*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 10*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
“Sijakupata, Fiona. Ni nini unaongelea?”
“Ofisi yako iko wazi, kila kitu kimevunjwa na kuchanwa. Nayo pia nimwambieje boss?”
Darren akaachama kwa mshangao.
ENDELEA
Si kwamba hakuwa amesikia alichoambiwa na Fiona, lah, ila hakuwa anaamini. Akauliza, “Unasemaje, Fiona?”
Fiona akarudia tena kumwambia alichomwambia hapo awali. Basi Darren akakosa ustahimilivu, akasimama na kujiandaa upesi aende huko tofauti kabisa na alivyokuwa ameshapanga. Ndani ya muda mfupi akawa kwenye gari lake, upesi akatimka.
Akiwa barabarani, akitingwa sana na mawazo, almanusura kumgonga mpita njia. Ni shukrani gari lake liliweza kusimama kwa wepesi kabla ya kumsomba mhanga. Akasimamisha gari na kushusha pumzi ndefu apunguze mihemko na kujiweka sawa kisha akaendesha tena mpaka ofisini.
Huko mtu wa kwanza kuonana naye akawa ni Fiona. Akiwa ametweta, akamwambia, “Tafadhali, Fiona. Nambie kilichojiri.” naye Fiona akamweleza kinaganaga kuwa ofisi yake imekutwa wazi na ikiwa shaghalabaghala!
“Lakini imewezekanaje?” Darren akastaajabu. “Jana nimeondoka baada ya kuifunga!”
Fiona akapandisha mabega. “Darren, nitayajuaje yote hayo?”
Darren akauliza, “Bossi yupo ndani?” Fiona akamjibu kwa kutikisa kichwa. Darren akanyookea huko. Akagonga mara moja na kufungua mlango. Boss alikuwa amejilaza kwenye kiti chake kirefu akiwa amekumbata viganja vyake. Amevalia suti nyeusi na tai nyekundu.
Darren akajieleza kwanini hakuwapo kazini siku hiyo, kuwa anaumwa, na hayo ya ofisi kukutwa wazi na vitu vikiwa hovyo, yeye hana habari nayo. Basi Bossi akamsikiza mpaka alipomaliza kisha asiseme jambo, hata salamu akiwa hajaitikia, akafungua droo ya meza yake na kutoa barua bahashani, akampatia Darren.
Darren akaitazama barua hiyo na kumuuliza, “Ya nini?”
“Utakapoisoma, utajua ya nini?” Mkuu akamwambia na kisha akamwonyeshea mkono mlangoni.
“Tafadhali, mkuu,” Darren akaomba. “Uniskize na kila ninachokuambia toka kwenye kinywa changu ni cha kweli tupu.”
“Darren!” Boss akaita kwa sauti kuu. “Naomba uende!”
“Tafadhali, naomba uniskize,” Darren akaendelea kuomba. Basi Boss akamwambia, “kaniletee hiyo kazi unayonambia uliifanya hiyo jana usiku!”
Upesi Darren akatoka na kwenda ofisi kwake. Huko kweli akakuta vitu vikiwa hovyo sana hata akatahamaki asipate majibu. Akajaribu kutazama tarakilishi yake, nayo ilikuwa imepasuliwa kioo, mashine ilikuwa chini! Akaishiwa na nguvu.
Akajikuta akikaa chini akiwa ameshika kichwa chake. Hakuwa anajua cha kufanya. Hakuwa anajua nini cha kusema. Kwa kama dakika tano akiwa amekaa hapo akapata wazo la kwenda kuonana na mlinzi. Alipoenda kwenye kibanda chake, hakumkuta. Mlinzi huwa anakuja nyakati za jioni na si muda ule.
Basi Darren akajikuta hana cha kujitetea. Akiwa ameinamisha kichwa chake chini akajongea kujiondokea. Kabla hajafika langoni, akaitwa, alipogeuka akamwona Roby.
“Ngoja, Dareen!” Roby alimpungia akikimbia. Alipomfikia akamwomba wakaketi kule mgahawani kwani anataka kuteta naye kidogo. Basi wakaongozana kwenda huko, na walipoagiza chakula, Roby akasema, “Nimesikia habari zako, Darren. Ni nini kimetokea?”
Darren akamweleza yale anayojua. Roby alipoyasikia akashangazwa, lakini hakusita kumpatia moyo. “Yote ni maisha, Darren. Nadhani sasa ni muda wa kuangalia mlango mwingine.”
Akamshika bega na kumwambia, “Ni muda wa kufanyia kazi lile shauri lako hivi sasa.”
“Nitawezaje, Roby?” Darren akasema kwa sauti ya chini. Macho yake yalikuwa yameingia ndani. Mdomo wake umemkauka. “Sina pesa hivi sasa. Nitawezaje kuyafanya hayo?”
Roby akatikisa kichwa. Akafikiri kidogo kisha akamwambia, “Ebu ngoja. Nadhani kuna kitu tunaweza kufanya. Niachie hii siku na kesho yake, nitakutafuta. Sawa?”
Basi Darren alipomaliza kula akajiendea zake. Alikuwa ametingwa sana na mawazo. Hata alipofika nyumbani kwake, mkewe akatambua kuwa mumewe hakuwa sawa. Alipomuuliza nini shida, Darren akampatia barua toka kwa bosi wake. “Nimefukuzwa kazi.”
Josephine akasoma barua hiyo na mpaka alipomaliza, machozi yakawa yamemjaa machoni mwake. Alikuwa amevunjika moyo, lakini akamtia moyo mumewe. “Usijali. Ni changamoto za maisha tu. Litapita.” kisha akambusu na kujilaza kifuani mwake.
Siku hiyo ikaenda Darren akiwa na mkewe na mtoto wake. Hata siku inayofuata wakaamka na kudumu siku nzima nyumbani. Darren akacheza na mwanaye na pia mkewe. Ilikuwa ni siku nzuri. Hakuwahi kukaa na familia yake katika namna ile tangu pale alipoipata. Kwa muda akasahau matatizo yake.
Siku iliyofuata, kama vile Roby alivyomuahidi, akamtafuta kwa njia ya simu. Walipoongea wakapanga kuonana majira ya jioni Roby akitoka kazini. Basi majira hayo yalipofika, Darren akaenda nyumbani kwa Roby kukutana naye.
Wakateta kujuliana hali kabla Roby hajaanza kumwambia Darren lengo la wito wake hapo.
“Lile wazo lako laweza kutimia Darren. Tunachokihitaji hivi sasa ni dhamira ya kweli, na si pesa!”
“Umepata pesa?” Darren akawahi kuuliza akitoa macho.
“Tuliza munkari, Darren,” Roby akasihi. “Sijapata pes yoyote, ila pesa ipo. Tunachotakiwa kufanya ni kuandika muswada wa mipango yetu, muswada mzuri wa kueleweka, alafu kuna mahali tutapeleka na kupata pesa.”
Darren akanywesha uso. “Roby, unadhani ni kitu chepesi namna hiyo?”
“Skiza, Darren. Najua ninachokuambia. Na ninakuambia kwa uhakika wote. Kuna kampuni mimi nimeshaongea nayo, nao wako radhi kusaidia kwa kila namna. Niamini mimi. Najua wewe ni mzuri kwenye maandishi, andika hiyo kazi nami nitakuonyesha namna mambo yanavyokwenda,” alisema Roby kwa kujiamini kisha akanyanyua glasi yake ya kinywaji na kuigongesha na ya Darren.
“Tutafanikiwa, Darren. Amini hivyo.”
Basi Darren akarudi nyumbani akiwa na mwanga wa matumaini. Akamkumbatia mkewe na kumjuza habari hizo, naye mkewe akafurahishwa sana. Akamwombea afanikiwe zaidi na zaidi.
Ulipofika usiku wa saa mbili, akaanza kuandika ule muswada ambao Roby alimtaarifu. Akaandika kwa ustadi akitumia masaa. Alipomaliza akausoma tena upya na upya. Akarekebisha aliyoyaona yanastahili, kisha akajilaza ikiwa ni saa tisa kasoro usiku.
Kesho yake akaonana na Roby na kumpatia ile kazi. Naye Roby akaipitia na kupendezwa nayo sana. Akatabasamu na kumwambia Darren, “Tumeshapata pesa hapa!”
Akamwahidi wataonana mwisho wa juma tena akiwa na majibu ya maana. Na kweli ilipofika mwisho wa juma, Roby akamwambia Darren wakutane kumpatia majibu ya ule muswada, ila si nyumbani tena bali kwenye jengo refu la HIGH TOWERING CONSULTANCY.
Darren akiwa na hamu kubwa, akajongea huko. Akakutana na Darren na mwanamke mrembo aitwaye Isabel. Mwanamke huyo alikuwa amevalia suti ya kijivu ilivyomkaa vema. Uso wake ulikuwa umepambwa na miwani nzuri ya macho. Nywele zake nyeupe na laini.
Kwa makadirio alikuwa na miaka thelathini na tano, sita ama saba. Hakuwa mnyimi wa tabasamu. Tabasamu lake zuri. Na alikuwa mtu mchangamfu, nadhifu mwenye macho ya kuvutia.
Roby akamtambulisha Darren kwa Isabel na kisha Isabel akajitambulisha kwa Darren kama ‘Executive Director’. Waliposalimiana na kutambulishana Isabel akakiri kuvutiwa na ule muswada na basi wao kama kampuni watawekeza takribani dola za kimarekani milioni kumi!
Swala hilo likamgusa sana Darren. Haukuwa uwekezaji mdogo huo kabisa. Aliona sasa ndoto yake inaenda kukamilika. Akashukuru na kisha akauliza ni kivipi uwekezaji huo utakuwa unarejeshwa.
Isabel akatabasamu kwanza kabla hajajibu, “ni mpaka pale mtakapoanza kutengeneza faida. Kampuni itakuwa inachukua gawio la asilimia ishirini tu la faida yenu nzima!”
Darren akaridhia. Akamkumbatia Roby akimwona kama malaika mwokozi kwake. Wakafungua akaunti ya pamoja na pesa ikaingizwa baada ya siku mbili tu. Na pasipo kukawia wakapata eneo na kuanza kulifanyia kazi kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya huduma za tiba ya wanyama.
Kwa kama mwezi mmoja tu, kila kitu kikawa tayari na huduma zikaanza kutolewa. Isabel naye akatembelea hilo eneo na kuomba kupewa mrejesho wa maendeleo ya huduma kila mwisho wa mwezi, lakini zaidi alikuwa amekuja na mbwa wake kwa ajili ya kumpatia chanjo.
Darren akamshughulikia kikamilifu na Isabel kabla hajaenda, akampatia Darren kadi yake ya biashara.
“Utan’tafuta utakapokuwa na tatizo.”
Kisha akamtazama Darren machoni na kumwambia, “Sawa?”
Darren akajibu, “Sawa.” akitabasamu.
***
Sent using
Jamii Forums mobile app