Riwaya: Pumbazo

Riwaya: Pumbazo

SEHEMU YA KUMI NA SITA

Majira ya saa mbili usiku akiwa anaambatana na watu
wawili wababe alirejea nyumbani.
Huku akamkuta mkewe akiwa mkiwa sana, akamsalimia
na hapohapo akamuulizia Aneth.
Mama akamtazama mumewe kwa muda na kisha akatoa
jibu lililozua tafrani katika kichwa cha mzee Fidelis.
Aneth alikuwa ametoweka na hajamuaga mtu yeyote
lakini ameacha ujumbe mfupi kabisa.
“SITAKANYAGA HAPA NA MAITI YANGU ITUPWE
JALALANI ISILETWE HAPA….Na kuanzia dakika hii
naitwa ANETH RAMADHANI JOSEPH.”
Mzee Fidelis alipigwa na bumbuwazi, wale watu
alioambatana nao walipojaribu kumuuliza
aliwagombeza na kisha kuwafukuzia mbali.
Wakaondoka huku wakijiuliza iwapo huyu mzee
amechanganyikiwa ama la!
______

MJI ulikuwa tulivu tofauti na siku nyingine, familia
ilishazoea ile tabia ya baba yao kufoka kila mara, iwe
anakuita ama likitokea kosa umefanya yeye anafoka
tu!
Uzuri alikuwa anafoka tu lakini alikuwa na mkono
mzito sana hakudiriki kuadhibu watoto wake hovyo,
alikuwa ni mtu wa mikwara tu. Mkiwa mezani mnakula
lazima atafute sababu ya kumgombeza walau mtoto
mmoja!
Ukila taratibu atakwambia unakula kama upo harusini,
ukila upesiupesi atakuuliza unakula harakaharaka
unawahi wapi.
Ukinawa mikono wa kwanza anakukaripia kuwa hauna
adabu unanawa kabla ya wakubwa, ukisubiri wakubwa
wanawe ndo wewe unawe anakukebehi kuwa utaratibu
huo ni wa kizamani yeyote anaweza akaanza kunawa.
Mkewe alikuwa anaingilia kati mara moja moja huku
akimtupia kijembe mumewe kuwa vita ya Kagera
ilimwathiri akili anajiona yupo sawa kwa kila
anachofanya.
Akishaambiwa hivi na mkewe anasusia chakula anaenda
chumbani, wakikutana huko wanayamaliza.
Japokuwa hali hii ukiisoma unaweza kudhani
ilisababisha familia hii isiwe na furaha,. Lakini tabia
hii ilifanya furaha itawale nyumbani na upendo
kuimarika zaidi miongoni mwa wanafamilia.
Lakini siku hazifanani!
Siku hii ukimya ulitawala sana, vilisikika vijiko
vikigombana na mabakuli na sahani, na midundiko ya
matonge kuanzia yanavyoshambuliwa na meno
mdomoni kisha kupita katika koromeo na kudondoka
tumboni.
Ukimya huu ukasababisha mama azungumze ili
kumchokonoa baba mwenye nyumba..
“Naona leo Pilipili imetiwa ndimu nyingi! Imeishiwa
makali?” usemi huu wa mama ukasababisha familia
nzima wavunje mbavu kidogo, kasoro mlengwa wa
kijembe hiki yeye alikuwa mtulivu.
Tofauti na matarajio ya wengi kuwa ataanza kugomba
kama kawaida yake au kurudisha kijembe kikubwa zaidi
haikuwa hivyo!
Kimya kikatanda tena!
“Afande Pilipili, unaumwa?” mkewe akamuuliza
kimasihara. Badala ya kujibu, baba mwenye nyumba
ambaye nyumba yake pia ilimwita kwa jina la utani la
Sajenti Pilipili akasimama badala ya kuelekea chumbani
akaelekea dirishani na kusimama akawa anatazama
nje.
Hapa sasa hayakuwa masihara tena mkewe
akamwendea na kumkokota wakaenda chumbani.
Tayari alishagundua kuwa ubavu wake haukuwa sawa
kabisa.
Utani kando, mapenzi yakachukua nafasi.
Ni huko chumbani ambapo Pilipili alimweleza mkewe juu
ya jinamizi la Rama linavyomsumbua na kumkosesha
raha. Akaelezea ni kiasi gani yule kijana asiyekuwa na
hatia alivyoingia katika domo la kifo kimasihara na
hapo akailaani kauli ya mkuu wake wa kazi ya kuamua
Rama aende Oman kwa oparesheni ya kumsaka Vonso.
“Sidhani hata kama Rama alitakiwa tu kulijua hilo
jina, ni jina zito sana kuliko umri wake! Sijui tu nini
kilitokea kati yetu…” akasita akamgeukia mkewe.
“Hivi unajua ameacha mke na mtoto mdogo… katoto
kadogo kabisa.”
Mkewe akataka kusema neno sajenti akaendelea,
“Halafu mkewe naye tumemsotesha rumande kizembe
tu!”
Mkewe akaguna kisha akamuuliza swali moja. “Lakini
mume wangu mbona Oman inasdifika kwa sheria kali
inawezekana vipi mtu kuuwawa kizembe hivyo!”
“Ni kweli sheria zao ni kali haswa lakini ukali wa
sheria hauzuii mtu mmoja kumtoa roho mwenzake kwa
sababu zisizojulikana.
Mkewe alimfariji na kumpa maneno ya kumtia nguvu
upya kabisa. Walau faraja hii ilimpa nguvu za
kutabasamu kidogo, Sajini Pilipili.
Kisha mkewe akabadili mada ili kumpunguzia mumewe
mzigo wa mawazo.
Wakati wanaanza kubadili mada, mlango wa chumbani
uligongwa mama Yohana akaenda kufungua.
Akamsikiliza mgongaji ambaye alikuwa ni mtoto wake.
“Baba Yohana, kuna ugeni….” Mkewe akamueleza kwa
utulivu huku akionekana kuchukia ugeni huo wa usiku!
Sajini akasimama na kutoka nje ya chumba chake.
Alipotoka tu akakutana na mwanamke akiwa
amesimama akibembeleza mtoto wake aliyekuwa
analia.
Sajini akashtuka vibaya mno!!
“Mama Jose!” akaita.
“Samahani kwa kukutembelea usiku huu imenibidi tu,
nahitaji kuzungumza nawe.” Alijibu mama Jose.
Sajini akajivuta na kutoka nje, mama Jose akamfuata
nyuma. Huku mkewe akiwasindikiza kwa macho yenye
viulizo vingi.
Walizungumza mengi sana huko nje, mama Jose
akajieleza.
“Sina pa kwenda Sajini, sina yeyote wa kunisikiliza, si
upande wa nyumbani kwetu wala upande wa mume
wangu… tafadhali naomba ufanye kitu.” Akasita
akamgeuza Jose ambaye alikuwa bado hajasinzia.
“Sajini, baba yangu… baba aliyenizaa mimi…
amempiga Jose kibao kwa nguvu zake zote… mwone
mwanangu asiyekuwa na baba anavyoanza
kuteseka…” akataka kuendelea koo likagoma kutoa
sauti, akajaribu tena kuzungumza akajikuta
anaangua kilio cha uchungu!
Kumwona mamaye analia, Jose naye akaanza kulia!!
Sajenti alijiskia vibaya sana na kuzidi kuwa upande wa
hatia! Alijiona amepambwa na damu mikononi mwake.
Ili kukabiliana na hatia hii, akaona ni heri amsaidie
kadri awezavyo mama Jose.
Akaamini kuwa msaada wake wa dhati pamoja na
ukaribu wake kwa Mama Jose utafuta kidogo
kumbukumbu ya Rama kupoteza maisha nchini Oman.
Sajenti Pilipili akachukua maamuzi ambayo yalimwaga
maji ya ubaridi katika moyo wake wa nyama uliokuwa
umeganda kwa sababu ya fikra juu ya Rama.
Baba wa mtoto mchanga!!
Kwa siku ile Mama Jose alilala pale nyumbani, siku
iliyofuata sajini aliwaagiza vijana wake wakatafuta
chumba na kuweka vitu vya msingi, baada ya siku tatu
mama Jose akaanza kuishi katika nyumba ya kupanga.
Mara kwa mara Sajini Pilipili alikuwa akienda kumjulia
hali.
Baadaye akamfungulia duka la vipodozi jirani na
nyumba aliyokuwa amempangishia!
Sajini Pilipili akabaki kuwa ndugu pekee wa Mama Jose.
Jose akaanza kumtambua sajini kama baba yake.
Rama akasahaulika!!
Wakati Rama anasahaulika Sajini kwa amri ya mkuu
wake wa kazi akatakiwa kufanya mawasiliano na Zay
B ili mara moja rejee nchini Tanzania akatulie
nyumbani kwao Zanzibar!
Na akatakiwa rasmi kulifunga jalada la kumsaka
Vonso na kampuni yake lililokaa wazi kwa miaka zaidi
ya kumi bila muafaka.
Ni simu hii ya kutoka Tanzania kwenda Oman iliyozuka
balaa jipya.
Majibu yakaelezea kuwa kuna wawakilishi rasmi
kutoka Tanzania walifika Oman katika makazi
aliyokuwa akiishi Zay B na kuelezea kuwa anatakiwa
mara moja nyumbani Tanzania, watu hao walikuja na
nyaraka zote za kiofisi kuthibitisha kuwa wapo pale
kihalali.
Watu wale wakatokomea pamoja na Zay B na mizigo
yake michache.
Walikuwa na tiketi ya ndege kabisa maalumu kwa ajili
ya Zay B.
Sajini Pilipili alichoka, lakini Inspekta generali wa
polisi alichoka zaidi.
Ilikuwa ni vita mpya!!
Vita dhidi ya watu wanaojulikana lakini wasiojulikana
kwao!!
IGP akaingia katika Pumbazo na kwa ghadhabu kubwa
sana ya kuona kuwa adui yao anawafanya kama
watoto wadogo. Akachukua simu yake akatafuta
namba aliyokuwa anaihitaji.
Akapiga na kusikiliza kwa muda, ikapokelewa na mtu
aliyekuwa kilabuni analewa, alizungumza kilevilevi.
IGP akakata simu huku akitokwa na tusi zito haswa
kwa lugha ya kifaransa.
Akaitazama simu ile kisha akalisoma lile jina katika
simu.
GEZA ULOLE!!
Akamalizia kwa kulitafsiri.
IGA UFE!
Na mwisho akaponyokwa na kicheko kisichokuwa
kichekesho!
_____

RAMA aliendelea kufanya kazi ngumu huku akipata
chakula kidogo tofauti na kazi ile iliyojaa suluba, siku
mkurugenzi akiwepo wanapewa chakula kizuri sana na
hawafanyishwi kazi nyingi sana.
Rama akaanza kujifunza kitu, kuna jambo lilikuwa
haliendi sawa hata kidogo katika chimbo lile. Akahisi
kuna manyanyaso ambayo wanafanyiwa lakini ni
nyuma kabisa ya upeo wea mkurugenzi.
Akafikiria kushtaki lakini mkurugenzi yule alikuwa
hazungumzi kiingereza wala Kiswahili.
Hapa sasa Rama akalazimika kubadili mfumo wake wa
kuishi maisha ya kimyakimya, akaamua kubadilika na
kuunda urafiki na wenzake katika geti nambari nne
ambao wote kwa pamoja walifahamu fika kuwa hatma
yao ni kufanya kazi kila siku na ili utoke mle ndani
lazima uwe umekufa!
OMANI haikujua kuhusu hili, Tanzania haikujua
kuhusu hili, Afrika ilikuwa gizani na dunia haikuwa na
huu ufahamu.
Walifahamu wachache walionufaika na mradi huu.
Katika kuunda urafiki na kuanza kuzungumza na
wenzake hasahasa wakati wa chakula… hatimaye
walianza kutambuana kwa majina na nchi
wanazotoka.
Rama akakutana na Latipha!
Binti kutoka Kenya ambaye mara yake ya mwisho
kuishi Afrika alitokea nchini Tanzania. Ni huyu ndiye
aliyemsimulia Rama na kuanza kumfungua akili yake
walau kidogo.
Alikuwa anamsimulia Rama huku wakiendelea kufanya
kazi, haikuwa rahisi binti yule kuanza kumsimulia
Rama kwa sababu hakuamini kuna msaada wowote
anaweza kuupata, aliiona hatma ya wote katika ficho
lile ni kifo cha kifedhuli.
Lakini ule ukarimu wa Rama kumsaidia yule binti kazi
walizokuwa wanapewa hatimaye Latipha aliamua
kumsimulia rama. Na alimsimulia haya huku akimpa
angalizo kubwa.

LATIPHA
Naitwa Latipha… Latipha Kasim Sadiki, nina miaka
ishirini na moja sasa. Nitakufa kabla sijafikisha miaka
ishirini na mbili, nitakufa kwa mateso makali sana,
nitakufa na kutupwa kama mzoga.
Mama yangu hatajua, wala ndugu yangu yeyote.
Mchwa na wadudu watakaonitafuna pekee ndio
watatambua kuwa mimi ni mfu.
Nilifanya kazi mbalimbali jijini Mwanza nchini
Tanzania, kwa asili mimi ni mkikuyu kutoka Kenya.
Nilienda Tanzania kutafuta maisha nikipitia njia ya
Mombasa kisha Tanga.
Nimefanya kazi katika mgahawa mdogo Mwanza,
kipato kilikuwa chini na dharau kubwa kutoka kwa
wateja nilizizoea.
Maisha yangu yalipata Nuru tena baada ya kukutana
na kijana mstaarabu sana anayeitwa Eric Mlewa….
Awali nilidhani kuwa ananitaka kimapenzi lakini siku
moja aliniita kando na kupeleleza juu ya mshahara
wangu, nikamjibu akastaajabu sana na kisha
akanieleza iwapo nipo tayari kufanya kazi hiyohiyo ya
mgahawa lakini nje ya Tanzania, nikamjibu nipo tayari
lakini sio nchini Kenya.
Akanieleza ni Oman, akasema mshahara ni mara kumi
ya ule niliokuwa napokea. Nilipokea taarifa ile kwa
furaha lakini sikuamini kama itatekelezeka, ajabu
kijana yule alikeleza.
Mara nikapigwa picha za paspoti, mara pasipoti
ikakamilika.
Hatimaye ikawa safari, nakumbuka jina moja lilikuwa
linasemwa mara kwa mara lakini sikutilia maanani kwa
sababu ya ushamba wqa kupanda ndege lakini nilisikia
juu ya kampuni inaitwa VONSO kama sikosei… na hata
tulipofika Dubai nilisikia tenma kuhusu hiyo kampuni,
na Oman vilevile nilisikia.
Lakini baada ya kufika Oman tukapokonywa pasi zetu
za kusafiria, tulikuwa wane… tukapokonywa simu
zetu. Mimi na mwenzangu, wenzetu wawili hawakuwa
na simu.
Tulipofika Oman haikuwa kazi ya mgahawa wala hoteli,
ilikuwa ni kazi ya ndani ya ntyumba za watu.
Makabidhiano yao yalifanyika katika lugha ya kiarabu
na hakuna nilichoambulia asilani.
Kaka yangu, kazi ni kazi aidha iwe ya mgahawa ama
la! Lakini kilichosababisha mimi kuwa hapa sio ugumu
wa kazi bali ni changamoto katika ile kazi… ni
changamoto hizo zitakazopelekea mimi kupoteza
maisha… na nitakufa kabla sijatimiza miaka ishirini na
mbili……”
Latipha alisita kusimulia, akatazama mlangoni,
alikuwa anaitwa na yule msimamizi.
“Anaenda kunibaka…” alisema Latipha kwa sauti ya
chini. Rama akasikia kauli ile…….
Lakini angefanya nini angali yule bwana alikuwa na
bunduki katika kiuno chake??
Akasubiri sana Latipha aweze kurejea na kuendelea
kumsimulia ilikuwaje hadi akaingia katika chimbo hilo
la mauti…..
Lakini kamwe Latipha hakuwahi kurejea katika macho
ya Rama!
Alikufa binti yule!
Hakika alikufa akiwa hajatimiza miaka ishirini na mbili
 
SEHEMU YA KUMI NA SABA

Wakati Rama anasahaulika Sajini kwa amri ya mkuu
wake wa kazi akatakiwa kufanya mawasiliano na Zay
B ili mara moja arejee nchini Tanzania akatulie
nyumbani kwao Zanzibar!
Na hapohapo akatakiwa rasmi kulifunga jalada la
kumsaka Vonso na kampuni yake lililokaa wazi kwa
miaka zaidi ya kumi bila muafaka.
Ni simu hii ya kutoka Tanzania kwenda Oman iliyozuka
balaa jipya.
Majibu yakaelezea kuwa kuna wawakilishi rasmi
kutoka Tanzania walifika Oman katika makazi
aliyokuwa akiishi Zay B na kuelezea kuwa anatakiwa
mara moja nyumbani Tanzania, watu hao walikuja na
nyaraka zote za kiofisi kuthibitisha kuwa wapo pale
kihalali.
Watu wale wakatokomea pamoja na Zay B na mizigo
yake michache.
Walikuwa na tiketi ya ndege kabisa maalumu kwa ajili
ya Zay B.
Sajini Pilipili alichoka, lakini Inspekta generali wa
polisi alichoka zaidi.
Ilikuwa ni vita mpya!!
Vita dhidi ya watu wanaojulikana lakini wasiojulikana
kwao!!
IGP akaingia katika Pumbazo na kwa ghadhabu kubwa
sana ya kuona kuwa adui yao anawafanya kama
watoto wadogo, huku akilidhalilisha jeshi kakamavu
kabisa la polisi la Tanzania
IGP hakuwa tayari dharau hizi ziendelee huku raia
wakiumia akaamua kuingia vitani tena, hakukubali
kurudi nyuma.
Akachukua simu yake akatafuta namba aliyokuwa
anaihitaji.
Akapiga na kusikiliza kwa muda, ikapokelewa na mtu
aliyekuwa kilabuni analewa, alizungumza kilevilevi.
IGP akakata simu huku akitokwa na tusi zito haswa
kwa lugha ya kifaransa.
Akaitazama simu ile kisha akalisoma lile jina katika
simu.
GEZA ULOLE!!
Akamalizia kwa kulitafsiri.
IGA UFE!
Na mwisho akaponyokwa na kicheko kisichokuwa
kichekesho!
____
SIMU ya sajenti Pilipili iliita, ndo kwanza likuwa
amefika nyumbani kwake majira ya saa mbili usiku
akiwa anatoka katika uwajibikaji.
Ilikuwa simu ya mkuu wakewa kazi, ambaye muda si
mrefu walikuwa wamezungumza juu ya ukimya na
utata mpya juu ya afande Zay B. afande aliyesifika
kwa kuwa na shabaha kali atumiapo silaha na askari
pekee wa kike aliyekuwa amewiva haswa katika
mapambano ya ana kwa ana!
Sasa alikuwa matatani!
Mikononi mwa wale waliouondoa uhai wa Rama.
Sajenti alipokea upesi huku akiliita jina la mkuu wake
kwa kutangulisha heshima ya ‘mkuu’.
“Pilipili… nakutumia namba ya mtu, sijui alipo kwa
sasa lakini nadhani ni kumbi za starehe namuhitaji
sana tafadhali naomba umlete usiku huu huu. Sitoki
ofisini nakusubiri wewe nay eye. Narudia tena
nakusubiri wewe nay eye, usije mwenyewe Pilipili.”
Akamaliza kuzungumza akakata simu IGP.
Afande pilipili akabaki kulalamika mwenyewe akijiona
ameonewa sana kwa maelezo yale yasiyohitaji yeye
kujibu lolote.
Akiwa bado anaduwaa akatumiwa namba ya simu,
ujumbe ule licha ya kuwa na namba ya simu ulikuwa na
maneno ya ziada.
“ANAJIITA GEZA….”
Sajenti pilipili alikuwa na uchovu lakini angefanya nini
na sheria zinamlazimu kuwajibika masaa ishirini na
nne. Tena hapa ameagizwa na mkuu wake wa kazi
anayemzidi vyeo.
Sajenti akaishia kujilaumu mwenyewe huku akigeuza
na kutoka nje ya nyumba yake.
Akapiga simu katika kitengo cha siri, akajieleza shida
yake na kuitaja ile namba ya simu akapewa maelekezo
ni wapi inapatikana.
Sajenti akatabasamu baada ya kusikia kuwa mwenye
ile namba yupo Magomeni Mikumi!
Alifurahi kwa sababu muhusika hakuwa mbali sana
kutoka eneo alilokuwepo yeye la Mwembechai!
Akaondoka hadi lile eneo akapiga tena simu
akaelekezwa zaidi, kisha wale waliokuwa
wanamuelekeza wakapiga simu ile inayotakiwa huku
Pilipili akiwa makini kabisa kutazama ni nani
atakayepokea.
Mtego wake wa kwanza kabisa aliuweka katika ukumbi
maarufu wea lango la jiji.
Kweli!? Akawa sahihi , akamuona mwanaume mmoja
asiyekuwa wa kisasa sana akinyanyua simu yake
kilevilevi na kuanza kuzungumza na upande wa pili.
“Nimemuona tayari!” sajenti Pilipili akautaarifu
upandewa pili kisha akamfikia yule mtu na kuketi
jirani naye kana kwamba hana habari naye.
Swali likaja, ataanzaje kumkamata? Je amtie pingu
ama azungumze naye… kistaarabu na kuondoka naye.
Utata huu ukamfanya awasiline na mkuu wake wa
kazi.
“Hebu nipatie niongee naye…” IGP alisema na mara
Pilipili akakurupuka kama mwendawazimu akamfuata
yule mwanaume. Akampatia simu!
Yule bwana badala ya kupokea akambwatukia pilipili!
Pilipili akajirekebisha akamweleza kuwa kuna mtu
anataka kuzungumza naye.
Hapo ndipo akaipokea.
“Geza ni mimi…ni mimi Sungura Sungura! Nakuhitaji
sana tafadhali…” alizungumza IGP.
Wkati IGP akitarajia Geza atajiuma uma ama
kushtuka haikuwa hivyo Geza akajibu kama
anayejiuliza.
“Sasa leo vipi kuhusu mademu wangu sasa, halafu
wako wawili.” Aliuliza Geza kwa sauti thabiti kabisa
bila wasiwasi.
“Mademu… ndo kina nani?” alihoji IGP.
“Nina mademu wawili…. Wasichana nawapa pombe nan
do kwanza tumeanza! Au nije nao!?” alihoji Geza
kiumakini kabisa.
Mazungumzo ya Geza Ulole yakamuacha hoi Pilipili,
hakuwahi kumjua kiumbe huyu hata siku moja sasa
anashanga aanavyoongea na IGP kama mtu na rafiki
yake ambaye wanataniana kupita kiasi.
Simu ikakatwa Geza akamgeukia Pilipili huku
akimkabidhi simu.
“Amekubali niongozane na mademu zangu.”
Akamweleza huku akisimama, akamshika mkono Pilipili
wakaondoka huku Pilipili akistaajabu mbona Geza
amesema anaongozana na wanawake lakini hajafanya
hivyo!
Loh! Ni vile tu alikuwa hamjui Geza vizuri!
Laiti kama angekuwa amewahi kukutana naye wala
asingehangaika na vituko vyake.
_____
MAONGEZI yao yalichukua muda mrefu, vibweka vya
Geza alivifahamu IGP lakini hivi havikusababisha
ausahau utendaji kazi wa raia mwema huyu ambaye
hapendi makuu lakini ukitaka ugombane naye basi
mnyime haki yake, amewahi kuwafikisha pabaya watu
mbalimbali waliokuwa wanaihujumu serikali na wala
hakuwahi kudai malipo.
Pia aliwahi kuwa MCHUMA JANGA pale aliponunua kesi
isiyomuhusu kabisa akitokea kijijini nmkoani Mwanza.
Kesi aliyoisikia redioni yeye akaamua kufunga safari
hadi Dar es salaam ili kuutafuta ukweli.
Huyu ndiye Geza, mwanaume asiyekuwa na ndugu.
Anadai kwa mdomo wake kuwa ndugu yake ni maisha ya
kumsaka adui na kumwadabisha.
Sasa amesikia juu ya kampuni iitwayo VONSO ama si
kampuni bali mtu, ambaye anasadikika kujihusisha na
vitendo vya unyanyasaji lakini hajawahi kupatikana
shuhuda kusema juu ya hili.
Geza akatabasamu aliposhirikishwa juu ya hilo,
akaambiwa kuwa atashirikiana kiukaribu kabisa na
Pilipili.
“Kwa hiyo na mimi nitapanda pipa kabisa kwenda Oman
doh! Nitafurahi siku hiyo… nikaone sasa watoto wa
kiarabu ikiwezekana sasa naoa hukohuko.” Geza
alizungumza huku akitabasamu.
Pilipili akashtuka akidhani yule bwana amerukwa na
akili.
IGP akamwambia ye akitaka kuoa aoe tu ila cha msingi
jibu kwanza lipatikane.
“We unajisemea tu kuoa unadhani wale mahari ni
mbuzi kumi na ng’ombe kama kwenu usukumani!” IGP
akarusha kijembe.
Akidhani kuwa amemuweza Geza, mara likamtoka jibu
Geza Ulole.
“Unadhani hii kazi nitaifanya bure, pesa mtakayonilipa
ndo hiyo nitatoa mahari! Lazima nioe mwarabu
nasema!”
IGP akakubali yaishe akawaaga wawili wale na
kuwasihi wafanye kazi kwa ushirikiano ili watoe
matunda mema.
Sajenti Pilipili alibaki ndani kwa muda kama wa dakika
moja wakati Geza akiwa ametoka nje tayari akiimba
nyimbo kwa kabila la kisukuma, hakuwa anaimba vizuri
lakini alionekana kufurahia sana.
Tutajuaje? Labda nd’o zilikuwa zinampandisha mori?
Acha aimbe bwana!
Huko ndani Sajenti Pilipili alimshangaawaziwazi mkuu
wake wa kazi kwa aina ya msaidizi aliyompatia,
alimchambua Geza haswa kwa kauli zake alizoziona
nzito lakini IGP akaziona ni nyepesi sana akawa
anatikisa kichwa tu.
“Tazama mkuu, nikitazama watu zaidi ya kumi
majasiri kabisa na machachari waliopambana katika
hili jambo kwa hiyo miaka kumi, tazama Shakir,
Nunda, Kazimoto, Vandame, Suzani gaidi la kike,
Inspekta Macha…. Wote hawa mkuu kweli kuna hata
mmoja ambaye anaweza kulinganishwa na huyu jamaa
yako sijui Giza……” hapo sasa IGP akampungia mkono
kumzuia asizungumze kwa sababu alimwona anayevuka
mipaka.
“Anaitwa Geza, zingatia jina lake” akasita
akamtazama kisha akamrushia swali.
“Hao wote uliowataja zaidi ya kuwasoma katika
mafaili umewahi kufanyanao kazi?” lilikuwa swali la
ghafla ambalo jibu lake ni HAPANA……
Pilipili hakujibu!
“Simama uende.. tazama unayefanyanaye kazi na sio
uliowasoma kwnye makaratasi waliojazwa sifa
kedekede angali walikuwa waoga wa kutupwa
waliojivika ubabe wa kuminya wafungwa kumbe wao
wakifinywa kidogo tu wanataja hadi rangi za nguo zao
za ndani…..” alizungumza kwa utulivu IGP.
Utulivu ule ulimaanisha kuwa anakaribia
kukasirika….. na lile jibu alilotoa lilikuwa tusi kwa
Sajenti Pilipili, anayesifika kwa kuminya wafungwa!!
Sajenti akasimama, akapiga saluti na kutoka nje!!
Huko nje Sajenti alimkuta Geza sasa hakuwa akiimba
tu, bali alikuwa anacheza ngoma anayoijua yeye huku
akijipigia makofi mwenyewe.
Sajenti alivyofika Geza naye akaimalizia ngoma yake
kwa vigelegele.
“Mwanamashimba namkumbukia hapa!” Geza
akazungumza akiwa anamwambia Sajenti. Sajenti
hakujibu akampuuza na kuzidi kuamini kuwa amepewa
mgonjwa wa akili afanye naye kazi nzito.
Kwa mara ya kwanza lile wazo lililopita kichwani mwa
Rama kuwa amegeuzwa chambo, sajenti naye akawaza
hivyo!!
“Mi nakwenda nyumbani kulala, tutakutana kesho
tuone tunapoanzia..” alizungumza kivivu huku akitaka
kuondoka.
Geza akaduwaa na hakumwacha hivihivi aende bila
kumtolea uvivu. Sasa hakuwa na masihara hata
kidogo. Akamdaka mkono, Sajenti akauhisi ule
ukakamavu katika mikono ya bwana huyu ambaye
alikuwa haelewekieleweki.
“Tumezungumzia hapo ndani kuwa dada zetu
wanakufa tena vifo vya kifedhuli, tumezungumzia kifo
cha afande Rama kijana mtiifu aliyekufa kwa sababu
zisizokuwa sababu, bado mmesema sijui afande
Zainabu naye yupomatatani… halafu wewe unaenda
kulala. Hivi mnatania mliyokuwa mnasema ama
mnamaanisha!?” Geza alihoji akiwa anamkazia macho
Pilipili.
Kijasho chembamba kikamtoka Pilipili.
Akataka kutoa hoja yoyote ya kujibu lakini akakosa la
kusema. Hakutarajia shambulizi lile la ghafla kutoka
kwa mshirika wake.
Geza akawa mshindi!
Pilipili hakurudi nyumbani kwake, wakaenda hadi
nyumbani kwa Geza Ulole.
Kalamu na karatasi mezani, Geza na Pilipili kazini!
Usiku ule ulizaa matunda ya awali kabisa.
Pilipili alirejea nyumbani kwake asubuhi huku akikiri
kuwa Geza Ulole ni kichwa kingine cha aina yake kati
ya vichwa alivyowahi kukutana navyo.
 
SEHEMU YA 18

UCHANGANUZI wa Geza Ulole katika lile karatasi
walilolitenga pale mezani ulikuwa uchanganuzi
yakinifu haswa uliokuwa na viulizo vingi sana ndani
yake.
Geza alielezea mashaka yake juu ya waziri wa mambo
ya nje ama kiongozi yeyote yule wa ngazi za juu
katika idara ya uhamiaji.
Geza akaenda mbali zaidi na kusema kuwa kama
hawapo katika hisa za kampuni hiyo isiyojulikana basi
wanapokea rushwa kubwa ili kurahisisha safari hizi
batili.
Hapa alikuwa anazungumza huku akiitazama picha ya
hayati Hajrati ambayo ilikuwa na zile jumbe za ajabu
ajabu nyuma yake zikiwa katika lugha ya kiarabu.
“Nautazama urembo wa huyu binti, kisha nasimama
mimi kama mwanaume kamili kabisa… hivi msichana
mrembo kama huyu akiniletea jeuri unadhani adhabu
yake nini?” aliuliza akamtazama Pilipili. Kisha
akamalizia kwa kutoa jibu mwenyewe.
“Nambaka huyu…. Na nikishambaka mara moja si
nitanogewa basi namgeuza kifaa changu cha
starehe… hauhisi kuwa yawezekana huyu binti
yalimkuta hayo….” Akasita akaitazama tena picha ya
Hajrati. Kisha akamtupia swali Sajenti Pilipili.
“Umesema alikuwa na pacha wake… na aliondoka
kwenda kufanya kazi nje ya nchi akiwa bado binti
kigoli….” Hakusubiri jibu akaendelea.
“Hapa nafumba macho na kumtazama huyu binti
alipokuwa kigoli alikuwa anavutia kiasi gani,
mwanaume kikawaida anataka vinavyovutia.”
Akaendelea kuzungumza mengi kisha akamuuliza
sajenti kuna kesi ngapi kama hizo za mabinti kupotea
baada ya kuondoka kwenda kufanya kazi.
Sajenti akafungua bahasha yake na kumkabidhi Geza.
“Anna miaka kumi na sita, Dorika miaka tisa,
Anastazia miaka ishirini, Lulu miaka kumi na nane….”
Akaishia hapo na kisha akaanza kukuna kichwa, na
hapo swali likamtoka. Swali zito kabisa lililokuwa na
maana kubwa kabisa.
“ Kwa nini wasichana pekee katika hii orodha?” aliuliza
swali hili kisha akasimama, halafu akamuuliza Sajenti
ni kazi zipi wanawake wa umri huo wanaweza kufanya
ili kujiingizia kipato.
“Kazi za ndani, kuuza dukani, kuuza baa…. Mi nadhani
hizo ndo kuu.” Alijibu Pilipili.
“Hilo la kuuza baa liondoe kwanza, maana si
umeniandikia kuwa Oman pana sharia kali sana. Sidani
kama nchi hiyo ipo tayari kuona watoto wadogo
wanateseka hadharani….! Alizungumza Geza.
Jibu lile likamkosha Sajenti, hapa akazidi kukiri
kimyakimya huku akimwomba msamaha katika nafsi
yake kwa kumfikiria Geza kama kichaa ama
mwendawazimu.
“Yote uliyoyataja ni kweli yanawezekana, lakini
naomba tufikirie juu ya mambo mawili tu, waarabu sio
wajinga waache kuajiri waarabu wenzao kwenye
maduka wakaajiri mswahili….. kwani hapa Tanzania
huwaoni? Wana umoja wa hali ya juu wa kubebana wao
kwa wao. Basi tushikilie mawili… ni kazi za ndani
pamoja na jingine kubwa kabisa ambalo litatuongoza…
kuna namna fulani ya kutumika kingono.” Geza
akasita na kuyaacha maneno yake yamwingie Sajenti.
Chumba cha Geza kilikuwa na mbu sana, walisikika
wakiunguruma na waling’ata haswa lakini sasa
Sajenti alikuwa amewasahau kutokana na maneno ya
Geza.
“Sasa Geza kwanini unataka tujihakikishie kuwa
mabinti hawa wanateseka katika utumwa wa ngono?”
aliuliza Sajenti kwa umakini kabisa.
“Unadhani ingekuwa ni kazi za ndani mtu amegoma
kufanya ndo wangemuua kama walivyomuua huyu dada
sijui Hajrati sijui nani majina ya kiarabu haya mi
sijui…” alijibu Geza.
Jibu lile likawapa uelekeo, kwa pamoja wakakubaliana
kuwa kuna msaada wanahitaji kutoka kwa IGP.
Walihitaji ruhusa maalumu ya kwenda uhamiaji na pia
kuonanana na wawakilishi wa waziri wa mambo ya nje.
Wakati wawili hawa wakianza rasmi harakati, huko
Oman Rama naye aliendelea kuitafuta kweli
itakayowatesa walioificha.
_____

RAMA ANASIMULIA.
ILIKUWA ni siku nyingine tena katika chimbo lile la
umauti, wenzangu walikuwa wanazidi kupukutika huku
wengine wapya wakiingia, watu walikuwa wamekata
tama sana na maisha na wengi hawakunijibu kwa
lolote nililotaka kuzungumza nao.
Wangeongea nini angali walikuwa wanajitabiria vifo
vyao?
Ndugu msikilizaji kifo kina dalili mbaya sana na
usiombe aliyepo pembeni yako anakufa kisha
unalazimishwa umbebe, umvue nguo zake na kisha
ukamtupe kama mzoga!
Hapa ndipo hofu ya kifo hutanda kwa kila mja!
Nilipokuwa mafunzoni JKT kambi ya Mafinga kuna
mwenzetu mmoja alipoteza maisha, watu tulidumu
katika hofu kwa majuma kadhaa kila mtu akijiona
kesho ni zamu yake kufa.
Sasa katika chimbo hili la mauti kila siku mtu mmoja
alikufa tena anakufa mnamuona anavyopambana
kuizuia roho isimsaliti na kuuacha mwili.
Nilikuwa nimeanza kuziona njia moja ama mbili za
kuweza kutoka katika chimbo lile, nilijua kabisa nikiwa
jasirinaweza kufika tena katika ile Oman halisi Oman
yenye sharia kali niwashtaki wachache hawa
wanaochafua jina la nchi, wachache wasiojua
umuhimu wa maisha ya wenzao bali utajiri na ufahari
wao.
Lakini kitu kilichonifanya nisichukue hatua ni kitendo
cha kuwaacha wenzangu nyuma huku nikijua wazi
kuwa watakufa tu!
Kibaya zaidi nilipotaka kuzungumza nao juu ya mpango
kabambe hawakuwa tayari kunisikiliza. Kwa mmoja
ama wawili waliozungumza walinisihi tu niachane na
maisha yao kwa sababu wao ni wa kufa tu!!
Majibu yao yalinikatisha tama, na hapa nikaamua
kupiga hatua mbele. Nikapiga goti kisha nikainama na
kusujudu nikamkabidhi Mungu kila kitakachotokea
mbele yangu.
Na hapa akili yangu yote nikaipeleka katika bomba la
maji ambalo hufunguliwa asubuhi kwa ajili ya kukinga
ili kusafishia vyuma vyao, kisha jioni kufungwa.
Kwa sababu nilikuwa nimeamua kujitoa muhanga
sikutaka kumshirikisha yeyote asiyetaka kuzungumza.
Usiku ulinikuta nikiwa macho, mahali tulipokuwa
tunalala tulichanganywa waume kwa wake. Nilimwona
bwana mmoja mweusi ambaye pia alikuwa msimamizi
katika chimbo hilo akimng’ang’aniza binti mmoja kwa
nguvu sana hatimaye akambaka.
Nilishuhudia kwa macho yangu kitendo kile, binti
alijaribu kupiga kelele lakini yule bwana hakujali
akaendelea na alichokuwa amekusudia.
Nilimtazama na kisha kuikariri sura yake mbaya
iliyojaa chuki!
Haikuwa mara ya kwanza kuona wakimbaka
mfanyakazi mwenzangu, lakini hii ya siku hii kwa
sababu tayari nilikuwa nimeamua kufanya kitu
nikamsubiri akolee!
Nikawa namsoma sura yake hadi akakolea na kujisahau
kama alikuwa anabaka akajiona yupo katika penzi
halali na hapo nikajirejea mafunzo tuliyopewa jeshini
ya kutembelea tumbo, nikatambaa hadi nikamkuta
akiwa amefumba macho akifurahia anachokifanya.
Nikamvuta nilipokuwa, na kabla hajaweza kusema
lolote nikamtandika ngumi kali katikati ya shingo.
Akabaki kukodoa macho asiweze kusema neno lolote,
nikamnyoonya akawa amelala kama wengine
walivyolala. Nikamdhibiti hadi nikahakikisha kuwa
amepoteza maisha, nikamvua nguo zake taratibu
kabisa akabaki uchi wa mnyama.
Ili nisiwaletee wenzangu balaa siku itakayofuata
nikafanya kama tulivyoagizwa.
Nikasimama na kuita jina la ALWATANI… wasimamizi
wote walipenda kuitwa hivyo.
Sijui kwa ulwatani gani waliokuwanao…
Alipoitika kiusingizisingizi nikamweleza kuna
mwenzangu amefariki.
Kama ilivyo kawaida yao akaniambia nikamzike.
Hilo ni kosa kubwa sana walilofanya.
Nikalibeba lile jinamizi na kutoweka nalo.
Nilipofika kule chumba cha maziko nikamtupa. Kisha
nikavaa nguo zake na moja kwa moja nikaelekea
katika bomba pana la maji…..
Kiunoni mwangu nikiwa na silaha ninayojua kuitumia.
Bunduki!
Hofu ilikuwa jirani yangu wakati wote, na nilikuwa
sawa kabisa kuwa na hofu kwani sikuchukua muda
mrefu katika bomba lile kabla sijaanza kukutana na
hekaheka!
Dunia ina mambo jama lakini haya mambo
ninayokusimulia omba yasikukute wewe!!
 
SEHEMU YA 19

Nilipotoka nje nikatazama mazingira halisi ya pale nje
ikiwa nitatoa kile kifuniko, basi kwa namna yoyote ile
maji yatatoka kwa kasi na kuzua balaa wale
wasimamizi wakigundua jambo hilo na huo utakuwa
nd’o mwisho wangu katika harakati za kutoroka na
badala yake nitaishia katika mikono yao watanitesa
sana na kuniua huku dunia ikiwa haijui lolote lile.
Sikutaka usiku huu wa matumaini upite hivihivi.
“Mwanajeshi kamwe harudi nyuma!!” niliikumbuka
kauli tuliyokuwa tunapewa mafunzoni.
Nami sikutaka kurudi nyuma, nikarejea tena hadi kule
walipokuwa wamelala wenzangu. Nikajikohoza kidogo
kisha nikamuita tena Alwatan na kumweleza kuwa
tumbo lilikuwa linaniuma sana.
Akaanza kunitusi sana, sikuchoka kumtia kero ili
atoke kule alipokuwa aje katika ukumbi wetu wa
kulala.
Mara nimwambie tumbo, mara nimwambie nimechoka
kuishi!
Kweli akaghadhabika akashuka huku akitokwa na
matusi mazito kiingereza na kiarabu.
Alipofika ukumbini akiwa hajajiandaa kabisa kwa
shambulizi nililolipanga alijikuta akisalimiana na
sakafu kisha nikatua juu yake, nikamkung’uta ngumi
tatu kali shingoni akakakamaa!
Ukitaka ushangae maisha tuliyokuwa tunaishi kule,
hakuna aliyejali kilichokuwa kinatokea wote walikuwa
wamejikatia tamaa ya kuishi!
Sasa niliuona uhuru zaidi, nikamvua na yeye nguo na
kumtupa kule ambapo walipatenga kwa ajili yetu pindi
tunapopoteza maisha!
Baada ya hapo nikaingia tena katika lile bomba, hapa
nikiwa na bunduki mbili katika himaya yangu. Zote
zikiwa na risasi!
Nilikifikia kile kifuniko na kukifungua kisha nikajiachia
maji yakanisukuma kwa kasi kubwa sana na kunitupa
nje, nilishtuka kiuno lakini kama nilivyosema nilikuwa
napigana ili ukweli huu uwafikie ninyi wasikilizaji na
wasomaji.
Maji yalimwagika kwa kasi kubwa sana hadi yalipokoma
pale ndani palikuwa kama bwawa. Maji haya
yaliwashtua baadhi ya mateka wenzangu, lakini
hawakuonyesha kujali, ni kama akili zao zilikuwa
zimepumbazika kupita kawaida hasahasa walipokuwa
wanautambua kuwa mwisho wao ni kifo.
Nikapenya tena na kuingia katila lile bomba nikaingia
katika chanzo cha maji yale!
Lilikuwa na tanki kubwa kiasi la maji, nikaingia na
kujikuta nikiwa napambana na giza nene sana, ombi
langu kwa muumba likiwa moja tu….
Aniepushe na wadudu hatari ambao kwa namna moja
ama nyingine wanaweza kuwa katika ile hifadhi.
Naam! Niliteseka narudia tena niliteseka sana lakini
kamwe sikuwahi kukata tama, lilikuwa ni giza nene
sioni mbele na wala sitaki kurudi nyuma tena.
Ndugu msikilizaji ukiamua kupigania jambo, kwanza
mtangulize Mungu kisha jiamini kuwa unaweza
kulifanya jambo uliloamua licha ya vikwazo
utakavyokutana navyo…. Na mwisho piga hatua mbele
na kamwe usikubali kurudi nyma.
Mimi Rama cha moto nilikiona, kila hatua niliyokuwa
namaliza ni afadhali kuliko ile niliyokuwa naingia!!!
Mbu wale sijawahi kukutana nao maishani ndugu
msikilizaji, na vile nilikuwa nimelowana walinipiga
haswa, na ni kama walikuwa wanaalikana!
,bu hawa wakanikumbusha siku ile nilipokuwa nahojiwa
na sajenti Pilipili kwa kesi isiyokuwa yangu kabisa.
Wakati namuwaza sajenti Pilipili na mateso aliyonipa
kabla ya kunitupa katika janga hili mara nikasikia
mchakacho fulani pale ndani, zilikuwa ni kama hatua
za kiumbe hai!
Mapigo ya moyo yakaanza kupiga kwa kasi sana, giza
lilikuwa nene mno na sikuwa naweza walau kubashiri
ni kiitu gani kile ndani ya lile tanki.
Je, ni mnyama mkali anajiandaa kunishambulia, ama ni
kiumbe hatarishi kinachonisaka?, ama ni wale walinzi
wamegundua hila ambayo nataka kuwafanyia na sasa
wanataka kunikwapua waniue kwa mateso makali?
Hofu ikachukua nafasi, nikajipapasa na kuitoa bunduki
moja….. lakini nitaielekeza wapi?
Hili lilikuwa swali gumu sana!
Nikatulia tuli huku nikingoja kile kiumbe kama
kitajaribu kushambulia basi na mimi nitashambulia
hapohapo, ila nilikuwa najiuliza kuhusu ile bunduki je
tayari imeandaliwa kutoa risasi? Maana nilikuwa
gizani na nilikuwa katika hofu kuu.
Kimoyomoyo nikamuomba Mungu ile bunduki iwe tayari
kwa ajili ya kufyatua ili adui yangu asiweze kuniwahi!
Nikiwa namwombea mabaya adui yangu mara nikasikia
tena hatua nyingine.
Adui yangu ananiona!! Nilijisemea.
Nikapiga hatua nyuma kwa kunyata.
Mungu wangu! Nikakutana na utelezi ukanivuta
nikapiga mweleka chini, bunduki ikanitoka na hapo
nikamsikia adui yangu akinikimbilia.
Nilitetemeka vibaya mno.
_______

NCHINI TANZANIA

SAJENTI Pilipili na Geza walikuwa wamepata Baraka
zote kutoka kwa IGP juu ya uhalali wao kutembelea
ofisi ya waziri wa mambo ya nje na pia ubalozini, pia
waliruhusiwi kufahamu mambo kadha wa kadha juu ya
mambo yanayotokea ubalozini na uhamiaji!
Katika mpango huu Geza Ulole alisimama kama
mwandishi wa habari wa kujitegemea.
Hawakuwa wawili katika safari hii, bali walikuwa
watatu.
Sajenti alikuwa hajaafikiana sana na mpango
aliousuka Geza ili kuupata mwanga wa tukio
wanalofuatilia lakini Geza alisimamia kile alichokiamini
na kisha akamsihi sajenti awe mtazamaji tu aone nini
kinatokea.
Walifika ofisi ya waziri wa mambo ya nje na Geza
akiwa kama mwandishi alihoji mambo kadha wa kadha
kisha akaingia pia yule binti waliyeongozana naye,
lakini hapakuwa na mabadiliko yule binti alimsalimia
waziri na hayakuonekana mabadiliko yoyote katika
sura ya waziri.
Kwa hapa wakawa wamegonga mwamba!
Safari yao ikaendelea, hatimaye wakafika uhamiaji.
Kwa sababu walikuwa na vitambulisho vya kuwaruhusu
kuingia bila kujalisha dharula yoyote eneo lile basi
ilikuwa rahisi sana kuingia.
Wakaingia wawili yule bintiakafuata nje.
Mazungumzo yao hayakupita hata dakika tano mara
yule binti akaingia mle ndani akiwa anatembea
upesiupesi.
Akafika na kumnong’oneza kitu Geza.
Geza naye akamnong’oneza sajenti, kisha wakaaga
na kuondoka wakidai kuna dharula.
“Alivyoniona amekodoa macho sana na akaangusha
bahasha yake…” alizungumza yule binti aliyejulikana
kwa jina la Nasra pacha wa marehemu Hajrati.
Geza akatabasamu kisha akamtazama Sajenti.
“Tumekaribia nusu ya safari yetu!”
Binti akaelekeza mahali alipoingia mtu yule.
“Nenda ukamdhibiti maana nikienda mimi mtaonota
maiti badala ya muhusika.” Geza alimweleza Sajenti.
Sajenti alimtazama kwa mshangao mkubwa sana Geza.
Lakini hakusema neno akaondoka na Nasra hadi katika
ile ofisi.
Wakaingia bila hodi.
La! Haula! Wakakuta watu watatu.
Mmoja kati yao akiwasimulia juu ya kukutana na
Nasra ambaye wote walimtambua kama Hajrati.
Kitendo cha wawili wale kuingia ghafla kikazua
tafrani.
Sajenti pilipili akalikumbuka swali aliloulizwa na Geza
wakati wa mpango huu.
“Hivi utachukua hatua gani ukikutana ana kwa ana na
mtu ambaye unaamini fika kuwa amefariki, na huenda
maiti yake uliyaona?”
Sasa majibu yalikuwa yanajionyesha wazi, wale watu
wote walikuwa wanamwogopa Nasra!
Wote wakijua ni Hajrati pacha wa Nasra yule
aliyepoteza maisha.
Sajenti akatoa kitambulisho chake na kisha
akawaweka chini ya ulinzi watu wale watatu.
Kwa sababu walijua walichokuwa wakikifanya
walijaribu kufanya kukuru kakara za hapa na pale
waweze kuchomoka katika mikono ya sajenti, na
mmoja wao alifanikiwa kupenyeza mlango kiasi cha
sajenti kuhisi kuwa amemponyoka.
Lakini alirejea mzima mzima ghafla akitua sakafuni.
Mara akaingia Geza!
“Nimemkosakosa teke aisee?” alisema Geza huku
akitabasamu.
Sajenti akabaki kuduwaa, lakini alianza kumzoea
Geza!
Unamkosaje mtu teke kisha anatua kama mzigo ndani?
Mpango wa Geza ukawa umenasa, watatu wale
wakaulizwa ikiwa wanamfahamu yule binti, wawili
wakakiri kumfahamu kwa jina la Hajrati mmoja
akaweka ugumu na kusema hajui lolote.
Huyu ndiye aliyeshughulikiwa ipasavyo hadi akasema
kila kitu alichokuwa anakijua.
Na jina lake aliitwa ERIC MLEWA!!
 
Mkuu ongeza vitu naona sasa tushapata mmoja aisee!!
 
Haaaa mkuuuu endiii kivipiii tusubirii ijayoo au ndio mwishoo kabisaaa ...mbona hatujapataa suruhishooo ra huyu rama ...kule kwenye shimooo...daaaa yanii hapaaa ndio Sanaa ya utunzi wa hadithi huniumizaaaa yaniiii duuuu
 
Back
Top Bottom