SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO
Mvua ilikuwa inanyesha na kuleta kiubaridi cha aina yake, kibaridi hiki kilikuja wakati muafaka na kuwafanya wakazi kulisahau joto kwa muda.
Nyumba nyingi walikuwa wamejifungia ndani ili kukwepa balaa la kunyeshewa.
Ni kawaida ya mji huu, mvua kuwa kitu tishio kwa wakazi.
Mvua ile ilitumiwa vibaya na wakazi wengine waliyoigeuza baridi ile kuwa mtaji wa kuzama nyumba za kulala wageni na wanawake wasiokuwa wao ama waume za watu!
Wakati watu wakiwa wamejifungia ndani, kuna wengine walijihifadhi katika nguo zao za kuzuia baridi na kuendelea na hekaheka zao.
Wakazi wawili, mwanaume na mwanamke walikuwa wakiongozana katika mvua ile ya rasharasha, mwanaume akitangulia mbele huku mwanamke akimfuata kwa ukaribu zaidi.
Wote hawa walikuwa wameivika miili yao nguo za kukabiliana na ubaridi ule.
Walikuwa kimya hatua kwa hatua hadi walipoifikia nyumba fulani iliyokuwa imejitenga kiasi kutoka katika nyumba nyingine.
Mwanaume alitazama kushoto na kulia kisha akaruka juu na kupapasa juu ya mlango akatoka na funguo.
Upesi akafungua akaingia ndani, huku nyuma akifuata na mwanamke.
Mlango ukafungwa!
“Hapa ndo nyumbani kwa Geza Ulole…..” Mwanaume akamweleza mwanamke, kisha akaendelea kuzungumza.
“Hapa hakuna umeme… kuna majirani tulikuwa tunachangia nao kulipia LUKU walikuwa wananinyonya.. nikawaambia wakate umeme wao waone kama ntakufa….” Aliendelea kuzungumza huku akitoa lundo la nguo lililokuwa katika kochi, ili yule mwanamke aketi.
“Kwa hiyo wakakata…”
“Walikata na hadi sasa sijafa… najua wanaumia sana!” alijibu Geza, na hapo cheko dogo likatoka kutoka kwa yule mwanamke.
“Ulisema unaitwa Zainabu au nani vile…” sasa alikuwa anautafuta mshumaa.
“Zay B…” akajitambulisha yule binti.
“Hilo ndo jepesi… Zay B.!” akarejea Geza huku tayari akiwa ameuwasha mshumaa.
Alipoketi tu, Zay B akafungua mfuko fulani na kutoka na makaratasi kadha wa kadha, wakayasoma tena kwa mara ya pili.
Makaratasi haya japokuwa hayakuwa katika muunganiko mzuri sana lakini ni haya yaliyowafanya wawili hawa walipofanikiwa kutoroka katika nyumba ile ya siri wasijipeleke kwa akina Sajenti Pilipili na IGP Sungura.
Makaratasi haya waliyapata baada ya Geza kupambana na yule mtu aliyemtisha na kumsimamisha wakati anatoka akiwa amembeba mgongoni Zay B.
Mtu huyu aliyewasimamisha alikuwa ameagizwa kuyapeleka mahali makaratasi yale, lakini bahati ikawa mbaya upande wake. Geza alimfyatua vibaya mno na kuundoa uhai aliokuwa anaumiliki.
Kosa alilofanya ni kumkaribia Geza aliyekuwa amembeba Zay B
Akamuuliza yeye ni nani Geza akajitambulisha kuwa yeye ni Solo. Jina ambalo alilisikia na kulikariri alipokuwa amebanwa na wale watu wawili aliowaacha ndani wakiwa hawana uhai.
Kujitambulisha kama Solo kukalegeza mashaka ya yule mtu, akaendelea kuwasogelea.
Geza akamsihi Inspekta Zay B afanye kitu.
“Legeza mikono yako…” Inspekta akamnong’oneza GEza. Geza akatii……
Kisha likabaki suala la kungoja yule mtu awakaribie zaidi. Zay B akahesabu hatua kwa hatua hadi alipofika panapotakiwa, akatokwa na pigo la umauti, yaani pigo ambalo litamtupa mbali adui yake huku na yeye akitua chini asiweze kuamka tena.
Ikawa!
Zay B akajitupa vizuri,akautumia mguu wake uleule uliojeruhiwa na Geza akamwadhibu yule bwana bunduki ikamtoka huku akitokwa na yowe la hofu.
Kabla hajakaa sawa Geza alikuwa amefika tayari, akamruka Zay B na kutua juu ya yule bwana akamshindilia ngumi nzitonzito hadi akalainika.
Huyu naye wakamuhoji maswali mawili matatu, akagoma kujibu.
Geza akamuua!
Wakaondoka na begi lake dogo.
Katika begi hilo wakayakuta makaratasi yaliyokuwa na maeolezo mbalimbali.
Kilichowavuta na kuwafanya waishi kwa tahadhari kubwa zaidi ni kukuta barua ikiwa imeandikwa ikitumwa kwenda kwa mtu aliyeitwa, Rabbit Sungura!!
Wote wakamuwaza IGP Sungura Sungura!!
Kengele ya hatari ikakung’uta vichwa vyao.
Wakakubaliana kwa sauti moja kuwa hawataenda kujionyesha mbele ya IGP wala sajenti Pilipili na badala yake watalitazama hili jambo kwa jicho la tatu.
Hatua ya kwanza ilikuwa Inspekta kupata tiba, hili walilifanyia Mlandizi mkoani Pwani nje ya jiji la Dar es salaam, baada ya Inspekta Zay B kuwa sawa walirejea jijini Dar es salaam na sasa wapo nyumbani kwa Geza Ulole.
Wanayasoma upya yale makaratasi, wakarudia kuisoma barua iliyoandikwa kwenda kwa Rabbit Sungura…. Wakakutana pia na barua kwenda kwa mtu aliyeitwa Vonso Almeida.
Jina hili likamshtua sana Inspekta Zay B.
Barua ile iliambatana na vitisho kedekede kuelekea kwa mtu aliyeitwa Vonso Lmeida.
Barua ile ikaambatana na majigambo kuwa wanaoandika barua hiyo wanafahamu fika kuwa Vonso anapatikana Kitunda. Na kama asipotii matakwa yao watamuua……
Wakaenda mbali zaidi kimajigambo na kutimiza masharti ya mkwara wakamtajia hadi nyumba aliyokuwa anaishi!
Barua ile ilipatikana pia ikiwa imeandikwa kiingereza na kuna nyingine ilikuwa katika kiarabu.
Zote zikitumwa kwa Vonso Almeida wa Kitunda.
Geza kama kawaida yake hakutaka wauache usiku upite.
Japokuwa Inspekta Zay B aliona kama ni uamuzi wa hatari sana na inawezekana maadui wakawawahi lakini Geza alitoa jibu lisilotarajiwa.
“Hakuna kitu napendelea katika maisha yangu kama michezo ya hatari. Hawa wajinga kwanza ni waoga yaani wanamuandikia mtu barua ya kumtishia kumuua? Ukitaka kuua usiandike barua we ua tu…..” akasita kidogo kisha akaendelea, “Yaani mimi enzi zangu shuleni, ukitokea ugomvi sijui wanaanza kuchora mstari atakayeuvuka mbabe… mi kabla hawajamaliza kuuchora tayari nishamvaa adui yangu nampiga ngumi ya usoni halafu nakimbia…” Geza akamaliza akimuacha Zay B akipambana kuzibana mbavu zake asicheke kwa sababu Geza alikuwa anamkumbusha mbali sana enzi za utoto.
“Kumbe na wewe ulipitia hizo..” Zay B akatia neno.
“Na nd’o chanzo cha kuacha shule mapema…. Wakati nipo darasa la sita kuna siku nilichelewa shule, ile mwalimu anataka kunichapa nikawa najaribu kukwepa… akaniuliza kama nataka kupigana naye. Akatupa fimbo chini akakunja ngumi…. Doh! Sijui nilipatwa na wazimu gani hata ile anatupa fimbo nikamtandika ngumi nikakimbia moja kwa moja, baadaye nikasimuliwa kuwa aling’oka jino.”
Zay B akastaajabu, akataka kuuliza zaidi lakini Geza akasihi waondoke kwenda eneo la tukio.
Hawakujua kuwa wakati wa balaa ulikuwa umewadia
______
Barabara ilikuwa mbaya sana kutokana na mvua kunyesha jijini Dar es salaam, na njia waliyopita ilikuwa na madimbwi mengi sana ya maji.
Hadi wanafika Kitunda nguo zao zilikuwa zimelowana kwa matope na pia kunyeshewa mvua ambayo bado ilikuwa inanyesha.
Geza asiyekuwa na utaalamu sana katika mambo ya namba za nyumba aliongozwa na Inspekta nyumba kwa nyumba hadi wakaifikia nyumba iliyokuwa imeandikwa katika ile barua.
Hakuna aliyekuwa na uhakika ikiwa nyumba ile ni sahihi ama la lakini walihitaji kumjua Vonso.
Wakauendea mlango na kubisha hodi kama mara tatu, mlango ukafunguliwa na mtoto mdogo.
Alikuwa ametawaliwa na usingizi hata hakukumbuka kusalimia.
Inspekta akamuuliza nani yupo ndani, bila wasiwasi mtoto akajibu kuwa babu yake yupo ndani.
Babu? Wakashangaa…..
Mtoto akaelezea kuwa babu yake alikuwa amelala zamani sana na hakuwa na kawaida ya kuamka asubuhi hadi panapokucha.
Geza hakukubali akamlazimisha yule mtoto amwamshe babu yake kwa sababu kuna jambo la msingi sana wanahitaji kumpa taarifa.
Mtoto akatoweka, baada ya dakika tano alirejea akiwa amemshika mkono mzee wa makamo kiasi.
Geza akamsalimia, mzee akawauliza wao ni akina nani.
Badala ya kujibu Geza akamuuliza iwapo yeye ni Mzee Vonso.
“Hapana naitwa mzee Magea… David Magea ndo jina langu!” alijibu huku akionekana kutetemeka.
Inspekta akaigundua ile hali, akatambua kuwa mzee alikuwa anadanganya.
“Mtakuwa mmekosea nyumba wanangu!” aliwaeleza huku akiwa anataka kuondoka.
Geza akamdaka mkono.
Akaisoma namba ya nyumba katika ile barua na kumuuliza kama ni nambari ya nyumba yake, mzee akatikisa kichwa kukubali.
“Sikiliza mzee sisi hatuna nia mbaya tupo hapa kukusaidia, hatupo hapa kwa sababu mbaya kabisa, kuna watu wabaya wanakutafuta. Ikiwa utasimamia msimamo kuwa we ni mzee Magea sijui mzee David shauri zako tutaondoka na wao wakifika watakucharanga mapanga wewe na mjukuu wako….” Alikoroma inspekta.
Kisha akafanya mkwara wa kumshika mkono Geza kama anayemtaka waondoke.
“Sikiliza,, sikiliza kidogo lakini aaargh! Lakini… ndio naitwa Vonso nyie ni akina nani…..” alijibu kwa kujilazimisha na sijue jibu lile iwapo lina msaada kwake ama amenunua balaa.
“Hutakiwi kulala katika nyumba hii leo….” Geza alimjibu.
“Ni kweli hautalala hapa tutaondoka wote mzee.” Ikasikika sauti mpya katika kile chumba.
Balaa!
Geza akapoteza umakini akageuka na kujikuta akichapwa ngumi kali begani akaenda chini, Inspekta Zay akawa makini zaidi tena katika ule ubora wake wa juu hasahasa akiwa na ghadhabu.
Akaruka juu juu na kufyatuka teke kali lililompata yule bwana kichwani akaenda alipokuwa Geza.
“Mbuzi kafia kwa muuza supu…” akaropoka Geza huku akimdaka yule bwana na kumtia kabali ambayo labda ilikuwa mara ya kwanza kupigwa katika maisha yake.
Alirusha miguu mpaka nafsi ilipopatwa uchovu ikaamua kuondoka zake.
Akatulia tuli.
Vonso alibaki akiwa amekodoa macho yake huku mjukuu akiwa hajui hili wala lile alikuwa ameuchapa usingizi.
Zay b upesi akaruka na kumdaka yule mtoto kisha Geza naye akamshika mzee Vonso wakatoka nje.
Huku wakamkuta bwana mmoja akiwa anavuta sigara.
Alipowaona akashtuka, ni kama hakutarajia kama watatoka salama humo ndani badala yake alitarajia mwenzake ndiye atakayetoka.
“Bastard!” akaponyokwa na lile neno huku akizikunja ngumi zake.
Inspekta Zay B akataka kujipeleka apambane naye Geza akaingilia huku akizungumza.
“Huyu hachukui hata dakika moja… ikizidi dakika moja nastaafu kupigana…” akazungumza Geza huku akijiweka sawa kumkabili yule bwana aliyeonekana kuwa mjuzi haswa katika hicho alichokuwa anakifanya.
Kweli haikuchukua hata nusu dakika, ile yule bwana anajiandaa kufyatuka, Geza akaingiza mkono wake mfukoni, akaichomoa ile bunduki aliyoizoea.
Akamfyatua kimya kimya mguu.
Akatokwa na yowe akatua chini kama mzigo.
“Si nilikwambia…” akajitapa huku akimsogelea yule bwana aliyekuwa anaugulia pale chini.
Akampiga kibao kikali sana usoni na kumuuliza maswali kadhaa kwa Kiswahili.
Akawa anajibu kwa kiarabu!
Geza akamtandika kibao kingine, akaanza kujibu kiingereza.
Kisha akamzamishia bisu katika mkono wake, “Mamaaa” akatokwa mayowe na hapo akagundua kuwa kumbe hata Kiswahili alikuwa anakijua.
Akambana maswali akayajibu.
Akajieleza kila kitu kuanzia mkutano mkubwa uliofanyika Mombasa, mkutano uliotoa orodha ya wanaostahili kuuwawa.
Geza akapekenyua katika mifuko yake na kuitoa ile orodha.
Ebwana eeh! Kati ya watu kumi walio katika orodha wanne kati yao walikuwa wamepigiwa tiki za rangi nyekundu tayari!!
ITAENDELEA!!!!