Riwaya: Salamu kutoka kuzimu

Riwaya: Salamu kutoka kuzimu

Status
Not open for further replies.
Mnavunja sheria kama hamna ruksa ya kuandika hadithi hizi hapa ni hatari kwa ustawi wa fasihi jamani tujifunze kununua vitabu
 
Mnavunja sheria kama hamna ruksa ya kuandika hadithi hizi hapa ni hatari kwa ustawi wa fasihi jamani tujifunze kununua vitabu

Kuna tofauti gani na kuangalia Muvi kwenye Dar Express au Machame Express? We Kama unacho kitabu tusaidie kuisogeza simulizi hili. Kwani Ben Mtobwa alisema ni lazima kununua kitabu?
 
utamu wa riwaya ndo umenoga sana,ila ndo mwendo wa kobe,tuvumilie tu! ntamaholo barige ;nyakasagani.blogspot
 
Last edited by a moderator:
Unaweza pitia google scholar huko utapata kusoma baadhi ya chapter za kitabu hiki
 
[h=3]SALAMU KUTOKA KUZIMU
[/h]SURA YA TATU IV


"Anakuja! Na atakufa!" Proper alimwambia Waridi.


"Ondoa hiyo mikunjo ya hofu usoni uvae suruali yako nzuri kama ilivyo. Akifika mpe tabasamu, mpe mapenzi, kisha mkaribibishe pombe. Usisahau chupa hilo hapo ni kwa ajii yake, akionja tu yamekwisha, asipoinywa mpake hii kwa hila".


Walikuwa katika chumba fulani, ghorofa fulani, katika jumba hili la light ambalo liko katika mtaa wa Lumumba, jijini Dar es Salaam. Proper alikodi chumba hiki kwa ajili ya kazi hii tangu jana alipomtoa Waridi kule hospitali. Usiku mzima aliutmia kumtisha Waridi kwa kila namna pale alipojaribu kuleta ubishi. Kisha alikuwa amemlazimisha kufanya naye mapenzi kwa njia zake za kinyama. Ilipofika alfajiri ndipo wakaanza kupanga mikakati ya mauaji.


Waridi alivishwa vazi jeupe la hariri, vazi hili lilifichua kila kitu kilichofaa kifichwa katika mwili wake. Kila jicho liliweza kuona mwili mzuri wa msichana huyo, ulikuwa ukimelelemeta kwa wekundu ndani ya mavazi hayo. Uso wake pia ulikuwa "kioo" kwa uzuri wake wa asili ulioshinikizwa kwa vipodozi murua vilivyotumiwa kistaarabu. Nywele zake zilitengenezwa kwa ile mitindo ya kisasa. Kwa kila hali, msichana huyu alionekana mtu tofauti kabisa na yule binti ambaye usiku wa jana tu alilala chini pale baa akiwa nusu uchi, akilia. Huyu alikuwa katika hali ambayo ilikusudiwa na ilitosha kuushinda ukaidi wa Joram Kiango dhidi ya wasichana warembo.


"Uwe msichana hodari. Ni kazi ndogo tu. Baada ya hapo utakuwa huru. Nitakulipa pesa za kutosha ukanisubiri Nairobi. Kutoka hapo tutakwenda zetu London au New York, tukatumie. Unasemaje?".


Waridi hakujibu.


"Mbona husemi neno?" Proper alimwuliza Waridi. "Hofu ya nini? Hii ni kazi ndogo mno kuliko ile uliyoifanya kwa Bomba. Na bado itakulipa pesa nyingi zaidi ya ule uchafu uliochukua. Jitie furaha na ucheke kidogo".


Kikcheko kilikuwa mbali na Waridi. Aliendelea kuduaa kama mzoga akisubiri lolote aliloelekezwa kulifanya. Hilo likamchukiza sana Proper.


Akasema. "Sikia wewe, endapo utavuruga tena mpango huu, sitasita kukuua papa hapa. Sasa hivi bado dakika ishirini Joram ataingia hapa. Nitakuwa chumba cha pili nikiangalia kila kitu. Ukishindwa au kuvuruga mpango huu nitakuua wewe na huyo Joram papa hapa. Nitakuua wewe kwanza na kisha Joram kwa hili hapa", akatoa bastola ndogo kutoka kwenye mfuko wa koti lake.


"Sipendi kukuua", Proper aliongeza. "Lakini ukinilazimisha nitaitumia kuwaua". Akaitazama tena saa yake. "JOram anaweza kuwa anakuja sasa. Natoka. Kumbuka kuwa niko karibu na tayari kukuua endapo utavuruga mpango huu. Sawa? Proper alitoka na kumwacha Waridi ameduwaa kama alivyokuwa.



Baada ya dakika kadhaa mlango wa chumba hiki uligogwa, kisha ukafunguliwa. Joram Kiango alichungulia ndani na kisha kuingia polepole macho yake yakiwa yamepumbazwa na uzuri wa Waridi. Hakutegemea.


"Sisiter... mimi ni mgeni wako nadhani. Naitwa Joram Kiango", alieleza Joram huku akiandaa tabasamu ambalo alijua linamfaa binti mzuri kama huyu.


Ndipo Waridi alipogeuka kumtazama.



ITAENDELEA 0784296253

cc.
Wakuu wangu Kirchhoff, LEGE, Kapo Jr, maph, Nyamajeje, Deo Corleone, kidi kudi, PEZE, DavidHard, Amorbwoy, Bujibuji, barige, peterchoka, kidi kudi, Willy Gamba 1
 
[h=3]SALAMU KUTOKA KUZIMU
[/h]SURA YA NNE


Kama kuna wanawake ambao husimbua mioyo ya wanaume mara tu watokeapo mbele yao hata wanaume hao wakajisahau na kuzisahau shughuli zao, basi ni dhahiri pia wapo wanaume ambao huisumbua mioyo ya wanawake kwa kiwango kile kile. Na kama kweli wapo, miongoni mwao yumo Joram Kiango. Hayo yalijidhihirisha baada ya Waridi kumtia machoni Joram alipoingia chumbani.


Moyo wake ulipoteza mapigo kwa sekunde kadhaa. Roho yake ilihisi kupaa nje ya mwili wake. Kadhalika, damu ilimsisimka kiasi cha kumfanya ahisi ganzi mwili mzima. Hivyo, hakuweza kuyaondoa macho yake juu ya umbo la Joram ambaye alimsogelea polepole. Nusura wazimu umpande Waridi alipoona uso na tabasamu la Joram, lililotosha kuwa tiba kwa maradhi yake. Maradhi aliyoamini kuwa hayangeweza kutibika.


Kwa bahati mbaya, Waridi hakuwahi kupenda mwanaume katika maisha yake. Hivyo hakujua mapenzi ni nini. Hakuwahi kuyaonja. Kama angejua, angefahamu nini kitatokea. Badala yake alihisi maumivu moyoni na huzuni kubwa akilini mwake. Akanusurika kutokwa na machozi. Hakujua nini kinamtokea. Isipokuwa kitu kimoja tu alikifahamu, Joram hakuwa mtu wa kufa, Hakuona sababu ya kumwua, Asingeweza...


Tazama alivyosimama mbele yake kwa upendo na utulivu kama malaika asiye na hatia. Tazama anavyochekelea kwa furaha kama nuru, Mtazame. La, huyu kijana si mtu wa kufa. Waridi akawa ameamua hivyo.


"Nadhani mimi ni mgeni wako, mpenzi, Joram alisema tena, akinyoosha mkono wake kumgusa Waridi kwenye bega lake la kuume.


Joram alikuwa ameshangazwa na uzuri wa msicha huyu. Vipi wengine waumbwe kwa upendeleo kiasi hiki wakati wengine wasitofautiane sana na vinyago? alijiuliza. Mavazi mazuri ya msichana huyu pia yalimchanganya Joram; yalikuwa mavazi mapya ya thamani kubwa, kisha ya kihuni kama yalivyondaliwa mahususi kwa ajili ya kumtongoza! Hicho hakikumshangaza Joram, Lakini alishangazwa na uso mzuri wa msichana huyu ukiwa katika dimbwi la majonzi, mashaka, hofu na msiba. Hilo halikumshangaza hata kidogo.


"Ndio...ka... karibu kaka", waridi alianza kusema huku akibabaika,


Joram alimvuta mkono na kumwongoza hadi kitandani, ambako alimketisha kisha naye akaketi kando yake huku akiendelea kuushika mkono wa Waridi.


"Nilikwambia kuwa sauti yako ni tamu kama ilivyo sura yako? Naamini sikukosea. Ama kweli umeumbika bibie. Ulimhonga nini muumba hata akakupendelea?"


Sauti ya Joram, tabasamu lake likasindikiza kila neno, hali hiyo ikamfanya Waridi aanze kuchangamka. Akasahau yote yaliyokuwa mbele yake na kujikuta kazama katika maongezi na Joram. Katika kipindi hicho kifupi bila kujifahamu Waridi alijikuta tayari akiwa ameufunua moyo wake wote kwa Joram, akimsimulia matatizo yake yote. Alipotanabahi alikuwa akisema: "Najisikia kutoweka nje ya nchi hii".


"Kwanini?".


Swahili hilo lilimzindia Waridi. Hakujua yapi alikuwa tayari kuyatamka ambayo hayakustahili kuiacha milki ya kinywa chake, Hofu ikamrejea. Akalikumbua jukumu lililokuwa mbele yake: kumfanya kijana huyu kuwa marehemu. Ama ni yeye atajayefanywa marehemu.


Hofu hiyo, ilizidi baada ya Joram kuinuka na kuiendea meza iliyokuwa na chupa mbili za pombe huku akisema: "Bia hii? Unaonaje nikianza kuimimina tumboni mwangu ili kupoza joto la Dar es Salaam kabla hujanieleza sababu za kuniita hapa? Siamini kwama kweli umeniita kwa ajili ya kunishukuru tu, yaani hilo likusukume kunitafuta..."


"Usinywe hiyo pombe", Waridi alifoka.


"Kwanini mpenzi? Nilidhani umeiandaa kwa ajili yangu", Joram alifuatwa na tabasamu la kukata na shoka.


Waridi alikuwa akitetemeka. Lakini asingeweza kusahau maneno ya yule mtu katili Proper alipomwambia: "Nitakuwa chumba cha pili... Ukishindwa tena nitakuua papa hapa..." Waridi hakupenda kufa, lakini pia hakuwa tayari kumuona kijana huyu asiye na hatia, afe. Afanye nini? Kwa kutojua la kufanya akaanza kulia. Mikono ya Joram ilitua tena mabegani kwa Waridi akimfariji na kumkumbatia huku akisema.


"Kama hutaki ninywe hii bia ni wazi kwamba kuna zawadi kubwa na tamu zaidi ya bia uliyoiandaa kwa ajili yangu. Kwa bahati mbaya nina mazoea ya kunywa pombe kabla ya yote. Kwa maana hiyo niruhusu ninywe bia moja tafadhali".


"Usi..." Waridi alijaribu kufoka tena. Joram alimzuia kwa kuuziba mdomo wake kwa kiganja cha mkono wake huku akiweka kinywa chakr karibu na sikio la Waridi, akamnong'oneza.


"Najua kitakachotokea. Sinywi pombe hiyo. Acha nijifanye kama nakunywa ili nimpumbaze huyu anayetaka kuniua. Nitakuomba wewe uwe msiri wangu. Mwache aamini kuwa ameniua. Mwache kila mtu aamini kuwa nimekufa. Nataka kufahamu hawa waliokusudia kuniua jambo gani wanakusudia kutenda".


waridi aliduaa. "Ume... umewezaje kujua? aliuliza kwa kunong'ona.


"Niliwahi kufika eneo hili mapema na kumsikia alivyokuwa akikuamru. Nawe pia lazima ufahamu kuwa uko hatarini. Huyu ni mtu hatari. Mara tuu utakapotoka hapa, toroka uende kokote asikoweza kukufikia. Sasa acha nijifanye nainywa pombe yake". Joram akaongeza sauti kusema. "Glasi? Acha ninywe kihuni".


Joram aliifungua chumpa moja na kuingia nayo msalani ambako aliimimina nusu kwenye tundu la choo, Akarudi na kuitua mezani huku akiendelea kuongea na Warid, mazungumzo yao yalifanyika taratibu kwa sauti ya chini. Mara kadhaa Joram alimshika waridi na kumtomasa hapa na pale kwa ajili ya kumtoa hofu.


"sasa mpenzi sikia", aliongeza. "Ninaye mgeni ambaye atakuja ofisini kwangu baada ya nusu saa kuanzia sasa. Baada ya kumalizana na mgeni huyo, leo kutwa nzima nitakuwa huru. Waonaje niende ofisini mara moja na kurudi sasa hivi? Naamini leo tutashinda pamoja kwa furaha sana. Naamini itakuwa siku njema twetu".


"Sawa", Waridi alijikongoja kujibu.


"Tafadhali nikukute, ukiwa kama ulivyozaliwa. Ikiwezekana, kitandani, sawa?"


"Bila shaka".


Mara tu Joram alipotoweka machoni mwake, Waridi alijikuta akirejewa na hofu. Ile hakika na ushujaa ambao alikuwa ameuhisi kwa kusikia sauti ya Joram na kuyaona macho yake yang'aavyo sasa ilikuwa kama ndoto tu. Ndoto ya kale. Hakujua lipi afanye. Akaendelea kuduwaa kimya, akitazama huku na huku kama aliyetegemea kumwona Zibril akimjia kwa lengo ka kutwa roho yake.


Waridi angetimua mbio Proper alivyoingia ghafla huku akimtazama Waridi kwa macho ya kutisha. Waridi angeweza kukimbia kama ukuta usingekuwa umemtenga na dunia ya nje. Alichofanya ni kurudi nyuma hatua kadhaa hadi alipoegemea ukuta, macho yenye hofu kayatoa kama kondoo aliyekuwa juu ya madhabahu, akisubiri kutolewa kafara.


"Mwanakharamu... malaya mkubwa, mwana wa malaya mkubwa...", Proper alifoka. "Umekosa walau ushujaa wa kunidanganya kuwa hawara yako amekunywa pombe niliyomwandalia? Mara hii umesahau kuwa mmekubaliana naye adai kuwa ameinywa ili asingizie kuwa kafa. Nakusikitikia Bi. mdogo. Namsikitikia pia huyo hawara yako. Hajui afanyalo. Anadhani kuwa anacheza na watoto wadogo kama alivyozowea. Nilikuwa nimemfanyia hisani kubwa ili afe kistaarabu hakutaka. Kajitia ujanja. Sasa atakufa kifo cha kusikitisha zaidi".


Jodor Proper aligeuka kama anataka kutoka. Mara kama aliyekumbuka jambo alimgeukia tena Waridi na kusema. "Nawe malaya mwovu hufai kuishi zaidi. Huna faida duniani wala haki ya kuishi tena. Utamfuata mpenzi wako Bomba akhera. Mpe salamu zangu, mwambie hongera kwa hila zake zisizo na ila". Akageuka na kutoka.


Machozi yalikuwa yamenyauka machoni mwa Waridi. Sasa aliiona dunia kama kitu ambacho kilikuwa kando yake. Naam, maisha yake yalikuwa ukingoni. Asingeweza kutilia mashaka sauti ile ya Proper yenye uhakika. Sauti ambayo masikioni mwake ilikuwa kama saut ya mauti yenyewe.


Kwanini aendelee kusubiri? alijiuliza. Kwanini asubiri kifo cha mateso na kashfa? Akajiuliza kwanini asitangulie? Sasa macho yake yalikuwa yakitambaa kila mahali kutafuta silaha yoyote ambayo ingefaa kumtoa roho. Mara macho ya waridi yakatua kwenye ile chupa yenye pombe yenye sumu iliyoandaliwa kwa ajili ya Joram, bila kufikiri kwa mara ya pili aliiendea ile chupa yenye pombe akajimiminia tumboni mwake.


Mara Waridi akapata faraja kubwa ambayo ilimfanya asahau hofu na kudharau vitisho vyote vilivyokuwa mbele yake. Alijiona yu njiani hatua chache tu kufika katika milki mpya. Milki ambayo itampa uhuru kamili.


Furaha hiyo ikamuongoza Waridi, alitoka ndani ya chumba hicho na kuiendea lifti. Akatelemka hadi chini. Aliiacha hoteli na kuanza safari ya kuelekea kituo cha mabasi. Mavazi yake yakiwa kama yalivyokuwa, umbo lake likiwa kama lilivyo, na sura yake nzuri ikiwa imepambwa na tabasamu, viliyafanya macho ya wanaume kumtazama kwa mshangao wenye tamaa. Baadhi waliguna walipomuona, wawili walimkonyeza na mmoja alidiriki hata kumfuata. Wote walipata tuzo kwa tamaa zao. Tuzo ambalo lilikuwa tabasamu pana zaidi ambalo liliwafanya wabaki wameduwaa nyuma yake hoi bin taabani.


Waridi akaendelea na safari yake. Mwendo wake ukiwa nyongeza nyingine ya maneno kwa watazamaji. Akiwa kajaza nyuma, kakatika kati na kunyooka alivyonyokeana, ilikuwa kana kwamba hatembei bali anafanya maonyesho ya miondoko kama wanavyofanya warembo katika mashindano ya miss. Mwenyewe akiwa hana habari hizo, aliendelea na msafara wake hadi alipokifikia kituo na kujiunga na umati wa watu waliokuwa wakisubiri usafiri wa umma.


"Gari hii hapa dada", mtu mmoja alimwambia Waridi. Ilikuwa teksi. Waridi hakufanya hiana, akajitosa ndani ya teksi hiyo huku akisema. "Nipeleke Mburahati",


"Vizuri, lakini waonaje kama tukipitia hapa Embassy Hoteli tukapate walau bia mbili mbili baridi?", dereva alitupa ndoano yake.


"Samahani, leo nina haraka, nitafute siku nyingine".


"Kesho".


"Sawa..." waridi alilaghai. Rohoni akiamini kuwa kesho hatakuwa Dar es Salaam. Hatakuwepo hapa nchini, wala popote Afrika. Atakuwa nje. Nje ya dunia. Aliendelea kuwaza kwa furaha huku akimwitikia dereva huyo, "Ndio", kwa kila dereva huyo alilosema wakati hata hamsikii. Walipofika mbele yavijumba vayo, Waridi alimtaka dereva asimame. "Ni hapa, asante kaka", dereva hakuyaamini masikio yake, "Yaani uaishi hapa. Katika vijumba hivi? Na unaishi hapa dada?", dereva alishawishika kuuliza.


"Hapa ndio kwangu", Waridi alijibu wakati akitelemka kutoka ndani ya gari.


"Hapa?", dereva aliuliza tena kwa mshangao. Hakutia neno lingine. Badala yake aligeuza gari lake na kurudi alikotoka kwa mwendo wa kasi.


Walidi akapokelewa na wenzake waliojawa na mshangao. "Iwe", alisema mmoja wao. "Ulikuwa wapi".


"Na ilitokea nini hata ukaondoka bila kuaga?", alihiji mwingine. Maswali yalikuwa mengi mno. Waridi hakuwa na muda wa kuyajibu yote. Wala hakukumbuka ajibu maswali gani. Alichokumbuka ni jinsi alivyoingia chumbani kwake na kujilaza kitandani akisubiri kifo. Usingizi mzito ukamchukua.


Alipoamka ilikuwa usiku wa saa tatu. Chumba cha pili kitanda cha mwenzake kilikuwa kikilalamika kwa uzito wa viumbe waliokuwa wakikitumia. Naye alikuwa akigongewa mlango. Mteja akainuka na kumwendea. Alikuwa mtu mwenye umbo la mwili wa mtoto na uso wa mzee. Alikuwa na pesa zake mkononi tayari. "Leo sifanyi kazi", Waridi alimwambia mteja huyo na kufunga mlango wake. Hakujali malalamiko ya mteja huyo. Alikuja mwingine. Na mwingine tena. Wote Waridi aliwakatalia. Nao wakaondoka shingo upande.


Halafu akaja huyu mteja ambaye hakukubali kuondoka. Alikuwa kavaa kofia kubwa iliyofunika uso wake na koti kubwa lililofunika hadi miguuni. Aliingia kwa kujlazimisha na kufunga mlango nyuma yake huku akisema, "Lazima".


"Leo sitaki".


"Hata kwa bei kubwa?".


"Hata ukitoa milioni".


Mtu huyo alicheka kidogo. "Mimi wanitaka. Umekuwa ukinisumbua muda wote huu", Alitupa koti lake chini na kubaki katika suruali na shati. Akaivua kofia yake na kuitupa juu ya koti. Ni hapo Waridi alipomtambua. Macho yenye hofu kubwa yakamtoka.


"Bila shaka utakuwa umenikumbuka ", alisema polepole. "Unadhani nilikusudia ufe kistaarabu kwa ile sumu?, Ile ilikuwa maalumu kwa ajili ya Joram Kiango peke yake. Wewe ni mwovu mwenye dhambi nyingi. Unastahili kufa kishenzi".


Kabla Waridi hajafahamu kama ilimpasa kufanya nini, alijikuta tayari kadakwa ghafla kwa mkono kwa mkono wenye nguvu, ambao uliibana mikono yake yote miwili. Haraka kamba zikapita mikononi mwake. Alipotanabahi kupiga kelele, alijikuta katupiwa dude fulani kinywani ambalo lilimziba kinywa. Mara akatupwa chini na kudungwa sindano ambayo ilimlegeza hata asiweze kutapatapa.


Kisha kisu kikali kilichomolewa kutoka ubavuni na kuanza kupita juu ya mwili wake. Maumivu yalikuwa makali ajabu, lakini hakuwa na uwezo wa kulalamika. Alichoweza kufanya ni kuendeleo kukodoa macho yenye dalili zote za hofu na maumivu. Macho hayo yalishuhudia mikono yake ikikatwa mmoja baada ya mwingine na kuwekwa juu ya kitanda. Kisha tumbo la waridi likafumuliwa na utumbo kumiminika katika sinia lililokuwa mezani. Baada ya sekunde kadhaa alikuwa tayari amekata roho pindi kichwa chake kilipokatwa na kuwekwa juu ya debe, kando ya kitanda.


Baada ya kuridhika na kazi yake. Proper alizivua nguo zake zenye damu na kuzifunika katika mifuko ya koti lake ambalo alilivaa na kisha kutoroka zake nje polepole kama wateja wengine. Hapo nje aliwakuta wateja kadhaa ambao walisimama kwa namna ya mstari wakisubiri zamu zao. Akafanya haraka kuiendea sehemu aliyoficha gari yake.


Mteja aliyeingia baada ya Proper aliduwaa kwa kutokumuona Waridi. Kisha alishangaa kuiona mikono ya mwanamke huyo iliyolala peke yake juu ya kitanda. Halafu akakiona kichwa kilicholowa damu, kimelala chali. Hakuyaamini macho yake. Na ilipomtokea kuamini alihisi akili yake ikipaa. Alipiga kelele kwa nguvu na kuanza mbio akielekea barabarani, Alianguuka, akainuka na kuendelea kukimbia.


Mtewa mwingine alichungulia tu na kugeuka akianza safari ya kurudi zake alikotoka kimya kimya.



Ni mteja wa tatu aliyetoa taarifa kwa majirani na wenzake kuhusu kilichomtokea Waridi. Yeye pia alitoweka. Majirani walichanganyikiwa kwa muda mrefu. Mmoja wao alitapika. Wawili wakalia kwa nguvu. Umati mkubwa wa watu ulifika. Polisi pia hawakuchelewa.


ITAENDELEA 0784296253
 
SALAMU KUTOKA KUZIMU
SURA YA NNE II
"Umesema u nani wewe?".
"Naitwa Joram Kiango".
Inspekta Mkwaju Kombora hakuyaamini masikio yake. Jina la Joram Kiango lilikuwa maarufu kichwani mwake kama mbwa anavyoifahamu harufu ya chui. Mzee huyu alimfahamu vyema Joram. Yule kijana machachari aliyefanya mengi dhidi ya wahujumu uchumi na majasusi hatari ambao jeshi la polisi lilielekea kukata tamaa. Yule kijana nadhifu sana, mpole sana, mwenye nguvu na akili. Si huyu mzee aliyesimama mbele yake katika vazi la Kiarabu, akiwa amevaa kanzu nyeupe, kapiga kilemba, mwenye ndevu nyingi, uso uliofunikwa na miwani na mkononi kashika fimbo ambayo ilimsaidia katika mwendo wake wenye dalili zote za udhaifu wa kizee,
"Joram?", Inspekta Kombora akauliza tena.
"Naona huniamini kwa vile hujanifahamu Inspekita", ilisema sauti ambayo Kombora alielekea kuifahamu kwa mbali,lakini sura haikuwa ya Joram.
"Pengine niondoe miwani na haya madevu ya bandia ili uweze kunitambua". Madevu yakatolewa na miwani ikavuliwa, Uso ulisimama mbele yake ukitabasamu, Alikuwa ni Joram Kiango halisi ambaye Inspekta Kombora alimfahamu vyema.
"Nini sasa unafanya Joram?", alishangaa Inspekta Kombora. "Mchezo huu una lengo gani?".
"Siyo mchezo inspekta. Niko kazini. Unionavyo hapa mimi ni marehemu. wapo watu wameniua. Nataka niendelee kuwa marehemu ili...
Inspekta Kombora alimkatisha na kumwekea mkono begani huku akisema, "Sikia Joram. Kama ni mzaha subiri nitakapokuwa huru ndipo utakapoufanya tena mchezo wako, tucheke pamoja. Kwa sasa niko katika mkasa mzito ambao unaweza kuhatarisha usalama wa jiji endapo mtu huyo mwenye roho ya kinyama hatapatikana".
Habari hiyo ikamvutia Joram. "Mtu gani?", Joram alihoji mara moja.
"Hujasikia tu? Nadhani wewe hupitwi na neno".
"Kusikia?".
"Kuhusu msichana huyo aliyeuawa kikatili kuliko ilivyowahi kutokea. Polisi wamefanya kuokota viungo vyake kimoja baada ya kingine ndipo ukapatikana mwili mzima wa marehemu. Mtu aliyefanya mauaji hayo ni mnyama zaidi ya wanyama wengine wa kawaida. Mtu mwenye kumchinja msichana mrembo kama yule".
"Sijakupata Inspekta, yaani..." kisha Joram akapunguza kasi kuhoji kuhusu tukio hilo kwa kituo. Inspekta Kombora akamweleza yote kuhusu tukio zima lilivyotokea usiku huo huko Mburahati.
Hakukuwa na sababun za kuupeleka mwili huo hospitali", Inspekta Kombora aliongeza. "Viongo vyote vya marehemu vimeletwa hapa katika chumba cha maabara. Kama utapenda kutazama vitu vya kutisha unaweza kwenda maabara, inatisha sana".
"Nitapenda kumwona tafadhali".
Inspeta Kombora akaiacha ofisi yake na kumuongoza Joram kuelekea maabara ambako alifungua friji na kutoa kichwa cha msichana mrembo. Joram alikitambua kichwa hicho kuwa cha Waridi. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake, alihisi machozi yakimdondoka. Aliyafukuza macho hayo kwa tabasamu huku akinong'ona kama mtu anayesali. "Ni Waridi! Mungu akurehemu. Naamini ni mapenzi yako kwangu ambayo yamekufanya ustahili adhabu hiyo ya kinyama. Naahidi nitakulipia kisasi".
Sala hiyo ilimfikia Inspekta Kombora. Akamgeukia Joram kwa mshangao na kusema, "Kumbe unamfahamu msichana huyu? Tafadhali turejee ofisini ili unisimulie kuhusu mkasa mzima ulivyotokea".
"Sijawa na cha kusimulia", Joram alijitetea. Hata hivyo alilazimika kusimsimulia Inspekta Kombora yote aliyoyajua. Alieleza jinsi alipomwona Waridi kwa mara ya kwanza pale baa akiwa ametegwa kwa sumu iliyokusudiwa kumwua yeye. Akaeleza pia yaliyotokea katika chumba ambacho waridi aliandaliwa kwa sumu ile ile ili amnyweshe Joram kwa hila. Ambacho Joram hakueleza ni jinsi alipofika hapo kabla ya wakati na kubahatisha, ingawa kwa taabu, kumwona mwuaji yule akitoa maelezo kwa Waridi. Hilo aliliacha ili apambane nalo binafsi. Hakupenda kuwaachia polisi ambao aliamini wangeweza kuharibu mapngo wake wa kumtia mikononi mwuaji.
"Ina maana binti huyu marehemu ndiye yule msichana aliyetoroka hospitali baada ya kuokotwa kando ya baa", Joram akatikisa kichwa kukubaliana na swali la Inspekta Kombora.
"Ndiye. Basi anastahili kifo cha aina hiyo. Kwa nini hakutoa taarifa polisi, tungeweza kumsaidia. Alishirikiana na wahalifu kuandaa njama za kufanya uhalifu".
"Inawezekana au isiwezekane", Joram alijibu kwa mkato. "Aweza kuwa alilazimika au kulazimishwa. La muhimu sasa ni kumpata huyo mwuaji".
"Ndio... apatikane haraka. Wewe humjui?".
Joram alikanusha. "Angalia bwana mdogo. Ninavyookufahamu mimi bila shaka wajua mwengi zaidi ya haya uliyonieleza. Nawe kama uonavyo hawa ni watu hatari kuliko unavyofikiri. Usiwachukulie mzaha, Ucheze nao kama ilivyo kawaida yako".
"Kawaida yangu sina mzaha wa mwuaji Inspekta", Joram alijibu. "Tena naamini kuwa nitawafikisha mikononi mwako mapema zaidi. Ninayo nafasi nzuri sana. Sasa hivi wao wanadhani kuwa nilikunywa ile dawa na sasa niko mahututi au marehemu tayari. Imani hiyo itawafanya wapate jeuri ya kuendelea na mipango yao kama walivyokusudia. Nataja kujua lengo lao, wanakusudia kufanya nini, na watu hawa ni akina nani, baada ya kufahamu hivyo nitawaleta mikononi mwako.
"Kazi hiyo ndiyo iliyonifanya nijibadili kuwa katika hali hii Inspekta. Nimeona nitoweke machoni mwao. Kusudi langu kwako ni kukuomba uitangazie dunia kuwa nimefariki ghafla. Nadhani watafurahi na kuendeleza mipango yao. Ndipo nitakapofufuka na kuwashangaza kwa kuwatia mikononi.
Walijadiliana kwa muda ofisini. Kombora akawa ameafikiana kwa taabu sana na Joram. Nia ya Joram ilikuwa awaachie polisi kufanya kazi yao kwa makini. Lakini maelezo ya Joram yalimtua Inspekta Kombora hata akakubali japo kwa shingo upande. "Kumbuka ninavunja sheria zote za kushiriki katika uongo mkubwa kama huu. Hivyo. usiniangushe kwa kushindwa kutimiza ahadi yako ya kuwatia watu hawa mikononi mwa sheria", Inspekta Kombora alimwambia Joram.
"Wanifahamu vizuri Inspekta. nakuhakikishia kuwa Siwezi kushindwa kamwe", Joram alimjibu akiweka vyema ndevu zake za bandia na kuvaa miwani yake. Akautwaa mkongojo wake na kuiacha ofisi ya Inspekta Kombora kwa mwendo ambao ulimfanya Inspekta huyo ambaye hucheka kwa nadra sana aangue kicheko kipana.
Usiku huo taarifa ya habari ya Radio Tanzania Dar es Salaam ilibeba habari ambazo ziliwashitua wasikilizaji wengi kote nchini.
"...Joram Kiango yule mpelelezi mashuhuri wa kujitegemea amefariki ghafla akiwa nyumbani kwake kwa maladhi ambayo bado hayajathibitishwa. Madaktari wanaendelea na uchunguzi watatoa taarifa za kifo hicho hivi karibuni baada ya uchunguzi,,,"
Haikuwa habari njema hata kidogo. Wala hakuna aliyetarajia kuisikia. Kila aliyemfahamu Joram alitegemea kuwa kijana huyo angeuawa au kufa kwa risasi au madhara mengine kutoka kwa adui zake. Kufa kwa maradhi! haiwezekani!.
Taarifa za habari za sauti ya Kenya na Ujerumani ziliidaka habari hiyo haraka na kuitagaza kwa mapana zaidi... "Yule kijana machachari"... Walisema wakenya, "The Iron boy..." walimwita hivyo wajerumani... "Amefariki leo ghafla. Yawezekana na njama za wahujumu ambao walimuogopa sana kijana huyu kama moto".
Ndipo watu walipolazimika kuamini. Wengi walisikitishwa na kifo hiki. Wengine walitoa machozi. lakini Wachache walishangilia.
 
Status
Not open for further replies.

Similar Discussions

Back
Top Bottom