Riwaya: Una nini Melissa?

Riwaya: Una nini Melissa?

*UNA NINI LAKINI MELISSA? – 03*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Basi Melissa akajivalia nguoze na kisha akaelekea stoo. Huko akateka chepe na kutoka ndani ya nyumba kisha akaelekea moja kwa moja kule mashariki ya mbali kukuta kaburi la Cecilia Goodwin, bibi yake Darren.

Hapo kabla hajafanya chochote akaita kwa kunong’oneza, “Tabitha!”

Kisha akaanza kuchimba kaburi.

ENDELEA

Akafukua kwanguvu ya ajabu. Alipumzika takribani mara mbili kwenye zoezi lake hilo kabla hajalimalizia kabisa. Akakuta jeneza kubwa ambalo alilitengua na chepe lake kisha akaliweka wazi.

Humo ndani yake akaukuta mwili wa Cecilia. Ulikuwa unaelekea kuharibika sasa, mikono yake imejifumbata kifuani. Akaukunjua na kisha akauketisha kitako na kusemezana nao!

Namna gani mtu aongea na wafu?

Melissa aliupiga mwili ule kofi dogo kisha akaita, “Tabitha! Tabitha! Tabitha!” mara tatu, na mara mwili ukafungua macho. Macho yaliyokuwa na rangi nyekundu kana kwamba uji wa volkani!

“Tabitha …” Melissa akasema kwa kunong’ona. “Kwanini lakini?” kisha akauliza.

“Kwanini lakini?” Akarudia tena. Saa hii macho yake yakiwa yanalenga machozi. “Nilidhani wewe utakuwa wa tofauti, Cecilia. Nilikuwa nimekosea kukuamini hivyo?”

Mwili ule ambao umefungua macho haukunena kitu. Uliendelea kumtazama Melissa ambaye alikuwa akiutazama na kuuliza kwa tija. Mwishowe Melissa alipomaliza kusema aliyokuwa anahitaji, akaurudisha mwili huo ndani ya jeneza lake, lakini kabla hajaufungia, mwili huo ukamshika mkono kwanguvu!

Ukafungua kinywa kutaka kusema jambo lakini mdomoni ukaishia kutoka upepo tu. Hakuna lililosikika. Melissa akiwa analia, akautazama. Napo asiseme tena kitu, akaenda zake. Na pasipo kurudishia kifusi alichokichotea nje, akaenda zake kumkuta Darren ndani ya nyumba.

Akanyookea bafuni na kukoga kisha akarejea sebuleni ambapo bado Darren alikuwa amejilaza. Akaketi pembeni yake alafu akalaza kichwa chake kochini akiwaza sana. Alishindwa kujizuia kutoa machozi. Kila alipoyafuta yakamiminika zaidi na zaidi. Mwisho wa siku akayaacha yamiminike kama mto.

Yakamwagikia Darren na kumwamsha. Darren akamtazama kwa kuduwaa. “Melissa, haujalala?”

Melissa hakujibu. Aliendelea kumwaga machozi. Basi Darren kwa kuguswa na moyo wa huruma, akamfariji mpenzi wake akitaka kujua ni nini kinamliza. Lakini Melissa hakuwa tayari kunena. Na kadiri Darren alipokuwa anamuuliza, akawa anapandwa na hasira.

Hatimaye alimkaba Darren na kumnyanyua juu kama sufi! Darren akapapatika akirusharusha miguu. Melissa akambamizia ukutani na kusema akiwa amefuma uso wake kwa hasira, “Nitakuua, Darren!” akarudia tena, “Nitakuua, Darren!”

Darren akatoa macho akikosa hewa. Akiwa anaelekea kujikatia roho, Melissa akambamizia kichwa ukutani, mwanaume huyo akazirai! Akamwacha aangukie chini na kisha yeye akarejea pale kitini. Akakaa hapo akiendelea kuwaza.

Akiendelea kumwaga machozi.

**

Ngo! Ngo! Ngo! Ngo! Darren alisikia sauti hiyo kwa mbali. Kichwa kilikuwa kinamuuma na bado hakuwa amefumbua macho. Macho yalikuwa mazito sana lakini akajitahidi kupandisha kope.


Alipotazama akajiona yupo sebuleni, na zaidi akiwa ameegemea ukuta. Kiuno chamuuma na pia kichwa. Kiuno ni kwasababu ya kukaa muda mrefu.

Akastaajabu akiangazaangaza. Hodi ikabishwa tena. Basi akasimama na kusonga mlangoni, hapo akakutana na mzee mmoja aliyevalia kofia ya ‘cowboy’ na overall ya jeans, mkononi amebebelea reki.

Mzee huyo mwenye sauti kavu, akasema, “Wewe kijana, ni wewe ndiye umefukua kaburi kule?”

Darren akatahamaki mzee huyo akimweleza kuwa kaburi lipo wazi. Pasipo kupoteza muda, wakaongozana mpaka huko na Darren akakuta kweli kaburi li wazi mpaka jenezani!

Akazama ndani ya shimo na kutazama jeneza. Lilikuwa limetenguliwa. Akahofia pengine itakuwa kuna vitu vimeibwa humo ndani. Basi akalifungua jeneza na kutazama mwili. Ulikuwa sawia ila macho yakiwa wazi. Akatahamaki.


Ni nini kinatokea hapa?

“Kijana ni nini kinaendelea?” akauliza yule mzee aliyekuja kumshtua Darren. Naue Darren hakuwa na jibu kwani hakuwa anajua lolote lile. Basi kwa kushirikiana na yule mzee wakafukia tena lile kaburi na alivyoenda kule ndani akampasha habari hizo Melissa. Melissa akaigiza kushtushwa.

“Inawezekanaje?”

“Sijui. Ni ajabu! Nadhani mahali hapa hapatakuwa salama tukienda. Napata mashaka sasa,” alisema Darren akiketi kitini. Akafikiria kwa muda kidogo kabla Melissa hajamkalia mapajani na kumtazama kimahaba.


“Unaonaje tukaendelea kukaa hapa kwa muda mpenzi?”

“Melissa, wewe ni mzima kweli? Vipi kazini?”

Melissa akaguna. “Kwani kazini kwenu hamna kuumwa?”

“Sijatoa taarifa hiyo!”

“Kwani hamna wanaoumwa ghafla, Darren?” Melissa akanong’oneza. Darren akasisimkwa na mwili. “Lakini Melissa …”

“Lakini kitu gani mpenzi?” Melissa akauliza akikata kiuno chake kwa mbali.

“Ni hatari!” Darren akashukiwa.

“Hatari lakini salama,” Melissa akamwambia kwa sauti laini kisha akambusu mdomoni. “Nataka kukaa na wewe zaidi Darren. Hamna mahali nitakapokuwa huru na wewe kama hapa. Hutaki hilo, mpenzi?”

“Unajua nataka lakini mazingira mpenzi yana--”

Melissa akakamata mdomo wa Darren na kuunyonya. Alishajua amefanikiwa kumteka mwanaume huyo, hatakiwi kuongea zaidi. Akamchezea mpaka alipoona yeye kuwa inatosha sasa.

Lakini baadae, ikiwa ni kwenye majira ya saa saba usiku, Darren anashtuka kitandani na kujikuta yu peke yake. Anatazama kushoto na kulia pasipo kumwona mtu aletoka kulala naye. Anastaajabu! Anapatwa na hofu.

Akatoka kitandani na kuangaza sebuleni, hamna mtu. Akaangaza chumba cha kwanza, napo hakuambulia jambo. Ila akiwa humo anasikia sauti ya kitu kikigongwa kwa taratibu … Tih! Tih! Tih!

Anafuatisha masikio yake ajue wapi sauti hiyo inatokea, mwishowe anajikuta ndani ya chumba cha tatu. Ila anapofika humo, sauti hiyo hukata. Anatazama kila kona ya chumba hiko pasipo kuona lolote la kutia shaka.

Hatambui nini kinaendelea.

Anajaribu kuita kwa taratibu, “Melissa!” na mara umeme unazima anakuwa kizani. Inachukua kama sekunde mbili tu, umeme unarudi! Darren anapotazama mlangoni, anauona mlango ukiwa wazi, unacheza kwenda mbele na nyuma!

Moyo wake ukapiga kwa hofu. Akapiga moyo konde na kuufuata, kisha akachungulia huko nje. Hakuona jambo nyuma yake, lakini mbele yake, alipotazama vema, akaona kutakuwa na mtu huko. Kule sebuleni kulikuwa na mwanga aliouhisi ni wa runinga. Lakini kama hiyo haitoshi, aliona pia na kivuli cha mtu!

Akaita, “Melissa!” na kuuliza, “ni wewe?”

Ajabu kile kivuli kikaanza kucheza kikizungusha kichwa chake kushoto na kulia, kulia na kushoto kana kwamba mwehu!

“Melissa!” Darren akaita tena. Saa hii sauti yake ilikuwa inatikisika. Alikuwa amejawa na mashaka zaidi. Mashaka juu ya Melissa. Mashaka juu ya roho yake!

Basi hakuwa na namna. Alijivika uanaume akasonga mbele japo kwa hatua za kusita. Alipojivuta mpaka sebuleni na kuchungulia, hakuona kitu! Alipotazama kile kivuli ndipo akajua kinatokea kwenye mwanga wa nje, mwanga upenyao dirishani!

Akatazama huko dirishani, akamwona mtu ambaye kabla hajamtambua, upesi akatoka mwangani na kujificha!

“Ni nani wewe?” Darren akauliza akijitahidi kukaza sauti. “Ni nani wewe, jitokeze kabla sijakufyatulia risasi!” akatishia lakini isisaidie kitu. Hakuna mtu aliyejitokeza wala kunena na yeye.

Basi akaenda stoo upesi na kuchukua fyekeo. Akiwa amelishika vema mkononi, akafungua mlango na kwenda nje. Akaita, “Melissa!” kimya. “Melissa!” kimya.

Akaizunguka nyumba nzima lakini hakuona kitu. Akiwa amerudi pale pale dirishani, akaona kivuli tena, mara hii kikiwa kinatokea ndani na si nje kama ilivyokuwa hapo awali! Kivuli hicho kikiwa ni matokeo ya kuhakisiwa kwa mwanga wa runinga.

Basi haraka Darren akatazama ndani, lakini napo akiwa bado hajamwona mtu huyo vema, akapotelea koridoni!

Basi upesi akakimbilia ndani. Akatazama kushoto na kulia, hakumwona mtu. Akatazama koridoni, napo hakumwona mtu. Akahisi mtu huyo atakuwa ameenda vyumbani, basi akaanza kusonga kwenda huko. Chumba cha kwanza akafungua na kutupa macho. Hamna mtu!

Chumba cha pili aliposhika mlango tu, runinga ikazimwa sebuleni! Alirusha macho yake akaona ni kiza huko. Moyo wake ukaruka pigo. Akahisi sasa anapoteza nguvu mwilini.

Hajakaa vema, akahisi uzito machoni, mara kidogo akapotezaa fahamu akidondoka kama furushi!

Alipokuja kupata fahamu, kwa mbali, akajiona yu ndani ya shimo. Na kwa juu kuna mtu mwenye chepeo akimwagia mchanga humo shimoni! Akimwaga kifusi kwa kifusi!

**

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*UNA NINI LAKINI MELISSA? -- 04*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Hajakaa vema, akahisi uzito machoni, mara kidogo akapotezaa fahamu akidondoka kama furushi!
Alipokuja kupata fahamu, kwa mbali, akajiona yu ndani ya shimo. Na kwa juu kuna mtu mwenye chepeo akimwagia mchanga humo shimoni! Akimwaga kifusi kwa kifusi!
ENDELEA
Akapiga kelele kali akisimama na kujipangusa michanga, akitema michanga. Alipotazama kule juu amwone ni nani anamwagia michanga hiyo amfukie kaburini, hakumwona!
Hakukuwa na mtu tena. Akapagawa. Akachanganyikiwa akijitahidi kujinasua shimoni. Alipotoka, akiwa ametota haswa, akaangaza macho yake kushoto na kulia akihema kwanguvu.
Na punde asikae hapo sana, akakimbia kwenda kule kwenye jengo, kabla hajafika akasikia sauti ya kike inamwita, "Darreeeen!" Alipogeuka kutazama akamwona Melissa kwa mbali. Melissa akiwa amevalia gauni jeupe lionyeshalo kwa ndani.
Na gauni hilo likiwa limechafuliwa kwa mabaki ya damu.
"Melissaa!" Darren akaita. Aliachama mdomo wake kwa kuduwaa na macho akiyakodoa. "Melissaa!" Akaita tena, mara hii akaanza kukimbia kurudi kule alipotokea, kule alipokuwa anamwona Melissa.
Alipomfikia akamkumbatia kwanguvu na kumuuliza, "Ulikuwa wapi Melissa? ... ulikuwa wapi mpenzi wangu?"
Lakini Melissa hakuwa anaongea kitu. Alimtazama Darren usoni kana kwamba mdoli. Naye Darren akapata shaka, "Melissa, upo sawa?"
Kabla Melissa hajajibu, Darren akasema, "Twende ndani!" Akimvuta Melissa mkono. Ila ajabu mkono wa Melissa ukanyofoka! Akajikuta ameubebelea na huku Melissa akiwa amesimama kama mstimu.
"Nini hiki?" Darren kutahamaki. Mara Melissa akakunja sura na kumtazama Darren kwa hasira. Akapanua mdomo wake kwa upana zaidi kisha akapiga kelele kali mno. Akamsogelea Darren kwa ukaribu na kumzaba kibao kikali, Darren akarukia mbali!
Alipokuja kufumbua macho yake akajikuta yu kitandani. Alikurupuka na kuangaza kando yake, alikuwa mwenyewe! Akaita, "Melissa?" Kimya. Akanyanyuka toka kitandani na kutazama koridoni. Hakukuwa na mtu. Akaita tena na tena, mara akasikia sauti ya mtu akigugumia kwa kilio huko sebuleni.
Akasonga huko na kuangaza. Kitini akamwona Melissa wake akiwa amejikunyata. Melissa analia.
"Melissa!" Akaita kwa sauti ya chini akisonga. "Melissa, kwanini unalia?"
Akaketi karibu ya mwanamke huyo. Akauweka mkono wake begani mwake na kumuuliza, "Melissa, kwanini unalia, mpenzi? ... hautaki kuwapo hapa? Wataka tuondoke?"
Melissa hakusema kitu. Akaendelea kulia. Naye Darren akaacha kumuuliza maswali na badala yake akawa anambembeleza tu anyamaze. Aliponyamaza akamkumbatia Darren kwanguvu na kumwambia, "nisamehe mpenzi?"
Darren hakumuuliza kisa nini. Aliona Melissa hayuko sawa na hakutaka yawe magumu zaidi. Atamuuliza baadae yote yakipoa na kuwa sawa. Akambusu mpenzi wake kwenye paji la uso na kisha akamkumbatia tena.

***

"Kweli!" Mama yake Darren, Sarah, alisema kwa mshangao. Alikuwa amekurupuka toka usingizini muda mfupi hapo nyuma, kando yake akiwa ameketi mume. Wote walikuwa na nyuso za kuhemkwa.
"Kwahiyo?" Baba akauliza. "Tunafanyaje sasa?"
"Twende!" Mama akaropoka. "Twende, Gerald!"
"Wapi?" Baba akatahamaki. "Unajua saa hizi ni muda gani, Sarah? Ni saa nane ya usiku!"
Mama akatazama kushoto na kulia kwake kisha akameza mate. Alifungua dirisha akatazama nje. Alikuwa amechanganyikiwa.
"Gerald!" Akaita. "Kama tusipofanya namna Darren anaweza akafa." Alipoteta hayo macho yake yakawa mekundu ghafla na kumwaga chozi.
"Usijali, Sarah. Hamna kitakachotokea mpenzi. Ni ndoto tu. Atakuwa salama," alisema Gerald.
Mama akainamisha kichwa akiendelea kulia. "Sijawahi ota ndoto kama hii kwa muda mrefu, Gerald. Nadhani kuna haja ya kwenda Reish jua litakapochomoza."
"Kufanya nini huko?" Gerald akang'aka. Sarah akamtazama akikunja ndita. "Una wazimu, Gerald? Unadhani ni sawa, sio? Huoni hali yangu ya mwanzoni itakuwa inaninyemelea?"
Gerald akashusha pumzi ndefu kisha akajirejesha kitandani. Sarah akamtazama pasipo kutia neno kisha akaendelea kuwaza zake na kidogo Gerald, mumewe, akamsihi alale na jua litakapokucha atafanya vile ambavyo anataka.
Basi akajilaza kitandani. Lakini hakufumba macho bali akiwandawanda huku na kule. Hata mumewe akapotelea usingizini na huku yeye bado anatazama kushoto na kulia. Hakuwa na usingizi. Alimwazia mwanaye vibaya. Alimwazia hayuko salama.
Akajigeuza huku na huko na hatimaye jua likachomoza. Akaamka na kuanza kujiandaa. Mumewe akamkuta akiwa tayari.
"Ulilala kweli, Sarah?"
Sarah akatikisa kichwa kuafiki lakini mumewe akatambua wazi kuwa mwanamke huyo hakulala. Macho yake yalikuwa mekundu yaliyochoka
Akajiandaa ndani ya muda mfupi na wakafunga safari na mkewe kwenda mahali huko, mbali kabisa katika jangwa la misitu.
Mahali huko palikuwa panaitwa Reish.
Walipozama ndani ya msitu huo wakanyookea mti mkubwa, Sarah akazamia humo ndani akimwacha Gerald hapo nje.

**

"Nadhani utakuwa sawa, si ndio?" Darren alinena punde alipomshusha Melissa nje ya makazi yake tokea kwenye taksi.
"Yah! Nitakuwa sawa," Melissa akajibu. Uso wake ulikuwa mpole. Alitabasamu kwa kuigiza alafu akaanza safari yake ya kwenda ndani. Darren akabaki hapo akimtazama mwanamke huyo akiishilia. Ila kidogo simu yake ikamtoa mawazoni na kumfanya aitazame. Alikuwa ni mama yake. Akaipokea na kuiweka sikioni.
Kabla hajaongea hata neno, Melissa aliyekuwa amekaribia na mlango wake akasimama. Alihisi jambo. Akageuza uso wake kumtazama Darren lakini Darren hakutuama tena pale, dereva taksi akatia moto chombo na kuyeya!
Melissa akalitazama gari hilo mpaka lilipopotea kabisa alafu akazama ndani moja kwa moja mpaka chumbani kwake. Akajitupia kitandani akiwaza mambo kadhaa, na mara kwa mara akawa anasema mwenyewe, "Tabitha! Tabitha!"
Baadae akatoa picha ya bibi yake Darren kwenye mfuko wake na kuiweka mezani.
Akaitazama picha hiyo kwa muda alafu akafunga madirisha ya chumba chake na kuwasha mishumaa. Baada ya hapo, toka uvunguni mwa kitanda chake akatoa majani makavu yaliyotunzwa ndani ya kisosi, akayatia moto na kuyafukizia ndani akinuwia. Alipomaliza akaichora picha ile ya bibi yake Darren akinena maneno ya kilatini. Punde mtu mmoja mmoja ndani ya picha akaanza kupotea na hatimaye akabakia bibi peke yake wengine wote wakiwa hawaonekani!
Watu hao waliopotelea pichani, katika namna ya ajabu, wakajiri kandokando ya mlango! Ila nyuso zao hazikuwa tena za mabinti wachanga kama vile ilivyoonekana, bali za wazee waliokongoroka. Na hapo, kufumba na kufumbua, naye Melissa akawa mzee kama wao! Wakakumbatiana kwanguvu kabla Melissa hajawaambia kwa uchungu, "Tabitha alitusaliti! ... Tabitha aligeukia binadamu!"
Ndipo akawaeleza ya kwamba nyumba yao ya kale, nyumba ya majini, ipo hai tofauti kabisa na vile Tabitha alivyokuwa anawaambia ya kuwa imepotea. Imemezwa!
Habari hizo zikawashangaza wale wazee. Wakataka kuiona nyumba hiyo lakini haikuwa inawezekana katika miili yao kwani Tabitha aliipoteza kabisa. Basi wakamsihi Melissa airudishe nyumba ile kwenye mikono yao haraka iwezekanavyo. Lakini pia awamalize binadamu hao mara moja. Binadamu wanaoishi hapo, na wale watakaokuja kukaa hapo.
Kwa kufanya hivyo atawarudisha wenzake tena duniani. Na watatawala tena kama ilivyokuwa kabla ya Tabitha kuwatia kifungoni na Melissa kutorokea mbali!
**
"Darren, picha iko wapi?" Kabla hata ya salamu mama akauliza. Alikuwa ametoa macho haswa kiasi cha kumwogopesha Darren.
"Picha gani?" Darren akauliza. Mama akamkaba koo na kupaza, "Picha ya bibi yako! Ile picha ya bibi yako iko wapi?"
Basi Darren akatazama kwenye mkoba wake. Hakuiona. Akahisi kuchanganyikiwa. "Ilikuwa humu ... ilikuwa humu!"
"Iko wapi sasa?" Mama akafoka kiasi cha kumshangaza Darren. "Mama kuna nini kwani?"
"Nataka picha!" Mama akasema kwa sauti ya chini ya msisitizo. "Nataka picha, Darren. Picha!"
"Haipo humu. Nadhaniii..."
"Unadhani nini? Nani kaichukua?" Mama akauliza akitoa macho. Darren akajibu, "Melissa. Nadhani kaichukua Melissa!" Basi upesi Mama akamdaka mkono na kumwambia, "twende huko upesi!"

***

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom