Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? --- 11*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

“Utan’tafuta utakapokuwa na tatizo.”

Kisha akamtazama Darren machoni na kumwambia, “Sawa?”

Darren akajibu, “Sawa.” akitabasamu.

ENDELEA

Aliporudi nyumbani alikuwa amechoka sana, lakini kabla hajajilaza akapata kuongea na mkewe juu ya maendeleo yake ya kazi. Mkewe naye akafurahishwa sana na hatua za mumewe, basi zaidi akamtia moyo.

Akamsihi tu kuwa anampenda na kila anapokuwa anakutana na gumu lolote basi akumbuke kuwa familia yake inampenda sana. Usiku ukawa mzuri na hata walipoimalizia kwa kula na kuoga.

Kesho yake kama ilivyo ada, Darren akaamka na kwenda kazini. Akafanya sana kazi pamoja na mwenziwe, kisha jioni ilipoingia Roby akamhasa waende mahali kupata chochote kitu kabla hawajaachana. Naye Darren akapendezwa na hilo wazo.

Wakaenda kwenye moja ya mgahawa wa KFC, hapo wakaagiza chakula na kinywaji. Wakala wakifurahia utamu wake na huku wakipiga soga za hapa na pale.

"Darren," Roby akaita na kusema, "Nadhani sasa ni wakati wa mimi kuoa!"

Darren akashangazwa. "Kweli?" Akamtazama Roby akikodoa.

"Ndio. Nina mpango huo. Vipi wasemaje?"

"Sina neno. Ni wazo zuri ila sijawahi kumwona mpenzi wako. Huwa unamficha kwa wivu nini?" Darren akasema na kisha wakaangua kicheko.

"Hapana ndugu. Nadhani tunapishana muda ndo' maana hujapata kumjua. Mwisho huu wa wiki tutakutana wote, nitamvesha pete ya uchumba!"

"Wow! Ni wazo zuri sana. Nami nakuunga mkono, Roby. Bila shaka itakuwa siku nzuri sana baina yetu."

“Ni kweli. Nampenda sana mchumba wangu. Japo bado mambo hayajakaa vema, naona ni muda stahili wa kumwonyesha mapenzi yangu kwake.”

“Nakupongeza sana kwa hilo. Vipi itakuwa ni surprise ama?”

“Ndio, itakuwa ni surprise. Naomba unipe wazo juu ya hilo, Darren. Sitaki aone kama niliyekuwa nikiyapanga yote haya.”

Basi Darren akampatia mawazo yake naye akayapenda sana. Wakakubaliana cha kufanya na muda wa kuyafanya kisha wakaagana na kila mmoja akaenda na njia yake.

Darren alipofika nyumbani akampasha habari hizo mkewe. Naye akafurahishwa nazo sana. Akakumbuka kipindi Darren anamvesha pete. Ilikuwa ni siku ya ajabu asiyoweza kuisahau maishani mwake.

“Ile siku ilikuwa ya kusisimua sana, Darren. Nami siwezi kusahau tabasamu lako na namna ulivyonipigia magoti. Haki ulifanya moyo wangu ukimbie kwa haraka. Nilijihisi fahari sana.”

Darren akafurahishwa na hayo maneno. Akanyanyuka na kumbeba mkewe kisha akamuuliza, “Na vipi kuhusu siku ile nilipokuwa nawe kanisani?”

Josephine akacheka kidogo akiziba mdomo wake kisha akatazama dari. “Loh! Ile ilikuwa ni siku ya maajabu kwangu, Darren! Nakumbuka kila jambo tangu asubuhi mpaka usiku wake. Nawezaje kusahau?”

Basi Darren akampeleka mkewe chumbani na kumlaza kitandani. “Tazama. Wewe ndiye furaha yangu ya kweli. Upendo wako umejaza ndani ya moyo wangu na mimi nafurahia uwepo wako kila siku.”

Ni kweli Darren alimpenda sana mkewe. Alishamsahau kabisa Melissa na vimbwanga vyake. Hakuwa anamkumbuka tena mdhalimu huyo. Mwanzoni hakuwa anaamini kama atakuja kumsahau Melissa. Alikuwa ameganda sana kwenye kichwa chake. Alimpa sana moyo wake. Ila kwa sasa dunia ilikuwa imegeuka.

Tena imegeuka na kubadili mhimili kabisa.

Lakini kwa Melissa …

Vipi kwa Melissa?

Darren hakuwa anajua. Na natamani asingekuwa analijua kamwe. Melissa alikuwa karibu yake kuliko alivyokuwa anadhani. Melissa alikuwa karibu yake pengine kuliko muda wowote ule.

Melissa alikuwa anafanya kazi yake. Tena taratibu na kwa ustadi wa hali ya juu. Mkono wake ulikuwa unagusa njia. Masikio yake yanaskiza upepo ukitikisa vipande vya majani. Sauti yake inaimbia fukweni mwa bahari.

Machho yake yakitawanyika kila pande. Na ndimi zake zikiwa zinasukutua mdomo kwa kila kona yake.

Melissa alikuwa ni shetani ambaye Darren asingewahi kumwazia kuwa. Ile tamu kwenye chungu. Lile tone la sumu ya mamba kwenye maji yaliyojaza jaba la miamba.

Siku zikapita, tena zikikimbia haswa. Na ile siku ya Roby kumvesha pete mchumba wake ikawadia. Siku hiyo Darren na Roby wakawasili mapema sana. Wakatengeneza mazingira ya kufanya mambo yao, ilikuwa ni pembeni ya fukwe ya bahari, na muda wa mchumba wa Roby kuwasili ulipowadia, Darren akajificha.

Walikuwa wameadhimia punde pale mpenzi wa Roby atakapotokea, basi Darren atajivika barakoa usoni na kuigiza amemkaba Roby na kumchoma kisu. Lakini kwa wakati huo huo atampatia Roby kijumba cha pete, hivyo wakati mchumba wa Roby atakapokuwa anamlilia mpenzi wake anayekufa, Roby atatoa kijumba cha pete na kumwomba akubali kuwa mke wake!

Ulikuwa ni mchezo wa hatari.

Basi Roby akamkumbatia mpenzi wake na kumuuliza kama amefurahia kuwapo hapo mwisho huo wa juma. Naye mpenzi wake akasema amefurahia.

Naye mpenzi wake huyo alikuwa ni Melissa.

Uzuri wake ulikuwa upo palepale. Macho yake mazuri ya kumlaghai nyoka atoke shimoni. Uso wake mtamu na sauti ya kukimbiza mapigo ya moyo.

“Kwanini umeamua kunileta ufukweni, Roby?” Melissa akateta kwa sauti yake tamu.

“Haujapapenda?” Roby akauliza wakiwa wanasonga mbele.

“Nimepapenda,” Melissa akamjibu. “Ila sikuwa nadhani kama utanileta huku. Kama ningelikuwa najua na kujipanga basi ningebeba na nguo za kuogelea. Au wewe umebebelea?”

“Hapana. Nipo kama nilivyo mpenzi.”

Basi wakazidi kusonga mbele zaidi na zaidi Roby akimvuta Melissa eneo la tukio. Ndani ya moyo wake alikuwa ana hamu kubwa ya kumshangaza Melissa. Alitamani kumwambia kuhusu mpango wake ila akajitahidi kujibana. Alitamani kupayuka kwa kupaliwa na furaha lakini akajibana sana.

Wakazidi kusonga.

Walipopiga hatua kama tatu tu ndipo Darren akawa amehakiki kile alichokuwa anakiona. Alimwona Melissa! Mwanamke aliyekuwa amemsahau. Alimwona Melissa, mwanamke mwenye kubebelea kitanzi mkononi mwake!

Akabaki akiduwaa, ameachama mdomo na kung’aza macho yake. Na pasipo kutarajia, Melissa akarusha macho kumtazama pale alipokuwapo. Macho kwa macho wakakutana.

“Melissa!” Darren akatamka akitikisa kichwa chake. “Niache Melissa!” akanong’oneza. “Niache Melissa!” kisha akajikusanya na kukimbia sana. Aliliendea gari lake na kuzama ndani akitupia barakoa yake pembeni.

Hakuamini alichotoka kuona. Ni kweli amemwona Melissa! Moyo wake ulimwenda mbio mno. Akahema sana akitokwa na jasho. Akataka kuwasha gari aende lakini mikono ikamtetemeka sana. Akaona ni kheri angoje kwani anaweza pata ajali akilazimisha kwenda.

Kule fukweni Roby akangoja sana. Akatazama kushoto na kulia akiwa anaishiwa na uvumilivu. Darren yuko wapi?

“Mpenzi,” Melissa akaita na kuuliza, “Kuna tatizo?”

“Hapana. Hamna ta--” Roby akateta akitupa macho. “Hamna tatizo!”

Basi baada ya kukaa sana hapo pasipo kuona kitu, akaamua kuondoka zake na mpenzi wake. Moyoni akabeba kinyongo kikubwa juu ya Darren. Akabeba pia na maswali, kwanini Darren amemfanyia hivyo? Kama kungalikuwa na tatizo si angemwambia mapema?

Moyo wake ukawa mzito. Akaghafirika sana.

Walipoenendea mahali ambapo Roby alipakia gari, Melissa akazama ndani lakini Roby akang’aza tena macho kama atamwona Darren. Bahati upande wake wa kulia, kwa mbali, akaona gari la Darren! Basi akalijongea upesi akimwambia Melissa amngojee kwa dakika chache.

Alipolifikia gari hilo, kwa ndani akamwona Darren, basi akaanza kufoka kabla hajafika, “Mambo gani hayo Darren unanifanyia? Ikama ungalikuwa hautaki si ungelinambia?”

Akachngulia dirishani kumtazama Darren. Akamwona akiwa amefumba macho kama mtu aliyemezwa na usingizi. Lakini matundu ya pua yake yakiwa yanachuruza damu kwa wingi!

Akatahamaki! “Darren!” akaita akifungua mlango upesi. Akamtikisa Darren kwanguvu akimwita lakini Darren hakuitikia kabisa. Zaidi damu zikarukia mpaka kwenye mikono ya Roby. Basi upesi Roby akamhamishia Darren kwenye kiti cha abiria na kisha akawasha gari kumwahisha Darren hospitalini upesi awezavyo!

Akiwa njiani, Darren akanong’ona kwa mbali, “Ni jini … Roby, Roby, ni jini … atakuua … ata--”

“Nini unasema Darren?” Roby akapaza sauti kuuliza, akitamani kumtazama Darren, akitamani kutazama barabara. Lakini Darren hakuweza kuongea tena. Macho yakajawa na ukungu na mwishowe akapotelea kabisa gizani.

“Roby …”

***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? ----12*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akiwa njiani, Darren akanong’ona kwa mbali, “Ni jini … Roby, Roby, ni jini … atakuua … ata--”

“Nini unasema Darren?” Roby akapaza sauti kuuliza, akitamani kumtazama Darren, akitamani kutazama barabara. Lakini Darren hakuweza kuongea tena. Macho yakajawa na ukungu na mwishowe akapotelea kabisa gizani.

“Roby …”

ENDELEA


Walipofika hospitali, Darren akatwaliwa na upesi akapewa msaada wa haraka kabla hajalazwa kupumzika. Roby akampigia simu mke wa Darren kumtaarifu na basi muda si mrefu mwanamke huyo akiambatana na mwanaye wakafika eneo la tukio.

Mwanamke huyo alikuwa amejawa na woga sana. Alipomwona mume wake chozi likamtoka akistaajabu ni nini kitakuwa kimemkumba.

“Sijui!” alisema Roby. “Nilimkuta akiwa ndani ya gari anachuruza damu!”

Basi wakaketi kungoja taarifa ya daktari. Muda kidogo Daktari akaja na kuwatoa hofu kuwa mgonjwa anaendelea vema, na kama hali yake ikitengemaa basi anaweza pia kuondoka ndani ya siku hiyo.

“Hatujaona kingine isipokuwa maumivu makali ya kichwa ambayo husababishwa sana na fatigue na msongo wa mawazo. Kila kitu kitakuwa sawa. Msijali,” alisema Daktari kabla hajaondoka zake.

Roby akawasiliana na Melissa na kumwelekeza ajiondokee atamkuta nyumbani kwani amepata udhuru. Melissa akastaajabu. Akamuuliza Roby ni wapi yupo naye aje kumwona.

“Hapana, Melissa. Hamna haja hiyo. We nenda nami nitakuja na kukueleza kila kitu. Sawa?” Melissa akakubali japo kwa shingo upande.

Roby akakaa hapo na Josephine mpaka majira ya jioni kuelekea usiku. Daktari alikuja na kuwaambia hali ya mgonjwa bado haijakaa sawa kiasi cha kumruhusu. Pengine kwa kesho mambo yatakuwa sawa.

Basi kwa utaratibu ikabidi abakie mtu mmoja na mwingine arejee nyumbani. Josephine akasisitiza yeye abaki, lakini angewezaje na ingali alikuwa na mtoto? Roby akamsihi aende nyumbani na yeye abakie na mgonjwa hapo mpaka jua litakapochomoza tena.

Swala hilo likawa gumu sana kwa Josephine. Aliwaza atalalaje pasipo mumewe? Hakuwahi kufanya vivyo tangu waoane. Lakini zaidi hakuwa anaamini kama mumewe atakuwa salama mbali na mikono yake.

Hakuwa na namna. Ilimpasa tu aende. Basi akaaga lakini akiahidi kuja hapo hospitalini asubuhi na mapema kumwona mumewe.

Alimkumbatia Roby na kumwambia, “Naomba umtazame vema.” macho yake mekundu yalikuwa yanachuruza machozi. Akaaga na kwendaze.

Akiwa anaenda, ndipo Roby akapata wazo la kumpeleka Josephine nyumbani kwake. Akamwita na kumwambia hilo wazo lake lakini Josephine hakuridhia. “Hapana. Baki hapa na Darren. Yeye anakuhitaji kuliko mimi.”

Roby akamsihi sana. Haitachukua muda mrefu kwani atamkimbiza na kurudi ndani ya muda. Asingejisikia vizuri kama angemwacha mwanamke huyo ajiendee mwenyewe. Kishingo upande, Josephine akaridhia. Roby akampakia kwenye gari na kuanza safari ya kuelekea nyumbani.

Wakiwa njiani, Josephine akampa pole Roby kwa yale yote yaliyotokea kwenye siku yake hiyo muhimu. “Ilitakiwa uwe una furaha mua huu. Nahisi hisia zako. Pole, Roby.”

Roby akatabasamu kwa huzuni. “Mambo hubadilika haraka,” akasema akiwa anatazama zake mbele waendapo. “Sikutarajia kama yangekuwa haya. Pengine hii haikuwa siku nzuri.”

“Mpenzi wako amekuelewa lakini?” Jospehine akauliza.

“Yeye hajui kinachoendelea,” Roby akamjibu. “Hakuona kitu. Ni mimi pekee ndiye niliyeshuhudia na kuchukua hatua ya kumkimbiza Darren hospitali!”

“Nashukuru sana Roby.”

“Huna haja ya kunishukuru, Jose. Ni jukumu langu. Darren ni rafiki na mshirika wangu. Kama nisingelifanya hivyo, nani mwingine angelitekeleza?”

Basi wakaendesha mpaka nyumbani kwa Darren, hapo Josephine akashuka na kumshukuru Roby alafu na kumuaga. “Uwe na safari njema. Tutakutana kesho mapema, Roby.”

Roby akatabasamu kuitikia kabla hajawasha gari na kurudi moja kwa moja hospitali. Huko akamkuta bado Darren hajapata ufahamu wa kusema anaweza kuongea. Basi akaketi zake sehemu ya kupumzikia na kutoa simu yake mfukoni kumtumia ujumbe mpenzi wake.

“Hey! Umelala?”

Baada ya muda kidogo ujumbe ukajibiwa, wakawa wanachat.

“Bado. Si umesema nikungoje?”

“Yah! Ila nahofia sitaweza kurudi usiku huu, Melissa.”

“Kwanini? Umeniahidi, Roby.”

“Najua. Ni jambo kubwa sana lilionizuia. Rafiki yangu ameumwa ghafla na kulazwa hospitali, sitaweza kumwacha. Nadhani unaona.”

Kukawa kimya kidogo. Roby akatuma tena ujumbe. “Umelala?”

“Hapana.”

“Umekasirika?”

“Hapana.”

“Usiwe hivyo mpenzi. Sikufanya kwa kudhamiria. Natumai unaelewa.”

“Sawa. Nikutakie usiku mwema, Roby.”

Ujumbe huo ulipoingia kwenye simu ya Roby, mwanaume huyo akatikisa kichwa na kung’ata simu yake kwa mawazo. Alishatambua kuwa Melissa alikuwa amekaraishwa. Basi akawaza kitu cha kufanya, mwishowe akaona ni vema atoke upesi kwenda kumwona Melissa alafu atarejea kwa Darren.

Wazo lake hilo likapitishwa na moyo wake pasipo kushirikisha ubongo. Akatumai akimwona Melissa basi ataweza kusuluhisha mambo. Akaendesha upesi na ndani ya nusu saa akawa yu kwenye makazi ya Melissa. Aligonga mlango na punde mwanamke huyo akamfungulia na kumkaribisha.

“Mbona upo hapa? Haukusema upo hospitali?” Melissa akauliza akiketi kitandani.

“Ndio, nilikuwepo huko,” Roby akajibu na kuongezea, “Niliona nije kukuona kwanza alafu nitarejea huko.”

Melissa akamtazama Roby kabla hajamwambia kwa ufupi, “Pole.”

Basi Roby akambembeleza mpenzi wake huyo na kumsihi awe na furaha kwani anataka awe hivyo kila atakapokuwa na yeye, lakini Melissa akasisitizia kutaka kujua wapi ambapo Roby alimpeleka rafiki yake, naye Roby pasipo kusita, akamjuza.

“ … Amelazwa huko. Nadhani kesho ataruhusiwa.”

Melissa alipojua alichokitaka, akaanza kumrembulia Roby akisaula nguo zake. Akamshawishi Roby alale naye kwani alikuwa ana hamu, naye Roby akashindwa kujizuiza, akalala na Melissa.

Punde tu walipomaliza kufanya tendo hilo, Roby akapitiwa na usingizi mzito sana. Alijikuta akiwa hajielewi. Mwili ulikuwa mzito mno. Hajiwezi.

Basi Melissa akatabasamu kabla hajajitoa kitandani na kujivesha nguoze. Alafu akauendea mlango na kuufungua atoke nje.


**

Kwa mbali alisikia sauti za watu wakiteta, akageuza shingo yake kutazama huko sauti zinapotokea lakini hakuwa amefungua macho.

Darren alikuwa anajihisi mchovu sana. Mwili wake umekuwa mzito na mpungufu wa nguvu. Kabla hajafungua macho akajiuliza kchwani mwake nini kilimtokea. Anajua yu hospitali lakini hakuwa anafahamu alifikaje hapo.

Akiwa anajaribu kukumbuka hilo, akajikuta akijiwa na jina la Melissa kichwani mwake! Akaukunja uso wake na kunong’ona, “Melissa … Melissa …”

Basi akafungua macho taratibu sasa aangaze kule ambapo sauti inatokea. Ilikuwa ni dirishani. Alipotazama huko akamwona Melissa akiwa amesimama kando. Mkono wake ameuweka kwenye kioo cha dirisha na macho yake yanamtazama!

Kinywani akahisi Melissa akiita, “Darren … Darren …” alafu mwanamke huyo akatabasamu na kupunga mkono wake.


***

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom