Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? -- 09*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akarejea na kuketi kitini kisha akawasha tarakilishi. Akaanza kuchapa na kuchapa. Ila hakudumu sana, akasikia tena sauti ya watu ikiteta na kucheka! Na mara hii, umeme ukamkatikia ndani ya ofisi!

Kidogo, akasikia sasa watu wakiteta ndani ya ofisi. Tena si mbali kabisa na yeye. Kwa kando ya kushoto!

ENDELEA

Akaogopa sana hata kushikwa na kitete cha hofu kuu. Aliwahi simu yake na kumulika awaone watu hao lakini hakufanikiwa kuona jambo. Alikuwa mwenyewe tu!

Akatwetwa jasho akihema. Moyo nao ukaenda pupa. Akiwa amewasha taa ya simu, akakusanya kila kilicho cha kwake asibake tena hapo. Akauendea mlango na kuufungua, hamaki haukufunguka! Aliuvuta na kuuvuta lakini kazi bure. Mlango ulikuwa mgumu kwenda mbele wala nyuma!

Akastaajabishwa na hili maana hakuwa ameutia loki mlango huo. Akaangaza kushoto na kulia kama ataona ufunguo lakini napo ikawa kazi bure, hakuona kitu. Basi akazidi kupatwa na hofu. Akazidi kuhemkwa akihisi kabisa hayuko mazingira salama.

Akihisi kitu fulani kibaya kitamtokea muda wowote ule. Basi jasho likazidi kummiminika. Akalowana makwapani, mgongoni na kifuani. Paji lake la uso likajawa na maji yatiririkayo ingali macho akiwa ameyakodoa haswa.

_Hakukuwa na mtu wa kumsaidia?_ Akawaza kichwani. Alitazama dirishani asione jambo bali kiza tu. Akapata wazo la kuita. Kweli akaita kwanguvu mara tatu akiomba msaada kwa yeyote aliyekuwapo karibu.

Lakini kuita kwake huko akaja kukuona ni bure. Hakusikia muitikio wala kitu chochote kile. Akajikuta anapoteza matumaini ya kusaidiwa. Akaumwa na kichwa akiwaza afanye nini. _je avunje mlango?_

Ila mlango huo haukuwa mwepesi hata kidogo. Kama ni kuuvunja basi yampasa atumie nguvu kubwa sana maana hakuwa na dhana hata moja mkononi. Na akisha kuuvunja je? Nini atakuja kusema kesho yake kwa mkuu wake wa kazi akamwelewa?

"Darren!" Akasikia sauti ya kike ikimwita kwa kunong'ona. Haraka akageuka na kuangaza akitumia simu yake. Uso wake ulifumwa kwa hofu sana na mkono wake ulioshikilia simu ulikuwa unatetemeka!

"Nani wewe? Unataka nini kwangu?" Darren akafoka. Mara akasikia sauti ya kiume ikimjibu kwa nje, "mimi mlinzi! Wewe nani humo?"

Darren akabaini kuna mtu amekuja kumsaidia. Akachungulia dirishani na kumwona mwanaume aliyevalia zare akiwa amesimama hapo. Akamsihi, "nisaidie kufungua mlango tafadhali!"

Yule mlinzi akabinya komeo na mara mlango ukafunguka! Haukuwa umefungwa kabisa.

"Mbona mlango u' wazi?" Akauliza mlinzi. Naye Darren hakuwa na majibu, na kwasababu ya kuona vitimbi, hakutaka kustaajabu, akajitoa nje na kufunga mlango huo.

"Nashukuru sana," akamwambia mlinzi kisha akatupa miguu yake kujiondokea. Mlinzi akamtazama akiishilia kisha akatikisa kichwa na kusema, "ukisoma sana tabu pia." Alafu akajiendea zake.

Darren akanyookea sehemu ya kuegeshea magari, akajipakia kwenye lile lililo kwake kisha akatimka. Hakuwa sawa kiakili. Na alijitahidi sana kuhakikisha hawazi yale mambo yaliyomtukia ofisini ili asije pata ajali barabarani kwasababu ya msongo.

Alipofika akamkumbatia mkewe kwanguvu na kumbusu kwenye paji lake la uso. Mtoto alikuwa tayari ameshalala.

"Darren," Josephine akaita. Uso wake ulikuwa hauna furaha. Ulijawa na makunyanzi na macho yake yakiwa mekundu. "Nilikukumbuka sana. Saa tano hii yaelekea saa sita. Hujawahi kuja nyumbani muda huu."

"Najua, mke wangu," Darren akampoza. Akamkumbatia na kumwambia, "haitatokea tena. Nakuahidi."

Basi Josephine hakuteta tena kuhusu hayo, akamwandalia mume wake chakula na kumkaribisha ale. Naye japo alikuwa tayari ameshakula, kwasababu ya kumpa motisha mumewe, akala pamoja naye.

Wakala kwa ukimya kwa kama sekunde kumi na mbili kabla Josephine hajauvunja ukimya kwa kumuuliza mumewe, "Ulisikia zile habari za moto?"

Darren akashtuka. Hata mkewe akatahamaki kwanini mumewe alishtuka vile. Bwana akasema, "sitaki hizo habari!' Akiwa amekunja uso. "Sitaki kuzisikia hata robo. Sawa?"

Hata Josephine hakujibu. Alikuwa amebanwa na tahamaki. Darren akasimama na kwenda zake ndani akiwa ameacha chakula pale mezani.

_Ana nini huyu?_, Josephine akabaki akiduwaa. Akajiuliza akiwa anatazama kile chakula kilichobakia. Mwishowe akakipeleka jikoni na kisha akazima kila kitu aende kumkuta mumewe chumbani.

Alipofika huko, akamkuta Darren akiwa bafuni anakoga. Basi akamgojea kitandani amuulize kulikoni. Alipotoka akamwomba msamaha kama alimkwaza, halikuwa lengo lake.

Lakini pia akataka kujua nini kilikuwa kinamsumbua mumewe. Kwanini aligeuka na kuwa mbogo upesi hivyo? Tangu ameolewa naye hakuwahi kumwona akiwa vile. Shida kitu gani haswa?

"Josephine, sitaki kusikia habari zile ulizonambia. Huwezi jua zimenisababishia matatizo kiasi gani. Tafadhali nisizisikie tena. Nakuomba." Huo ukawa usemi wa mwisho kwa Darren kabla hajajilalia. Na siku hiyo hakumkumbatia mkewe kama ilivyo ada.

Alijilaza kando ya kitanda akiwa anatazama ukutani. Mkewe naye akalala, tena haikuchukua muda sana akapitiwa na usingizi akimwacha Darren macho.

Baada ya muda kidogo, Darren akaamua kujigeuza na kumkumbatia mkewe. Hapo baada ya muda kidogo akabebwa na usingizi mzito. Alikuwa amechoka sana. Ni hofu tu ndiyo ilimkawiza.

Yalipotimia majira ya saa tisa ya usiku, muda wa shetani, majira ya malaika mkengemfu, Darren akagutuka toka usingizi asijue nini kimemwamsha! Alitazama kushoto na kulia kwake. Kote kulikuwa salama. Akarejesha kichwa chake kitandani aendelee kulala.

Lakini kabla hajaupata huo usingizi, ghafla ya ajabu akasikia mtoto akilipuka kwa kilio! Akashtuka sana. Mtoto huwa analala chumba cha pili yake hivyo ni ngumu kujua kinachomsumbua. Inamlazimu mtu aende kumtazama.

Basi akajaribu kumwamsha Josephine, ila akawa mzito. Aliishia kugugumia na kuguna. Naye Darren akawaza mwanamke huyo atakuwa amechoka kwa kulelea mtoto siku nzima, hivyo acha amsaidie kwa kwenda kutazama.

Akatoka kitandani na kufungua mlango, alafu akaelekea kule kwenye chumba cha mtoto kwa upesi. Alipoingia humo akamkuta mtoto akilia sana. Mdomo ameutanua na macho yake yanamwaga machozi.

Akamnyanyua na kumbembeleza. Baada ya muda kidogo mtoto akanyamaza lakini asilale. Akambembeleza tena zaidi na zaidi, bado hakuwa anataka kulala. Mpaka kwenye majira ya saa kumi inayoelekea saa kumi na moja, ndipo mtoto akaanza kufumba macho yake kwa usingizi.

Basi akamlaza na yeye kurudi chumbani akajilalie kwa muda mdogo uliobakia. Alichoka sana. Alipojiweka tu kitandani akajikuta akipitiwa na usingizi mkali wa kumlaza fofofo.

Kuja kuamka, ilikuwa ni saa nne ya asubuhi!

"Josephine! Josephine! Mbona hukunamsha lakini?" Akang'aka akiwa amewehuka. Alikuwa nyuma ya muda sana. Saa nne! Kazi gani hiyo ya kwenda muda huo?

"Nilikuamsha Darren!" Akasema Josephine. "Mara ya kwanza ukanambia nikuache ulale maana umechoka. Mara ya pili ukanambia nisikusumbue!"

"Mimi?" Darren akatoa macho akijinyooshea kidole.

"Ndio, wewe Darren!" Josephine akamjibu akimbembeleza mtoto. "Sasa ningefanyaje? Nikaona nikuache!"

Darren akajaribu kufikiria hicho anachomwambia mkewe. Hakuwa anakumbuka hata tone. _Yeye kusema hayo?_

Kama haitoshi, Josephine akamwambia kuwa, "uliamka mara ya tatu wewe mwenyewe. Ukaenda bafuni na kisha ukatoka kutazama dirishani. Nilipokuuliza hauendi kazini leo? Ukanijibu wataka kupumzika. Darren haukumbuki au wataka tu kun'tania?"

Darren akatikisa kichwa. Akajikuna kichwa akijaribu kuwaza lakini hakuwa anakumbuka lolote lile. Akachukua simu yake na kumpigia dada Fiona, secretary, kumuuliza juu ya kazini.

"Sikia Fiona, sijiskii vema. Naomba uniandikie note umpelekee boss."

"Nimwambieje?" Fiona akauliza. "Muda huu kweli ni wa kutoa taarifa, Darren?"

"Tafadhali Fiona, fanya namna yoyote kunisaidia. Nitashukuru ukifanya hivyo."

Kukawa kimya kidogo.

"Sawa," Fiona akajibu na kuongezea, "na vipi kuhusu ofisi yako?"

"Imefanyaje?" Darren akauliza.

"Darren hujui ulichofanya?" Fiona akauliza kwa mshangao.

"Sijakupata, Fiona. Ni nini unaongelea?"

"Ofisi yako iko wazi, kila kitu kimevunjwa na kuchanwa. Nayo pia nimwambieje boss?"

Darren akaachama kwa mshangao.

**

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 10*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Sijakupata, Fiona. Ni nini unaongelea?”

“Ofisi yako iko wazi, kila kitu kimevunjwa na kuchanwa. Nayo pia nimwambieje boss?”

Darren akaachama kwa mshangao.

ENDELEA

Si kwamba hakuwa amesikia alichoambiwa na Fiona, lah, ila hakuwa anaamini. Akauliza, “Unasemaje, Fiona?”

Fiona akarudia tena kumwambia alichomwambia hapo awali. Basi Darren akakosa ustahimilivu, akasimama na kujiandaa upesi aende huko tofauti kabisa na alivyokuwa ameshapanga. Ndani ya muda mfupi akawa kwenye gari lake, upesi akatimka.

Akiwa barabarani, akitingwa sana na mawazo, almanusura kumgonga mpita njia. Ni shukrani gari lake liliweza kusimama kwa wepesi kabla ya kumsomba mhanga. Akasimamisha gari na kushusha pumzi ndefu apunguze mihemko na kujiweka sawa kisha akaendesha tena mpaka ofisini.

Huko mtu wa kwanza kuonana naye akawa ni Fiona. Akiwa ametweta, akamwambia, “Tafadhali, Fiona. Nambie kilichojiri.” naye Fiona akamweleza kinaganaga kuwa ofisi yake imekutwa wazi na ikiwa shaghalabaghala!

“Lakini imewezekanaje?” Darren akastaajabu. “Jana nimeondoka baada ya kuifunga!”

Fiona akapandisha mabega. “Darren, nitayajuaje yote hayo?”

Darren akauliza, “Bossi yupo ndani?” Fiona akamjibu kwa kutikisa kichwa. Darren akanyookea huko. Akagonga mara moja na kufungua mlango. Boss alikuwa amejilaza kwenye kiti chake kirefu akiwa amekumbata viganja vyake. Amevalia suti nyeusi na tai nyekundu.

Darren akajieleza kwanini hakuwapo kazini siku hiyo, kuwa anaumwa, na hayo ya ofisi kukutwa wazi na vitu vikiwa hovyo, yeye hana habari nayo. Basi Bossi akamsikiza mpaka alipomaliza kisha asiseme jambo, hata salamu akiwa hajaitikia, akafungua droo ya meza yake na kutoa barua bahashani, akampatia Darren.

Darren akaitazama barua hiyo na kumuuliza, “Ya nini?”

“Utakapoisoma, utajua ya nini?” Mkuu akamwambia na kisha akamwonyeshea mkono mlangoni.

“Tafadhali, mkuu,” Darren akaomba. “Uniskize na kila ninachokuambia toka kwenye kinywa changu ni cha kweli tupu.”

“Darren!” Boss akaita kwa sauti kuu. “Naomba uende!”

“Tafadhali, naomba uniskize,” Darren akaendelea kuomba. Basi Boss akamwambia, “kaniletee hiyo kazi unayonambia uliifanya hiyo jana usiku!”

Upesi Darren akatoka na kwenda ofisi kwake. Huko kweli akakuta vitu vikiwa hovyo sana hata akatahamaki asipate majibu. Akajaribu kutazama tarakilishi yake, nayo ilikuwa imepasuliwa kioo, mashine ilikuwa chini! Akaishiwa na nguvu.

Akajikuta akikaa chini akiwa ameshika kichwa chake. Hakuwa anajua cha kufanya. Hakuwa anajua nini cha kusema. Kwa kama dakika tano akiwa amekaa hapo akapata wazo la kwenda kuonana na mlinzi. Alipoenda kwenye kibanda chake, hakumkuta. Mlinzi huwa anakuja nyakati za jioni na si muda ule.

Basi Darren akajikuta hana cha kujitetea. Akiwa ameinamisha kichwa chake chini akajongea kujiondokea. Kabla hajafika langoni, akaitwa, alipogeuka akamwona Roby.

“Ngoja, Dareen!” Roby alimpungia akikimbia. Alipomfikia akamwomba wakaketi kule mgahawani kwani anataka kuteta naye kidogo. Basi wakaongozana kwenda huko, na walipoagiza chakula, Roby akasema, “Nimesikia habari zako, Darren. Ni nini kimetokea?”

Darren akamweleza yale anayojua. Roby alipoyasikia akashangazwa, lakini hakusita kumpatia moyo. “Yote ni maisha, Darren. Nadhani sasa ni muda wa kuangalia mlango mwingine.”

Akamshika bega na kumwambia, “Ni muda wa kufanyia kazi lile shauri lako hivi sasa.”

“Nitawezaje, Roby?” Darren akasema kwa sauti ya chini. Macho yake yalikuwa yameingia ndani. Mdomo wake umemkauka. “Sina pesa hivi sasa. Nitawezaje kuyafanya hayo?”

Roby akatikisa kichwa. Akafikiri kidogo kisha akamwambia, “Ebu ngoja. Nadhani kuna kitu tunaweza kufanya. Niachie hii siku na kesho yake, nitakutafuta. Sawa?”

Basi Darren alipomaliza kula akajiendea zake. Alikuwa ametingwa sana na mawazo. Hata alipofika nyumbani kwake, mkewe akatambua kuwa mumewe hakuwa sawa. Alipomuuliza nini shida, Darren akampatia barua toka kwa bosi wake. “Nimefukuzwa kazi.”

Josephine akasoma barua hiyo na mpaka alipomaliza, machozi yakawa yamemjaa machoni mwake. Alikuwa amevunjika moyo, lakini akamtia moyo mumewe. “Usijali. Ni changamoto za maisha tu. Litapita.” kisha akambusu na kujilaza kifuani mwake.

Siku hiyo ikaenda Darren akiwa na mkewe na mtoto wake. Hata siku inayofuata wakaamka na kudumu siku nzima nyumbani. Darren akacheza na mwanaye na pia mkewe. Ilikuwa ni siku nzuri. Hakuwahi kukaa na familia yake katika namna ile tangu pale alipoipata. Kwa muda akasahau matatizo yake.

Siku iliyofuata, kama vile Roby alivyomuahidi, akamtafuta kwa njia ya simu. Walipoongea wakapanga kuonana majira ya jioni Roby akitoka kazini. Basi majira hayo yalipofika, Darren akaenda nyumbani kwa Roby kukutana naye.

Wakateta kujuliana hali kabla Roby hajaanza kumwambia Darren lengo la wito wake hapo.

“Lile wazo lako laweza kutimia Darren. Tunachokihitaji hivi sasa ni dhamira ya kweli, na si pesa!”

“Umepata pesa?” Darren akawahi kuuliza akitoa macho.

“Tuliza munkari, Darren,” Roby akasihi. “Sijapata pes yoyote, ila pesa ipo. Tunachotakiwa kufanya ni kuandika muswada wa mipango yetu, muswada mzuri wa kueleweka, alafu kuna mahali tutapeleka na kupata pesa.”

Darren akanywesha uso. “Roby, unadhani ni kitu chepesi namna hiyo?”

“Skiza, Darren. Najua ninachokuambia. Na ninakuambia kwa uhakika wote. Kuna kampuni mimi nimeshaongea nayo, nao wako radhi kusaidia kwa kila namna. Niamini mimi. Najua wewe ni mzuri kwenye maandishi, andika hiyo kazi nami nitakuonyesha namna mambo yanavyokwenda,” alisema Roby kwa kujiamini kisha akanyanyua glasi yake ya kinywaji na kuigongesha na ya Darren.

“Tutafanikiwa, Darren. Amini hivyo.”

Basi Darren akarudi nyumbani akiwa na mwanga wa matumaini. Akamkumbatia mkewe na kumjuza habari hizo, naye mkewe akafurahishwa sana. Akamwombea afanikiwe zaidi na zaidi.

Ulipofika usiku wa saa mbili, akaanza kuandika ule muswada ambao Roby alimtaarifu. Akaandika kwa ustadi akitumia masaa. Alipomaliza akausoma tena upya na upya. Akarekebisha aliyoyaona yanastahili, kisha akajilaza ikiwa ni saa tisa kasoro usiku.

Kesho yake akaonana na Roby na kumpatia ile kazi. Naye Roby akaipitia na kupendezwa nayo sana. Akatabasamu na kumwambia Darren, “Tumeshapata pesa hapa!”

Akamwahidi wataonana mwisho wa juma tena akiwa na majibu ya maana. Na kweli ilipofika mwisho wa juma, Roby akamwambia Darren wakutane kumpatia majibu ya ule muswada, ila si nyumbani tena bali kwenye jengo refu la HIGH TOWERING CONSULTANCY.

Darren akiwa na hamu kubwa, akajongea huko. Akakutana na Darren na mwanamke mrembo aitwaye Isabel. Mwanamke huyo alikuwa amevalia suti ya kijivu ilivyomkaa vema. Uso wake ulikuwa umepambwa na miwani nzuri ya macho. Nywele zake nyeupe na laini.

Kwa makadirio alikuwa na miaka thelathini na tano, sita ama saba. Hakuwa mnyimi wa tabasamu. Tabasamu lake zuri. Na alikuwa mtu mchangamfu, nadhifu mwenye macho ya kuvutia.

Roby akamtambulisha Darren kwa Isabel na kisha Isabel akajitambulisha kwa Darren kama ‘Executive Director’. Waliposalimiana na kutambulishana Isabel akakiri kuvutiwa na ule muswada na basi wao kama kampuni watawekeza takribani dola za kimarekani milioni kumi!

Swala hilo likamgusa sana Darren. Haukuwa uwekezaji mdogo huo kabisa. Aliona sasa ndoto yake inaenda kukamilika. Akashukuru na kisha akauliza ni kivipi uwekezaji huo utakuwa unarejeshwa.

Isabel akatabasamu kwanza kabla hajajibu, “ni mpaka pale mtakapoanza kutengeneza faida. Kampuni itakuwa inachukua gawio la asilimia ishirini tu la faida yenu nzima!”

Darren akaridhia. Akamkumbatia Roby akimwona kama malaika mwokozi kwake. Wakafungua akaunti ya pamoja na pesa ikaingizwa baada ya siku mbili tu. Na pasipo kukawia wakapata eneo na kuanza kulifanyia kazi kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya huduma za tiba ya wanyama.

Kwa kama mwezi mmoja tu, kila kitu kikawa tayari na huduma zikaanza kutolewa. Isabel naye akatembelea hilo eneo na kuomba kupewa mrejesho wa maendeleo ya huduma kila mwisho wa mwezi, lakini zaidi alikuwa amekuja na mbwa wake kwa ajili ya kumpatia chanjo.

Darren akamshughulikia kikamilifu na Isabel kabla hajaenda, akampatia Darren kadi yake ya biashara.

“Utan’tafuta utakapokuwa na tatizo.”

Kisha akamtazama Darren machoni na kumwambia, “Sawa?”

Darren akajibu, “Sawa.” akitabasamu.


***

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom