Riwaya: Pumbazo

Riwaya: Pumbazo

asante mkuu Yankee kwa kuindeleza pale ilipoishia...samahani wote kwa kuwakwanza nilipata safari ya ghafla nikajikuta nipo mbali hivi vitu...

ila kesho asubuhi inshallah tutaendelea na kumalizia pale Yankee alipoishia

tupo pamoja
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA
Hili jambo liliwavuruga akina Geza na kujiona wapo
dakika kadhaa nyuma ya wapinzani wao. Lakini walau
waliwahi kumdaka Vonso waliamini kuwa huyu lazima
atawaonyesha njia zaidi.
Yule bwana ambaye Geza amemchapa risasi ya mguu
kimyakimya alikuwa bado chini, Geza akamwendea na
kumnyanyua kisha akampa kitisho kikali.
Sasa Geza alikuwa na ghadhabu isiyopimika na hii ni
baada ya kuona kuwa ule mchezo ulikuwa umekolea
tayari.
Wakaondoka na yule bwana wakitumia usafiri wa
pikipiki kwa dhana kwamba yule ni mgonjwa wao
wanamuwahisha hospitali na kila mara Geza
alimkumbusha kuwa akileta masihara anamtandika
risasi bila huruma.
Sasa alitakiwa kuongoza njia.
Geza alipanda pikipiki moja na yule bwana huku
Inspekta Zay B akipepea na mzee Vonso na mjukuu
wake.
Wakati wawili hawa wakiwa katika harakati hizi za
‘ukizubaa umezikwa’ kuna bwana mwingine naye
alikuwa katika harakati hizi lakini yeye aliongozwa na
hisia pamoja na hasira kali.
____
PIKIPIKI aliyokuwa amepanda ilimpeleka hadi
alipokuwa anahitaji kufika. Aliamini kiuhakika kabisa
kuwa alikuwa hajakosea hata kidogo njia.
Alishuka akamlipa dereva kisha akaenda mlangoni na
kugonga mlango.
Hakuwa na saa mkononi lakini mara ya mwisho wakati
anatazama saa yake ilikuwa yapata saa nane usiku na
dakika nyingi.
Hakujali kuhusu muda alikuwa anaongozwa na hasira
hivyo hakuna alilojali.alikuwa amesubiri vya kutosha
na aliona kuwa siku hii ilikuwa muafaka kabisa
kuuvunja ukimya, upelelezi wake wa kimyakimya
ulikuwa umegonga mwamba akaamua kujionyesha
wazi.
Alibisha hodi zaidi na zaidi, hatimaye alisikia sauti
ikimuuliza yeye ni nani.
“Rama! Mimi ni Rama…. Baba Jose…” alijitambulisha
kwa sauti iliyosikika vyema.
“Nani? We nani…” sauti ya kike ikahoji kisha
akamsikia muulizaji akiondoka kwa kasi, “Baba
Aneth… we baba Aneth amkaa…” aliisikia sauti.
Ukimya ukatanda baada ya muda akasikia akiulizwa
tena yeye ni nani, akajitambulisha kiufasaha zaidi.
“Tafadhali naomba mfungue mlango nina jambo la
msingi sana” alizungumza.
“Wewe ni Rama yupi. Maana Rama amekufa huko
Oman….” Alihoji mzee Fidelis ambaye ni baba mzazi wa
Aneth.
Rama akajieleza kwa ufupi juu ya kilichotokea,
hakutaja kuhusu chimbo la umauti bali alidai kutekwa
na sasa yupo huru.
Akawasisitiza kuwa hajafa!
Nani afungue mlango? Hilo likawa swali, mama Aneth
akamsihi baba Aneth afungue… wote walikuwa waoga
wakiamini kuwa ule huenda ni mzimu.
Baba Jose akaenda mbali zaidi na kuhisi ni mzuka wa
baba Jose umekuja kulipa kisasi kwa kitendo chake cha
kumchapa makofi mtoto wake mdogo.
“Baba na mama… tafadhali tafadhali sana, je kuna
ambaye aliona maiti yangu… sijafa nawaomba
mfungue tafadhali… nina jambo la muhimu..” alisihi
sana.
Baba Aneth akaufungua hatimaye, lakini alikuwa
mwenye hofu bado.
Rama akamsalimu lakini hakutaka kuingia ndani
akayamalizia mazungumzo nje.
“Nimeenda nyumbani kwangu, sijakuta mtu… nina
shida na mke wangu…. Sijui kama yupo hapa?” aliuliza
Rama akionekana mwenye wasiwasi na asiyetaka
kupoteza muda kabisa..
“Umejaribu kumpigia simu yake…” aliuliza mama huku
akiwa nyuma ya mgongo wa mumewe.
“Nimejaribu lakini sijapata majibu mazuri, nahitaji tu
kuonana naye….”
Baba Aneth akamtazama Rama usoni, lile tukio la
kumpiga Jose kofi la haja shavuni likajirudia akajiona
mwenye hatia kubwa sana.
Na kitendo cha mwanaye kuondoka akiwa amesusa
kilikuwa kinamtesa sana.
Mzee Fidelis akaona hii ni fursa ya kuitafuta suluhu na
mwanaye kupitia kurejea kwa mume wake.
Akachukua simu yake akaziandika nambari za Aneth na
kupiga, simu iliita bila kupokelewa.
Anamaanisha alichoapa!! Aliwaza mzee Fidelis.
“Sasa mwanangu, naomba ulale hapa sebuleni kisha
asubuhi nitakuelekeza alipohamia Aneth… sio mbali
sana….nadhani sasa hivi si muda mzuri” Alitoa
muafaka, Rama hakuafiki alihitaji kwenda usiku
huohuo.
“Doh! Basi sawa nitakupeleka lakini asijue kama ni
mimi nimekupeleka maana naona anaishi… aah anaishi
na mwanaume fulani na ni kama hataki watu wajue
anapoishi mimi nilimwona kibahati tu nikafuatilia hadi
nikapajua anapoishi….” Mzee Fidelis alitoa majibu
yaliyomtia ukakasi Rama, ni kweli alihisi kabisa mkewe
amemsaliti tayari lakini kimoyomoyo alikuwa anaomba
hisia zake zisiwe kweli hata kidogo.
Sasa baba mtu anapigilia msumari mwingine!
Eti ni kweli Aneth mkewe anaishi na mwanaume.
“Sawa baba sitamweleza! Na vipi kuhusu Jose
mwanangu” alijibu kinyonge.
“Yupo, anaishi naye..”
Mzee Fidelis akaingia na kujiandaa kisha akamuaga
mkewe na kuondoka.
“Rama mwanangu!” mama Aneth alimuita, Rama
akageuka
“Usichukulie hasira… kila mtu alijua umekufa
nakuomba sana mwanangu sawa…. Mkumbuke mmezaa
mtoto….” Alisihi mama Aneth huku akijenga picha
jinsi Rama atakavyomshambulia Aneth kwa makofi na
mateke pindi atakapomfumania na mwanaume
mwingine.
Roho ikamuuma!.
Maneno haya yakawa yanashindilia ngumi nyingi zaidi
katika fundo la maumivu ya Rama.
Akazidi kuumia!
Walipanda pikipiki moja watu wawili. Wakaenda kwa
mwendo wa dakika ishirini na tano wakawa wamefika
mahali stahiki. Wakashukia umbali wa mita zipatazo
mia mbili kutoka nyumba anayoishi Aneth.
“Huyo mwanaume unamfahamu baba? Au aliwahi kuja
kujitambulisha kabla yangu nyumbani?” Rama alihoji
huku akitetemeka midomo.
Sauti ya Rama ilimuumiza mzee Fidelis alijua wazi
kijana huyu anapitia uchungu mkali wa mapenzi.
“Hapana namfahamu kwa wadhifa wake tu lakini si
mengineyo…”
“Kwa hiyo mama Jose alifuata pesa kwa jamaa sio?!”
alihoji Rama huku machozi yakimlengalenga.
“Looh! Rama mwanangu, hapa nitakudanganya mi sijui
lolote, kuna muda niligombana naye kidogo ndo
akaondoka na nikagundua anaishi na huyo
mwanaume…ni askari tu!” alijibu huku akibinua
mabega kujitoa katika hatia ya uchonganishi.
Kusikia kuwa mama Jose ameangukia kwa askari,
Rama akashtuka na kuanza kumchimba zaidi mzee
Fidelis juu ya muonekano wa huyo mwanaume.
“Mwanangu… huyo mwanaume wanasema tu yupo ila
mimi sijawahi kumuona, wanasema anaingia usiku
sana na kutoka asubuhi..”
“Sawa baba asante sana…. Nitakujuza kitakachojiri”
alizungumza kinyonge Rama huku akimgongagonga
mgongoni baba mkwe wake ambaye alipanda pikipiki ili
aweze kuondoka zake kabla Rama hajafanya
alilokusudia.
“Rama usiwaletee vurugu zozote, anaweeza kuwa na
bunduki huyo bwana mkazua mengine… licha ya yote
yaliyopita Rama mi nawapenda sana nyote wawili.
Ninajua makosa yangu ya wakati wa nyuma na
nimeyajutia.. sitaki kuwapoteza Rama” alizungumza
kwa hekima sana mzee Fidelis, hii ikiwa ni mara yake
ya kwanza kabisa kuzungumza hivi dhidi ya Rama.
Rama akatikisa kichwa kukubali, pikipiki ikaondoka.
Rama akawasindikiza kwa macho, akawa anamtazama
mzee Fidelis na kukiri katika nafsi yake kuwa hakika
mzee yule alikuwa amebadilika.
Ile anataka kugeuka ili aelekee katika nyumba ile
kufanya alilokusudia mara ukasikika mlio wa risasi,
tairi ya pikipiki ikafyetuliwa baba mkwe akarushwa
kule na dereva naye akibaki hoi. Rama alikuwa
ameshtukizwa sana, alibaki kuduwaa…
Lakini hakutukubali iwe namna yay eye kufikia mwisho
kirahisi vile, akajirusha pembeni na kisha akajificha
katika jumba lililokuwa linaendelea kujengwa. Akiwa
anahema juu juu sana akawa anachungulia kule
lilipotokea tukio la ghafla akajisahau kuwa ficho huwa
ni la wote sio la mtu mmoja.
Ubaridi ukapenya katika shingo yake, na kisha ikawa
amri tulivu kabisa.
“Ukipiga kelele ama kufanya jaribio lolote la kipuuzi
nakuua!” sauti ilimtisha nyuma yake.
Alikuwa ametekwa!
Rama akasalimu amri kwa kunyoosha mikono juu.
Akavamiwa na kupigwa ‘mtama’ akatua chini, na hapo
akajikuta akitazamana na mdomo wa bunduki.
“Nauliza mara moja kifuatacho kitendo….” Ilihoji ile
sauti na kuendelea, “Rabbit Sungura yupo wapi?
Sihitaji jibu la sijui ama la nasambaratisha kichwa
chako…..” ilikoroma ile sauti isiyokuwa na punje ya
masihara. Na hapo kwa macho yake Rama akakiona
kidole cha yule bwana aliyeuziba uso wake kikianza
kuvuta kiwambo cha kuruhusu risasi itoke.
Lakini ghafla ukasikika mshindo mkubwa, Rama
aliyekuwa amefumba macho akafumbua. Hakuwa chini
peke yake…
Alikuwa pamoja yule bwana lakini tayari alikuwa maiti.
“Take the gun!” aliisikia sauti ikimsihi, hakutaka
kujua ni nani akaichukua bunduki kutoka pale chini,
kisha akabiringita na kujiweka tayari kwa pambano
lolote litakalokuja mbele yake.
Kwa mbali alimwona baba mkwe wake pamoja na dereva
wakiwa bado wametulia tuli!!
Rama akiwa katika ficho lake, mara akamwona
mwanamke akitoka katika ile nyumba, macho yake
hayakumdanganya alikuwa amemuona mke wake wa
ndoa akiwa amevaa nguo nyepesi kabisa ya kulalia
iliyoyachora maungo yake.
Mara nyuma yake akatoka mtu aliyemfahamu fika.
Angeweza kuwa mwanaume mwingine asinge jali.
Lakini alikuwa ni sajenti Pilipili akiwa amevaa pensi
pekee huku akiwa kifua wazi na bunduki yake mkononi.
“Simameni hapohapo mlipo wendawazimu wakubwa
nyinyi!” Rama alitoka katika ficho lake akiwa
ameielekeza bunduki kuwaelekea Aneth na Sajenti
Pilipili.
Wote wakasimama wakijua ni adui.
“Sajenti umenitupa Oman niende kufa ili ufanye
haya?” alilalamika.
Mara Aneth akiwa amembeba Jose mgongoni aligeuka.
“Mume…”
“Shhhh!!! Hakuna mume wako hapa… mbele yako ni
mwanaume mwenye roho mbaya kupita kiasi…..
ukipiga hatua mbele zaidi ninakuua malaya wewe,
nawe muuaji tupa hiyo bunduki chini kabla
sijaielekezea hii bastola katika korodani zako…”
Sajenti akaiachia bunduki yake huku akiwa amepigwa
na butwaa kumuona Rama akiwa hai.
“Rama… ni nini hiki?” alihoji.
“Unaniuliza ni nini hiki…. Hiki ni kituko cha mwaka,
mwanaume mmoja mwenye madaraka anaamua
mwenzake afe ili amrithi mkewe… simple tu kama
hivyo.” Alijibu Rama huku akilazimisha tabasamu.
Alikuwa mwenye hasira kali sana na alikuwa tayari
kuua.
Macho yake yalikuwa yanawatazama watu wawili
ambao kwa jinsi mavazi yao yalivyokuwa basi muda si
mrefu walikuwa wametoka kuridhishana kimapenzi.
Akafumba macho huku akimjengea picha jinsi Aneth
alivyokuwa akifanya jitihada ili kumfurahisha sajenti
Pilipili kitandani.
Huenda Jose alikuwa bado hajalala, kwa hiyo
mwanangu amemuona mama yake anafanya mapenzi
na mwanaume mwingine!
Aliwaza Rama huku akiuma meno yake kwa ghadhabu
kali…..
Nawaua! Aliapa…….
Kisha ghafla akafyatua risasi!!
 
SEHEMU YA MWISHOO
Bunduki ilikuwa haipo katika kiwambo cha kuzuia sauti
ilitoa mlio mkubwa sana baada ya Rama kufyatua.
Alikuwa amefyatua hewani
Mama Jose akaanguka chini, akawa amemwangukia
Jose. Jose akaanza kulia.
Kilio chake kikapenya katika masikio ya Rama…..
Akajikuta anaishiwa nguvu, akaishusha bunduki yake
chini.
Akakimbilia alipokuwa mama Jose akamkwapua mama
Jose huku akiwa makini kabisa kumtazama Sajenti
asije kuzua balaa lolote.
“Rama… sajenti aliita, “ kisha akaendelea “sio muda
huu Rama, sio muda huu hatuwezi kuzungumza lakini
elewa kuwa hili ni pumbazo….” Alitaka kuendelea
kuzungumza lakini ghafla akapokea pigo maridhawa
kutoka kwa Rama. Lilikuwa pigo ambalo hakulitarajia,
teke kali likatua katikati ya miguu yake.
Sajenti akatoa kilio kikubwa haswa cha uchungu.
“Nyamaza mwanangu!!” Rama alimbembeleza Jose
aliyekuwa akitokwa na kilo kikubwa bado.
“Rama hebu nisikilize kidogo!” alisihi sajenti. Rama
akamtazama lakini hakusema neno lolote.
“Rama unalodhani si sawa hata kidogo, tuondoke eneo
hili si salama kwetu hata kidogo. Tazama Rama
ningekuwa na nia mbaya nisingefyatua risasi na
kumuua huyo bazazi aliyetaka kukumaliza, kwanini
nisimwache akuue ili nifanye hayo unayowaza kuwa
nilikuwa nafanya!! Rama kuwa mwanaume imara sina
nifanyalo na mkeo, nimekuwa nikimlinda…”
alizungumza kwa kufoka sajenti.
Rama akaanza kuingiwa na yale maneno, na palepale
sajenti akatokwa na teke kali la haja likaipiga ile
bunduki ikarushwa mbali.
Rama aliyekuwa amebeba mtoto akataka kuikimbili
lakini tayari Sajenti alikuwa ameokota bunduki yake
kisha akamwonya Rama asipige hatua zaidi.
“Kwa hiyo unataka kuniua ili umfaidia mke wangu
sajenti…” alizungumza kinyonge.
“Niue lakini usimwache mwanangu hai.. tuue sote.
Ubaki na mwanamke wako..” alimalizia Rama.
“Rama mimi ni mtu mzima, unajua kuhusu familia
yangu Rama.. nimewahi kukueleza hapo kabla familia
yangu ni kitu cha muhimu kupita kitu kingine duniani,
Rama nipo hapa kwa sababu tu nimetakiwa kuwepo
sijawahi na wala sina mpango wowote wa kushiriki
dhambi hii unayonitamkia. Rama mtandao wa Vonso
umechachamaa, ni hawa waliotaka kukuua dakika
kadhaa nyuma, Rama hatupo sehemu salama. Simama
kama mwanajeshi weka haya mambo kando!” akasita
akameza mate kisha akatoa amri.
“Ninazungumza kama mkuu wako wa kazi sasa, mpatie
mtoto mama Jose kisha pick up the gun tunaingia
vitani!!”
Ilikuwa sauti ya amri haswa Rama akatii!
Lakini ni kama alichelewa sana kutii, walijikuta
wamezungukwa na watu wanne wenye silaha nzito
kabisa.
Hakuna ambaye alithubutu walau kufyatua risasi
kutoka katika bunduki yake.
Wakatekwa na kufungwa vitambaa vyeusi usoni,
wakapakiwa katika gari na watu wasiowajua.
Ndani ya gari sajenti alimlaumu Rama kwa kuendeshwa
na hisia zaidi kuliko uhalisia
_____
MWAKA 1965, Visiwani Zanzibar.
ILIKUWA imepita miaka miwili bada ya mapinduzi ya
Zanzibar yaliyofanya kisiwa hiki kuwa huru kutoka
katika utawala wa mwarabu.
Waarabu ni moja kati ya watu ambao hawakufurahia
kabisa jambo hili kwa sababu walizoea kuishi katika
kisiwa hicho. Lakini si waarabu pekee wapo waswahi
wachache ambao pia hawakufurahia jambo hili.
Mmoja kati ya waswahili hao alikuwa ni Sameer bin
Alafat ambaye baadaye alibadili jina lake na kujiita
Vonso Almeida, jina alilotunukiwa na mtawala wake
ambaye ni mwarabu.
Huyu alikuwa ananeemeka kutokana na uwepo wa
waarabu, aliwafanyia kazi na kuwanyenyekea
walivyotaka na kujikuta akiipata ridhiki yake kiulaini
sana.
Kuna waswahili walikuwa wakimchukia lakini hakujali
kwa sababu kila mmoja alikula kwa jasho lake.
Kitu cha msingi ni kwamba katu hakuwahi kuvujisha
siri zozote alizojua kuhusu harakati za kuusaka
uhuru.
Waarabu walimpenda kwa sababu ya unyenyekevu
wake, na hata baada ya uhuru walimuuliza iwapo yupo
tayari basi waende naye Oman.
Vonso akakubaliana nao.
Aliyazoea mazingira ya Oman upesi sana na ni huko
alipujifunza mengi kuhusu waarabu, aligundua kuwa ni
watu wasiopenda kufanya kazi za mikono, badala yake
wanapenda kufanyiwa kila kitu.
Hizi kazi yeye aliziweza na aliamini kuwa wazanzibari
wengi tu wanaziweza kwa sababu walizoea suluba za
utumwa.
Akiwa ametimiza umri wa miaka thelathini mnamo
mwaka 1975 akiwa sawa kabisa na waarabu wa Oman,
Vonso alianza kuwatafutia neema wazanzibari
wenzake. Kila akienda Zanzibar anaondona na
wanaume watano na wasichana watano na kuwapeleka
Oman kufanya kazi ambapo walikuwa wanapata malipo
mazuri kabisa.
Waarabu wenginje waliposikia juu ya hili na wao
wakaanza kumsumbua Vonso awatafutie wafanyakazi.
Hatimaye mwaka 1980 Vonso akafungua kampuni yake
ya kusaidia watu kupata ajira akaiita Vonso Almeida!.
Kampuni hii ilimwingizia kipato, lakini pia ukawa
mwanzo way eye kupumzika na kuwaacha watu
wengine wasafiri kwenda Tanzania bara na visiwani
kusaka wanaohitaji kufanya kazi nje ya Tanzania.
Kuna tetesi zilianza kuvuma miaka ya 1985 ambazo
zilimtesa sana Vonso ambaye ni mcha Mungu!
Alisikia kuwa kuna baadhi ya vijana wake wanachukua
rushwa ya ngono kwa wanawake kabla ya kuwafikisha
Oman ambapo wanakuja kufanya kazi.
Alilikemea jambo hili lakini hakutajiwa muhusika,
kampuni nayo ikazidi kuwa kubwa!
Mnamo mwaka 1990 kesi zikawa nyingi sana za
unyanyasaji, sasa haikuwa kutoka kwa waswahili peke
yao bali waarabu kwenda kwa waswahili.
Vonso alikuwa anawaheshimu sana waarabu kwa jinsi
walivyomtunza kuanzia uvulana hadi anakimbilia uzee
wake.
Kuliko kuzua mabishano nao, akaamua kung’atuka
katika kiti chake cha ukurugenzi.
Akawaambia maneno yake machache sana, wenzake
ambao wote walikuwa wanamzidi kisomo.
“Kama mnalofanya mnalijua ni dhambi na mnalificha
huku mkiendelea kulifanya wallah! Nawaapia mwenyezi
Mungu atawahukumu siku moja…!
Wasomi wakacheka wakampuuza!
Vonso akaondoka lakini hakuwakabidhi hati wala
katiba ndogo ya kampuni yake.
Akarejea Tanzania bara badala ya Zanzibar, akaanza
kufanya ujenzi na kisha akahamia nyumbani kwake
maeneo ya Kitunda akatulia tuli akajisahaulisha kabisa
kama aliwahi kuwa na kampuni kubwa kabisa iliyokuwa
inamuingizia pesa.
Na ili asahau zaidi juu ya ile kampuni, alipotua pale
Kitunda akajitambulisha kwa jina la David Magea!
Wakamzoea kwa jina la mzee Magea.
Maisha yakaendelea!
Miaka inakatika na sasa yupo mikononi mwa akina
Geza usiku wa manane pakiwa na hekaheka juu ya
kampuni yake inayojishughulisha na biashara ya
utumwa wa kisasa.
Si kijana tena sasa ni mzee!
Maelezo ya Vonso yaliwagusa sana Inspekta na Geza,
wakamuuliza maswali mawili matatu.
Akaelezea kila alichokuwa anakitambua.
Geza akamwagiza Inspekta waende kuwahifadhi mahali
Vonso na mjukuu wake ili wao waingie kazini moja kwa
moja.
Ikawa hivyo!
_______
MAKUTANO YA PUMBAZO
KIMYA kilikuwa kimetanda haswa, na giza lilikuwa
limetawala. Baadaye taa ikawashwa…
Mateka kadhaa wakaonekana wakiwa na vitambaa
vyeusi usoni.
Hakuna mateka aliyepewa nafasi ya kujitetea zaidi ya
kuitwa jina lake na anapoitika anasogezwa mbele zaidi
katika foleni.
Liliitwa jina la Ramadhani, akaitwa Sajenti Pilipili,
akaitwa Mama Jose, akaitwa Jose yule mtoto
akawekwa peke yake huku analia, hakuna aliyejali,
akaitwa mzee Fidelis, akaitwa Rabitt Sungura, lakini
hakuwa amepatikana bado.
Kisha kikafua kitendo cha bunduki kuandaliwa kwa ajili
ya kuwaondoa katika uso ule wa dunia kwa kosa la
aidha kugundua juu ya harakati za chimbo la mauti
ama namna yoyote ile.
“Geza….. chukua wawili na mimi nachukua wawili wale
wenye silaha…” alinong’ona inspekta Zay B kutokea
katika kona waliyokuwa wamejificha wakiwa
wameingia mapema zaidi kuliko kundi lile la watu
wengi… alipomgeukia Geza aligundua kuwa Geza
alikuwa akibubujikwa na machozi.
Ilikuwa mara yake ya kwanza kabisa kumuona Geza
katika hali ile hakuweza kuhoji kwa sababu muda
ulikuwa unazidi kwenda.
Inspekta akahesabu hadi tatu kisha akafyatua risasi
akiwaangusha wale wawili lakini Geza alimfyatua
mmoja tu na hakutumia risasi tena akatoka mbio
kutoka katika lile ficho.
Inspekta akabaki kuduwaa ni nini kilikuwa kinamsibu
Geza.
Geza akajirusha na kumkamata yule bwana aliyediriki
kumshika yule mtoto na kumweka katika orodha ya
wanaostahili kufa bila kujali kilio chake. Alikibamiza
kichwa cha yule bwana chini mara kadhaa akaamka
naye akajirusha naye chini.
Kwa kifupi Geza aliua kwa hasira kali zaidi kuliko mara
zote alizowahi kuua.
Baada ya hapo alisimama akiwa amelowa damu.
“Sina mtoto lakini ole… ole kwa atakayediriki katika
hii dunia kumnyanyasa mtoto mdogo mbele yangu..”
alisema huku akimsogelea Jose, akamfungua kile
kitambaa cheusi na kumkumbatia.
“Ba…. Ba….” Jose alisema kwa sauti ya kitoto
toto….
Zay b akatokwa machozi.
Baada ya dakika kadhaa Zay B alikuwa anapiga saluti
ya heshima mbele ya Sajini Pilipili.
Rama alikuwa amekumbatiana na mkewe huku
wakihofia kumwomba Geza awapatie mtoto
aliyeonekana kumzoea na kumpenda tayari.
Fahamu zilikuwa zimerejea kwa mzee Fidelisi na
dereva wa bodaboda, wao walikuwa wakijiuliza kulikoni
na hakuna aliyewajibu.
“Vonso ni mtu hatari sana..” Sajenti alisema, Geza
akacheka kwa sauti…. Hii ilikuwa mara yake ya
kwanza kutokwa na kicheko kikubwa vile.
Inspekta Zay B akaelezea kwa kifupi juu ya Vonso na
hapo akampa pole Rama kwa yaliyomsibu.
“Mbona uliniacha nikatekwa Zay B” Rama alihoji.
“Nilipokupungia mkono nilikuwa nimetekwa tayari…
tumshukuru Mungu kuwa tupo hai.” Alijibu kwa sauti
tulivu yenye mahadhi ya Zanzibar.
Rama akatabasamu.
_____
Mwili wa Rabbit Sungura ulikutwa katika ufukwe wa
bahari ya hindi jijini Dar es salaam ukiwa ulishapoteza
uhai muda mrefu sana.
Nchi za Tanzania na Oman zilishirikiana kikamilifu
kuwatia nguvuni wote waliohusika katika mkakati huu
wa kiuaji.
Maafisa wa uhamiaji walikamatwa kwa fujo katika
msako huo, huku wengine wakikutwa na hatia.
Wahusika katika mpango huu walifikishwa mbele ya
sheria, wale wa Tanzania walihukumiwa maisha jela
huku wale wa Oman wakihukumiwa kunyongwa.
Wakati haya yanatokea familia ya Rama pamoja na ile
ya Aneth kwa pamoja walikuwa wanasheherekea upya
harusi ya watoto wao hawa.
Watu baki kadhaa akiwamo Nasra walijumuika pia
katika hili
Yaliyopita si ndwele ndo walivyosema!!
Geza kama kawaida yake, alipotea katika uso wa
wanadamu na kuendelea na maisha yake mbali kabisa
na jiji la Dar es salaam, hakuwepo hata katika ule
mgao wa zawadi kubwa waliyotunukiwa wote
walioshiriki katika kung’amua uozo huu wa miaka
kumi.
Sajenti Pilipili na Inspekta Zainabu walipandishwa
vyeo, huku IGP akirejeshwa kazini baada ya
kupelelezwa na kuonekana hausiki na hakujua juu ya
mwanaye kushiriki katika mkakati ule.
Umoja kati ya Oman na Tanzania ukazidi kukua
maradufu huku ulinzi ukiimarishwa zaidi ili tukio kama
hili lisiweze kutokea tena asilani.
Ile siku IGP anarejeshwa kazini alipokea ujumbe
kutoka katika namba mpya.
“Ujue hadi leo sijalipia zile bia pale baa
walipokunywawale mademu! Mtume Pilipili
anapafahamu wanadai kama elfu sita mia tano hivi!
Msalimie Zay B mwambie tutakutana tena”
Mtuma ujumbe hakuandika jina lake, lakini IGP
alijikuta anatabasamu.
“Vipi mkuu!” alihoji sajenti akiwa pamoja na IGP.
“Geza kanitumia ujumbe….”
Wakajikuta wanacheka kwa pamoja, safari hii wote
walikuwa wanamjua vizuri!
Na huu ndo mwisho wa riwaya hii ya Pumbazo.
Ni Tungo kutoka kwa mwandishi George Iron Mosenya,
tungo hii ni haikuwa na nia yoyote mbaya kwa jamii
yoyote ile.
Ikiwa kwa namna moja ama nyingine imevunja amani
ya nafsi yako.
Ninakuomba radhi!
 
Uwiiii, jaman mzaramo wewe!!!!!! Haya bana.
 
Ahsante sana, hasa nami nianze kazi maana zlikuwa zmelala
 
Back
Top Bottom