*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 11*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
“Utan’tafuta utakapokuwa na tatizo.”
Kisha akamtazama Darren machoni na kumwambia, “Sawa?”
Darren akajibu, “Sawa.” akitabasamu.
ENDELEA
Aliporudi nyumbani alikuwa amechoka sana, lakini kabla hajajilaza akapata kuongea na mkewe juu ya maendeleo yake ya kazi. Mkewe naye akafurahishwa sana na hatua za mumewe, basi zaidi akamtia moyo.
Akamsihi tu kuwa anampenda na kila anapokuwa anakutana na gumu lolote basi akumbuke kuwa familia yake inampenda sana. Usiku ukawa mzuri na hata walipoimalizia kwa kula na kuoga.
Kesho yake kama ilivyo ada, Darren akaamka na kwenda kazini. Akafanya sana kazi pamoja na mwenziwe, kisha jioni ilipoingia Roby akamhasa waende mahali kupata chochote kitu kabla hawajaachana. Naye Darren akapendezwa na hilo wazo.
Wakaenda kwenye moja ya mgahawa wa KFC, hapo wakaagiza chakula na kinywaji. Wakala wakifurahia utamu wake na huku wakipiga soga za hapa na pale.
"Darren," Roby akaita na kusema, "Nadhani sasa ni wakati wa mimi kuoa!"
Darren akashangazwa. "Kweli?" Akamtazama Roby akikodoa.
"Ndio. Nina mpango huo. Vipi wasemaje?"
"Sina neno. Ni wazo zuri ila sijawahi kumwona mpenzi wako. Huwa unamficha kwa wivu nini?" Darren akasema na kisha wakaangua kicheko.
"Hapana ndugu. Nadhani tunapishana muda ndo' maana hujapata kumjua. Mwisho huu wa wiki tutakutana wote, nitamvesha pete ya uchumba!"
"Wow! Ni wazo zuri sana. Nami nakuunga mkono, Roby. Bila shaka itakuwa siku nzuri sana baina yetu."
“Ni kweli. Nampenda sana mchumba wangu. Japo bado mambo hayajakaa vema, naona ni muda stahili wa kumwonyesha mapenzi yangu kwake.”
“Nakupongeza sana kwa hilo. Vipi itakuwa ni surprise ama?”
“Ndio, itakuwa ni surprise. Naomba unipe wazo juu ya hilo, Darren. Sitaki aone kama niliyekuwa nikiyapanga yote haya.”
Basi Darren akampatia mawazo yake naye akayapenda sana. Wakakubaliana cha kufanya na muda wa kuyafanya kisha wakaagana na kila mmoja akaenda na njia yake.
Darren alipofika nyumbani akampasha habari hizo mkewe. Naye akafurahishwa nazo sana. Akakumbuka kipindi Darren anamvesha pete. Ilikuwa ni siku ya ajabu asiyoweza kuisahau maishani mwake.
“Ile siku ilikuwa ya kusisimua sana, Darren. Nami siwezi kusahau tabasamu lako na namna ulivyonipigia magoti. Haki ulifanya moyo wangu ukimbie kwa haraka. Nilijihisi fahari sana.”
Darren akafurahishwa na hayo maneno. Akanyanyuka na kumbeba mkewe kisha akamuuliza, “Na vipi kuhusu siku ile nilipokuwa nawe kanisani?”
Josephine akacheka kidogo akiziba mdomo wake kisha akatazama dari. “Loh! Ile ilikuwa ni siku ya maajabu kwangu, Darren! Nakumbuka kila jambo tangu asubuhi mpaka usiku wake. Nawezaje kusahau?”
Basi Darren akampeleka mkewe chumbani na kumlaza kitandani. “Tazama. Wewe ndiye furaha yangu ya kweli. Upendo wako umejaza ndani ya moyo wangu na mimi nafurahia uwepo wako kila siku.”
Ni kweli Darren alimpenda sana mkewe. Alishamsahau kabisa Melissa na vimbwanga vyake. Hakuwa anamkumbuka tena mdhalimu huyo. Mwanzoni hakuwa anaamini kama atakuja kumsahau Melissa. Alikuwa ameganda sana kwenye kichwa chake. Alimpa sana moyo wake. Ila kwa sasa dunia ilikuwa imegeuka.
Tena imegeuka na kubadili mhimili kabisa.
Lakini kwa Melissa …
Vipi kwa Melissa?
Darren hakuwa anajua. Na natamani asingekuwa analijua kamwe. Melissa alikuwa karibu yake kuliko alivyokuwa anadhani. Melissa alikuwa karibu yake pengine kuliko muda wowote ule.
Melissa alikuwa anafanya kazi yake. Tena taratibu na kwa ustadi wa hali ya juu. Mkono wake ulikuwa unagusa njia. Masikio yake yanaskiza upepo ukitikisa vipande vya majani. Sauti yake inaimbia fukweni mwa bahari.
Machho yake yakitawanyika kila pande. Na ndimi zake zikiwa zinasukutua mdomo kwa kila kona yake.
Melissa alikuwa ni shetani ambaye Darren asingewahi kumwazia kuwa. Ile tamu kwenye chungu. Lile tone la sumu ya mamba kwenye maji yaliyojaza jaba la miamba.
Siku zikapita, tena zikikimbia haswa. Na ile siku ya Roby kumvesha pete mchumba wake ikawadia. Siku hiyo Darren na Roby wakawasili mapema sana. Wakatengeneza mazingira ya kufanya mambo yao, ilikuwa ni pembeni ya fukwe ya bahari, na muda wa mchumba wa Roby kuwasili ulipowadia, Darren akajificha.
Walikuwa wameadhimia punde pale mpenzi wa Roby atakapotokea, basi Darren atajivika barakoa usoni na kuigiza amemkaba Roby na kumchoma kisu. Lakini kwa wakati huo huo atampatia Roby kijumba cha pete, hivyo wakati mchumba wa Roby atakapokuwa anamlilia mpenzi wake anayekufa, Roby atatoa kijumba cha pete na kumwomba akubali kuwa mke wake!
Ulikuwa ni mchezo wa hatari.
Basi Roby akamkumbatia mpenzi wake na kumuuliza kama amefurahia kuwapo hapo mwisho huo wa juma. Naye mpenzi wake akasema amefurahia.
Naye mpenzi wake huyo alikuwa ni Melissa.
Uzuri wake ulikuwa upo palepale. Macho yake mazuri ya kumlaghai nyoka atoke shimoni. Uso wake mtamu na sauti ya kukimbiza mapigo ya moyo.
“Kwanini umeamua kunileta ufukweni, Roby?” Melissa akateta kwa sauti yake tamu.
“Haujapapenda?” Roby akauliza wakiwa wanasonga mbele.
“Nimepapenda,” Melissa akamjibu. “Ila sikuwa nadhani kama utanileta huku. Kama ningelikuwa najua na kujipanga basi ningebeba na nguo za kuogelea. Au wewe umebebelea?”
“Hapana. Nipo kama nilivyo mpenzi.”
Basi wakazidi kusonga mbele zaidi na zaidi Roby akimvuta Melissa eneo la tukio. Ndani ya moyo wake alikuwa ana hamu kubwa ya kumshangaza Melissa. Alitamani kumwambia kuhusu mpango wake ila akajitahidi kujibana. Alitamani kupayuka kwa kupaliwa na furaha lakini akajibana sana.
Wakazidi kusonga.
Walipopiga hatua kama tatu tu ndipo Darren akawa amehakiki kile alichokuwa anakiona. Alimwona Melissa! Mwanamke aliyekuwa amemsahau. Alimwona Melissa, mwanamke mwenye kubebelea kitanzi mkononi mwake!
Akabaki akiduwaa, ameachama mdomo na kung’aza macho yake. Na pasipo kutarajia, Melissa akarusha macho kumtazama pale alipokuwapo. Macho kwa macho wakakutana.
“Melissa!” Darren akatamka akitikisa kichwa chake. “Niache Melissa!” akanong’oneza. “Niache Melissa!” kisha akajikusanya na kukimbia sana. Aliliendea gari lake na kuzama ndani akitupia barakoa yake pembeni.
Hakuamini alichotoka kuona. Ni kweli amemwona Melissa! Moyo wake ulimwenda mbio mno. Akahema sana akitokwa na jasho. Akataka kuwasha gari aende lakini mikono ikamtetemeka sana. Akaona ni kheri angoje kwani anaweza pata ajali akilazimisha kwenda.
Kule fukweni Roby akangoja sana. Akatazama kushoto na kulia akiwa anaishiwa na uvumilivu. Darren yuko wapi?
“Mpenzi,” Melissa akaita na kuuliza, “Kuna tatizo?”
“Hapana. Hamna ta--” Roby akateta akitupa macho. “Hamna tatizo!”
Basi baada ya kukaa sana hapo pasipo kuona kitu, akaamua kuondoka zake na mpenzi wake. Moyoni akabeba kinyongo kikubwa juu ya Darren. Akabeba pia na maswali, kwanini Darren amemfanyia hivyo? Kama kungalikuwa na tatizo si angemwambia mapema?
Moyo wake ukawa mzito. Akaghafirika sana.
Walipoenendea mahali ambapo Roby alipakia gari, Melissa akazama ndani lakini Roby akang’aza tena macho kama atamwona Darren. Bahati upande wake wa kulia, kwa mbali, akaona gari la Darren! Basi akalijongea upesi akimwambia Melissa amngojee kwa dakika chache.
Alipolifikia gari hilo, kwa ndani akamwona Darren, basi akaanza kufoka kabla hajafika, “Mambo gani hayo Darren unanifanyia? Ikama ungalikuwa hautaki si ungelinambia?”
Akachngulia dirishani kumtazama Darren. Akamwona akiwa amefumba macho kama mtu aliyemezwa na usingizi. Lakini matundu ya pua yake yakiwa yanachuruza damu kwa wingi!
Akatahamaki! “Darren!” akaita akifungua mlango upesi. Akamtikisa Darren kwanguvu akimwita lakini Darren hakuitikia kabisa. Zaidi damu zikarukia mpaka kwenye mikono ya Roby. Basi upesi Roby akamhamishia Darren kwenye kiti cha abiria na kisha akawasha gari kumwahisha Darren hospitalini upesi awezavyo!
Akiwa njiani, Darren akanong’ona kwa mbali, “Ni jini … Roby, Roby, ni jini … atakuua … ata--”
“Nini unasema Darren?” Roby akapaza sauti kuuliza, akitamani kumtazama Darren, akitamani kutazama barabara. Lakini Darren hakuweza kuongea tena. Macho yakajawa na ukungu na mwishowe akapotelea kabisa gizani.
“Roby …”
***
Sent using
Jamii Forums mobile app