SEHEMU YA KUMI NA TATU
RAMA alisubiri kwa siku mbili zaidi ili aweze kusikia
kuwa anatafutwa.
Lakini haikuwa hivyo, siku zilikatika bila kuona dalili
yoyote ya matumaini.
Rama alijutia kila alichokifanya hadi kumfikisha hapo
gerezani lakini hakujutia kulibadili jina lake kutoka
lile la Ramadhani na kujiita Alexander ili kukwepa
rungu la kuadhibiwa kwa kosa la kunywa pombe ilihali
yeye ni muumini wa dini ya kiislamu nchini Oman jiji la
Muscat.
Laiti kama Rama angejitambulisha kwa jina lake halisi
angekuwa matatani zaidi na si ajabu angeweza
kupoteza uhai wake.
“Zay B atanitafuta kwa jina la Rama!” alijifikiria
akiwa ndani ya gereza na kutambua wazi kuwa hiyo
italeta utata mkubwa sana, kichwa kilimuuma na
hakuwa na yeyote wa kumpa msaada katika mazingira
yale.
Kuhusu kumtegemea Zay B hilo ama yeyote yule
anayemtambua kwa jina la Ramadhani alifuta kabisa
kichwani kwake ili asizidi kujiumiza kifikra.
Na hapo rasmi akajiandaa kisaikolojia kutumikia
kifungo cha miezi sita gerezani.
Tabasamu la karaha likamponyoka, kisha akajiita kwa
sauti ya chini jina lake jipya.
Alexander!
_____
GEREZA lilimpokea Rama katika namna ya kipekee,
alikuta makundi makuu matatu ya wafungwa katika
gereza lile huku kundi lililokuwa na nguvu sana likiwa
lile la waarabu, kundi dhaifu likiwa la wafungwa wenye
asili ya kihindi hawa walikuwa kama watumwa wa
waarabu. Na walinyenyekea haswa kila kilichosemwa
na wafungwa wa kiarabu…
Kundi la watu weusi lilikuwepo kama halipo, wafungwa
weusi walikuwa wachache sana hivyo Rama hakuweza
kutambua upesi ni maisha gani wanapitia katika
gereza hilo.
Waarabu wa Pemba hujuana kwa vilemba!
Hata weusi nao hujuana kwa rangi zao!
Rama alipoingia gerezani, wafungwa weusi wawili
pekee katika gereza lile walimpokea, mmoja alikuwa
mfungwa kutoka nchini Brazil anayengoja nchi yake
ifanye utaratibu wa kumrudisha nyumbani akatumikie
kifungo, na mfungwa mwingine alikuwa anatokea
Jamaica.
Mbrazil akiwa pale kwa kosa la kukamatwa na madawa
ya kulevya huku yule wa Jamaica akitumikia kifungo
kwa kukamatwa na misokoto ya bangi pamoja na
vitambulisho feki.
Kesi zao zilikuwa tofauti kabisa.
Lakini walau waliweza kuzungumza kiingereza na
kuelewana, japokuwa kwa shida.
Kitu kimoja cha msingi alichokigundua Rama ni kwamba
gereza lile lilikuwa linatoa huduma nzuri sana na
wafungwa walikuwa wanajaliwa sana. Kuanzia suala
la kulala hadi chakula.
Gereza lilitoa usawa lakini wafungwa kwa wafungwa
ndo walionekana kunyimana usawa.
Hali nzuri ya utulivu na ya amani aliyoitazama pale
hakutaka kuamini kuwa miezi sita yote patakuwa
hivyohivyo, aliamini kuwa wale wafungwa
wanaojifanya gereza lilijengwa kwa ajili yao ipo siku
wataanza ‘kumzingua’
Kweli baada ya juma moja kupita ndipo vitimbi
vikaanza kutoka kwa wafungwa wenye asili ya
kiarabu.
Wakati vitimbi hivi vikianza gerezani nchini Oman, huko
nchini Tanzania, kwa kauli moja wote waliofahamu
juu ya oparesheni iliyompeleka Rama nchini Oman
walitamka wazi kuwa Rama anasadikika kupoteza
maisha nchini Oman.
Waliyatamka haya katika kikao cha dharula
kilichomuhusisha pia mke wa Rama.
Bi Aneth akiwa na mwanaye Jose.
Tofauti na wengi walivyodhani kuwa mama Jose
atatoa kilio kikubwa sana hivyo wakawa wameandaa
namna ya kumfariji, lakini baada ya taarifa ile mama
Jose alitulia tuli akiwa na mwanaye mgongoni.
Kisha baada ya sekunde kadhaa akaangukia mezani
akitanguliza uso.
Na kisha akatulia zaidi.
Mama Jose alikuwa amepoteza fahamu!!
Sajenti Pilipili aliingiwa na mchecheto mkubwa haswa,
akachukua simu yake upesi na kuwasiliana na Zay B
ambaye alikuwa Oman.
Akamueleza kilichotukia nchini Tanzania baada ya
taarifa ile, kisha akamuonya juu ya habari ya Rama
kuingizwa katika oparesheni ile iishie kwao na isiende
mbali zaidi.
Hofu yao ilikuwa juu ya umoja wa mataifa, ukifahamu
juu ya jambo hili ambalo Rama amelifanya pasi na hiari
yake mwenyewe na kisha kumgharimu maisha yake.
Hali ilikuwa tete!!
Baada ya kuzungumza na Zay B, akampigia simu
inspekta jenerali wa polisi na kumweleza hali halisi.
“Pilipili nilikuonya lakini….” Alizungumza kimalalamiko
kisha akakata simu bila kusikiliza lolote kutoka kwa
Pilipili.
Hili nalo likamvuruga zaidi Inspekta Pilipili, akaanza
kuona dalili ya kuachiwa jumba hili bovu kumuangukia
yeye peke yake.
Inspekta jenerali alikuwa anajitoa kimyakimya!
Pilipili akabaki kuduwaa, akifikiria walivyoshirikiana
vyema katika maamuzi haya baada yay eye kupeleka
wazo…. Sasa anageukwa.
Pumbazo!
____
ILIKUWA ni siku tulivu kabisa baada ya wafungwa
kufanya shughuli za hapa na pale kisha kupata chakula
cha mchana, Rama akiwa na mfungwa kutoka Jamaica
wakipiga soga, mara mfungwa wa kiarabu aliwaendea
na kuwasemesha kiarabu.
Hakuna aliyeelewa!
Kwa mara nyingine tena Rama akamkumbuka ustadhi
Karimu ambaye alikuwa mwalimu wake wa madrasa,
kitendo cha kuzikimbia zile mboko za madrasa sasa
kikawa kinamgharimu asiweze hata kulinasa neno
moja la kiarabu. Ustadhi Karim licha tu ya kufundisha
maandiko tukufu,lakini pia alikuwa akiwafundisha
maneno mawili matatu ya kiaerabu nje ya maandiko.
“Unazungumza nini we jamaa?” Rama naye akamuuliza
Kiswahili, kisha akataka kuendelea kuzungumza zaidi
Kiswahili akagundua kuwa hata yule mjamaika hakuna
anachoambulia.
Kitendo cha kuzungumza kiswahuli kikamfanya yule
mwarabu amtolee macho, kisha akapaza sauti
akiendelea kuzungumza kiarabu.
Punde yakaingia mapande ya watu wawili, ni wafungwa
Rama alikuwa akiwafahamu.
“Wamesema waarabu tunanuka!!” sasa alizungumza
kiingereza yule bwana.
Rama na yule mjamaika wakagutuka, mjamaika
akaingiwa hofu zaidi. Bila shaka alikuwa anafahamu
fika usumbufu wa wale watu waliofanya gereza kama
la kwao.
Bila kuuliza swali lolote wakawaamrisha Rama na
mjamaika wapige magoti.
Mjamaika akaenda chini Rama akahoji kulikoni!
Hiki ni kitu ambacho waarabu wale hawakutaka
kusikia, wakachukizwa na ukaidi wa Rama.
Mwarabu mmoja akamtandika konde la usoni, lakini
halikumuingia vizuri Rama aliyewahi kurudi nyuma.
Hapo sasa wafungwa wengine walianza kusogea
kutazama kinachojiri!
Jela jela tu! Huwa inafikia kipindi hata maaskari jela
wanaacha gomvi kama hizi zitokee wajionee sinema za
bure!!
Kuona Rama amemkwepa akamfuata akirusha makonde
mfululizo kizembe.
“Sitaki kupigana na wewe bila sababu jamaa…” Rama
akazungumza Kiswahili maksudi!
Hawakumuelewa zaidi aliwapandisha hasira!
Rama alikuwa hajanyanyua mkono wake hata mara
moja kurusha ngumi, alitambua kuwa wao walikuwa
wachache sana wenye rangi nyeusi na tayari aliuona
ubaguzi wa waziwazi hivyo kujitia kurusha ngumi ni
kujitafutia balaa.
Rama akawa upande wa kufyata! Hakurusha ngumi….
Lakini hili halikumfanya mwarabu amuache, sasa
walikuwa wawili….. wote wakitaka kumkaribisha Rama
kwa kipigo gerezani ili awaheshimu.
“Nitawaumiza jamani achene…” akazungumza
kiingereza, sasa hakurudi nyuma bali alisimama imara.
Maneno haya ya kishujaa yakawashangaza wale
waarabu.
Wakajaribu kuyapima kwa vitendo.
Askari mkakamavu kutoka Tanzania aliyeacha kazi hiyo
kwa sababu ya kuogopa ushirikina akasimama imara
akakunja ngumi.
Kikazuka kivumbi cha hali ya juu.
Ebwana wee! Waarabu wana ushirikiano jama….
Alipoweza kuwapasua wale wawili kwa ngumi
motomoto, wale wafungwa wengine wakamfuata ili na
wao waweze kumkabili.
Alipambana katika maana halisi ya ule usemi wa
‘kupambana kiume’
Mwishowe umoja wa waarabu ukamwangusha chini,
askari wakaingilia kati Rama akiwa hoi akivuja damu.
Ushujaa wake siku ile ukazua gumzo gerezani, na hata
alipopata nafuu na kurejea tena gerezani wengi
walikuwa wanamuogopa na hakuna aliyemtikisa.
Alikumbuka kuwapa onyo huku akiwa bendeji,
akawaeleza kuwa nchini Tanzania aliua samba wawili
kwa mikono yake mwenyewe hivyo wakimgusa tena
ataua wawiliwawili.
Licha ya umoja, waarabu ni waoga pia.
Japokuwa ulikuwa ni mkwara, wakafyata!!
Mkwara ule ukapenya hadi nje ya selo kupitia wale
wafungwa waliomaliza muda na maaskari jela
walioamua kuzishirikisha familia zao na marafiki pia.
Hatimaye zikafika mbalizaidi sifa zile.
Baada ya mwezi mmoja wa kutumikia kifungo, kwa
mara ya kwanza Rama ama Alexander kwa pale
gerezani akapata mgeni.
Mgeni aliyemtambua kwa jina la Alexander.
Maajabu, jina feki kisha unapata mgeni anakutambua
kwa jina hilo??
Rama akamsikiliza kwa makini, yule bwana alikuwa na
nia ya kumsaidia Rama ili aweze kuwa huru.
Akaelezea kuwa yeye ni muislamu na ni mtanzania,
ameguswa na kitendo cha Rama kufungwa jela kwa
kuvunja sharia asizozijua!
Alikuwa ni ngozi nyeusi na aliongea lugha ya Rama!
Rama akafarijika na kukubaliana na yule bwana
aliyeahidi pia kumrejesha nchini Tanzania.
Lakini kigezo cha Rama kuukubali msaada huu ni
kwamba alihitaji hatua zifanyike za yeye kukutana
kwanza na mwenyeji wake wa nchini Oman!
Akawatajia Zay B!
Yule mgeni akamweleza kuwa hilo halina tatizo.
Baada ya siku tatu Rama akatembelewa tena….
Mbele yake alikuwa ni yule mgeni akiwa ameambatana
na Zay B, yule mwanadada askari wa kizanzibar Nchini
Oman!!
Zay B hakuzungumza kabisa bali alimpungia tu mkono
Rama kwa muda mrefu huku akionyesha majonzi ya
waziwazi.
Rama akatambua kuwa Zay B anamuonea huruma kwa
uwepo wake gerezani.
Kwa siku hii hapakuwa na mazungumzo mengi, Rama
akakubali kiroho safi kabisa ule msaada.
Msaada kutoka kwa mgeni anayezungumza Kiswahili!
Alikuwa amedumu gerezani kwa mwezi mmoja na siku
kadhaa.
Akaachiwa huru kabisa…. Asijue wale waliomsaidia
walikuwa na nia gani.
Alipoivuta hewa nje ya gereza kitu cha kwanza
kilichokuja katika akili yake ni Vonso!
Akaapa kwa kila majina aliyojua kuwa anajitoa katika
msako huo asioujua, akafikia maamuzi magumu ya
kwenda ubalozi wa Tanzania na kuelezea kwa kina
tukio lake ili aweze kusaidiwa!
Hiyo ilikuwa ni azma yake ya kwanza kabisa katika
uhuru ule.
Alibaki na hatihati iwapo amshirikishe Zay B ama
ajichukulie maamuzi ya kibinafsi!
Akaweka kituo katika wazo lile na kujipa muda zaidi
wa kufikiri!
Waliingia katika jumba la kifahari, hakujiuliza sana
juu ya jumba lile kwa sababu Muscat kuna majumba
mengi zaidi ya kifahari zaidi ya lile, geti likafunguliwa
wakapita, likafunguliwa na geti la pili, hatimaye geti
la tatu likafunguliwa, na hapo palikuwa kama ukumbi.
Rama akashtuka ghafla anasukumwa kwa nguvu sana,
kwa sababu hyakutarajia kitendo kile akajikuta
anapiga mweleka chini, kabla hajafukurukuta
alifungwa kamba kwa nyuma. Kisha kamba ile ikaanza
kuvutwa na kitu kisichojulikana ili kumnyanyua Rama,
kamba ile haikuishia kumnyanyua ikazidi kumvuta juu
katika namna ya kumnin’iniza.
Hapo sasa Rama alianza kupiga mayowe. Lakini wale
watu waliomfunga kamba hawakujali.
Sasa alikuwa hewani na kamba ikizidi kumvuta kwenda
juu.
Alivutwa hadi akatokea upande mwingine wa juu
kabisa.
Mara alipofika juu akasikia watu wakipiga makofi kwa
juhudi sana.
Rama akageuka kutazama makofi yanapotokea.
Hakuamini macho yake asilani, akafumbua na kufumba
kisha akafumbua tena…. Hali ilikuwa kama akili yake
ilivyokuwa imetafsiri!
BALAA!x