? Sitaki kuwasiliana na wewe. Naomba uachane na mimi. Tafadhali. Na kama ukiendelea kunisumbua basi nitamwambia Roby juu yako.”

Melissa akaangua kicheko.

“Huoni utakuwa umenirahisishia kazi, Darren?” akauliza. “Kama ukimwambia Roby kuhusu mimi na wewe, nami nitamkubalia kila kitu na kumwongezea taarifa zaidi. Mosi, urafiki na ubia wenu utakuwa hatihati, pili, utakuwa umenisafishia njia ya mimi kurudi kwa--”

Darren akakata simu. “Shenzi!” akatupia simu kochini na kudaka kichwa chake kwa mawazo.

Melissa akasonya akitazama simu yake, kisha akamtazama Roby aliyekuwa amelala kitandani fofofo. Akanyanyuka na kujiondokea zake akimwacha mwanaume huyo hajielewi A wala Z.

Akashuka mpaka chini na huko akapanda gari la Roby na kutimka akienda tusipopajua.

Baada ya muda kidogo, Darren akamwona akiwa anasinzia. Alikuwa tayari ameshakula na ni usiku sasa. Aliwaza kumlaza mtoto huyo alafu aende mwenyewe hospitali, lakini akasita. Atamwachaje mtoto hapo? Akafikiri afanye nini.

Baada ya muda kidogo akaona ni kheri tu kama ataenda na mtoto huyo hospitali. Asingekuwa na amani kama mtoto huyo angelibaki mwenyewe nyumbani. Hakuwa na budi. Akajifungia mwanaye kifuani kwa kibebeo maalum kisha akabeba chupa ya maziwa endapo kama mtoto atahitaji hapo baadae.

Akajiweka kwenye gari na safari ya kwenda hospitali ikaanza. Alifikiri sana alipokuwa njiani. Maisha yalikuwa yamebadilika pasipo mkewe, inabidi atafute namna, hawezi akawa anaongozana na mtoto muda wote. Vipi akihitaji kwenda kazini?

Akiwa kwenye foleni la mataa, akakubali na nafsi yake kuwa kwa kipindi hiki ambacho mkewe anaumwa, inabidi amtafute ‘babysitter’ atakayemtazama mtoto na kumpa mahitaji yake. Na pale mkewe atakaporejea kwenye hali yake basi mhudumu huyo atajiendea zake.

Ila akapata tena wazo jingine, vipi kama akiwa anampeleka mtoto huyo mahali pa kutunzia watoto, ‘daycare’, huko awe anampitia akitoka kwenye mihangaiko yake?

Kidogo wazo hili likawa gumu. Aliona ni kama kumtupa mtoto wake kwa kufanya hivyo. Hapana, siwezi, akawaza. Hakuwa na imani sana na hiyo njia hivyo akachagua ile ya kwanza, amtafute dada atakayekuwa anamsaidia.

Akaendesha gari mpaka hospitali. Alipofika huko akazima gari lake na kukwea kwenda juu. Aliposonga kuendea pale ambapo mkewe alikuwa amepumzishiwa, akastaajabu kumwona Melissa!

Mwanamke huyo alikuwa amesimama akitazamatazama huku na huko, mkononi mwake ana simu kubwa nyeusi anayoipigapiga kiganjani. Alikuwa ni kama mtu aliyepotea.

Darren akamfuata kwa hasira na kusimama mbele yake akimuuliza, “Umekuja kufanya nini hapa Melissa?”

“Kukuona,” Melissa akajibu kwa tabasamu. “Kwani kuna ubaya?”

“Melissa, nikuambie mara ngapi wewe?”

“Kwani Darren mimi nimekuambia mara ngapi? Ushawahi kunielewa?”

“Hivi hauogopi hata Roby akijua upo hapa.”

Melissa akaguna kwa cheko. “Roby?” akauliza na kisha akatabasamu. “Hawezi jua. Amejilalia hajiwezi!”

“Melissa, nikuombeje uachane na maisha yangu? Nikuombeje, ebu niambie. Melissa achana na maisha yangu. Naku--” Mara nesi akapita na kuzama ndani ya chumba alicholazwa Josephine. Kidogo tena, mlinzi aliyekuwa amevalia sare zake akajongea eneo hilo na kuuliza, “Kuna tatizo hapa?”

Darren akamtazama Melissa, Melissa akamjibu mlinzi, “Hamna tatizo, bwana. Waweza tu kuendelea na majukumu yako mengine.”

Lakini kabla mlinzi hajaondoka hapo, mara nesi akatoka chumba cha mgonjwa akiwa anatembea kwa kasi sana. Darren akapatwa na hofu. Kidogo tu, nesi akarejea na daktari wakazama mule chumbani.

Kama baada ya robo saa, daktari akatoka na kumwambia Darren kuwa mke wake amefariki.


**
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ---- 20*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lakini kabla mlinzi hajaondoka hapo, mara nesi akatoka chumba cha mgonjwa akiwa anatembea kwa kasi sana. Darren akapatwa na hofu. Kidogo tu, nesi akarejea na daktari wakazama mule chumbani.

Kama baada ya robo saa, daktari akatoka na kumwambia Darren kuwa mke wake amefariki.

ENDELEA

Darren alihisi daktari anamtania. Aliuliza mara nne kama alichoambiwa ni kweli na daktari asibadilishe maneno akarejelea kauli yake ile ile na kisha kumpa pole Darren kwa kumpoteza mtu wake wa karibu.

Darren akalia kama mtoto mdogo. Msalaba huu ulikuwa ni mkubwa sana kwake. Hakujiona kama anaweza kuubeba. Bado alikuwa anamhitaji mke wake haswa kipindi hiki ambacho mtoto ni mdogo.

Ataishije? Alijiuliza akiwa anamwaga machozi kwenye benchi. Melissa alijaribu kumtuliza lakini asifanikiwe. Bwana huyo aliendelea kulia kwa uchungu kwa kumpoteza mpendwa wake. Mwishowe hata machozi na sauti ikawa imemkauka.


**

Baada ya watu wote kuondoka na kumwacha makaburini, Darren aliijipangusa mdomo wake na kutazama kaburi la mkewe. Bado halikuwa limesimikwa jina wala maelezo yoyote yale. Macho yake yalikuwa makavu na meupe, hakulia siku hiyo.

Alichuchumaa na kusema mwenyewe akiamini anateta na mkewe, “Nakupenda sana, mke wangu. Umeondoka tukiwa hatujamaliza tofauti zetu. Roho inaniuma sana kwa hilo lakini sina cha kufanya. Nisamehe sana mpenzi.”

Aliposema maneno hayo akanyamaza kwanza. Macho yakaanza kujawa na machozi. Akajipangusa na kuendelea kusema, mara hii sauti yake ikiwa inatetemeka. “Sijui nitaishi vipi pasipo wewe. Sijajua …” akajipangusa chozi. Alikuwa anahisi kifua chake kinawaka moto. Moyo umekuwa mzito sana. Alikuwa anajihisi hovyo, hovyo ambayo haiwezi kuelezeka.

“Umekuwa mwanamke wangu wa kujivunia kwa muda wote huo. Siwezi kueleza ni kwa namna gani ulijaza upendo na furaha ndani ya nyumba yangu. Hakika hakuna wa kuziba pengo lako. Maisha yangu hayatakuwa sawa tena pasipo na wewe.”

Kisha akanyanyuka na kuendea gari, akajipakia kwenye viti vya nyuma na kufunga mlango, gari likaondoka. Dereva alikuwa Roby, pembeni yake akiwa amekaa Melissa.

Japo watu walikuwa wawili kwenye gari, Darren hakuongea chochote. Alikuwa kwenye ulimwengu wake wa pekee kabisa. Akiwa amelaza kichwa chake kwenye kiti, alikuwa anatazama nje. Uso wake ulikuwa umepooza na kupwaya. Alikuwa mbali sana kimawazo.

Gari lilisimama mbele ya nyumba yake, Roby akamgeukia na kumuuliza kama yuko sawa, lakini hakuwa anasikia kitu. Ilimbidi Roby arejelee swali lake mara tatu ndipo Darren akamtazama na kumjibu. “Niko sawa, nashukuru.”

Na kabla halijaongezewa neno lingine, akafungua mlango na kutoka ndani ya gari. “Kwaheri!” akapunga mkono wake mara moja kwa Roby kisha akajigeuza na kuelekea ndani kwake.

Basi baada ya hapo maisha ya Darren yakabadilika kabisa. Hakuwa mtu wa kuzungumza bali kukaa kimya na kujitenga. Mara nyingi alikuwa ni mtu wa mawazo sana na hata kulia. Ndani ya juma moja tu akapungua uzito kwa kiasi kikubwa sana. Alikuwa ni kana kwamba mtu anayeliwa na kansa hatua ya nne.

Hakuwa na raha. Ilikuwa ni nadra kwake kutabasamu ama kucheka. Roby akajitahidi sana kukaa naye na kumhasa lakini haikusaidia. Naye Isabel akajaribu sana kujiweka karibu na Darren, lakini bado jitihada zake zikagonga mwamba. Darren hakuwa anataka kukaa karibu na mtu. Alikuwa anataka kukaa mwenyewe tu.

Akirudi nyumbani humuuliza dada wa kazi juu ya maendeleo ya mtoto kisha anamwona mwanaye kwa muda mfupi na kwenda kujilaza. Siku nyingine akawa anarudi nyumbani akiwa na chupa za vinywaji vikali. Anakunywa pasipo kujionea huruma na kisha analala kama mfu.
Siku nyingine hata kazini akawa haendi. Anakunywa tu siku nzima. Afya yake ikaendelea kuzorota.

Ikiwa ni mwezi mmoja umepita tangu Josephine afariki, Darren akajiona sasa anahitaji msaada. Alionana na mwanasaikolojia na kumweleza shida yake kwa ajili ya ‘counselling’. bwana huyo mwanasaikolojia, bwana Hamlet, akajitahidi kadiri ya uwezo wake kumsaidia Darren kwa kumpatia ushauri, lakini Darren akaenda mbele zaidi kwa kumwambia na yale mengine yakutisha. Mambo anayoona usiku na viumbe wa ajabu.

Hapo bwana Hamlet akasita kumshauri. Mwanzo alihisi Darren atakuwa amekanganyikiwa kutokana na kumpoteza mtu wake wa karibu lakini baadae akaja kuelewa baada ya Darren kumwambia alishawahi kuyaona mambo hayo hata kabla ya mkewe kufariki.

“Tafadhali, unaweza kunisaidia?” Darren alilia. Bwana Hamlet akamtazama kwanza mwanaume huyo kwa mafikirio kisha akamsihi apate muda wa kupumzika zaidi, pia kama itakuwa inawezekana basi akatafute mahali pengine pa kuishi mbali na hapo alipo. Pengine yaweza kumsaidia.

Darren akashukuru kwa ushauri na kwenda zake. Alipojiweka kwenye gari akafikiria kwanza maneno aliyoambiwa na bwana Hamlet.

Akiwa fikirani humo, mara upepo wa wastani ukapuliza kiasi na kupeperusha gazeti fulani lililokuwa chini mpaka kwenye kioo cha gari lake. Gazeti hilo lilikuwa la kale kidogo. Upande ambao ulijipachika kiooni ulikuwa na picha ndogo tatu na maelezo kadha wa kadha.

Katika maelezo hayo, mojawapo ilisomeka; *“MWANAMKE ANAYESUMBULIWA NA VIUMBE WA AJABU, APOTEA.”*

Habari hiyo ilikamata fahamu za Darren. Kidogo upepo ukalisomba gazeti hilo na kulitupia kando na kuliburuza zaidi na zaidi. Darren akatoka kwenye gari na kulikimbilia. Akalinyaka na kurudi ndani ya gari. Akatulia na kusoma taratibu habari ile ambayo ilimkamata hisia.

Alipomaliza kusoma akaliweka gazeti hilo kando na kutazama akiwa amejawa na mawazo. Kidogo akawasha gari na kuendea anwani ya nyumba ambayo ameona taarifaze kwenye gazeti.

Alitembea barabarani kwa masaa matano. Ilimlazimu aweke mafuta ili akamilishe safari yake. Alipofika, ilikuwa ni nyumba ya mbao yenye ukubwa wa wastani, akagonga na punde akafunguliwa na binti mwenye makamo ya miaka ishirini, akaeleza shida yake anataka kuonana na wazazi.

Binti akamkaribisha ndani na kidogo akaja mwanamke mnene kidogo mwenye nywele fupi nyeusi. Mwanamke huyo alikuwa ana macho makali na mkononi mwake alikuwa amebebelea kitambaa alichokuwa anatumia kukaushia vyombo. Yule binti aliyemkarimu mgeni akaenda zake chumbani.

“Habari, naitwa Darren.”

“Karibu, naweza kukusaidia,” aliuliza yule mwanamke akiwa anatazama kwa mashaka. Hakuwa na imani machoni. Darren akaeleza shida yake akionyesha lile gazeti. Alikuwa anataka kusikia habari zaidi za yule mwanamke aliyepotea. Kwa namna moja ama nyingine alikuwa anaona habari hiyo na ile ya maisha yake zinawiana.

Baada ya kusema hivyo yule mwanamke mwenyeji akatazama chini na kisha akarudi alipotokea, jikoni, kisha baada ta muda kidogo akarudi akiwa hana kile kitambaa bali ana kisu. Kidogo Darren akahofia. Mwanamke yule akaketi kiti kitazamanacho na Darren alafu akaweka kisu chake mezani.

Kisu kilikuwa kina mpini wa bluu, na kama ungekitazama vema ungeona maandishi yasomekayo ‘stainless steel’ kwenye shina la makali yake. Kilikuwa ni kisu kirefu chenye ncha kali. Darren alishindwa kujizuia kutokutazama kisu hicho.

“Upo tayari na utasadiki?” akauliza mwanamke yule akiwa anamtazama Darren machoni.

“Ndio, nipo tayari,” Darren akajibu. Basi mwanamke yule akanyanyua kisu kile na kukichomeka kwanguvu mezani. Kisu kikachimba meza na kusimama dede. Darren akazidi kuhofu.

Basi mwanamke yule akaanza kusimulia kwa sauti yake inayofanana na kasuku. Akiwa ameongea sentensi mbili tu, upepo ukapuliza dirishani na kupeperusha pazia kama bendera. Darren akatazama huko upesi akiwa mjawa wa mashaka.



**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom